Shaka amemtia shime Rais Samia Suluhu Hassan azidi kukanyaga na kupiga hatua za maendeleo

Pfizer

JF-Expert Member
Mar 25, 2021
298
511
SHAKA:RAIS SAMIA KANYAGA
TWENDE,CHAMA KINARIDHISHWA, WANANCHI WANAKUELEWA

KATIBU wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM, Itikadi na Uenezi, Shaka Hamdu Shaka, amemtia shime Rais Samia Suluhu Hassan azidi kukanyaga na kupiga hatua za maendeleo kwa kuwa Chama na wananchi wanaona na kuridhishwa na kazi kubwa anayoifanya.

Shaka ameyasema hayo leo Oktoba 13, 2022 wakati wa ufunguzi wa Chuo cha Ufundi Stadi (VETA) cha Mkoa wa Kagera katika hafla ambayo imefanyika mjini Bukoba mgeni rasmi akiwa Rais Samia.

"Kwa ufupi tu niseme ajenda za Watanzania kuhusu maendeleo ziko kwenye mikono salama chini ya uongozi wa serikali ya Chama Cha Mapinduzi inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan.

"Kama uko juu ya mlima ukiangalia chini utaona ni mbali, lakini mheshimiwa Rais tunakwenda, Kanyaga twende mambo ni mazuri, huu ni utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM, Ibara ya 80 ya 2020-2025," amesema.

Shaka amesema Chama kimefuatilia na kinatambua kuwa Rais Samia katika kipindi chake kifupi madarakani amefanikiwa kujenga vyuo vya VETA katika wilaya 29 na mikoa minne.

"Ujenzi huu hapa ni kimoja tu, lakini tumefuatilia kwa karibu kama Chama, Rais (Samia) umejenga vituo kama hivi katika uongozi wako katika wilaya 29 na mikoa minne, hongera sana mheshimiwa Rais kwa mapinduzi haya makubwa na utekelezaji huu wa kuwakomboa vijana wa Kitanzania.

"Ndugu zangu ukienda katika hesabu za haraka haraka katika kipindi cha mwaka mmoja cha uongozi wa Rais Samia, ametumia karibia sh. bilioni 79 kujenga vituo kama hiki kwa ajili ya ukombozi wa vijana wa Tanzania," amesema.

RAIS SAMIA ANAISHI
MAONO YA NYERERE

Aidha, Shaka alitumia fursa ya kutoa salamu Chama katika hafla hiyo kueleza namna Rais Samia anavyoenzi kwa vitendo maono ya Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere wakati huu Watanzania wakiadhimisha miaka 23 ya kifo chake.

"Naomba niseme neno moja lenye uzito wa hali ya juu, Mheshimiwa Rais leo tukiwa tunashuhudia makabidhiano ya chuo hiki cha kisasa kabisa, wote tunakumbuka na wote tunafahamu kwamba tuko kwenye kumbukizi ya miaka 23 ya kifo cha hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

"Ndugu Rais tukikumbuka wasia na tukimbuka moja ya kumbukumbu muhimu ambazo tumeachiwa na mwasisi wa taifa hili, ni maono pamoja na misingi baada ya kuasisiwa kwa taifa.

"Baada ya uhuru, Mwalimu Julius Nyerere alihimiza, alikuwa na maono na mtazamo kwamba siku moja Tanzania iwe na taasisi au kuwa na vyombo ambavyo vitawasaidia Watanzania, katika kuwajengea uwezo wa kujiajiri kwa mantiki nzima ya kupambana na umasikini.

"Mwalimu Nyerere katika kitabu chake cha 'Uhuru na Maendeleo' alisema ukitaka kuleta maendeleo kwa wananchi washirikishe, mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, Chama Cha Mapinduzi kinakupongeza kwa dhati kabisa kwa kuishi kwa vitendo maono na dira ya baba wa taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere wakati huu tukiwa katika kumbukizi ya miaka 23.

Chuo hicho cha VETA Mkoa wa Kagera kimejengwa katika Kata ya Nyakati, Kijiji Cha Burugo ambapo ujenzi wake umegharimu sh. bilioni 22.4 kikijengwa kwa msaada wa serikali ya China.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom