Riwaya: Ufukwe wa Madagascar

mwamba c

JF-Expert Member
Jan 2, 2017
690
2,361
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
Mtunzi: Kelvin Mponda
SEHEMU: 2

Begi langu dogo la mgongoni lenye mifuko mingi yenye vipenyo tofauti ambapo mle ndani pia niliweka nguo
zangu chache muhimu za kubadilisha.
Baada ya muda mfupi nikawa nimemaliza kujiandaa huku nikiwa katika mwonekano mpya wa suruali nyeusi ya jeans, buti ngumu za ngozi miguuni, fulana nyekundu yenye mstari mweupe kifuani, shati zito la jeans la rangi ya samawati, saa ya kijasusi mkononi na kofia nyeusi ya kapelo.
Wakati nikitoka nje na kufunga mlango wa mbele wa nyumba yangu nikaliona gari la jeshi aina ya Nissan Patrol likiegesha mbele ya nyumba yangu kando ya mti mkubwa uliyokuwa eneo lile. Dereva wa gari lile akawasha taa za mbele na kuzima mara mbili katika namna ya kunifahamisha kuwa tayari alikuwa amefika kunichukua nami bila kupoteza muda mara tu nilipomaliza kufunga mlango haraka nikashuka ngazi za baraza yangu nikielekea kwenye lile gari.
Dereva wa lile gari la jeshi Nissan Patrol nilimfahamu kwa jina moja tu la Mayunga mwenye cheo cha Koplo na vilevile askari komando wa daraja la pili. Kijana tuliyeelekeana kwa umri, mrefu na mweusi mwenye macho makali na mikono imara, mtu asiye na maneno mengi lakini mcheshi.
Nilipolifikia lile gari nikafungua mlango wa mbele na kuingia ndani. Dereva wa lile gari Koplo Mayunga akanipigia saluti kwa heshima zote na kunisalimia kwa utulivu kwani alikuwa akikifahamu vizuri kwa cheo changu cha kijeshi cha Luteni nami nikaitikia salamu yake kwa bashasha zote.
“Pole na majukumu” nikamwambia huku nikitabasamu wakati alipokuwa akinipokea begi langu dogo na kuliweka siti ya nyuma.
“Nishapoa afande wangu, nikupe pole wewe uliyemwacha shemeji yangu usiku wa manane kama huu kajikunyata mwenyewe kitandani”
Maelezo ya Koplo Mayunga yakapelekea wote tuangue kicheko hafifu mle ndani huku kila mmoja akionekana kufurahishwa na utani ule na hapo safari yetu ikaanza. Tulipofika njiani nikamuuliza Koplo Mayunga kama alikuwa akifahamu lolote juu ya wito wangu usiku ule. Hata hivyo alinijibu kuwa alikuwa hafahamu chochote ingawa alinidokeza kuwa hata yeye alikuwa ameamshwa usiku ule na kutakiwa kumpeleka Brigedia jenerali Ibrahim Gambari ofisini kwake. Kusikia vile haraka hisia za hatari zikaanza kujengeka kichwani mwangu huku nikizama kwenye tafakuri.
Muda huu wa usiku manane jiji la Dar es Salaam lilikuwa limemezwa na utulivu wa aina yake. Magari machache yalionekana kukatisha barabarani wakati safari yetu ilipokuwa ikiendelea. Katika baadhi ya mitaa maarufu wasichana waliokuwa wakifanya biashara ya ngono maarufu kama dada poa walionekana kujaribu bahati zao kwa wanaume wapita njia na hali ile ilinisikitisha sana.
_____
Saa tisa na nusu usiku Koplo Mayunga aliegesha gari lile Nissan Patrol kwenye viunga vya maegesho ya magari vya ofisi ya taifa ya idara kuu ya ujasusi eneo la Upanga jijini Dar es Salaam. Nami bila kupoteza muda nikamshukuru kwa huduma yake ya usafiri kisha nikachukua begi langu na kufungua mlango nikishuka.
Wakati nikitembea kuelekea kwenye ofisi zile za makao makuu ya idara ya ujasusi nikayatembeza macho yangu kutazama huku na kule nikilipeleleza jengo la ghorofa la ofisi zile zenye ulinzi wa kuaminika masaa ishirini na nne wiki nzima. Nikaiona taa ikiwa inawaka kwenye chumba kimoja kilichokuwa kwenye ghorofa ya pili ya jengo lile na hapo nikawa na hakika kuwa mkuu wa idara ya taifa ya ujasusi Brigedia jenerali Ibrahim Gambari alikuwa akinisubiri ofisini kwake.
Walinzi makini wa jengo lile hawakujisumbua kunizuia kwani walikuwa wakinifahamu vizuri kuwa mimi ni nani. Hivyo wakanisalimia kwa heshima zote za kiaskari wakati nilipokuwa nikiharakisha kupanda ngazi za jengo lile kuelekea ghorofa ya pili ilipokuwa ofisi ya jemadari yule chakaramu.
Ofisi ya Brigedia jenerali Ibrahim Gambari ilikuwa mkono wa kushoto mara baada ya kumaliza kupanda ngazi za kuingia ghorofa ya pili kwenye korido pana, hatua chache baada ya kuipita ofisi ya usalama wa taifa ya sera na mipango ambayo kwa wakati huu ilikuwa imefungwa.
Hatua chache zilizofuata nikawa nimeifikia ofisi ya mkuu wa idara ya ujasusi Brigedia jenerali Ibrahim Gambari. Nilipofika mlangoni nikasimama na kuupimia utulivu wa mle ndani. Ofisi ilikuwa tulivu na hapakuwa na sauti yoyote ya maongezi iliyosikika mle ndani hivyo nikahisi kuwa Brigedia jenerali Ibrahim Gambari huwenda alikuwa peke yake mle ndani. Bila kupoteza muda nikaanza kugonga hodi pale mlangoni. Ukimya kidogo ukapita kisha kutoka mle ndani ya ofisi nikasikia sauti nzito ya kiume yenye mamlaka ikiniambia.
“Ingia ndani Tibba”
Ruhusa ile ikanipelekea nikikamate vizuri kitasa cha ule mlango kisha nikakizungusha haraka na kuusukuma ule mlango kwa ndani huku nikipiga hatua zangu za kijeshi kuingia mle ndani. Hii haikuwa mara yangu ya kwanza kuingia kwenye ofisi ya Brigedia jenerali Ibrahim Gambari hivyo wakati nikiingia mle ndani tayari nilikuwa na picha kamili ya mandhari ya ofisi ile.
Ilikuwa ni ofisi pana yenye zulia jekundu sakafuni na meza ndefu ya ofisini yenye viti ishirini na viwili. Viti kumi na mbili upande wa kushoto na viti vingine kumi na mbili upande wa kulia. Haraka nikayatembeza macho yangu mle ndani na namna ya mpangilio wa viti kwenye ile meza kubwa ya ofisini nikahisi kuwa kikao kizito kilikuwa kimefanyika mle ndani muda mfupi uliyopita.
Brigedia jenerali Ibrahim Gambari alikuwa ameketi nyuma ya meza yake kubwa ya ofisini mwisho wa ofisi ile upande wa kushoto akiwa katika uso wa kusawajika huku akiwa ameegemea kiti chake cha ofisi. Ukimya ndani ya ofisi ile ukanifanya nisikie sauti hafifu ya hatua zangu wakati nilipokuwa nikikatisha kuelekea kwenye ile meza ya ofisini ya Brigedia jenerali Ibrahim Gambari. Mara moja nilipoitazama sura ya jemadari yule haraka nikatambua kuwa tayari mambo yalikuwa segemnege.
Brigedia jenerali Ibrahim Gambari alikuwa ameketi kwenye kiti chake cha ofisini huku mche wa sigara ukiteketea taratibu kwenye pembe ya mdomo wake na macho yake yakitazama karatasi ndogo aliyokuwa ameishika mkononi. Nilipomchunguza vizuri haraka nikatambua kuwa hapakuwa na mazingira ya kuleta mzaha kama vile ilivyokuwa kawaida yetu. Juu ya meza ile ya ofisini kulikuwa na vitabu na mafaili machache yaliyopangwa kwa ustadi pembeni ya kibao kidogo kilichochongwa vizuri kwa maandishi ya kutanabaisha cheo cha kamanda yule pamoja na kidau cha wino na mhuri wa ofisi.
Upande wa kushoto wa ofisi ile kulikuwa na picha kubwa ya baba wa taifa la Tanzania, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na picha nyingine za viongozi wa jamhuri ya muungano wa Tanzania zikiwa zimetundikwa ukutani. Upande wa kulia kulikuwa na rafu kubwa ya mbao iliyosanifiwa kwa ustadi wa hali ya juu. Ndani ya rafu ile kulipangwa vitabu na mafaili chungu nzima yaliyoshika vumbi na kupoteza nuru kutokana na kuhifadhiwa kwa muda mrefu ingawaje mazingira ya mle ndani yalikuwa nadhifu na yanayovutia kwa mpangilio wa samani za kisasa. Mbele ya ofisi ile ukutani kulikuwa na ramani tatu kubwa. Ramani moja ya nchi ya Tanzania, ramani ya pili ya bara la Afrika na ramani ya tatu ya Dunia
Hatimaye nikaifikia ile meza ya ofisini ya Brigedia jenerali Ibrahim Gambari na macho yetu yalipokutana nikafunga mguu na kupiga saluti moja ya nguvu mbele ya jemadari yule. Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaitikia salamu yangu ya kijeshi kwa utulivu kisha akanikaribisha niketi kwenye kochi moja la sofa lililokuwa likitazamana na ile meza yake mle ndani.
Naam! sasa nilikuwa ana kwa ana nikitazamana na mwanausalama na kamanda yule wa jeshi Brigedia jenerali Ibrahim Gambari. Umri wa miaka hamsini na miwili bado ulikuwa haujatosha kabisa kuzipokonya nguvu zake mwilini. Macho yake makali yakanitazama kwa makini pasipo kusema neno lolote huku akionekana kuipa utulivu akili yake. Alipoiegemea mikono yake pale juu ya meza na kuketi vizuri akavunja ukimya.
“Karibu sana Tibba!” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaongea huku akinipa mkono wa karibisho.
“Nashukuru sana afande” nikamwitikia jemadari yule kwa utulivu huku akili yangu ikiwa bado kwenye tafakuri ya kutaka kufahamu dhumuni la wito ule. Mara tu nilipoketi kwenye lile kochi Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akanitazama kwa uyakinifu kabla ya kuvunja ukimya.
“Huwenda ukawa umeshangazwa sana na wito wangu usiku wa manane kama huu” kisha akaweka kituo kidodo na kukohoa kabla ya kuendelea.
“Lakini huu ni wajibu wetu sote tuliyoukubali kwa ridhaa yetu wenyewe tangu tulipojiunga na jeshi la wananchi wa Tanzania na kuweka kiapo cha kufa na kupona cha kulitumikia jeshi hili” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaweka kituo tena kasha akanitazama kwa utulivu na hatimaye kunipa ile karatasi aliyokuwa ameishika mkononi. Haraka nikanyoosha mkono wangu kuipokea ile karatasi kisha nikajiegemeza vizuri kwenye lile kochi nikayapitia maelezo yaliyokuwa kwenye karatasi ile.
Mara tu nilipoanza kusoma yale maelezo kwenye ile karatasi mapema nikatambua kuwa ile karatasi ilikuwa ni faksi na faksi ile ilikuwa imetumwa masaa machache yaliyopita kutoka kwenye ofisi kuu ya ubalozi wa Tanzania jijini Bujumbura nchini Burundi.
Nilipomaliza kusoma maelezo yaliyokuwa kwenye faksi ile haraka nikatambua nini dhumuni la wito ule wa usiku. Ile faksi ilikuwa imetumwa na kitengo cha usalama cha ubalozi wa Tanzania nchini Burundi ikieleza kuwa balozi wa Tanzania nchini Burundi, Meja jenerali mstaafu ndugu Adam Mwambapa alikuwa ametekwa na watu wasiofahamika muda mfupi baada ya jaribio la mapinduzi ya kijeshi kufanyika nchini humo. Mara tu nilipomaliza kusoma taarifa ile moyo wangu ukapoteza utulivu kabisa huku kijasho chepesi kikianza kunitoka sehemu mbalimbali za kwa mwili wangu.
“Nini kimetokea?” hatimaye nikauliza kwa udadisi huku nikiyapeleka macho yangu kumtazama kamanda yule mbele yangu.
“Bado ni kizungumkuti kwani hadi wakati huu hakuna yeyote anayefahamu kinachoendelea. Mimi pia nimeshtuka kama wewe na kwa kweli hizi ni taarifa za kustaajabisha na kusikitisha sana” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaongea katika hali ya simanzi huku taratibu akiviminyaminya vidole vyake vya mikononi katika hali ya kuupisha utulivu kichwani mwamke.
“Mna uthibitisho gani juu ya taarifa hizi?” nikamuuliza Brigedia jenerali Ibrahim Gambari kwa utulivu huku nikirudia kusoma kwa makini maelezo ya kwenye ile faksi.
“Hakuna namna ya kupingana na taarifa hizo kuwa siyo za kweli au lah!. Kama unavyoona mwenyewe faksi hiyo imetumwa na idara ya usalama ya ubalozi wetu wa nchini Burundi”
“Mmejaribu kupata maelezo ya kina juu ya hili tukio?” nakauliza kwa udadisi.
“Tumekosa ushirikiano wa kutosha kutoka kwa maafisa usalama wa nchini Burundi kutokana na hali ya tete ya usalama wa nchi hiyo ilivyo kwa sasa” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaongea kwa utulivu huku akiupeleka mche wake wa sigara mdomoni na nilipomtazama nikatambua bado alikuwa akitafakari juu ya lile tukio la kutekwa kwa balozi Adam Mwambapa.
“Hili ni tukio la kushangaza sana” nikaongea kwa utulivu huku nikiendelea kutafakari yale maelezo kwenye ile faksi.
“Pia ni pigo kubwa kwa serikali ya jamhuri ya muungano wa Tanzania na idara yetu ya ujasusi”
“Wewe una mtazamo gani juu ya suala hili?” nikamuuliza kamanda yule.
“Bado ni mapema sana kutoa mwelekeo sahihi wa hili tukio la utekaji wa balozi wetu Adam Mwambapa ingawa naweza kulihusisha na hali ya machafuko ya kisiasa yaneyoendelea nchini Burundi” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaongea kwa utulivu baada ya kuitoa sigara yake mdomoni na kupuliza wingu zito la moshi wake pembeni na hapo kikafuatia kitambo kifupi cha ukimya baina yetu huku kila mmoja akionekana kuzama kwenye tafakuri nzito kichwani mwake. Niseme kuwa balozi Adam Mwambapa hakuwa mgeni kabisa katika fikra zangu kwani kabla ya kustaafu jeshi na kuteuliwa na rais kushika wadhifa wa balozi wa Tanzania nchini Burundi aliwahi pia kushika nyadhifa nyingi za kijeshi ikiwemo cheo cha mnadhimu mkuu wa jeshi la wananchi Tanzania. Hivyo alikuwa ni mtu mzoefu sana kwenye masuala ya kijeshi ya ulinzi na usalama na alivimudu vyema vyeo vyake vyote kwa weledi wa hali ya juu. Ndiyo kisa hata baada ya kustaafu jeshi serikali haikutaka mchango wake upotee hivihivi hivyo rais akamteua Meja jenerali mstaafu ndugu Adam Mwambapa kuwa balozi wa Tanzania nchini Burundi miaka minne iliyopita.
Kiongozi yeyote wa jeshi hasa mtu aliyewahi kushika madaraka ya juu jeshini kama Meja jenerali mstaafu ndugu Adam Mwambapa inapotokea kuwa ametekwa au kutoweka katika mazingira ya kutatanisha huwa ni tishio kubwa kwa serikali iliyopo madarakani na hata kwa usalama wa nchi kwa ujumla. Kwani kiongozi wa jeshi wa namna ile aliyelitumikia jeshi kwa miaka mingi huwa anafahamu siri nyingi za nchi yake hususani katika masuala ya usalama. Hivyo yeyote aliyemteka jemadari yule mstaafu wa jeshi la wananchi Tanzania ndugu Adam Mwambapa kwanza alipaswa kuwa ni mwanajeshi au kikundi cha kijeshi chenye maarifa ya juu sana katika medani za mapambano ya kijeshi. Vilevile utekwaji wake ulipaswa kuwa na sababu za msingi za kuhalalisha kitendo hicho kwa watekaji.
Niliendelea kutafakari kwa sababu hizo zingekuwa zipi na wakati nikiwa katika hali ile mara hisia mbaya zikanijia na hapo moyo wangu ukapoteza utulivu kabisa pale nilipowaza kuwa huwenda watekaji hao walitaka kupata taarifa fulani kutoka kwake. Taarifa ambazo bila shaka zilikuwa na mahusiano ya moja kwa moja na serikali ya Tanzania kama siyo vyombo vyake vya ulinzi. Nani anayeweza kufanya tukio la namna ile na kwa sababu gani?. Nikajiuliza pasipo kupata majibu.
Nikiwa nimezama kwenye tafakuri ile akili yangu ikaenda mbele zaidi katika kuunda hoja kichwani. Nikaanza kuziorodhesha nchi zote za Afrika ya Mashariki nikianzia kwa Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, na hatimaye Burundi. Nilipomaliza nikaanza kutathmini vizuri hali ya mahusiano ya kisiasa yaliyopo baina ya nchi hizi za Afrika Mashariki. Tathmini yangu ikanieleza kuwa mahusiano ya nyanja zote baina ya nchi zile bado yalikuwa mazuri ingawa kulikuwa na misuguano ya kawaida ya hapa na pale. Nilipotafakari kwa kina juu ya misuguano hiyo bado haikuweza kuniridhisha kuwa ingeweza kuwa sababu toshelevu ya kutekwa kwa balozi wetu tena na moja ya nchi hii jirani iliyopo kwenye ushirika wa jumuiya ya nchi za Afrika Mashariki. Hivyo nikaishilia kumeza funda kubwa la mate huku akili yangu ikiendelea kusumbuka.
“Kikao cha wanausalama kilichomalizika muda mfupi uliyopita kabla ya wewe kufika hapa kimeazimia kuwa itakuwa ni vyema sana tukikubadhi jukumu hili wewe” maelezo ya Brigedia jenerali Ibrahim Gambari yakawa yamezirudisha fikra zangu mle ndani na hapo nikayapeleka macho yangu kumtazama kwa makini kana kwamba sikuwa nimemsikia kwa makini kamanda yule.
“Una maana gani?” nikamuuliza kamanda yule kwa utulivu huku nikifahamu fika uelekeo wa maongezi yake.
“Hatuwezi kulifumbia macho suala hili kama unavyojua kuwa ndugu Adam Mwambapa ni kiongozi mkubwa serikalini na jeshini. Yeyote aliyemteka bila shaka anataka kupata taarifa nyeti kutoka kwake kuhusiana na serikali yetu na vyombo vyetu vya usalama. Hiki ndiyo tunachodhani wote kwa pamoja ndiyo kisa tukaona kuwa tukutume nchini Burundi ukatafute ukweli juu ya mashaka tuliyonayo” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaweka kituo huku akiyakung`uta majivu ya sigara yake kwenye kibeseni kidogo cha majivu kilichokuwa pale juu ya meza halafu akayapeleka macho yake kunitazama kwa utulivu.
“Lakini hii ni kazi ngumu sana na ya hatari kufanywa na mtu mmoja” nikatumbukiza hoja yangu huku nikimtazama Brigedia jenerali Ibrahim Gambari katika sura ya kukata tamaa.
“Hakuna mtu aliyesema kuwa hii ni kazi rahisi hasa kwa kuzingatia hali ya usalama ya nchi ya Burundi ilivyo kwa wakati huu. Hata hivyo tunaamini kuwa ni wewe tu utakayeweza kuifanya kwa ufanisi na kutuletea majibu mazuri ya hakika ndani ya muda mfupi huku sisi tukiwa nyuma yako kukupa msaada wowote utakaouhitaji” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaweka kituo kidogo akikohoa kusafisha koo lake kabla kuendelea.
“Tanzania ni nchi yenye bahati sana kwa kutokumezwa na majanga ya chuki ya ukabila ukifananisha na hizi nchi nyingine zilizosalia za Afrika Mashariki. Hii inatokana na Mungu mwenyewe kumjalia hekima ya juu sana baba wa taifa hili Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ya kuzitumia vizuri tofauti zetu za rangi ya ngozi, imani na makabila katika kutengeneza mshikamano thabiti wa kutufanya tuwe wamoja.
Wapo wapumbavu wachache wanaojaribu kupenyeza nadharia ya udini na ukabila katika mfumo wa maisha ya watanzania wakijitafutia manufaa yao. Ndiyo maana hata sasa katika baadhi ya taasisi za serikali au binafsi aina ya wafanyakazi wake itakutanabaisha kuwa nadharia ya udini na ukabila bado inaabudiwa na kuzidi kuota mizizi. Hali hii ni mbaya sana kwa sababu hujenga.....ITAENDELEA
 
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 3
Mtunzi:Kelvin Mponda
...chuki ya muda mrefu na pale chuki hiyo inapokomaa huzaa machafuko ambayo mtanzania wa kwaida itamgharimu kupambana kufa na kupona kuipigania pumzi yake”
“Lakini nionavyo mimi hali hii hutegemeana sana na utashi wa kiongozi aliyeko madarakani, kwani kama kiongozi ana utashi mdogo na mbinafsi na washauri wake ni watu anaofanana nao kimtazamo ni rahisi kumuona anatoa fursa nyingi kwa watu wa dini yake au kabila lake pasipo kuangalia mustakabali mzima wa taifa. Kwa kufanya hivyo jamiii ya mlengwa wa kushoto hujihisi kutengwa na hivyo ubani wa chuki ya udini na ukabila kuzidi kufukiza” nilimaliza kuongea huku nikipiga mwayo hafifu wa uchovu.
“Tunataka kiongozi ambaye ataweza kutufanya wamoja pamoja na uwepo wa tofauti katika imani na makabila yetu. Kwa mfano, Rwanda na Burundi ni nchi ambazo watu wake wanabaguana kwa ukabila kwa kiwango cha juu sana. Hali hiyo imepelekea kunawiri kwa chuki mbaya ya ukabila miongoni mwao. Chuki ambayo imeondoa kabisa hali ya kuaminiana wenyewe kwa wenyewe katika kila maeneo. Ndiyo maana migogoro na machafuko ya kisiasa ni vigumu kumalizika kabisa katika nchi hizi. Kama Tanzania haitalivalia njuga hili suala la udini hapa nchini basi na sisi pia hatutakuwa salama kwa siku za usoni” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaweka kituo akivuta sigara yake taratibu na alipoitoa sigara ile mdomoni na kuupuliza moshi wake pembeni akaendelea.
“Napenda uelekee nchini Burundi kufanya hii kazi huku tayari ukiwa na picha kamili kichwani kuwa unaenda kuonana na watu wa namna gani. Jaribio la mapinduzi ya kijeshi lililotangazwa usiku wa leo nchini Burundi siyo jambo geni sana katika nchi hiyo. Nchi ya Burundi inaundwa na mjumuiko wa makabila matatu lakini yasiyo na uwiano sawa kwa ujumla wa hesabu yake. Raia wa Burundi wa kabila la Hutu ndiyo wengi zaidi kwa asilimia 85, asilimia 14 katika sehemu iliyosalia inaundwa na kabila la Tutsi ambao wengi wao ndiyo walioshikilia nyadhifa za juu serikalini na jeshini. Asilimia moja iliyosalia inaundwa na watu wa kabila la Twa ambalo ni kabila la wawindaji. Hivyo ukitazama utagundua kuwa watu wa kabila la Hutu ni wengi zaidi katika jumla ya idadi ya raia wanchi hiyo.
Mapinduzi ya kijeshi nchini Burundi yalianza kutokea mwaka 1976 wakati serikali ya rais Michael Micombero wa kabila la Tutsi ilipopinduliwa kijeshi na mtutsi mwingine Kanali Jean-Baptiste Bagaza kwa sababu alizozijua yeye mwenyewe. Baada ya Kanali Jean-Baptiste Bagaza kuingia madarakani chini ya chama chake cha UPRONA-Unité pour le progrès National, aliendelea kuongoza nchi hiyo hadi mwaka 1984 ambapo joto la demokrasia lilikuwa limekolea vizuri.
Uchaguzi mkuu wa rais ulipofanyika Burundi haukuleta mabadiliko yoyote kwani Kanali Jean-Baptiste Bagaza na chama chake cha UPRONA walijinadi kuibuka na ushindi wa kishindo wa silimia 99.6 dhidi ya wapinzani wao na hivyo kuendelea kubaki madarakani. Ingawa utafiti unaeleza kuwa uchaguzi huo haukuwa wa haki kama zilivyo chaguzi nyingi za nchi za bara la Afrika” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaweka kituo akikohoa kidogo na kuyakung`uta majivu ya sigara yake kwenye kile kibeseni kidogo cha majivu ya sigara kilichokuwa pale mezani kabla ya kuendelea.
“Hata hivyo utawala wa Kanali Jean-Baptiste Bagaza ulishutumiwa vikali kwa kuliwekea vikwazo kanisa la Roman Catholic ambalo lina waumini asilimia 65 ya raia wote wa nchi ya Burundi kwa kile kilichodaiwa kuwa kanisa hilo lilikuwa likiingilia mambo kadhaa ya serikali. Kufuatia hali hiyo serikali ya Kanali Jean-Baptiste Bagaza haikuendelea kutabaruku zaidi madarakani kwani ilipofika mwezi Septemba 1987 wakati Kanali Jean-Baptiste Bagaza alipokuwa amesafiri kwenda jijini Quebec nchini Canada kuhudhuria mkutano wa viongozi wa nchi zinazongumza lugha ya kifaransa. Serikali yake ikapinduliwa na binamu yake Meja Pierre Buyoya na hivyo utawala mwingine wa jeshi kushika hatamu. Baada ya kusikia juu ya mapinduzi hayo Kanali Jean-Baptiste Bagaza haraka alirudi nchini mwake lakini uwanja wa ndege wa Bujumbura ulikuwa tayari umefungwa. Hivyo Kanali Jean-Baptiste Bagaza akakimbilia jijini Nairobi lakini Kenya ilikataa kumpokea hivyo akaelekea nchini Uganda na baadaye kutorokea nchini Libya ambapo huko alipewa hifadhi ya ukimbizi wa kisasa.
Mara baada ya Meja Pierre Buyoya kujiingiza madarakani kwa mapinduzi ya kijeshi na kutangazwa kuwa rais wa nchi ya Burundi tarehe 2 Oktoba mwaka 1987. Alitangaza haraka kubadili katiba ya nchi hiyo na kuondoa vikwazo vyote vilivyokuwa vimewekwa na serikali ya Kanali Jean-Baptiste Bagaza dhidi ya kanisa la Romanic Catholic hasa kwa kuwa yeye alikuwa muumini wa kanisa hilo.
Meja Pierre Buyoya akaendelea kushikilia madaraka ya nchi ya Burundi hadi pale ulipofanyika unaosemekana uchaguzi wa kwanza wa kidemokrasia tarehe 27 mwezi Juni mwaka 1993. Katika uchaguzi huo uliosemekana wa kweli na wa haki, Melchior Ndadaye mhutu aliibuka mshindi na kutangazwa kuwa rais wa nne wa nchi hiyo. Hata hivyo Melchior Ndadaye hakufanikiwa kutimiza ahadi zake za kukuza uchumi wa nchi ya Burundi na kupunguza chuki ya ukabila baina ya waburundi kwani alishika madaraka kwa kipindi cha miezi mitatu tu kabla kupinduliwa kijeshi na hatimaye kuuwawa tarehe 21 Oktoba 1993.
Mapinduzi ya kijeshi dhidi ya serikali ya rais mhutu Melchior Ndadaye na kuuwawa kwake na mawaziri wake sita kuliamsha hisia kali za chuki kwa watutsi dhidi ya wahutu nchini Burundi na hivyo kupelekea kulipuka kwa vita kali ya ukabila kati ya watutsi na wahutu nchini humo, hivyo ukafanyika umwagaji damu wa kutisha. Katika mazingira hayo waliompindua rais Melchior Ndadaye na hatimaye kumuua hawakupata nafasi ya kushikilia dola hivyo ndugu Francois Ngeze, mwanasiasa wa kawaida akawekwa kuwa rais na kushikilia utawala wa nchi hiyo kwa muda.
Hata hivyo Ngeze alikataa kuwapa ushirikiano wa kutosha viongozi wote wa mapinduzi ya kijeshi na badala yake akamuita aliyekuwa waziri mkuu wa kipindi hicho kabla ya mapinduzi hayo ya kijeshi, mama Sylvie Kinigi, mtutsi ambaye alikuwa ameyakimbia mapinduzi hayo na kuomba hifadhi kwa ubalozi wa Ufaransa.
Makamanda wa jeshi hawakuwa na namna ya kukataa hivyo wakakubali kuwa mama Sylvie Kinigi ashikilie uongozi wa nchi kama rais wa mpito wakati katiba ya nchi hiyo ikifanyiwa marekebisho baada ya ile katiba ya awali kupelekea machafuko makubwa ya kisiasa na umwagaji mkubwa wa damu uliotokana na vita ya ukabila.
Ilipofika mwezi Januari mwaka 1994, bunge la nchi ya Burundi likamchagua ndugu Cyprien Ntaryamira ambaye hapo awali alikuwa waziri wa kilimo enzi za utawala wa rais Melchior Ndadaye kuwa rais wa nchi hiyo. Rais Cyprien Ntaryamira alikuwa mhutu hivyo kitendo cha mhutu kuchaguliwa kuwa rais wa nchi hiyo kiliamsha hisia tofauti kwa watutsi raia wa nchi hiyo. Waziri mkuu mtutsi mama Sylvie Kinigi akamtambua Cyprien Ntaryamira kama rais hata hivyo muda mfupi baadae akajiuzulu wakati rais Cyprien Ntaryamira akiapishwa na hivyo nafasi yake kuchukuliwa na ndugu Anatole Kanyenkiko. Kwani mama Sylvie Kinigi alikuwa akionekana kuwa ni mkosoaji na mtu wa kuogopwa kwa namna ya uongozi wake. Muda mfupi baada ya kujiuzulu mama Sylvie Kinigi akaondoka nchini Burundi” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaweka kituo huku akinitazama kwa utulivu na kisha kuniuliza.
“Nadhani unayafuatilia vizuri maelezo yangu”
“Ondoa shaka” nikamwambia na hapo akaendelea.
“Rais wa Burundi ndugu Cyprien Ntaryamira na rais wa Rwanda kipindi hicho ndugu Juvénal Habyarimana, wote wahutu, waliuwawa jioni ya tarehe 6, Aprili, 1994 kwa shambulio la kulipuliwa kwa ndege yao wakati ndege hiyo ilipokuwa ikijiandaa kutua kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kigali nchini Rwanda. Tukio hilo lilipelekea mauaji ya kimbari nchini Rwanda.
Baada ya kifo cha rais Cyprien Ntaryamira uongozi wa nchi ya Burundi ukachukuliwa na ndugu Sylvestre Ntibantunganya ambaye hapo awali alikuwa ni spika wa bunge la Burundi ambaye pia kwa kabila ni mhutu. Hata hivyo ndugu Sylvestre Ntibantunganya hakufaidi sana madaraka yake kwani ilipofika tarehe 21 mwezi Julai mwaka 1996, waasi wa kihutu walivamia kambi moja ya wakimbizi nchini Burundi na kuua watu zaidi ya 300. Tukio hilo likapelekea rais Sylvestre Ntibantunganya siku mbili zilizofuata aikimbie ikulu na kwenda kujificha kwenye ubalozi wa Marekani nchini Burundi.
Jeshi likachukua madaraka ya nchi ya Burundi tarehe 25 mwezi Julai mwaka 1996 na aliyekuwa waziri wa ulinzi ndugu Firmin Sinzoyiheba akatangaza kupitia redio ya taifa kuwa Meja Pierre Buyoya mtutsi ndiye rais wa serikali ya mpito. Mapinduzi hayo yalipingwa vikali na taasisi za kimataifa akiwemo rais wa Marekani wa kipindi hicho Bill Clinton, katibu mkuu wa umoja wa mataifa wa kipindi hicho ndugu Boutros Boutros-Ghali na katibu mkuu wa umoja wa Afrika wa kipindi hicho, mtanzania mwenzetu ndugu Salim Ahmed Salim. Hivyo hayo yalikuwa ni mapinduzi ya kijeshi mara ya nne kuwahi kufanyika nchini Burundi na pia ya mara ya pili kwa Meja Pierre Buyoya kutwaa madaraka ya nchi hiyo.
Kufuatia hapo vikwazo mbalimbali vikawekwa na tasisi za kimataifa ili kuibana serikali ya Meja Pierre Buyoya juu ya namna yake kutwaa madaraka kwa mapinduzi ya kijeshi. Hata hivyo kufuatia vyombo mbalimbali vya asuluhishi hatimaye Major Pierre Buyoya akakubali kukabidhi madaraka mwaka 2003 ambapo aliyekuwa makamo wake wa rais ndugu Domitien Ndayizeye ambaye ni mhutu akaapishwa kuwa rais wa nchi hiyo wa serikali ya mpito. Madaraka ambayo aliyoyashikilia hadi tarehe 26 mwezi Agasti mwaka 2005 alipomkabidhi kiti cha uongozi wa nchi hiyo ndugu Pierre Nkurunziza baada ya kuibuka mshindi kwenye uchaguzi mkuu wa rais wa nchi hiyo” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaweka kituo kisha nikamuona akimalizia kuvuta sigara yake na kipisi kidogo kilichosalia akakitupia kwenye kile kibeseni cha majivu pale mezani kisha akasogeza nyuma kiti chake cha ofisini na kusimama.
Upande wa kulia wa sehemu ile kulikuwa na kabati kubwa la mbao, Brigedia jenerali Ibrahim Gambari alipolifikia lile kabati akafungua na kuchukua chupa ya chai na vikombe viwili vya dongo, mkebe mdogo wa kuhifadhia sukari na pakiti moja ya kahawa. Aliporudi pale mezani akafungua ile chupa ya chai na kumimina maji ya moto kwenye vile vikombe kisha akaichana ile pakiti ya kahawa na kumimina kahawa mle ndani. Vijiko vichache vya sukari ya Kilombero vikatosha kutengeneza mchanganyiko makini wa kahawa yenye harufu nzuri na ladha ya kuvutia.
“Karibu tupashe tumbo joto” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akanikaribisha baada ya kumaliza kukoroga mchanganyiko ule kwenye vile vikombe kisha akanyanyua kikombe kimoja na kukishika hewani. Kwa ishara ile nikafahamu kuwa alikuwa akinisubiri tugongeshe vikombe vyetu kama ishara ya umoja na urafiki wetu ama Cheers. Mara tu tulipogongesha vikombe vyetu hewani kila mmoja akavuta funda moja la kahawa na kukiweka kikombe chake mezani.
“Nashukuru sana kwa kahawa maana tumbo langu lilikuwa limepoa mno” nikaongea kwa utulivu huku nikitabasamu.
“Kahawa ni kinywaji kizuri sana hasa wakati wa baridi” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaongea kwa utulivu kisha akaweka kituo. Nilipomtazama haraka nikajua kuwa alikuwa akifikiria jambo fulani lakini hatimaye akavunja tena ukimya.
“Ukirejea kwenye maelezo yangu ya hapo awali sasa utagundua kuwa nchi ya Burundi tangu ilipopata uhuru wake kutoka kwa mkoloni mwaka 1962, tayari imeshatawaliwa na viongozi kumi na moja hadi kufikia wakati huu. Mapinduzi ya kijeshi yamefanyika mara nne na ndiyo maana hapo awali nikakueleza kuwa mapinduzi ya kijeshi katika nchi ya Burundi siyo jambo geni. Hivyo ni vizuri kuwa utakapokuwa unaingia kwenye nchi hii uwe unafahamu vizuri hali ya usalama wa nchi hiyo jinsi ilivyo” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaweka kituo akinyanyua kikombe na kuvuta funda jingine la kahawa huku akinitazama.
“Balozi Adamu Mwambapa alikuwa akiishi na familia yake huko nchini Burundi?” nikamuuliza jemadari yule huku na mimi nikikizoa kikombe changu pale mezani na kuvuta funda moja la kahawa.
“Hapana!, familia yake ipo Tukuyu mkoani Mbeya, kwenye nyumba yake aliyoijenga baada ya kustaafu. Ingawa mara kwa mara familia yake husafiri na kwenda kumsalimia huko jijini Bujumbura nchini Burundi, hususani pale anapokuwa ametingwa kwa muda mrefu na shughuli za kiofisi zinazo mnyima muda wa kurudi nchini Tanzania na kuisalimia familia yake”
“Familia ya balozi Adam Mwambapa imeshafahamishwa juu ya kutekwa kwake?”
“Bado haijafahamishwa kwani hata sisi wenyewe hatuna muda mrefu sana tangu tulipopata taarifa hizi. Kutakapopambazuka tutafanya utaratibu za kuipasha habari familia yake hasa baada ya kuandaa mazingira stahiki”
“Vyombo vya habari je vinafahamu?”
“Tumekubaliana kutovujisha taarifa hizi kwa vyombo vya habari. Hatutaki idara yetu ya usalama ionekane dhaifu na serikali ilaumiwe kwa kutokuwajibika ipasavyo kuwalinda viongozi wake. Hili ni agizo kutoka kwa rais lakini vilevile kuvujisha kwa taarifa hizi kwa waandishi wa habari kunaweza kumfanya mtu yeyote aliyehusika na tukio hili kuipima vizuri nguvu yetu ya usalama na hivyo kutukwepa kiulaini. Hivyo tumeonelea kuwa mambo yote yawe kimyakimya hadi hapo tutakapokuwa tumefanikiwa kwenye mipango yetu”
“Mmefanya vyema” nikaongea kwa msisitizo huku nikionesha kufurahishwa na hoja ile. Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akavuta tena funda jingine la kahawa na kuweka kikombe chake juu ya meza kisha akakohoa kidogo na kuendelea.
“Tunataka uende jijini Bujumbura nchini Burundi ukapeleleze kwa kina juu ya hili tukio la kutekwa kwa balozi wetu na ni matumaini yetu kuwa kwa moyo wako wa uzalendo utarudi salama hapa Dar es Salaam huku ukiwa umeongozananaye. Sitarajii kuwa itakuwa ni kazi rahisi lakini naamini kuwa utaifanya kwa weledi wako wote na kuiletea heshima kubwa idara yetu ya ujasusi na serekali yetu kwa ujumla” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaongea huku akinitazama kwa macho yake chakaramu. Ukimya wa mle ndani ukanipelekea nisikie kelele za mapanga boi ya feni namna yalivyokuwa yakikata upepo kwa utulivu kwenye ya dari ya ofisi ile.
“Rais wa Burundi kwa sasa yuko wapi?”
“Yupo hapa jijini Dar es Salaam kuhudhuria mkutano wa 13 wa viongozi wa nchi za Afrika Mashariki huku suala la machafuko ya kisiasa nchini Burundi likiwa ni ajenda kuu ya mkutano huo”
“Anafahamu juu ya kile kinachoendelea sasa hivi nchini kwake?”
“Nina hakika kuwa huwenda anafahamu lakini kwa wakati huu hawezi kuwa na msaada wowote kwetu. Tunachokifanya sisi ni sehemu ya wajibu wetu wa kikatiba katika kuhakikisha usalama wa raia wetu ndani na nje ya nchi. Hivyo hatuna sababu yoyote ya kuendelea kusubiri”....ITAENDELEA
 
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 4
Mtunzi:Kelvin Mponda

“Ni kweli” nikaongea kwa utulivu na hapo nikamuona Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akivuta mtoto mmoja wa meza yake ya ofisini kisha akachukua nyaraka fulani na kunikabidhi. Nilipozipokea na kuzichunguza kwa makini nikagundua kuwa zilikuwa ni pasipoti tatu za kimataifa za kusafiria.
Pasipoti ya kwanza ilinitambulisha kama raia wa Tanzania na kazi yangu ni mfanyabiashara mwenye jina la Paul Masha. Pasipoti ya pili ilinitambulisha kama mnyarwanda, kazi yangu dereva na jina langu ni Jean Baptiste Gatete na nilipochunguza vizuri katika zile nyaraka nikaona leseni ya udereva yenye utambulisho wa jina la Jean Baptiste Gatete, raia wa Rwanda. Pasipoti ya tatu na ya mwisho, ilinitambulisha kama raia wa Burundi mwenye jina la Céléstine Desire Bizimana, kazi yangu mfanyabiashara.
Nilipozikagua vizuri zile pasipoti nikagundua kuwa zote zilikuwa zimegogwa mihuri mara kadhaa katika vituo fulani vya uhamaji mipakani katika nchi zile katika namna ya kuonesha kuwa tayari nilikuwa nimefanya safari kadhaa maeneo hayo. Pia katika nyaraka zile kulikuwa na kadi tatu za ATM za benki tofauti zilizokuwa nchini Rwanda na Burundi. Mbali na kadi zile pia kulikuwa na vitambulisho vinne vyenye majina yangu.
Kitambulisho cha kwanza kilinitambulisha kama kada wa chama kilichokuwa madarakani nchini Burundi cha CNDD–FDD-Conseil National pour la Défense de la Démocratie-Forces de Défense de la Democratie. Kitambulisho cha pili kilinitambulisha kama kada wa chama pinzani cha siasa nchini Burundi kiitwacho MSD-Mouvement pour la Solidarité et la Démocratie na kitambulisho cha tatu kilinitambulisha kama kada wa chama kingine pinzani cha siasa nchini Burundi kiitwacho ADC-lˊAlliance des Democrates pour le Changement au Burundi (ADC-Ikibiri). Kitambulisho cha mwisho kilinitambulisha kama kada wa chama kingine pinzani cha siasa nchini Burundi kiitwacho FNL-Forces Nationales de Libération hapo mwanzo chama hicho kikifahamika kama PALIPEHUTU-FNL, kikundi hatari cha waasi kilichokuwa kikipigania maslahi ya watu wa kabila la wahutu nchini Burundi.
Kwa kweli nyaraka zile muhimu zilikuwa zimenishangaza sana. Sikujua ni wakati gani nyaraka zile zilikuwa zimeandaliwa hata hivyo nilikuwa nikiifahamu vizuri idara yetu ya ujasusi chini ya Brigedia jenerali Ibrahim Gambari namna ilivyokuwa makini katika kuratibu harakati za kijasusi. Hususani pale linapojitokeza suala la dharura kama la kutekwa kwa balozi wetu nchini Burundi, Meja jenerali mstaafu ndugu Adam Mwambapa. Kwa kweli nilikuwa nimeridhishwa vizuri na maandalizi yale ya safari ya kijasusi ya kushtukiza.
Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akavuta funda jingine la kahawa na alipokiweka kile kikombe pale mezani akanyanyua mkono na kuitazama saa yake ya mkononi kabla ya kuvunja tena ukimya.
“Taarifa za kiintelijensia zinaeleza kuwa tayari wimbi kubwa la wakimbizi kutoka nchini Burundi limeanza kumiminika kwenye kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu, Kasulu mkoani Kigoma hapa kwetu Tanzania. Hivyo tumeona kuwa lisingekuwa jambo la busara kuwa wakati wakimbizi hao wakiendelea kuingia hapa nchini wewe upishanenao katika njia hiyohiyo ukienda nchini Burundi. Sidhani kama hiyo ni njia salama isitoshe yeyote aliyefanya tukio hili huwenda akawa ametega mitego yake katika njia hiyo kumnasa mtu wetu yeyote tunayekusudia kumtuma.
Kwa hiyo tumeonelea kuwa itakuwa vyema ukiingia nchini Burundi kwa kutokea jijini Kigali nchini Rwanda na nyaraka nilizokupa bila shaka zinatosha kukamilisha mpango huo. Wakati utakapokuwa kwenye harakati nadhani unajua ni namna gani ya kuwasiliana na mimi au idara yetu ya ujasusi. Hivyo ni matumaini yangu kuwa utakuwa ukinijulisha kwa ukaribu kila hatua utakayofikia” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akahitimisha maelezo yake kisha akaitazama tena saa yake ya mkononi na aliporidhika na mwenendo wa majira yake akakinyakua kile kikombe chake cha kahawa pale mezani na kugida funda la mwisho la kahawa. Alipokitua kile kikombe pale juu mezani tayari kilikuwa tupu.
Nilifahamu kuwa tukio lile lilikuwa limeashiria kuwa maongezi yetu mle ndani na Brigedia jenerali Ibrahim Gambari yalikuwa yamefika tamati. Hivyo na mimi nikachukua kikombe changu cha kahawa pale mezani na kugida mafunda mfululizo hadi pale kahawa ile ilipoisha na wakati nikifanya vile Brigedia jenerali Ibrahim Gambari alikuwa akinitazama kwa utulivu.
Nilikuwa wa kwanza kusimama muda mfupi kabla Brigedia jenerali Ibrahim Gambari kufanya hivyo na hapo nikafunga mguu wangu na kupiga saluti ya heshima mbele ya jemadari yule ambapo aliitikia vyema na kunipa mkono wa kuagana.
“Nakutakia safari njema yenye mafanikio Tibba. Tambua kuwa nimekupa jukumu hili kwa sababu nakuamini sana kijana wangu” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaongea kwa sauti tulivu ya kusihi na katika sauti yake nikaiona hali ya huruma na unyenyekevu huku simanzi na masikitiko yakiwa yamejificha nafsini mwake.
“Mungu atanitangulia” nikaongea kwa utulivu huku nikilazimisha tabasamu usoni mwangu ingawa tabasamu hilo lilikataa kabisa kuumbika pale nilipoanza kutafakari juu safari zangu za kijasusi namna zilivyokuwa zikitawaliwa na mazingira ya hatari katika kuupigania uhai wangu. Wakati nikilichukuwa begi langu na kulitundika begani Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akanikabidhi tiketi ya ndege ya shirika la ndege la RwandaAir yenye jina langu ambayo ingenisaidia kusafiri hadi jijini Kigali nchini Rwanda kabla ya kuendelea mbele na safari yangu.
“Mayunga atakupeleka hadi uwanja wa ndege wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaongea kwa utulivu huku akinitazama. Nikaipokea ile tiketi na kuichunguza kwa makini na kwa kufanya vile nikaliona jina langu la bandia la Paul Masha na hapo tabasamu hafifu likaniponyoka usoni. Tiketi ile ya ndege ilikuwa ikinionesha kuwa ningesafiri saa kumi usiku na ndege ya shirika la ndege la RwandaAir iliyokuwa ikitokea jijini Nairobi kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa Jomo Kenyatta nchini Kenya.
“It is our responsibility to defend the respect of our government and the territories of our country as well!” Brigedia jenerali Ibrahim Gambari akaongea kwa utulivu huku akinipigapiga begani kwa mkono wake na kutabasamu katika namna ya kunitia moyo.
“I love my country sir! and not my government” nikamwambia Brigedia jenerali Ibrahim Gambari huku na mimi nikimpigapiga begani kwa ucheshi kisha nikaanza kuzitupa hatua zangu taratibu nikiondoka kwenye ofisi ile.
Muda mfupi baadaye nikaufikia mlango wa ile ofisi na kuufungua huku nikiwa na hakika kuwa macho ya Brigedia jenerali Ibrahim Gambari yalikuwa nyuma yangu yakinisindikiza. Mara nilipoufungua ule mlango nikageuka na kumtazama tena Brigedia jenerali Ibrahim Gambari na nilichokiona usoni mwake lilikuwa ni tabasamu la mwisho la kuagana huku jemadari yule akiwa ameitia mikono yake mifukoni. Bila kupoteza muda nikamtupia tabasamu jepesi la buriani kisha nikatoka nje ya ofisi ile na kufunga mlango.
_____
Nilimkuta Koplo Mayunga akiwa tayari amepitiwa na usingizi huku ameuegemea usukani wa gari lile la jeshi Nissan Patrol, katika eneo la maegesho ya magari la ofisi zile za makao makuu ya idara ya ujasusi jijini Dar es Salaam. Askari yule makini akawahi kushtuka kutoka usingizini wakati nikiukaribia mlango wa mbele wa gari lile na hapo akawahi kushusha kidogo kioo cha mlangoni na kunitazama. Kisha akajisogeza upande wa pili akifanya jitihada kidogo za kufyatua kabari ya mlango ule. Bila kusubiri zaidi nikaufungua ule mlango wa sehemu ya abiria kando ya dereva na kuingia ndani. Koplo Mayunga akanikaribisha kwa bashasha zote huku uso wake ukitengeneza tabasamu hafifu la kichovu kwani macho yake legevu yaliashiria kuwa alikuwa katikati ya lepe zito la usingizi.
“Nipeleke uwanja wa ndege wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere bila kupoteza muda kwani nina safari nzito ya kikazi” nikamwambia Koplo Mayunga huku nikilitupia begi langu kwenye siti ya nyuma na kisha kufunga vizuri mkanda wa siti yangu tayari kuanza safari.
“Vipi afande kuna usalama?” Koplo Mayunga akaniuliza kwa udadisi wakati akiwasha gari na kulitoa kwenye yale maegesho.
“Mambo siyo shwari ndugu yangu, nimekabidhiwa jukumu zito na sina budi kuwajibika” nikaongea kwa utulivu wakati tulipokuwa tukiyaacha maegesho yale.
“Pole sana afande wangu!” Koplo Mayunga akanifariji huku akiliondoa gari kwenye maegesho yale na kuingia mitaani.
“Nishapoa!” nikaongea kwa utulivu huku akili yangu ikianza kuzama kwenye tafakuri ya kina juu ya safari ile ya kijasusi isiyoeleweka vizuri. Koplo Mayunga hakuwa mtu wa maneno mengi hivyo baada ya pale kikafuatia kitambo kirefu cha ukimya wakati tulipokuwa tukiiacha barabara ya mtaa mmoja na kuingia barabara ya mtaa mwingine kuelekea uwanja wa ndege wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere jijini Dar es Salaam.
Tulikuwa tumefika mbali katika safari yetu wakati Koplo Mayunga alipoyarudisha tena mawazo yangu mle ndani na kuniuliza.
“Unasafiri na ndege ya saa ngapi afande?”
“Saa kumi usiku huu”
“Ondoa shaka kwani tutawahi kufika kiwanja cha ndege mapema zaidi” Koplo Mayunga akaongea kwa utulivu akinitia moyo hata hivyo sikutia neno badala yake nikayapeleka macho yangu dirishani nikitazama mandhari ya barabara za jiji la Dar es Salaam usiku ule.
Hali ya hewa ilikuwa tulivu na giza zito lilikuwa limetanda angani. Wakati tukiendelea na safari njiani tulipishana na magari machache na kwa kuwa wakati ule wa usiku hapakuwa na foleni za magari hivyo mwendo wetu ulikuwa wa kasi sana na hivyo kuyapeleka magurudumu ya gari letu kuteleza kwenye barabara ile ya lami kama kambare kwenye tope. Wakati ule wa usiku maduka yaliyopakana na barabara za jiji la Dar es Salaam yalionekana kufungwa na baadhi ya magari yalionekana kuegeshwa kwenye sehemu za wazi au kwenye gereji bubu.
Niliitazama mitaa ile ya jiji la Dar es Salaam huku kichwani nikijiuliza kama ningepata nafasi nyingine ya kuizuru mitaa ile nikiwa hai. Hisia zangu ziliniambia kuwa nilikuwa nikielekea kukabiliana na jambo kubwa la hatari sana ingawa picha kamili ya hatari hiyo ilikataa kuumbika kichwani. Nikaendelea kuzikumbuka ndoto zangu za ujanani za kuwa na mafanikio mazuri kama kuwa na mke mwema na watoto wenye siha njema lakini sasa ndoto zile nilianza kuzitilia mashaka kama kweli zingetimia wakati nilipoziweka kwenye tathmini ya mzani wa kifo.
Kama isingekuwa kiapo cha kazi ya jeshi leo hii ningeweza kabisa kukataa ombi la Brigedia jenerali Ibrahim Gambari kisha na ningeandika barua ya kuomba kustaafu na baada ya kulipwa mafao yangu ningeamua kufanya biashara au shughuli nyingine halali za kujiingizia kipato kama walivyo watanzania wengi. Lakini jambo hilo kwa sasa lisingewezekana kwani woga ulikuwa ni kinyume kabisa na taratibu za jeshi letu. Hata hivyo japokuwa kazi ya ujasusi ilikuwa ni kazi ya roho mkononi lakini niseme kuwa nilikuwa nikiipenda sana kuliko kazi yoyote nyingine duniani hali iliyonipelekea niifanye kwa weledi wa hali ya juu na jitihada za aina zote na hivyo kunipelekea kila nitumwapo nirudi na majibu mazuri ya kushangaza huku ugumu wa kazi yenyewe ukiendelea kuwa siri yangu moyoni. Nikiwa bado nimezama kwenye tafakuri ile nikajikuta nikiyakumbuka makovu matatu ya risasi yaliyokuwa kwenye paja langu la mguu wa kushoto na makovu mengine ya misumari yaliyokuwa viganjani ambayo nilikuwa nimeyapata kwenye harakati zangu mbalimbali za kajasusi. Kwa kweli nikajikuta nikimeza funda kubwa la mate kuzitowesha kumbukumbu zile mbaya.
Mawazo yangu yaliporudi tena mle ndani ya gari nikashtuka kuwa tayari tulikuwa tumefika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Mara baada ya kuvuka geti la kuingilia kiwanjani pale Koplo Mayunga akaendesha gari taratibu huku akiyatembeza macho yake huku na kule akitafuta sehemu nzuri ya maegesho na baada ya muda mfupi hatimaye akawa amepata sehemu nzuri ya maegesho na kusimama.
Sikuwa na muda wa kupoteza kwani kwa mujibu wa ratiba iliyokuwa kwenye tiketi ile ya ndege niliyopewa na Brigedia jenerali Ibrahim Gambari ni kuwa zilikuwa zimesalia dakika ishirini tu kabla ya ndege ya shirika la ndege la RwandaAir kuanza safari yake ya kuelekea jijini Kigali nchini Rwanda. Hivyo bila kupoteza muda nikafyatua kabari ya mkanda wa siti yangu kisha nikachukua begi langu kutoka ile siti ya nyuma na kushuka. Koplo Mayunga alitaka kushuka garini na kunisindikiza hata hivyo nilimshukuru na kumtaka asipoteze muda wake kwani nilikuwa na muda mfupi sana kabla kuanza safari yangu kuelekea jijini Kigali nchini Rwanda hivyo tukaagana bila yeye kushuka.
Koplo Mayunga akaniaga kwa kunipungia mkono dirishani huku akinitakia safari njema yenye mafanikio katika harakati zangu. Nikamshukuru huku nikiliacha tabasamu langu likijivinjari usoni mwangu ingawaje moyoni nilihisi kuwa ni kama aliyekuwa akiniambia pumzika kwa amani mpiganaji.
_____
Mtikisiko uliotokea baada ya magurudumu ya ndege ya shirika la ndege la RwandaAir, Boeing 737-800 kuanza kutua kwenye kiwanja cha ndege cha kimataifa cha Kigali International Airport ukanishtua kutoka usingizini. Nilipoyafumbua macho yangu nikayatembeza taratibu mle ndani ya ndege nikitazama huku na kule na kwa kufanya vile nikagundua kuwa abiria wenzangu wote mle ndani walikuwa macho tayari wamejiandaa kwa tukio lile la kutua kwa ndege. Hivyo haraka nikajua kuwa ni mimi tu ndiye ambaye nilikuwa sijaisikia sauti ya msichana mrembo mhudumu wa ndege ile wakati alipokuwa akiwatangazia abiria wa ndege ile kufunga mikanda wakati ndege ile ilipokuwa ikijiandaa kutua.
Kushoto kwangu alikuwa amekaa mama mmoja wa kinyarwanda ambapo nilikuwa nimemtambua haraka kutokana na mwonekano wake huku akiwa na watoto wake wawili, mmoja wa kike na mwingine wa kiume. Hata hivyo watoto wale walikuwa wamepitiwa na usingizi huku wamezuiliwa vyema na mikanda ya siti za ndege ile. Nilipoyapeleka macho yangu kutazama dirishani mara moja nikauona mwanga hafifu wa pambazuko la alfajiri na hapo nikakumbuka kuitupia macho saa yangu ya mkononi. Majira yalionesha kuwa tayari ilikuwa imetimia saa kumi na mbili na robo alfajiri na hapo nikajua kuwa tulikuwa tumetumia muda wa masaa mawili na dakika ishirini tangu tulipoanza safari kutoka uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere jijini Dar es Salaam hadi uwanja ule wa ndege wa kimataifa wa Kigali nchini Rwanda...ITAENDELEA
 
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 5
Mtunzi:Kelvin Mponda

Muda mfupi baada ya ndege yetu kusimama mbele ya jengo la uwanja ule wa ndege mlango wa ndege ulifunguliwa na hapo abiria wakaanza kushuka. Usingizi wa masaa mawili safarini ulikuwa umenipunguzia uchovu kwa kiasi kikubwa hivyo nikafyatua mkanda wa siti na kusimama. Nililichukua begi langu dogo la mgongoni kutoka sehemu maalum ya kuwekea mizigo kwenye sehemu ya juu ya ndege ile kisha nikaunga kwenye foleni ya abiria waliokuwa wakishuka. Abiria tuliyokuwa tukishuka kwenye ndege ile tulikuwa wachache na hapo nikakumbuka kuwa ndege ile ilikuwa ikielekea Entebbe International Airport, kiwanja cha ndege cha kimataifa cha nchi ya Uganda.
Mara tuliposhuka kwenye ile ndege tukaingia kwenye jengo kubwa la kiwanja kile cha ndege cha Kigali lenye migahawa ya kisasa na ofisi mbalimbali za utawala zikiwemo ofisi za uhamiaji za nchi ya Rwanda. Kwa kuwa sikuwa na mzigo wowote mkubwa nikawatangulia abiria wenzangu wenye mizigo nikipenya haraka na kulifikia dirisha moja la ofisi za uhamiaji ziliyokuwa pale kiwanjani.
Nilipofika kwenye dirisha lile nikapenyeza vibali vyangu vyote vya kusafiria kwenye dirisha dogo la kioo la chumba kidogo kilichomhifadhi msichana mmoja mlimbwende aliyeonekana kuyazingatia vema maadili ya kazi yake kwa uchangamfu wa sura yake. Msichana yule afisa uhamiaji akavipokea vibali vyangu vya kusafiria huku akinipa pole ya uchovu wa safari na kuliachia tabasamu lake maridhawa likizitongoza fikra zangu.
Mambo yote yalikuwa chapuchapu kwani yule afisa uhamiaji alimaliza haraka kuingiza taarifa zangu kwenye kompyuta yake kisha akagonga mhuri kwenye hati yangu ya kusafiria na kuniruhusu kuingia rasmi nchini Rwanda. Bila kupoteza muda nikaipokea hati yangu ya kusafiria na kuitia mfukoni huku tabasamu langu la kichokozi likizigalagaza vibaya hisia za afisa yule mlibwende. Kisha nikamkonyeza kidogo kumchombeza huku nikianza kuzitupa hatua zangu kwa utulivu kuliacha eneo lile. Afisa yule uhamiaji akabaki ameduwaa kwa furaha huku macho yake yakinisindikiza nyuma yangu hadi pale nilipopotea mbele yake.
Hali ya hewa ya baridi ya wastani yenye kiasi kikubwa cha unyevunyevu ikanikumbusha kuwa sikuwa nchini Tanzani, jijini Dar es Salaam kama nilivyozoea na badala yake hali ile ilikuwa ni ishara tosha kuwa tayari nilikuwa nimeikanyaga ardhi ya nchi ya Rwanda, jijini Kigali.
Nilikuwa na kiasi kidogo cha faranga za kinyarwanda ambacho nilikuwa nimekipata baada ya kubadilisha kwa shilingi za kitanzania kabla ya kuanza safari yangu jijini Dar es Salaam katika duka moja la kubadilisha fedha za kigeni lililokuwa kule kwenye kiwanja cha ndege cha kimataifa cha Mwalimu Julius Kambarage Nyerere jijini Da es Salaam.
Hii haikuwa mara yangu ya kwanza kufika nchini Rwanda hususani jijini Kigali hivyo kwa kiasi fulani sikuwa mgeni kabisa wa mazingira yale ingawa sikuwa nimewahi kufika jijini Bujumbura nchini Burundi. Hivyo mara baada ya kutoka nje ya uwanja ule wa ndege wa kimataifa wa Kigali dereva mmoja wa teksi mjanja akaniwahi haraka kabla ya wenzake baada ya kuhisi hitaji langu. Mzee yule wa makamo mrefu na mwembamba mwenye sura ya ucheshi akiwa amevaa kofia nyeusi ya pama, shati jeupe na sweta jeusi, suruali ya kijivu na makubasi ya ngozi miguuni akawahi kunifungulia mlango wa teksi yake hata kabla sijaafikiana naye na kumueleza hitaji langu. Kwa ushawishi ule sikuwa na pingamizi hivyo nikaingia ndani.
Mara tu nilipoingia ndani ya ile teksi yule dereva wa teksi akanisemesha kwa lugha ya kinyarwanda na alipoona kuwa sielekei kumuelewa akabadili lugha na kunisemesha kwa kifaransa. Sikuwa mgeni wa lugha ile kwani miongoni mwa lugha nilizokuwa nikizifahamu na kuzizungumza vizuri ilikuwa ni lugha ya kifaransa. Idara yangu ya kijasusi ilikuwa imenipeleka jijini Paris nchini Ufaransa kujifunza vizuri lugha ya kifaransa kwa muda wa miaka mitatu. Kisha miaka miwili mingine nikiitumia jijini Lisbon nchini Ureno kujifunza vizuri lugha ya kireno na hatimaye mwaka mmoja nikiutumia katika chuo kikuu cha Cape town nchini Afrika ya kusini kukipiga vizuri msasa kiingereza changu.
“Toi cʼest un Rwandais?” Wewe ni mnyarwanda? dereva yule akaniuliza
“Non, je ne suis pas un Rwandais, je suis un Burundais” Mimi siyo mnyararwanda, mimi ni raia wa Burundi, nikaongea kwa utulivu
“Oh! donc toi cʼest un Burundais, bienvenu à Kigali. Moi je suis un Tutsi, et toi?” Oh! kumbe wewe ni raia wa Burundi, karibu sana Kigali. Mimi ni mtutsi wewe je?
Nikaupisha utulivu nikimtazama mzee yule huku nikiwa nimeshtushwa na namna hisia za ukabila zilivyokuwa zikimtafuna nafsini mwake kwa kitendo cha kujitambulisha kwangu kuwa yeye ni mtutsi. Hata hivyo sikutaka kutofautiana na hisia zake.
“Moi aussi je suis un Tutsi, bien que je ne peus pas parler cette langue” Mimi pia ni mtutsi ingawa siwezi kuzungumza lugha hiyo. Maelezo yangu yakampelekea yule mzee aangue kicheko hafifu kabla kuniambia
“Ça ne mʼetone pas, car la plus part de jeunes de ce jours ne connaîssent pas leur langue maternelle” Sishangai kwanini vijana wengi wa zama hizi hawajui kuzungumza lugha zao za asili, wengi wanadhani ni ushamba.
Maelezo yale yakapelekea wote kwa pamoja tuangue kicheko hafifu cha katikati ya maongezi na kabla kicheko kile hakijafika ukomo yule mzee dereva wa teksi akaniuliza.
“Tu ne mʼa pas encore dis là où tu vas?” Bado hujaniambia unaelekea wapi?
“Amaine moi à Nyabugogo, où il ya la guarre des bus qui maine vers Bujumbura” Nipeleke Bugogo ilipo stendi ya mabasi ya kuelekea Bujumbura.
Kitambo kifupi cha ukimya kikafuatia wakati mzee yule dereva wa teksi akiitoa teksi yake kwenye maegesho yale ya teksi ya uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kigali. Sehemu ya maegesho teksi maarufu kama Kanombe Airport Park na kuingia barabara ya KK 18 Avenue na wakati tukiingia kwenye barabara ile nikakumbuka kumuuliza yule dereva.
“Ça coute combine dʼici jusquʼ à Nyabugogo?” Ni pesa kiasi gani kutoka hapa hadi Nyabugogo?
“30 franc seulement mon jeune garçon” Faranga 30 tu kijana wangu, yule dereva wa teksi akaniambia
“Amaine moi, sʼil vous plait!” Nipeleke tafadhali!
Safari yetu ikaendelea na tulipofika mbele kidogo sehemu kulipokuwa na barabara pacha tukaiacha barabara ya KK 18 Avenue na kuingia upande wa kushoto tukiifuata barabara ya mtaa wa KK 218. Safari yetu ikaendelea mbele na baada ya kitambo kifupi cha safari ile tukawa tumeifikia barabara nyingine pacha. Tulipofika pale mara nikamuona yule mzee dereva wa ile teksi akiingia upande wa kulia akiiacha barabara ya mtaa wa KK 271 kushoto kwake na kuingia barabara ya upande wa kulia ya Airport View. Wakati tukiendelea na safari mara nikakumbuka kumuuliza yule dereva.
“Est ce que, je peus trouver le bus qui va à Bujumbura ce matin?” Nitaweza kupata basi la kuelekea Bujumbura asubuhi hii?
“Ne tʼinquiéte pas!” Ondoa shaka!, yule mzee akaniambia kabla ya kuendelea.
“Ce matin il y a beaucoup de bus, qui vont à Bujumbura, Nairobi, Kampala, jusquʼ à Kigoma Tanzanie” Muda huu wa asubuhi mabasi huwa ni mengi sana pale, kuelekea Bujumbura, Nairobi, Kampala hadi Kigoma Tanzania.
Wakati tukiendelea na safari nikayatembeza macho yangu taratibu kutazama kwenye vioo vya ubavuni vya lile gari ili kuchunguza kama kungekuwa na gari lolote likitufuatilia. Niliporidhika kuwa hakuna gari lolote lililokuwa limetufungia mkia nyuma yetu nikageuka na kumtazama yule dereva wa teksi kabla ya kuanza kuyatathmini vizuri mandhari ya eneo lile tulilokuwa tukilipita. Kitu cha kwanza kilichokuwa kimenivutia ni juu hali nzuri ya usafi iliyokuwa katika jiji la Kigali pamoja na mpangilio mzuri wa makazi ya watu ingawaje kwa wakati ule watu wengi walikuwa majumbani mwao.
Baada ya kitambo kifupi cha safari yetu hatimaye tukawa tumetokezea kwenye barabara kuu ya magari iliyokuwa ikifahamika kama barabara ya KN 5. Mara tu tulipoingia kwenye barabara ile tukashika uelekeo wa upande wa kushoto huku upande wa kulia kwetu tukiiacha sehemu ya maegesho ya teksi ya eneo la Remera inayofahamika kama Remera Taxi Park. Baada ya kuingia kwenye barabara ile mwendo wetu ukaongezeka huku dereva yule wa teksi akionekana kuwa makini na sheria zote za barabarani wakati tulipokuwa tukipishana na magari machache na watembea kwa miguu kando ya barabara ile.
Safari yetu ikiwa inaendelea mimi nikatumia wasaa ule kufanya utalii usio rasmi. Kwanza nikaiona Ndoli Joint Supermarket upande wa kushoto kwenye mzunguko wa barabara kuelekea tawi la benki ya Equity eneo la Kisimenti na sehemu ulipo uwanja wa mpira wa miguu wa Amahoro. Tulipoupita mzunguko ule wa barabara tukaendelea mbele na safari huku nikiyashuhudia majengo marefu ya ghorofa yaliyokuwa yamepakana na barabara ile upande kwa upande wa kushoto na kulia.
Safari yetu ikiwa inaendelea upande wa kushoto nikauona mgahawa wa kisasa wa kiitaliano uitwao Sole Luna Italian ukifuatiwa na hoteli ya Beauséjour. Bado tuliendelea na safari tukiifuata barabara ile kuu ya magari. Baada ya kitambo kirefu cha safari ile hatimaye tukawa tumeufikia mzunguko mkubwa wa barabara uitwao KG 2 Round About baada ya kulipita jengo la bunge la Rwanda upande wa kulia. Mara tu tulipomaliza kuuzunguka mzunguko ule wa barabara mbele yetu nikaliona jengo la Casino Kigali. Dereva wa ile teksi akaiacha barabara KN 5 upande wa kushoto ielekeayo eneo la Kigali Centenary Park akiifuata barabara ya RN 3.
Safari ikaendelea na wakati tukiendelea kuifuata barabara ile mbele kidogo upande wa kulia nikaliona jengo la Discover Rwanda Youth Hostel, kisha jengo la British High Commission upande wa kushoto. Tulipozidi kusonga mbele upande wa kulia nikaiona hoteli yenye hadhi ya nyota nne iitwayo Hotel Umubano, kisha tukalipita jengo la Carnegie Mellon University la nchini Rwanda. Barabara ile ilikuwa ikikatisha kwenye eneo lenye majengo mengi yaliyokuwa yakitumika kama ofisi za serikali ya Rwanda na taasisi nyingi za kimataifa. Yule dereva wa teksi akionekana kuanza kuchoshwa na ukimya uliokuwa ukiendelea kushika hatamu mle ndani akanichokoza kwa swali.
“Tu viens dʼoù?” Unatoka wapi?
“Je vien du Congo Kinshasa” Natokea Congo Kinshasa, nikamjibu kwa utulivu dereva yule wa teksi na hapo akaendelea kuniuliza.
“Pour quoi tu nʼa pas dessandu à lˊaéroport de Bujumbura?” Kwanini hukushukia uwanja wa ndege wa Bujumbura?
“Lʼavion que je me suis envolé avec, passé ici à Kigali, et jʼai vu que cʼest ne pas mauvais si jʼatterrisse ici, et aller à Bujumbura par bus” Ndege niliyopanda ilikuwa inapitia hapa Kigali hivyo nikaona siyo vibaya kushukia hapa ili niende Bujumbura kwa usafiri wa basi. Maelezo yangu yakampelekea yule mzee dereva wa teksi ageuke kidogo na kunitazama kisha kitambo cha ukimya kikafuatia huku nikiwaza kuwa huwenda alikuwa akiyatafakari kwa kina yale maelezo yangu. Safari ikaendelea na baada ya kitambo kifupi cha safari ile mara nikamuona tena yule dereva wa teksi akigeuka na kutazama upande wa kulia wa ile barabara kabla ya kuvunja tena ukimya akiniuliza.
“Tu as vis votre ambassade du côté droit?” Umeziona ofisi za ubalozi wenu upande wa kulia?. Swali la yule dereva wa teksi likanipelekea haraka nigeuke na kutazama upande wa kulia wa ile barabara na hapo nikaliona jengo la ofisi za ubalozi wa Burundi. Kuliona lile jengo kukanifanya nikumbuke kuwa nilikuwa nimemdanganya yule dereva wa teksi kuwa mimi ni raia wa Burundi hivyo haraka nikajua kwendana na maongezi yale.
“Oui, jʼai déjà été là plusière fois, quand jʼai travaillé ici au Rwanda” Ndiyo, nimewahi kufika pale mara kadhaa wakati nilipokuwa kikazi hapa Rwanda. Nikamwambia yule dereva wa teksi huku nikiyapa utulivu macho yangu kulitazama lile jengo lenye ofisi za ubalozi wa Burundi nchini Rwanda.
Tulipofika mbele kidogo upande wa kulia nikaliona jengo kubwa la ghorofa la ofisi kuu ya idara ya uhamiaji ya nchi ya Rwanda ama Rwanda Immigration and Emigration. Safari ikaendelea na tulipolipita lile jengo mbele kidogo tukakutana na mzunguko mwingine wa barabara ambapo tuliuzunguka taratibu na kushika uelekeo wa upande wa kulia tukilipita jengo la ghorofa la hoteli ya Grill Marks kwa upande wa kulia. Safari yetu bado ikaendelea na baada ya kitambo kifupi cha safari ile mbele tukaja kukutana na barabara pacha. Tulipofika pale tukaiacha barabara ya KN 8 Avenue upande wa kulia na kunyoosha mbele tukiifuata barabara ya mtaa wa KG 704 iliyokuwa ikikatisha katikati ya makazi ya watu wenye afya kiuchumi. Wakati tukiingia kwenye barabara ile yule dereva wa teksi akavunja tena ukimya akiniambia.
“Jʼai eu ľinformation quʼll y a eu un type dˊattentat contre le gouvernement de president Nkurunziza à Bujumbura au Burundi” Nimesikia vyombo vya habari vikitangaza kuwa kumefanyika jaribio la mapinduzi ya kijeshi dhidi ya serikali ya rais Nkurunziza, Bujumbura nchini Burundi.
“Oui, même moi aussi je lʼai compris, et je pense que cˊest pour ce la même les vols iternationaux à lʼaéroport, de Bujumbura ont été areter, à cause de lʼinsécurite” Ndiyo, hata mimi nimesikia, nadhani ndiyo maana hata safari za ndege za kimataifa zimesitishwa kwenye uwanja wa ndege wa Bunjura kuhofia usalama.
Bado tuliendelea na safari yetu na tulipofika mbele tukaingia upande wa kulia tukiifuata barabara ya mtaa wa KG 702 halafu mbele kidogo tukakutana na barabara ya RN 3. Tulipoifikia barabara ile tukaingia upande wa kushoto tukiifuata barabara ya KN 8 Avenue. Mara tu tulipoingia kwenye barabara ile mwendo wetu ukaongezeka na nilipochunguza nikagundua kuwa tulikuwa tukizunguka kurefusha safari. Tukio lile likanifanya nigutuke kuwa yule dereva wa teksi alikuwa akifanya ujanja wa kunizungusha ili hatimaye anitoze pesa nyingi kwa safari ile. Hata hivyo nilimezea kwani kwa upande mwingine nilikuwa nimefurahi kwa kulitalii jiji lile la Kigali nchini Rwanda japo kwa sehemu tu.
Kufikia wakati ule sehemu nyingi za jiji la Kigali zilikuwa zimeanza kuchangamka huku watu wakijitokeza na shughuli nyingine za kibinadamu zikianza kufanyika katika baadhi ya maeneo. Maduka yalikuwa yameanza kufunguliwa na baadhi ya ofisi za kutoa huduma muhimu kama benki na posta...ITAENDELEA
 
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 6
Mtunzi:Kelvin Mponda
Baada ya kitambo kifupi cha safari ile mara tukalipita jengo la BK ATM upande kulia na kisha kukatisha katikati ya kituo cha kujazia mafuta cha Hashi Energy upande wa kushoto na kituo kingine cha kujazia mafuta cha Kobil upande wa kulia. Baada ya safari fupi mbele kidogo tukaja kukutana na barabara nyingine kubwa ya magari iitwayo KN 7. Tulipofika pale tukaingia upande wa kulia tukiifuata barabara KN 7 kwa upande wa kulia.
Sasa tulikuwa tukielekea eneo la Nyabugogo sehemu ilipokuwa stendi kuu ya mabasi ya kuelekea jijini Bujumbura nchini Burundi. Baada ya safari ndefu hatimaye tukawasili stendi kuu ya Nyabugogo ya mabasi ya kuelekea maeneo ya mbali na jiji la Kigali na nje ya nchi ya Rwanda. Maeneo kama Bujumbura nchini Burundi na Kigoma nchini Tanzania. Yule dereva wa teksi akataka kunishushia kando ya kituo cha maegesho ya teksi cha stendi kuu ya Nyabugogo hata hivyo kwa kuwa sikutaka kusumbuliwa na madereva wa teksi waliokuwa eneo lile hivyo nikamwambia anishushie nje ya jengo la Banque Commerciale du Rwanda. Umbali mfupi kutoka yalipokuwa makutano ya barabara ya Kigali kwenda Gatuma. Barabara ya KN 1 na ile barabara ya KN 20 Avenue.
Bila kupoteza muda nikachukua wallet yangu kutoka mfukoni na kuhesabu faranga 20 za pesa ya kinyarwanda na kumpa na wakati akizipokea na kuzihesabu nikamwambia.
“Merci pour votre meyen de transport” Nashukuru kwa usafiri. Yule dereva wa teksi haraka akamaliza kuhesabu zile pesa na kuzitia mfukoni huku uso wake ukitengeneza tabasamu la kirafiki.
“Ne te derange pas, dʼautre fois quand tu arrives à lʼaéroport, et tu as besoin de transport, chercher moi au nom de Gael Mugenzi” Ondoa shaka wakati mwingine ukifika pale kiwanja cha ndege, ukihitaji usafiri niulizie kwa jina la Gael Mugenzi. Nikatikisa kichwa huku nikitabasamu katika namna ya kumuonesha yule dereva wa teksi kuwa nilikuwa nimeafikiana vizuri na hoja yake huku nikifahamu fika kuwa uwezekano wa mimi kuonana naye ulikuwa mdogo na pengine mahusiano yetu yalikuwa yakiishia pale.
“Ne te derange pas!” Ondoa shaka!, nikaongea huku nikifungua mlango wa ile teksi na kushuka.
“Bon voyage Monsieur” safari njema ndugu, yule mzee dereva wa teksi akaniambia na kuniaga kwa kunipungia mkono dirishani huku tabasamu lake la kibiashara likigoma kwenda likizo kisha akageuza teksi na kushika uelekeo wa kule tulipotoka.
Niliendelea kusimama eneo lile nikiitazama ile teksi namna ilivyokuwa ikitokomea mitaani kisha nikashika uelekeo wa kwenye lile jengo la Banque Commerciale du Rwanda, eneo lile la Nyabugogo.
Kulikuwa na magari machache yaliyokuwa yameegeshwa nje ya jengo lile la benki wakati nilipokuwa nikikatisha kuelekea ndani ya lile jengo. Mara tu nilipoingia mle ndani nikashtukia kuwa benki ile ndiyo kwanza ilikuwa inafunguliwa muda ule kwani mle ndani kulikuwa na wateja wachache sana. Niliuacha upande wa kushoto kwenye ofisi za benki ile zinazoshughulika na masuala ya mikopo na huduma kwa wateja nikashika uelekeo wa kulia kwenye madirisha matano ya kuta za vioo yaliyokuwa na wahudumu wa benki ile. Nilichagua dirisha moja lenye msichana mrembo mfanyakazi wa benki ile kisha nikapenyeza kadi yangu ya visa nikitaka kuchukua pesa ya kutosha ambayo kwa namna moja au nyingine nisingeweza kuitoa kupitia mashine za ATM za benki ile zilikokuwa nje ya lile jengo.
Msichana yule akanisalimia kwa bashasha zote huku akionekana kubabaika kidogo na uzuri wangu na kwa kweli niseme kioo cha kabati langu kule nyumbani kwangu Dar es Salaam siku zote hakikuacha kuniridhisha kuwa nilikuwa miongoni mwa wanaume wachache wenye mvuto wa hali ya juu kwa wasichana warembo wa sampuli ile. Nilihudumiwa haraka baada ya kumaliza kujaza fomu ya kutolea pesa kupitia kadi yangu ya visa na baada ya muda mfupi kupita nikakabidhiwa kiasi kile cha pesa katika dola za kimarekani. Kisha nikatenga kiasi kingine cha pesa kutoka katika zile dola za kimarekani na kukibadili kwenda kwenye pesa ya faranga za Burundi. Nilipomaliza nikamshukuru yule msichana mrembo mfanyakazi wa ile benki kwa kunifanyia kazi ile kwa haraka isiyo ya kawaida na kwa kweli roho yangu haikutaka nimuache hivihivi. Hivyo nikampa yule dada ahsante ya pesa yenye thamani ya mlo mmoja kamili wa mchana kwenye hoteli ya daraja la tatu huku nikiitia pesa yangu mfukoni na kushika uelekeo wa nje ya lile jengo la benki ya biashara ya Rwanda.
Saa yangu ya mkononi ilionekana kuwa ilikuwa ikielekea kutimia saa mbili kasoro asubuhi wakati nilipokuwa nikitoka nje ya benki ile kuelekea eneo ilipokuwa stendi ya mabasi ya kuelekea jijini Bujumbura nchini Burundi. Jua lilikuwa limeanza kuchomoza ingawaje hali ya hewa ilikuwa ya baridi ya kiasi na siyo kama lile joto la jiji la Dar es Salaam nchini Tanzania. Pilika za watu zilikuwa zimeanza kushamiri na hivyo kuupelekea mji ule kuanza kuchangamka. Tofauti na vile hapakuwa na ziada nyingine kwani miji mingi ya bara la Afrika kwa namna moja au nyingine ilikuwa ikifanana kwa mandhari na maendeleo.
Maelekezo kupitia kwenye mabango ya kando ya barabara hatimaye yakanifikisha kwenye ofisi za mabasi ya kuelekea jijini Bujumbura nchini Burundi katika stendi ile ya Nyabugogo. Kama yalivyokuwa maeneo mengi ya stendi za mabasi hususani katika nchi za Afrika basi stendi ile ya mabasi ya Nyabugogo kuelekea jijini Bujumbura nchini Burundi ilikuwa imetawaliwa na pilikapilika nyingi za kibinadamu. Pilika za wachuuzi wa biashara ndogondogo, wauza magazeti, wauza matunda kwenye masinia, migahawa midogo kwa ajili ya kuuza vyakula kwa wasafiri na maduka ya bidhaa mbalimbali kuzunguka eneo la stendi ile.
Wafanyakazi wa ofisi zile za mabasi walinipokea kwa bashasha zote hata hivyo hali niliyoikuta katika ofisi zile ilinitia wasiwasi siyo kidogo. Kulikuwa na abiria wengi katika ofisi za mabasi ya stendi ile na mizigo ya abiria ilikuwa imetelekezwa katika namna ya kuashiria kuwa huduma za usafiri zilikuwa zimesitishwa kwa muda ingawaje wafanyakazi wa ofisi zile bado walikuwa wakiendelea kukatisha tiketi kwa abiria waliokuwa wakiendelea kufika eneo lile.
Hatimaye nikaamua kuwauliza abiria niliyowakuta eneo lile na baada ya kudadisi nikagundua kuwa safari za mabasi yote ya kuelekea jijini Bujumbura nchini Burundi zilikuwa zikisuasua kutokana na hali ya machafuko ya kisiasa iliyokuwa ikiendelea nchini humo. Kwa kweli hali ile ilinikatisha tamaa kwani taratibu nilianza kuona dalili za kutofika jijini Bujumbura kwa siku ile. Niliendelea kujishauri na hatimaye nikaamua kuachana na wazo la kukata tiketi baada ya kuhisi kuwa huwenda kungetokea usumbufu mkubwa wakati wa kudai nauli zetu pale ambapo ingetokea kuwa safari za kwenda jijini Bujumbura zingesitishwa rasmi.
Nikiwa bado nipo lile eneo la stendi ya mabasi ya Nyabugogo nikasimama na kuanza kuyatembeza macho yangu eneo lile katika namna ya kuzichunguza sura za abiria waliokuwa eneo lile wakisubiri usafiri wa kuelekea jijini Bujumbura nchini Burundi. Kwa kufanya vile nikagundua kuwa akina mama na watoto walikuwa wachache sana eneo lile ukilinganisha na vijana na wazee.
Nikiwa bado ninaendelea na uchunguzi wangu dhidi ya watu waliokuwa eneo lile mara nikajikuta nikivutiwa na msichana mmoja aliyekuwa amesimama peke yake mbali kidogo na eneo lile. Alikuwa msichana mrefu na mweusi mwenye haiba nzuri ya kuvutia. Nywele zake nyeusi ndefu na laini alikuwa amezifunika kwa kofia kama yangu. Sura yake ndefu kiasi yenye macho makubwa ya kike na legevu. Pua yake ndefu na mdomo laini wenye kingo pana kiasi zilizopakwa lipstick ya rangi nzuri ya chocolate pamoja na vishimo vodogo mashavuni mwake vilinifanya nibabaike kidogo kwa uzuri wake wakati nilipomtazama. Msichana yule alikuwa amevaa fulana nyepesi nyeupe iliyoyaficha vyema matiti yake imara yenye ukubwa wa wastani na juu yake alikuwa amevaa shati zito jeusi la kitambaa cha jeans.
Nikiwa na hakika kuwa msichana yule alikuwa hafahamu chochote kuwa nilikuwa nikimtazama kwa kificho nikaendelea na udadisi wangu. Kiuno chake chembamba kiasi chenye misuli imara kiliizuia suruali yake ya rangi nyeusi ya jeans iliyolichora vyema umbo lake matata lenye kuitaabisha vibaya nafsi ya mwanaume yoyote asiyekuwa na msimamo. Miguuni alikuwa amevaa buti ngumu za ngozi na kwa kweli msichana yule alikuwa akipendeza sana. Hisia za upweke zikiwa zimeanza kunitawala nikaanza kuvuta picha juu ya namna gani nitakavyokuwa baada ya kufanikiwa kutengeneza urafiki na msichana yule mlimbwende. Mgongoni alikuwa amebeba begi.
Hatimaye miguu yangu ikawa myepesi ghafla na hivyo kujikuta nikipiga hatua zangu za kivivuvivu kumsogelea huku uso wangu ukianza kutengeneza tabasamu la kirafiki. Msichana yule akawahi kugeuka na kunitazama wakati nilipokuwa nikimkaribia na hapo nikamsalimia.
“Bonjour Mademoiselle” Habari za asubuhi Dada. Msichana yule akageuka kunitazama kwa mshangao kidogo kabla ya kulegeza uso wake na kutabasamu
“Bonjour Monsieur” Hatimaye akaitikia salamu yangu huku akinitazama kwa utulivu na kweli ukaribu ule ukanipelekea niutathmini vizuri uzuri wa msichana yule. Mfinyanzi alikuwa ametulia kwa makini wakati wa kumuumba kisura yule!
“Tu vas aussi au Burundi?” Unaelekea Burundi, nikamuuliza yule mlimbwende
“Oui!” Ndiyo! yule msichana akaitikia huku akitikisa kichwa chake taratibu na kunitazama usoni katika namna ya kukubali kisha akaniuliza.
“Et toi aussi tu te dirige vers le Burundi?” Na wewe pia unaelekea Burundi?
“Oui, Mais, cʼest ma première fois dʼaller au Burundi” Ndiyo, lakini ni mara yangu ya kwanza kwenda Burundi. Yule msichana akanitazama kidogo kwa utulivu huku uso wake ukishindwa kuonesha tashwishwi yoyote na hatimaye akaniuliza tena.
“Cʼest ne pas un bon mement dʼaller visiter Bujumbura, que-ce-que tu vas faire au Burundi” Huu siyo wakati mzuri wa kwenda kutembea Bujumbura. Unaenda kufanya nini Burundi?. Swali la yule msichana likaipelekea haraka akili yangu kuchangamka huku nikitunga uongo mzuri kichwani na hatimaye nikapata wazo.
“Je vais chercher mon grand frère, il est là depui longtemps, il est partis chercher la vie, et pour le moment je nʼai pas des communication avec lui” Naenda kumtafuta kaka yangu, kwa muda mrefu amekimbilia huko kutafuta maisha na sasa sina mawasiliano naye. Nikaongea kwa kujiamini huku uso wangu ukiendelea kutengeneza tabasamu la kirafiki na kwa hakika tabasamu langu lilifanikiwa kuziteka hisia za mlimbwende yule kwani nilimuona akipumbazika na uzuri wangu.
“Bujumbura cʼune grande ville, comment-est-que tu vas chercher quelquʼun sans avoir ses informations?” Bujumbura ni mji mkubwa, utawezaje kumtafuta mtu bila ya kuwa na taarifa zake? yule msichana akaniuliza huku akinitazama na hapo nikatabasamu kidogo na kuangua kicheko hafifu kisichokuwa na maana yeyote kisha nikamwambia.
“Je sais que cʼest une chause difficile, mais je nʼai pas le moyen. Ça fait cinq ans que je nʼai rien compris de lui. La darnière fois quʼon a communiqué, il a dit quʼil hapité à lʼavenue de la jeunesse au bord de la route de la chaussé du peuple Murundi” Nafahamu kuwa ni jambo gumu lakini sina namna. Miaka mitano imepita bila ya kusikia chochote kutoka kwake. Mara ya mwisho tulipowasiliana alisema kuwa anaishi mtaa wa Avenue de la Jeunesse kando ya barabara ya Chaussee du peuple Murundi.
“Oh! je connais cet avenue, cʼest ne pas loin du centre ville. Quand on va arrive à Bujumbura je vais te diriger” Oh! naufahamu vizuri huo mtaa, haupo mbali sana kutoka katikati ya mji. Tukifika Bujumbura nitakuelekeza. Nikayafurahia sana maelezo ya msichana yule huku nikihisi kuwa nilikuwa nimepata rafiki mzuri mwenyeji wa jiji la Bujumbura.
“Ja vais te remercier beaucoup” Nashukuru sana. Nikamwambia yule mlimbwende
“Moi jʼarrive à lʼavenue Bulevard du ler Novembre dans la ville de Bujumbura” Mimi nitafikia mtaa wa Boulevard de ler Novembre jijini Bujumbura. Yule msichana akaniambia.
Nikamtazama msichana yule kwa utulivu huku nikitabasamu katika namna ya kuzidi kutengeneza urafiki naye. Mitaa mingi ya jiji la Bujumbura nilikuwa nikiifahamu kupitia ramani ndogo ya nchi ya Burundi niliyopewa na Brigedia jenerali Ibrahim Gambari kabla ya kuanza safari yangu jijini Dar es Salaam. Kitambo kifupi cha ukimya kikapita huku kila mmoja akiupisha utulivu kichwani mwake na nikiwa katika hali ile swali fulani likanijia kichwani.
“Tu es de Bujumbura?” Wewe ni mwenyeji wa Bujumbura?. Nikamuuliza.
“Qui, mais cʼest ne pas du tuot” Ndiyo, japo siyo sana. Yule mrembo akaniambia huku akinitazama katika namna ya kuonesha kufurahishwa na maongezi yangu.
“Cʼest le voyage de combien dʼheures dʼici?” Ni safari ya masaa mangapi kutoka hapa?. Nikamuuliza yule mrembo na baada ya kufikiri kidogo akanijibu.
“Dans sept heures ou huit heures si lʼatmosphere et calme” Masaa saba hadi nane kama hali ya hewa ni tulivu.
“Comment est la securité?” Vipi kuhusu hali ya usalama?. Swali langu likampelekea yule mlimbwende atabasamu kidogo huku akinitazama na hapo nikapata nafasi nzuri ya kuyaona meno yake meupe yaliyopangika vizuri na vishimo vyake mashavuni. Alikuwa msichana mrembo sana ambaye katika kumbukumbu zangu sidhani kama niliwahi kuonana na msichana kisura wa namna ile. Tabasamu lake lilipokoma akavunja ukimya.
“Le gouvernement seforce a securisé cette route, mais il y a des mauvais actes pendant la nuit” Serikali inajitahidi kudumisha usalama katika barabara hii ingawa kumekuwa na vitendo vya kiharamia nyakati za usiku.
“Tu as déjà voyage pendant la nuit?” Umewahi kusafiri nyakati za usiku? Nikamuuliza yule dada na swali langu likampelekea anikate jicho la kiaina na namna ya utazamaji wake ukanitia mashaka kidogo.
“Cʼest comme ça que les qents disent” Watu ndiyo wanavyosema. Jibu lile likanipelekea nigeuke vizuri na kumtazama usoni msichana yule na kwa kufanya vile nikawa nimegundua kuwa maelezo ya mrembo yule yalikuwa hayaendani kabisa na mwonekano wa sura yake. Hali ile ikapelekea maswali chungu mzima yaanze kuibuka kichwani mwangu. Sikujua kwanini nilishikwa na hali ile ya wasiwasi lakini moyo wangu ulikosa utulivu kidogo ingawa nilimezea na kuendelea kutabasamu kabla ya kuzidi kumchombeza zaidi kisura yule.
“Tu ne mʼa pas encore dis votre nom la belle?” Hujaniambia unaitwa nani mrembo?. Nikamuuliza huku nikitabasamu.
“Moi?” Mimi?. Yule mrembo akaniuliza kwa kujibalaguza huku akifahamu fika kuwa swali langu lilikuwa likimlenga yeye. Angalau nikaliona tena tabasamu lake maridhawa likichomoza usoni mwake na kuusuuza vizuri mtima wangu...ITAENDELEA
 
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 7
Mtinzi:Kelvin Mponda

“Oui!, je vois que cʼest ne pas mauvais quʼon seconnaissent, si ça ne te derange pas” Ndiyo! nimeona siyo vibaya tukafahamiana, kama hutojali. Nikaongea kwa utulivu huku nikimtazama yule kisura.
“Je mʼappelle Amanda Egide, et vous?” Naitwa Amanda Egide, wewe je?
“Je mʼappelle Jean Baptiste Gatete” Naitwa Jean Baptiste Gatete. Nikamwambia yule mlimbwende kwa kujiamini kana kwamba lile lilikuwa jina langu halisi.
“Toi cʼest un Rwandais?” Wewe ni mnyarwanda?. Amanda akaniuliza na swali lake likaibua hisia mpya kichwani mwangu huku nikishindwa kuelewa nini maana ya swali lile.
“Oui, mais pour le moment je vis à Lubumbashi en D R Congo” Ndiyo, ila kwa sasa naishi Lubumbashi, jamhuri ya kidemokrasia ya nchi ya Kongo. Jibu langu likampelekea Amanda ageuke vizuri na kunikata jicho tena na nilipomtazama usoni sikuona tashwishwi yoyote usoni mwake na badala yake alikaa kimya akiupisha utulivu kama afikiriaye jambo fulani. Hali ile ikaniacha njia panda na kwa kuwa sikupenda hali ile ya ukimya iendelee kutawala hivyo nikavunja ukimya na kumuuliza tena Amanda.
“Tu penses quʼon va trouver le transport aujourdʼhui?” Unadhani leo tutapata usafiri?
“Je nʼai pas la précision, mais ça dependra de lʼétat de la sécurité au Burundi” Sina hakika ingawa itategemea na hali ya usalama itakavyokuwa nchini Burundi. Amanda akaniambia huku akiitazama saa yake ya mkononi.
Tuliendelea kuongea hili na lile huku nikimuuliza maswali Amanda juu ya mambo mbalimbali ambayo kwa namna moja au nyingine nilikuwa na hakika kuwa yangeweza kunisaidia katika harakati zangu mbele ya safari. Kwa kweli nilikuwa nimefurahi sana kumpata rafiki na mwenyeji wa jiji la Bujumbura na vitongoji vyake. Kwani kwa namna nyingine nilikuwa nimeanza kupata matumaini kuwa safari yangu isingekuwa na vikwazo sana katika kuzifikia sehemu muhimu nilizokuwa nikizihitaji mara baada ya kufika jijini Bujumbura. Wakati tukiendelea na maongezi nikagundua kuwa idadi ya wasafiri wa kuelekea jijini Bujumbura ilikuwa ikiendelea kuongezeka taratibu kwenye zile ofisi za yale mabasi huku dalili za kuanza safari zikizidi kufifia.
Ilipotimia saa tano asubuhi matumaini ya kupata usafiri wa kuelekea jijini Bujumbura nchini Burundi yakawa yametoweka kabisa baada ya wafanyakazi wa ofisi zile za mabasi kutoa tamko kwa abiria waliokuwa pale kuwa serikali ya nchi Rwanda ilikuwa imetoa tamko la tahadhari ya usalama kupitia waziri wake wa ulinzi. Kuwa safari zote za kuelekea jijini Bujumbura nchini Burundi zilikuwa zimetolewa tamko la kusitishwa kutokana na hali ya machafuko ya kisiasa ilivyokuwa ikiendelea kuota mizizi katika nchi hiyo. Taarifa zile zikaibua zogo la aina yake baada ya abiria waliokata tiketi eneo lile kuanza kudai nauli zao.
Kwa kweli nilikata tamaa sana hasa kwa kuchukulia kuwa nilikuwa tayari nimepoteza muda wangu mwingi eneo lile na hasa nilipoanza kuwaza kuwa kutokana na hali ile nisingeweza tena kupata nafasi ya kusafiri na mlimbwende yule Amanda. Njaa nayo ilikuwa imeanza kuniuma hivyo nilichowaza ilikuwa kwanza ni kutafuta mgahawa wowote wa jirani na eneo lile ambapo ningepata mlo wa nguvu huku nikipanga hatua inayofuata. Nilipomtazama Amanda naye nikamuona kuwa ni kama aliyekuwa amekatishwa tamaa sana na tamko lile la kusitishwa kwa usafiri wa kuelekea nchini Burundi. Hata hivyo sikuweza kufahamu kuwa alikuwa akiwaza nini kichwani mwake.
“Est-ce quʼil y a un bon restaurant dans ce milien, là où on peut prendre le petit dejeuner?” Kuna mgahawa wowote mzuri eneo hili ambapo tunaweza kupata kifungua kinywa?. Nikamuuliza Amanda.
“Le restaurant du coin des amis, il est derière le bâtiment de Kigali Nightmare, cʼest ne pas loin dʼici” Mgahawa wa kona ya marafiki upo nyuma ya jengo la Kigali Nightmare, siyo mbali sana kutoka hapa. Amanda akaniambia kwa bashasha zote huku akionekana kufurahishwa na wazo langu.
Muda mfupi baadaye tulikuwa ndani ya mgahawa wa kisasa wa Le Restaurant du coin des amis uliyokuwa nyuma ya jengo refu la biashara la Kigali Nightmare, barabara ya mtaa wa KN 8. Ulikuwa ni mgahawa mzuri wa kisasa wenye huduma zote muhimu kama aina ya vyakula mbalimbali vya watu wa mataifa tofauti na utulivu wa kutosha. Tulipoingia mle ndani nikagundua kuwa kulikuwa na raia wengi wa kutoka nje ya nchi ya Rwanda husani wazungu ambao wengi walikuwa ni wafaransa ambao niliwatambua haraka baada ya kuwasikia vizuri wakizungumza lugha ya kifaransa.
Hatimaye tukatafuta meza moja iliyojitenga kwenye kona moja ya mgahawa ule na kuketi. Sehemu ile tuliyoketi ilituwezesha sote kuona nje ya mgahawa ule kupitia kuta safi za vioo zilizokuwa zikitazamana na barabara pana ya lami. Mhudumu mmoja wa mgahawa ule alipokuja kutusikiliza nikamuagiza Hot chocolat chaud na supu nzito ya ng’ombe yenye saladi na chapati tatu za unga wa ngano wa ata. Amanda yeye akaagiza wali wa kuku na saladi ya mboga za majani.
Vyakula vile vilipoletwa na mhudumu tukaanza kuvishambulia huku kila mmoja akionekana kuwa na njaa na wakati tukianza kupata mlo ule ndiyo nikapata wasaa mzuri wa kumchunguza Amanda kwa jicho la wiziwizi. Hisia zangu zikanipelekea nijisikie furaha kwa kuketi pamoja na msichana yule mrembo hasa pale nilipogundua kuwa watu wengi waliokuwa mle ndani ya ule mgahawa walikuwa wakitutazama kwa jicho la wivu. Hakika tulipendeza sana na kuonekana kama wapenzi tulioshibana na kuendana vizuri sana.
Wakati nikiendelea kupata mlo nikagundua kuwa hata Amanda naye alikuwa akinitazama kwa jicho la wizi. Hata hivyo sikutaka kumnyima nafasi ile hivyo mara kwa mara nikawa nikizuga kutazama nje ya mgahawa ule kupitia kuta safi za vioo vya ule mgahawa. Pamoja na yote macho ya Amanda hayakuhama kwangu badala yake yalikuwa makini kufuatilia kwa karibu kila tukio nililokuwa nikilifanya.
Mara kwa mara nilipoacha kutazama nje ya mgahawa ule niliyatembeza macho yangu kuzitazama sura za watu waliokuwa mle ndani na kwa kufanya vile nikagundua kuwa mle ndani kulikuwa na huduma ya Wi-Fi (Wireless Fidelity). Huduma ya mtandao wa intaneti kwa mtu yeyote mwenye kifaa kinachoweza kunasa taarifa za kimtandao wa intaneti kama simu za kisasa za mkononi au kompyuta.
Hali ile ikanipelekea nipate wazo la kuwasiliana na mratibu wangu wa safari za kijasusi na vilevile mkuu wa idara ya taifa ya ujasusi Brigedia jenerali Ibrahim Gambari jijini Dar es Salaam Tanzania. Lengo langu likiwa ni kutaka kumueleza kuwa tayari nilikuwa nimefika nchini Rwanda na sasa nilikuwa katika harakati za kuelekea jijini Bujumbura nchini Burundi. Hivyo nikaichukua simu yangu ya mkononi na kuiunganisha na huduma ile ya mtandao wa intaneti ndani ya ule mgahawa. Tukio ambalo pia lingempelekea Brigedia jenerali Ibrahim Gambari kupitia GPRS aweze moja kwa moja kuitambua sehemu ile niliyokuwa.
Mtandao wa intaneti uliponasa vizuri kwenye simu yangu ya mkononi nikaandika taarifa fupi ya ujumbe wa elektroniki nikimueleza Brigedia jenerali Ibrahim Gambari hatua niyofikia kwenye harakati zangu. Wakati nikifanya vile Amanda akawa akinitazama kwa kuibaiba hata hivyo sikumtilia maanani. Ule ujumbe wa taarifa fupi ulipoenda nikaizima simu yangu na kuitia mfukoni huku nikiliachia tabasamu langu maridhawa likielea usoni. Mara tu ule ujumbe ulipoenda na kisha kuizima simu yangu kabla ya kuitia mfukoni nikashangaa kumuona Amanda naye akiitoa simu yake ya mkononi haraka kutoka mfukoni na kuitazama kisha akayahamishia macho yake kunitazama kidogo kabla ya kuyahamisha pembeni. Nikamuuliza kama kulikuwa na shida yoyote.
“Est-ce quʼl y a un problème?” Kuna shida yoyote?
“Non, je regardè le temps” Hapana, nilikuwa natazama muda. Amanda akaniambia huku akiendelea kupata mlo na wakati tukiendelea kula akili yangu ikawa ikiendelea kusumbuka katika namna ya kuwaza kuwa ni kwa namna gani ningepata usafiri wa kuelekea jijini Bujumbura nchini Burundi kwa siku ileile.
“La nouriture dʼici goûte bien” Chakula cha hapa kina ladha nzuri. Huku akitabasamu Amanda akaniambia.
“Cʼest juste, laisse moi parler que je nʼai jamais mangé la nouriture qui goûte bien ici au Rwanda, comme à ce restaurant” Ni kweli, niseme kuwa sijawahi kula mlo wenye ladha nzuri hapa nchini Rwanda kama kwenye mgahawa huu. Nikamwambia Amanda huku nikitabasamu.
Maongezi baina yetu yakaendelea ndani ya ule mgahawa huku tukiendelea kupata mlo taratibu na sote tulionekana kufurahishwa na urafiki ule ulioanzia njiani. Amanda alinieleza mambo mbalimbali kuhusu nchi ya Burundi ambayo hapo mwanzo nilikuwa siyafahamu na mimi sikuacha maongezi yale yaelemee upande mmoja hivyo nikawa nikitia vionjo vya hapa na pale vilivyompelekea Amanda ajikute akicheka mara kwa mara.
Tulipomaliza kupata mlo tukaagiza juisi ya parachichi tukishushia taratibu kusindikiza maongezi yetu huku kichwani nikiendelea kufikiria juu ya safari yangu ya jijini Bujumbura nchini Burundi.
Ilipofika saa nane mchana nikaanza kuhisi kuwa tulikuwa tumetumia muda mwingi kukaa ndani ya mgahawa ule kwani hata wale watu waliotukuta mle ndani nao walikuwa wamehudumiwa na hatimaye kuondoka. Hivyo nikamuita mhudumu mmoja wa ule mgahawa na kulipa bili ya ule mlo wote tuliokula mimi na Amanda. Niliporudishiwa chenchi nikamuomba Amanda kuwa tuondoke eneo lile na bila upinzani wowote Amanda akakubaliana na ombi langu hivyo tukachukua mabegi yetu na kutoka nje ya ule mgahawa tukirudi tena kule kwenye ile stendi ya mabasi ya Nyabugogo.
Tulipokuwa tukitembea njiani nikanunua gazeti moja la nchini Rwanda liitwalo La Nouvelle Relève lililokuwa likiandikwa kwa lugha ya kifaransa baada ya kuona taarifa fulani kwenye gazeti lile iliyokuwa ikielezea kwa kina juu ya hali ya machafuko ya kisiasa iliyokuwa ikiendelea nchini Burundi.
Mara tu tulipofika kwenye ile stendi ya mabasi ya Nyabugogo haraka nikagundua kuwa wale abiria wengi waliokuwa eneo lile wakisubiri usafiri wa kuelekea jijini Bujumbura nchini Burundi hawakuwepo. Nilipoendelea kuchunguza nikagundua kuwa zile ofisi za yale mabasi kwenye ile stendi bado zilikuwa wazi hali iliyonipelekea niingiwe na wasiwasi kuwa huwenda usafiri wa dharura ulikuwa umepatikana wakati mimi na Amanda tulipokuwa tukipata mlo kwenye ule mgahawa.
Amanda akawahi kuuliza kwa wale wafanyakazi wa ofisi za yale mabasi kama kulikuwa na usafiri wowote ulioondoka kuelekea jijini Bujumbura kwa kipindi kile ambacho hatukuwepo pale stendi. Wale wafanyakazi wakatuambia kuwa hapakuwa na basi lolote lililosafirisha abiria kuelekea nchini Burundi huku wakitufafanulia kwa kina juu ya tamko lililotolewa na waziri wa ulinzi wa serikali ya Rwanda juu ya kusitishwa kwa safari zote za kuelekea nchini Burundi kufuatia hali ya machafuko ya kisiasa iliyokuwa ikiendelea nchini humo tangu jaribio la mapinduzi ya kijeshi lilipofanyika.
Maelezo ya wale wafanyakazi wa ofisi za yale mabasi yakanipelekea niondoe kabisa matumaini ya kupata usafiri wa kuelekea jijini Bujumbura nchini Burundi kwa mabasi yale badala yake akili yangu ikaanza kuchangamka nikianza kufikiria njia mbadala. Nikiwa katika hali ile mara nikamuona Amanda akiniacha pale niliposimama na kwenda kuzungumza na kijana mmoja aliyekuwa amesimama kando ya eneo lile kama mtu aliyekuwa akitusikilizia. Nilimuona Amanda akizungumza na kijana yule na baada muda mfupi wa maongezi yale Amanda akageuka na kunionesha ishara ya kuniita kwa mkono akinitaka nimfuate pale aliposimama na yule kijana. Nikafanya vile na nilipowafikia pale waliposimama kupitia maongezi yao nikaelewa kuwa kulikuwa kumepatikana usafiri wa mtu binafsi wa kuelekea jijini Bujumbura nchini Burundi. Hivyo yule kijana alikuwa ni mhusika mmojawapo wa gari hilo ambalo kwa mujibu wa maelezo yake ni kuwa gari hilo lilikuwa limeegeshwa nyuma ya kituo kimoja cha kujazia mafuta kilichokuwa jirani ne eneo lile. Akihofia kukamatwa na askari endapo angeliegesha gari lile pale stendi na kutafuta abiria. Kwani tayari serikali ya Rwanda ilikuwa imetoa tamko la usitishwaji wa safari za kuelekea nchini Burundi.
Nikamuuliza yule kijana kuwa nauli ingekuwa faranga ngapi za pesa ya kinyarwanda na hapo akatueleza kuwa alikuwa akitoza dola za kimarekani 50 kwa kila abiria mmoja. Nikageuka kumtazama Amanda nikitaka kufahamu kama alikuwa akilichukuliaje suala lile. Amanda akanifanyia ishara kuwa nisiwe na wasiwasi wote kwani usafiri wa magendo wa namna ile ulikuwa ni jambo la kawaida kufanyika katika stendi ile hususani pale inapotokea shida ya usafiri. Maelezo ya Amanda yakanipelekea nisione sababu ya kuwa na wasiwasi hivyo nikakubaliana na wazo lile na hapo kwa pamoja tukaanza safari ya kuelekea kwenye hilo gari huku yule kijana akituongoza mbele yetu.
Wakati tukitembea mara kwa mara Amanda alikuwa akigeuka na kunitazama katika namna ambayo kwa kweli sikuweza kuielewa. Hata hivyo niliipa akili yangu utulivu huku nikiendelea kutafakari juu ya kazi iliyokuwa ikinikabili mbele yangu.
Baada ya mwendo mfupi wa safari yetu hatimaye tukawa tumekifikia kituo kimoja cha kujazia mafuta kiitwacho Hass Petroleum kilichokuwa nyuma ya ile stendi kuu ya mabasi ya Nyabugogo. Kituo hicho kikipakana na duka kubwa la vipuli vya magari.
Tulipolikaribia vizuri eneo lile mara nikaliona gari moja aina ya Land Rover 110 lenye muundo wa kizamani la rangi ya kijivu likiwa limeegeshwa kando ya kituo kile cha kujazia mafuta. Tulipolifikia lile gari nikagundua kuwa mle ndani kulikuwa tayari kuna watu watatu. Mbele kulikuwa na dereva wa lile gari. Mwanaume mwenye umri wa kukadirika wa kati ya miaka thelathini na tano hadi arobaini, mrefu na mweusi mwenye macho makali akiwa amevaa kofia nyeupe ya pama na koti zito jeusi la kujikinga na baridi. Alikuwa ameketi kwenye ile siti ya dereva akiendelea kusubiri abiria. Ile sehemu ya abiria nyuma yake kulikuwa na watu wawili, vijana wa makamo yangu. Mmoja mrefu na mwembamba na mwingine mfupi na mnene.
Tulipolifikia lile gari tukawasalimia wale watu waliokuwa mle ndani ya gari kiungwana na wote wakaitikia kwa pamoja. Hata hivyo mimi sikukaa kwenye zile siti zilizokuwa mbele kama wale watu tuliyowakuta walivyokuwa wamekaa ila badala yake nikafungua mlango wa nyuma kabisa wa lile gari na kuketi kwenye siti za kutazamana.
Amanda akaonekana kutaka kupingana na uamuzi wangu wa kukaa kule nyuma lakini mara akaghairi msimamo wake pale alipoona nikimfanyia ishara kwa kichwa kuwa aingie kule nyuma ya lile gari ili tukae wote. Hivyo nayeye akafanya vilevile na alipoingia kule nyuma ya gari akaenda na kuketi mbele yangu upande wa pili na kutokana na muundo wa siti za lile gari mtindo ule wa ukaaji ukatupelekea tujikute tukitazamana huku tabasamu lake maridhawa likiendelea kuziadhibu vibaya hisia zangu...ITAENDELEA
 
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 8
Mtunzi:Kelvin Mponda

...Yule kijana aliyetuleta kwenye lile gari alipoona kuwa tayari tumeingia akageuza na kurudi kule tulipotoka na hapo nikajua kuwa alikuwa akienda kutafuta abiria wengine wa kujaza nafasi zilizosalia. Dereva wa lile gari akageuka nyuma haraka na kudai nauli na hapo nikapata nafasi ya kuiona vizuri sura yake. Macho yake makali yakatutazama kwa utulivu huku akitengeneza tabasamu jepesi usoni mwake lililoyapelekea meno yake yaliyopoteza mng’ao kwa ukungu wa moshi wa sigara wa miaka mingi kuonekana vizuri huku akiwa ameibana njiti moja ya kiberiti kwenye pembe ya mdomo wake. Hata hivyo macho ya dereva yule nikayaona yakajikita zaidi kwenye kumtazama Amanda na hapo nikajua kuwa jamaa alikuwa amebabaishwa sana na uzuri wa Amanda.
Bila kupoteza muda nikachukua wallet yangu kutoka mfukoni na nilipoifungua nikahesabu noti zenye thamani ya dola mia moja na kumpa yule dereva kama malipo ya nauli yangu na Amanda. Amanda kuona vile akajibalaguza kwa kujidai kuwa anataka kujilipia hata hivyo nikamfanyia ishara kuwa aachane na mpango wake.
Yule dereva akazipokea zile pesa na kuanza kuzihesabu na wakati akifanya vile na mimi nikapata wasaa mzuri wa kuweza kulipeleleza lile gari pamoja na wale abiria tuliowakuta mle ndani. Wale abiria wawili walionekana kuwa ni vijana waliokuwa na hamsini zao na sikuwatilia maanani. Hatimaye nikayahamishia macho yangu nikimtazama yule dereva huku nikitafakari namna alivyokuwa amemtazama Amanda na kisha kunikata jicho la kiaina kabla ya kuipokea ile pesa yangu. Lile gari Land Rover 110 lilikuwa ni la mtindo wa zamani ingawa bado lilionekana kuwa bado ni imara na lenye uwezo mzuri wa kumudu safari yetu. Ingawa sikuwa na uzoefu na safari za namna ile lakini niliamini kuwa maeneo mengi ya bara la Afrika yalikuwa yakifanana hivyo nikaupisha utulivu huku nikijaribu kuvuta picha ya kule tulipokuwa tukielekea.
Wakati nikiendelea na tathmini yangu mara yule kijana aliyetuleta pale awali nikamuona akija huku akiwa ameongozana na abiria wengine wanne. Walipofika kwenye lile gari, abiria wawili wakaingia kule mbele na wale abiria wawili waliosalia wakaingia kule nyuma tulipokuwa mimi na Amanda. Walikuwa ni vijana watatu na mzee mmoja na hivyo kupelekea Amanda awe ndiye msichana pekee mle ndani. Wale vijana walipoingia mle ndani tukawapisha wakae mbele yetu huku mimi na Amanda tukiendelea kukaa sehemu ya nyuma kabisa ya lile gari. Tulisalimiana vizuri na wale vijana na baada ya pale kila mmoja akaendelea na hamsini zake hata hivyo kule nyuma ya gari tukawa tayari tumeenea na hivyo kupelekea abiria mmoja tu kusalia kabla ya kuanza safari yetu.
Kwa muda mrefu tukaendelea kukaa ndani ya lile gari eneo lile huku ukimya ukiendelea kutawala mle ndani. Mara kwa mara nikamuona Amanda akinitazama na kila macho yetu yalipokutana kila mmoja alitabasamu pasipo kuongea neno lolote ingawa nilipomchunguza vizuri Amanda nikagundua kuwa macho yake yalikuwa na uchovu mwingi. Yeyote ambaye angetutazama angeweza kudhani kuwa mimi na Amanda tulikuwa ni wapenzi tulioshibana au pengine tulikuwa ni mke na mume lakini ukweli ni kwamba siri tulikuwa tukiifahamu sisi wenyewe. Tukiwa katika hali ile hatimaye Amanda akapitiwa na usingizi na kukiegemeza kichwa chake juu ya begi lake la mgongoni alilokuwa amelipakata mapajani mwake. Nikamuhurumia sana Amanda kwa hali ile lakini sikuwa na namna ya kumsaidia.
Hali ya ukimya ilipoonekana kuzidi kutawala mle ndani nikaanzisha mada za hapa na pale kwa wale abiria wenzangu katika namna ya kuchangamsha watu lakini hata hivyo mwitikio ulikuwa hafifu sana na hapo nikagundua kuwa ile ilikuwa ni nchi nyingine yenye tamaduni tofauti kabisa na nchi yangu ya Tanzania ambapo utu, undugu na urafiki lilikuwa ni suala la kawaida kabisa. Kiasi kwamba katika mazingira kama yale maongezi ya kirafiki lingekuwa ni jambo la kushabikiwa na kufurahiwa sana.
Kupitia vioo vya madirisha ya lile gari niliweza kuliona wingu zito la mvua lililokuwa likijitengeneza taratibu angani na hivyo kuashiria kuwa mvua kubwa ilikuwa mbioni kunyesha.
Ilipotimia saa kumi na moja jioni safari ikaanza baada ya abiria mmoja aliyekuwa akisubiriwa kupatikana. Yule kijana aliyekuwa akitafuta abiria akaingia mbele kwenye lile gari na kukaa kwenye siti ya abiria upande wa kushoto wa dereva na yule abiria mwingine aliyepatikana akaingia na kukaa kwenye ile siti ya abiria iliyokuwa ikifuatia baada ya ile siti ya nyuma kabisa tuliyoketi na hapo safari ikaanza.
Tulipokuwa tukiondoka eneo lile Amanda akashtuka kutoka usingizini kisha akanitazama kidogo kabla ya kuyahamisha macho yake kuwatazama kwa makini wale abiria wote waliokuwa mle ndani. Alipoyarudisha tena macho yake kwangu akatabasamu kidogo kama kawaida yake huku myumbo wa gari lile barabarani ukimpotezea umakini. Tukabaki tukitazamana tu ingawa kila mmoja alikuwa amezama kwenye fikra zake.
Dereva wa lile gari Land Rover 110 alionekana kuwa mzoefu sana na mwenye kuvijua vizuri vichochoro vingi vya jiji la Kigali. Hivyo akawa akiendesha kwa mbwembwe huku akiwa makini kuchagua barabara za kupita kwa kuhofia kusimamishwa na askari wa usalama barabarani.
Muda mfupi baadaye taratibu tukaanza kuliacha jiji la Kigali nyuma yetu katika mwendo wa masafa marefu huku sauti pekee iliyokuwa ikisikika mle ndani ya gari ikiwa ni ile sauti ya muungurumo wa injini ya lile gari na mnuko wa harufu nyepesi ya mafuta ya petroli. Muda mfupi baadaye tukawa tumeifikia barabara kuu ya kuelekea nchini Burundi.
Mara tu tulipoingia kwenye ile barabara nikageuka kutazama nyuma kupitia kwenye kioo cha mlango wa nyuma wa lile gari na hapo nikagundua kuwa mwendo wetu ulikuwa wa kasi mno. Hali iliyopelekea ile taswira ya yale majengo marefu ya ghorofa ya katikati ya jiji la Kigali na nyumba za makazi ya watu kutoweka taratibu katika upeo wa macho yangu kadiri lile gari Land Rover 110 lilivyokuwa likichanja mbuga kwenye barabara ile. Muda mfupi baadaye hatimaye tukawa tumetokomea kabisa mbali na jiji la Kigali na kuanza kuingia kwenye barabara iliyokuwa ikikatisha katikati ya vichaka na miti mirefu ya msituni tukishuka mabonde na kupanda milima mwendo wa kasi.
Safari ikiwa inaendelea nikaanza kuzichunguza tena nyendo za watu waliokuwa mle ndani kisha nikayapeleka macho yangu kwa yule dereva wa lile gari. Niliporidhika na mwenendo mzima wa ile safari nikaingiza mkono kwenye begi langu nikilichukua lile gazeti la La Nouvelle Relève nililolinunua wakati tulipokuwa tukitoka kwenye ule mgahawa wa Le Restaurant du coin des amis wakati ule na Amanda. Kisha nikalifunua hadi nilipoufikia ukurasa wa tatu sehemu kulipokuwa ni zile taarifa za machafuko ya kisiasa yaliyokuwa yakiendelea nchini Burundi. Kulikuwa na maelezo mengi katika habari ile lakini nilijaribu kwa kila hali kuisoma kwa haraka taarifa ile huku nikiruka maelezo mengine yasiyokuwa na umuhimu kwangu na hivyo kusoma dondoo muhimu tu.
Maelezo aliyonipa Brigedia jenerali Ibrahim Gambari kabla ya kuanza safari yangu ya kijasusi jijini Dar es Salaam nikagundua kuwa hayakuwa yametofautiana sana na kile kilichokuwa kimeandikwa katika taarifa ile. Hata hivyo kulikuwa na ziada nyingine niliyokuwa nimeipata katika ile taarifa. Kwanza niligundua kuwa kiongozi wa jaribio la mapinduzi yale ya kijeshi ya kuiondoa madarakani serikali ya Burundi ya rais Pierre Nkurunziza mwenye cheo cha Meja Jenerali akifahamika kwa jina la Godefroid Niyombare. Taarifa zile zikaendelea kueleza kuwa Meja jenerali Godefroid Niyombare hapo kabla aliwahi kushikilia madaraka ya cheo cha Military chief of staff na vilevile aliwahi kuwa balozi wa Burundi nchini Kenya na pia aliwahi kuwa mkuu wa idara ya ujasusi ya nchi ya Burundi.
Taarifa zikaendelea kueleza kuwa wakati wa vita ya kikabila nchini Burundi, Meja jenerali Godefroid Niyombare alikuwa kamanda wa kijeshi wa kihutu katika kikundi cha kijeshi cha waasi cha wakati huo kikifahamika kwa jina la CNDD-FDD-Conseil National pour la Défense de la Démocratie-Force pour la Défense de la Démocratie na vilevile aliwahi kushiriki katika mazungumzo ya amani na kikundi kingine cha waasi cha FNL-Forces Nationales de Libération. Baada ya vita hiyo ya kikabila Meja jenerali Godefroid Niyombare alipewa cheo cha mkuu wa majeshi ya Burundi chini ya utawala wa rais Pierre Nkurunziza.
Ilipofika Februari 2015 Meja jenerali Godefroid Niyombare akaenguliwa kwenye cheo cha mkuu wa idara ya ujasusi nchini Burundi na rais Pierre Nkurunziza baada ya walaka wake wenye kurasa 10 kuvuja. Walaka ambao aliuandika katika kumkosoa rais Pierre Nkurunziza juu ya kuandaa mazingira ya kutawala nchi zaidi kwa muhula wa tatu. Kitu ambacho kilikuwa ni kinyume kabisa na katiba ya nchi hiyo.
Tarehe 13, mwezi Mei, mwaka 2015 kupitia kituo binafsi cha redio nchini Burundi, Meja jenerali Godefroid Niyombare akatangaza rasmi kuingʼoa madarakani serikali ya rais Pierre Nkurunziza kupitia tukio la mapinduzi ya kijeshi wakati rais Pierre Nkurunziza alipokuwa jijini Dar es Salaam nchini Tanzania kuhudhuria mkutano wa 13 wa wakuu wa nchi za Afrika Mashariki. Chini ya habari ile pia kulikuwa na taarifa nyingine iliyoeleza kuwa Meja jenerali Godefroid Niyombare pia aliwahi kushiriki katika mpango wa amani barani Afrika nchini Somalia-African Union Mission to Somalia.
Nikasoma maelezo mengine kuwa Meja jenerali Godefroid Niyombare pia aliwahi kuwa kwenye kamati ya mipango ya kikundi kilichokuwa kikifahamika kwa jina la IMBONERAKURE ingawa sikuweza kufahamu IMBONERAKURE maana yake nini kwa vile pale hapakuwa na maelezo ya kujitosheleza. Hatimaye nikamalizia kusoma taarifa ile kwenye lile gazeti kisha nikalikunja na kulichomeka kwenye mfuko wa pembeni wa begi langu. Nilipomtazama Amanda nikagundua kuwa alikuwa tayari amepitiwa tena na usingizi.
Lile gari lilikuwa likienda mwendo kasi ingawa hata hivyo yule dereva alionekana kuwa makini sana huku akionekana pia kuizoea vizuri ile barabara. Nikayatembeza tena macho yangu kuwatazama abiria wengine waliokuwa mle ndani na hapo nikagundua kuwa hata wao walikuwa wamepitiwa na usingizi. Nikaendelea kuwatazama kwa utulivu watu wale huku wakionekana kuelemewa sana na uchovu. Hata hivyo pamoja na mimi kuwa na uchovu mwingi lakini kamwe sikuuruhusu usingizi unichukue kwa kuzingatia vigezo viwili vikubwa. Kwanza nilikuwa mgeni kabisa wa barabara ile na mazingira yake. Pili binafsi niliona kuwa lilikuwa ni jambo gumu sana na la hatari kwa mtu aliyeko usingizini kuweza kujitetea kikamilifu pale inapotokea hatari ya namna yoyote.
Miale hafifu ya jua la machweo ilikuwa mbioni kutoweka katika safu za milima mirefu yenye misitu mizito ambapo barabara ile ilikuwa ikikatisha kando yake na hivyo kulifanya wingu jepesi la giza kutanda angani. Hata hivyo mwanga mkali wa taa za mbele za lile gari Land Rover 110 ulijitahidi kwa kila hali kulifukuza giza lile lililotanda mbele ya ile barabara wakati gari lile lilivyokuwa likijitahidi kukata upepo na kutokomea mbele zaidi. Kupitia kwenye vioo vya madirisha ya lile gari niliweza pia kuona manyunyu hafifu ya mvua iliyotokana na wingu zito lililokuwa limetanda angani. Hakuna aliyekuwa akiongea na hivyo mle ndani ya gari kulitawaliwa na kiasi kikubwa cha ukimya wa namna yake. Safari bado ilikuwa ikiendelea.
_____
Nilikuwa nimezama katikati ya tafakuri nzito nikiwaza namna ya kuanza harakati zangu mara baada ya kufika jijini Bujumbura nchini Burundi pale niliposhtushwa na kupungua ghafla kwa mwendo wa lile gari letu. Haraka nikainua kichwa na kuyatembeza macho yangu nikitazama huku na kule na hapo haraka nikaona kizuizi cha barabarani kilichokuwa umbali mfupi mbele yetu kabla ya kuanza kupanda mlima. Mvua kubwa ilikuwa ikinyesha na usiku tayari ulikuwa umeingia.
Wakati tukikikaribia kile kizuizi haraka nikagundua kuwa kulikuwa na askari watatu wa barabarani katika kizuizi kile. Askari mmoja alikuwa amesimama katikati ya barabara mbele ya kizuizi kile akimuonesha dereva wetu ishara ya mkono kuwa apunguze mwendo na kusimama. Askari wawili waliosalia mmoja alikuwa amesimama upande wa kushoto na mwingine alikuwa amesimama upande wa kulia wa barabara ile. Askari wale wote walikuwa wamevaa makoti marefu ya mvua huku wamezishika vyema bunduki zao mkononi.
Kitendo cha mwendo wa lile gari letu kupungua ghafla kikawapelekea wale abiria wengine washtuke kutoka usingizini haraka na kutazama kule mbele huku Amanda akiwa miongoni mwao.
Nikiwa bado nimeketi mle ndani nikayahamishia macho yangu tena kwa yule dereva wetu huku nikijaribu kumchunguza kama alikuwa na wasiwasi wowote juu ya lile tukio la kusimamishwa kwetu na wale watu walioonekana kuwa ni askari wa usalama barabarani. Sikuona tashwishwi yoyote usoni mwake badala yake nikamuona akikazana kupangua gia za lile gari Land Rover 110 huku taratibu akipunguza mwendo. Nikayahamisha tena macho yangu kumtazama Amanda pale alipoketi na hapo nikagundua kuwa hata yeye alikuwa amezama katika kuwatazama wale askari waliokuwa wakitusimamisha.
Hatimaye gari letu likasimama hatua chache mbele ya yule askari kando ya ile barabara sehemu kulipokuwa na kile kizuizi kisha yule dereva akageuka nyuma haraka na kutuambia.
“Si un policien vous interoge, disez que nous allons à Huye aux enterrement” Askari akiwauliza mwambieni kuwa tunaelekea Huye kwenye msiba. Sote tukatikisa vichwa taratibu kuonesha kukubaliana na hoja yake kisha yule dereva akafungua mlango wa gari na kushuka taratibu akipiga hatua zake za woga kumfuata yule askari wa usalama barabarani. Tukio lile likanipelekea nizidi kuwa makini zaidi kumtazama yule dereva kule alipokuwa akielekea huku mara kwa mara macho yangu yakiwatazama wale askari wengine kule waliposimama.
Kikapita kitambo kifupi cha maongezi kati ya yule dereva na yule askari wa usalama barabarani na wakati huo wote mimi nilikuwa makini kuwatazama. Mwishowe nikamuona yule dereva wetu akichukua wallet yake ndogo kutoka mfukoni na kuifungua kisha akatoa noti moja na kumpa yule askari. Yule askari akaipokea ile noti haraka na kuitia mfukoni kisha taratibu akaanza kupiga hatua zake akilisogelea gari letu. Yule askari alipolikaribia lile gari akageuka na kumuuliza yule dereva wetu kwa sauti ya ukali.
“Où est-ce que vous alez?” Mnaelekea wapi?
“Nous allons à Huye Monsieur” Tunaelekea Huye bwana mkubwa. Nikamsikia yule dereva akimwambia yule askari na hapo nikamuona yule askari akizunguka na kuja nyuma ya lile gari na wakati yule askari akija kule nyuma ya gari akawa akitukata jicho la hadhari watu wote tuliokuwa mle ndani. Yule askari alipofika kule nyuma ya gari akafungua ule mlango na hapo wote tukageuka na kumtazama kwa shauku, na yeye akatutazama kidogo mmoja baada ya mwingine kwa udadisi kabla ya kumuuliza yule dereva.
“Tu transportes les passagés?” Unabeba abiria eh?
“Non!” Hapana!
“Et les gents qui sont ici dereiere?” Na hawa watu huku nyuma ni akina nani?. Yule askari akamuuliza yule dereva kwa hasira huku akitukodolea macho...ITAENDELEA
 
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 9
Mtunzi:Kelvin Mponda

...“Non! commandant, nous sommês des frères, nous allons au deil” Hapana! afande, sisi ni ndugu tunaenda msibani. Yule dereva akajitetea huku akilazimisha tabasamu la kirafiki usoni mwake. Yule askari akamtazama yule dereva kwa makini kabla ya kumwambia.
“Donne moi votre permis de conduire” Nipe leseni yako ya udereva. Yule askari akamwambia yule dereva huku akiyahamisha macho yake kututazama tena.
“Comment vous allez?” Habari zenu?. Yule askari akatuuliza na hapo wote tukamwitikia kwa pamoja.
“Nous allons bien!” Nzuri!. Sote tukaitikia na hapo yule askari akachunguza kule nyuma ya gari tulipoketi na hatimaye kufunga mlango huku akiipokea leseni ya udereva ya yule dereva wetu na kuanza kuikagua. Kitambo kifupi cha ukimya kikapita wakati yule askari wa usalama barabarani akiendelea kuikagua leseni ya yule dereva wetu na wakati akifanya vile wale askari wenzake wakawa tayari wamekwisha karibia lile gari letu. Hata hivyo sikupenda yafanyike mahojiano zaidi kwa kukwepa kupoteza muda mwingi eneo lile na kuzuia kuibuliwa kwa mambo mengine yaliyokuwa yamefunikwa.
Hata hivyo hatimaye bahati ikaangukia upande wetu kwani haukupita muda mrefu mara nikamuona yule askari akimrudishia leseni yake yule dereva wetu na hivyo kuturuhusu kuendelea na safari. Dereva wetu akaipokea ile leseni na kushukuru huku akiingia kwenye gari. Wale askari wengine wakawahi kuondoa kile kizuizi cha barabarani kilichokuwa kimeandikwa kwa lugha ya kifaransa POLICE CONTROLE au kwa lugha ya kiingereza POLICE CHECK POINT. Muda ule ule bila ya kupoteza muda dereva wetu akawasha gari na kuingia barabarani huku akijitahidi kwa kila hali kutabasamu mbele ya wale askari wakati akiondoka eneo lile kwa kasi. Angalau moyo wangu ukapata utulivu baada ya kuona tukiondoka eneo lile la kizuizi pasipo rabsha yoyote.
Mwendo wetu ulikuwa siyo wa kubabaisha. Baada ya mwendo mfupi wa safari yetu mbele kidogo tukavuka daraja na tulipoingia upande wa kulia tukaanza kupanda mlima mkubwa. Wakati tukianza kupanda ule mlima nikageuka nyuma na kuwatazama wale askari wa barabarani na hapo nikawaona kuwa wote walikuwa wamesimama katikati ya ile barabara nyuma yetu wakitutazama namna tulivyokuwa tukitokomea mbele yao. Nikaendelea kuwatazama wale askari na kadiri gari letu lilivyokuwa likitokomea ndivyo taswira ya askari wale ilivyokuwa ikitoweka machoni mwangu. Hatimaye tukatokomea kabisa mbele yao katika barabara ile tukikatisha katikati ya msitu mnene wenye giza zito huku mvua kubwa ikiendelea kunyesha. Hali iliyopelekea barabara ile izidi kutisha wakati ule wa usiku.
Safari ikiwa bado inaendelea kikafuatia kitambo kirefu ukimya mle ndani na hapo nikayatembeza tena macho yangu taratibu kuwatazama wale abiria wenzangu waliokuwa mle ndani. Sikuona tashwishwi yoyote katika nyuso zao na kila mmoja alionekana kushika hamsini zake. Nikageuka kumtazama Amanda na hapo nikamuona kuwa bado alikuwa akitazama kule nyuma tulipotoka. Nilichokiona usoni mwake ilikuwa ni hali ya kupoteza utulivu na kwa namna nyingine nilimuona ni kama aliyekuwa amezama kwenye fikra fulani. Kuanzia pale sikumuona tena Amanda akilala na badala yake mara kwa mara tukawa tukitazamana na hatimaye nyuso zetu kuishia kwenye tabasamu zito la kupimana hisia huku mawazo mengi yakiendelea kupita kichwani mwangu.
Safari ilikuwa ndefu lakini yule dereva wetu alijitahidi kuwa makini huku akiendesha kwa mwendo kasi lakini wenye tahadhari za aina zote. Baada ya kitambo kirefu cha safari yetu wale abiria wengine waliokuwa mle ndani wakawa wamepitiwa na usingizi tena na hivyo kupelekea watu watatu tu mle ndani tuwe macho. Yaani mimi, yule dereva wa lile gari na Amanda hata hivyo hakuna aliyemsemesha mwenzake.
Safari ikaendelea huku tukivuka mabonde na milima, misitu minene na vichaka, madaraja na kona mbalimbali za ile barabara. Njiani tukapishana na wanyama wadogo kama Fisi, Digidigi, Fungo, Nguruwe mwitu, Paka shume,Kicheche,Dondoro na Swala waliokuwa wakivuka barabara kwa mwendo kasi baada ya kushtushwa na makelele ya injini na mwanga wa gari letu. Safari bado ikaendelea huku mvua kubwa ikiendelea kunyesha. Njiani katika baadhi ya maeneo tukakatisha katikati ya makazi ya watu lakini kwa wakati ule wa usiku nyumba zile zilionekana kama vichuguu yatima kwani wakazi wake wengi walikuwa usingizini kwenye nyumba za Tembe.
_____
Tulikuwa tumemaliza kushuka mteremko mrefu kabla ya dereva yule kukata kona kali kuingia upande wa kushoto na kulikaribia daraja ambalo mara baada ya kulivuka tungeanza kupanda mlima mwingine wakati nilipohisi tena kuwa mwendo wa gari letu ulikuwa ukipungua kwa ghafla. Hisia mbaya zikanijia akilini na hapo haraka nikainua kichwa na kuyapeleka macho yangu kule mbele ya lile gari kutazama. Miale mirefu ya mwanga mkali wa taa za lile gari Land Rover 110 ukafichua vizuri kile kilichokuwa mbele yetu kwenye ile barabara. Kitu ambacho bila shaka kilikuwa kimempelekea yule dereva wetu kupunguza mwendo wa gari kwa ghafla.
Kiasi cha umbali usiopungua mita sitini mbele yetu kulikuwa na mawe makubwa yaliyokuwa yamepangwa barabarani katika namna ya kuzuia gari lolote kupita na kuendelea na safari yake. Nikageuka haraka nikiyatembeza macho yangu kuwatazama abiria wenzangu waliokuwa mle ndani na hapo nikajua kuwa wote walikuwa usingizini isipokuwa mimi, dereva wa lile gari na Amanda ambaye kwa wakati ule na yeye alikuwa makini sana akitazama kule mbele ya gari. Amanda akanikata jicho la haraka la kunitahadharisha huku akirudia kutazama tena kule mbele. Nikiwa nimeupisha utulivu akilini mwangu, mitupo ya mapigo ya moyo wangu yakaongezeka mara dufu huku nywele zikinicheza kwa hadhari.
Nilipomtazama dereva wa lile gari haraka nikagundua kuwa alikuwa ameanza kuchachawa huku damu ikianza kumchemka mwilini kwa hofu. Tukio lile likampelekea yule dereva aanze kupangua gia huku akipunguza mwendo taratibu.
Haraka nikayapeleleza mazingira yale na kugundua kuwa hapakuwa na uwezekano wa kuyakwepa yale mawe kwa kupita kando ya ile barabara. Kwani ile barabara ilikuwa nyembamba na kando yake kulikuwa na miteremko mikali iliyokuwa imemezwa na misitu minene ya mvua. Hivyo kwa mahesabu ya haraka hapakuwa na namna ya kuendelea na safari yetu pasipo kusimama na kuyaondoa yale mawe ya kizuizi cha barabarani. Hisia zangu zikaniambia kuwa mambo hayakuwa shwari tena hivyo nilipaswa kufanya maamuzi ya haraka kabla macho yangu hayajaniletea tafsiri ya taswira mbaya iliyokuwa mbioni kuumbika kichwani mwangu. Mara moja nikayapeleka macho yangu kumtazama Amanda na macho yetu yalipokutana niliweza kuiona hofu iliyokuwa imejengeka usoni mwake na hapo nikamshika mkono wake taratibu huku macho yangu yakimueleza nini tulichopaswa kufanya muda ule. Tukiwa katika hali ile akili yangu ikarudishwa mle ndani baada ya mlio mkali wa risasi kusikika eneo lile.
Sasa nilikuwa na hakika kuwa tulikuwa tukielekea kukabiliana na utekaji na wakati nikitafakari nikawaona watu wawili wakijitokeza mbele yetu kwenye vichaka vilivyokuwa kando ya eneo lile huku mikononi wakiwa wameshika bunduki. Sikuona namna ya kuchomoka na ushindi wa haraka katika mkasa ule hivyo haraka nikafyatua komeo la ule mlango wa nyuma wa lile gari huku tayari nikiwa nimemuonesha ishara fulani Amanda kuwa asishtuke na kupiga kelele kisha nikamshika mkono haraka na kumsukuma nje na mimi nikafuatia. Hata hivyo mimi niliwahi kufika chini mapema zaidi nikitua kwa mgongo wangu ingawa sikuumia kutokana na begi langu nililokuwa nimelivaa vyema mgongoni.
Amanda aliwahi kuniangukia kwa juu na begi lake mgongoni na kweli nilijisikia faraja sana kwa tukio lile la kuangukiwa na mrembo kisha kwa mtindo wa sarakasi wa judo nikaikamata vyema mikono yake na kuibana miguu yake. Halafu nikamvuta na hapo tukawa tukijiviringisha haraka kama gurudumu la gari tukiiacha barabara ile na kupotelea kwenye kichaka kilichokuwa jirani na eneo lile. Kitu kilichonishangaza zaidi ni kuwa Amanda alikuwa mwepesi sana kuufahamu mtindo ule sarakasi wa judo huku akiendana vyema na mijongeo yangu na baada ya muda mfupi tukawa tumepotelea kwenye kichaka kizito kilichokuwa jirani na eneo lile.
Amanda alikuwa ameshtuka sana na kushikwa na hofu kutokana na tukio lile hata hivyo alikuwa makini sana kufuata maelekezo yangu. Muda mfupi uliyofuata tukajibanza kwenye kichaka kile kando ya barabara na hapo nikapata nafasi nzuri ya kutazama kile kilichokuwa kikiendelea kule mbele kwenye lile gari. Dereva wa lile gari letu Land Rover 110 alikuwa amepagawa haraka baada ya kuhisi jambo baya lilikuwa mbioni kutokea kule mbele. Hivyo akaingiza gia na kukanyaga mafuta akiongeza mwendo na kwa kweli sikuweza kutambua haraka dhamira ya tukio lile. Hata hivyo yule dereva hakufika mbali kwani muda ule ule nikasikia mlio mkali wa risasi huku lile gari Land Rover 110 ikiendelea kutimua mbio. Muda mfupi baada ya pale kukafuatiwa na milio miwili mingine ya risasi ambayo haraka nilishtushwa na matokeo ya kazi yake.
Risasi moja ilikuwa imepasua kioo cha mbele cha lile gari Land Rover 110 na kuacha tundu dogo lililozungukwa na nyufa nyingi usawa wa siti ya yule dereva na nilipochunguza kwa haraka nikashikwa na hamaki. Risasi ile ilikuwa imekifumua vibaya kichwa cha yule dereva na kutoboa bodi la lile gari ikiendelea mbele na safari. Ile risasi ya pili ilikuwa imepasua gurudumu la upande wa kushoto wa lile gari na hivyo kulifanya lile gari liende likiyumbayumba barabara nzima kabla ya hatimaye kugota kwenye yale mawe huku injini yake ikiendelea kuunguruma. Amanda akataka kupiga yowe la hofu hata hivyo nikawahi kumzuia kwa kumziba mdomo kwa kiganja changu.
Tukiwa kwenye kile kichaka tumejibanza tukaendelea kutazama kule mbele. Kikapita kitambo kifupi cha ukimya eneo lile na hapo nikaanza kuona watu fulani wakianza kujitokeza kwenye vichaka vilivyokuwa kando ya eneo lile. Nilipowachunguza haraka watu wale nikagundua kuwa idadi yao walikuwa saba na wote walikuwa vijana wa makamo yangu huku wakiwa na bunduki zao mikononi. Niwatazama haraka vijana wale na hapo nikashikwa na hasira kwa namna walivyokuwa wakijitapa na kuangua vicheko vya ushindi.
Wakati wale watekaji wakiendelea kusherehekea ushindi wao ghafla nikamuona mtu mmoja akitoka ndani ya lile gari Land Rover 110 na kuanza kutimua mbio akirudi kule tulipotoka. Hata hivyo yule mtu hakufika mbali kwani kufumba na kufumbua nikasikia mlio wa risasi kisha nikamuona yule mtu akitupwa hewani na kupiga yowe kali ya uchungu. Nilipomchunguza haraka mtu yule nikamkumbuka vizuri kuwa alikuwa miongoni mwa wale vijana wawili tuliokuwa tumekaa nao kule nyuma ya lile gari. Yule kijana alipoanguka chini akatulia kimya huku uhai ukiwa mbali na nafsi yake kwani ile risasi iliyofyatuliwa ilikuwa imepenya upande wa kushoto wa mgongo wake na kuacha tundu kubwa la moyo linalovuja damu.
Baada ya muda mfupi lile gari likawa tayari limezingirwa na wale vijana wenye bunduki mikononi huku wakilipigapiga bodi la lile gari ubavuni kwa mikono yao. Nilipowatazama wale vijana nyusoni mwao nikagundua kuwa hakuna aliyekuwa na hofu ya kumwaga damu ya mtu hata kidogo.
“Mumanuke mwese vubavuba!”. Nikamsikia kijana mmoja miongoni mwao akifoka kwa hasira na kwa kweli sikuweza kufahamu maana ya maneno yale ingawa haraka niliifahamu lugha ile kuwa ilikuwa ni kinyarwanda. Nikakumbuka kuwa nilikuwa nimemdanganya Amanda kuwa mimi ni mnyarwanda niliyekuwa nikiishi jijini Lubumbashi nchini D.R.Congo. Hata hivyo sikutaka maneno yale yanipite hivihivi bila ya kujua maana yake hivyo nikageuka na kumuuliza Amanda.
“Quʼest-ce que it dit?” Anasemaje?. Swali langu likampelekea Amanda ageuke na kunitazama kwa mshangao kisha akaniambia kwa sauti ya kunong’ona iliyojaa hofu.
“Il dit que dessandez vous tous”. Anawaambia kwa lugha ya kinyarwanda wale watu waliomo ndani ya lile gari kuwa.
“Kuwa wote shukeni chini haraka”. Nikamtazama Amanda kwa utulivu huku nikitafakari kisha nikayapeleka tena macho yangu kutazama kwenye lile gari na hapo nikamsikia kijana mmoja miongoni mwa wale vijana akifoka kwa sauti.
“Kandi ntihagire uwibeshya ngo yiruke”. Quʼil nʼause pas personne de dessandre. Amanda akanitafsiria kwa kifaransa akimaanisha.
“Asithubutu mtu yoyote kukimbia”. Mwingine akasikika akiongea kwa ghadhabu baada ya wale watu kwenye lile gari kuanza kushuka chini kwa haraka ya hofu.
“Zana ibyo ufite byose ntugire icyo uhisha”. Enleves toutes chause que vous avez et mattez-les par terre, ne cachez pas. Amanda akaniambia kwa kifaransa akimaanisha.
“Toa kila kitu ulichonacho na uweke chini na usijaribu kuficha kitu”. Yule kijana akaendelea kufoka kwa hasira huku wale abiria wenzetu wakiendelea kushuka kwenye gari kwa hofu.
Kwa kweli nilifadhaishwa na kushikwa sana na hasira juu ya tukio lile huku akili yangu ikiendelea kusumbuka katika namna ya kutaka kupambana na wale watu hatari na kuzima kabisa jaribio lile la kishenzi na la kinyama kuwahi kufanyiwa binadamu. Hata hivyo nafsi yangu ikanionya juu ya mpango wangu wa kuingilia kwani wale watu walikuwa makini sana huku wakijipanga katika mtindo wa kulizunguka lile gari. Wakilipa mgongo na kuelekeza bunduki zao katika pande zote tayari kukabiliana na rabsha yoyote ambayo ingejitokeza. Mwenzao mmoja tu ndiye aliyekuwa akishughulika na wale abiria wenzetu. Na wakati wale abiria wenzetu wakiendelea kushuka yule kijana mtekaji akaendelea kufoka kwa kinyarwanda.
“NʼImana iravuga ngo udakora ntakarye” Amanda akaendelea kunitafsiria kwa kifaransa baada ya kufahamu kuwa nilikuwa sikijui kinyarwanda.
“Même Dieu le déclare, ce lui qui ne travaille pas quʼil ne mange pas”. Hata Mungu anasema asiyefanya kazi na asile. Nilimsikiliza Amanda kwa utulivu na kuyaelewa vizuri maelezo yake kwa lugha ya kifaransa na hapo nikajikuta nikisikitika kwani wale watu hatari walikuwa wakiyatumia maneno ya Mtume Paulo katika kitabu cha Biblia kubariki kitendo chao kile cha kishetani.
Wale abiria wenzetu wakaendelea kushuka huku kila mmoja akijipekua na kutoa vitu vyake vyote mifukoni na kuviweka pale chini barabarani pamoja na mizigo yao iliyokuwa kwenye lile gari. Yule kijana mtekaji hatari akawa akimpekua mtu mmoja baada ya mwingine katika namna kuhakikisha kuwa hakuna aliyeficha kitu huku akiwavua wale abiria viatu na kila aliyemaliza kupekuliwa akawa akisogea mbele na kusimama.
Baada ya muda mfupi hatimaye wale abiria wenzetu wakamaliza kushuka kwenye lile gari na ule upekuzi ukafika kikomo. Yule mzee, abiria mwenzetu bahati mbaya baada ya kupekuliwa akawa amekutwa na pesa nyingi alizokuwa amezificha kwenye nguo yake ya ndani. Mara nikamuona yule kijana hatari akimtazama yule mzee kwa hasira kisha akamzaba makofi mawili ya nguvu...ITAENDELEA
 
Safi, lakini mkuu utaimaliza au ndo matangazo then tukanunue Kitabu??
 
RIWAYA; UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 10
Mtunzi:Kelvin Mponda

....yaliyompelekea yule mzee apepesuke lakini hata hivyo hakuanguka na aliposimama vizuri akaambiwa asogee mbele hatua sita. Haraka nilifahamu nini maana ya agizo lile na hapo hasira zikanipanda. Nikataka nitoke pale kichakani na kwenda kuingilia kitendo kile cha kinyama lakini Amanda aliwahi kunizuia akinivuta mguu wangu kwa nguvu zake zote hali iliyopelekea mtikisiko hafifu katika kile kichaka tulichojificha. Tukio lile likampelekea mmoja wa wale watekaji aliyekuwa akitazama ule upande wetu ahisi kitu na kuanza taratibu kusogea eneo lile. Sote tukajibanza na kutulia kimya huku kila mmoja akiusikiliza vyema mwenendo wa mapigo yake ya moyo namna yalivyokuwa yamepoteza utulivu kwenye kichaka kile. Yule mtu hatari akiwa ameielekeza bunduki yake kwenye kile kichaka akaendelea kusogea taratibu pale tulipojibanza lakini hatimaye nikamuona akisita na kusimama huku akitazama pale tulipojibanza kwa makini. Wale wenzake wakawa wamegeuka na kumtazama yule mwenzao kwa shauku lakini kitendo cha yule mtekaji hatari kusita na kugeuza akirudi kule alipotoka kikawapelekea na wale wenzake nao waache kumtazama na kuendelea na hamsini zao.
Nikameza funda kubwa la mate na kumshukuru Mungu kwa kutuepusha na ule mtutu wa bunduki ya yule mtekaji aina ya AK-47 iliyotuama vyema katika mikono yake chakaramu. Nikageuka kumtazama Amanda pembeni yangu na hapo nikamuona ameganda kama sanamu akionekana kutoamini vizuri kile kilichotokea mbele yetu. Muda uleule sote tukashtushwa na milio kadhaa ya risasi na hapo tukageuka na kutazama kule kwenye lile gari.
Risasi nne za yule mtekaji hatari zilikuwa zimeacha matundu yakivuja damu katika sehemu ya tumbo na kifua cha yule mzee aliyetuhumiwa kuficha pesa kwenye nguo yake ya ndani huku pesa zake zikichukuliwa. Yule mzee akapiga yowe dogo la hofu kisha akaanguka pale barabarani na kutulia kimya kifo tayari kikiwa kimemchukua.
Kwa kweli nilisikitika sana na kushikwa na ghadhabu juu ya tukio lile hata hivyo sikuwa na namna ingawa roho iliniuma sana. Wakati hali ile ikiendelea mara nikamuona kijana mmoja miongoni mwa wale watekaji akichepuka na kwenda kuipekua ile maiti ya yule kijana wa kwanza kabisa ambaye aliuwawa wakati alipokuwa akijitahidi kutoroka. Mchezo mzima uliokuwa ukiendelea eneo lile ulikuwa kama mkanda wa video ya kubuni. Hata hivyo lilikuwa ni tukio halisi huku mimi nikiwa miongoni mwa watazamaji.
Wakati lile sakata likiendelea eneo lile mara nilimuona mmoja wa wale watekaji akiingia ndani ya lile gari na kupitisha msako na alipotoka nje akawauliza wale abiria wenzetu waliosalia.
“Mwari muri bangahe hano imbere?”. Vous etaitent à combien ici?. Amanda akanifafanulia kwa kifaransa akimaanisha.
“Mlikuwa wangapi humu ndani?”
“Twari icumi”. Abiria mmoja akajibu kwa woga huku akitetemeka kwa hofu na nilipogeuka kumtazama Amanda akanitafsiria kwa kifaransa juu ya yule abiria alivyojibu.
“On était à dix”. Tulikuwa kumi. Jibu la yule abiria mwenzetu likawapelekea wale watekaji watazamane kwa mshangao kabla ya mmoja wao kuuliza.
“Ko mbona muri amunani babiri barihehe?”. Vous êtes à huit, où sont les deux?. Nilipomtazama Amanda akaniambia akimaanisha kuwa yule kijana mtekaji alikuwa akiwauliza wale abiria kuwa
“Mbona mko nane, waili wako wapi?”. Lile swali likawapelekea wale abiria wenzetu watazamane na kushangaashangaa huku dhahiri wakionekana hawajui kile kilichokuwa kimetokea na hapo nikawa na hakika kuwa hakuna mtu aliyetuona wakati tulipokuwa tukiruka kwenye lile gari mimi na Amanda. Wale watekaji wakatazamana kidogo na sikuona kama walikuwa na muda wa kuendelea kusubiri zaidi kabla ya mmoja wao kufoka kwa hasira.
“Mwese mujye ku murongo”. Vous tous à l ligne. Amanda akaniambia akimaanisha kuwa yule mtekaji alikuwa akiwaambia wale abiria.
“Haya wote pangeni mstari”. Wale abiria walipopanga mstari yule mtekaji akatoa amri nyingine akisema kwa kinyarwanda.
“Nimuririmbe, igishoro cy’umukene ni imbarage ze!”. Chanter, le capitale d’un povre c’est ses forces!. Akimaanisha.
“Imbeni, mtaji wa masikini ni nguvu zake mwenyewe!”
Ilikuwa ni amri ya udhalilishaji na ya fedheha hata hivyo niliwaona wale abiria wenzetu wakianza kuimba kwa hofu na wakati wakifanya vile wale watekaji wakawa wakiangua kicheko cha dhihaka huku baadhi yao wakikusanya vile vitu walivyowapora wale abiria pale chini barabarani na ile mizigo yao. Niliendelea kutazama kilichokuwa kikiendelea eneo lile hata hivyo nafsi yangu haikuniruhusu kuingilia tukio lile kwani sikuwa na silaha yoyote na wale watekaji walionekana kujizatiti kila eneo na bunduki zao mkononi. Wale abiria walipomaliza kuimba yule mtekaji akafoka kwa sauti akiwaambia wale abiria.
“Ntimuzibeshye guca muri uyu muhanda mwijoro ikindi gihe”. Nʼoser plus de passé cette route pendant la nuit. Amanda akaniambia kwa kifaransa akimaanisha kuwa yule mtekaji alikuwa akiwaambia wale abiria wenzetu kuwa.
“Msithubutu tena kupita barabara hii nyakati za usiku”. Hofu ikanishika wakati nilipoyasikia vizuri maelezo yale kutoka kwa Amanda na wakati nikiendelea kutafakari nafsi yangu ikashtushwa na ule unyama uliokuwa ukifanyika eneo lile.
Wale watekaji wote walikuwa wamewasogelea wale mateka pale walipokuwa wamesimama kisha mwenzao mmoja akawapa ishara ya kichwa ambayo muda mfupi uliofuata nilielewa maana yake. Wale watekaji wakaielekeza mitutu ya bunduki zao kwa wale mateka na hapo nikasikia milio kadhaa ya risasi. Zile risasi zilipokoma wale mateka wote wakawa wameanguka chini wakiugulia majeraha ya zile risasi na baada ya muda mfupi lile eneo lote likamezwa na ukimya wa kifo.
Kwa kweli nilihuzunishwa sana na tukio lile hasa pale nilipowakumbuka wale abiria wenzetu wakati tulipokuwa tukianza safari yetu jioni ile kule stendi ya Nyabugogo jijini Kigali Rwanda siku ile. Amanda akataka kupiga yowe la hofu hata hivyo niliwahi kumziba mdomo baada ya kuhisi hatari ambayo ingetukabili pindi wale watekaji ambapo wangelisikia yowe lile pale kichakani.
Wale watekaji walipomaliza kuutekeleza ule unyama wao haraka wakachukua vile vitu walivyopora na kuanza kukimbia wakilitoroka eneo lile. Sikuwa na namna yoyote ya kufanya badala yake nikajitahidi kumbembeleza Amanda aliyekuwa ameanza kuangua kilio cha kwikwi huku akitetemeka kwa hofu.
Tuliendelea kujibanza kwenye kile kichaka kwa muda usiopungua robo saa tukiendelea kutathmini hali ya usalama wa eneo lile. Nilipojiridhisha kuwa wale watekaji hatari wangekuwa tayari wametokomea msituni sikuona sababu ya kuendelea kujibanza kwenye kile kichaka. Hivyo nikasimama taratibu na kutoka kwenye kile kichaka nikijitokeza kwenye ile barabara. Hata hivyo nilimuonya Amanda na kumtahadharisha kuwa aendelee kujibanza kwenye kile kichaka na kuendelea kuchunguza hali ya usalama wa eneo lile huku nikimtaka anishtue pale ambapo angehisi jambo lolote la hatari.
Nilijitokeza kwenye barabara ile kwa tahadhari na kuanza kutembea taratibu nikielekea kwenye lile gari huku nikiyatembeza macho yangu kutazama huku na kule. Mvua kubwa bado ilikuwa ikiendelea kunyesha na kupitia mvua ile niliweza kusikia kelele za mjongeo wa maji mengi yaliyokuwa yakiendelea kukatisha kwenye lile daraja lililokuwa umbali mfupi nyuma yetu. Muda mfupi uliofuata nikawa nimefika kwenye ile sehemu iliyokuwa na ile miili ya wale abiria wenzetu waliouwawa. Kwa kweli roho iliniuma sana wakati nilipokuwa nikiitazama miili ile. Damu nyingi ilikuwa imesambaa eneo lile. Niliendelea kuwatazama wale watu waliolala pale chini na kwa kweli sikuona dalili ya uhai kwa mtu hata mmoja.
Nikiwa na hakika kuwa macho ya Amanda kule kichakani yalikuwa makini kuzitazama nyendo zangu nikaendelea kutembea hadi nilipolifikia lile gari pale lilipokuwa limegotea kwenye yale mawe. Nilipofika nikaanza kulizunguka lile gari nikilichunguza kwa makini na hapo nikagundua kuwa halikuwa limepata uharibifu mkubwa zaidi ya kioo chake cha mbele kilichokuwa na tundu dogo la risasi na gurudumu moja la mbele la upande wa kushoto lililokuwa limepasuliwa kwa shambulio la risasi za wale watekaji.
Bila kupoteza muda nikaufungua ule mlango wa dereva na kuushusha chini ule mwili wa yule dereva ambao ulikuwa umeharibiwa vibaya kwa shambulio la risasi kichwani. Wakati nikiushusha chini mwili ule nikajikuta nikimkumbuka dereva yule namna alivyokuwa makini kuimudu safari yetu barabarani. Nilipomaliza kuushusha ule mwili nikauburuta na kwenda kuulaza kando ya ile barabara kisha haraka nikarudi kwenye lile gari na kuanza kufanya upekuzi mle ndani.
Ndani ya muda mfupi nikawa nimefanikiwa kupata sanduku dogo jeusi la chuma lenye vifaa vya matengenezo ya dharura ya lile gari juu ya sanduku lile kukiwa na maandishi meupe yanayosomeka vizuri Tools box. Nilipolifungua sanduku lile baada ya pekuapekua ya hapa na pale nikafanikiwa kupata jeki ya gari na spana kadhaa muhimu. Muda mfupi uliofuata nilikuwa mbele nje ya lile gari upande wa kushoto nikitia jeki na kulifungua lile gurudumu lililopasuliwa kwa shambulio la risasi la wale watekaji.
Kazi ya kulifungua lile gurudumu niliifanya kwa wepesi wa hali ya juu na ndani ya muda mfupi tu nikawa nimefanikiwa kulifungua lile gurudumu na kulikokota haraka hadi kule nyuma ya gari ambapo nililipandisha na kulihifadhi mle ndani. Kisha nikalifungua gurudumu la akiba lililokuwa limefungwa nje ya ule mlango wa nyuma wa lile gari. Nilipomaliza nikalikokota haraka lile gurudumu na kwenda kulifunga kule mbele. Hata hivyo nilikuwa makini katika kutathmini mazingira ya eneo lile na kujihami na kitu chochote kibaya ambacho kingekuwa mafichoni kuninyemelea.
Upepo mkali ulikuwa ukivuma sambamba na mvua kubwa iliyokuwa ikiendelea kunyesha eneo lile lenye mabonde na miinuko yenye misitu na giza nene. Ndani ya muda mfupi nikawa nimemaliza kufunga lile gurudumu na nilipochungulia ndani ya lile gari nikauona ufunguo wa lile gari ukiwa mahala pake. Haraka nikaenda mbele ya lile gari na kuanza kuyasogeza yale mawe kando ya barabara. Nilipomaliza na kuridhishwa na kazi yangu nikapiga mruzi mwepesi kumshtua Amanda kule kule kichakani.
Kitambo kifupi cha ukimya kikapita kisha taratibu na kwa tahadhari nikamuona Amanda akijitokeza kwenye kile kichaka yalipokuwa maficho yetu huku mgongoni akiwa na yale mabegi yetu. Nilipomtazama vizuri nikagundua kuwa bado alikuwa amishikwa na woga na wasiwasi mwingi. Nikawahi kumpokea yale mabegi kisha nikafungua mlango wa nyuma wa lile gari Land Rover 110 na kuyatupia ndani. Wakati nikiufunga ule mlango wa nyuma wa lile gari Amanda tayari alikuwa ameshaingia ndani ya gari na kuketi kwenye siti ya abiria iliyokuwa kando ya dereva. Hivyo haraka nikarudi kule mbele ya lile gari ambapo niliufungua mlango wa dereva na kuketi nyuma ya usukani. Kisha nikatumia muda mfupi kufuta mabaki ya damu yaliyotokana na majeraha mabaya yule dereva aliyeuwawa kwa shambulio la risasi nikitumia kitambaa kidogo kilichokuwa nyuma ya ile siti ya dereva.
Ndani ya muda mfupi tu nikawa nimemaliza zoezi lile na kukitupa nje kile kitambaa. Nilipoyapeleka macho yangu kumtazama Amanda nikagundua kuwa alikuwa ameacha kulia ingawa bado alionekana kuwa ni mtu mwenye woga na wasiwasi mwingi kama ambaye bado haamini kile kilichokuwa kimetokea eneo lile muda mfupi uliopita. Macho yetu yalipokutana Amanda akajitahidi kuumba tabasamu hafifu usoni mwake hata hivyo hakufanikiwa kwani badala yake alionekana ni kama mtu anayetaka kulia na kucheka kwa wakati mmoja. Hata hivyo nikaumba tabasamu hafifu la matumaini usoni mwangu huku nikimuuliza.
“Comment, tu es bien”. Vipi upo sawa?.
“Nʼaye pas doute”. Ondoa shaka. Amanda akaongea kwa utulivu akiniambia. Sikupenda tuendelee kukaa eneo lile hivyo haraka nikafunga ule mlango wa dereva na kuvaa mkanda wa siti. Muda mfupi uliofuata nikawasha gari na kuondoka kwa kasi eneo lile huku mawazo mengi yakipita kichwani mwangu wakati nilipoanza kuwakumbuka wale abiria wenzetu waliouwawa ambao tulikuwa nao pamoja kwenye lile gari muda mfupi uliopita. Kwa kweli nilishikwa na huzuni isiyoelezeka kuwa nikishindwa kujilaumu au kujipongeza kwa kutokuingilia kati udhalimu ule na kuyaokoa maisha yao. Wakati nikiendelea kufikiri zaidi sikuona kama nilipaswa kulaumiwa pale nilipokumbuka kuwa sikuwa na silaha yoyote ya kujitetea wakati tukio lile la mauaji ya wale abiria wenzetu lilipokuwa likitokea. Vilevile wale watu hatari watekaji walionekana kuwa makini sana kwa kutoruhusu tukio lolote ambalo lingepelekea kuvurugika kwa mipango yao. Kisha nikamkumbuka Amanda na kuwaza kuwa hata yeye alikuwa kikwazo wakati nilipotaka kuingilia unyama ule huku nikiwaza kuwa huwenda hata yeye aliiona hatari ambayo ingetukabili sote endapo ningejitia kuingilia kati.
Mshale wa mafuta katika dashibodi ya lile gari Land Rover 110 ulionesha kuwa bado kulikuwa na mafuta ya kutosha kwenye lile gari ingawa sikuwa na hakika kama mafuta yale yangeweza kutufikisha hadi mwisho wa safari yetu. Kwani sikuwa nikiufahamu vizuri umbali uliokuwa umesalia mbele yetu. Wakati nikiingiza gia na kukanyaga mafuta nikageuka na kumuuliza Amanda kwa utulivu.
“Est-ce quʼil y a un tragé dʼici jusquʼ au frontiere de Rwanda et Burundi?. Kuna umbali mrefu kutoka hapa hadi ulipo mpaka wa nchi ya Rwanda na Burundi?. Swali langu likapelekea kitambo kifupi cha ukimya mle ndani huku Amanda akionekana kufikiria jambo fulani kisha akaongea kwa utulivu.
“Pas moin de trois heures de voyage”. Siyo chini ya safari ya masaa matatu kutoka hapa tulipo. Jibu la Amanda likanipelekea nigeuke na kumkata jicho kidogo kabla ya kugeuka na kutazama mbele huku nikimwambia.
“Ne tʼen fait mon amour, maintenant nous sommês bien”. Ondoa shaka mpenzi sasa tupo salama. Amanda akageuka na kunitazama, safari hii uso wake ukionekana kujawa na furaha ya tumaini kama mtu aliyepewa ahadi ya uhai wa milele.
Mwendo wangu wa kuendesha gari ulikuwa wa uhakika huku nikishuka mabonde na kupanda milima katika baadhi ya maeneo na kukatisha kwenye sehemu zenye misitu mizito iliyojitenga mbali na makazi ya watu. Kuna wakati barabara ile ilikatisha katika miji midogo ya nchi ya Rwanda yenye nyumba duni za udongo hata hivyo hatukusimama. Wakati wote tukiendelea na safari Amanda alikuwa kimya ingawa usingizi ulionekana dhahiri kuwa mbali naye huku...ITAENDELEA
 
RIWAYA: UFUKWE WA MADAGASCAR
SEHEMU: 11
Mtunzi:Kelvin Mponda

...akionekana kusumbuliwa na kumbukumbu ya yale matukio ya nyuma. Kila nilipokuwa nikiona kuwa ukimya ulikuwa ukizidi kushika hatamu mle ndani ya gari nilimchangamsha Amanda kwa maswali machache na utani wa hapa na pale nikijitahidi kumsahaulisha kwa muda yale yote yaliyotokea nyuma yetu. Hata hivyo sina hakika sana kama nilifanikiwa kwa kiwango nilichokitaka.
“Je te remerci Jean de mʼavoir sauveˊ”. Nashukuru sana kwa kuyaokoa maisha yangu Jean. Amanda akaniambia kwa utulivu huku akitabasamu na hapo nikageuka tena na kumtazama huku nikiangua tabasamu hafifu.
“Si cʼest ne pas Dieu, à ce coment on serait de morts”. Kama siyo Mungu huwenda muda huu tungekuwa wafu. Nikaongea kwa utulivu na hapo Amanda hakutia neno badala yake akatikisa kichwa chake kidogo akionesha kukubaliana na hoja yangu na kisha kikafuata kitambo kidogo cha ukimya huku Amanda akionekana kama anaewaza jambo fulani. Hatimaye akavunja tena ukimya na kuniuliza.
“Jʼai pensé que tu parles le kinyarwanda?”. Nilidhani kuwa unafahamu kuzungumza kinyarwanda?.
“Non!, mois cʼest une Rwandaise mais, me parents sont partis à Lubumbashi au Congo et jʼetais encore très joune. Cʼest pour ce la que je nʼai pas eu la chance dʼapprendre le kinyarwanda”. Hapana!, mimi ni mnyarwanda lakini wazazi wangu walihamia Lubumbushi nchini Congo mimi nikiwa bado mdogo sana. Hivyo sikupata nafasi ya kujifunza kinyarwanda. Nilijitahidi kudanganya hata hivyo Amanda hakuzungumza neno lolote badala yake alikaa kimya akiupisha utulivu huku akitazama nje kupitia dirishani na nilipomtazama nikajua kuwa alikuwa amezama tena kwenye tafakuri.
Swali la Amanda kwa namna moja au nyingine lilikuwa limeamsha hisia zangu na kuyaruhusu mawazo mengi kuanza kupitia kichwani. Kwani kwa namna moja au nyingine nilianza kuhisi kuwa Amanda alikuwa ameanza kushikwa na wasiwasi juu ya nyendo zangu. Hata hivyo nilifahamu kuwa sikupaswa kumlaumu juu ya mashaka yake dhidi yangu.
Mvua kubwa ilikuwa ikiendelea kunyesha katika barabara ile iliyokuwa ikikatisha katika eneo kubwa lenye misitu minene. Mvua ile sasa ilikuwa ikikokota takataka nyingi za msituni kutoka milimani. Takataka hizo zikikatisha barabarani na kuporomokea mabondeni hali iliyopelekea nipunguze mwendo na kuongeza katika nyakati tofauti ili kujihami na ajali. Hata hivyo mwendo wangu bado ulikuwa wa kasi mno lakini makini kwelikweli.
_____
Saa yangu ya mkononi ilionesha kuwa nilikuwa nimeendesha gari kwa muda wa saa moja na robo tangu tulipoanza safari ile na Amanda baada ya lile tukio la utekaji na mauaji ya kule msituni kufanyika.
Wakati nilipoyapeleka macho yangu kutazama kwenye dashibodi ya gari nikashtuka kuona taa ndogo ya njano ikiwaka na mshale wa mafuta ukienda kombo na hapo nikajua kuwa mafuta kwenye lile gari yalikuwa yakielekea kuisha. Hali ile ikanitia hofu kwani kwa mujibu wa maelezo ya Amanda ni kuwa tulikuwa tumebakiwa na umbali mrefu kabla ya kuufikia mpaka wa nchi ya Rwanda na Burundi.
Bila shaka Amanda alikuwa ameshtushwa na hali ya mashaka iliyokuwa usoni mwangu baada ya kutazama mwenendo wa mafuta kwenye dashibodi ya lile gari. Hivyo haraka akageuka kunitazama kabla ya kuniuliza kwa shahuku.
“Est-ce quʼil y a un problèm?”. Kuna shida yoyote?.
“Le carburant va ceterminer dʼici là, est-ce quʼil y a une station aux environs?”. Mafuta yanaelekea kuisha, kuna kituo chochote cha kujazia mafuta karibu na hapa?. Nikamuuliza Amanda huku nikilipuuza lile swali lake na hapo Amanda akatulia kidogo kama anayejaribu kukumbuka. Kisha akayapeleka macho yake kutazama nje kupitia dirishani na hapo nikajua kuwa alikuwa akijaribu kuyakumbuka mazingira yale. Alipogeuka kunitazama akaniambia.
“Il ya lʼune devant nous, mais cʼest plus de deux kilometre dʼici où sommes. Est-ce que le carburant est terminé?”. Kipo kituo kimoja mbele yetu lakini ni zaidi ya mwendo wa kilometa mbili kutoka hapa tulipo. Vipi mafuta yameisha?. Amanda akaniuliza kwa wasiwasi.
“Ça cedirige vers la fin, et on risque de ne pas continuer avec le voyage”. Yanaelekea kuisha na huwenda tukashindwa kuendelea na safari. Nikaongea kwa utulivu huku nikijitahidi kuudhibiti vizuri usukani wa lile gari kwenye kipande kile korofi cha barabara.
“Dieu aide nous”. Mungu tusaidie. Nikamsikia Amanda akiongea katika namna ya kukata tama hata hivyo mimi sikutia neno lolote.
Mara baada ya kukivuka kipande kile kifupi korofi cha barabara mbele kidogo tukaanza kupanda mlima na wakati tukipanda ule mlima nikatembeza macho yangu kutazama huku na kule. Tulikuwa tukiyakaribia makazi ya watu na kitendo cha kuanza kuona makazi yale ya watu kikafufua matumaini nafsini mwangu huku nikiwaza kuwa huwenda tulikuwa tukikikaribia pia kituo cha kujazia mafuta. Nikajikuta nikifarijika baada ya kuwaza kuwa hata kama ingetokea kuwa tumekosa mafuta eneo lile lakini kitendo tu cha kuyafikia makazi ya watu ilikuwa ni usalama tosha kwetu.
Mara tu tulipomaliza kuupanda ule mlima tukaanza kushuka mteremko mrefu mbele yetu na wakati tukishuka nikaanza kuuona mji mdogo wenye nyumba nyingi. Nyumba hizo baadhi zikiwa ni za kisasa na nyingine kuukuu za vijijini. Nikamuuliza Amanda kama alikuwa akilifahamu jina la mji ule na hapo akaniambia kuwa jina ule mji lilikuwa limemtoka kidogo. Tuliendelea kushuka kwa kasi na uchunguzi wangu ukaniletea majibu kuwa ule mji haukuwa na umeme. Baadhi ya wakazi wake walikuwa wakitumia majenereta na wengine paneli za sistimu za umeme wa jua. Ulikuwa ni mji mkubwa kiasi lakini kwa wakati ule wa usiku wa manane sikumuona hata mtu mmoja akirandaranda barabarani.
Tulipomaliza kushuka ule mteremko tukaanza kukatisha katikati ya makazi ya watu barabara ile ilipokuwa ikipita na kando ya barabara ile nikaona maduka, baa, mashine za kusaga na zahanati. Lakini kwa wakati ule vyote vilikuwa vimefungwa.
Tuliendelea kukatisha katikati ya yale makazi ya watu wa mji ule mdogo kisha tukaingia upande wa kulia tukiifuata ile barabara na kwa kufanya vile tukajikuta taratibu tukianza kuuacha ule mji mdogo nyuma yetu. Sasa macho yangu yakawa makini kutazama huku na kule nikitarajia kuona kituo cha kujazia mafuta kando ya barabara ile. Sikuona kituo chochote cha kujazia mafuta na tulikuwa tukizidi kuuacha ule mji mdogo nyuma yetu na hali ile ikanipa mashaka hata hivyo sikusimama.
Nilipokuwa mbioni kutaka kumuuliza Amanda juu ya kituo kile cha kujazia mafuta ambacho hapo awali alinihakikishia kukifahamu mara ghafla nikakiona kituo kimoja cha kujazia mafuta upande wa kulia mara baada ya kuvuka daraja lenye mto uliyopakana na mianzi mingi kando yake.
Sasa sikuwa na mashaka kuwa kituo kile cha kujazia mafuta ndiyo kile kilichokuwa kimezungumziwa na Amanda hapo awali wakati nilipomuuliza. Muda mfupi uliyofuata nikachepuka upande wa kulia na kwenda kuegesha gari kwenye upande wenye pampu ya kujazia mafuta ya petroli chini ya paa kubwa la kituo kile cha kujazia mafuta.
Kulikuwa na maroli mawili ya mafuta yaliyokuwa yameegeshwa kando ya kituo kile na zaidi ya pale hapakuwa na gari lolote jingine eneo lile. Mara tu tuliposimama kutoka kwenye ofisi ya kituo kile cha kujazia mafuta kilichokuwa kando ya eneo lile ambacho kilikuwa kikiwaka taa. Mlango wa ofisi ile ukafunguliwa kisha akatoka mwanaume mmoja mrefu ambaye sikuwa na mashaka kuwa alikuwa mfanyakazi wa kituo kile huku akiwa amejifunika kwa mwamvuli na mkononi ameshika kurunzi. Wakati yule mtu akija pale tuliposimama nikamuona mtu mwingine akisogea taratibu eneo lile na nilipomchunguza haraka nikagundua alikuwa ni mlinzi wa pale kutokana na mavazi yake na bunduki aliyoishika mkononi.
Bila kupoteza muda nikalichukuwa begi langu na nilipolifungua nikachukua kiasi cha fedha kisha nikafungua mlango na kushuka nikielekea nyuma kwenye tenki ya mafuta ya lile gari. Nilipofika nikauondoa mfuniko wa lile tenki haraka na wakati huo tayari yule mfanyakazi wa kile kituo cha mafuta alikuwa tayari amekwishafika eneo lile. Hivyo tuliposalimiana nikamwambia ajaze mafuta kwenye lile tenki huku wote tukiwa tumejikinga mvua na ule mwamvuli. Zoezi lile likafanyika kwa muda mfupi tu na mafuta yalipojaa nikamlipa yule mfanyakazi wa kile kituo cha kujazia mafuta kiasi cha pesa nilichopaswa kulipa kisha nikachepuka kidogo kwenda kwenye choo cha kile kituo kushusha haja ndogo. Muda mfupi baadaye nikarudi na kuingia kwenye gari na hapo safari yetu ikaanza tena tukiondoka eneo lile na kuingia barabarani.
Wakati tukianza safari ile nikakumbuka kuliweka vizuri lile begi langu na nilipokuwa nikifanya vile nikashtukia kuwa hali ya lile begi ilikuwa tofauti na vile nilivyokuwa nimeliacha baada ya kutoa zile fedha za kujazia mafuta. Kwa uchunguzi wa haraka nikajua kuwa lile begi lilikuwa limefanyiwa upekuzi wa hila na usio na umakini kiasi cha kunifanya nigutuke haraka. Kwa kweli moyo wangu ulipoteza kabisa utulivu ingawa kamwe sikuruhusu hali ile ionekane usoni mwangu.
Hapakuwa na mtu mwingine niliyekuwa nimemuacha mle ndani isipokuwa Amanda. Kwa kweli nilihisi hali ya baridi nyepesi ikiutafuna mtima wangu hasa pale nilipokumbuka swali la Amanda kuwa kwanini mimi nilikuwa sifahamu kuzungumza kinyarwanda wakati hapo awali nilikuwa nimejinadi kwake kuwa mimi ni mnyarwanda. Amanda alikuwa amelipekuwa begi langu kwa siri kutafuta nini?. Nikajiuliza kichwani hata hivyo nikapiga moyo konde na kujipa uvumilivu ingawaje kwa namna fulani nikaanza kujionya juu ya kuwa makini na mtu niliyekuwa nikiongozana naye kwenye ile safari. Nikiwa katika hali ile mara Amanda akaniuliza kwa utulivu huku akitazama mbele.
“Tu restes à Bujumbura jusquʼ à quand?”. Utakaa kwa muda gani Bujumbura?.
“Après avoir vu mon grand frère je nʼaller pas tarder, je veux rentrer à Lubumbashi au Congo”. Mara baada ya kuonana na kaka yangu sitakaa sana nitarudi nyumbani Lubumbashi nchini Congo. Nikamwambia Amanda wakati nilipokuwa nikiingiza gia na kukanyaga mafuta na kuzidi kutokomea mbali na ule mji mdogo.
“Et comment si tu ne parviens pas à seracontrer avec votre grand frère?”. Na vipi usipofanikiwa kuonana na huyo kaka yako?. Amanda akaniuliza kwa udadisi.
“Il faudra que je rentre à la maison très tôt”. Itabidi nirudi nyumbani mapema. Nikamwambia Amanda huku nikijitahidi kuumba tabasamu hafifu usoni mwangu kasha baada ya hapo kikafuatia kitambo kifupi cha ukimya na nilipomtazama Amanda nikajua kuwa bado alikuwa kwenye mawazo.
Nilipoitazama saa yangu ya mkononi nikagundua kuwa ilikuwa ikielekea kutimia saa saba usiku. Mvua bado ilikuwa ikiendelea kunyesha katika barabara ile iliyokuwa ikikatisha msituni kwenye mabonde na milima. Ukimya wa usiku ule ukatupelekea tusikie vizuri ile sauti ya makelele ya ile injini ya gari wakati nilipokuwa nikiingiza gia na kukanyaga mafuta katika nyakati tofauti.
Sasa tulikuwa mbali kabisa na ule mji mdogo nyuma yetu huku angalau tukiwa na hakika na safari ile. Amanda alikuwa msichana mrembo sana ambaye mwanaume yeyote angejisikia fahari sana walau kubadilishana naye mawazo. Hivyo kitendo kile cha kusafiri peke yetu kwenye lile gari kilikuwa kimeamsha hisia za furaha kubwa moyoni mwangu kwa kuambatana na mrembo yule kando yangu. Nikiwa katika mawazo yale mara Amanda akazirudisha fikra zangu mle ndani kwa kuniuliza.
“Tu as la femme et des enfants?”. Una mke na watoto?. Swali lile likanipelekea nitabasamu kidogo huku nikigeuka kumtazama Amanda.
“Je ne suis pas encore marié, et je nʼai pas une fiancée”. Bado sijaoa na wala sina mchumba. Nikaongea kwa utulivu huku nikishindwa kuelewa uelekeo wa maongezi yale ingawa kwa namna moja au nyingine yalielekea kunifurahisha. Kitambo kifupi cha ukimya kikapita kisha nikageuka na kumuuliza Amanda.
“Et toi, tu es mariée?”. Na wewe vipi umeolewa?. Swali langu likampelekea Amanda atabasamu kidogo huku akiviminyaminya vidole vya mikono yake kama mtoto anayedeka kisha akaniambia huku akigeuka na kunitazama. Lile tabasamu lake maridhawa likikataa kwenda likizo usoni mwake.
“Je ne suis pas encore mariée mais jʼai un fiancé”. Sijaolewa ila nina mchumba. Amanda akaniambia kwa utulivu huku akijitahidi kusahau yaliyopita.
“Où est votre fiancé?”. Mchumba wako yuko wapi?. Nikamuuliza.
“Il est en Amerique pour les études”. Yupo masomoni nchini Marekani. Amanda akaniambia kwa kujisifu akijitahidi kunionesha ni kwa namna gani alikuwa na bahati ya uhakika wa maisha mazuri kwa kuolewa na mwanaume msomi ingawa nilimtazama kidogo na kumhurumia wakati nilipowaza kuwa atakuwa katika hali gani pale ambapo huyo mwanaume anayemtarajia aolewe naye abadili mawazo ghafla na kumuoa msichana mwingine.
“Très bien, sʼans doute vous aller vous mariés très tôt quand il rentrel!”. Vizuri sana, bila shaka mtafunga ndoa yenu mapema sana jamaa atakaporudi. Nikamwambia Amanda huku moyoni nikijihisi wivu kwa kutokuwa na nafasi yoyote katika moyo wa mlimbwende yule wa ajabu.
“Oui, si Dieu le veut”. Ndiyo, Mungu akipenda. Huku akionesha furaha usoni na kujiona kuwa ni msichana mwenye bahati Amanda akaniambia kwa ujivuni.
“Il sʼappelle comment?”. Anaitwa nani?. Nikamuuliza Amanda huku wivu ukinisimanga moyoni.
“Jean-marie”. Amanda akaniambia kwa kujiamini na kwa kweli jibu lake likapandisha wivu mkubwa moyoni mwangu hali iliyonipelekea nimeze funda kubwa la mate kuupoza mtima wangu. Nikabaki nikimuonea wivu Jean-marie kwa kuopoa malkia wa nguvu kiasi kile.
Kwa kweli niliumudu vyema usukani wa gari na mwendo wangu ulikuwa siyo wa kubabaisha nikipanda milima na kushuka mabonde kama upepo huku akili yangu ikijikita katika kuwaza hali ya mambo itakavyokuwa baada ya kufika jijini Bujumbura nchini Burundi. Nikiwa katika mawazo yale mara Amanda akaniuliza tena...ITAENDELEA
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom