Sheria mpya, TAKUKURU ile ile ni kujidanganya

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,293
33,078
TUMEKUWA tukifuatilia mjadala ulioibuka bungeni na kwingineko, kuhusu muswada wa Sheria ya Gharama za Uchaguzi ambao tunaambiwa karibuni utafanywa kuwa sheria.
Tuseme mwanzoni kabisa kwamba sisi tunauona muswada/sheria hii kuwa ya muhimu sana katika mazingira ya siku zijazo, yanayojaribu kurekebisha uchafu ambao tumekuwa tukiushuhudia katika kila muda wa uchaguzi unapofika.
Wakati mwingine tumekuwa tukijiuliza: Kila mtu amekuwa akiimba kwamba tunataka kujenga demokrasia nchini, tupate viongozi safi na makini waliotokana na ridhaa ya umma, lakini haohao waimbaji ndio ambao wamekuwa msitari wa mbele katika kutumia fedha kununua ushindi.
Sisi huwa tunashangaa tunapowasikia wakijinadi. Tuseme tu kwamba gonjwa hili limekuwa ni kubwa, na si tu kwamba ni kubwa bali limeenea hadi katika ngazi za chini kabisa za jamii yetu. Linajitokeza kwa nguvu si katika chaguzi za kisiasa tu, bali hata katika uchaguzi mdogo kama wa urais wa chuo ama wa mwakilishi wa darasa. Fedha lazima zitumike ili mshindi apatikane! Huko ndiko tulikofika.
Tunaposikia sasa kwamba kuna sheria inakuja kupambana na uchafu huu katika uchaguzi, tunaliona hili kama hatua chanya. Kwamba sasa vyombo husika vitakuwa na nafasi ya kuchungulia na kuchukua hatua kuanzia katika ngazi za chini kabisa za uchaguzi kwenye vyama vyetu vya siasa.
Kwa kauli na hali ya mambo tunayoyaona, ni kwamba vita hii dhidi ya fedha chafu katika siasa inatarajiwa kuongozwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).
Hatuna shaka kubwa na TAKUKURU kama chombo kiongozi wa vita hii. Ina uwezo wa kuongoza vita hii. Lakini ingekuwa na uwezo zaidi kama ingefanya mawili matatu. TAKUKURU ifike mahali iaminike mbele ya jamii kama mpambanaji wa kweli wa uchafu unaosababishwa na rushwa nchini.
Ilivyo, si wengi wanaoiamini. Tunakumbuka matukio yaliyofuatia kamatakamata ya Elisa Mollel na Lekule Laizer kule Arusha, yakitajwa kuongozwa na TAKUKURU. Ama ushiriki wake katika suala la Richmond ambao maelezo yake hayakupata kukidhi kiu yote, na hivi karibuni, uchunguzi wa posho mbalimbali za wabunge ambao ama umevia au umekwama katika mazingira ambayo unaweza kutafsiri kuwa ya nipe nikupe.
Kwa hiyo ni rai yetu kwamba ili sheria hii ishike sawasawa, TAKUKURU itabidi ionyeshe na ionekane kuwa ni chombo safi kisicho na upande.
Kusaidiana na hili, pafanyike hatua za makusudi za kuelimisha jamii juu ya sheria hii mpya, kuanzia sasa, wakati wa uchaguzi na baada, ili wazo hili lijikite ndani ya mioyo ya jamii nzima.
Kwa nini tunaomba elimu kwa jamii? Tunaijua jamii yetu ilivyo, wengi huenda hata hawajasikia kuwa kuna sheria inakuja kuzuia kuhonga na kuhongwa. Si ajabu kwamba hata wengi wetu hatujui kwamba lile suala la takrima lililoimbwa sana na chama kimoja cha siasa ili kuhalalisha uhongaji, lilikwisha kufanywa haramu na Mahakama. http://www.raiamwema.co.tz/news.php?d=2097
hs3.gif
 
Back
Top Bottom