Ghazwat
JF-Expert Member
- Oct 4, 2015
- 23,718
- 66,262
Wakazi wa Kijiji hicho walijikuta katika taharuki kubwa, baada ya tembo wapatao tisa kuvamia kijiji hicho wakitokea Pori la Akiba la Lwafi.
Wakizungumza na chanzo hiki wananchi hao walisema, tembo hao waliingia kijijini hapo jana saa mbili asubuhi na walilazimika kujifungia ndani na watoto wao kwa kuogopa madhara.
Mmoja wa wananchi hao, James Katiya, alisema baada ya tembo hao kuonekana katika kijiji hicho, wakazi wote kijijini hapo walipata hofu na wengi wao kujifungia ndani huku wachache wakitumia mwanya huo kuwapiga picha tembo hao kitu ambacho kiliwaweka hatarini.
Alisema mmoja wa watu aliokuwa katika harakati za kupiga picha, alifukuzwa na tembo na alipomkaribia alimfunika tembo huyo usoni kwa koti alilokuwa amelivaa, hali iliyosababisha tembo kupoteza mwelekeo, hivyo kunusurika kuuawa na tembo huyo.
Diwani wa Kata hiyo, Egid Ngomeni, alisema baada ya kupata taarifa za kijiji hicho kuvamiwa na tembo, alitoa taarifa kwa Halmashauri ya wilaya na pori la Akiba la Lwafi na baada ya muda askari wanyama pori wa halmashauri na wale wa hifadhi ya pori la akiba la Lwafi walifika eneo la tukio.
Alisema kuwa askari hao walifanikiwa kuwaswaga tembo hao na kuwarudisha katika pori la akiba la Lwafi, ingawa alisema hakuna mtu aliyejeruhiwa.
Kaimu Mkuu wa Pori la Akiba la Lwafi, Ramadhani Abdul, alidai askari wapo kazini kuendelea kuwarudisha tembo hao ndani ya pori.
Abdul alisema kuwa kwa sasa wanyama pori wameongezeka sana katika maeneo ya vijiji, na kwamba huenda tembo walikivamia kijiji hicho kutokana na kusogea karibu sana na hifadhi hiyo kinyume cha sheria.
Alisema sheria ya Hifadhi ya Wanyama Pori kifungu cha 74 namba 5 ya mwaka 2009 haitekelezwi licha ya kuwataka watu waishi mita 500 kutoka katika mpaka wa hifadhi.
Abdul alifafanua zaidi kuwa licha ya askari hao kuendelea kuwarudisha tembo hao kwenye pori la akiba, pia wanatoa elimu kwa jamii kuhusu sheria hiyo.