Riwaya ya mikataba ya kishetani na Ben Mtobwa

nameless girl

JF-Expert Member
Apr 22, 2012
4,195
2,658
  • 1
    ALIKUWA mwanamke! Tena mwanamke wa haja! Alisimama pale, uso wake
    ukiwa umeelekezwa kwangu; kama anayesubiri nifanye kazi yangu! Naapa kuwa, kwa mara ya
    kwanza, katika maisha yangu ya udunguaji, nilisita kubonyeza tufe la mwanangu, AK 47 ambaye
    nilimpenda kuliko wanangu wengine wote niliopata kuwatumia.
    Alikuwa pale, kasimama, huku uso wake ukielekea kwangu mara kwa mara.
    ‘Ananisubiri!’ Niliwaza.
    Sikujua kwa nini nilisita. Maelekezo yote niliyopewa yalikuwa barabara; atakua amevaa
    suruali ya kitambaa, yenye rangi nyeusi na koti lake la rangi ile ile juu ya shati yenye rangi ya
    bendera ya taifa. Atatoka nje ya mlango wa hoteli saa nne na robo, akiwa katikati ya Rais wa
    Nchi kulia kwake na mgeni wake, bilionea wa viwanda na machimbo ya madini upande wa pili.
    Pale mlangoni watasita kidogo kuagana kabla ya kuelekea kwenye hafla maalumu. Mwondoe
    akiwa pale pale mlangoni.
    Maelekezo yalikuwa sahihi. Muda ulikua uleule uliopangwa. Na zaidi ya yote mavazi,
    yalikuwa yaleyale yaliolekezwa. Wala si hayo tu, mamilioni ya dau langu lililolipwa katika fedha
    za kigeni tayari yalikuwa yamekwisha ingia kwenye akaunti yangu ya benki wiki moja iliyopita
    na kuhamishiwa katika benki mbalimbali, kwa majina tofauti, kabla ya sehemu ya pesa hizo kuja
    Dar es Salaam kwa matumizi yangu madogo madogo.
    Purukushani za wapiga picha wa televisheni na magazeti zilikuwa nyingi. Kila mmoja
    alikuwa akihangaikia kupata picha bora zaidi, ama ya Rais ama ya mgeni, au wote kwa pamoja.
    Vichwa vyao na kamera zao zilipita mbele yao kwa namna iliyonifanya nipoteze shabaha. Lakini
    hilo lisingenizuia. Walengwa wangu walikuwa juu ya wapiga picha kwa ngazi moja. Isitoshe,
    mimi ni mtaalamu. Sekunde moja tu ya kutikisa kichwa ilitosha kabisa kumdungua muhanga
    wangu bila tatizo.
    Hata hivyo, nilisita kumtekenya mwanangu.
  • Kitu gani basi kilifanya nisite kumbonyeza kidogo tu mwanangu ili nimalize kazi hiyo na
    kuendelea na ziara yangu ya kutembelea ziwa Tanganyika ambako nilikusudia kuwinda viboko
    kijiji cha Buhingu na kisha kuwashuhudia sokwe wa milima ya Kasoge? Kitu gani kiliutia uzito
    moyo wangu wa kishetani, ambao daima ulifurahia kuiona risasi yangu ikimpaisha mtu angani
    na kisha kumdondosha chini huku akiwa tayari ametokwa na uhai wake? Kitu gani? Kitu gani?
    Kitu ga…
    Mara nikakumbuka. Zilikuwepo sababu nyingi, kubwa zikiwa mbili. Ya kwanza, ilikuwa
    urahisi wa kazi hii. Katika maisha yangu haya, sijapata kazi rahisi kama hii, upewe hela nyingi
    Zaidi ya ambazo ungeomba, upewe wajihi wa mtu unayetakiwa kumwondoa, siku, saa na vazi
    atakalokuwa amevaa! Ilikuwa nyepesi mno. Natumaini ni wepesi huo ulionitia mchecheto kiasi
    cha kunifanya nisite kufanya vitu vyangu.
    Sababu ya pili, mhanga wangu alikuwa mwanamke, tena mzuri! Sijapata kumuua
    msichana mzuri kama huyu wala kuombwa kumuondoa duniani mwanamke. Hili pia lilinikoroga
    kichwa.
    Kulikoni? Nilijiuliza. Kisha nikajikumbusha taratibu za kazi zetu. Ukishapokea malipo
    yako, ukishaweka utaratibu madhubuti wa kumuondoa mhanga wako, kamwe usianze kujiuliza
    maswali. Hiyo ni kazi ya polisi na wapelelezi na anayewajibika kujibu ni mteja wako, sio wewe.
    Wazo hilo lilinifanya nimnyanyue tena mwanangu mpenzi, kumwelekeza kule
    alikokusudiwa. Nikarekebisha lensi na kuzivuta nyuso zao kwangu. Ilikuwa imepita nusu dakika
    tu toka niliposita kuibonyeza. Walikuwa wangali palepale mlangoni. Raisi alikuwa amegeuka
    kusalimiana na mtu fulani. Ningeweza kumwondoa, kupitia kisogo chake kwa urahisi kabisa.
    Kwa bahati, sikutumwa kufanya hilo. Yule bepari wa viwanda na madini naye alikuwa pale,
    kaduwaaduwaa. Ningeweza kumwondoa kwa bei rahisi vile vile kupitia upande mmoja wa sikio.
    Mhanga wangu alikuwa kama anayeendelea kunisubiri. Uso wake mzuri ukiwa
    umeelekezwa kwangu na macho yake yalikuwa na dalili za wasiwasi na vitone vya jasho
    jembamba katika paji lake la uso, paji ambalo nilililenga vizuri kana kwamba nipo katika
    mazoezi ya shabaha. Nikamtekenya mwanangu. Sekunde moja, mbili, tatu… Mara mhanga
    wangu alipaa kama futi moja angani na kisha kutua kama gunia miguuni mwa Rais, akiwa tayari
    mzoga. ‘Mkono wa Jibril haujapata kukosea’ niliwaza nikicheka kimoyomoyo.
  • Purukushani iliyofuatia hapo haikuwa na kifani. Nilitamani sana kuitazama walao kwa
    dakika mbili pindi wanausalama wakicharuka kama waliopigwa ufunguo. Wanne, waliokuwa
    nyuma ya msafara huo; walichupa angani, mmoja akimpitia Rais kwa kumbo ambalo
    lilimwangusha na kumlalia kama ngao huku wenzake wakiwavuta na kurejea ndani. Wakati
    huohuo ving’ora vililia, polisi wakiivamia barabara na kufunga mitaa. Raia wa kawaida,
    waandishi na wafanyakazi wengine walikuwa taabani zaidi, huyu akianguka pale, yule
    akikimbilia kule kana kwamba wamepagawa. Sikuweza kujizuia kucheka.
    Nilimwona mwanausalama mmoja akitazama huko na huko, kisha macho yake yakaelekea
    upande wa pili wa mtaa, katika jengo nililokuwepo mimi na kutoa maelekezo kwa wenzake
    ambao walianza kujipanga kulizingira jengo hilo.
    Ulikuwa wakati wangu wa kuondoka. Nilimbusu mwanangu ambaye bado alikuwa na joto
    la risasi ile moja aliyotema. Nikamfungua na kumkunja taratibu na kisha kumweka katika
    briefcase yake vizuri. Juu yake nilirudishia vitu mbalimbali vya kudanganyia, ambavyo
    vingemlaghai mtu yeyote ambaye angepata wazimu wa kuikagua.
    Haikuwa kazi kubwa kuliacha jengo hilo. Watu wote walikuwa wameduwaa,
    wakishangazwa na purukushani ambazo zilikuwa zikiendelea upande wa pili wa mtaa.
    Nikaipuuza lifti na kufuata ngazi ambazo zilinitoa ghorofa ya tano na kunipeleka ya nne, ya tatu,
    ya pili. Hapo nilipanda lifti hadi chini. Wakati nikitoka nje ya lifti hiyo watu wawili, waliovaa
    suti waliingia harakaharaka, mikono yao ikiwa mifukoni.
    Hatukutazamana usoni, lakini sikuhitaji kuambiwa kua hao walikuwa wana usalama
    wakifuatilia uelekeo wa ilikotokea risasi. Nilitamani kuwapa pole. Nilitamani kuangua kicheko.
    Lakini yote hayo sikuyafanya. Niliondoka zangu bila kuangalia nyuma nikihisi macho yao
    yakilitazama umbo langu la nyuma hadi mlango wa lifti ulipojifunga.
    Sikuwa na wasiwasi. Nilijua wasingenishuku kwa lolote. Nani anaweza kumshuku
    msichana mrembo, aliyevaa nguo fupi na viatu vya mchuchumio huku nywele zake ndefu
    kaziachia kama msichana wa Kihebeshi? Nani angepata muda wa kushuku wakati harufu ya
    marashi aliyopaka yalitawala katika chumba cha lifti alichokiacha punde?

KWA ANAYEHITAJI VITABU VYA MTOBWA TUTAFUTAN KWA NAMBA 0763044459....
STORY HII ITAWAJIA KILA SIKU MPAKA ITAKAPOKWISHA...
 
***

Alikuwa mwanamke mzuri, zaidi ya uzuri wa haja. Picha zake katika televisheni na kurasa za kwanza za magazeti yote ya siku hiyo zilithibitisha hilo. Angeweza kushiriki urembo wa dunia na akashinda; angeweza kucheza filamu yoyote ile na akawa kivutio. Picha zilifichua uso wake mzuri uliojaa ucheshi, huku macho yake yakionyesha ung’aavu na hekima. Kiwiliwili chake chenye urefu wa kadiri, kilichojaa uhai na matumaini yote katika maisha. Hata sauti yake, pale televisheni moja iliporusha maneno yake mawili matatu enzi za uhai wake, ilithibitisha jambo moja; hakuwa mtu wa kufa.

Lakini tayari alikuwa marehemu! Mipango ya mazishi yake bila shaka ilikuwa ikiandaliwa!

Kwa jina aliitwa Cleopatra. Mumewe aliitwa Twalib. Kwasababu alizozifahamu mwenyewe, Cleopatra hakupata kulitumia jina la mumewe katika shughuli zake za kiofisi zaidi ya lile la baba yake Abeid ingawa Twalib lilikuwa jina zito katika jamii.

Magazeti yalisema na kudodosa hili na lile juu ya kifo chake. Hata hivyo, lililokuwa wazi katika kauli na maandishi yote ni utata juu ya kifo chake. Wingu zito lilitanda juu ya kifo hicho kutokana na swali zito lililokuwa likisumbua vichwa; muuaji alimkusudia yeye kweli au alikuwa amemlenga Rais?

Gazeti moja lilikwenda mbele zaidi, katika habari yao ambayo iliandikwa pia kama maoni, ilibebwa na kichwa cha habari; KWA VYOVYOTE VILE HAKUWA MTU WA KUFA.

Nani atafikiria kumuua Cleopatra? Liliandika. Hakuna hata sababu moja iliyowazi ya kupelekea mtu yeyote, awe na akili timamu au mwendawazimu kuchukua uamuzi wa kumuua kinyama tausi huyu ambaye hakupata kuwa na madhara kwa jamii wala mwanajamii yeyote.

Cleopatra alikuwa msomi, mwenye shahada ya Udaktari aliyoipata akiwa na umri usiozidi miaka thelathini na mitano. Alipata kuwa na kipindi muhimu sana cha ushauri wa kijamii katika televisheni mbili tatu nchini. Alikuwa mtumishi mwaminifu na mchapakazi hodari katika Ikulu ya Dar es Salaam. Hata kifo kimemkuta wakati akilitumikia taifa, tena mbele ya Rais aliyekuwa katika hafla nzito ya kumshawishi tajiri mkubwa wa viwanda duniani kuwekeza nchini.

Tunasema hakuwa mtu wa kufa! Bado tunaamini kuwa risasi iliyomuua haikumkusudia yeye. Ni kwa mtazamo huo ndipo tunaposisitiza haja kubwa ya uchunguzi makini wa haraka, kujua kitu gani hasa kilitokea hata mshumaa huu uliokuwa nuru kwa wanawake wote duniani na mfano kwa kila mwanaume, kuzimika ghafla…

Gazeti jingine lilizifuatilia habari hizo kwa mtindo wake. Liliwasiliana na ofisi ya Rais kutaka kujua Rais anajisikiaje kuponea tundu la sindano katika tukio hilo na iwapo anadhani risasi ilimkusudia yeye au marehemu.

No comment!

Pengine comment pekee ambayo uchunguzi wa gazeti hilo ulifanikiwa kupata ni pale walipofanikiwa kuzungumza na mume wa marehemu. Aliwashangaza, kama alivyowashangaza pia wasomaji, kwa taarifa yake kuwa yeye na Cleopatra walikuwa wametengana kwa zaidi ya miezi sita iliyopita! Kisa?

No comment.

Picha ya Twalib Khalfan ilitoka sambamba na ya marehemu mkewe katika habari hizi. Kila mmoja alikuwa akiitazama kamera huku anacheka. Mapenzi yalikuwa wazi kabisa katika macho ya tausi hawa wawili. Gazeti hilo halikuishia hapo. Lilivuka mipaka kwa kupendekeza kuwa kwa uzoefu wao, katika maswala yenye utata kama hayo yupo Mtanzania mmoja tu ambaye angeweza kuaminika katika kuyapatia ufumbuzi. Walimtaja mtu huyo kama Joram Kiango. Madai hayo yalifuatiwa na maelezo mafupi ya mikasa mingi ya kitaifa na kimataifa aliyopata kuitatua ama kwa ubongo wake ama kwa risasi ya bastola yake.

Waliyapamba maelezo hayo kwa picha ya Joram Kiango, akiwa ameketi katika bustani moja nchini, macho yake yakiwa yameinamia gazeti. Kando yake alikuwepo mwandani wake, msichana mwenye umbile nadra kwa uzuri wa ziada ambaye maelezo chini ya picha yake yalimtaja kwa ufupi ‘Bi Nuru’

Gazeti hilo lililalamika kuwa jitihada zao zote za kumpata Joram Kiango ili walao atoe maoni yake juu ya tukio hilo la aina yake, ziligonga mwaba. Kwamba walifika nyumbani kwake Ilala na kubaini kuwa hajaonekana kwa miezi. Walipita katika hoteli zote maarufu ndani na nje ya jiji na kupata jibu lilelile; hajaonekana kwa miezi.

Yuko wapi Joram Kiango?

Ilimalizia kauli ya mwandishi wa habari hiyo katika hali ya kukata tamaa.


***

Joram Kiango alizipokea habari hizo kwa njia ya mtandao wa intaneti akiwa angani. Alikuwa ndani ya ndege ya Emirates, aliyoipanda Amsterdam baada ya kushuka toka katika City Hopper ya KLM iliyomtoa Frankfurt. Alikuwa njiani toka nchini Ujerumani, katika mji wa Maizn, ambako alikuwa masomoni akipigania shahada yake ya udaktari wa falsafa. Mhadhiri wake Profesa Oed Matzke alikuwa nae sambamba kwa miezi miwili akinakili awamu ya mwisho ya kazi yake ili aweze kuvishwa hadhi ya Udaktari.

Akiwa amechoka kusoma kitabu cha Bill Clinton, The Art of Giving, aliamua kufungua kompyuta. Ndege hii ya kisasa ilikuwa na kompyuta kwa kila abiria, ambayo unaweza kuitumia kwa kutazama filamu, intaneti, kupiga simu pamoja na kuona wapi uliko katika anga hilo.

Kama kawaida yahoo ilikuwa na habari kadhaa za kimataifa; mtafaruku wa uchaguzi nchini Kenya, mauaji ya Bi Bhitto nchini Pakistan, purukushani za Hillary Clinton na Obama katika mbio za kuwania kuteuliwa kugombea Urais nchini Marekani kwa tiketi ya Democratic na kadhalika.

Habari iliyomshtua ni ile ya nyumbani, ‘RAIS ANUSURIKA KUUAWA,’ ambayo ilichukua nafasi ya nne ya habari hizo za siku hiyo. Hakuitegemea. Hivyo, ilimshtua sana, kwani kwa utamaduni na hulka ya Watanzania hilo lilikuwa jambo geni.

Aliisoma habari hiyo kwa kituo mara tatu, akihariri kati ya taarifa halisi na ushabiki wa mwandishi. Haikumchukua muda kujikuta akijiuliza swali lilelile lililokuwa likisumbua vichwa vya watu wengi; walikusudia kumuua Rais?

Jibu halikuwa rahisi kiasi hicho. Aliamua kuachana na habari hizo na kufungua e-mail yake; jkiangoyahoo.com. Kama alivyotegemea alikutana na ujumbe toka kwa Nuru. “Nimekutafuta sana kwa simu hupatikani. Una habari kuwa Rais ameponea chupuchupu…” Joram alizisoma tena habari za tukio lile la Dar es Salaam kwa mtazamo wa Nuru. Alimsoma katikati ya mistari na, hivyo, kuona matarajio ya msichana huyo kumshawishi ili ajitome katika uchunguzi wa tukio hilo.

Alitabasamu.

Ili kujiepusha na blaablaa nyingi za simu ambazo zingeweza kumvurugia mkondo wa masomo yake, Joram alikuwa ametoa kadi yake ya simu ya nyumbani na kuweka ya muda. Hivyo akiwa katika anga la Kenya, kuelekea Nairobi, aliitupa kadi ile ya Ujerumani na kuirejesha ya Tanzania. Hazikupita dakika tano, simu iliita. Na hakuwa mwingine zaidi ya Nuru. “Umepata e-mail yangu?” aliuliza

“Naam” alimjibu

“Kwahiyo una maoni gani?”

“Maoni gani?” Joram aliuliza baada ya kucheka. “Nuru naona umeanza. Mimi na wewe ni nani katika nchi hiyo hata tusumbue vichwa vyetu mara kwa mara kwa matukio yasiyotuhusu? Nimesema na narudia kusema kuwa tukio la Mtambo wa mauti lilikuwa la mwisho.”

Joram alimsikia Nuru akicheka upande wa pili wa simu. Kisha alisema, “Tusidanganyane Joram. Mimi nakufahamu vilivyo. Wewe si mtu wa kukaa kimya wakati Rais wa nchi yako anatishiwa kuuawa.”

“Hatuna hakika kama walikusudia kumuua,” joram alimkumbusha.

“Na ni hilo lililofanya kila mtu akufikirie. Hatuwezi kukaa kimya wakati kitendawili cha tukio hili hakijateguliwa,” alisema kabla ya kuuliza, “Unarejea lini?”

“Leo, muda mfupi baadaye tutakuwa pamoja. Kumbuka nakuja kupumzika. Siji kufanya kazi za wavivu wanaofura matumbo na kusahau wajibu wao. Watu wanaowasahau raia na kutumia vyeo vyao kuwalinda mafisadi”

Kicheko cha Nuru kilimkatiza Joram

“Sasa unacheka nini?”

“Nimefurahi. Huyu ndiye Joram Kiango ninaemfahamu.”




kwa riwaya hizi unaweza kuzipata kupitia 0763044459
 
Kwa jina aliitwa Cleopatra. Mumewe aliitwa Twalib. Kwasababu alizozifahamu mwenyewe, Cleopatra hakupata kulitumia jina la mumewe katika shughuli zake za kiofisi zaidi ya lile la baba yake Abeid ingawa Twalib lilikuwa jina zito katika jamii.
Pamoja Sana Nameles Girl
 
Back
Top Bottom