Che Kalizozele
JF-Expert Member
- Jul 20, 2008
- 777
- 49
Deusdedit Jovin
Januari 7, 2009
NIMESOMA taarifa ya Askofu wa Jimbo Katoliki la Rulenge-Ngara, Severine NiweMugizi, iliyotolewa kwa maelekezo ya Mamlaka Kuu ya Kanisa Katoliki iliyoko Roma, na kuchapishwa katika gazeti la Kiongozi, toleo namba moja la mwaka 2009, kuwa hivi sasa Privatus Karugendo ni mwamini mlei asiye na daraja la upadre kuanzia tarehe 14 Septemba 2008 ilipotolewa Hati ya Baba Mtakatifu yenye namba ya protokali 4182/08.
Hata hivyo, kwa mujibu wa Katekisimu Mpya ya Kanisa Katoliki: Ni kweli, aliyepewa Daraja (la upadre) halali aweza, kwa sababu kubwa, kuruhusiwa kuacha wajibu na kazi zinazohusiana na Daraja; au anaweza kuzuiliwa asitekeleze. Lakini hawezi kurudia katika hali ya mlei kwa maana halisi, kwa sababu alama iliyochapwa kwa kupewa daraja ya dumu daima. Wito na utume unaopokewa siku ya kupewa Daraja (la upadre) humtia alama ya kudumu.
Hivyo basi, kwa kuzingatia nukuu hiyo ya Katekisimu ya Kanisa Katoliki kifungu cha 1583, wito na utume unaopokewa siku ya kupewa Daraja (la upadre) humtia alama ya kudumu mhusika hadi kifo chake.
Na kwa sababu ya dosari hii ya kimantiki kama inavyojionyesha kwenye hukumu ya Papa Benedikto wa XVI, mtu yeyote anaweza kushawishika na akaamini kwamba huenda hata sababu zilizotolewa kama msingi wa kumwondoa Padre Privatus Karugendo kutoka katika hali ya utumishi wa kipadre zinayo dosari kama hii.
Hivyo, kwa lengo la kuweka kumbukumbu za kihistoria sawasawa kwa faida ya kizazi hiki na vizazi vijavyo, bila kupinga uhalali wa hukumu ya Baba Mtakatifu na Mahakama ya Kanisa iliyochunguza kesi hii, nakusudia kudodosa muundo wa kimantiki wa hoja zake, kuzifafanua hoja hizo, na hatimaye kuzihakiki kwa lengo la kubaini iwapo zinakidhi viwango vya kitaaluma na kiimani au kinyume chake.
Kutokana na sababu zilizotolewa katika gazeti ka Kiongozi, ni wazi kwamba, upotofu wa imani anaohusishwa nao Padre Karugendo unahusu maadili katoliki ya kijinsia (catholic sexual ethics).
Hivyo, ni muhimu sana hapa kuyafupisha maadili hayo ili ufupisho huo uweze kuwa msingi wetu hapo baadaye wakati wa kuzinyumbulisha na kuzifafanua sababu zilizotumiwa kumtimua Padre Karugendo.5
Kimsingi, maadili Katoliki ya Kijinsia yanaweza kufupishwa mara moja katika kanuni tatu pekee kama ifuatavyo:
Kanuni ya kwanza kuhusu maadili katoliki ya kijinsia inasema kwamba, tendo lolote la kupeana zawadi ya mwili lazima lifanyike ndani ya ndoa ya mwanamume na mwanamke pekee.
Kanuni hii maana yake ni kwamba, ni mwiko tendo lolote la kupeana zawadi ya mwili kufanyika nje ya ndoa ya mwanamume na mwanamke.
Kanuni ya pili kuhusu maadili katoliki ya kijinsia inasema kwamba, mara zote tendo la kupeana zawadi ya mwili kati ya mwanamume na mwanamke lazima lifanyike katika namna ambayo itaruhusu kutungwa kwa mimba iwapo yai la kike ni pevu.
Kanuni hii maana yake ni kwamba, ni mwiko kwa tendo la kupeana zawadi ya mwili kati ya mwanamume na mwanamke kufanyika katika namna ambayo haitaruhusu kutungwa kwa mimba wakati yai la kike ni pevu.
Na kanuni ya tatu ambayo ni kanuni ya maadili katoliki katika ujumla wake inasema kwamba, waumini wanawajibika kuutii uamuzi unaofanywa na maaskofu wao katika jina la Kristo, kuhusu masuala yote ya imani na maadili, na kisha kuushika uamuzi huo kwa moyo mmoja.
Kanuni hii maana yake ni kwamba, ni mwiko kwa waumini wanaowajibika kuutii uamuzi uliofanywa na maaskofu wao katika jina la Kristo, kuhusu masuala yote ya imani na maadili, kuukaidi uamuzi huo katika namna ambayo inaonyesha utovu wa nidhamu kwa maaskofu hao.
Kinachoruhusiwa na kanuni hii ni kwamba muumini anaweza kujizuia kutii uamuzi wa maaskofu pale anapokuwa na shaka juu yake, lakini bila kuyapinga waziwazi, na wakati huo akaendelea kufanya uchunguzi zaidi, huku akiwa na utayari wa kukubali uamuzi wa mwisho wa maaskofu kuhusu suala husika.
Kutokana na kanuni hizo tatu hapo juu, inafuata kimantiki kwamba matendo yafuatayo ni haramu kwa mujibu wa maadili katoliki:
Tendo la kupeana zawadi ya mwili nje ya ndoa kwa ajili ya kuingiza tupu ya kiume kwenye tupu ya kike (adultery); tendo la kupeana zawadi ya mwili kabla ya ndoa kwa ajili ya kuingiza tupu ya kiume kwenye tupu ya kike (fornication); tendo la kupeana zawadi ya mwili kwa ajili ya kuingiza tupu ya kiume kwenye tupu ya nyuma ya binadamu (sodomy);
Aidha, matendo yafuatayo ni haramu kwa mujibu wa maadili katoliki: tendo la kupeana zawadi ya mwili kwa ajili ya kusisimua tupu za mbele kwa kutumia vidole (masturbation); tendo la kupeana zawadi ya mwili kwa ajili ya kusisimua tupu ya mbele ya mwanamume kwa kutumia mdomo (fellatio); tendo la kupeana zawadi ya mwili ambapo angalau mmojawapo amekula kiapo cha useja; tendo la kupeana zawadi ya mwili ambapo angalau mmojawapo amevaa kondomu kwenye tupu yake ya mbele (condomised intercourse).
Kadhalika, tendo la kuunga mkono matendo haya yanayoitwa haramu kimaadili kwa mujibu wa imani katoliki au matendo yanayofanana nayo (theological and doctrinal dissent) ni haramu kimaadili.
Na sasa basi, kutokana na hitimisho hili kuhusu maadili katoliki ya kijinsia, tunaweza kuzielewa zaidi sababu zilizotoloewa na Papa Benedikto wa XVI kama chanzo cha kutimuliwa kwa Padre Privatus Karugendo.
Na katika muktadha huu, uchanganuzi unaonyesha kwamba Baba Mtakatifu amemtimua Padre Karugendo, angalau, kwa sababu kuu sita:
Kwanza, Baba Mtakatifu anasema kwamba, wakati maadili katoliki ya kijinsia yanasema kwamba ni mwiko tendo lolote la kupeana zawadi ya mwili kufanyika nje ya ndoa ya mwanamume na mwanamke, Padre Privatus Karugendo anawahimiza vijana ambao hawajaoana kutumia kondomu kama kinga dhidi ya maambukizi ya virusi vya ukimwi (VVU) kila wanapoamua kwa hiari yao wenyewe kujinufaisha na haki yao ya kupeana zawadi ya mwili, na hivyo kupotosha maadili katoliki.
Pili, Baba Mtakatifu anasema kwamba, wakati maadili katoliki ya kijinsia yanasema kwamba ni mwiko tendo lolote la kupeana zawadi ya mwili kufanyika nje ya ndoa ya mwanamume na mwanamke, Padre Privatus Karugendo anawahimiza wanandoa kutumia kondomu kama kinga dhidi ya maambukizi ya VVU kila wanapoamua kwa hiari yao wenyewe kuchepuka nje ya ndoa kwa lengo la kuhemea zawadi ya mwili, na hivyo kupotosha maadili katoliki.
Tatu, Baba Mtakatifu anasema kwamba, wakati maadili katoliki ya kijinsia yanasema kwamba ni mwiko tendo lolote la kupeana zawadi ya mwili kufanyika nje ya ndoa ya mwanamume na mwanamke, Padre Privatus Karugendo anawahimiza watawa waliokula kiapo cha useja kutumia kondomu kama kinga dhidi ya maambukizi ya VVU na mimba zisizotarajiwa kila wanapoamua kwa hiari yao wenyewe kuchepuka nje ya kiapo chao kwa lengo la kuhemea zawadi ya mwili kwa muda, na hivyo kupotosha maadili katoliki.
Nne, Baba Mtakatifu anasema kwamba, wakati maadili katoliki ya kijinsia yanasema kwamba ni mwiko tendo lolote la kupeana zawadi ya mwili kufanyika nje ya ndoa ya mwanamume na mwanamke na kwamba ni mwiko kwa tendo la kupeana zawadi ya mwili kati ya mwanamume na mwanamke kufanyika katika namna ambayo haitaruhusu kutungwa kwa mimba wakati yai la kike ni pevu, Padre Privatus Karugendo anawahimiza vijana ambao hawajaoana kutumia kondomu kama kinga dhidi ya mimba zisizotarajiwa kila wanapoamua kwa hiari yao wenyewe kujinufaisha na haki yao ya kupeana zawadi ya mwili, na hivyo kupotosha maadili katoliki.
Tano, Baba Mtakatifu anasema kwamba, wakati maadili katoliki ya kijinsia yanasema kwamba ni mwiko kwa tendo la kupeana zawadi ya mwili kati ya mwanamume na mwanamke kufanyika katika namna ambayo haitaruhusu kutungwa kwa mimba wakati yai la kike ni pevu, Padre Privatus Karugendo anawahimiza wanandoa kutumia kondomu kama kinga dhidi ya mimba zisizotarajiwa kila wanapoamua kwa hiari yao wenyewe kujinufaisha na haki yao ya kupeana zawadi ya mwili, na hivyo kupotosha maadili katoliki.
Na sita, Baba Mtakatifu anasema kwamba, wakati maadili katoliki yanasema kwamba, waumini wanawajibika kuutii uamuzi unaofanywa na maaskofu wao katika jina la Kristo, kuhusu masuala yote ya imani na maadili, na kisha kuushika uamuzi huo kwa moyo mmoja, Padre Karugendo ameandika makala nyingi kwenye magazeti akiwajulisha waumini wenzake na viongozi wa Kanisa Katoliki maoni yake juu ya kile kinachohusu Kanisa lakini bila kuzingatia ukamilifu wa maadili na imani ya Kanisa wala heshima kwa viongozi wake na waamini kwa ujumla, jambo ambalo linamaanisha kwamba amekiuka mafundisho ya imani katoliki yanayokataza uasi wa wazi dhidi ya mamlaka halali.
Hatimaye, kutokana na sababu hizi sita, Baba Mtakatifu anasema kwamba, kwa mujibu wa sheria za Kanisa Katoliki, kila kosa lililotendwa na Padre Privatus Karugendo adhabu yake ni kutimuliwa kutoka katika huduma ya upadre. Hivyo, amehitimisha kwamba ni halali kwake kumtimua Padre Privatusi Karugendo, uamuzi ambao hauna rufaa dhidi yake.
Hata hivyo, sisi waumini wa kanuni ya kuona, kuhukumu na kutenda yatupasayo, kanuni ambayo inatukuzwa sana na Baba Mtakatifu, hatuwezi kuishia hapo. Kuna maswali mawili muhimu lazima yajibiwe kitafiti.
Swali la kwanza ni hili: je, utaratibu uliotumika kumtimua Padre Privatus Karugendo ni halali kwa mujibu wa taratibu za Kanisa Katoliki? Na swali la pili ni hili: je, sababu zilizotolewa kama msingi wa kutimuliwa kwa padre Privatus Karugendo ni sahihi?
Katika ajira yoyote, mwajiri anapomtimua kazi mwajiriwa, na mwajiriwa akakata rufaa dhidi ya uamuzi wa mwajiri, wasuluhishi (mediators, arbitrators and adjudicators) hutafuta kujibu maswali haya mawili. Na kwa kweli taarifa kwamba hakuna rufaa dhidi ya uamuzi wa Papa zinatuhimiza kuchunguza jambo hili kwa kina.
Hili ni lazima kwa mtu yeyote anayemwabudu Mungu wa haki za binadamu. Na kwa kuwa Kanisa Katoliki linajinadi kama taasisi inayokuza na kuhami haki hizo tunatarajia itaharakisha kuweka bayana mambo haya. Vinginevyo, uamuzi wa Papa Benedikto wa kumi na sita unaweza kuwa ni pigo kubwa sana kwa Kanisa Katoliki.
Katika makala zijazo nitachunguza mambo haya kwa kina kabisa. Na kwa kuanzia nitachunguza uhalali wa kanuni mbili. Kanuni moja ni inayosema kwamba ni mwiko tendo lolote la kupeana zawadi ya mwili kufanyika nje ya ndoa ya mwanamume na mwanamke.
Na kanuni nyingine inasema kwamba ni mwiko kwa waumini wanaowajibika kuutii uamuzi uliofanywa na maaskofu wao katika jina la Kristo, kuhusu masuala yote ya imani na maadili, kuukaidi uamuzi huo katika namna ambayo inaonyesha utovu wa nidhamu kwa maaskofu hao.
Usahihi wa kanuni hizi mbili zikishapembuliwa vizuri uchambuzi mwingine kuhusu sababu za kumtimua Padre Karugendo unakuwa ni rahisi.
Simu:
0734 800808
0734 800808
Last edited by a moderator: