Serikali yakiri matumizi mabaya ya fedha za walipa kodi

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
MATUMIZI mabaya ya serikali na kuendelea kupanda kwa mfumuko wa bei za bidhaa kwa zaidi ya mara mbili katika kipindi cha kati ya mwaka 2005 na sasa ni chanzo cha maisha magumu ya wananchi, Tanzania Daima limebaini.


Katika wakati ambapo wananchi wapatao milioni nane wanalala au kushinda njaa kwa sababu ya ugumu wa maisha, serikali jana ilikiri kupitia kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Uchumi, Ramadhan Kijjah, imekuwa inatumbua shilingi mbili, wakati ina uwezo wa kukusanya shilingi moja.


Akitoa tathmini ya serikali kuhusu hali ya uchumi kwa kipindi cha miaka minne iliyopita, Kijjah alisema mapato ya serikali kwa mwaka ni sh trilioni tano, lakini matumizi ya serikali ni Sh trilioni 10.


Akijadili tathmini hiyo, mchumi na mwanasiasa, Profesa Ibrahim Lipumba, alisema matumizi hayo makubwa ya serikali yanaathiri vibaya Watanzania wa kawaida, kwani yanachochea mfumuko wa bei unaosababisha gharama za maisha kuwa za juu.


Wakati Kijjah akikiri kwamba kimsingi, mapato ya serikali yamepanda kutoka Sh trilioni 2.167.6 mwaka 2005/06 hadi Sh trilioni 5.096 mwaka 2009/10, Profesa Lipumba alisema kama serikali ingekuwa makini, kulingana na ulaji mkubwa inaoonyesha, makusanyo ya sasa yangekuwa makubwa zaidi na yangekusanya kwa nidhamu.


Alisema serikali inawaachia watu fulani fulani (hakuwataja) na makampuni makubwa yasilipe kodi.


Kwa sababu hiyo, Profesa Lipumba alisema uchumi wa nchi unayumba na kufanya maisha ya Mtanzania yazidi kudorora.


“Hakuna ukusanyaji mzuri wa kodi; watu wanaachiwa, makampuni yanayochimba madini hayalipi kodi ya kutosha….hilo lina athari,” alisema Profesa Lipumba.


Kumbukumbu zinaonyesha kuwa mwaka 2004/05 wakati utawala wa Rais Benjamin Mkapa ukielekea ukingoni matumizi ya serikali yalipanda kutoka Sh trilioni 2.1 hadi Sh. trilioni 2.7 mwaka 2005/06 wakati Rais Jakaya Kikwete anaingia madaraka.


Mbali ya hilo taarifa hiyo ya Kijjah ilionyesha kwamba mfumuko wa bei umepanda kwa zaidi ya mara mbili katika kipindi cha kati ya mwaka 2005 ulipokuwa ni asilimia 5 hadi kufikia asilimia 12.2 Desemba mwaka jana kabla ya kushuka kidogo na kuwa asilimia 10.9 Januari mwaka huu.


Hata hivyo Kijjah, alisema serikali imechukua hatua ili kukabiliana na matumizi hayo makubwa. Alisema imeongeza idadi ya wahasibu na wakaguzi wa ndani katika ngazi zote kuanzia wizara hadi serikali za mitaa.


“Kuanzishwa kwa kitengo cha ufuatiliaji wa matumizi ya umma (bajeti) katika miradi iliyoidhinishwa: Ofisi ya Mkaguzi Mkuu (CAG) imeongezewa nguvu za kisheria kuweza kufanya kazi zake bila kuingiliwa na taasisi yoyote.”


Katibu mkuu huyo ambaye alikuwa amefuatana na naibu wake, John Haule, aliongeza ili kupunguza matumizi makubwa ya serikali, yanahitajika marekebisho katika Sheria ya Manunuzi ya Umma ya mwaka 2004 ikiwa ni pamoja na kutoa elimu kwa watendaji wake.


“Sera ya mapato ya mwaka 2009/10 inalenga kukusanya mapato ya ndani yasiyopungua sh milioni 5,096,016 sawa na asilimia 16.4 ya pato la taifa,” alisema.


Kuhusu thamani ya fedha, Kijjah alisema, shilingi iliendelea kuporomoka kutoka wastani wa shilingi 1,195.75 kwa dola ya Kimarekani mwaka 2008 hadi kufikia shilingi 1,318.71 mwaka jana.
 
Haya matumizi mabaya ya fedha za walipa kodi yanachangiwa pia na gharama kubwa ya safari za rais. Hebu wataalamu wetu watupe upembembuzi yakinifu wa kile kilichopatikana katika safari za rais na kile kilichopatikana katika safari hizo kama hutakuta kina shabihiana na huyu katibu(mchumi) kwamba tunazalisha sh 1 na tunatumia sh2.
 
Kikulacho ki nguoni mwako ..huu ni usemi ambao hauepukiki kwa sasa japo tunaweza kucha matumizi mabaya tukiwa na viongozii makini .lakini vile vile viongozi makini ni vigumu kuwapata kwa sababu ya 70% ya mzee Vasco aliyoisema.
 
ndio wamebaini leo? au ndio mkakati wa kuandaa uongo wa kuja kusema kipindi cha kampeni kuwa "sasa tuchagueni tukakusanye mapato, manake serikali yenu ilikuwa ndio imeanza mkakati wa kukusanya kodi zaidi,sasa inabidi tukaukamilishe" manake hawakawiagi
 
Serikali imesema inatumia Sh. trilioni 10 kwa mwaka wakati mapato yake ni Sh. trilioni tano tu ambazo inazikusanya kutoka vyanzo vyake mbalimbali.



Takwimu hizo zilitolewa jana jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Uchumi, Ramadhani Kijja, alipokuwa akitoa taarifa ya mafanikio ya serikali ya awamu ya nne katika kipindi cha kati ya mwaka 2005 hadi 2010.
Kadhalika, Kijja aliwaambia waandishi wa habari kuwa mfumuko wa bei unazidi kupanda ambapo hivi sasa umefikia asilimia 10.
Mwaka jana Benki ya Dunia iliishauri serikali kuchukua hatua mbalimbali ili kupunguza kiwango cha mfumuko wa bei wakati uliporipotiwa kufikia asilimia saba.
Hata hivyo, Kijja alisema mapato ya serikali yamepanda kwa mwezi kutoka Sh. bilioni 150 mwaka 2005/6 hadi Sh. bilioni 400 hivi sasa.
Katibu Mkuu huyo alisema kiasi kinachopungua serikali inakipata kupitia misaada ya kutoka nchi wafadhili pamoja na mikopo kwa lengo la kufidia pengo la Sh. trilioni tano.
Kwa upande wa uchumi, alisema unakua kwa kusuasua kutokana na matatizo mengi yaliyojitokeza baada ya serikali ya awamu ya nne kuingia madarakani.
Aliyataja matatizo hayo kuwa ni pamoja na ukame ambao ulisababisha uzalishaji wa mazao ya kilimo kushuka pamoja na mtikisiko wa uchumi ulioikumba dunia kuanzia mwaka 2008.
Akizungumzia suala la ukuaji wa uchumi, Kijja alisema unakua kwa asilimia 7.2 na kuongeza kuwa serikali inafanya jitihada kadhaa kwa lengo la kuupandisha zaidi.
Aidha, Kijja alisema pato la Mtanzania mmoja mmoja kwa mwaka limekua na kufikia wastani wa Dola za Marekani 525 kutoka Dola za Marekani 444 mwaka 2007.
Akizungumzia mipango ya serikali katika kukuza uchumi, alisema imepanga kuimarisha kilimo kwa kuwawezesha wakulima kuendesha kilimo cha umwagiliaji.
Alisema kuwa serikali itaendelea kuisadia sekta ya elimu ili kupata wasomi wengi miaka ijayo na kwamba hiyo ni mojawapo ya njia za kulisaidia taifa.
Kuhusu wajasiriamali, alisema serikali itaendelea kuweka mazingira ya amani ili kila mwananchi aweze kushiriki kuchangia pato la taifa kwa namna moja ama nyingine kadri atakavyoweza.
Kuhusu kudhibiti matumizi ya fedha za serikali, Kijja alisema serikali imeteua Naibu Mhasibu Mkuu wa Serikali ambaye atakuwa anashughulikia fedha zinazokwenda katika Halmashauri mbalimbali nchini.
Alisema kuwepo kwa ofisa huyo kutasaidia ufuatiliaji wa karibu wa matumizi ya fedha za serikali.
Wakati huo huo, serikali imewataka wananchi kuwasilisha Benki Kuu ya Tanzania (BoT) fedha zote zilizochakaa ili kutengeneza zingine badala ya kuendelea kuzikataa mitaani.
Fedha ambazo wananchi wengi wanazikataa ni pamoja na zile za sarafu za Sh. 50 na Sh. 100 na kuwashauri wananchi kuzipeleka BoT ili zikafanyiwe kazi.
Kwa mujibu wa Kijja, kila wizara inatakiwa kutangaza mafanikio yake na changamoto zinazoikabili serikali ya awamu ya nne tangu ilipoingia madarakani.
Licha ya wananchi wengi kuendelea kulalamikia kupanda kwa gharama za maisha, lakini Kijja jana alisisitiza kuwa maisha bora kwa kila Mtanzania yanawezekana.




CHANZO: NIPASHE


0 Maoni | Kuwa wa kwanza kutoa maoni
 
Hata allocation of our natural resources pia ni matumizi mabaya na ndio chanzo kikubwa sana katika umaskini wa taifa letu hivyo kama budget ndio hivyo hata jinsi gani ya kukusanya na kufanya mtawanyiko wa uchumi uwe imara
 
Back
Top Bottom