Sambwee Shitambala

Paparazi Muwazi

JF-Expert Member
Dec 23, 2007
310
79
Wanabodi, wakati nafanya uchambuzi kuhusu matokeo ya Mbeya, nimeona katika archive yetu hotuba ya Bwana Shitambala, nimeisoma imenifanya nijiulize maswali mbalimbali ambayo pengine wapo ambao mna majibu yake yanayoweza kuniongezea mambo ya kuyaweka kwenye makala ya uchambuzi kuhusu Mbeya vijijini.

Sambwee Shitambala: Aliingia kwa hamasa katika siasa. Akatoa hotuba hii hapa chini na kuisambaza kwa vyombo vya habari wakati wa kurudisha fomu. Lakini ghafla akawekewa pingamizi na kuengeuliwa. Baada ya matokeo kutangazwa Mbeya Vijijini, je ndio mwisho wake kisiasa au ndio safari ya kisiasa inaanza? Je, atakwenda mahakamani kutetea haki ya mawakili kuapisha ikiwemo kuapisha wagombea.


HOTUBA YA SAMBWEE SHITAMBALA- MGOMBEA MTEULE (CHADEMA) ALIYOITOA KATIKA OFISI YA CHAMA WILAYA YA MBEYA VIJIJINI WAKATI WA KUELEKEA KURUDISHA FOMU YA KUGOMBEA TUME YA TAIFA YA UCHAGUZI 27 DISEMBA 2008

Waheshimiwa viongozi wa CHADEMA;
Watanzania wenzangu, wanaMbeya Vijijini-wageni waalikwa,
Mabibi na Mabwana, itifaki zote nimezingatia.

Amani iwe kwenu.

Awali ya yote nimshukuru mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha jumuika pamoja leo mkiwa mmekusanyika kunindikiza kwenda kurejesha fomu za kugombea ubunge jimbo la Mbeya vijijini katika uchaguzi mdogo wa marudio jimbo la Mbeya vijijini. Tunajumuika leo, ikiwa ni siku moja toka kusherehekea sikukuu ya Noeli ambayo kwa waamini; ni kumbukumbu ya kuzaliwa kwa ukombozi.

Nawashukuru kwa kujumuika nami kunisindikiza kwa kuwa suala la kurejesha kwangu fomu, na kugombea kwa kwangu; si la kwangu peke yangu, ni suala la umma. Mtafahamu kwamba CHADEMA inaamini katika falsafa ya “Nguvu ya Umma”, kwa umma wa watanzania ndio una mamlaka juu ya viongozi wao. Chini ya falsafa hii, mimi ambaye CHADEMA imeniteua kugombea ubunge katika kura za awali na Kamati ya Utendaji ya Wilaya ya Mbeya Vijijini iliteua katika uteuzi wa awali Disemba 17 na baadaye kuthibitishwa na Kamati Kuu Disemba 20; nawajibika kwa umma wa wanachama. Naamini, ndio maana mmeamua kujitokeza kunisindikiza kutekeleza wajibu wa demokrasia na maendeleo. Na mara baada ya kurejesha fomu kwa tume ya uchaguzi leo Disemba 27 na kuteuliwa kuwa mgombea, nitawajibika kujieleza kwa umma wa wananchi wa Mbeya vijijini katika kampeni. Hivyo leo, sitazungumza nanyi kwa nia ya kupiga kampeni, wakati wake bado. Baadhi yenu hapa, mmenidhamini na kuweka saini zenu katika fomu yangu ya kugombea, kila mmoja kwa wakati wake; kila mmoja akiwa na sababu ya kwanini ameamua kunidhamini. Nichukue fursa hii kuwaeleza, maono yangu kuhusu dhamira yetu ya pamoja, ambayo naamini ndio sababu ya nyinyi kunidhamini na wengine wengi zaidi kunithamini kwa kujitokeza kunisindikiza kwenda kurujesha fomu. Tutaipeleka fomu hii kwa msimamizi wa uchaguzi ambaye ofisi yake ipo Mbeya Mjini kutokana na halmashauri kutokuwa na makao makuu yake ndani ya wilaya yetu; tunahitaji uongozi mbadala utakaotoa msukumo wa kuhakikisha makao makuu ya Mbeya vijijini yanakuwa Mbeya Vijijini.

Taifa letu linapita katika wakati mgumu wenye ombwe la uongozi katika maeneo mbalimbali; ambalo kwa bahati, chini ya mfumo wa vyama vingi kuna tumaini la kupata uongozi mbadala. Ni wajibu huu wa kidemokrasia umenifanya nijitokeze kuchukua fomu ya kugombea; ni wajibu huu huu wa kihistoria ndio unaotufanya leo kujumuika pamoja kunisindikiza kurejesha fomu hii ya kugombea.

Nayakumbuka maneno ya Mwalimu Nyerere niliyojifunza wakati nikiwa shule ya msingi Uyole kati ya mwaka 1977 na 1982; kwamba ili taifa liendelee linahitaji watu, ardhi, siasa safi na uongozi bora. Nikiyatafakari maneno hayo wakati huu; naona watu katika nchi yetu wameongezeka hata hapa Mbeya Vijijini, wakiwa na utamaduni ule ule wa ukarimu. Pamoja na kuongezeka kwa umasikini na gharama za maisha, watanzania wana matumaini ya mabadiliko. Na ongezeko hili la watu, limelazimisha kuwepo mifumo ya kidemokrasia ya uwakilishi; hivyo, fomu hii ninayoipeleka leo, si yangu- ni fomu ya umma, wadhamini waliopo ni wanawakilisha dhamira ya wote wanaotaka niwe muwakilishi wa wananchi wa Mbeya vijini katika Bunge la Tanzania. Kitendo cha kukubali dhamana hiyo, ni ishara ya kuukubali wajibu wa kuwa mtumishi na kiongozi wa watu. Hivyo ndivyo, uongozi wangu utakavyokuwa.

Nikiyatakari maneno hayo, naona ardhi bado tunayo. Tena mkoa wetu wa Mbeya umejaliwa ardhi yenye rutuba na rasilimali. Ni mkoa uliojaliwa ardhi yenye kuzalisha mazao mbalimbali, na ardhi yenye madini mbalimbali. Hali iko hivyo pia hapa kwetu Mbeya Vijijini. Lakini pamoja na hali hiyo, sera za umiliki wa ardhi hazikidhi matakwa ya umma; na katika maeneo ambayo wananchi wamenyanganywa ardhi kwa sababu moja au nyingine wamekuwa wakipata fidia kidogo na wengine wakikosa kabisa. Hata wanaondesha kilimo katika ardhi waliyopo bado tija imekuwa si ya kutosha. Na kwa upande mwingine, rasilimali ikiwemo madini zimekuwa hazitumiki ipasavyo katika kuleta maendeleo. Katika hali hii, mimi niliyepata fursa ya kusoma kwa kodi zenu wananchi wenzangu shahada ya sheria pale Chuo Kikuu cha Dar es salaam na baadaye kwenda kusoma shahada ya pili ya Sheria Chuo Cha Keele Nchini Uingereza, naamini nina deni kwenu. Sehemu ya kulipa deni hilo, ni kutumia taaluma yangu ya uanasheria kuwatetea wananchi wanakosa haki zao ikiwemo haki ya ardhi, lakini pia kutumia uwakili wangu kuwawakilisha wananchi katika vyombo vya kutunga sheria ili kutoa wigo mpana zaidi wa kutetea rasilimali za wananchi wa Mbeya vijijini na taifa kwa ujumla. CHADEMA imeonyesha dhahiri kuwa na wabunge wenye kutetea rasilimali za Taifa, kama Zitto Kabwe na wengine.

Nikiyatafakari maneno hayo; tunakosa mahitaji muhimu mawili ya maendeleo, siasa safi na uongozi bora. Hivyo, tunaongozana leo kwenda kurudisha fomu kama ishara ya kuonyesha dhamira yetu ya pamoja katika kuleta siasa safi na uongozi bora katika Jimbo letu la Mbeya Vijijini na taifa kwa ujumla ili kuunganisha watu watumie ardhi yetu katika kuleta maendeleo.

Tunachokiona leo, ni siasa chafu hususani ndani ya CCM; zenye kuchochea mifarakano, ukabila. Hapa mkoa wa Mbeya zimekuwa zikitokeza katika sura ya makundi ambayo hatimaye yamekuwa yakikwaza maendeleo. Siasa hizi chafu, zimekuwa zikichafua fursa ya baadhi ya watu wazuri katika jamii kushindwa kuchaguliwa kuwa viongozi. Wakati umefika, wa wote wasiopenda siasa chafu, kuunga mkono mabadiliko; bila kujali kabila, chama au hali. Siasa hizo chafu, zinajitokeza pia wakati wa uchaguzi, siasa za kuwahonga wapiga kura, siasa za vitisho kwa wananchi, siasa za uongo na pengine siasa za ushirikina. Leo tunakwenda kurudisha fomu, tukiwa na dhamira ya kuleta tumaini jipya la siasa safi katika mkoa wa Mbeya, siasa za hoja na sera; siasa zenye maadili ya kisiasa. Siasa zenye kuamini kwamba sauti ya watu ni sauti ya Mungu. Na kwa kweli, dhamira hii ya pamoja nilishaanza kuitekeleza miaka mingi nyuma kabla hata ya kuwaza kuwa mbunge. Mathalani, wakati Diwani wa CCM na wananchi wenzake wa kata ya Isuto wa vyama mbalimbali walipobambikiziwa kesi wakati wakiwa katika kuunganisha nguvu kupingana na ufisadi; nilijitolea kuwatetea katika mahakama kama chombo cha usimamizi wa sheria. Dhamira yetu ya pamoja leo ninaporudisha fomu, ni kutaka kuongezewa wajibu wa uongozi, ili niweze kutoa mchango mkubwa zaidi katika kukabiliana na aina zote za ufisadi na matumizi mabaya ya madaraka.

Hatima ya yote, ni siasa hizo safi ndizo zitakazotuletea uongozi bora katika jimbo letu la Mbeya vijijini na taifa kwa ujumla. Uongozi bora unaotambua mahitaji ya watu. Na ili tupate uongozi huo, tuhahitaji kubadili mfumo wa utawala. Ni siasa safi ndizo zitakazoleta uongozi wenye uadilifu utakaotutoa katika utamaduni wa ufisadi. Huu ni uongozi wenye kuelewa kwamba mabadiliko ya Kweli, hayawezi kuletwa na mafisadi wale wale, wa chama kile kile, chenye uoza ule ule, wakiendeleza yale yale kwa ari, nguvu na kasi mpya. Ni muhimu wananchi wote wakatambua kwamba kwa falsafa ya chukua chako mapema, Tanzania yenye neema haiwezekani. Uchaguzi wa Mbeya vijijini ni fursa ya kuongeza tofali lingine katika msingi huo. Naamini wote ambao mmenidhamini na kunisindikiza leo, mmefanya hivyo mkielewa vyema uadilifu wangu na dhamira yangu ya kupambana na aina zote za ufisadi.

Tufike mahali tukubaliane, kwamba ni matatizo ya mfumo wetu wa uongozi ndiyo yametufikisha hapa tulipo. Ambapo, gharama za maisha zimepanda kwa ari, nguvu na kasi mpya. Huku bei ya mafuta ikiwa imeshuka duniani hali ni tofauti Tanzania kutokana na usimamizi mbovu na mzigo wa kodi wenye athari zaidi kwa masikini. Pembejeo na mbolea ya ruzuku ambayo kimsingi si hisani ya serikali bali ni mchango wa kodi yangu mimi na wewe, imepanda bei, chanzo kikuu kikiwa ni ufisadi katika mfumo wa usambazaji. Hata katika mfumo wa kugawiwa pembejeo kwa vocha, mbolea inafikia watu wachache tena hata hao kwa kiasi kidogo. Na katika kipindi hiki cha uchaguzi, tayari mbolea imeanza kutumiwa kisiasa kuwagawa watu na kuwaghilibu. Ni wakati wa wananchi kuamka kuelewa kwamba ni zao la kodi na jasho lao, serikali ni chombo tu cha kuratibu upatikanaji. Na kiongozi wa kuunganisha nguvu hiyo ya pamoja, hawezi kuwa mbunge wa chama ambacho ndio kimeweka mfumo huo mbovu bali mbunge wa kambi ya upinzani. Hivyo, ni wakati wa wananchi wa Mbeya Vijijini kuunga mkono upinzani na kutimiza wajibu wa kihistoria wa kuongeza upinzani bungeni kupitia CHADEMA, chama mbadala.

Ni uongozi bora wa CHADEMA ndio uliowezesha wananchi wa Karatu kupata maji baada ya kuukataa utawala wa miaka mingi wa CCM ulioshindwa kutimiza wajibu wake. Ndio uongozi bora wa CHADEMA wenye sera mbadala ndio uliowezesha kule Tarime watoto wa watanzania wa kawaida kusomeshwa bure kupitia mapato ya kwenye madini. Ni uongozi bora wa CHADEMA uliosukuma kufuta kwa michango ya manyayaso kule Kigoma Ujiji. Sio uongozi unaoweka nguzo za umeme miaka mingi zioze bila ya kuvuta umeme kwa wananchi waliowengi. Sio uongozi unaokusanya michango ya ujenzi wa sekondari kwa manyanyaso na kushindwa kukwepa kusoma kwa wananchi mapato na matumizi ya michango mbalimbali. Hivyo, uongozi mbadala unahitajika Mbeya Vijijini kwa ajili ya kukabiliana na changamoto zinazokabili wilaya yetu na jimbo letu. Uchaguzi wa Januari 25 ni hatua muhimu katika safari yetu ya pamoja na kuelekea katika njia sahihi ya demokrasia na maendeleo.

Tumaini jipya limekuja Mbeya Vijijini, hili ni tumaini la mabadiliko ya kweli. Tumaini la kuwapima viongozi, sio kwa maneno yao tu; bali kwa matendo yao. Ni wakati wa kuwatambua kwa matendo yao. Wale wanaohubiri kupinga dhuluma, huku wakishiriki na kushirikishwa kutoa rushwa ili wachaguliwe kuwa viongozi; tuwatambue kwa matendo yao. Wale wanaojinadi kuwatetea wananchi huku wakiwazunguka na kuwanyanganya ardhi na mali zao bila fidia inayostahili; tuwatambue kwa matendo yao. Wale wanajifu uhuru huku wakirudisha taifa katika ukoloni mamboleo wakutegemea wageni kwa kisingizio cha uwekezaji uchwara wenye kuwanyonya raia; tuwatambue kwa matendo yao. Wale wanaojitangaza kutetea haki za wafanyakazi huku wakiwanyonya wafanyakazi kwa kuwalipa chini ya kima cha chini; tuwatambue kwa matendo yao. Wale wanaohubiri kuwa wacha Mungu mchana na usiku kubariki ushirikina; tuwatambue kwa matendo yao. Mbwa mwitu, hata ajivike ngozi ya kujifunika na kujifanya mchungaji wa kundi la kondoo; tuhakikishe anafichuliwa. Ndio namna pekee ya kurudisha taifa letu katika misingi ya uongozi bora. Tuyasikilize maneno yao, tuyachambue matendo yao; tuuweke bayana uongo wao, na hatimaye ukweli utufanye tuwe huru. Mapambano ya ufisadi yaliyochochewa na harakati za CHADEMA ikiwemo kupitia ile orodha ya mafisadi iliyotolewa na Mbunge Dr Slaa na wenzake, yanapaswa kuungwa mkono na wote wanaochukia ufisadi; halaiki hii inayonisindikiza kurudisha fomu ni ishara ya kuniunga mkono niwe kamanda wa zaida katika mapambano hayo.

Na huu ni wajibu wa pamoja; si wa jibu wangu pekee, wala si wajibu wa nyinyi mlionidhamini na mnaonisindikiza pekee. Nilipokuwa mtoto, baba yangu Mzee Shitambala Mwaifani Mwalyego-mzaliwa Lwanjilo na kuhamia Uyole kwa ajili ya usimamizi wa uchifu; alikuwa akinilea na kunifundisha kuhusu uwajibikaji. Ni malezi haya ndiyo yaliyonifanya hata nilipokuwa Mwalimu pale Sekondari ya Irambo tulikuwa tukiunganisha juhudi na maarifa. Naamini, ni kwa sababu hii niliweza kustaafu jeshi kwa heshima zote nikiwa na cheo cha kapteni ili kunipa fursa ya kuwajibika kwa upana zaidi katika kutumikia umma kama mwanasheria. Ninaposimama mbele yenu leo, mkiwa mmenidhamini na wengine kuamua kunisindikiza kwenda kurejesha fomu; naiona safari ya uwajibikaji wa pamoja tunayoianza katika kuleta demokrasia na maendeleo Mbeya Vijijini. Safari hii inahitaji baraka na kuungwa mkono na machifu wote; bila kujali itikadi, kabila, eneo ama hali hali. Ni mwito wa wajibu wa pamoja wa kutetea haki za wananchi, kukemea maovu na kuhamasisha maendeleo. Ni wajibu wa wazee wanaotaka kuona matunda ya uhuru walioyatazamia yanapatikana kwa kizazi cha sasa na vijavyo. Ni wajibu wa wanawake ambao ni chimbuko la maendeleo na wazazi wa ukombozi. Ni wajibu wa vijana ambao wameona mabadiliko katika mataifa mbalimbali na wamekuwa nguvu ya mabadiliko hayo. Leo nimeeleza hii dhamira ya pamoja ambayo inatuunganisha, leo haikuwa siku ya kampeni; hivyo, nimedokeza tu dhamira yangu, lakini ahadi zangu na za chama changu, kuhusu nini tutawafanyia wananchi wa Mbeya, nitaeleza wakati nazindua kampeni baada ya kupitishwa na Tume ya Uchaguzi kutokana na fomu ninayoipeleka leo nikiwa nanyi. Ni wajibu wa kila mmoja kila mahali, na tuianze sasa safari ya ushindi.

Mungu awabariki kwa kunisikiliza.
 
Upinzani kama hawawezi kuungana kwa maslahi ya Taifa, ushindi wasahau kabisa, maana mpaka mbeya vijijini wanamchagua mtu ambaye hata shule hakufika mbali compared na huyu mwanasheria (ambaye team yake ilimuangusha kwa kutomsaidia kufuata procedures). I hope atajaribu tena. better luck next time.
 
Upinzani kama hawawezi kuungana kwa maslahi ya Taifa, ushindi wasahau kabisa, maana mpaka mbeya vijijini wanamchagua mtu ambaye hata shule hakufika mbali compared na huyu mwanasheria (ambaye team yake ilimuangusha kwa kutomsaidia kufuata procedures). I hope atajaribu tena. better luck next time.

Mwanahabari

Kipi ni kipi sasa? Ameshindwa kuwa kuwa wapinzani hawawezi kuungana au kwa kuwa timu yake ilimuungusha?

Kama ni kuungana mbona Tarime hawakuungana lakini bado Mwera wa CHADEMA akashinda?

Nakwambia hata huyu Shitambala angeshinda uchaguzi hata kama wapinzani wasingeungana kama isingekuwa lile pingamizi.

Asha
 
Shitambala kwa Msimamizi wa Uchaguzi-akizungumzia pingamizi la CCM kwa kushirikiana na CUF:


Mimi naamini kwamba wananchi wa Mbeya Vijijini hawahitaji kiongozi anayezusha ili apewe ushindi wa mezani. Mimi niko tayari kupambana kwa kura na si technicalities za kubuni. Huu ni wakati wa tumaini jipya la mabadiliko katika taifa letu lenye kuhitaji siasa safi na uongozi bora. Hivyo, mapingamizi haya yapaswi kuwa kikwazo kwa dhamira yangu ya kuwatumikia wananchi na nia ya wananchi ya kuchagua Mbunge mwenye msimamo wa kupambana na aina zote za ufisadi na kutetea rasilimali za Taifa.


Shitambala wa Tume ya Uchaguzi-akitaka Tume itumie mamlaka yake kuwapa wananchi wagombea wote:

KWAMBA msimamizi wa uchaguzi amekosea kisheria kwa kushindwa kuelewa hali halisi ya demokrasia ya vyama vingi na mahitaji ya wapiga kura wa jimbo la Mbeya Vijijini kwa kuwanyima haki ya kuwa na uwanja mpana wa uchaguzi kwa ridhaa yao. Kuniengua mimi ni kulazimisha watu wa Mbeya Vijijini kuchagua vyama ama wagombea waliobakia ambapo ni kinyume cha Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Ninaomba tume izingatie kifungu 38(1)(4)(proviso) cha sheria ya uchaguzi namba ya mwaka 1985.

Chanzo: Mbeya vijijini: Kampeni, uchaguzi na yatokanayo - Page 40 - JamiiForums.com
 
Upinzani kama hawawezi kuungana kwa maslahi ya Taifa, ushindi wasahau kabisa, maana mpaka mbeya vijijini wanamchagua mtu ambaye hata shule hakufika mbali compared na huyu mwanasheria (ambaye team yake ilimuangusha kwa kutomsaidia kufuata procedures). I hope atajaribu tena. better luck next time.

Wewe hajachaguliwa huyo; amepata asilimia 20 ya asilimia kama 27 waliopiga na 7 zimenda upinzani ulikuwepo; aislimia zote zilizobaki zinamsubiria shitambala 2010; ndio maana hawakuenda kupiga hata kura; ni haki yao kwa nini wajisumbue bure; sasa subiria moto utawaka zidi; hakuna kuungana ni wizi mtupu; kila chama chene sera kinasonga mbele wengi mamluki tu
 
Dah, inaelekea Shitambala ni mzuri sana kwa risala.

CCM imefanya kosa sana kumtoa/kumwekea pingamizi kwenye kinyang'anyiro cha Ubunge wakati huu. Ubunge wenyewe ni wa mwaka mmoja tu. Ila mtaji anaoelekea kuuvuna Shitambala ni mkubwa sana. Mwaka 2010, CCM itaona ilichokipanda wakati huu kwa gharama kubwa. Maana wamemjenga sana kisiasa mtu huyu. Hii si mara ya kwanza kwa CCM kufanya makosa kama haya. Mara ya kwanza ilikuwa bungeni walipompa adhabu Zitto Kabwe. Jamaa ndipo alipojizolea ubingwa wa nguvu zaidi. Inaelekea CCM inaanza kuishiwa wataalamu wa siasa.
 
Back
Top Bottom