Sanaa na kazi za ubunifu za Afrika zakaribishwa nchini China

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,003
1,024
Na Kelvin Ogome

dsafasf.jpg


Takwimu zilizotolewa katika ripoti ya Benki ya Dunia inaonyesha kuwa, asilimia 7 ya pato la jumla barani Afrika hutokana na utalii. Kando na kilimo na uchimbaji madini, mataifa mengi ya Afrika hutegemea utalii na watalii kujiendeleza kiuchumi. Hili ni dhihirisho kamili kuwa utalii ni nguzo muhimu sana katika uchumi wa bara la Afrika na ulimwengu kwa jumla.​

Kuanzia mwanzoni mwa mwaka 2020, sekta ya utalii imeshuhudia wimbi kali la hali mbaya na kupungua zaidi kwa mapato. Kila taifa ulimwenguni limerekodi kupungua kwa watalii na shughuli za kitalii kutokana na kuzuka kwa janga la virusi vya Corona.

Pia mifumo legevu ya kutangaza shughuli za kitalii imechangia pakubwa katika kupungua kwa pato litokanalo na utalii kulingana na wataalam na wahusika katika sekta hii.

Nchini Kenya katika mtaa wa Madaraka jijini Nairobi, utalii na shughuli za kitalii kwa jumla unachukua mkondo mpya. Kituo cha Bobu Africa kinaendeleza mfumo wa kipekee wa utalii. Tofauti na ilivyo kawaida ambapo mataifa hunadi vivutio vya utalii kama vile mbuga za wanyama, milima na maeneo ya Kijiografia, kituo hiki kinaendeleza sekta ya utalii kwa kubuni na kukusanya kazi za sanaa kuzinadi katika mataifa ya nje na mapato hutiririkia moja kwa moja hadi kwa wasanii wa bara la Afrika.

Bi. Yingying Shi, mkurugenzi na mwanzilishi wa kituo cha Bobu Africa anasema,“Afrika imebarikiwa na tamaduni na sanaa za kipekee, kwa siku zijazo iwapo kazi hizi hazitahifadhiwa vyema, ulimwengu utapoteza pakubwa, hapa Bobu Africa, tumejikita katika uhifadhi na uendelezaji wa sanaa”. “Ni mapenzi yangu ya dhati kwa sanaa na kazi hizi bunifu za Kiafrika ndiyo yalinifanya kuacha kazi yangu ya utangazaji katika kituo cha Xihnua ili niendeleze zoezi la kuhifadhi kazi hizi.” Aliongezea.

Bobu Africa, ni kituo cha sanaa kilicho na matawi katika nchi nne za Afrika mashariki (Kenya, Uganda, Tanzania, Rwanda). Kituo hiki ambacho kinatokana na jina la mti wa zamani barani Africa- Mbuyu(Baobab) uliotumika sana kuchonga vinyago hukusanya kazi za sanaa kutoka Afrika kisha kuzitangaza nje.

Vile vile, kupitia kituo hiki, wasanii wa bara la Afrika hupata mafunzo ya namna ya kuboresha kazi zao na kuziuza, “Utandawazi umetawala ulimwengu. Wasanii wengi wa Afrika wamesalia katika mifumo ya kale ya sanaa, tunachofanya hapa ni kuwafunza namna ya kuboresha kazi zao na pia kuwasaidia kuziuza katika mataifa ya kigeni kama China na nchi nyingine za Ulaya”, alisema Millicent Otieno, meneja mauzo wa kituo hiki.

Kupitia kituo hiki, Bi. Yingying Shi ameweza kusambaza bidhaa za sanaa kutoka Afrika kwenye makongamano na maonyesho kadhaa nchini China na kupanua soko la bidha za sanaa. “Kazi yetu si kuwafunza wasanii na kuhifadhi sanaa pekee. Tunafanya mengi, tumetangaza na kuuza kazi za sanaa za Afrika katika maonyesho ya sanaa kwenye mikoa mingi nchini China, mwezi juliopita tulitangaza bidhaa hizo kwenye maonyesho. Tunatarajia kuendeleza hilo” .

Sababu kubwa ya utalii na utamaduni wa kiafrika unaelekea kusahaulika ni kwamba mashirika na watu waliotwikwa jukumu la kutangaza utalii katika mataifa ya nje ya bara la Afrika hutangaza tu kuhusu mbuga na wanyamapori kisha kusahau mambo ya utamaduni na sanaa jambo ambalo wasanii wanasema ni hatari mno. “Utalii si wanyama pekee, utalii unajumuisha mambo mengi, hata kutembea Afrika kujifunza lugha moja au tamaduni zetu ni utalii. Tunafaa kuutangaza utalii kwa upana na wala si wanyama pekee” anasema Lynne Atieno, msanii katika kituo cha Bobu Afrika.

Kwa siku ya kawaida, Lynne hufika hapa na wasanii wenzake kisha kufanya mkutano kujadili ni kazi zipi za sanaa zinazohitajika nje, kupitia majadiliano na mashauriano ya kila siku wabunifu na wasanii katika kituo hiki hubuni, kuchora picha, mapambo na hata kuchonga vinyago. Baadhi ya picha huwekwa kwenye nguo na mavazi ambayo hutumiwa kuuza kazi za sanaa za Afrika nje ya nchi hasa nchini China ambapo 70% ya kazi hizi huuzwa.

Kituo hiki ambacho kimetoa zaidi ya nafasi 15 za ajira kwa raia wa Afrika pia huandaa safari za watalii kutoka mataifa ya nje kutembelea bara la Afrika kuzidisha ufahamu wao wa tamaduni za bara hili. Kwa mfano, kila mwaka wanaposherehekea sikukuu ya mwaka mpya wa jadi wa China, yaani Spring Festival, watalii kutoka China husherehekea sikukuu hiyo kwa kupanda Mlima Kilimanjaro, safari inayoandaliwa na kituo cha Bobu Afrika.
 
Back
Top Bottom