Sheria ya Gharama za Uchaguzi Mwiba kwa Wabunge!

Buchanan

JF-Expert Member
May 19, 2009
13,199
1,969
Na Mwandishi Wetu, Dodoma

WABUNGE sasa wanaweweseka na utekelezaji wa sheria waliyoipitisha wenyewe ya Gharama za Uchaguzi, huku Mwanasheria Mkuu wa Serikali akiisisitizia Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kuwabana wabunge wanaokwenda kinyume na sheria hiyo.

Aidha, Spika wa Bunge, Samuel Sitta amewataka wabunge hao wanaomaliza muda wao Agosti mosi mwaka huu, kutofanya mambo yao gizani.

Hoja ya wabunge kulalamika kuvamiwa na Takukuru wanapotoa misaada hivi sasa majimboni iliibuliwa na Spika Sitta jana asubuhi bungeni.

"Waheshimiwa wabunge, nimepata taarifa kutoka kwa baadhi yenu kwamba wabunge katika baadhi ya shughuli wanazofanya majimboni, wanavamiwa na Takukuru.

"Kuna wanaotoa vyerehani kwa akinamama, kwa mfano uliahidi kuwa utawapa…sasa unavamiwa. Kwa hiyo, katika hili nitamtaka Mwanasheria Mkuu wa Serikali atoe ufafanuzi baada ya kipindi cha Maswali na Majibu ili tuweze kutulia katika majimbo yetu," alisema Sitta.

Katika ufafanuzi wake, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema, licha ya kuwataka wabunge waisome kwa makini Sheria ya Gharama za Uchaguzi, lakini aliiagiza Takukuru iendelee na kazi yake ya kuwanasa wote wanaokiuka sheria hiyo.

"Lakini naomba mzingatie hili na hapa afadhali nibaki peke yangu ... naomba vyombo vinavyohusika na hasa Takukuru, tekelezeni wajibu wenu, kamateni vyerehani vya rushwa," alisema Jaji Werema na kuongeza:

"Nanyi wabunge, tafadhali jibuni maswali mtakayoulizwa … kwa mujibu wa sheria hii, hata nami nina mamlaka ya kuwashughulikia."

Jaji Werema aliyetumia muda wake kusoma vipengele muhimu vya sheria hiyo na Katiba ya Tanzania kuhusu uhai wa Bunge, alisema wabunge wanastahili kuendelea kutoa misaada hadi Bunge litakapovunjwa kisheria.

Kwa mujibu wa Spika Sitta, Rais Jakaya Kikwete atalihutubia Bunge Ijumaa wiki hii saa 10 jioni, lakini kwa fununu alizonazo, Bunge litavunjwa kisheria Agosti mosi.

Kwa hiyo, Jaji Werema alisema kwa sasa wabunge wana haki ya kutimiza ahadi zao kwa kuchangia huduma za kijamii kama vile maji, elimu na barabara.

"Wana haki ya kusukuma ahadi zao kama za shule kwa ujenzi wa mabweni ya wasichana, barabara, huduma za kijamii, kutoa vyerehani kwa akinamama.

"Lakini naomba mzingatie sheria hii. Muisome kwa makini, hampaswi kutoa zawadi binafsi, mnatakiwa iwe kwa vikundi," alisema Mwanasheria Mkuu wa Serikali.

Alisema kwa mujibu wa sheria hiyo, Ibara ya 21 (1) kifungu kidogo (a), kinazungumzia suala la ushawishi kabla, wakati wa kampeni na baada ya uteuzi, kwa kumhusisha mhusika mwenyewe au mtu aliyemtuma kufanya kwa niaba yake.

Akizungumza baada ya ufafanuzi huo wa Jaji Werema, Spika Sitta alisema kwa msingi huo, wabunge wanatakiwa kutekeleza ahadi zao ndani ya muda mfupi uliobaki hadi Agosti mosi mwaka huu.

"Ila naomba waheshimiwa hao wahusika watambue kuwa kuna Mfuko wa CDTF (Maendeleo ya Jimbo) … na tayari wabunge wamepewa fedha na wengine wamechukua wiki hii," alisema Sitta na kuongeza:

"Ninachoomba kama alivyoeleza Mwanasheria Mkuu, tuwe wawazi … hivi unakutwa na Takukuru usiku, ukiwa na pick-up, hakuna watu wala usomaji risala … mbunge makini hufanya mambo yake kwa watu hadharani, watu wanasoma risala, hiyo ndiyo dawa."

Source:
HabariLeo
 
Hakuna ujanja mtakamatwa wote mh Sitta. Kama hukuwapa wapiga kura wako vishawishi na ahadi kabla, ujue imekula kwako. Usitafute visingizio ili ugombane na takakuru. Ni nyie wenyewe mlipitisha sheria hizo.
ZIFUATENI SASA
 
wadau nina shida ya kupata chapisho la sheria ya gharama za uchaguzi kwa kiswahili,nasikia wabunge walipewa kama kuna mdau anayo atundike hapa au anielekeze wapi pa kupata ili tuwasaidie watz wa vijijini
 
Tofauti na uchaguzi wa mwaka 2010, mwaka huu binafsi sijasikia hata mara moja sheria ya gharama za uchaguz ikizungumzwa na tume ya taifa ya uchaguzi na wadau wa uchaguzi.

Ina maana umuhimu wa sheria ile umetoweka?Nini hasa chanzo cha hali hii?

Tujadiliane
 
Back
Top Bottom