Shairi langu.....toka kifungoni(BAN)

CAMARADERIE

JF-Expert Member
Mar 3, 2011
4,419
1,920
Namba nawe mlimwengu, pulikiza matamko
Nikweleze neno langu, uzinduwe bongo lako
Nayo nda M'ngu si yangu, na ayani haya yako
Uwatapo haki yako, utaingiya motoni

Simama uitete, usivikhofu vituko
Aliyo nayo mwendee, akupe kilicho chako
Akipinga mlemee, mwandame kulla endako
Uwatapo haki yako, utaingiya motoni

Amkani mulolala,na wenye sikio koko
Isiwe mato kulola,natutizame twendako
Tuwate na kuduwala,usingizi si mashiko
Uwatapo haki yako,utaingiya motoni

Teteya kwa kula hali, usiche misukosuko
Siche wingi wala mali,sabilisha roho yako
Unyonge usikubali, ukaonewa kwa chako
Uwatapo haki yako, utaingiya motoni

Siche kifaru na ndovu, wangazidi nguvu zako
Wapempe kwa uwekevu, unusuru haki yako
Siandame wapumbavu,kilicho chako ni chako
Uwatapo haki yako, utaingiya motoni

Cha mtu hakifitiki,kikafungiwa kiliko
Huzuka kikawa hiki,kazana utwae chako
Uwatapo yako haki,fahamu ni dhara kwako
Leo na kwa Mola wako,utaingiya motoni

Fumbuwa unyang'arize, uone duniya yako
Bure sijiangamize,kuangalia wendako
Utatupa upoteze,wende ambapo si pako
Uwatapo haki yako,utaingiya motoni

Kadhalika nako pia,huko ambako sikwako
Huwezi kujitetea,wala huwi na mashiko
Basi iwaze duniya,kwani ya kale hayako
Uwatapo haki yako ,utaingiya motoni

Kadi tamati shairi,sitii la ongezeko
Mwanati iwa tayari, utete haki yako
Unyonge usiukiri,Jifunge ufe kwa chako
Uwatapo haki yako, utaingiya motoni
 
Hakika ni ushari mzuri sana uliotungwa na Ahmad Nassir ( Malenga wa Mvita)
 
UZURI
Uzuri Wa uso mwema
Unavuta vitu vyote
vya macho ya kutazama
Walakini kwa kupima uzuri wa,
tabia bora unapopita po pote

uzuri kupita kupita huu
katika hii dunia
nawapa msisahau,
Ni nzuri Wa tabia
Ni johari ya heshima duniani
kila mara

Huendeshwa na tabia
kama tabia Si njema,
si ajabu kupotea.
Kitu kilicho adhama ni tabia
na busara

Kwa kutengeza tabia
Rai yangu na fikira
Vyuo katika dunia
Vingekuwa na tijara
kwa kuwa nayo daima sera na
tabia bora.


From Malenga wa Mvita by Ahmad Nassir
 
NYANI AONE KUNDULE

Funguweni masikizi, mupate yangu sikiya
Ninenayo mumaizi, kesho musije kuliya
Naeleza waziwazi, musije kosa sikiya
Na uwe mwamko mpya, nyani aone kundule.

Ni wa kale wanenele, katu haiwezekani
Bara hadi maji male, mbinguni na duniani
Nyani haoni kundule, hata kwa Kudura ipi
Na uwe mwamko mpya, nyani aone kundule.

Ela itawezekana, japo shime akitiya
Apate kuzindukana, kwa mizani kujitiya
Uzito wake kuona, bila tu kwa kukisiya
Na uwe mwamko mpya, nyani aone kundule.

Leo sikizi funguwa, hilino suwala tata
Fanya hima kwiyelewa, kesho usije kujuta
Nafusiyo kuelewa, kabula mwiya kupita
Na uwe mwamko mpya, nyani aone kundule.

Hata uwe jamadari, na tiara bega zima
Usipo jitahadhari, "cheni" usimame wima
Uizidishe fahari, ja aloumbwa kwa chuma
Na uwe mwamko mpya, nyani aone kundule.

Chunga unaposimama, kaguwa wako msingi
Chunga usije terema, ukabiringa "biringi!"
Jigange panapouma, japo mganga hagangi
Na uwe mwamko mpya, nyani aone kundule.

Hata uwe profesa, wajuwa duniya nzima
Ama ni mwenyi mapesa, manoti ni chungu nzima
Au mrembo kipusa, popote twakutazama
Na uwe mwamko mpya, nyani aone kundule.

Usinite mnafiki, kunirushiya matusi
Lau japo hutosheki, usijawe wasiwasi
Mbona kalamu hushiki, pamoya na karatasi?
Na uwe mwamko mpya, nyani aone kundule.
 
Back
Top Bottom