Riwaya: Mvamizi

RIWAYA; MVAMIZI

NA BAHATI K MWAMBA.

SEHEMU YA TANO



Alizima kurunzi yake na kutaka kutimka lakini alijikuta akisita kufanya hivyo baada ya wazo fulani kupita kichwani mwake, alirejea kuiwasha kurunzi yake kisha alianza kuzikagua zile maiti moja baada ya nyingine. Alikagua kwa umakini akiwa anatarajia kuona baadhi ya vitu kutoka kwa wale jamaa; alihitaji kupata utambulisho wao au alama zozote mwilini mwao ambazo zingeliweza kumpa majibu ya maswali baadhi aliyokuwa anajiuliza.

Waliowengi hakuna alichoambulia lakini mmoja kati yao, soksi za miguu yake zilikuwa zimehifadhi vitu viwili vilivyogeuka kuwa muhimu sana kwa usiku ule. Alikutana na karatasi moja iliyokuwa ina majina mawili na namba nne tu. Alipojaribu kuzisoma namba zile, aligundua ni namba za makazi ya mtu japo hakuwa na uhakika na kile alichokifikiria. Kitu kingine ndicho kilichomshitua zaidi baada ya kukiona na hakujua kilikuwa kwa mtu yule kwa bahati mbaya au kilikuwa pale makusudi. Lakini kama ni makusudi, kwa nini kilikuwa kimefichwa miguuni mwa mtu na kilionekana kuhitajika baada ya operesheni ile ya usiku.

Pito Fizo alivitizama vile vitu alivyokuwa ameshika mkononi mwake. Alishika karatasi yenye jina la mtu na namba za makazi na pia alishika force number(namba za utambulisho jeshini) ambazo hubandikwa juu ya mifuko kwenye sare za jeshi kwa kila mwanajeshi. Kilichomshangaza si kuikuta pale bali kilichomshangaza ni kuikuta ikiwa imeambatana na bendera ya Tanzania na kwa mwonekano pekee, ilimpa uhakika namba ile ni ya mwanajeshi wa jeshi la Tanzania.

Alibaki na swali moja kichwani ambalo hakupata majibu yake kirahisi, kwa nini ipo kwa watu wale ikiwa imehifadhiwa kwa kificho namna ile? Ina maana gani kwa watu wale?

Hakupata majibu ya kile alichokuwa anajiuliza na aliona kuendelea kujiuliza katika mazingira hatarishi kama yale, ni kuiuza roho yake kwa bei ya kutupa. Alianza kupiga hatua kuondoka eneo lile akiwa bado ameiwasha kurunzi yake..

Hakupiga hatua nyingi, macho yake yaliona jambo ambalo lilimfanya asimame na kutazama kwa umakini mkubwa huku moyo wake ukiongeza kasi ya mapigo.

Aliogopa akiwa bado hajaelewa vema kile alichokiona, moyo wake ulitiwa ganzi la butwaa.

Kuhakikisha anaelewa vema kile alichokiona chini, aliamua kupiga goti moja chini na kuinamisha uso wake hadi usawa wa ardhi, mkono wake ulioshika kurunzi ukisogea karibu kabisa na uso wa ardhi iliyokuwa imetifuliwatifuliwa na kuondolewa nyasi hadi ulipobaki udongo ambao ulikuwa umebeba ujumbe mzito kwa Komando mdunguaji.

Pito Fizo alikuwa anatazama mchoro ambao huchorwa mara chache sana kwenye uwanja wa vita. Mchoro ambao huwa umebeba ujumbe mzito kwa unaemhusu.
Mchoro ule endapo ungelikutana nao ulikuwa unakupa taarifa ngumu na ambayo ni lazima ukubaliane nayo kwa masilahi ya usalama wako na wengine, ni mchoro unaokuweka kwenye ramani ya kifo endapo utakubaliana na kile ulichoelewa kutoka kwenye mchoro huo. Mchoro ule ulimpa taarifa mbili ambazo hakuwa anazitegemea kwa usiku ule.
Ndani ya mchoro uliokuwa umezungushiwa duara kulikuwa na mfano wa mti ulioota juu ya mti mwingine, huku tunda moja likianguka chini. Pia kulikuwa na mishale miwili iliyoachana pande; mmoja ukielekea mashariki na mwingine magharibi. Mchoro wote ulikuwa mchoro njiti lakini ulieleweka vema. Mti ulioota juu ya mti mwingine na tunda moja kuanguka ilimaanisha operesheni imeingiliwa na baadhi ya watu wamepoteza maisha pia, ilimaanisha kuna jambo la kusalitiana miongoni mwa watu walioifahamu operesheni ile. Lakini mishale ile ilikuwa na maana ya kuwa kuna kugawana majukumu miongoni mwao, mshale mmoja ilimaanisha jukumu hilo litachukuliwa na mmoja tu na mshale mwingine ulioelekea Magharibi ilimaanisha kutelekezwa gizani kwa manufaa ya wengi.

Pito Fizo alibaki akiutazama mchoro kwa sekunde kadhaa baada ya kuuelewa na sekunde hizo alikuwa anatafuta alama ya mchoraji ili ajue aliyeuchora. Nje ya mduara kulikuwa na alama ya nukta iliyofifia na alipoiona alisimama.

“John Ndula!” Alijisemea huku mguu wake wa kulia ukifuta pale palipokuwa pamechorwa. Akili yake ilikuwa inafanya kazi kuliko uwezo wa kawaida wa kufikiri. Kila alichokuwa anajaribu kuwaza na kuwazua hakupata mwanya wa kujua afanye nini kwa wakati kama huo. Alinyanyua mkono wake wa kushoto na kuitizama saa yake ambayo ilimwonesha ilikuwa ni saa tisa za usiku.

Aliposhindwa njia ya kuanza kufanya kile alichoelekezwa, aliafikiana na ubongo wake kuwafuata wenzake na waondoke wote na kama ni kuwatafuta wabaya wao basi wafanye wakiwa ndani ya Tanzania na si vinginevyo. Alichukua kisu chake kidogo kilichokuwa na dira kwenye kitako chake, alitazama uelekeo ambao walikuwa wamekubaliana kukutana na msaada. Hakuhitaji kuendelea kubaki pale alianza kukimbia kuelekea mashariki mwa pale alipokuwa, alihitaji kuwahi kabla ya wengine hawajaondoka. Kabla hajakimbia hatua sabini, masikio yake yalisikia vishindo vya watu wakiwa umbali wa hatua chache mbele yake, haraka bila kujiuliza aliruka na kuangukia kwenye nyasi ndefu zilizokuwa kando ya njia aliyokuwa anaitumia kuelekea upande wa mashariki. Alipotua chini hakutaka kutulia, alianza kukimbia huku akiwa ameinama na kutafuta sehemu ambayo angeliweza kuwaona waliokuwa wanakimbia kwenye njia aliyokuwa anaitumia. Alipoapata sehemu ambayo aliweza kuona vema, alitulia huku akiweka vema bunduki yake tayari kwa lolote ambalo lingelitokea.

Miwani ya kuonea gizani aliyokuwa ameivaa usoni mwake ilimwezesha kuona kundi kubwa la watu waliojizatiti kwa silaha za moto wakikimbia kuelekea upande ambao kulikuwa na miili ya wapiganaji ambao hawakuwa na uhai. Watu wale walikuwa wamevaa sare sawa na zile walizokuwa wamevaa wale watu ambao walikuwa wamekutana na dhahama ya risasi kutoka kwa makomando waliokuwa wameuvamia msitu ule bila taarifa. Kundi lilipita kwa kasi na sekunde chache baadae mtu wa mwisho alipita na haraka bila kusita na yeye alitoka nyuma kwa tahadhari huku kichwani mwake akisahau kile kilichokuwa kinamkimbiza kuelekea upande wa mashariki mwa pale walipokuwa.

Hatua zake hazikuwashitua wale jamaa ambao walionekana kutaharuki baada ya kukuta wenzao wamelala chini kama kuku wa mdondo. Walizingira eneo lile huku kiongozi wao akiwasiliana na watu upande wa pili kupitia simu ya upepo. Baada ya maelezo kadhaa, miili isiyo na uhai ilibebwa na kuondolewa pale huku wengine wakiweka ulinzi wa hali ya juu.
Mambo yote yalifanyika huku Pito Fizo akiona kila hatua na katikati ya maongezi ya kiongozi wao kuna majina mawili alisikia yakitajwa na kujirudia mara kwa mara, mwanzo hakuelewa kilichokuwa kinazungumzwa, lakini ilitokea kama turufu ambayo hakuwa ameitegemea ambapo katikati ya maongezi, kiongozi aliongea maneno machache ya kiingereza ambayo bado jina moja ambalo lilijirudia mara nyingi zaidi ya mengine, lilitajwa tena.

‘Dualo Ebanjo!’ Lilikuwa ni jina lilogonga ngoma za masikio ya Pito kila baada ya maneno machache ambayo alimakinika kuyafuatilia..

“Dualo Ebanjo na Carlos Guiremales.” Pito alirudia hilo jina taratibu huku akiinuka pale alipokuwa amejibanza huku kumbukumbu za kusudio lake la kuungana na wenzake likirejea tena.

Alisimama huku akijaribu kupima uzito wa jambo analotaka kucheza nalo.

“Dhalimu ni Dhalimu tu!” Alijisemea huku akitupilia mbali wazo lake la kuwafuata wenzake. Aliamua kuvaa roho ya umauti kuweza kupambana na kile ambacho alielekezwa kufanya.

“Nahitaji kuwa mwepesi!” Alisema huku akitua begi lake lililokuwa na vifaa kadhaa ikiwemo vifaa tiba vya dharura, kisha alianza kuvua mavazi yake hadi aliposalia na bukta mwilini mwake. Nguo zake zote aliziweka pamoja kisha alichukua kiberiti na kuziwasha moto. Lengo lake ilikuwa ni kupoteza ushahidi endapo angelikamatwa huko aendako ili iwe rahisi kukana uhusika wa nchi yake, hivyo alikuwa anajaribu kuiweka mbali nchi yake na kile walichokuwa wameenda kukifanya ndani ya Angola.

Alihakikisha nguo zimeteketea na kubaki jivu pekee, alichukua bunduki yake na kisu kisha alianza kukatiza katikati ya pori akiwa na bukta na viatu(buti) pekee mwilini mwake. Alikuwa anaelekea kwenye kiota cha miiba, kiota ambacho kiliwatoa Tanzania nyakati za usiku na bahati mbaya sana hawakufanikiwa kukifikia na kulichukua yai lilokuwa linahifadhiwa kwenye kiota kile.

“Yawezakana msaliti yupo nchini kwetu, lakini utambulisho wake nitaupata huku huku labda nife kabla ya kuwafikia..” Alijisemea huku akipambana kupita kwenye majani marefu ambayo yalimkwaruza kwenye mwili wake usio na nguo.

Kufika kwenye kiota cha miiba ilimhitaji kutumia zaidi ya dakika kumi na tano kwa mbio za mchakamchaka. Kiota cha miiba kama wao walivyopenda kuita, ilikuwa ni kambi ya jeshi iliyojitenga mbali na mji. Kambi ile ilikuwa na kashifa ya kuhifadhi wahalifu wengi ambao hunufaika na wizi wa madini ya almasi nchini Angola, pia ilikuwa ni kambi inayotoa mafunzo ya kijeshi kwa wapiganaji wa makundi mbalimbali ya waasi. Mara zote viongozi wa nchi ya Angola walikuwa wakipinga uhusika wa kambi hiyo katika udhalimu huo huku wakati mwingine wakiomba ushahidi wa tuhuma hizo kwa mataifa yaliyokuwa yanainyoshea kidole kambi hiyo na baadhi ya viongozi wa kijeshi walioiongoza. Hakuna nchi iliyowahi kutoa ushahidi wa moja kwa moja kuhusu tuhuma hizo ijapokuwa, tuhuma zao ziliendana na vielelezo vya kuunganisha matukio yaliyokuwa yakionesha uhusika wa baadhi ya viongozi wa kambi ile ya jeshi ambayo ilikuwa na umaarufu mkubwa ndani na nje ya Angola. Nchi nyingi zilijitahidi kutuma majasusi wao kuingia ndani ya mji wa Chipipa ili kujitahidi kupata uthibitisho wa tuhuma zao, lakini mara nyingi Chipipa iligeuka kuwa sumu kwa majasusi hao kwa kuwa waliowengi hawakubahatika kurejea nchini mwao.

Kuwepo kwa makomando toka nchini Tanzania ilikuwa ni miongoni mwa operesheni chache za namna ile zilizofanyika kwa usiri mkubwa, lakini tofauti na mataifa mengine ambayo yaliituhumu Angola, nchi ya Tanzania haikuwahi kuituhumu wala kuonesha dalili za kuituhumu, lakini kambi ile ilikuwa imemhifadhi mtu muhimu na mwenye siri nzito. Operesheni ile ambayo haikufanikiwa ilikuwa ni moja ya majaribio ya kumnasa mtu huyo ambae aliwahi kuhudumu kwenye jeshi la nchi. Kupatikana kwake kulikuwa na umuhimu mkubwa sana kwa masilahi mapana ya nchi, lakini bahati mbaya misheni ilishindikana na sasa alikuwa amesalia komando mmoja tu, ambae alikuwa anajaribu kucheza patapotea.

Dakika kumi na nane zilitosha kumfikisha komando Pito Fizo. Kambi ya Chipa alimaarufu kwa jina la kiota cha miiba ilikuwa mbele yake umbali wa mita hamsini. Taa kubwa na zenye mwanga mkali zilikuwa zinamulika eneo kubwa la kambi huku wanajeshi kadhaa wakiwa wanaranda huku na huko, wakiwa wamejizatiti vema na silaha zao mikononi. Kambi ile aliifahamu vema kupitia michoro ya picha mbalimbali walizokuwa wanazitizama siku chache kabla ya usiku huo.
Alitulia tuli kwenye kilima kilichokuwa pembeni kidogo mwa kambi. Alikaa kwenye kilima kile kwa sababu kilikuwa ni miongoni mwa sehemu salama ambazo hazikuwekewa ulinzi madhubuti licha ya kuwa kilikuwa ni kilima cha kimkakati. Hakujua ni kwa nini kilima kile hakikuwa na ulinzi au pengine ni kwa sababu ukubwa wa kambi ulipofusha uwezo wa maamuzi wa walinzi wa kambi.

Wakati akiwa ametulia na bunduki yake mkononi, macho yake yalikuwa yanawatizama makamanda wachache waliokuwa wakizurura ndani ya kambi lakini muda wote hakuweza kuona watu waliovalia mavazi yanayofanana sawa na yaliyovaliwa na watu aliowaona msituni.

“Ina maana watu wale hawafungamani na kambi hii?” Alijiuliza huku akielekeza macho kwenye lango kuu la kuingilia ndani ya kambi na kuna kitu alikuwa anatizama langoni pale.

Alikuwa analitizama gari moja aina ya VasesGuage lililokuwa linaingia ndani ya ile kambi. Gari lile lilikuwa la kijeshi likiwa limefunikwa juu kwa turubai zito. Kilichomvutia ni mabishano yaliyokuwa yakiendelea pale kati ya dereva na mmoja ya walinzi wa getini. Hakufahamu walikuwa wanabishana nini licha ya kuwa gari lilikuwa la jeshi.

Baada ya mabishano ya takribani dakika sita, hatimae aliona lile gari likiruhusiwa kuingia na walinzi kuendelea na majukumu yao.

“Ninahitaji kuingia ndani ya kambi” Alisema huku akitupia macho yake kwa mlinzi mmoja aliyekuwa juu ya kidungu kilichokuwa na taa kali iliyokuwa ikizunguka pande kadhaa za kambi.

“Kambi hii ina vidungu vinne, nakihitaji kidungu cha upande wa kusini ili niingie ndani ya kambi” Aliwaza huku akishuka juu ya kilima na kuchukua uelekeo wa upande wa kusini ambako kulikuwa na mto uliokuwa unatiririsha maji.
Kambi ile ilikuwa kando ya mto Chipa, uliokuwa unatokea Congo DRC.

Aliambaa ambaa kwenye giza huku mara chache akijitahidi kukwepa mwanga wa taa uliokuwa ukitembezwa kuzunguka kambi, kila baada ya sekunde chache.
Alipofika upande wa kingo za mto, macho yake yaliweza kuona mitumbwi sita ya injini ambayo iliyumika kuwavusha wanajeshi upande wa pili wa mto au kuwasafirisha kuelekea mjini Chipipa. Mitumbwi yote ilikuwa ni ya kujaza upepo, mitumbwi maalumu kwa safari za kijeshi.
Aliambaa na kingo huku akiwa makini kuotea maeneo ambayo angeliweza kumuona mlinzi wa eneo lile lakini hadi anaifikia, hakuweza kuona mtu yeyote. Aliitizama kwa umakini huku akisoma ukubwa wa injini zilizokuwa zimefungwa kwenye mitumbwi ile, akiwa na lengo la kuona uwezo wa kila injini. Dakika moja ilitosha kuikagua mitumbwi ile ambayo ilikuwa inaelea kwenye kingo za mto. Aliufuata mtumbwi mmoja na kung'oa nanga yake fupi, kisha aliusukuma taratibu na kuutenga mbali na mitumbwi mingine. Alipohakikisha umbali upo vile alivyotarajia, alirejea kwenye ile mitumbwi mitano aliyokuwa ameicha na alipoifikia alianza kuharibu injini zake kwa umakini mkubwa, zoezi ambalo lilichukua dakika mbili kukamilika. Alipohakikisha amemaliza kufanya uharibifu taratibu alianza kuvuka daraja dogo lililojengwa kwa ajili ya kuruhusu maji ya mto yapite kwa chini, huku upande wa juu ukianza ujenzi wa ukuta mfupi ambao ulibeba kidungu kimoja. Alihitaji kukutana na mlinzi aliyekuwa juu ya kidungu kile. Alivuka kikaravati huku akikwepa mwanga wa taa kutoka kwenye kile kidungu. Kuna wakati ilimlazimu kutambaa kama mnyama kemodo na kuna wakati alikimbilia tumbo mithili ya mamba aliyeshiba supu ya swala. Mikimbio yake yote ilikuwa ni kwa nia ya kukwepa kuonekana na mlinzi aliyekuwa kwenye kidungu.

Kidungu kile kilikuwa kimejengwa imara kwa nguzo nne za chuma na kwenye nguzo mbili kuliwekwa ngazi ndefu kuelekea juu, sehemu ya kukaa mlinzi. Pito Fizo alizitazama zile nguzo kisha alianza kuzikwea ngazi taratibu bila papara huku mara chache akisitisha mwendo na kuwaruhusu mbu waushambulie mwili wake ambao haukuwa na nguo, zaidi ya bukta fupi yenye mifuko mitatu iliyokuwa imesheheni silaha muhimu, huku kiuononi kukiwa na mchipi ulioshika vema mpina wa kisu kikubwa cha maangamizi. Wakati anapanda juu ya kidungu hakuacha kufuatilia waya mweusi wa umeme ambao uliwezesha taa kuwaka na alipokaribia kuingia ndani ya kidungu, aliushika na kuuvuta mara mbili kwa nguvu kiasi kilichofanya taa ianze kusinzia. Lengo la kufanya hivyo, alihitaji kumweka bize mlinzi ambae angelianza kuhaingaika na taa lakini pia hakutaka zoezi lake libebe umakini wa walinzi wengine ambao walikuwa karibu na pale, hivyo alihitaji kuharakisha kutenda lilompeleka kule juu na kisha atibu tatizo la taa.

Wakati taa inazima na kuwaka, ni wakati huo ambao Pito Fizo alifanikiwa kuingia kwenye kidungu akiwa nyuma ya mlinzi ambae alikuwa ameiweka kando bunduki yake, akishughulikia taa. Hiyo ni nafasi aliyoihitaji kuliko wakati mwingine, haraka alichomoa kisu chake na kwenda kukijaza mgongoni mwa mlinzi huku mkono wake wa kushoto ukiziba mdomo wake asiweze kupiga kelele.
Kukurukakara za kupambania uhai hazikuzaa matunda na hatimae mlinzi aliaga dunia, akimwacha Pito akiwa amechukua nafasi yake ya ulinzi.

Pito Fizo alijua namna ya kufanya na taa ilirudi kuwaka vema, kisha alianza kuizingusha kama alivyokuwa akifanya mlinzi aliyekuwa zamu usiku huo. Alimulika kila kona ambayo alihotaji kuimulika na wakati akiendelea kumulika, macho yake yaliangukia upande wa kaskazini mwa pale alipokuwa. Upande huo ulikuwa umefunikwa vema na msitu mkubwa, huku nyasi zikikamilisha msemo wa ‘msitu' msitu mnene kwa kufunga vema ardhi ya upande huo. Upande huo ndiyo ulikuwa mgongo wa kambi na kulionekana barabara nzuri ikiwa inaelekea katikati ya msitu uliokuwa upande huo wa kasikazini.

Wazo moja la hatari likapita kichwani mwake na alihitaji kulifanyia kazi kabla hajaelekea ndani ya kambi kufanya kilichokuwa kimempeleka pale.

.
.
.
.IMEANDIKWA NA BAHATI K MWAMBA.

SIMU; 0656741439/0758573660
 
RIWAYA; MVAMIZI
NA; BAHATI K MWAMBA

SIMU; 0758573660/0656741439...


Pito Fizo alijua namna ya kufanya na taa ilirudi kuwaka vema, kisha alianza kuizingusha kama alivyokuwa akifanya mlinzi aliyekuwa zamu usiku huo. Alimulika kila kona ambayo alihitaji kuimulika na wakati akiendelea kumulika, macho yake yaliangukia upande wa kaskazini mwa pale alipokuwa. Upande huo ulikuwa umefunikwa vema na msitu mkubwa, huku nyasi zikikamilisha msemo wa ‘msitu' msitu mnene kwa kufunga vema ardhi ya upande huo. Upande huo ndiyo ulikuwa mgongo wa kambi na kulionekana barabara nzuri ikiwa inaelekea katikati ya msitu uliokuwa upande huo wa kasikazini.

Wazo moja la hatari likapita kichwani mwake na alihitaji kulifanyia kazi kabla hajaelekea ndani ya kambi kufanya kilichokuwa kimempeleka pale.

Alihitaji kuweka taharuki ndani ya kambi ili iwe rahisi kwake kuingia na kutoka bila kikwazo, pia alihitaji kupata mavazi ya kawaida ambayo aliamini atayapata ndani ya kambi, mavazi ambayo yangempa hadhi ya mtu wa kawaida endapo angelifanikiwa kuingia mjini Chipipa au sehemu nyingine yoyote ambayo angelifanikiwa kuingia.

Aliteremka haraka juu ya kidungu na alipofika chini aliiweka sawa bunduki yake ambayo alikuwa ameining'iniza mgongoni wakati alipokuwa anapanda juu. Alitizama pande zote ambazo zingeliweza kuwa hatarishi kwake alipoona kila kitu sawa, alianza kujongea kwa umakini huku akitumia vivuli vya miti na vichaka vya nyasi kama kinga ya kutokuonekana kirahisi.

Alifanikiwa kufika bila kuonekana. Hakuhitaji kutumia muda mwingi kutafakari alilokusudia, haraka alitoa kiberiti kutoka kwa moja ya mifuko iliyokuwa kwenye bukta yake kisha aliwasha nyasi kavu na kilichofuata ni moto mkubwa kuanza kuunguza nyasi na miti iliyokuwa imeachwa kwa kuikinga kambi na pia eneo lile lilitumika kimkakati.

Baada ya kuwasha moto alikimbilia sehemu nyingine na kuwasha pia kisha alitoroka eneo lile na kuelekea upande mwingine wa kambi ambao aliamini utakuwa salama. Alifika eneo alilolikusudia bila kizuizi na alitulia tuli akitizama hekaheka za baadhi ya wanajeshi walivyokuwa wakihangaika kupiga filimbi ili kuwaamsha waliolala. Dakika mbili baadae kambi nzima ilikuwa kwenye hekaheka nzito na ni wakati huo ambao aliuhitaji kuliko wakati mwingine kwenye maisha yake. Haraka bila kujiuliza alivuta wavu uliokuwa umezungishiwa kama uzio wa kuingia kambini, alipata nafasi kidogo ambayo aliitumia kupenya na kuingia ndani ya kambi huku bunduki yake ikiwa mkononi tayari kwa lolote ili kutetea uhai wake.

Pilikapilika za wenyeji wa kambi zilimrahisishia kutoonekana kirahisi, kwa sababu wakati wao wanapigana vikumbo kuchukua silaha na wengine kuchukua vifaa vya kuzimia moto kwa dharura, yeye alitumia mwanya huo kupenya kwa kasi kuelekea ilipokuwa jenereta ya umeme ambayo ilikuwa inasambaza umeme kambi nzima. Alipoifikia alitumia nusu dakika kufungua mfuniko wa tanki la mafuta na kutia fumba kadhaa za mchanga, kisha alifunga vizuri na kukimbilia upande wa vyoo vya wanawake vilivyokua kusini mwa kambi.

Alifika vyooni na kuingia moja ya choo na ambacho alikilenga tangu awali. Choo kile hakikuwa choo cha kawaida, kwani hakikuwa kinatumiwa na mtu yeyote na mlangoni kuliandikwa bango kubwa liloonesha choo kile hakitumiki kwa haja yoyote. Pengine wenyeji walijua ni kwa nini, lakini wageni wengi hawakuruhusiwa kabisa kukitumia choo kile. Alipoingia ndani yake alikuta kukiwa na mlango mwingine kwa ndani ambao ulikuwa haujafungwa. Aliusukuma na macho yake yakakutana na sinki la choo ambalo lilionekana kusahaulika kufanyiwa usafi kwa muda mrefu. Hakuwa na shida na sinki lile ambalo alijua liko pale kwa sababu gani. Kwa kutumia nguvu kidogo alifanikiwa kuliondoa sehemu yake na hapo macho yake hayakukutana na tundu la choo bali kulikuwa na mlango mdogo wa mbao. Aliuvuta mlango ule na kukutana na njia ndogo iliyoruhusu mtu kupita.

Hakuwa na muda wa kupoteza, haraka aliingia kwenye njia na kabla hajazama kabisa aliuvuta mlango na kujifungia kisha alianza kushuka ngazi chache ambazo zilimfikisha kwenye njia iliyokuwa imefunikwa kwa giza kubwa. Alitembea huku akihesabu hatua za miguu yake na alipofikisha hatua mia, alisimama. Baada ya kusimama alichukua kurunzi yake yenye ukubwa wa kalamu ya wino na kuiwasha, aliangaza huku na huko hadi alipofanikiwa kuziona ngazi nyingine zilizokuwa umbali wa hatua kumi kutoka pale alipokuwa, alizifuata na kuanza kuzipanda hadi alipofika mwisho na kulikuwa na mlango mwingine mdogo sawa na ule aliongilia. Aliusukuma taratibu hadi ulipofunguka, hakufanya haraka kutoka nje, alitulia kwa sekunde chache akipima utulivu. Aliporidhika na utulivu aliamua kutokeza upande wa juu ambapo alijikuta akitokea kwenye chumba kilichokuwa kimebebwa na utulivu mkubwa. Chumba kile kilikuwa na ukimya mkubwa huku taa yenye mwanga hafifu ikimulika mule ndani. Kitanda chenye ukubwa wa sita kwa sita na godoro lake, viti viwili na meza moja vilikuwa ni miongoni mwa vitu vilivyokuwa ndani ya chumba kile.

Pito Fizo alisimama katikati ya chumba huku shingo yake ikizunguka kila pembe. Ndani ya kile chumba kulikuwa na kabati kubwa na la kisasa; alilitizama kwa umakini mkubwa huku akijaribu kushindana na hisia zake kuhusu kitakachokuwa ndani yake.

Aliamua kuachana nalo na alipiga hatua kuufuata mlango uliokuwa hatua moja kutoka lilipokuwa kabati, kabla hajaufungua alisimama pembeni yake huku mkono wake wa kushoto ukiwa umeshika kitasa cha mlango na mkono mwingine ukiwa umeishika vena bunduki yake. Alifumba macho na kuvuta pumzi kisha alitulia tuli akijaribu kuotea uwepo wa kiunbe hai yeyote nje ya ule mlango. Hakusikia sauti wala mjongeo, akazishusha pumzi zake na kufumbua macho kisha akaivuta mlango kwa kasi huku mwili wake ukichomoka kwa kasi zaidi na kujitupa kwenye nje ya kile chumba alichokuwemo huku bunduki yake ikiwa tayari kumchakaza yeyote ambae angeliingilia majukumu yake.

Hakukuwa na mtu, haraka alinyanyuka na kuangaza kwa umakini pale alipokuwa. Naam, alikuwa ameingia kwenye ofisi ya mkuu wa kamandi ya Chipa kikosi namba ishirini na sita. Ukutani mwa ile ofisi kulikuwa na picha kubwa ya rais wa Angola na kulikuwa na picha ya mkuu wa jeshi la Angola, lakini kulikuwa na picha nyingine ya mwenye ile ofisi. Aliifuata picha ya mkuu wa kambi na kuitizama kwa ukaribu, sura yake ikakaa vema kwenye ubongo wake. Aliachana na picha hiyo, macho yake akayatupia kwenye meza ya kiofisi iliyokuwa mle ofisini na akavutiwa na vitu vichache vilivyokuwa juu yake huku ikioneka mhusika wa ofisi ile, alitoka muda mfupi uliopita. Haraka alipiga hatua na kusogea pale mezani na kabla hajafanya lolote, umeme ulikatika na taa zikazima. Kiza kikatamalaki nje na ndani ya ile kambi. Kwa Pito Fizo haikuwa ajabu kwani alishalitegemea hilo na yeye ndiye chanzo cha umeme kukatika baada ya kuweka mchanga kwenye tanki la mafuta na kwa kufanya vile, mirija ya inayosambaza mafuta ilishindwa kupitisha kiasi cha mchanga kilichofanikiwa kupenya na hiyo ilisababisha jenereta kujizima kwa sababu mafuta hayakuwa yakitembea inavyotakiwa.

Wakati watu wakipambana na giza zito liloikumba kambi pasipo kutarajiwa, Pito alikuwa anawasha kurunzi yake na kuanza kukagua vile alivyoviona juu ya meza. Kulikuwa na simu ndogo na kulikuwa na karatasi tatu ndogo ambazo zilikuwa ni tiketi za ndege. Tiketi mbili zilionesha zilishatumika siku moja nyuma na jina la mtumiaji lilikuwa ni Carlos Guerimales. Tiketi nyingine ya tatu ilikuwa hajatumika na muda wa matumizi ulionesha ni siku iliyofuata mida ya saa tano ahsubuhi na jina la mtumiaji lilimshitua kidogo, alilifahamu vema kabisa.

“Huyu mjinga anatimka. Hii ni hatari kama bado atakuwa anaule mzigo.” Aliwaza huku akitupia macho upande wa pili ambao ulikuwa na nyaraka zilizokuwa zimepangwa vema. Akilini mwake hakuona umuhimu wa kuzitawanya ili kutafuta chochote kitu, hakutaka kujipa tumaini hasi kuhusu kutokuwa makini kwa watu wale waliomfanya afike ndani ya ofisi ile nyeti. Hakutaka kuamini kuwa chochote kinachohusu mkasa ule kitakuwa kinahifadhiwa sehemu nyeupe kama ile, hakutaka kupoteza muda wake.

Aliachana na ile ofisi kwa kuwa lengo la kuingia pale ofisini halikuwa kukagua nyaraka bali aliingia pale ofisini kwa kuwa, mtu waliemhitaji alikuwa akiishi kwenye kile chumba kilichokuwa nyuma ya ofisi na alikuwa akikaa na kuishi hapo kwa muda wote ambao alikuwa anatafutwa na vyombo vya ulinzi na usalama wa nchi ya Tanzania. Alienda pale kuhakikisha kama yule mtu atakuwa bado yupo au atakuwa ameshatoroshwa baada ya kugundulika uwepo wake pale, pia alitaka kujiridhisha na hujuma walizofanyiwa na kwa mazingira yale ilihalalisha hisia zao kuwa, walikuwa wanahujumiwa na mtu aliyekuwa karibu na yule waliekuwa wanamfuata.

Aliondoka ndani ya ofisi ile kupitia njia iliyokuwa imemfikisha pale, lakini baada ya kufika kwenye chumba kilichokuwa kinamhifadhi mbaya wake, aliamua kufanya ukaguzi mdogo lakini lengo lake alikuwa anahitaji kupata mavazi ili kuusitiri mwili wake, hakuhitaji kuendelea kukaa vile hadi mapambazuko. Mkono wake wa kulia uliendelea kuimiliki bunduki huku mkono wa kushoto ukifungua mlango wa kabati. Macho yake makali yakisaidiwa na mwanga wa kurunzi aliyokuwa ameing'ata mdomoni, yaliona vitu viwili kwa wakati mmoja; kulikuwa na nguo chache zilizokuwa zimekunjwa vema na kuhifadhiwa, pia kulikuwa na bunduki aina ya pump action. Shida yake haikuwa ile bunduki, alihitaji mavazi na alianza kuzipangua nguo kuona kama atapata inayomtosha. Haikumchukua muda mrefu kupata tisheti nyeusi na suruali ya jinzi nyeusi pia, aliichukua suruali na kujipima ukubwa wa kiuno chake kwa kuikunja na kuizungusha shingoni mwake ambapo ilitosha vema, alitabasamu huku akiikunjua na kuivaa harakaharaka bila kuhitaji kuvua viatu vyake. Baada ya kuvaa nguo zote ambazo zilimkaa vema mwilini mwake, macho yake yalirejea kwenye rundo lingine la nguo ambazo hakuwa amezifikia. Alizitizama kwa sekunde chache kisha alizipangua mojamoja huku akiwa makini bila kujua alimakinika na kitu gani. Hakupangua nguo nyingi hatimae mikono yake ikakutana na kitu kilichomfanya azipangue nguo zile, kitu ambacho wakati anapangua aliongozwa na hisia tu na si uono wa kile alichokikuta.

Kompyuta mpakato ikiwa imekunjwa na kuhifadhiwa katikati ya rundo la nguo safi na chafu zilizokuwa zimekunjwa na kuwekwa kabatini. Aliishika ile kompyuta huku akisoma jina la kampuni iliyounda kompyuta ile, kisha aliipiga pigo moja na kuivunja. Hakuwa na haja kompyuta nzima, shida yake ilikuwa ni Hard disc ambayo aliichukua na kuiweka kwenye mfuko wa suruali yake.

Wakati akijiandaa kuondoka macho yake yalirudi ilipokuwa bunduki, aliitazama huku roho ya matanio ikimzoga, alitamani kuichukua lakini alisita kufanya hivyo baada ya kuhisi atajiongezea mzigo mwingine usio na manufaa mikononi mwake ukizingatia, bunduki ile haikuonekana kuwa na risasi za kutosha. Aliitazama bunduki iliyokuwa mkononi mwake na wazo fulani likapita kichwani mwake na alihitaji kulifanyia kazi haraka iwezekanavyo. Kama mwizi aliyevamia nyumba ya kutunza sarafu, alianza kukagua kile chumba kama asiye na akili nzuri; alivuta hiki na kile hadi alipofanikiwa kupata alichokuwa anakihitaji ijapokuwa hakikuwa kinakidhi mahitaji yake.

Aliupata mkasi mdogo uliokuwa umehifadhiwa kwenye droo ya kitanda. Alishika ule mkasi na kuibinua bunduki yake ambapo bomba lake lilitazama juu, kisha aliuchukua mkasi na kuingiza kwenye tundu la kutolea risasi na ulipokaa kama alivyohitaji, alianza kupanua ukubwa wa tundu la bunduki hadi upana aliouhitaji, kisha aliondoka ndani ya kile chumba kama alivyokuwa ameingia.

Dakika tatu baadae alikuwa anatokea kwenye vyoo vya wanawake, alitulia kidogo kupima usalama kabla hajatokeza nje na masikio yake yalizisikia hekaheka zilizokuwa zikiendelea huko nje hasa maeneo ilipokuwa jenereta ambapo hapakuwa mbali na vile vyoo.

Kwa hatua fupifupi huku akitanguliza ncha ya kiatu chake ardhini ili asitoe vishindo, alitokeza nje ya vyoo na kukutana na giza kubwa likiwa limeiteka kambi huku upande wa pili akiona moto ukizidi kuteketeza pori na kelele za makamanda zilisikika wakijipa morali ya kuuzima moto ule.

Pito Fizo hakutaka ile kambi ipoe wala makamanda watulize nyoyo zao baada ya kuona hakuna tishio, alipanga kuwavuruga upya na yeye apate mwanya wa kutoroka ndani ya kambi kwa sababu utulivu ungeendelea kuwepo, ilimaanisha kwake ingelikuwa ni ngumu kutoroka kwa sababu, umakini wa walinzi ungelimfanya aonekane kirahisi, lakini kama angetia fujo yoyote huku akitumia giza kama silaha yake ya ulinzi, ingemrahisishia kazi ya kutoroka kwa kuwa kila kamanda angehaha kujua adui alipo na wapo wangapi.

Pale alipokuwa aliona kuendelea kutembea ni kurahisisha kivuli chake kuonekana na yeyote ambae angalikuwa maeneo yale,aliona ni vema atumie mbinu za kimedani kuweza kufika lilipokuwa jenereta, alilala chini kifudifudi kisha alianza kutambaa kwa mwendo uliotwa Low Crow ambapo, alitambaa kwa kuuvuta mguu mmoja huku mikono yake hasa viwiko vikifanya kazi ya kuuvuta mwili mzima na kichwa chake akiwa amekilaza chini na huku mara chache akikiinua na kutazama alipokuwa akielekea. Kufanya vile ilikuwa inamrahisishia kuonekana kama kifusi kinachotembea kwenye nyasi fupi zilizokuwa zimekatwa kwa urefu sawa na ingelimfanya adui yeyote kuingiwa na udadisi wa kujua ni kitu gani badala ya kushambulia na hiyo ingemrahishia kujitetea kama angelionekana.

Komando Pito Fizo alitambaa kwa mita chache kisha aliinua kichwa na kutizama mbele yake ambapo alizidi kukaribia ilipokuwa jenera na mafundi waliokuwa wanajitahidi kuirudisha kwenye ubora wake. Baada ya kushusha kichwa chini hakuendelea kutumia low crow tena, aliona ni kama anachelewa kuwafikiwa wale jamaa ambapo aliamua kutumia mtindo wa High Crow ambapo aliiweka bunduki juu ya mgongo wa mkono wake, kisha alitumia viwiko vyake kusogea mbele huku miguu yake akiwa ameitanua na ikipishana kufuata viwiko vya mikono yake, aliamua kuongeza kasi ya kutambaa chini huku kichwa akiwa amekiinua na macho yakitazama mbele hatua mia moja. Kama ungelifanikiwa kumuona ungelivutiwa na aina ya mwendo wake lakini bahati mbaya wakati huo hakuwa anampango wa kumfurahisha yeyote, bali alikuwa yupo kwenye majukumu mazito ya kuiuza roho yake akijaribu kuliokoa taifa lake.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom