Riwaya: Mvamizi

Kudo

JF-Expert Member
Nov 2, 2017
1,809
6,081
RIWAYA: MVAMIZI
NA; BAHATI K MWAMBA.
SIMU: 0758573660/0656741439.
1:
CHIPIPA, ANGOLA…

Pembezoni kidogo mwa mji mdogo wa Chipa ulioko ndani ya mkoa wa Chipipa nchini Angola, kulikuwa na tukio lililokuwa linaendelea katikati ya giza nene. Tukio ambalo lilikuwa linafanywa kwa siri na umakini mkubwa ndani ya msitu mnene uliozunguka mji ule mdogo, ambao ulitumika kama kituo kikubwa cha uuzaji Almasi kutoka kwenye migodi iliyoko kilomita chache.

Helkopita isiyo na sauti aina ya Chinook H-47K ilikuwa imeganda angani mita mia tatu kutoka usawa bahari. Kwenye mlango mmoja kulikuwa na kamba mbili nene zikining'inia. Sekunde chache baadae kamba zile zilianza kutambaliwa na viumbe ambao walitoka ndani ya helkopita. Viumbe wale walishuka kwa kasi na kwa umakini mkubwa huku silaha zikiwa mikononi mwao, tayari kwa lolote. Viumbe wanane wenye miguu miwili walishuka chini na kwa kutumia kamba na walipofika chini walitikisa kamba mara mbili na helkopita iliondoka huku kamba zikivutwa ndani kwa kasi kubwa.

Baada ya viumbe wenye miguu miwili na mikono miwili kufika chini salama na kuruhusu helkopita iondoke, walikimbia kwa mtindo wa zigizaga kuelekea kwenye kichaka kilichokuwa karibu na pale waliposhukia. Ilipendeza kuwatazama namna walivyokuwa wanakimbia huku silaha zao zikiwa mikononi, kofia vichwani mwao na mabegi yenye uzito wa kilo kumi na tano yakiwa migongoni mwao. Licha ya kuvaa landboot nzito, lakini mikimbio yao haikuwa na vishindo, walikimbia kwa ufasaha na kwa malengo maalumu mithili ya watuhumiwa waendao mahakama ya kijeshi. Ilivutia kuwatizama ijapokuwa wao hawakuwa na lengo la kumvutia yeyote aliyekuwa akiwatizama. Kila mmoja alikuwa na bunduki aina ya M4 carbine 5.56×45mm yenye urefu wa sentimita 36.83 na caliber ya 5.56.

Bunduki zote zilikuwa na telescope stock. Vichwani mwao walivaa kofia za chuma zilizozungushiwa mchipi uliobeba Night gogle ambayo ilikuwa imekaa usawa wa paji la uso wa kila mmoja. Vifuani mwao walivaa tactical vests zenye chest rig, viganja vyao vilifunikwa na glavu za ngozi, huku mikanda yao ikiwa imebana vema viuno vyao na kufunikwa na maga pochi zilizosheheni magazini zenye risasi za kutosha.

Magoti yao yalibanwa vema na protective pads huku mapajani mwao kukiwa na holsters zikiwa zimebana vema bastola zilizoshiba risasi. Kila mmoja sikio lake lilikuwa na wireless earpiece kwa ajili ya kuwasiliana wawapo kwenye jambo lililokuwa limewapeleka maeneo hayo.

Wote wanane walifika kwenye kichaka huku kila mmoja akimlinda mwenzake na hatari yoyote ambayo ingelijitokeza.

“Tuna dakika thelathini za kufanya kilichotuleta huku. Hatutakiwi kuvuka zaidi ya dakika thelathini na mbili. Umakini unahitajika ili tuweze kurejea tukiwa salama.” Mmoja wa makomando aliwambia wenzake huku akijipapasa kwenye mifuko yake na punde alitoa karatasi ndogo, ambayo ilikuwa imechorwa michoro ambayo si rahisi kutafsirika.

Aliitazama karatasi ile kwa nusu dakika kisha aliikunja na, kuirejesha mfukoni huku macho yake yakizunguka kuwatazama wenzake ambao walikuwa wamepiga goti moja chini, mithili ya wafukuza upepo kwenye mbio za mita mia moja. Ni yeye pekee aliyekuwa amesimama.

“Tunahitaji kutumia dakika saba kwa safari ya mwendo haraka kufika kwenye kiota cha miiba. Tutatumia dakika kumi na tano kukipekuwa kiota na kuchukua yai letu na kuondoka.” Aliwambia wenzake huku akibeba vema bunduki yake na kuivaa vema shingoni mwake.

“Kumbukeni kosa moja litatufanya tu…” Alisita kusema huku kwa kitendo cha haraka na wepesi mkubwa, akijirusha chini kwa umakini mkubwa na kutulia huku silaha yake ikiwa tayari kuachia risasi zilizokusudiwa. Kitendo cha yeye kujirusha chini hakukifanya peke yake, wenzake walishakifanya sekunde mbili mbele yake.

Walifanya hivyo baada ya kuhisi kuvunjika kwa kitu mita chache kutoka walipokuwa. Kujirusha kwao kuliambatana na kutambaa chini kwa mtindo maalumu huku wakigawana uelekeo, kulizunguka eneo ambalo walisikia sauti ya mvunjiko.

Sekunde chache zilitosha kulifanya eneo lile liwe chini ya uangalizi mkubwa, huku upekuzi ukifanyika kwa umakini mkubwa kuhakikisha kinafahamika kilichosababisha mlio ule ambao, haukuwa wa bahati mbaya. Masikio yao hayakukubaliana na bahati mbaya, bali ni makusudi kabisa yalifanyika kuitoa ile sauti ya kuvunja kijiti. Umakini wao ulikuwa mkubwa kwa sababu uwepo wao pale ulikuwa ni kwa ajili yao, hawakuwa wametarajia uwepo wa mtu mwingine yeyote.

“Pito!” Komando mmoja aliita na haraka aliyeitwa alisogea pale kwa kasi kubwa.

“Hiki ni nini?” Pito aliulizwa. Hakujibu haraka, badala yake aliinama chini na kuanza kupapasa taratibu na kisha alimtizama aliyemuita.

“Hapa kulikuwa na moto uliozimwa dakika chache zilizopita!” Pito alisema huku akiinuka na kuanza kuangaza kando ya lile eneo.

Makomando wote walisogea pale paliposemekana kuwashwa moto, kila mmoja alijiridhisha kuhusu uwepo wa moto uliozimwa muda mfupi, kabla ya wao kufika pale.

“Change plan!” Komando kiongozi aliwambia wenzake, kisha walibadili uelekeo na kuanza kukimbia kwa kasi ndani ya lile pori lililoshiba miti na nyasi nene. Walikimbia kwa umakini, bunduki mkononi night goggles zikiwa machoni ili kuwawezesha kuona ndani ya giza nene.

Walikimbia umbali wa kilomita moja, kisha Komando kiongozi alinyoosha mkono juu na kuukunja ngumi. Ishara ambayo ilionwa vema na makomando wengine na kilichofuata ni kila mmoja kusimama huku akichukua upande wa kuwalinda wenzake, huku wakimweka Komando kiongozi katikati yao.

Haraka Komando kiongozi alitoa karatasi yenye michoro anayoweza kuitafsri yeye na kuitizama kwa umakini mkubwa. Alipohakikisha ameelewa kilichochorwa kwenye karatasi, alirudisha mfukoni na kuwaambia wenzake..

“Hatupo mbali na kiota cha miiba, ijapokuwa uelekeo huu ni kutokea mbele ya kiota. Kila mmoja anaelewa kipi cha kufanya ili kulifikia yai na kulibeba likiwa salama. Upande wa mbele unachangamoto ambayo tulishaipigia mazoezi, hivyo utekelezaji kwa kuzingatia muda ni….” Alisita kuendeea kuzungumza, haraka alichuchumaa chini na kumtazama jamaa mmoja ambae alikuwa na begi mgongoni likiwa na kifaa maalumu cha kuunganisha mawasiliano baina yao. Si yeye tu aliyemtizama, wengine nao walimtizama na yeye aliinuka haraka na kulitua begi lake. Kisha alitoa kile kifaa alichokuwa amekibeba na kukiweka chini. Alibofya hapa na pale na kuwageukia wenzake.

“Hakuna uingiliano wa mawasiliano. We are safe.” Alisema huku akikifunga.

“Not safe!”Kamanda alikataa huku akimpa ishara Pito.

“Kila mmoja amesikia chafya ikipigwa na hakuna ambae ameipiga miongoni mwetu. It’s a trap!” Alisema huku akihema kwa jaziba. Operesheni ilikuwa mikononi mwake na uhai wa wenzake ulikuwa mikononi mwake. Kusonga mbele wakati kuna mauzauza yameanza kujitokeza, ilikuwa ni kuuza uhai wao kwa bei rahisi. Lakini kurudi nyuma pia ilimaanisha walichoenda kukifanya kitakuwa hakijafanikiwa.

Komando kiongozi alimtizama Pito. Kisha akamshika bega na kumpa ishara kwa kichwa na alipoutoa mkono wake begani, haraka Pito aliondoka pale mithili ya mwizi anavyotoroka katikati ya umati wa watu.

Walibaki makomando saba wakiwa wametulia katikati ya pori nene. Huku kiongozi wao akiwa bado hajapata maamuzi sahihi ya kufanya na alitegemea kupata taarifa sahihi kutoka kwa Pito. Aliobaki nao aliwapa ishara ya kuvua wireless earpiece zilizokuwa masikioni mwao. Kila mmoja aliivua na walibaki kumtazama.

“We are in a killing ground. Kila mmoja awe makini kuhakikisha mwenzake anakuwa salama. Tunabadili uelekeo na kutafuta eneo zuri na salama huku tukingoja ripoti ya Nyoka. Ikiwa ndivyo sivyo, tuna abort mission.” Aliwambia wenzake na kisha alianza kuondoka pale walipokuwa na kuelekea upande mwingine. Kila walichokuwa wanakifanya kilikuwa kinawaweka nje ya muda. Lakini hawakuwa na namna, waliijua thamani yao ndani ya jeshi lao na walijua madhara ya kufanyiwa shambulio la kushitukiza, hasa kutoka kwa adui ambae anajua uwepo wao pale.

Makomando saba walihama eneo huku komando wa mwingine ambae alikamilisha pack ya makomando nane, akiwa yuko msituni akijaribu kunyatia harakati za mtu ambae alikuwa ameingilia mipango yao.

Pito Fizo alikuwa ni komando miongoni mwa makomado wa kutumainiwa. Hakuwa komando tu, alikuwa ni komando mlengaji akiwa amefuzu kwenye shule ya walenga shabaha na kuwa miongoni mwa wanafunzi bora ambao walifaulu kila idara; kuanzia idara ya shabaha, hesabu, mbio na ujifichaji.

Kila mara alikuwa akijumuishwa kwenye pack ya makomando kwa ajili ya misheni nje ya nchi. Ufanisi wake awapo kwenye uwanja wa vita ulimfanya awe miongoni mwa makomando wa kuaminika huku akipewa kipaumbele, upande wa kulenga shabaha. Kuna wakati aliondolewa kwenye orodha ya uwajibikaji kivita na kupelekwa kitengo cha usalama, lakini hakudumu, alikataa na kuomba kurejea kwenye uwanja wa vita.

Aliamini yeye si wa kukimbizana na wahalifu wavivu, ambao walipachikwa majina ya ujasusi; aliamini yeye ameletwa Duniani kupambana na wahalifu wenye silaha nzito katikati ya misitu minene. Alipenda kujificha juu ya miti na kupigwa jua huku akiwa ameshindia matone kadhaa ya maji. Aliona fahari kukimbia katikati ya kiza kinene, huku akiwala vichwa maadui zake na kuwasafishia njia wenzake. Kwake kukaa sehemu moja ndani ya siku mbili akingoja windo, ilikuwa ni kawaida na hakuwahi kujuta kulala juu ya miti au kwenye nyasi akisubiri windo lake likae pahali anapohitaji ili atimize lengo lake.

Maisha ya Pito Fizo yalitawaliwa na hekaheka za msituni kuliko anasa za kidunia. Hakupenda kufanya kazi ya kukaa na kuripoti kambini kila siku. Alipenda kuishugulisha akili yake na mambo ya vita. Kupiga hesabu za kulishinda windo lake, kukimbizana na maadui msituni kwake ilikuwa ni furaha isiyokifani.

Wakati vijana wengine wakishabikia mchezo wa kubeti, yeye alikuwa anabeti maisha yake na maadui. Kila alipokuwa akienda misheni, ndani kwake huacha karatasi yenye pande mbili; upande wake na upande wa adui yake ambapo, hutiki upande wake kama mshindi hivyo akiwa kwenye uwanja wa mapambano, hupigana ili kuokoa mkeka wake na kila arudipo na ushindi huweka rekodi kwenye kitabu chake cha kumbukumbu, kisha huenda kanisani na kusali kwa siku saba mfululizo na kisha huhamia msikitini ambapo, huswali kwa siku saba swala tano. Katika siku zote hizo za kusali na kuswali huambatana na mfungo.

Kwenye maisha yake aliamini kuna Mungu anaemlinda kwenye nyakati zote ngumu anazopita. Lakini alishindwa kujua ni Mungu yupi kwa sababu waisilamu huamini wanae Mungu wa haki na Wakristu nao huamini Mungu wanaemwamini. Pito Fizo aliamua kutumika kote kama shukrani kwa Mungu mmoja anaeabudiwa kwa imani mbili tofauti. Yeye aliamini imani zote ni sawa na zinaabudu Mungu mmoja na hazipaswi kunyosheana vidole. Mara zote alipenda sana kuwaadhibu maadui wanaojificha kwenye mgongo wa dini. Aliamini hao ndiyo wanaoiweka dunia kwenye matatizo kwa kigezo cha udini, huku wakiwa na agenda ya udhalimu nyuma yao.

Alisali na kuswali pia kwa lengo la kumuomba Mungu msamaha, endapo aliua mtu ambae hakuwa dhalimu.
Pito Fizo alipenda vita na aliamini Mungu amemlata Duniani kupigana vita na si kitu kingine. Aliamini uwezo wake wa kulenga shabaha, kupigana na kuwatoroka maadui ni kipaji alichopewa na Mungu. Licha ya kupigana vita, lakini alikuwa ni mtu wa dini haswaa.

Komando Pito Fizo baada ya kuondoka na kuwaacha wenzake, alizunguka eneo walilokuwepo kwa umbali wa mita mia tano kwa pande tatu za Dunia, huku ule upande wa nne akiuacha kwa kuwa wenzake walikuwa upande huo na kama kungelikuwa na tatizo, wangelimtaarifu kupitia vifaa maalumu walivyofunga masikioni mwao. Alizunguka kwa umakini mkubwa lakini hadi anamaliza, hakuwa amefanikiwa kukutana na kitu chochote chenye kutia shaka ijapokuwa, akili yake ilikuwa inaamini kabisa kuna kitu hakikuwa sawa.

Wazo moja likampitia kichwani na haraka aliamua kulifanyia kazi. Aliachana na hizo pande na badala yake aliamua kuelekea upande ambao wenzake waliamua kuutumia kama eneo lao la kimkakati. Aliamua kulikagua eneo hilo na kisha angelirejea kwa wenzake.

Lakini jambo moja ambalo hakujua ni kuwa, eneo alilokuwa anafikiria kuliendea tayari lilikuwa limeshasheheni wenyeji kutisja wa kutisha. Hilo hakujua na wenzake pia hawakujua tayari wameshapokelewa na mwenyeji mwenye macho na mikono ya chupa.

Msitu wa Chipa uligeuzwa duka la roho katikati ya giza nene.
 
Screenshot_20201030-151244.png
 
RIWAYA; MVAMIZI.
NA; BAHATI K MWAMBA.

SIMU; 0656741439.

SEHEMU YA PILI


Komando Pito Fizo baada ya kuondoka na kuwaacha wenzake, alizunguka eneo walilokuwepo kwa umbali wa mita mia tano kwa pande tatu za Dunia, huku ule upande wa nne akiuacha kwa kuwa wenzake walikuwa upande huo na kama kungelikuwa na tatizo, wangelimtaarifu kupitia vifaa maalumu walivyofunga masikioni mwao. Alizunguka kwa umakini mkubwa lakini hadi anamaliza, hakuwa amefanikiwa kukutana na kitu chochote chenye kutia shaka ijapokuwa, akili yake ilikuwa inaamini kabisa kuna kitu hakikuwa sawa.

Wazo moja likampitia kichwani na haraka aliamua kulifanyia kazi. Aliachana na hizo pande na badala yake aliamua kuelekea upande ambao wenzake waliamua kuutumia kama eneo lao la kimkakati. Aliamua kulikagua eneo hilo na kisha angelirejea kwa wenzake.

Lakini jambo moja ambalo hakujua ni kuwa, eneo alilokuwa anafikiria kuliendea tayari lilikuwa limeshasheheni wenyeji wa kutisha. Hilo hakujua na wenzake pia hawakujua tayari wameshapokelewa na mwenyeji mwenye macho na mikono ya chupa.

Msitu wa Chipa uligeuzwa duka la roho katikati ya giza nene.

*****
Akiwa anaendelea kukagua mazingira ya upande ambao wenzake walikuwa wamejificha, pua zake zilinusa harufu ya baruti. Alisimama na kujaribu kunusa kwa utulivu.
Ni kweli pua zake hazikuwa zimemdanganya hata kidogo, kulikuwa na harufu ya baruti na hiyo ilimaanisha kulikuwa silaha iliyotumika muda mfupi uliopita. Kwa uharaka na umakini mkubwa alichumpa na kuangukia kwenye nyasi ndefu na kutulia huku akijaribu kupambana na mwelekeo wa upepo, ili aweze kusikia sauti yoyote na aifuate. Akiwa anangoja kusikia chochote karibu yake, alipata wazo la kuwataarifu wenzake na hapo ndipo alijikuta akishindwa kuamua huku kwa mara ya kwanza, hofu ikamshika akiwa kwenye uwanja wa vita.
Kila alipojaribu kuita upande wa pili kupitia vinasa sauti, aliishia kusikia miluzi ya hitilafu upande wa pili.
“Kuna tatizo!” Alijisemea huku na yeye akivua vinasa sauti na kuviweka mfukoni, havikuwa na umuhimu tena kwake. Kitu kikubwa wakati huo ilikuwa ni kujua upande ambao kulikuwa na mtu ambae aliamini ndiye aliyepiga risasi na kufanya eneo lile kuwe na harufu ya baruti.

Aliangaza vema eneo alilokuwepo, pembeni yake kulikuwa na mti ambao ulikuwa na matawi yaliyosheheni majani ya kutosha. Aliutazama kwa umakini na kisha alianza kujongea taratibu kuufuata. Aliufikia na kuukagua kwa ukaribu zaidi. Aliporidhika na usalama, haraka aliukwea na kwenda kutulia kwenye tawi liloweza kuhimili uzito wake. Aliweka vema bunduki yake huku akitumia lenzi ya bunduki yake kuangaza pande tofauti za eneo lilokuwa mbele yake.

Alitulia zaidi ya dakika tano bila kuona kitu. Kwake hiyo haikuwa sababu ya kumfanya ashindwe kuendelea kuvumilia kukaa juu ya mti. Aliamini uvumilivu wake ungemwezesha kuona kitu au mtu ambae alipiga risasi maeneo yale au la, basi angeliweza kuona nyendo za kitu chochote mazingira yale ikiwemo wenzake ambao hakuwa anajua kimewakuta kitu gani.

Wakati Pito Fizo akiwa anapambana kujua kilichokuwa kinatishia usalama wao, wenzake walikuwa kwenye hekaheka nzito za kuokoa uhai wao.
****
Baada ya Komando kiongozi kumtuma mmoja wa vijana wake, aliamrisha wenzake wahame upande huku wakiwa wamezima mawasilino yao. Walikubaliana kutumia ishara kuwasiliana. Hawakuwa na hofu juu ya mawasiliano na yule aliyetumwa, walimwamini na waliamini wakati wowote wataungana nae kwa kuwa alikuwa ni mbombezi wa kutafuta kilichojificha.

Kila mmoja alichukua upande wake huku umakini ukiwa ni wa hali ya juu. Kila mmoja silaha yake alikuwa ameibana vema kifuani huku kidole kikiwa tayari kwenye tundu la kifyatua risasi. Walikaa umbali mfupi baina yao na eneo dogo walilohisi ni salama, waliliweka chini ya himaya yao.

Kila mara komando kiongozi alikuwa anatizama saa yake, muda ulizidi kuwatupa mkono na tayari walikuwa nje ya muda kwa zaidi ya dakika kumi na tano. Kuwa nje ya muda lilikuwa ni jambo ambalo hawakulidhania na kamwe hawakutarajia kama operesheni ile ingeliingiliwa kirahisi namna ile.

Komando John Ndula ambae alikuwa ni kiongozi wa makomando nane walioko ndani ya misitu ya Chipa, alianza kujikuna kichwa chake kwa tafakari nzito. Alihitaji kufanya jambo ili kuokoa muda na kufanya lililowapeleka huko japokuwa, alihofu kuwapoteza vijana wake kwa kuwa hakujua lengo la adui kuamua kuwachezesha mchezo wa kuwapotezea muda. Alisita kusonga mbele kwa sababu hakujua namna wenyeji walivyojipanga kuwapokea pale ambapo wangeliingia eneo walilokusudia.

“Operesheni imeharibika na kinachofuata ni kurudi nyuma na kuondoka hapa Angola. Ijapokuwa itakuwa ni kosa la kiufundi, lakini thamani ya vijana wangu ni kubwa na bado wanahitajika kuliko sasa.” Aliwaza huku akipiga mluzi kidogo kwa lengo la kumuita aliyekuwa karibu yake. Sekunde chache baadae alisikia mtu akijikohoza kando yake.

“Nadhani turejee kwenye uwanja wa mapokeo. Nahodha anangoja ishara ya chuma ili atufuate.” Komando John Ndula alimwambia komando aliyekuwa amejitokeza baada ya kuitwa.

“Lakini tutakuwa tumeirudisha nyuma operesheni nzima na itachukua muda mrefu tena kumpata huyo jamaa.” Komando aliyeitwa alitoa ushauri wake kwa kiongozi.

“Inaweza kuwa sahihi ulichosema lakini nadhani umeona namna tulivyokaribishwa, hii inamaanisha ujio wetu hapa unafahamika na pengine tuliyemfuata atakuwa ameshahamishwa kabla ya usiku wa leo.”

“Sawa, lakini vipi kuhusu Pito?”

“Yule si mgeni msituni, atatukuta njiani.” John alijibu huku akianza kutembea taratibu kuelekea upande mwingine huku akipiga mluzi hafifu.

“Psiiiih!”
Kimya!
“Psiiiiiih!”
Kimya!
Komando John alisita kusogea mbele, kengele za tahadhari ziligonga hisia zake. Alihisi kuna kitu hakikuwa sawa kwa wenzake. Haraka aligeuka kwa yule komando aliyekuwa nae na macho yao yakagongana. Wote macho yao yalisema lugha moja.
Hatari!
Haraka waliweka sawa silaha zao na kuanza kutambaa chini kwa umakini mkubwa huku masikio yao, yakiwa tayari kupokea sauti yoyote ambayo ingeliashiria hatari dhidi yao.
Hatua chache mbele yao waliona mwili wa mtu ukiwa umelala chini kihasarahasara, uhai ukiwa mbali na mwili wake. Komando John Ndula alinyoosha vidole viwili juu kisha alikunja kidole kimoja na kutikisa mkono mara mbili, kisha alitambaa kwa kasi kuelekea pale ulipokuwa mwili wa mtu.

“Shiiit!” Alijikuta akiropoka huku akihangaika kukusisha vidole shingoni mwa mtu yule ili kujaribu kusikia mapigo ya mishipa ya yule mtu, lakini alikutana ubaridi wa majimaji yaliyokuwa yanachuruzika kutoka shingoni mwa yule mtu. Alipomtizama vema aliishia kuona mchirizi mkubwa ulioenea shingoni mwake huku damu ikitoka taratibu na haikuhitaji elimu ya utabibu kujua mtu yule alichinjwa dakika tano zilizopita.
Chozi la uchungu lilimtoka komando John Ndula baada ya kuona komando wake amekufa kifo cha aibu, kifo cha kuviziwa na kuchinjwa na mtu ambae hakufahamika.

Kwa kile alichokiona hakutaka kuendelea kubaki pale, haraka alitoa kurunzi ndogo na kuiwasha kisha aliirusha mita tatu kutoka walipokuwa. Baada ya kuirusha, alitulia kuona kama lengo lake litatimia ndani ya wakati alioutarajia. Dakika moja baadae komando wake mmoja alitokea huku akiwa anahema kwa nguvu. Haraka na yeye alitokea huku yule aliyekuwa nyuma yake akiendelea kumlinda kwa kila hatua aliyopiga.

“Kuna mtu anatutizama. Bila shaka tumesalia sisi watatu na wengine watatu tuwatafute haraka iwezakanavyo, maana mmoja amepatikana na kisu cha shingo kimembeba shujaa wetu!” John Ndula alisema kwa hisia na kisha walianza msako wa kutafuta makomando wengine ambao hawakujua hali zao. Kwa namna walivyokuwa wamelibeba eneo lile, hawakutegemea kutumia muda mrefu kuwapata.
Msako ulifanyika ndani ya dakika nne na makomando wengine wawili walipatinana, lakini komando mmoja hakuonekana hata baada ya jitihada nyingi kufanyika. Hawakuona silaya yake iliyotelekezwa wala chochote cha kuwaonyesha kuhusu komando huyo. Wakati walipoanza kukata tamaa ya kupatikana kwake, hatimae komando mmoja aliona mburuzo mkubwa kuelekea katikati ya msitu.

“Amejeruhiwa na anaburuzwa..” John aliwambia wenzake.

“Lakini nahisi huu ni mtego!” Komando mwingine alisema huku akijaribu kufuatilia mburuzo ule.

“Lakini hatuwezi kuacha mwili wa mtu huku ugenini. Hata akisalia mmoja kati yetu, ni lazima aturejeshe nyumbani tuzikwe kwa heshima. Huo mtego wake tunatakiwa kuutegeu na kumchukua mwenzetu haraka iwezekanavyo.” Komando John Ndula alisema huku akiziweka pamoja maiti za makondo wengine watatu.

“Move!” Alisema huku akianza kusonga mbele bila kungoja ushauri wa makomando waliokuwa chini yake. Jaziba ilizidi kiwango cha kufikiri hasa alipodhani muuaji amedharau taaluma yao ya ukomando na si ukomando tu, bali makomando waliofuzu hatua zote za vikwazo. Ilikuwa kama dharau kuviziwa na kuchinjwa kirahisi katikati ya giza nene.
Jambo moja ambalo hakujua Komando huyu ni kuwa,moto huzimwa kwa moto na uwepo wao ndani ya misitu ya Chipa ulifahamika kwa wenyeji wa misitu ile. Komando John Ndula alikuwa anaucheza mchezo ambao alishapangiwa namna ya kuucheza afikapo nchini Angola.
 
RIWAYA; MVAMIZI

NA; BAHATI K MWAMBA.

SEHEMU YA TATU..


Kwa kile alichokiona hakutaka kuendelea kubaki pale, haraka alitoa kurunzi ndogo na kuiwasha kisha aliirusha mita tatu kutoka walipokuwa. Baada ya kuirusha, alitulia kuona kama lengo lake litatimia ndani ya wakati alioutarajia. Dakika moja baadae komando wake mmoja alitokea huku akiwa anahema kwa nguvu. Haraka na yeye alitokea huku yule aliyekuwa nyuma yake akiendelea kumlinda kwa kila hatua aliyopiga.

“Kuna mtu anatutizama. Bila shaka tumesalia sisi watatu na wengine watatu tuwatafute haraka iwezakanavyo, maana mmoja amepatikana na kisu cha shingo kimembeba shujaa wetu!” John Ndula alisema kwa hisia na kisha walianza msako wa kutafuta makomando wengine ambao hawakujua hali zao. Kwa namna walivyokuwa wamelibeba eneo lile, hawakutegemea kutumia muda mrefu kuwapata.
Msako ulifanyika ndani ya dakika nne na makomando wengine wawili walipatinana, lakini komando mmoja hakuonekana hata baada ya jitihada nyingi kufanyika. Hawakuona silaya yake iliyotelekezwa wala chochote cha kuwaonyesha kuhusu komando huyo. Wakati walipoanza kukata tamaa ya kupatikana kwake, hatimae komando mmoja aliona mburuzo mkubwa kuelekea katikati ya msitu.

“Amejeruhiwa na anaburuzwa..” John aliwambia wenzake.

“Lakini nahisi huu ni mtego!” Komando mwingine alisema huku akijaribu kufuatilia mburuzo ule.

“Lakini hatuwezi kuacha mwili wa mtu huku ugenini. Hata akisalia mmoja kati yetu, ni lazima aturejeshe nyumbani tuzikwe kwa heshima. Huo mtego wake tunatakiwa kuutegeua na kumchukua mwenzetu haraka iwezekanavyo.” Komando John Ndula alisema huku akiziweka pamoja maiti za makondo wengine watatu.

“Move!” Alisema huku akianza kusonga mbele bila kungoja ushauri wa makomando waliokuwa chini yake. Jaziba ilizidi kiwango cha kufikiri hasa alipodhani muuaji amedharau taaluma yao ya ukomando na si ukomando tu, bali makomando waliofuzu hatua zote za vikwazo. Ilikuwa kama dharau kuviziwa na kuchinjwa kirahisi katikati ya giza nene.
Jambo moja ambalo hakujua Komando huyu ni kuwa,moto huzimwa kwa moto na uwepo wao ndani ya misitu ya Chipa ulifahamika kwa wenyeji wa misitu ile. Komando John Ndula alikuwa anaucheza mchezo ambao alishapangiwa namna ya kuucheza kabla hajaikanyaga ardhi ya Angola.

*****
Mburuzo uliendelea kusogea mbele na makomando walizidi kuufuata huku umakini ukiwa mkubwa, hakuna ambae alitaka kugeuzwa kuwa daraja la kifo. Walitembea umbali wa zaidi ya mita mia tano hadi ambapo macho yao yaliona kile ambacho hawakukitarajia. Mbele yao kulikuwa na mti mkubwa na mrefu, si mti tu bali kulikuwa na kitu cha ziada kwenye ule mti. Kulikuwa na kiumbe kikining'inia kwenye tawi la mti. Kiumbe yule alikuwa ni komando mwenye sare sawa na za Komando Ndula na wenzake.

“Oh my God! Amenyongwa!.” Komando mmoja alijikuta ameropoka bila kutarajia huku tayari risasi moja ikiwa imeshatoka kwenye bunduki yake na kwenda kukata kamba. Mwili wa komando ulishuka kwa kasi na kabla haujafika chini, tayari komando mwingine alikuwa ameshafika chini na kuudaka kwa ustadi mkubwa huku Komando John Ndula na yule aliyepiga risasi, wakiwa wamemzunguka na kumlinda na hatari yoyote.

Hawakutaka kupoteza muda, komando aliyemdaka mwenzake alimweka begani na kuanza kutoka lile eneo kwa mwendo wa nusu kukimbia na nusu kutembea, wenzake wakiwa wamemweka katikati; mmoja mbele na mwingine nyuma nao wakitembea na nusu kukimbia.

Wakiwa wametembea umbali wa mita kadhaa, ghafla nyuma yao risasi zilianza kusikika na kitendo bila kuchelewa walichepuka na kuingia porini kidogo ili kumpoteza uelekea aliyekuwa anawashambulia kutokea nyuma.
Risasi ziliendelea kurindima huku aliyekuwa akiwashambulia akizidi kuwasogelea.

“Engage!!” Komando John Ndula aliwambia wenzake huku nae akianza kushambulia na kwa kauli aliyokuwa ameitoa, ilimaaisha wenzake waanze kushambulia huku wakilindana na kurudi nyuma. Walirusha risasi kufuata uelekeo wa adui aliyekuwa anawashambulia. Mwanzo walidhani ni mmoja lakini kadri dakika zilivyokuwa zinasogea, milio ya bunduki ilizidi kuongezeka huku wao wakianza kuelemewa.

“Tusishambulie!” John aliwambia wenzake huku akienda kumpokea komando mwenzake aliyekuwa ameubeba mwili wa yule aliyekufa. Alimbeba begani kisha alianza kukimbia kwa kasi huku akibadili uelekeo na wenzake nao walimfuata kwa nyuma.

“Watch my six!” Komando Ndula aliwambia wenzake akiwa na maana, waulinde mgongo wake.

Kitendo cha wao kuacha kushambulia kilizidi kuwaweka matatani zaidi, walizidi kushambuliwa kwa kasi zaidi huku adui akizidi kuwasogelea.

“Let’s play this game!” Komando mmoja alisema huku akichomoa bomu la mkono na kuondoa pini ya usalama, kisha alitumia nguvu zake zote kurusha bomu kule washambuliaji walikokuwa. Baada ya kurusha bomu haraka aliokota silaha yake na kuwageukia wenzake..

“Huu mchezo utaaamuliwa kwa pembe tatu!” Alisema huku akimtizama Komando kiongozi.

“OK! Tucheze hii ngoma.” John Ndula alikubaliana na mwenzake kisha alimshusha yule komando mwingine ambae alikuwa hana uhai.

“Sorry my brother!” Alisema huku akimfumba macho kwa kutumia vidole vyake viwili.

“Suma utaelekea magharibi na Cuizaro utaelekea mashariki na mimi nitasonga mbele.” Alisema huku akiwatizama kwa umakini ili kuona kama maelezo yake yanaeleweka.

“Nitasogea bila kushambulia, nitasubiri ishara yenu na tutashambulia kwa pamoja.”

“Copy!” Walijibu na kuondoka kwa kasi huku kila mmoja akielekea upande aliolekezwa na kiongozi wao nae alisonga mbele kwa umakini mkubwa huku kila mara akisimama na kujaribu kubashiri mwendo wa adui yao.

Baada ya kurusha bomu ukimya ulikuwa umechukua hatamu, lakini ukimya huo haukuwafanya makomando washindwe kulizingira eneo ambalo mashambalulizi yalitoka. Hesabu zao zilikuwa sahihi kwani wakati wao walipokuwa wanazidi kusogea na kuliweka kati eneo lile, ni wakati huohuo ambao maadaui nao walikuwa wamejikusanya wakijaribu kupanga namna ya kuwashambulia mahasimu wao kwa weleledi zaidi ya mwanzo. Bahati mbaya kwao ni kuwa walitumia muda mrefu kujipanga kuliko wenzao ambao walizidi kuwasogelea kwa ukaribu zaidi.

Wa kwanza kuwaona wakiwa wamejikusanya alikuwa ni Cuizaro ambae alikuwa upande wa mashariki, alitafuta sehemu tulivu na kutulia huku akiendelea kuwasikiliza japo lugha walioitumia haikuwa lugha aliyozoea kuisikia. Waliongea Kireno.

Dakika mbili baadae Suma nae alikuwa amefanikiwa kusogelea kwa ukaribu zaidi huku nae akisikia kile walichokuwa wanakipanga na kwa haraka alijaribu kuwahesabu, walikuwa kumi na mbili kwa idadi yao tena wakiwa wamejizatiti kwa silaha zao nzito.

Suma alikadiria muda aliotumia kuwafikia wale jamaa, alisubiri kwa dakika mbili zaidi ili kuwapa nafasi makomando wenzake waweze kusogea na kushambulia kwa kushitukiza. Dakika mbili zilipotimia alivuta kiondoa usalama kwenye bunduki yake, kisha aliinuka kwa kasi na kuanza kumwaga risasi kuelekea kwa wale jamaa ambao nao walianza kushambulia, lakini kwao ilikuwa kazi bure kwa sababu nyuma yao alikuwepo Cui ambae alianza kushambulia kwa shabaha kubwa huku kila risasi yake ikiondoka na kichwa cha mtu. Wale jamaa hawakuwa wametegemea shambulizi dhidi yao hivyo wengine walikimbilia upande wa mbele yao ambako risasi hazikuwapo lakini walijidanganya, mbele yao walikutana na mtu mwenye roho ya kunguni, roho ya ukatili mkubwa. Walikutana na Komando John Ndula ambae hakutaka kuchelewesha, aliwatandika risasi bila kujiuliza.

Dakika mbili zilitosha kulifanya eneo lile liwe chini ya umiliki wa makomando watatu, ambao walianza kulikagua eneo lile kuona kama kuna yeyote kati ya wale jamaa atakuwa bado anapumua, pia walikuwa wanatafuta vifaa vya mawasiliano vya wale jamaa, ambao walikuwa wamevaa gwanda maalumu za operesheni za jangwani.

“Kamanda! Ona hii.” Cui aliwambia John huku akimpa kipande cha karatasi alichokitoa kwenye mifuko ya mmoja wa wale adui zao ambao walikuwa wamesanbaratika chini bila uhai.
Komando John alikipokea kikaratasi kile na kuanza kukiangalia kwa umakini mkubwa, kisha aliwageukia vijana wake..

“Hii ni ramani kama tuliokuwa nayo sisi. Yaani michoro yake inafanana kila kitu na hii nilionayo. Inaonesha kila njia ambayo tungeliitumia kupita na kwenda kule tulikokuwa tumekusudia, lakini pia inaonesha hadi eneo letu la msaada.”

“Kwa hiyo hawa jamaa walijua ujio wetu, walijua kila kitu kuhusu operesheni hii?”

“Hilo si la kuuliza, nadhani wote mmeona tulivyochezeshwa mchezo wa kitoto hadi kupelekea kupoteza wenzetu wanne na mmoja tukiwa hatuelewi alipo.”

“Lakini wote tujiulize, wamewezaje kuupata mchoro wa operesheni kirahisi na kwa haraka kiasi hicho?” Suma aliuliza swali ambalo lilikuwa linagonga vichwa vyao.

“Basi kuna tatizo huko jikoni tulikotoka. Mamluki wamejaa tele na ndiyo wanaochochea kuni.” Cuizaro aliendeleza hoja yake yenye wasiwasi.

“Tupambanie pumzi yetu kwanza. Tukifanikiwa kuchomoka humu salama, tutajua cha kufanya tukifika nyumbani.”

“Sasa tutafanya nini ikiwa eneo letu la msaada wanalifahamu?”

“Hatuna namna ni lazima tutokee eneo la msaada. Kikubwa tusiache wenzetu huku. Miili yote tutaondoka nayo.”

“Lakini tunamsahau sana Pito Fizo na hatuelewi alipo, Je, tutamuacha?” Suma aliuliza.

“Kwa hali ilivyo siyo rahisi kumtafuta, kikubwa tuliowengi tupo pamoja, atatusamehe kwa hili.” John alimjibu huku akianza kupiga hatua kuelekea walikokuwa wameuacha mwili wa komando mwenzao.

“Twende tuipitie ile miili na tupotee kwenye hili pori la Chipa” Aliendelea kutoa maagizo ambayo yalieleweka vema kwa wenzake.

Safari ya kuukacha msitu wa Chipa ilianza huku wakiwa hawajui Pito Fizo alipo na kama yupo hai ama tayari na yeye atakuwa ameingia kwenye mikono isiyo salama.

Komando John Ndula alikuwa na sababu zake za kutaka kuwahi kutoka ndani ya msitu wa Chipa. Pia alikuwa anamwamini sana komando Pito Fizo na aliamini huko aliko yuko salama na alichokifanya ni kuacha ujumbe kwa siri bila wenzake kuona. Aliacha ujumbe wa mchoro aliouchora kiwiziwizi bila wenzake kuelewa na mchoro ule aliuacha pale walipowashambulia wale wenyeji wasio wema. Ijapokuwa alikuwa anajaribu kubeti hisia zake lakini hisia za ushindi zilikuwa juu kuliko hisia za kushindwa.
John aliacha ujumbe mzito huku yeye nae akiwaza kutenda jambo zito zaidi ili kuhakikisha kundi lake linasafishika, kwa sababu kushindwa kwao kurudi na walichoagizwa huku wakirejea na miili ya wenzao isiyo na uhai, ilikuwa ni aibu kubwa na jina lake kuchafuka kwa kushindwa kuongoza vema operesheni. Si hivyo tu, pia vifo vya wenzake vilimuumiza na aliamini tatizo lilianzia walikotoka na ni lazima ajue waliofanikisha kufeli kwao wakiwa ugenini.

Lakini ataweza kupambana na mzizi wa uliojichimbia? Hakujua!.
.
.
.
.
.ENDELEA KUWA NAMI.
 
RIWAYA; MVAMIZI

SEHEMU YA NNE



Wa kwanza kuwaona wakiwa wamejikusanya alikuwa ni Cuizaro ambae alikuwa upande wa mashariki, alitafuta sehemu tulivu na kutulia huku akiendelea kuwasikiliza japo lugha walioitumia haikuwa lugha aliyozoea kuisikia. Waliongea Kireno.

Dakika mbili baadae Suma nae alikuwa amefanikiwa kusogelea kwa ukaribu zaidi huku nae akisikia kile walichokuwa wanakipanga na kwa haraka alijaribu kuwahesabu, walikuwa kumi na mbili kwa idadi yao tena wakiwa wamejizatiti kwa silaha zao nzito.

Suma alikadiria muda aliotumia kuwafikia wale jamaa, alisubiri kwa dakika mbili zaidi ili kuwapa nafasi makomando wenzake waweze kusogea na kushambulia kwa kushitukiza. Dakika mbili zilipotimia alivuta kiondoa usalama kwenye bunduki yake, kisha aliinuka kwa kasi na kuanza kumwaga risasi kuelekea kwa wale jamaa ambao nao walianza kushambulia, lakini kwao ilikuwa kazi bure kwa sababu nyuma yao alikuwepo Cui ambae alianza kushambulia kwa shabaha kubwa huku kila risasi yake ikiondoka na kichwa cha mtu. Wale jamaa hawakuwa wametegemea shambulizi dhidi yao hivyo wengine walikimbilia upande wa mbele yao ambako risasi hazikuwapo lakini walijidanganya, mbele yao walikutana na mtu mwenye roho ya kunguni, roho ya ukatili mkubwa. Walikutana na Komando John Ndula ambae hakutaka kuchelewesha, aliwatandika risasi bila kujiuliza.

Dakika mbili zilitosha kulifanya eneo lile liwe chini ya umiliki wa makomando watatu, ambao walianza kulikagua eneo lile kuona kama kuna yeyote kati ya wale jamaa atakuwa bado anapumua, pia walikuwa wanatafuta vifaa vya mawasiliano vya wale jamaa, ambao walikuwa wamevaa gwanda maalumu za operesheni za jangwani.

“Kamanda! Ona hii.” Cui aliwambia John huku akimpa kipande cha karatasi alichokitoa kwenye mifuko ya mmoja wa wale adui zao ambao walikuwa wamesanbaratika chini bila uhai.
Komando John alikipokea kikaratasi kile na kuanza kukiangalia kwa umakini mkubwa, kisha aliwageukia vijana wake..

“Hii ni ramani kama tuliokuwa nayo sisi. Yaani michoro yake inafanana kila kitu na hii nilionayo. Inaonesha kila njia ambayo tungeliitumia kupita na kwenda kule tulikokuwa tumekusudia, lakini pia inaonesha hadi eneo letu la msaada.”

“Kwa hiyo hawa jamaa walijua ujio wetu, walijua kila kitu kuhusu operesheni hii?”

“Hilo si la kuuliza, nadhani wote mmeona tulivyochezeshwa mchezo wa kitoto hadi kupelekea kupoteza wenzetu wanne na mmoja tukiwa hatuelewi alipo.”

“Lakini wote tujiulize, wamewezaje kuupata mchoro wa operesheni kirahisi na kwa haraka kiasi hicho?” Suma aliuliza swali ambalo lilikuwa linagonga vichwa vyao.

“Basi kuna tatizo huko jikoni tulikotoka. Mamluki wamejaa tele na ndiyo wanaochochea kuni.” Cuizaro aliendeleza hoja yake yenye wasiwasi.

“Tupambanie pumzi yetu kwanza. Tukifanikiwa kuchomoka humu salama, tutajua cha kufanya tukifika nyumbani.”

“Sasa tutafanya nini ikiwa eneo letu la msaada wanalifahamu?”

“Hatuna namna ni lazima tutokee eneo la msaada. Kikubwa tusiache wenzetu huku. Miili yote tutaondoka nayo.”

“Lakini tunamsahau sana Pito Fizo na hatuelewi alipo, Je, tutamuacha?” Suma aliuliza.

“Kwa hali ilivyo siyo rahisi kumtafuta, kikubwa tuliowengi tupo pamoja, atatusamehe kwa hili.” John alimjibu huku akianza kupiga hatua kuelekea walikokuwa wameuacha mwili wa komando mwenzao.

“Twende tuipitie ile miili na tupotee kwenye hili pori la Chipa” Aliendelea kutoa maagizo ambayo yalieleweka vema kwa wenzake.

Safari ya kuukacha msitu wa Chipa ilianza huku wakiwa hawajui Pito Fizo alipo na kama yupo hai ama tayari na yeye atakuwa ameingia kwenye mikono isiyo salama.

Komando John Ndula alikuwa na sababu zake za kutaka kuwahi kutoka ndani ya msitu wa Chipa. Pia alikuwa anamwamini sana komando Pito Fizo na aliamini huko aliko yuko salama na alichokifanya ni kuacha ujumbe kwa siri bila wenzake kuona. Aliacha ujumbe wa mchoro aliouchora kiwiziwizi bila wenzake kuelewa na mchoro ule aliuacha pale walipowashambulia wale wenyeji wasio wema. Ijapokuwa alikuwa anajaribu kubeti hisia zake lakini hisia za ushindi zilikuwa juu kuliko hisia za kushindwa.
John aliacha ujumbe mzito huku yeye nae akiwaza kutenda jambo zito zaidi ili kuhakikisha kundi lake linasafishika, kwa sababu kushindwa kwao kurudi na walichoagizwa huku wakirejea na miili ya wenzao isiyo na uhai, ilikuwa ni aibu kubwa na jina lake kuchafuka kwa kushindwa kuongoza vema operesheni. Si hivyo tu, pia vifo vya wenzake vilimuumiza na aliamini tatizo lilianzia walikotoka na ni lazima ajue waliofanikisha kufeli kwao wakiwa ugenini.

Lakini ataweza kupambana na mzizi uliojichimbia? Hakujua!.

*****

Pito Fizo alikuwa ametulia tuli juu ya mti, hakutaka kuwa na papara yoyote ambayo ingemfanya ashindwe kumalizia kile alichokuwa anajaribu kuvizia. Licha ya kuwa katikati ya giza nene lakini kwa msaada wa miwani ya kuonea gizani aliweza kuona kiumbe kikihama kutoka upande mmoja kwenda mwingine kwa utaratibu maalumu. Kiumbe yule alikuwa amebeba silaha ya raifoni sawa na aliyokuwa amebeba yeye. Alimtizama namna alivyokuwa anatembea kwa mwendo tahadhari kubwa, lakini si tahadhari tu, kuna jambo lingine aligundua kuhusu mtu yule aliyekuwa anatembea kwa kuvizia katikati ya giza kubwa. Huyo mtu alikuwa anatembea kwa kufuata hatua za mtu aliyetangulia kupita njia ile. Alitembea kwa kufuata nyayo mithili ya wanakijiji wanaosaka ng'ombe walioibwa kijijini.

“Spotter!” Pito alijisemea taratibu baada ya kugundua mtu yule alikuwa anafuata nyendo zake na aligundua ni spotter kwa sababu kila mara alimuona akisimama na kupepesa na midomo yake, ikimaanisha alikuwa anawasiliana na mtu mwingine ambaye hakuwa mbali na eneo lile.
“Anafuata nyayo zangu!” Alijisemea huku akiharakisha kushuka kwenye mti. Aliona kuendelea kukaa pale ni kuendelea kujiweka kwenye nafasi mbaya zaidi. Alihitaji kufanya jambo kabla ya yule jamaa hajafika kwenye ule mti.

Wakati alipokuwa akishuka kwa utaratibu maaulumu bila kumshitua adui yake, ni wakati huohuo ambao masikio yake yalisikia mlipuko wa bomu umbali wa zaidi ya mita mia tano kwa makadirio.

“Kumekucha!” Alisema huku akidondoka juu ya mgongo wa ardhi na bila kutulia alikimbilia kwenye kichaka kilichokuwa kando ya mti na kisha alianama chini na kukimbia mithili ya kware kuelekea upande ambao alikuwa amemuona yule jamaa. Haikumpa shida kubashiri mienendo ya adui yake kwa sababu adui alitumia nyayo zake kumfuata, hivyo yeye alichoamua kufanya ni kukumbuka namna alivyopiga hatua kuelekea kwenye mti.

Akiwa amelala chini na nyasi kukibeba kimo chake, masikio yake yalisikia vitu viwili kwa wakati mmoja. Kwa makadirio yaleyale ya awali, umbali wa kama kilomita mia tano yalisikia milio ya risasi na kwa harakaharaka aliweza kutafsiri aina mbili za bunduki ambapo; mlio mmoja ulikuwa ni wa aina ya bunduki sawa na ile aliyokuwa ameibeba na mlio mwingine ulikuwa wa bunduki aina ya Uzi12. Mara moja aligundua wenzake watakuwa wapo mapambanoni, lakini sauti nyingine ilikuwa ni sauti ya hatua za mtu ambae hakuwa mbali na pale alipokuwa amejificha. Kwa utulivu kabisa alianza kujiinua taratibu bila papara, huku macho yake akiwa ameyalekeza pale aliposikia vishindo vya mtu akitembea.

Alimuona!

Alimuona jamaa akiwa amevaa vazi la kificho huku akiwa ameshika raifoni mkononi mwake. Kwa ukaribu zaidi aliweza kugundua namna jamaa alivyokuwa akitumia mlalo wa nyasi kama kiashiria cha kumjulisha upitaji wa kiumbe.

“Huyu bwege anaakili nyingi za kufuata nyayo. Lakini walijuaje nimetoka kwenye kundi?” Alijiuliza huku akiongeza umakini na kuiacha silaha yake chini huku akichomoa kisu alichokuwa amekipachika kwenye ala yake iliyokuwa imebanwa vema na mkanda wa kiuno. Taratibu alianza kujiinua huku macho yake yakiwa makini kuzifuata nyendo za adui yake ambae bado alikuwa anajaribu kuotea uelekeo wake.
Adui alikuwa anazidi kusogea kwenye hesabu za Mamba mtu bila kujua na alipokaribia ulipokuwa mti ambao awali Pito alikuwa ameupanda, alisimama na kuanza kuwasiliana na mtu ambae hakuwa anaonekana. Wakati akiendelea kutoa taarifa huku akiwa makini kutazama juu ya mti, alishangaa akirukiwa na kiumbe kizito kilichompeleka chini kwa kasi kubwa. Alipiga kelele za woga kwa kuhisi amevamiwa na Simba ama Chui, lakini fikra zake zilibadilika baada ya kuguswa na kitu cha baridi shingoni mwake huku kile kifaa alichokuwa amekipachika sikioni mwake kikinyofolewa kwa kasi na aliyekinyofoa alikipachika sikioni mwake. Jamaa alitaka kujitetea baada ya kuwa na uhakika kuwa aliyejuu yake ni binadamu kama yeye, ila jitahada zake hazikuzaa matunda zaidi ya kuambulia maumivu baada ya kuchezea makonde mawili yaliyomwacha akihema kama kinda la ndege lilovembewa.

Pito Fizo baada ya kumlainisha kwa makonde mawili yenye uzito wa kilo kadhaa, alirejesha kisu shingoni mwake huku akijaribu kuelewa kile alichokuwa anakisikia kupitia kifaa alichopora kutoka kwenye sikio la mtu aliyekuwa amemdhibiti chini.
Licha ya kutumia dakika na sekunde kadhaa akimsikiliza mtu aliyekuwa anaongea upande wa pili, lakini hakuweza kuelewa kilichokuwa kinazungumzwa, aliambulia kugundua taharuki ya yule aliyekuwa akiongea na bila shaka ni baada ya kusikia kelele kutoka kwa mwenzake.

“Wajinga wanaongea kireno..” Aliongea kwa kuhamaki baada ya kushindwa kuelewa kilichozungumzwa upande wa pili, pia hakujua uelekeo wa huyo aliyekuwa anaita na kuongea kwa hamaki.

“Bahati mbaya sina muda wa kupoteza kukuhoji!” Alisema huku akiingiza kisu chake kikali shingoni mwa mateka wake, alipitisha mara mbili na kuruka pembeni akikwepa damu zilizokuwa zimeanza kuruka kwa kasi.
Hakutaka kuendelea kumtazama marehemu mtarajiwa, bali alihitaji kukabiliana na yule aliyekuwa akipeana maelekezo na mwenzake ambae alikuwa amenyamaza na hakusikika akisema lolote.

Alipiga hatua zake ndefu na kurejea alipokuwa ameitelekeza bunduki yake, aliikota huku kichwa chake kikiwa jambo la kufanya ili amalizane na huyo mtu ambae hakuwa anaonekana. Aliwaza zaidi ya nusu dakika, kisha aliamua kufanya jambo la ajabu kabisa, jambo ambalo mwenye akili timamu hatoweza kulifanya katikati ya msitu mkubwa kama ule na si ukubwa wa msitu pekee, bali ni msitu uliojaa hujuma.

Kutoka pale alipokuwa alipiga risasi tatu bila mpangilio kisha aliamua kutembea eneo lile bila tahadhari yoyote ile, lengo lake alitaka mdunguaji aliyejificha aanze kushambulia. Lakini wakati wote alioamua kuzagaazagaa pale, alikuwa anajifanya kuwasiliana na mtu huku akinyooshea vidole mahali fulani. Lengo lake alitaka mdunguaji ampige risasi ya malengo kwa sababu, mdunguaji atampiga risasi ya kichokozi ili amtoe mafichoni yule aliyekuwa akielekezwa jambo au la basi afuatilie nyendo zake wakati wote ambao atakuwa anatafuta msaada baada ya kujeruhiwa. Kwenye sanaa ya ulengaji kuna kanuni kadhaa huzingatiwa ili kula vichwa vya watu wote ambao watakuwa kwenye mchoro wako wa kifo, hivyo Pito aliamua kuitumia kanuni hiyo kujitoa sadaka yeye akiamini kabisa mdunguaji atakuwa anataka kumuona na aliyekuwa anazungumza nae ili akamilishe kazi yake. Na kweli, yule jamaa aliyekuwa anawasiliana na mwenzake aliweza kuingia kwenye mtego bila kujua baada ya kumuona adui yake akirandaranda huku akitoa maelekezo fulani. Kwa akili yake alihitaji kununua roho za hao wote waliokuwa wanaelekezwa, hivyo alihitaji kumchapa risasi moja yule jamaa aliyekuwa anazunguka zunguka ili wenzake watoke mafichoni na kwenda kumsaidia. Alimenga sawia kwenye mkono wake wa kushoto, kisha akaachia risasi moja iliyoenda kutua sawia kwenye nyama za Pito Fizo na kumpeleka chini kwa kishindo.

Pito Fizo alilitegemea hilo, baada ya kudondoka chini alitambaa kwa kasi na kwenda kujibanza kwenye kichaka huku akijaribu kukabiliana na maumivu ya mkono yaliyoanza kuutafuna mwili wake. Hakutaka kuyapa maumivu nafasi ya kuchezea muda wake, haraka alivunja kijiti kikavu kilichokuwa kando yake na kuking'ata mdomoni kisha alilala chini na kuachanisha miguu yake huku akiiweka vema silaha yake kuelekea kule ilikotoka risasi iliyopekenyua mkono wake. Haikuwa kazi ngumu kukadiria umbali wa risasi iliyompata kwa kukadiria kani iliyomsukuma hadi chini, huku uelekeo ukiwa sawia kichwani mwake. Aliachia risasi nne kwa mzingo wa msitatiri yaani; alipiga risasi mbili usawa wa masikio mawili ya aliyemkusudia, kisha alipiga usawa chini kwa kufuata kipimo kilekile alichokitumia wakati alipokuwa akichagua pande za kupiga juu. Kulala kwake akiwa ameachanisha miguu huku kichwa akiwa amekilaza juu ya mgongo wa bunduki yake, kulimsaidia kukadiria hesabu za kile alichokikusudia.

Lengo la kupiga risasi nne kwa mtindo maalumu, alikusudia kumchanganya mdunguaji aliyekuwa amejificha na alikusudia kumkosa ili mlengaji akurupuke alipokuwa amejificha au ajibu kwa kurusha risasi.

Mdunguaji aliyekuwa amejificha umbali wa mita sabini kutoka alipokuwa Pito, alichanganywa na risasi nne zilizomkosa kwa sentimita chache kichwani huku nyingine mbili zikipekenyua tawi la mti alilokuwa amelala juu yake. Haraka bila kufikiria, aliachia risasi mbili mfululizo huku akiinua raifoni yake na kukimbilia chini ya mti, kisha alikimbia zigizaga kuutafuta mti mwingine ajibanze. Hakujua alikuwa amefanya kosa ambalo hakupata nafasi ya kulijutia na hakugundua kosa lake hadi pale yalipomfika makubwa.

Wakati risasi mbili zinatoka kwenye mdomo wa bunduki, mwanga wa mlipuko ulionwa vema na jicho la Pito na akawa makini kuona tukio linalofuata ambalo halikuchelewa kwani, alimuona yule jamaa namna alivyoshuka kwenye mti kwa kasi na kuelekea kwenye mti mwingine uliokuwa pembeni. Yule jamaa alipojibanza huku akijaribu kupima utulivu wa pale alipokuwa ni wakati huohuo risasi moja ilichomoka kutoka kwenye bunduki ya Pito na kwenda kujaa shingoni, bila hata kuhema alienda chini kwa kilutanguliza magoti chini huku bunduki yake ikiachana na mikono yake.

Pito Fizo hakutaka kushuhudia matokeo ya kazi yake, alinyanyuka na kuanza kukimbia huku akichukua uelekeo ambao alisikia risasi na milipuko ikitokea, kabla hajakutana na sekeseke la wenyeji wa msitu ule ambao walimwibia muda wake. Hakukimbia umbali mrefu, maumivu yalizidi kuutafuna mwili wake. Alisimama na kutafuta pahali salama ambapo angeliweza kujifanyia huduma ya dharura.

Haraka haraka alichana vazi lake upande wa mkono ambao ulipata dhahama kisha alichukua kisu chake kikali na kukimwagia kimiminika ambacho alikitoa kwenye begi lake. Alianza kuongeza ukubwa wa jeraha kwa kujichana mwenyewe hadi aliporidhika na uwazi aliouhitaji. Kwa kutumia vidole vyake alifanikiwa kutoa kipande kidogo cha risasi kilichokuwa kimekwama kwenye nyama zake. Alipohakikisha hakuna masalia yoyote ya risasi, alimwaga kimiminika kingine kwenye jeraha huku aking'ata fizi zake kuyakabili maumivu. Alipohakikisha dawa aliyoimwaga kwenye jeraha imeenea vema, alichukua kipande cha soksi yake aliyoikata na kujifunga vema juu ya jeraha kwa kuzungushia kipande chote.

Dakika chache baadae alikuwa anaweka silaha yake begani huku akichukua kibuyu cha maji na kunywa funda kadhaa, kisha alikirejesha kiunoni na kuanza kukimbia kuelekea zilikosikika risasi muda mfupi uliopita.

Mbio zake zilimfikisha ulipotokea mlipuko wa bomu na risasi. Kwa umakini mkubwa alilikagua eneo lile kwa zaidi ya dakika tano bila kujitikisa, macho yake pekee ndiyo yaliyokuwa yakizunguka huku na huko huku masikio yake yakiwa tayari kupokea sauti yoyote ambayo ingelihatarisha usalama wake.
Alipohakikisha usalama upo, alipiga hatua taratibu huku akivuka miili kadhaa ya wapiganaji ambao walikuwa wamepoteza uhai baada ya kukutana na dhahama ya mlipuko, huku wengine wakiwa wamesabaratika chini kwa miili yao kuraruliwa na risasi. Taratibu aliingiza mkono wake kwenye moja ya mifuko yake na alipoutoa alikuwa ameshika kurunzi nyembamba ambayo huitwa penlight. Aliiwasha na kuanza kulikagua eneo lile hatua kwa hatua akiwa na lengo la kuona kama atakutana na mwili wa komando yeyote ambae walikuwa timu moja. Katika miili yote kumi na mbili hakuweza sura anayoifahamu. Alishusha pumzi kwa ahueni baada ya kuona hakuna majeruhi wala maiti ya yeyote anaemfahamu, aliamini watakuwa salama.

Alizima kurunzi yake na kutaka kutimka lakini alijikuta akisita kufanya hivyo baada ya wazo fulani kupita kichwani mwake, alirejea kuiwasha kurunzi yake kisha alianza kuzikagua zile maiti moja baada ya nyingine. Alikagua kwa umakini akiwa anatarajia kuona baadhi ya vitu kutoka kwa wale jamaa; alihitaji kupata utambulisho wao au alama zozote mwilini mwao ambazo zingeliweza kumpa majibu ya maswali baadhi aliyokuwa anajiuliza.

Waliowengi hakuna alichoambulia lakini mmoja kati yao, soksi za miguu yake zilikuwa zimehifadhi vitu viwili vilivyogeuka kuwa muhimu sana kwa usiku ule. Alikutana na karatasi moja iliyokuwa ina majina mawili na namba nne tu. Alipojaribu kuzisoma namba zile, aligundua ni namba za makazi ya mtu japo hakuwa na uhakika na kile alichokifikiria. Kitu kingine ndicho kilichomshitua zaidi baada ya kukiona na hakujua kilikuwa kwa mtu yule kwa Bahati Mbaya au kilikuwa pale makusudi. Lakini kama ni makusudi, kwa nini kilikuwa kimefichwa miguuni mwa mtu na kilionekana kuhitajika baada ya operesheni ile ya usiku.

Pito Fizo alivitizama vile vitu alivyokuwa ameshika mkononi mwake. Alishika karatasi yenye jina la mtu na namba za makazi na pia alishika force number(namba za utambulisho jeshini) ambazo hubandikwa juu ya mifuko kwenye sare za jeshi kwa kila mwanajeshi. Kilichomshangaza si kuikuta pale bali kilichomshangaza ni kuikuta ikiwa imeambatana na bendera ya Tanzania na kwa mwonekano pekee, ilimpa uhakika namba ile ni ya mwanajeshi wa jeshi la Tanzania.

Alibaki na swali moja kichwani ambalo hakupata majibu yake kirahisi, kwa nini ipo kwa watu wale ikiwa imehifadhiwa kwa kificho namna ile? Ina maana gani kwa watu wale?

Hakupata majibu ya kile alichokuwa anajiuliza na aliona kuendelea kujiuliza katika mazingira hatarishi kama yale, ni kuiuza roho yake kwa bei ya kutupa. Alianza kupiga hatua kuondoka eneo lile akiwa bado ameiwasha kurunzi yake..

Hakupiga hatua nyingi, macho yake yaliona jambo ambalo lilimfanya asimame na kutazama kwa umakini mkubwa huku moyo wake ukiongeza kasi ya mapigo.

Aliogopa akiwa bado hajaelewa vema kile alichokiona, moyo wake ulitiwa ganzi la butwaa…
.
.


IMEANDIKWA NA BAHATI K MWAMBA.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom