BAK
JF-Expert Member
- Feb 11, 2007
- 124,790
- 288,005
Na Mhariri
MwanaHALISI
MwanaHALISI
WAZIRI Mkuu, Mizengo Pinda anasema, "haraka haraka nayo haina baraka." Alikuwa akizungumzia suala la serikali kuchukua hatua pale jambo linalohusu jamii nzima linapotokea.
Msemo huu ambao kwa asili hauna neno "nayo," unahimiza busara kuzingatiwa kabla ya mtu kutenda jambo.
Je, ni kweli waziri mkuu amesahau kuna misemo mingine isemayo, kwa mfano, "Chelewa chelewa utakuta mtoto si wako;" "Asiyesikia la mkuu huvunjika guu," "Mficha uchi hazai" na "Mficha ugonjwa, kifo kitamuumbua?"
Leo hii dunia nzima inaishangaa Tanzania na serikali yake. Inaona serikali ya nchi hii haina hata uwezo wa kujua lipi zuri na lipi baya, jambo ambalo watu hufunzwa au huiga tangu utotoni.
Chukua mifano hii: Kulikuwa na mjadala juu ya nafasi ya Zanzibar katika Muungano iwapo ni nchi au la. Ilichukua muda mrefu kusema lolote na bado suala hilo linatokota. Ni ngojangoja.
Kuna mgogoro wa Zanzibar. Rais Kikwete aliuita "Mpasuko." Serikali haitafuti ufumbuzi. Bado ni ngojangoja.
Ufisadi ni unyama. Ni ukwapuaji wa kinyama wa fedha na maliasili za nchi na kuzitumia kwa manufaa binafsi ya watu wa ndani au nje ya nchi.
Leo hii bado serikali inaendeleza mijadala juu ya mafisadi, hadi wabunge wanagawanyika pande mbili: Hawa wanataka ufisadi na kuutetea na hawa wanapinga unyama huu. Ni ngojangoja ya Pinda.
Wazazi wa wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu, kwa muda mrefu sasa, wamekuwa wakilia na kutaka serikali iweke utaratibu wa kugharimia elimu yao kwani, kwa raslimali zilizopo, hilo linawezekana.
Serikali haisemi lolote la maana. Inajua jibu moja tu: Hakuna fedha. Inaacha walie na kusaga meno na ikiwezekana watawanyike na kuacha masomo. Ni ileile ngojangoja.
Yapo masuala mengi ambayo serikali inapaswa kuchunguza na kuchukulia hatua kabla wananchi hawajachoka.
Hata kwa ngazi ya familia, lazima awepo kiongozi wa kuchukua hatua msimamo kwa masuala na inakuwa vema kama kiongozi anashirikisha wadau wote.
Tunahimiza siku zote serikali ichukue dhamana iliyopewa na wananchi ya kuongoza kwa kuonyesha njia. Haidhuru hata kama uamuzi wa kwanza utakuwa na kasoro.
Afadhali kuwa na mwenye maamuzi yenye kasoro zinazosahihika kuliko asiyetoa uamuzi wowote.
Serikali isiyo na uamuzi katika masuala makubwa, hata madogo, ni kama haipo; na kama hakuna serikali, basi kuna vurugu. Wananchi hawakuchagua vurugu.