Elections 2010 Sababu kumi za kutompigia jakaya kikwete kura 2010

PillowTalk

Member
Sep 24, 2010
95
5
Uchaguzi wa mwaka huu ni tofauti sana na chaguzi zilizopita kwa vile kwa maoni yangu nchi yetu iko katika njia panda.Kiuchumi,kisiasa na kijamii.Nina sababu za kutomchagua mgombea wa CCM kwa kila nyanja niliyoizungumzia.Na ni vyema niseme tangu awali kuwa mwaka 2005 nilimchagua Kikwete.
Huu ndio uchambuzi wangu:

  1. Ameendekeza siasa za chuki na utengano.Hili linathibitishwa na jinsi alivyofanikiwa kukigawa chama chake mwenyewe kiasi kwamba hakimpi msaada anaostahili mgombea kwa tiketi ya chama.Kukosekana kwa viongozi wenzake waandamizi katika chama kwenye kampeni zake,madai ya kuhamisha ofisi za kampeni kutoka ilipo ofisi ndogo ya CCM Lumumba kwenda maeneo ya upanga,Kushirikisha watoto wake na mkewe katika masuala mazito ya kitaifa.Hizi zote ni dalili za kiongozi asiyekubalika hata ndani ya chama chake mwenyewe!Kiongozi asiye ambilika namna hii hatufai hata kidogo.Ni hatari kwa ustawi wa taifa letu.
  2. Ameshindwa kusimamia uchumi wa taifa.Mfumuko wa bei ni wa juu mno,bei za kila aina ya bidhaa zimepanda maradufu.Rais haonekani kuliona hili wala kutupa mwelekeo wa nini kinafanyika katika kurekebisha hii hali.Nimekuwa nikifuatailia mikutano yake ya kampeni ili kubaini jinsi anavyokerwa na hili swala lakini nasikitika kusema kuwa inaonekana kwake hii si tatizo.Anapoteza muda wa maana kuzungumzia mambo yasiyo na tija kwetu wananchi na anaacha mambo ya msingi sana.Maendeleo yeyote yasiyoniletea mimi unafuu na uwezo mkubwa zaidi wa kukabiliana na changamoto za maisha yangu katika uhalisia wake hayana maana.
  3. Kukithiri kwa rushwa na kasi isiyoridhisha ya kupambana na ufisadi.Hapa Rais Kikwete ametupoteza wengi wetu tuliokuwa na matumaini naye.Kitendo cha yeye kuamua kuwasafisha hadharani watu ambao yeye mwenyewe ameshiriki kutuaminisha kuwa si wasafi kwa kuwafungulia mashtaka na au kuwaondoa katika utumishi wa umma kinatoa picha moja tu.Kuwa atakapo takiwa kuchagua,Rais wetu yuko radhi kuangalia maslahi yake binafsi na ya kikundi kidogo cha mafisadi kuliko maslahi ya sisi wananchi wengi.Vinginevyo asingethuduti kutudhihaki kwa kejeli ile.
  4. Kushindwa kusimamia misingi ya utawala bora na utawala wa sheria.Katika kipindi cha miaka mitano iliyopita nchi yetu imeshuhudia ukiukwaji mkubwa wa utawala wa sheria.Tumejionea jinsi baadhi ya watu walivyo kingwa ili mkondo wa sheria usipite.Mifano ni mingi na sina haja ya kuirudia.Kitendo cha hivi karibuni cha kuwanyima wafanyakazi haki yao ya kikatiba ya kugoma kutokana na kutoridhishwa na mazingira duni ya kazi na mishahara isiyokidhi mahitaji tena kwa vitisho na kejeli ni dalili ya kiongozi ambaye amepoteza uhalali wa kuongoza kidemokrasia.Pia Kikwete ameingilia sana utawala wa sheria kwa kuingilia mamlaka na kazi za mahakama.Mfano ni jinsi alivyo mpandisha jukwaani Mwakalebela mjini iringa ilihali Mwakalebela anakabiliwa na kesi mahakamani inayohusiana na tuhuma za rushwa wakati wa kura za maoni za CCM.
  5. Kushindwa kudhibiti ufujwaji wa fedha za umma.Nadhani Kikwete ataongoza kwa kuwa Raisi aliyesababisha upotevu mkubwa zaidi wa fedha za umma kwa kutochukua hatua!Mbali na ripoti mbalimbali za kimahesabu zilizokwisha kutolewa huko nyuma ambazo idadi ya fedha zilizoibwa inatia kizunguzungu.Hivi majuzi Mthibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali amesema katika ripoti kuwa mwaka huu pekee kutokufuatwa kwa taratibu za manunuzi kumesababisha upotevu wa shilingi Bilioni 2.8 (Tshs 2,897,251,674) Hakuna hata mtu mmoja mbaye amefunguliwa mashtaka juu ya hili!
  6. Kutosimamia uwajibikaji katika serikali.Kwa vile Rais ni kiongozi mkuu wa serikali kuanguka kwa uwajibikaji serikalini lazima kuhusishwe na Rais mwenyewe.Hata pale ilipoonekana hadharani kuwa raisi anapaswa kuchukua hatua za kuwawajibisha watendaji wabovu serikalini yeye amebaki kimya!Mfano ni uchakachuaji wa mafuta mpaka magari yake mwenyewe!,Udanganyifu mkubwa unaofanywa na watumishi ikulu (Rejea kusaini sheria ya matumizi ya fedha za uchaguzi iliyochakachuliwa!),Magari ya wagonjwa hewa n.k(Inasemekana Raisi huyu ameongoza kwa kudanganywa na wasaidizi wake!)Huu si upole….Ni udhaifu wa kiuongozi ambao ni hatari kwa kiongozi mkuu wa nchi!
  7. Kuwadanganya watanzania kwa nia ya kuwagawa kwa misingi ya dini na kikabila.Hivi karibuni katika ziara za kampeni mikoa ya kusini Rais amezungumzia sasa hatari ya viongozi kuchochea udini na ukabila.Akaenda mbali zaidi na akakemea propaganda za kichochezi.Mwanzoni mwa wiki hii,wakati akihutubia kwenye kilele cha maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka 11 tangu muassisi wa taifa hili afariki dunia Rais Kikwete aliwaelezea hao wanaoeneza meseji hizo kuwa ni watu hatari kwa umoja na usalama wa Taifa.Akasema hii sio njia sahihi ya kutafuta kura kwa vile ingeweza kusababisha matatizo zaidi. “Nafikiri hili tatizo lina kuwa kubwa zaidi…Viongozi hawawezi kupimwa kwa matusi au lugha mbaya dhidi ya wapinzani wako..Hii inaonyesha kuwa watanzania wameanza kubaguana wao kwa wao” Lakini hivi karibuni imethibitika kuwa yeye mwenyewe ndiye kinara wa uchochezi huo.Chama anachokiongoza kimetuma message futi za simu kwa watu zikiwa na ujumbe wa kichochezi na unaolenga kumchafua mgombea wa Chadema.Meseji hizo si chache,ni zaidi ya milioni tano(5) kwa mtandao wa Vodacom pekee. Wataalamu wa teknohama wamethibitisha chanzo na muhusika wa sms hizo.Na kibaya zaidi ni kuwa muhusika anayeitwa Rashid Shamte ana uhusiano wa karibu na CCM.Ushahidi wa kimazingira unaonyesha kuwa kuna uhusiana kati ya tovuti ya JK na tovuti zingine zilizotumika kama inavyoonyesha na hapa nakukuu "
    Kikwete2010.co.tz is a domain controlled by two name servers at co.tz. Both are on different IP networks. The name server kikwete2010.co.tz stated in SOA record is not in the list of name servers. Incoming mail for kikwete2010.co.tz is handled by two mail servers also at co.tz. Both are on different IP networks. kikwete2010.co.tz has one IP number (41.77.226.253).212.233.84.in-addr.arpa, 229.77.41.in-addr.arpa, 228.77.41.in-addr.arpa and 227.77.41.in-addr.arpa share name servers with this domain. 6telecoms.co.tz share mail servers with this domain.”Hata gazeti la The Guardian limethibitisha hayo na wahusika hawajachukuliwa hatua zozote za kisheria!
  8. Kutoa ahadi nyingi mno zisizotekelezeka.Kwa mtu mwenye akili ni lazima upime uwezo wa unaowazungumza ili nawe uzungumze katika upeo unaofanana.Kikwete amekuwa akitoa ahadi za ajabu na zisizo na mantiki kwa mtu mzima mwenye fikra zake!Mwalimu Nyerere aliwahi kusema kuwa mtu mzima akikuambia jambo la kijinga na wewe unajua ni jambo la kijinga na ukakubali….Anakudharau…Mimi nafikiri Kikwete anawadharau watanzania.Mfano mdogo huu hapa:anasema atampatia kila mwanafunzi Computer ambayo imeunganishwa na mtandao wa internet!Lakini je hili linawezekana katika kipindi cha miaka mitano ijayo?Anzia umeme,ni 10% tu ya watanzania wanapata umeme na 0.05% ya watanzania ndo wanaweza kutumia computer na wana weza kupata mtandao!!Anatudharau kwa kukubali kitu ambacho tunajua ni cha kijinga kwa hali yetu ya sasa.Hadi sasa inakadiriwa kuwa Kikwete ameshatoa ahadi zinazofikia Tshs 60 trilioni wakati bajeti ya serikali kwa mwaka ni Tshs 3.4 trilioni!
  9. Kuwadanganya watanzania kuwa elimu bure haiwezekani!Serikali ya Kikwete imeshindwa kutoa elimu bure au hata kuboresha ubora wa elimu inayotolewa sasa kwa vile elimu si kipaumbele cha serikali hii.Serikali hii imeshindwa hata kuratibu na kusimamia mfumo wa elimu unaotolewa na shule za binafsi kiasi kwamba ada za shule hizo hazina udhibiti,viwango vya elimu havidhibitiwi,sifa za waalimu na wakufunzi hazidhibitiwi,Kwa ujumla serikali ya Kikwete imeshindwa kusimamia mfumo wetu wa elimu hata katika mazingira ya sasa!Nasema Kikwete amewadanganya watanzania kwa vile ni kutokuwa makini kwa serikali yake kunakopoteza mabilioni ya shilingi bure mfano:Mwaka huu pekee serikali ya kikwete imeshatoa misamaha ya kodi inayofikia shilingi bilioni 695 sawa na asilimia 2.3 ya bajeti yote ya mwaka huo.Wakati serikali inapoteza pesa nyingi hivyo kwa misamaha isiyo na tija bado inatarajia kukopa shilingi trilioni 1.3 kutoka mashirika ya fedha ya nje! Nchi kama Malawi,Burundi,Kenya,Uganda na Zambia zote zinatoa aina fulani ya elimu ya bure mpaka walau kidato cha nne au sita na kwa lazima!Pia kuna mfumo wa kutoa elimu bure unaotumika katika nchi kama Finland,Denmark,Ujerumani na Sweden.Pia naomba ieleweke kuwa elimu bure haimaananishi bila gharama!Inamaananisha kuwa gharama za kuwasomesha watoto wa taifa hili zitabebwa na taifa zima na si mzazi mmoja mmoja kwa vile uwekezaji katika elimu ni wa manufaa ya taifa zima!Sote tutachangia kwa kodi zetu kufanikisha hili.Isitoshe elimu bure haimaananishi kuwa serikali ijayo itafuta shule na taasisi za elimu za binafsi,La hasha!Wazazi wenye uwezo na utashi wa kuwasomesha watoto wao katika shule za binafsi wataruhusiwa kuendelea kufanya hivyo.Cha msingi hapa ni kuwa shule za umma zitakuwa bure,zenye ubora na zitakazo kidhi mahitaji ya elimu endelevu ili elimu iwe chachu ya maendeleo ya taifa letu!
10.Na mwisho nitamnyima kura yangu kwa vile ameninyima haki yangu ya msingi ya kupata nafasi ya kumpima kwa kumlinganisha na wagombea wengine wa nafasi ya urais kwa kukwepa mdahalo au aina nyingine yeyote ya mahojiano ambayo watazamaji au wasikilizaji watapata fursa ya kuuliza maswali na au kushiriki (Interractive dialoque).Kuna lingine kubwa zaidi.Kitendo cha CCM kuwakataza wagombea wake kushiriki katika midahalo ya aina yoyote ni kitendo cha dharau isiyo na kifani.Hii ni kwa sababu hawa ni viongozi ambao wakichaguliwa watasimamia mustakabali wa uchumi wetu na nchi yetu .Kukataa kuongea na sisi ili tuwafahamu na kuwapima kwa kuwapambanisha na wagombea wa vyama vingine ni sawa na kutuambia kuwa CCM iko juu yetu!Kwamba tunataka tusitake wanao uwezo wa kutuletea wanaye mtaka na wana uwezo wa kuhakikisha anapita hata bila ya ridhaa yetu!Wanatunyima nafasi ya kuwaona na kuwapima wale wanaotaka kupewa fursa ya kuiongoza nchi yetu miaka mitano ijayo.Ninataka na nina haki ya kuona uwezo wa wagombea katika kujenga hoja na si kupiga porojo majukwaani kama viongozi wa dini wasioulizwa swali wala kujibiwa!!





:israel:


"True freedom must be expressed through the human ability to think critically, to analyze and to make informed decisions about oneself, his society and the world "- Sidanganyiki2010
 
Back
Top Bottom