Serikali inapodharau wananchi

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,790
288,007
Serikali inapodharau wananchi

Ndimara Tegambwage
Tanzania Daima

SITAKI wananchi wakubali kudharauliwa na serikali waliyoiweka madarakani. Sitaki serikali iwaone kama wapiga kelele tu, kwa mtindo wa ‘wacha waseme, usiku watalala.’

Ni wiki ya nne sasa tangu wananchi waitake serikali yao iwaeleze ilikuwaje helikopta ya Jeshi la Wananchi (JWTZ) ikabeba ‘raia’ wa Marekani, Uingereza, Canada na Australia kwa safari za kibiashara nchini.

Maswali makuu ni iwapo jeshi sasa limeingia katika biashara, kwa kukodisha baadhi ya zana zake za kivita; iwapo linakodisha helikopta peke yake au hata silaha nyingine; na nani ananufaika na biashara ambayo inaweza kuteketeza usalama wa nchi.

Imethibitika sasa kwamba watu hao kutoka nje ya nchi hawakuwa watumishi wa serikali za nchi zao; wala hawakuwa wametumwa na serikali. Aidha, nchi hizo hazina mkataba wala ushirikiano wa aina hiyo na jeshi au Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Lakini serikali imeendelea kukaa kimya. Hakuna maelezo. Na moja ya njia kuu za serikali kuficha ukweli, kuzima hoja, kuua mjadala na hata kusema uongo, ni kukataa kusema.

Kukataa kusema kuna maana ya kutokuwa na jibu sahihi; kupuuza kilio cha wananchi; kutojali; kudharau hoja iliyoko mezani; na kudharau wananchi kwa msingi kuwa ‘hata hivyo hawana la kufanya.’

Kwa mujibu wa sheria zinazotawala jeshi, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa ndiye msemaji mkuu wa chombo hicho.

Waziri amepewa jukumu la kulinda na kutawala vitu viwili muhimu katika jeshi. Kwanza, kutawala askari; na pili, asimamie na kulinda silaha.

Kwa ufupi, na kwa maana halisi ya kiufundi, askari na silaha ni ‘vifaa’ muhimu na maalumu chini ya uangalizi wa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa; kwa sasa Profesa Juma Kapuya.

Askari ni neno linalotumika kutofautisha mtu na kitu, lakini katika maana halisi ya jeshi, askari ni silaha. Ni silaha inayopumua; inayoishi katika mabweni ya jeshi; tofauti na silaha nyingine inayotunzwa katika ghala.

Waziri anapaswa kujua askari amepelekwa wapi na kwa kazi ipi; lini na kwa kipindi gani. Anapaswa kujua kifaa au silaha hii au ile iko wapi, imesogezwa wapi, kwanini; inatumikaje huko ilikopelekwa; inatumiwa na nani, kwa muda gani na iwapo ni kwa manufaa ya jeshi na nchi.

Katika hili la helikopta, Kapuya anapaswa kujua majina ya raia wa nchi za nje ambao walikutwa na ndege; walikuja nchini kwa shughuli gani; nani aliwapeleka kwake au kwa msaidizi wake kuomba helikopta.

Ni waziri huyohuyo ambaye anapaswa kujua iwapo ‘wageni’ waliomba msaada wa helikopta au walilipa kiasi gani ili wapewe silaha muhimu ya jeshi.

Waziri ndiye anaweza kujua rubani wake wa silaha inayoruka amelipwa kiasi gani cha posho, ikiwa nyongeza kwa mshahara wake wa kila mwezi.

Lakini ni Kapuya ambaye siku chache baada ya kutunukiwa uwaziri; wakati wa fungate ya ushindi wa Rais Jakaya Kikwete, alichukua ndege ya JWTZ kwenda jimboni kwake.

Vyombo vya habari vilipohoji matumizi ya ndege ya jeshi, ni Kapuya aliyejibu, kwa jeuri isiyomithilika na kwa kuuliza, ‘Nisipotumia ndege nitumie farasi?’

Mara hii, Kapuya hana hata jeuri ya kutoa jibu la kejeli au angalau kueleza kuwa anajua lolote juu ya helikopta. Alinukuliwa na waandishi wa habari akisema yuko jimboni hakuwa na lolote la kusema.

Inawezekana kweli, watu kutoka nje walikuwa wanapiga picha ambazo zingetumika kusaidia shughuli za utalii hapo baadaye, lakini Wizara ya Utalii ina bajeti na mipango yake ambayo haiingiliani na silaha za jeshi.

Hata kama watatokea wenye kisingizio kwamba Wizara ya Utalii ilikuwa inajua kuwepo kwa wapiga picha hao kutoka nchi za nje, helikopta ya jeshi inafanya nini katika biashara hii ya kitalii?

Matumizi ya vyombo vya jeshi katika shughuli binafsi na za watu wa nje, ni ushahidi tosha kwamba jeshi limeingizwa kwenye biashara ya watu binafsi.

Katika kila biashara kuna ushindani. Katika ushindani kuna kupata na kupoteza. Katika mazingira ya ushindani kwa kutumia rasilimali za watu wengi kuna wanaosikitika, wanaolalamika na wanaopinga matumizi ya zana za kazi kwa manufaa ya watu binafsi na wachache.

Silaha zinazopumua ambazo ndizo hutumia silaha bubu katika tasnia ya kijeshi, huweza kujenga hisia kutumiwa na watu binafsi na hivyo kugawanyika, hasa linapokuja suala la masilahi.

Huo unaweza kuwa mwanzo wa mgawanyiko ndani ya ngome ambazo hazikuwahi kufikiria kutumiwa kwa biashara, bali kwa ulinzi, na ulinzi pekee wa nchi hii.

Profesa Kapuya aseme anachojua juu ya helikopta ya jeshi. Kunyamaa kwake ni kuasisi maafa yatokanayo na ulegevu katika safu za ulinzi wa nchi.

Mwandishi wa makala hii anapatikana kwa simu: 0713 614872; Barua pepe: ndimara@yahoo.com; www.ndimara.blogspot.com


 
Back
Top Bottom