Miss Zomboko
JF-Expert Member
- May 18, 2014
- 4,500
- 9,279
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Majaliwa Kassim Majaliwa amewaonya baadhi ya viongozi wakiwemo Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya kwa kutoa matamko na takwimu kuhusu mlipuko wa ugonjwa wa covid-19 nchini.
Majaliwa amesema hayo jana Jumatatu, Aprili 6, 2020 wakati akihutubia bungeni jijini Dodoma; “Kuhusu homa kali ya mapafu ya virusi vya Corona, Serikali imeendelea kuchukua hatua mbali mbali na kama alivyosema Waziri wa Fedha, tume imeshaundwa na Serikali itatoa muelekeo kutokana na athari zinazoendelea kujitokeza.
“Mkuu wa Wilaya, Mkuu wa Mkoa kila mmoja anatamka atakavyo, nilishasema atakayetoa taarifa za ugonjwa ni Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, na kama itabidi nitatoa mimi mwenyewe na kama italazimika sana atatoa Makamu wa Rais au Mheshimiwa Rais mwenyewe. Utaratibu huu utasaidia kuleta taarifa za uhakika, hii hali ya Wakuu wa mikoa na Wilaya kutoa matamko kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge hapa, haiko sawa.
“Hospitali za Rufaa za Kanda na Mikoa nazo zinaratibiwa kutoa huduma ya upimaji sambamba na maeneo ya mipakani. Shughuli hizo za upimaji zinafanyika kwa usimamizi wa Maabara Kuu ya Taifa ya Afya ya Jamii kwa lengo la kuthibitisha ubora wa vipimo,” alisema Majaliwa.