Riwaya: Mateka

25phiri12

Senior Member
Jun 19, 2021
120
92
RIWAYA: MATEKA
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890

(KIPANDE CHA KWANZA)

UTANGULIZI
Licha ya baridi kuwa kali kwa sababu ya mvua iliyokuwa ikiendelea kunyesha, lakini bi Nadia Ali Rayan aliendelea kutokwa na jasho huku moyo wake ukimwenda mbio kama mtu aliyekimbia mashindano ya mbio ndefu. Hakuwa tayari kushuhudia mtoto wake akiangukia mikononi mwa vyombo vya usalama au magenge ya kihalifu. Mtoto wake alikuwa akisakwa usiku na mchana na vyombo vya usalama ili ashitakiwe na kuhukumiwa kwa makosa ya jinai aliyokuwa akiyafanya, vile vile alikuwa akisakwa na magenge ya kihalifu ili yamteketeze kwa usaliti na mauaji aliyokuwa akiyafanya dhidi yao. Bi Nadia Ali Rayan alikuwa tayari hata kuua kila atakayemsogelea mwanae kwa lengo la kumkamata au kumdhuru.

Japokuwa mwanae alikuwa mhalifu na alilitambua hilo lakini hakuhalalisha kifo chake. Aliamini mwanae hakuzaliwa kuwa mhalifu bali dunia ndiyo iliyoamua awe hivyo. Aliamini mwanae alikuwa akilipiza kisasi cha maisha ya nyuma aliyoyaona au kusimuliwa kuhusu familia yake. Kumbukumbu za bi Nadia Ali Rayan zilisafiri miaka mingi iliyopita, akakumbuka kifo cha mume wake kilichosababisha atengeneze taswira mpya ya maisha yake, ilikuwa kumbukumbu mbaya sana ambayo kila anapoikumbuka huhisi kumwaga damu za maadui zake. Ni heri mume wake angeugua akamuuguza mpaka akafariki kuliko kilichotokea. Mume wake aliuliwa mchana kweupe. Bi Nadia Ali Rayan aliamini kwa asilimia mia moja kuwa magenge ya wauza madawa ya kulevya yaliyokuwa yakishirikiana na mume wake ndiyo yaliyosababisha kifo hicho. Uchunguzi wa kifo cha mume wake ulifichwa fichwa, ukapakwa mafuta mpaka ushahidi ukakosekana.

Miaka ilisogea, bi Nadiya Ali Rayan akapotezana na familia yake iliyobaki. Hata hivyo mtoto wa bi Nadiya Ali Rayan alikuwa akiishi chini ya kivuli cha mama yake pasipo yeye mwenyewe kujua, alijua alikuwa akipambana na wahalifu waliomuua baba yake kwa nguvu zake mwenyewe, kumbe nguvu za mama yake zilihusika kwa asilimia kubwa kwa kila hatua na tukio alilokuwa akilifanya. Siku hiyo mtoto aliangukia mikononi mwa mama yake baada ya dunia nzima kumuangukia ikihitaji kuondoa maisha yake, na siku hiyo hiyo ndiyo alibaini ukweli kuhusu mama yake mzazi. Ukweli kuwa mama yake alikuwa hai na alikuwa akimiliki genge kubwa la kigaidi lililokuwa likiendelea kufanya kazi za kigaidi nyuma yake pasipo yeye mwenyewe kujua. Bi Nadiya Ali Rayan alimtazama kwa huzuni mwanae aliyekuwa kitandani akiipigania roho yake baada ya kujeruhiwa vibaya kwa kitako cha bastola alichopigwa usiku uliopita. Walikuwa wameshaongea mara chache lakini mara chache hizo hawakufikiana muafaka mzuri kutokana na hali ya mtoto wake. Chozi lilimtoka kisha sauti nyembamba toka moyoni kupitia mdomoni mwake ikasikika

“Kuanzia siku uliyotoweka mikononi mwangu nilikupatia jina la Aqsa, sitaki kukuita jina lako la zamani kwa sababu sio kitu tena mbele yangu. Kwa sasa, Jina Aqsa linafahamika nchi nzima lakini hata wewe ufahamu kama ni jina lako”

Japokuwa mwanae alikuwa hoi kitandani lakini aliisikia vizuri kauli ya mama yake, alifumbua macho na kumtazama mama yake aliyekuwa ametengeneza mifereji ya machozi usoni mwake. Mtoto akalazimisha kutabasamu lakini mbavu zake zikamsaliti, mbavu zilimuuma sana. Tabasamu likaishia njiani. Akafungua mdomo wake na kuongea huku akimtazama mama yake usoni
“Sasa leo hii nimemfahamu Aqsa ni nani? Nilikuwa sijui chochote kuhusu neno Aqsa…sasa nimetambua nastahili kuitwa Aqsa”
Akakohoa kikohozi kikavu kilichosababisha afumbe macho kwa maumivu aliyoyasikia, kisha akaendelea kuongea na mama yake

“Lazima nimalize kazi niliyoianza mama, lazima niwasambaratishe wote watakaojaribu kunizuia…nashukuru kwa jina jipya mama. Sasa naitwa Aqsa, jina toka kwa mama yangu niliyempoteza miaka mingi. Asante mama”

Huzuni iliyokuwa imetawala sura ya bi Nadiya Ali Rayan ilianza kupotea taratibu baada ya kusikia mtoto wake akimuita ‘mama’, ilikuwa imepita miaka mingi pasipo kusikia akiitwa namna hiyo. Vile vile alifurahishwa zaidi na kauli kutoka kwa mtoto wake, kauli iliyojaa ujasiri wa kupambana. Kauli iliyokosa chembe ya hofu japokuwa alikuwa kitandani akiugulia maumivu makali yaliyosababishwa na harakati za mapambano yake. Ndivyo alivyohitaji bi Nadiya Ali Rayan. Mtoto jasiri kwake ndiyo mtoto. Suala la mtoto wake kuongelea jina lake jipya hakulipa nafasi ya kuanza kulijadili. Hakutaka maongezi marefu kuhusu mada hiyo, alichotaka ni mtoto wake kufahamu kuwa jina la Aqsa ni jina lake na siyo vinginevyo.

Lilikuwa jina zuri sana kwa upande wake kwa sababu jina hilo lenye asili ya Kiarabu lilikuwa na maana ya ‘mwenye akili’ au ‘intelligent’ kwa watu wa mataifa ya magharibi. Japokuwa lilikuwa jina lenye maana nzuri lakini jina hilo lilikuwa na sifa mbaya sana katika taifa hilo, lilikuwa ni miongoni mwa majina yaliyokuwa yakitafutwa usiku na mchana kwa lengo la kudhibitiwa na mamlaka zenye dola lakini ilishindikana. Hakuna aliyekuwa na ushahidi wa kumfahamu Aqsa, japokuwa wapelelezi waliendelea kuwatilia mashaka baadhi ya watu. Akili ya mama na mtoto iliamini kuendelea kufanya mauaji kila inapowezekana, wao waliamini mauaji watakayofanya dhidi ya maadui zao yatakuwa faraja kwa wapendwa wao waliouliwa kinyama miaka mingi iliyopita. Walinuka roho ya visasi na waliamini hakuna mtu au idara itayoweza kuwazuia kutimiza azma yao. Waliimba mauaji.

1
RWAMA MWANZO, 2020
David Samson alimtazama mpenzi wake aliyekuwa akihesabu pesa iliyokuwa juu ya meza yao chakavu, meza iliyopoteza rangi yake ya asili kwa kupauka chaka chaka. Mpenzi aliyeishi nae kama mke na mume pasipo vigezo vyovyote, hawakuwa na baraka yoyote toka upande wowote wa asili yao. Mwanamke yule aliipata idadi kamili ya pesa, akamwambia David Samson.

"Imebaki mia saba na hamsini mpenzi"

Kichwa cha David kilikuwa moto kwa mawazo, hakujua afanye nini kwa wakati huo ili apate pesa kwa haraka, pesa atakayotumia katika huduma za kujifungua kwa mpenzi wake huyo, pamoja na huduma za kujikimu katika maisha yao. Mwanamke wake alikuwa na mimba ya miezi tisa, walitegemea kupata mtoto wao wa kwanza siku yoyote. Aliwaza kuomba msaada kwa ndugu na jamaa lakini aliamini hawezi kusaidiwa kwa sababu ameshawachosha kwa uombaji wake wa pesa. Alikuwa akinuka madeni kwa ndugu na marafiki zake. Upande wa mwanamke wake aliyefahamika kwa jina la Winnie Ngocho hakukuwa na namna yoyote wangeyoweza kuitumia ili kuupata msaada wao, kwa sababu upande ule haukuridhia kabisa David Samson kuishi na mtoto wao. Hivyo basi, walimzira mwana wao na kumfukuza moja kwa moja wakimwambia asije kugeuza kichwa nyuma kuwatazama. Walimaanisha kumuondoa kwenye idadi ya wana familia na ukoo kwa ujumla. David Samson aliinamisha kichwa chini kama kobe anayetunga sheria kisha akakiinua, tayari alikuwa ana majibu ya nini alichopaswa kufanya. Alimwambia Winnie Ngocho

"Acha nitoke niende mtaani kutafuta pesa, lazima pesa ipatikane kwa sababu siku yoyote unaweza kupata uchungu wa kujifungua"

Ilikuwa kauli nzuri katika masikio ya mpenzi wake lakini bado ilimpa mashaka na taharuki za kutosha. Ilibidi kuuliza ili apate ufafanuzi zaidi

"Unaenda wapi kutafuta pesa?"

David Samson alishindwa kumjibu mpenzi wake, aliamini akimwambia akiwazacho akilini mwake lazima apate pingamizi kali toka kwake. Aliapa kutomwambia kabisa. Swali la Winnie Ngocho lilikuwa na maana sana kwa sababu David Samson hakuwa na kazi yoyote baada ya kufukuzwa kazi ya ulinzi aliyokuwa akiifanya katika kampuni ya ujenzi iliyokuwa ikiongozwa na kampuni toka nchini China. David Samson aligeuza kichwa akamkazia macho mpenzi wake kisha akamwambia

"Ukimzaa mwanangu utamwita jina langu, endapo akiwa wa kike utamwita jina lako au jina la marehemu mama yangu"

Kauli ya David Samson ilikuwa ngumu kueleweka katika kichwa cha mpenzi wake, ilikuwa kauli tata kuwahi kusikia kutoka kwake. Winnie Ngocho alijiuliza maswali kadhaa wa kadhaa akilini mwake lakini alikosa majibu kamili. Baadhi ya maswali hayo yalikuwa

“Anataka kunitoroka na kuniacha peke yangu? Anataka kujiua? Anawaza nini kichwani kwake?”

Winnie Ngocho alipoinua kichwa chake kwa lengo la kuuliza maswali yake lakini hakubahatika kumuona mpenzi wake, David Samson alikuwa ameshatoka ndani ya nyumba hiyo. Hofu ikampanda Winnie Ngocho, mawazo yakazidi maradufu kichwani kwake. Uchungu wa uzazi ukachukua nafasi. Akaanza kulia kwa uchungu, kilio kile kilifanikiwa kuyafikia masikio ya David Samson aliyekuwa nje akivaa viatu tayari kwa kuondoka. David Samson alirudi ndani haraka akamkuta mpenzi wake akilalamika kwa uchungu. Macho yalimtoka pima David Samson. Alimbeba mpenzi wake mikononi mpaka barabarani, bahati ilikuwa upande wake kwa sababu alifanikiwa kuiona bajaji na kuisimamisha. Haraka kwa sauti ya kitetemeshi alimwambia dereva wa bajaji
"Tupeleke hospitali ya mkoa haraka"
Dereva alipoona hali ya Winnie Ngocho na uharaka aliokuwa nao David Samson aliamini hapo ndipo pa kupatia pesa, aliamini dau lolote atakalosema lazima wakubali. Aliongea

"Utanilipa elfu kumi ndugu yangu"

David Samson hakuwa na muda wa kujibizana na dereva, alimpandisha mpenzi wake kisha naye akapanda. Hata hakuelewa alichoambiwa, akili yake ilikuwa ikiwaza maumivu aliyokuwa akiyapitia mpenzi wake. Safari ilianza kwa mwendo kasi kwa sababu David Samson alikuwa akimshinikiza dereva wa bajaji awahi ili kunusuru maisha ya mpenzi wake pamoja na mtoto aliyekuwa njiani. Walifika hospitali, Winnie Ngocho akachukuliwa na manesi haraka wakampeleka wodi namba moja, wodi maalumu kwa masuala ya uzazi. David Samson alibaki na dereva wa bajaji. Alijisachi mfukoni kama mtu atafutaye pesa lakini hakuwa na kiasi chochote mfukoni. Akakumbuka hata ile shilingi mia saba na hamsini ya akiba imebaki katika nyumba walichopanga, akili ikawaza moto. Akamtazama dereva wa bajaji kisha akamuuliza

“Hivi ulisema shilingi ngapi?"

Dereva hakupendezwa kabisa na swali lile, aliamini kitakachofuata ni usumbufu kwa sababu alishuhudia jinsi David Samson alivyokuwa akihangaika kujisaji mifukoni pasipo kupata chochote. Akamjibu kwa hasira

"Elfu kumi jamaa"

David Samson alishituka kama mtu aliyeona au kusimuliwa kitu cha ajabu au chenye kutisha. Alikataa katakata akimwambia dereva yule kuwa hawezi kumlipa pesa kubwa kiasi kile sehemu ambayo kwa kawaida hulipa elfu mbili mpaka tatu. Mzozo ukaibuka. Kipindi mzozo ukiendelea, mmoja kati ya manesi waliompokea Winnie Ngocho alifika eneo lile na kuwatuliza kwa maneno ya upole. Walipotulia akamuuliza David Samson kwa sauti ya utulivu

"Bila shaka wewe ndiye uliyekuja na yule dada mwenye uchungu aliyevaa gauni lekundu?"

David Samson alijibu kwa haraka kwa sauti ya kuhema juu juu kutokana na majibizano aliyokuwa nayo na dereva wa bajaji

"Ndiyo dada yangu, wala hujakosea"

Sasa ilikuwa zamu ya nesi kuongea lakini alisita kidogo, akamkazia macho David Samson aliyekuwa na hofu pamoja na taharuki ya kutaka kufahamu nini kinachoendelea. Nesi akaongea

"Mwanamke uliyemleta ana njia ndogo ya kujifungua, siyo nzuri kwa mtu anayehitaji kujifungua kwa njia ya kawaida. Daktari na manesi wanajaribu uwezekano wa kumsaidia kujifungua kwa njia ya kawaida lakini lolote laweza kutokea. Ikishindikana kabisa atajifungua kwa upasuaji. Waweza kujiandaa kwa gharama za upasuaji pia japokuwa hatuombei apasuliwe"

Akili ya David Samson ilipaa kabisa akawa kama akiota huku amesimama wima, alishindwa kuongea wala kujibu chochote. Kwa mbali alisikia kelele za dereva wa bajaji, kelele zilizosisitiza kulipwa elfu kumi yake ya nauli. David Samson aliona jinsi maji yalivyozidi unga. Hakuwa na jibu lolote kwa nesi wala kwa dereva wa bajaji. Akili yake ikaikumbuka kauli ya rafiki yake kipenzi, kauli iliyomsisitiza kuwa jasiri ili afanikiwe kimaisha. Sasa aliona ni wakati wa kukubaliana na kauli ile ili aweze kupata pesa na kutatua matatizo yanayomzunguka. Nesi alivyoona ukimya wa David Samson alimpuuza na kuondoka zake eneo lile. Mzozo wa David Samson na dereva wa bajaji ukaanza upya, safari hii dereva alikuwa moto sana tofauti na awali. David Samson ilibidi awe mpole kama mtoto aombaye pesa ya ada kwa mzazi wa kambo. Akamwambia dereva wa bajaji

"Mimi ni mwanaume mwenzako naomba unielewe, sina pesa ya kukulipa ndugu yangu. Nimevurugwa hapa".

Kauli hiyo ilikuwa kama tusi kwenye masikio ya dereva yule. Kelele zikaongezeka maradufu. Watu wakajaa kushuhudia nini kilichokuwa kikiendelea, vile vile hata walinzi wenye kazi ya kudumisha ulinzi na usalama wa hospitali walifika haraka. Walijaribu kuwasikiliza wote, makosa yakaangukia kwa David Samson kwa kutolipa nauli, japokuwa hata dereva wa bajaji alikosolewa vikali kwa bei aliyoitaja. Baadhi ya raia walimtetea David Samson wakiamini atakuwa amevurugwa na hali ya mwanamke wake. Dereva alizidi kuwa mkali akihitaji pesa yake. Kelele zilivyozidi zilikuwa kero, David Samson akaamua kuondoa kero hilo, alikuwa tayari kujidhalilisha ili maneno yaishe. Alimwambia dereva yule kuwa ampe saa, mkanda na viatu alivyovaa ili awe amelipa deni lake. Dereva alikubali haraka sana, aliamini vitu vile vilikuwa na thamani kubwa kuliko pesa anayodai. Lakini kabda David hajavua chochote, ilisikia sauti nyororo ikisema

"Usimdhalilishe mwanaume mwenzako, muache aondoke zake nitamlipia deni lake"

David Samson aligeuka nyuma kumtazama aliyeongea, hakika alikuwa ni mrembo. Alikutanisha macho na mtoto mwenye asili ya Kiarabu akimtazama kwa huruma. Binti yule alitoa noti mbili za shilingi elfu kumi, moja akamkabidhi dereva wa bajaji na nyingine akamkabidhi David Samson kisha akamwambia

"Utafanya nauli ya kurudi kwako"

David Samson alimshukuru sana dada yule aliyekuwa kama malaika aliyetumwa na Mungu aende kumuokoa na aibu ya dunia. Dereva wa bajaji hakuwa na neno la kuongeza, hakumuaga yeyote wala hakuhitaji kumbeba tena David Samson kwa sababu walikuwa wameshatibuana vibaya. David Samson baada ya kumuaga binti yule wa Kiarabu aliondoka ndani ya jengo la hospitali haraka huku akili yake ikiwaza mpango alioambiwa na rafiki yake. Japokuwa alipewa pesa ya nauli lakini aliamua kutembea kwa miguu, aliamini akitumia pesa hiyo kwa wakati huo hatopata pesa nyingine. Mawazo yakarudi kumfikiria mpenzi wake aliyemuacha wodini, akazifikiria gharama alizoambiwa

"Eti gharama za upasuaji"

Aliamini lazima aingie kwenye kazi aliyoikataa awali. Ilikuwa kazi hatari lakini hakujali tena, alihitaji kupata pesa za haraka. Kipindi akipiga hatua kuelekea kwa rafiki yake, akili nyingine ilimkumbusha umuhimu wa kuandaa chakula cha mpenzi wake aliyemuacha wodini. Alibadilisha mawazo ya kwenda kwa rafiki yake. Aliona bora aende kwenye nyumba aliyopanga amuombe mpangaji mwenzake amsaidie kuandaa chakula cha mpenzi wake ili akipeleke hospitali. Ndivyo alivyofanya. Alimpatia Edna ile elfu kumi aliyopewa na dada yule mwenye asili ya Kiarabu. Edna hakuwa na hiyana yoyote, alikubali kuandaa chakula cha Winnie Ngocho. Alienda dukani kisha sokoni akanunua mahitaji ya Winnie Ngocho kisha akaingia jikoni na kuanza kupika. Kipindi upishi ukiendelea, David Samson alihisi akizidi kuchelewa kwenda kwa rafiki yake mwenye kazi za kijasiri. Aliondoka kimya kimya pasipo kumuaga Edna, akatokomea kusiko julikana.

Edna alipomaliza kuandaa chakula hakumuona David Samson, alipojaribu kumpigia simu iliita pale pale alipokuwepo. David Samson aliiacha simu yake makusudi. Edna alimsubiri David Samson pasipo mafanikio, masaa ya kuona wagonjwa yalipokaribia Edna aliamua kubeba chakula mwenyewe na kuelekea hospitali. Kitendo kile kilimuudhi sana Edna na kilimshangaza sana kwa David Samson kuondoka bila kumuaga na kuelekea mahali pasipo julikana wakati anafahamu hali ya mwanamke wake. Edna alifika hospitali na kapu lake la chakula. Mungu siyo Athumani, alikuta Winnie Ngocho amejifungua mtoto wa kike kwa njia ya kawaida. Lakini kitendo cha Edna kupeleka chakula pasipo uwepo wa David Samson kilimpa mashaka sana Winnie Ngocho aliyekuwa amembeba mtoto wake kipenzi mikononi. Alipomuuliza Edna ndiyo alizidi kuchanganyikiwa zaidi na kupatwa na taharuki.

Kipindi akiendelea kupambana na mshangao wake ghafla aliletewa risiti ya malipo ya huduma zote alizokuwa ameshahudumiwa hospitali hapo. Alipoitazama risiti ile kilikuwa kiasi kikubwa cha pesa kulingana na hali waliyokuwa nayo. Alijiuliza, David amepata wapi pesa hiyo haraka hivyo? Kwanini risiti iletwe na nesi? David yupo wapi?
Winnie akamuuliza nesi aliyemkabidhi risiti ile

"David yupo wapi?"

Jibu la nesi lilimuacha Winnie mdomo wazi, nesi alijibu

"Aliyenipa risiti alijitambulisha kwa jina moja la Zimwi, na siyo David. Kijana mwenye rasta fupi, alisema ni mdogo wako mnayefatana"

Jibu la nesi lilimvuruga zaidi Winnie Ngocho, eti mdogo wake wanayefatana wakati yeye ndiye mtoto wa mwisho katika familia yao! Alihisi kuna kitu hakipo sawa. Alimfikiria David Samson, sasa aliamini atakuwa ameenda kufanya kazi aliyomkataza kujihusisha nayo. Aliiona hatari mbele yake.
Zilipita siku mbili tangu Winnie Ngocho aruhusiwe kutoka hospitali. Mtoto wake wa kike aliyempa jina la Lucia, jina la marehemu mama yake na David Samson. Mtoto alikuwa na afya nzuri kabisa. Siku zote hizo hakufanikiwa kumuona David. Hofu na hali ya sitofahamu vilizidi kuchanganya akili ya Winnie Ngocho, alishangaa sana siku zilivyozidi kusonga pasipo kumuona kipenzi chake aliyekuwa akitamani kuwa naye kila dakika. Alijiuliza maswali akajijibu mwenyewe. Alishangazwa na kitendo cha David kushindwa kwenda kumuona mwana wake wa pekee.

Siku zilisogea kama kawaida, maisha ya shida yalikuwa rafiki yake. Siku moja jioni ya saa kumi na mbili Winnie Ngocho alipokea mgeni asiye mfahamu kabisa. Mgeni yule alikuwa akinukia marashi ya bei ghari sana, mgeni alijitambulisha kuwa ametumwa na mama yake ampelekee zawadi ya kujifungua. Winnie Ngocho alishangaa sana kusikia taarifa kutoka kwa mama yake mzazi aliyemkana na kumkataa baada ya kuamua kuishi na David Samson. Mgeni yule alimkabidhi begi dogo Winnie Ngocho alilomuhakikishia kuwa limetoka kwa mama yake kipenzi. Mgeni aliaga na kuondoka zake pasipo kujitambulisha kuwa yeye ni nani haswa. Winnie Ngocho hakujali hilo, yeye alifurahishwa pasi kifani na zawadi kutoka kwa mama yake mzazi. Baada ya kumaliza shughuli zake za nyumbani, Winnie Ngocho alifungua begi lile kwa lengo la kuangalia zawadi kutoka kwa mama yake. Alipata mshangao mkubwa na mapigo ya moyo yakaongezeka maradufu, haikuwa zawadi toka kwa mama yake kama alivyoambiwa awali na mgeni yule bali ilikuwa zawadi kutoka kwa mpenzi wake, David Samson. Begi lilikuwa na picha ya David Samson, kipande kidogo cha karatasi pamoja na noti nyingi za fedha. Alisoma kipande kile cha karatasi kilichokuwa na ujumbe uliosema

"Napambana kwa ajili yako na mwanangu. Chunga sana maisha yenu, uhai wenu ndiyo uhai wangu"

Winnie Ngocho alielewa fika kuwa aliyempa begi hilo atakuwa sehemu moja na mpenzi wake, na aliamini aliamua kumpa pesa zile kwa njia ile kwa sababu aliogopa kuulizwa maswali mengi kuhusu mpenzi wake. Moyo ulimuuma sana na kujilaumu kwanini hakufungua zawadi ile mbele ya mgeni wake. Alitamani asiitumie pesa aliyotumiwa kwa kuamini itakuwa haramu yenye damu za watu lakini alikosa jeuri hiyo, hali ngumu ya maisha aliyokuwa nayo ilimwambia kuwa pesa zile ni halali kabisa. Siku zilisogea kama kawaida, siku mara wiki mbili zikapita pasipo kumuona David Samson. Lakini suala la kupata pesa katika mazingira ya kutatanisha liliendelea kama kawaida. Kuna siku aliamka na kukuta mfuko wenye pesa mlangoni kwake, siku zingine watoto wadogo wa mtaani kwake walimpelekea bahasha ya kaki yenye hela na alipowauliza wamepewa na nani bahasha ile walimjibu hawamjui kabisa, na hawajawahi kumuona mtaani kwao. Vile vile aliendelea kupokea ujumbe tofauti tofauti wenye kumsisitiza kujitunza yeye pamoja na mwanae. Matumaini ya kumuona David Samson yalianza kupotea taratibu.
***
Ulikuwa usiku wa manane, nyota zilikuwa zimelipamba anga kila kona ya dunia. Mji ulikuwa kimya huku raia wengi wakiendelea kuota njozi njema za mafanikio. David Samson alikuwa kazini. Alikuwa amevaa begi dogo la mkanda mmoja, ndani ya begi hilo kulikuwa na madawa ya kulevya aina ya heroine aliyokuwa akiyapeleka katika pwani ya ziwa Kuu, sehemu maarufu kwa jina la forodhani. Sehemu maalumu ambayo wavuvi huegesha vyombo vyao vya majini. Alihakikishiwa kuwa akifika eneo lile atakutana na kijana mweusi mwenye miraba minne, amkabidhi begi hilo kisha aondoke zake. Ndivyo ilivyokuwa. Alifanikiwa kumuona kijana huyo wa miraba minne akamkabidhi begi lile kisha wakaagana. Kijana mwenye mwili wa miraba minne aliwasha boti lake la mwendo kasi kisha safari ya kuelekea nchini Congo ikaanza. David alibaki akijiuliza

"Atawezaje kuingia na mzigo wa madawa nchini Congo?"

Hakika David Samson alikuwa hajakomaa kwenye biashara hiyo. Taratibu akageuka na kuanza kurudi alipotoka. Lakini Mungu hakuwa upande wake, ghafla alishangaa mwanga mkali wa tochi ukimpiga usoni. Alibabaika kwa hofu. Kabda hajachukua hatua yoyote alisikia sauti kali ya kukwaruza ikimshurutisha kusimama na kuweka mikono juu. Kilikuwa kitendo cha haraka sana kilichomchanganya. Alibaki akitetemeka kama mtoto mdogo na alishindwa kutii amri ile kwa sababu hakuelewa kabisa alichoagizwa kufanya. Taswira ya mpenzi wake akiwa na mimba ikamjia kichwani. Moyo ukamuuma sana kuona anaelekea kwenye shimo la hewa. Shimo litakalo mtenga na familia yake. Mwanaume aliyemshurutisha awali akaipaza sauti yake kwa mara ya pili

"Naitwa kapteni Mussa toka jeshi la polisi, upo chini ya ulinzi kwa kujihusisha na biashara haramu ya madawa ya kulevya"

Mwanzo David Samson alimurikwa na tochi moja, lakini muda huo alikuwa akimurikwa na matochi zaidi ya saba kitu kilichomaanisha aliyepaza sauti hakuwa peke yake. Mwanga uliongezeka maradufu machoni, macho ya David Samson yakashindwa kuvumilia kabisa akajikuta akiukinga uso wake kwa mikono ili kupambana na mwanga ule, lakini alihisi kuna miale ya mwanga iliendelea kupenya. Alitamani ageuke nyuma ili atimue mbio lakini alijihakikishia kitendo hicho lazima kimpeleke kuzimu, aliamini lazima apigwe risasi za mgongo kisha kifo kichukue nafasi yake. Akili ilikataa, aliona bora aende gerezani kwa sababu atapata wasaa wa kuonana na mwanae pamoja na mpenzi wake, Winnie Ngocho. Alibaki amesimama wima kama mlingoti wa umeme huku mikono yake ikiendelea kupambana na mwanga uliokuwa ukimshambulia pasipo huruma. Vijana zaidi ya saba waliokuwa na matochi zenye mwanga mkali walimfuata taratibu. Walikuwa wakijihakikishia usalama wao. Walipomfikia hawakuwa na jambo la kuuliza wala kuongea. David Samson alipigwa kitako cha bunduki kichwani, alishindwa kuvumilia maumivu yake, mikono iliyokuwa usoni ikipambana na mwanga ilihamia kichwani mahali aliposhambuliwa. Alipiga kelele zilizomaanisha alikuwa akipitia maumivu makali, kijana mwenye sauti kali ya kukwaruza hakujali kilio cha David Samson, alipaza sauti

"Kaa kimya mpuuzi wewe, unaleta utoto hapa"

Sauti ile ilipenya vizuri katika masikio ya David Samson, alijikuta akikaa kimya pasipo kupenda, kwa mbali alisikika akilia kilio cha kwikwi. David Samson aliinua kichwa chake kisha akawatazama vijana wenye matochi, alijihakikishia walikuwa zaidi ya saba, hakuna hata mmoja aliyekuwa amevaa mavazi ya polisi japokuwa walikuwa na silaha za moto. Vijana wale walikuwa wamevaa mavazi ya kisasa yanayopendwa na vijana wanaoanza kubarehe mpaka vijana wenye miaka thelathini na sita au arobaini. Hakujali muonekano kwa sababu polisi siyo lazima avae jezi zake, kuna baadhi ya kazi humlazimu kuvaa kiraia. David Samson alijaribu kujitetea lakini vijana wale hawakuwa na muda wa kumsikiliza. Walimfunga pingu mikononi kisha akavishwa soksi usoni, soksi iliyomzuia kuona chochote. Alikuwa akiona giza mbele yake. Aliinuliwa kwa nguvu na kuanza kuongozwa njia, hakujuwa walikuwa wakielekea wapi kwa sababu soksi aliyovishwa ilitoa pingamizi la kutosha. Alijutia maamuzi yake ya kujiunga katika kundi haramu linalosambaza na kuuza madawa ya kulevya ndani na nje ya nchi, alikumbuka mara kadhaa alivyokatazwa na mpenzi wake kuhusu kujiingiza kwenye mtandao huo. Aliuona usaliti wake, usaliti uliomponza sasa. Akajisemea moyoni

"Nisamehe Winnie wangu, sikusikiliza kauli yako. Acha dunia inifunze"

Hakika hakusikiliza kauli ya mpenzi wake lakini angefanya nini wakati alikuwa akihitaji pesa za haraka kwa ajili ya kumsaidia mpenzi wake pamoja na mtoto?
Safari ya kibubu bubu ilishia ndani ya gari, David Samson aliingizwa garini kisha akalisikia likiondoka kwa mwendo wa wastani. Hakujuwa ni aina gani ya gari na walikuwa wakielekea kituo gani cha polisi, alichojuwa yeye walikuwa ndani ya gari linaloelekea kituo cha polisi. Alijisemea na kujiapiza ndani ya moyo wake kuwa hatawataja wenzake anaofanya nao kazi, alijihakikishia kuwa hata apigwe namna gani hatofungua mdomo wake kuwataja wenzake. David Samson alihofia usalama wa familia yake, aliamini endapo akiwataja wenzake atakuwa ameihatarisha familia yake. Aliamini lazima waishambulie na kuiteketeza kabisa. Hakutaka kusikia suala la kifo cha mpenzi wake wala mtoto. Aliamini yeye ndiye wa kuwatetea kwa sababu hawakuwa na msaada sehemu nyingine. Hakika alitaka kosa alilolifanya limuhukumu mwenyewe.

ITAENDELEA
MATEKA%20COVER.jpg
 
Iko vizuri nasubiri sehemu ya Pili. Ila matukio yako haraka sana, by the way congrats kwako 👊
 
Nina isubiri sehemu ya pili kwa hamu mno,arosto ya siku zote hizi si mchezo . Cheza kama Pele tuendelee
 
RIWAYA: MATEKA
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890

(KIPANDE CHA PILI)

Jogoo waliendelea kuwika, walipaza sauti zao kwa nguvu hali iliyoonesha walikuwa na hadhi na vigezo vyote vya kuitwa madume ya mbegu. Sauti zile za jogoo zilisikika maradufu katika masikio ya David Samson kwa sababu siku hiyo hakupata wasaa wa kulala hata dakika moja. Siyo kwamba alikosa kitanda cha kulalia, hapana, alikuwa juu ya kitanda na chumba safi zaidi ya alichokuwa akikimiliki chumbani kwake. Usingizi ulimpaa siku hiyo, nafasi ya usingizi ilijazwa na mawazo tele. Usiku kucha alijiuliza maswali pasipo majibu, kila swali lililomjia kichwani lilikosa majibu sahihi. Baadhi ya maswali yaliyomchanganya zaidi yalikuwa

"Hapa ni wapi, mbona siyo polisi? Au walionikamata siyo polisi?"

Kichwa kiliwaka moto kwa mawazo. Alitazama saa yake ya mkononi ikamuonesha kuwa ni saa moja kasoro dakika kumi asubuhi, akajisachi mfukoni kwa lengo la kutoa simu yake yenye chapa ya Samsung lakini hakuiona. Simu hiyo alinunuliwa na kundi lake linalojihusisha na uuzaji wa madawa ya kulevya baada ya kuiacha simu yake nyumbani. Kitendo cha kuikosa simu mfukoni kilimaanisha ilichukuliwa na watekaji kwa lengo la kumzuia kufanya mawasiliano na mtu yeyote. Alijiuliza mara mbili

"Waliichukua saa ngapi? Mbona sijalala kabisa?"

Alikosa majibu ya maswali yake. Aliendelea kujihakikishia kuwa yupo chini ya watu hatari zaidi asiojuwa kama ni polisi au laah! Kipindi akiendelea kupambana na mawazo kichwani, ghafla mlango wa chumba alichomo ukafunguliwa kisha akaingia kijana wa makamo, kijana mwenye umri wa miaka isiyozidi ishirini na saba. Kijana yule alikuwa mtanashati sana mwenye kunukia vizuri, kichwani alikuwa na rasta fupi zilizopendezesha kichwa chake kilichobeba sura nzuri. David Samson alimkazia macho kijana yule aliyekuwa akipita hatua taratibu kama mtu aliyelazimishwa kwenda mahali alipo, alijihakikishia siyo mmoja wa wachache aliofanikiwa kuona sura zao usiku uliopita alipokamatwa. Kijana mtanashati alifika mbele ya David Samson akajitambulisha huku sura yake ikiwa na bashasha ya furaha na uchangamfu uliotukuka

"Naitwa Zimwi, karibu katika maskani hii"

Siyo jina tu bali hata sura ya Zimwi ilikuwa ngeni katika utashi wa David Samson, alibaki kamkodolea macho kama mtu aliyehitaji maelezo zaidi. Zimwi aliyekuwa amekaa kwenye moja ya viti vilivyopatikana ndani ya chumba hicho alielewa hali ya David Samson, lakini hakujali chochote. Aliendelea na ufafanuzi wake

"Mimi ndiye niliyefanya malipo ya huduma alizopatiwa mpenzi wako kipindi alipokuwa hospitali kwenye nshu yake ya kujifungua"

David Samson alipata mwanga wa nani aliyefanya malipo ya huduma alizopewa mpenzi wake kwa sababu awali yeye na watu wake aliokuwa akishirikiana nao kwenye masuala ya madawa ya kulevya walishindwa kuelewa nani aliyelipa. Kijana aliyekuwa akisambaza pesa kwa Winnie Ngocho hakukuta deni lolote la matibabu siku aliyoenda kulipa deni hilo. Hawakuelewa Winnie Ngocho alilipaje, mwisho wa siku waliamini atakuwa alisaidiwa na wapangaji wenzake. Hawakujua nyuma ya pazia kuna mtu alikuwa akifatilia maisha ya David Samson. Zimwi akaendelea kutoa maelezo

"Familia yako ipo salama, wala usiwe na hofu yoyote lakini mbele ya siku za usoni wanaweza kuwa sehemu mbaya zaidi...tumegundua huwa mnampelekea pesa za matumizi kwa njia zenu za kijambazi, hakika wote mtaingia mikononi mwetu tu"

Ujasiri ukamvaa David Samson baada ya kujihakikishia mtu yule siyo polisi bali ni mtekaji, alihitaji kumfahamu zaidi

"Wewe ni nani haswa? Mbona sikuelewi!"

Kijana aliyejitambulisha kwa jina la Zimwi wala hakuonesha dalili yoyote ya kushangazwa na swali ya David Samson, alitegemea kuulizwa swali lile toka awali. Akimtazama David Samson usoni kisha akamjibu kwa sauti ya kujiamini

"Kama nilivyokwambia naitwa Zimwi. Hilo ni jina la kazi zangu, kazi kama hii inayoendelea"

David aliamini atakuwa kwenye mikono ya maadui wa kundi lake analolitumikia, aliamini hivyo kwa sababu mara kadhaa makundi yanayojishuhurisha na masuala ya kuuza na kununua madawa ya kulevya hugeukana yenyewe kipindi cha kufanya biashara. Hali hiyo hutengeneza uadui kati yao, uadui ambao hupelekea vita kali ya kuwindana na kuuwana. Hakika alijiona yupo kwenye mikono ya Zimwi halisi aliyetumwa kuchukua roho yake. Kijana yule mtanashati mwenye rasta kichwani akaendelea kutoa ufafanuzi zaidi

"Jina langu kamili naitwa Alimas Jumbe, nafanya kazi katika kitengo cha siri kinachopambana na kudhibiti uuzaji na usambazaji wa madawa ya kulevya nchini"

Utambulisho huo ulimaanisha David Samson hakuwa kwenye mikono salama japokuwa hakuwa kwenye mikono ya wahalifu aliowafikiria awali. Aliamini kitendo cha yeye kukamatwa na watu wanaojihusisha na shughuli za kupiga vita madawa ya kulevya kilikuwa hakina nafuu yoyote. Utofauti mkubwa aliouona ni kuwa, akiwa chini ya watu hao hawatamuua bali watampeleka mahakamani kisha kifungo kitachukua mkondo wake. Zimwi aliendelea na maelezo yake

"Tulifatilia nyendo zako muda mrefu baada ya kugundua una ujamaa na wauzaji wa madawa ya kulevya, tukatega mitego yetu. Siku, wiki na miezi ikapita pasipo kukutia mtegoni. Upelelezi uliendelea kimya kimya mpaka siku tuliyojihakikishua kuwa u miongoni mwa wasambazaji wa madawa ya kulevya katika taifa hili"

Hofu ilizidi kupanda katika mwili wa David Samson, mwili ukamtetemeka sana, akahisi kama yupo ndotoni lakini ubongo wake ukakataa. Ukamuhakikishia hakuwa ndotoni bali yupo kwenye maisha halisi. Akafikiria maneno aliyoambiwa kuwa alikuwa kwenye rada muda mrefu. Akamkumbuka rafiki yake aliyemshawishi kuingia kwenye biashara hiyo eti kwa lengo la kumsaidia kiuchumi, hapo ndipo akili yake ilipomuhakikishia kuwa atakuwa alionwa akiongozana au kuongea na mtu huyo ambaye ni tishio kwa matukio ya kihalifu ndani ya mipaka ya nchi ya Malosha. Mtu ambaye anatafutwa usiku na mchana ili adhibitiwe pasipo mafanikio. Picha ya mpenzi wake akiwa kwenye hali ya uchungu ikamjia kichwani kisha akakumbuka kauli aliyoambiwa na Zimwi kuwa ndiye aliyemlipia gharama za huduma alizopatiwa hospitali. Swali likajengeka kichwani kwake

"Kwanini alilipa deni hilo?"

Alikosa majibu sahihi. Midomo iliendelea kutetemeka kama mtu aliyekuwa sehemu yenye baridi kali. Akilini kwake hakuona njia yoyote ya kukwepa gereza. Kipindi David Samson akiendelea kupambana na mawazo yake, akashitushwa na kauli ya Zimwi, kauli iliyosema

"Tazama picha ya mtu huyu kisha uniambie yupo wapi na njia gani sahihi ya kumpata"

David Samson aliipokea simu ya Zimwi huku mikono ikimtetemeka, akaitazama ile picha iliyokuwa kwenye simu. Hakika haikuwa sura ngeni hata kidogo, ilikuwa sura aliyoifahamu vizuri, ilikuwa ni sura ya rafiki yake aliyemshawishi kujiunga kwenye mtandao wa biashara ya madawa ya kulevya. David Samson aliinua kichwa chake akamtazama Zimwi aliyekuwa makini akisubiri majibu. Midomo ya David Samson iliendelea kutetemeka, sasa ilitetemeka zaidi ya awali. Hofu ilimjaa moyoni akashindwa kuchukua maamuzi yoyote, akabaki kamtumbulia macho Zimwi huku kichwa chake kikitafakari jibu la kutoa.

Lakini kabda hajatoa jibu lolote, alishuhudia mtu mwingine akiingia ndani ya chumba hicho. Alimkazia macho vizuri ili kujihakikishia kama alikuwa akimfananisha au ndiye yule yule aliyemuona siku zilizopita. Akili yake ilimuhakikishia kuwa ni yule binti mrembo aliyemlipia pesa ya nauli ya bajaji aliyokuwa akidaiwa na dereva yule mkorofi. Binti mwenye asili ya Kiarabu. Macho ya binti yule yalipokutana na macho ya David Samson akaachia tabasamu angavu, siyo kwamba binti yule alifurahi mpaka akaachia tabasamu, hapana, ilikuwa ni njia ya kumlaghai mateka wake. Msichana yule wa Kiarabu aliyekuwa amepambwa kwa tabasamu maridhawa, tabasamu lililosababisha David Samson kuona meno yake mazuri yaliyopangwa na kupangika mahali pake alikuwa amevaa mavazi yenye asili na tamaduni za Kihindi.

Kichwani alikuwa amefunga mtandio mrefu uliofika mpaka mgongoni. Alikuwa binti mwenye asili ya kiarabu Uhindini. Macho ya David Samson yaliendelea kumtazama yule binti mpaka alipofika mbele yake. Msichana yule wa Kiarabu akavuta kiti, akakaa jirani zaidi ya David Samson aliyekuwa juu ya kitanda. Sasa walikuwa ana kwa ana kimtazamo lakini kiakili David Samson alikuwa amesafiri mbali zaidi, hakika hakuwa mahali pale. Alishindwa kuelewa matukio yote yaliyomtokea, alifikiria kauli ya Zimwi kuwa ndiye aliyelipa gharama za matibabu ya mpenzi wake kisha akakumbuka alivyolipiwa pesa ya nauli na msichana aliye mbele yake. Sasa aliamini alikuwa akifatiliwa muda mrefu kama alivyoambiwa na Zimwi, aliamini familia yake itakuwa bado ikifatiliwa ili wafatiliaji wapate wanachokihitaji kwa haraka. Aliiona hatari. Mawazo na maswali vilipishana akilini kwake akashindwa ashike kipi na aache kipi. Hakika alivurugwa. Kipindi akiendelea kuandamwa na mawazo na maswali huku akimtazama binti wa Kiarabu aliyekuwa mbele yake, ghafla akashitushwa na salamu

"David Samson, hujambo?"

Hakushangazwa na kitendo cha msichana yule kufahamu jina lake kamili kwa sababu kwa mujibu wa maneno yao walishamfatilia muda mrefu. Japokuwa alishitushwa na salamu iliyomtoa mawazoni lakini hakuna alichosikia zaidi ya jina lake, alibaki kamtumbulia macho yule binti kama mtu anayeulizia

"Umesemaje?"

Msichana wa Kiarabu hakujali hali ya David Samson, aligeuza kichwa chake akamtazama Zimwi aliyekuwa kimya baada ya yeye kuingia kisha akamwambia

"Unaweza kutupisha tafadhari"

Zimwi hakuwa na neno lolote, aliinuka alipokuwa amekaa kisha akatokomea kusikojulikana. Kitendo kile kilirudisha mawazo ya David Samson mahali pake, sasa aliamini kuna jambo lilikuwa likienda kutokea baada ya kumshuhudia Zimwi akiondoka ndani ya chumba kile. Kwakuwa kichwa cha David Samson kilikuwa mbali kimawazo hivyo basi hata kauli aliyoambiwa Zimwi hakuielewa, sio kwamba hakuisikia, hapana, aliisikia kama kelele ya mwangwi masikio kwake. Akajiuliza

"Anaelekea wapi?"

Alikosa jawabu kamili. Msichana wa Kiarabu akafungua mdomo wake kwa mara nyingine kisha akaongea

"Umeanza lini kujihusisha na biashara ya kuuza na kusambaza madawa ya kulevya?"

Safari hiyo David Samson alielewa alichouliza lakini jawabu la swali lilikuwa gumu kutoka. Siyo kwamba alikosa jawabu la swali hilo, la hasha, bali aliamini huo siyo wakati na mahali sahihi pa yeye kuongelea maswala hayo. Akili yake ilimwambia lazima akajieleze katika ofisi zao na siyo mafichoni namna hiyo. Alijifanya jeuri na kiburi mbele ya binti wa Kiarabu. Binti yule wa Kiarabu akamuuliza David Samson kwa mara ya pili, safari hiyo aliongeza sauti tofauti na awali

"Umeanza lini kujihusisha na biashara ya madawa ya kulevya?"

David Samson aliyejawa na ujasiri wa ajabu, hata yeye hakujua wapi alipopata ujasiri huo. Alijibu kwa sauti ya juu

"Hapa siyo mahala sahihi pa kujieleza, nipelekeni ofisini kwenu nitaongea kila kitu"

Binti wa Kiarabu akauona ujasiri wa David Samson. Sasa aliona kama akichezewa mwili wake na mwanaume asiyempenda pasipo ridhaa yake. Hasira zikapanda kichwani. Urembo wa sura yake ukapotea ghafla baada ya kuruhusu makunyanzi ya hasira. Dimpo zake zikawa ndita. Hakika hakuwa mrembo wa dakika kadhaa zilizopita. Hali ile ilimuogopesha David Samson lakini alijikaza kiume ili aelewe ukweli kamili kuhusu watu wao. Bado akili yake ilikuwa na hofu ya kuwaamini kama ni watu wa kitengo cha siri kinachopambana na wauza madawa ya kulevya. Binti wa Kiarabu akasimama wima, akaanza kupiga hatua moja baada ya nyingine ndani ya chumba kile. Akili yake ilikuwa ikiwaza kitu cha kufanya, kitu kitakachokomoa jeuri ya David Samson. Akili yake ikakosa cha kufanya, sasa hasira zikachukua nafasi, hasira zikapata kitu cha kufanya. Akatafuta jina katika simu yake, alipolipata akapiga. Aliyepigiwa alipokea simu, msichana wa Kiarabu akampa maelekezo mazito

"Naona huyu mpuuzi analeta ubishi wa kujieleza, hatuna haja ya kumbembeleza. Nenda kamkamate mpenzi wake na mwanae uwalete hapa mara moja"

Kauli hiyo ilisikia vizuri katika masikio ya David Samson, aliamini familia yake ipo matatani kwa ajili yake. Alibabaika kama mtoto, akataka kuongea akasita. Akashuka kitandani haraka mpaka aliposimama msichana wa Kiarabu, akapiga magoti huku akisema kwa sauti ya kitetemeshi

"Samahani sana dada yangu, naomba msiiguse familia yangu. Nitaongea kila kitu mnachohitaji kujua kutoka kwangu"

Simu ya binti yule ilikuwa bado ipo sikioni lakini aliisikia vizuri kauli ya David Samson. Akimtazama David Samson aliyekuwa amepiga magoti mbele yake kisha moyo wake ukatabasamu baada ya kuamini anaelekea kushinda vita kama alivyopanga. Akabadilisha kauli yake, lakini bado haikuwa na nafuu kwa David Samson bali iliendelea kumuumiza kama ile kauli ya awali, binti yule alimwambia aliyekuwa akiongea nae kwa njia ya simu

"Amekubali kuwa ataongea kila kitu lakini kwakuwa awali alionesha dharau, jeuri na usumbufu yatupasa tumfunze adabu. Waweza kumuacha mpenzi wake lakini mchukue mtoto wake"

Baada ya kauli hiyo binti wa Kiarabu akakata simu. Sura yake ya awali ikarudi mahala pake, urembo wake ukajihidhirisha kwa mara nyingine. David Samson alimshika miguu huku akimbembeleza kuwa yupo tayari kwa lolote lakini wasiiguse familia yake lakini alikuwa ameshachelewa. Binti wa Kiarabu hakumtazama hata usoni bali sauti yake ilisikika katika masikio ya David Samson

"Baada ya nusu saa nitaingia na mtoto wako ndani ya chumba hiki. Nafikiri ndiyo utaongea vizuri bila kubembelezwa"

Baada ya kauli hiyo alijitoa kwenye mikono ya David Samson kisha akatokomea nje kama Zimwi alivyofanya muda mfupi uliopita. Ukimya ulitawala katika chumba alichokuwa David Samson, ukimya huo haukumaanisha chochote katika akili yake. Kichwani alizisikia kelele, kelele zilizokinzana zenyewe kwa zenyewe, kelele zenye majuto ndani yake. Hakika kelele hizo zilistahili kuitwa mawazo mazito yaliyoelemea kichwa chake. Muda wote macho ya David Samson yalikuwa yakiutazama mlango wa chumba hicho akisubiri kuona ahadi aliyopewa, ahadi ambayo ni adhabu upande wake, ahadi ya kutekwa kwa mtoto wake. Mlango ulikuwa wazi kabisa, pasipo kufungwa. Akili ikamwambia ajaribu kufanya jaribio la kutoroka lakini akili hiyo hiyo ikamsisitiza kuwa watekaji hawakuwa wajinga kuacha mlango wazi namna ile. Aliamini ulikuwa mtego, mtego unaoweza kumuongezea adhabu endapo akakamatwa.
Akaamua kutulia tuli. Akatazama saa yake ya mkononi ikamuonesha nusu saa aliyoambiwa kuwa mtoto wake atakuwa mbele yake ilikuwa imeshapita, ilikuwa imepita saa na dakika kadhaa.

Hakujua nini kilichokuwa kikiendelea na nini hasa hatima ya familia yake. Kipindi akiendelea kupambana na mawazo mazito kichwani alimuona binti wa Kiarabu akiingia akiwa na mtoto mchanga mikononi. Mtoto alikuwa akinyonya maziwa yaliyokuwa kwenye chupa lenye chuchu ya bandia. Macho yalimtoka pima David Samson, aliamini kuwa watu wale hawakutania kuhusu ahadi yao. Akili ya David Samson ikamfikiria mpenzi wake, Winnie Ngocho, hakujuwa atakuwa kwenye hali gani baada ya kunyang'anywa mtoto wake mchanga. Alihisi kuchanganyikiwa. Alitamani kuinuka lakini miguu ilikataa akabaki akimtazama binti wa Kiarabu huku midomo yake ikitetemeka kwa hofu na uwoga. Tabasamu halikuisha kutawala katika sura ya mrembo aliyembeba mtoto wa David Samson, alikuwa akipiga hatua huku akimpapasa mtoto yule kichwani. Mrembo yule alikaa kwenye kiti alichokalia awali kisha pasipo salamu yoyote akamwambia David Samson

"Nafikiri hujawahi kumshika mwanao, leo nimemleta uweze kumshika na yeye ahisi mikono ya baba yake"

Kauli hiyo ilimtoka binti wa Kiarabu huku akimkabidhi David Samson mtoto wake wa pekee. David Samson alimpokea malaika wake kwa mikono miwili. Alimtazama usoni, hakika aliiona sura ya marehemu mama yake. Hakupata muda wa kumtazama sana mwanae kwa sababu alishituliwa kwa swali

"Ulianza lini kujihusisha na kundi linalouza na kusambaza madawa ya kulevya?"

Macho ya David Samson yaliyokuwa akimtazama mtoto wake alirudi kumtazama binti wa Kiarabu aliyekuwa makini akisubiri jibu la swali lake. David Samson hakuwa na pingamizi wala ubishi wowote, aliamini akiweka pingamizi atakuwa amenunua majanga katika familia yake. Alimjibu mrembo wa Kiarabu

"Siku niliyompeleka mpenzi wangu hospitali kujifungua ndiyo siku hiyo hiyo niliyoingia rasmi katika mtandao huo"

Binti wa kiarabu alionesha dalili ya kutoridhishwa na majibu ya David Samson, aliamini kulikuwa na uongo ndani yake kwa sababu alikuwa ameshamuona David Samson na mmoja wa wauza madawa ya kulevya mkubwa miaka kadhaa iliyopita, kitu kilichomaanisha walikuwa na uhusiano wa karibu tangu miaka mingi iliyopita. Binti yule akamkazia macho David Samson kisha akamuuliza

"Unataka kuniaminisha kuwa umemfahamu Aman Collence ndani ya kipindi hiki kifupi kilichopita?"

Sasa David Samson alielewa nini maana ya swali aliloulizwa awali, alielewa binti wa Kiarabu alitaka kusikia kauli gani. David Samson akamjibu

"Aman Collence ni rafiki yangu wa muda mrefu, tulikutana mtaani tukazoeana miaka mingi iliyopita, japokuwa maisha yetu yapo tofauti sana kwenye suala la pesa na kipato"

Binti wa Kiarabu akamchukua mtoto aliyekuwa mikononi mwa David Samson kisha akaendelea kuuliza maswali ili kupata ufafanuzi zaidi

"Ilikuwaje mpaka mkawa marafiki?"

Lilikuwa ni swali gumu kwa David Samson. Alifikiria sababu iliyopelekea akawa na urafiki na Aman Collence hakuiona kabisa kwa sababu kijana yule wa kitajiri hakuwa na marafiki wengi kipindi walipoanza urafiki wao, alikuwa mkimya na mtu wa kujitenga sana. David Samson alijibu kwa sauti ya kutetemeka

"Nilijikuta nipo ndani ya urafiki nae, urafiki nilioshindwa kuelewa chanzo chake halisi. Nafikiri yeye ndiye aliyehitaji urafiki na mimi, yeye ndiye atakuwa na majibu sahihi"

Binti wa Kiarabu alitabasamu, akamtazama mtoto wa David Samson aliyekuwa mikononi mwake akiishambulia chuchu ya bandia, akarudisha macho kwa David Samson kisha akamuuliza

"Unapenda maisha ya mwanao? Kama jawabu ni ndiyo, basi hutakiwi kunificha chochote...sisi siyo wahalifu wala wauaji, tunapambana na wauzaji na wasambazaji wa madawa ya kulevya. Sasa inapotokea adui anakuwa mbishi kutoa ushirikiano lazima tumuoneshe umuhimu wa kutoa ushirikiano, lazima atoe ushirikiano kwa njia yoyote tutayohisi itatusaidia"

Binti wa Kiarabu akatazama saa iliyokuwa katika mkono wake wa kulia kisha akarudisha macho kumtazama David Samson, akamuuliza

"Kama hufahamu sababu ya wewe kuwa na urafiki na Aman Collence inakuwaje unafanya naye kazi ya uuzaji wa madawa ya kulevya ndani na nje ya mipaka ya nchi yetu?"

Lilikuwa swali lepesi kwa David Samson lakini majibu yake yaliendelea kumkandamiza mwenye mbele ya binti wa Kiarabu

"Maisha yangu ni magumu sana, ugumu wa maisha yangu na ushawishi wa Aman Collence ulionihitaji nimsaidie kusambaza biashara ya baba yake ndivyo vilivyosababisha nikaingia ndani ya mkondo huo. Mimi siyo muhusika kabisa lakini Aman aliahidi kunisaidia kimaisha endapo nikimsaidia kazi yake. Sikuwa na pingamizi kwa sababu nina uhitaji mkubwa wa fedha"

Majibu ya David Samson yalizidi kutengeneza maswali katika kichwa cha binti wa Kiarabu, akauliza haraka

"Unamaanisha humfahamu baba yake na Aman? Namaanisha mzee Collence"

David Samson alikubali kwa kichwa akimaanisha hamfahamu kabisa baba yake na Aman Collence, mzee aliyeaminika kuwa ndiye mkuu wa genge la madawa ya kulevya linalosimamiwa na Amani Collence. David Samson alifafanua kwa mdomo kuwa hawajawahi kumuona mzee Collence katika ngome hiyo japokuwa Aman Collence huwasisitiza kuwa mzee huyo asiyeonekana ndiye bosi wao. David Samson alifafanua zaidi kuwa kwa muda mfupi aliokaa katika ngome hiyo ameona ugumu na uimara wake kwa sababu ina ulinzi mkali na endapo mtu asiyehusika akigundulika eneo lile hupigwa risasi au kunyong'wa kikatili. Maneno ya David Samson yalimuingia vizuri binti wa Kiarabu. Aliyaamini kwa asilimia kubwa kwa sababu alikuwa ameshajaribu mara kadhaa kuwatuma vijana wake kuingia ndani ya ngome hiyo kwa lengo la kuichunguza na kupata taarifa kamili kabla hawajachukua uamuzi wa kuivamia lakini hawakurudi kamwe, hali iliyomaanisha waliuliwa kabla hawajakamilisha kazi iliyowapeleka. Hakika ngome ile ilikuwa ngumu kuingia kwa mtu asiyehusika. Binti wa Kiarabu akapata wazo, wazo aliloamini ni sahihi zaidi, akamtazama David Samson usoni kama mtu aliyekuwa akikagua kitu kisha akamwambia

"Unatakiwa kurudi ndani ya ngome ile, urudi kama mpelelezi wangu ili nifahamu kila kitu kabla sijapanga mashambuzi dhidi yao"

Ilikuwa kauli mbaya sasa katika masikio ya David Samson, aliifikiria mara mbili mbili akaona hawezi kuifanya kazi hiyo kwa sababu kazi hiyo ilimaanisha kifo, ilimaanisha kuyaweka maisha yake rehani. Moyo ukasema hapana, lakini alipomtazama mtoto wake aliyekuwa kwenye mikono ya binti wa Kiarabu alijikuta akipata jawabu lililokinzana na matakwa ya moyo wake. Aliamini akikataa kutimiza alichoambiwa anaweza kusababisha maafa ya familia yake, aliona bora yeye afe lakini siyo mwanae na mpenzi wake.

ITAENDELEA
 
Hadithi hiko vyema kabisa,nitaendelea kusubiri mwendelezo kwa siku za usoni.

mambo ni 🔥
 
RIWAYA: MATEKA
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890

(KIPANDE CHA TATU)

Japokuwa giza lilikuwa totoro lakini halikumaanisha chochote katika akili ya David Samson, alitembea peke yake barabarani huku akiwa na tofauti ndogo na chizi, alikuwa akiongea peke yake. Akijiuliza maswali na kujijibu mwenyewe. Akili yake iliwaza namna atakavyofanikisha kazi aliyopewa na kuiwasilisha kwa binti wa Kiarabu aliyempatia namba ya simu na barua pepe yake baada ya kurudishiwa simu yake. Aliona hafiki aendako, akaamua kusimamisha pikipiki kisha akamwambia dereva

"Nipeleke Kabutuka"

David Samson aliamua kwenda kwa mpenzi wake kabla hajaianza rasmi kazi ya kifo, alitaka kumuomba msamaha na kumuelezea kila kitu kilichotokea kisha amuhakikishie kuwa lazima mtoto wao apatikane haraka iwezekanavyo. Pikipiki ilisimama nje ya nyumba aliyopanga. David Samson aliitazama nyumba aliyopanga huku kichwani akitafakari maneno ya kumuelezea mpenzi wake ili amuelewe. Alitazama saa yake ya mkononi ikamuonesha kuwa ilikuwa saa sita na robo usiku. Akijihakikishia mpenzi wake atakuwa ameshalala fofofo, au kama atakuwa macho basi atakuwa kwenye dimbwi zito la mawazo juu ya mtoto wake. David Samson aliingia uwani, palikuwa kimya kabisa. Kila mpangaji alikuwa chumbani kwake akitafuta usingizi au akiwa amelala usingizi mzito. David aligonga dirisha la chumbani kwake huku akisema

"Winnie! Winnie! Nifungulie mlango"

Muda huo Winnie Ngocho alikuwa macho, kichwa chake kikiwaza hatima ya familia yake. Macho yake mazuri yalikuwa yamevimba na mekundu kwa kilio alichopitia siku hiyo. Winnie Ngocho alijihakikishia kuwa sauti aliyoisikia ikimuita ilikuwa ya mpenzi wake. Alibabaika kwa mshangao, hofu ikamtafuna. Akajiuliza

"Siku zote alikuwa wapi?"

Hasira zilimjaa akatamani asiitike wala asiinuke kwenda kufungua mlango lakini moyo ulikataa kabisa, moyo wa Winnie Ngocho ulikuwa umehifadhi hisia za David Samson. Kitendo cha kutomfungulia mlango kingemaanisha kupingana na hisia zake. Winnie Ngocho alijikokota toka kitandani pasipo kuitika kauli ya David Samson, akafungua mlango kisha akarudi kitandani. Hakusubiri mpenzi wake aingie. David Samson aliingia taratibu kisha akamtazama mpenzi wake aliyekuwa kwenye nyuso ya huzuni na hasira, moyo ulimuuma sana kujiona mkosaji mbele yake. David Samson akafunga mlango kisha akavua nguo. Wote walikuwa kimya pasipo neno lolote. David Samson alitamani kuanzisha mazungumzo lakini aliogopa, alihofia hasira za mpenzi wake. Aliingia bafuni kuoga. Chumba chao kilikuwa na choo na bafu ndani. Alipotoka kuoga alimkuta mpenzi wake amekaa kitako tofauti na alivyomuacha, sasa aliamini umefika wakati wa maswali na majibu. Hakika alichokiwaza kilikuwa tofauti na mpenzi wake. Bila hata salamu, Winnie alimwambia David

"Kesho naenda kwenu kumuelezea baba yako juu ya maisha yetu, nikitoka kwenu naenda nyumbani kukaa. Yani una bahati sana leo kunikuta hapa…Japokuwa nilifukuzwa nyumbani kwa ajili yako lakini nitaenda kuwabembeleza, nafikiri watanielewa. Siwezi kukaa na wewe pasipo mwanangu"

Kauli hiyo ilisikika vizuri katika masikio ya David Ngocho, alitamani amwambie mpenzi wake hapana, lakini alijua atazua balaa lingine, bora akubaliane na hali. David Ngocho alimuomba msamaha mpenzi wake, alizunguka zunguka lakini mwisho wa siku ilibidi amwambie ukweli wote, ukweli uliomuumiza sana Winnie Ngocho. Hasira za Winnie Ngocho zikageuka kuwa huzuni na huruma. Akamkumbatia mpenzi wake kisha akamuuliza

"Una uhakika gani waliomchukua mtoto wetu ni kitengo cha siri kinachopambana na wauza madawa ya kulevya?"

Swali hilo lilikuwa gumu sana kwa David Samson kuthibitisha kwa sababu hata yeye alikuwa na mashaka juu ya wale watu. Awali Winnie Ngocho alitamani kumwambia David Samson asiendelee kujishughulisha na makundi hayo ya kigaidi lakini uhitaji wa mtoto wake ulikinzana na mawazo hayo. Winnie Ngocho alianza kumlaumu mpenzi wake kwa kujihusisha kwenye mtando wa biashara haramu aliyomkataza tokea awali. David Samson hakuchoka kuomba msamaha na kusisitiza kuwa hakuwa na namna nyingine ya kupata pesa kwa haraka zaidi ya kuingia kwenye uhalifu ule. Mwisho wa siku walikubaliana jambo moja la kufanya. Walikubaliana kuwa lazima David Samson arudi kwenye ngome ya kifo na afanye kila kitu alichoambiwa na kukiwasilisha kwa binti wa Kiarabu.

Winnie Ngocho alimsisitiza mpenzi wake kuwa makini kwa sababu aliamini akigundulika au mambo yakienda ndivyo sivyo hakuna adhabu nyingine atakayopewa zaidi ya kifo. Walilala usingizi wa mashaka sana kwa sababu hakuna aliyekuwa akifahamu hatima ya familia yao. Ilipofika saa kumi na moja kasoro David Samson alimuaga mpenzi wake, waliagana kwa huzuni sana kwa sababu David Samson alimuhakikishia mpenzi wake kuwa hatapata muda wa kwenda kumtembelea lakini alimuhakikishia kumpigia simu pindi apatapo nafasi. David Samson alimsisitiza mpenzi wake asimpigie wala kumtumia ujumbe kwa sababu akifanya hivyo anaweza leta hali ya sitofahamu, au kutiliwa mashaka.

David Samson alimkabidhi mpenzi wake kiasi kikubwa cha pesa alichopewa na binti wa Kiarabu ili akiache nyumbani, kitachotumika kipindi atakachokuwa bize kutafuta taarifa na mambo mengine katika ngome ya kifo. Winnie Ngocho alizishangaa zile pesa zilivyokuwa nyingi lakini David Samson hakujali chochote. Alitoka ndani ya chumba chao na kuondoka zake. David Samson aliamua kuondoka masaa hayo ili asije kuonwa na majirani zao. Hakutaka watu wafahamu kama alifika nyumbani kwake siku hiyo.
3
Yalikuwa yamepita masaa mawili tangu David Samson apigishwe magoti na kijana aliyekuwa rafiki yake kipenzi, kijana aliyemshawishi kuingia katika biashara haramu ya madawa ya kulevya. Magoti hayo ilikuwa ni sehemu ya adhabu ya kuchelewa kurudisha taarifa ya mzigo aliotumwa kumpelekea kijana mwenye mwili wa miraba minne. David Samson alizidisha chuki dhiki ya Amani Collence, kijana ambaye alikuwa rafiki yake wa muda mrefu. Hakuamini alivyokuwa akishurutishwa kama mtoto, alishindwa kubisha kwa sababu vijana zaidi ya nane mwenye miili iliyojengeka kwa mazoezi walikuwa sehemu ya ulinzi wa Aman Collence. Amani Collence alitembea kushoto mara kulia huku akiendelea kumuangalia David Samson aliyekuwa akitetemeka kwa sababu magoti yalikuwa yameshatengeneza ganzi ya kutosha. Aman Collence aliongea kwa sauti ya juu

"Tunapokuwa kazini hakuna habari ya urafiki, yakupasa kuchapa kazi kama ulivyoagizwa"

David Samson hakuwa na kauli yoyote, aliendelea kupiga magoti kama mtoto mdogo aliyesahau kufanya zoezi la somo la hisabati shuleni. Moyoni alifura hasira haswa lakini hakuwa na jinsi zaidi ya kuvumilia na kufata kauli za Amani Collence. Aliifikiria kauli ya Amani Collence iliyomaanisha hakuna urafiki kwenye masuala ya kazi, hakika aliiona ilikuwa sahihi. Aliikumbuka kazi aliyopewa na binti wa Kiarabu, kazi iliyohusu kulisaliti kundi lake ili apewe mtoto wake akiwa hai na salama. Sasa aliamini hakuna urafiki kazini, alijiapiza moyoni kuwa lazima afanye kazi ya binti wa Kiarabu, lazima amsaliti Amani Collence na kundi lake. Kipindi David Samson akiendelea kupambana na mawazo yake alishitushwa na kauli ya Amani Collence, kauli aliyoshindwa kuilewa awali lakini baada ya maelezo ya kutosha alielewa kila kitu. Kauli hiyo ilisema

“Kuna kundi linatufatilia sana, kundi hilo linataka kuteketeza ngome yangu. Linawafahamu wanachama wetu karibia wote, wewe hawakujui hata kidogo kwa sababu bado mgeni katika biashara hizi. Yakupasa uingie ndani ya kundi hilo ili upate taarifa zao za ndani”

Zilikuwa sentensi chache lakini zilizomchanganya sana David Samson, aliinua kichwa akamtazama Amani Collence aliyekuwa akipiga hatua kwenda mbele kisha nyuma. Amani Collence aliendelea kutoa ufafanuzi wa kauli zake

“Sababu kubwa ya kukushawishi ujiunge kwenye himaya yangu ni suala hili, tangu awali nilikuwa nikitafuta mtu mwenye uwezo mzuri wa kufikiria na kuhoji mambo kama wewe lakini bahati haikuwa kwangu. Mara zote nilimkosa mtu huyo lakini Mungu akajibu maombi yangu, leo hii mtu huyo nimempata. Mtu huyo ni wewe mwenyewe. Naamini juu ya uwezo wako, naamini kipaji chako na ninajua huwezi kuniangusha kabisa katika kazi hii yenye kuhitaji umakini”

David Samson alimkazia macho rafiki yake aliyegeuka kuwa adui, sasa aliamini anapelekwa kuwachunguza magaidi wa upande mwingine, aliona jinsi atakavyoshindwa kutekeleza kazi aliyopewa na binti wa Kiarabu. Sauti ilipita moyoni

“Hapana, siwezi kuondoka mahali hapa mpaka nikamilishe kazi niliyopewa itakayofanikisha kumuokoa mwanangu kwenye mdomo wa kifo”

David Samson akaamua kuvunja ukimya wake, akaongea kwa sauti ya kitetemeshi, sauti iliyodhihirisha alikuwa amechoka hoi bin taabani

“Mbona sielewi, unamaanisha nini?”

Amani Collence alitabasamu kama kawaida yake, tabasamu lililoonesha nuru ya uso wake wa kuvutia kisha akajibu

“Kuna kundi la wauza madawa ya kulevya linaloongozwa na binti mwenye asili ya Uarabuni, kundi hilo ni tishio kwetu, ni kundi lenye nguvu kama sisi”

Amani Collence akaweka kituo. Akaendelea kutembea tembea ndani ya chumba kile cha adhabu huku akijipiga piga kifuani kuonesha uhalisia wa maneno yake, akaendelea kumuelezea David Samson aliyekuwa amepiga magoti

“Kuna biashara tulifanya na kundi hilo, biashara iliyohusisha kiasi kikubwa cha pesa lakini siku ya biashara walitugeuka na kufanikiwa kuchukua kila kitu kilichokuwa mezani. Namaanisha walichukua pesa zote pamoja na mzigo wa madawa ya kulevya uliokuwa sehemu ya biashara”

David Samson alibaki njia panda. Akamfikiria binti wa Kiarabu aliyemteka mtoto wake kisha akamtuma arudi kundini kutafuta taarifa na mienendo yote ya kundi la Amani Collence kwa lengo la kumuokoa mtoto wake. Alihisi kuchanganyikiwa, akili yake ikamuaminisha na kumuhakikishia kuwa binti wa Kiarabu aliyezungumziwa atakuwa ni yule aliyemteka mwanae. Sasa akajihakikishia kuwa hakutekwa na watu wanaopinga uuzaji wa madawa ya kulevya bali alitekwa na wauzaji nguli wa madawa ya kulevya. Alibaki njia panda kuhusu majukumu mapya aliyoambiwa na Amani Collence, majukumu yaliyomtaka apenyezwe kwenye kundi la binti wa Kiarabu kwa lengo la kumpeleleza. Aliuona ugumu wa kazi hiyo, akabaki kamtolea macho Amani Collence aliyekuwa amesimama mbele yake baada ya kuchoka kutembea tembea ovyo ndani ya chumba kile. Amani Collence akaendelea na mazungumzo

“Mpango wa kukuingiza kwenye kundi hilo ulishakamilika siku nyingi, leo hii utakuwa ndani ya kundi hilo tena siyo kama kibaraka bali mfanyakazi wao mkubwa atakayehusishwa kwenye mambo mengi na makubwa ya kibiashara”

Kauli hiyo ilimshangaza zaidi David Samson, alishindwa kuelewa kilichomaanishwa na Amani Collence. Eti atakuwa mfanyakazi mkubwa atakayehusishwa kwenye mambo mengi na makubwa ya kibiashara! Alijiuliza mwenyewe

“Kivipi?”

Alikosa majibu ya maswali yake, alibaki kamtolea macho Amani Collence aliyekuwa mbele yake. Amani Collence alielewa hali ya David Samson akaamua kufafanua zaidi ili kumuweka David Samson karibu na mawazo yake

"Kundi la wauza madawa ya kulevya tunalotaka kukuingiza linafanya mawasiliano na kundi letu mama lililo Afrika Kusini pasipo wao kujua kama kundi hilo na kundi hili ni kitu kimoja"

Amani Collence aliendelea kuona mshangao wa David Samson usoni kwake, mshangao uliomaanisha alikuwa haelewi chochote zaidi ya kusikia sauti inayoeleza. Amani Collence alifafanua zaidi

"Baada ya kundi hilo lililo chini ya binti wa Kiarabu kufanikiwa kuchukua kila kitu toka mikononi kwetu, hatukulifumbia macho suala hilo. Tuliandaa mpango wa kulipiza kisasi na kuliteketeza kabisa. Kuna mzee na vijana waliopo Afrika Kusini ambao huratibu biashara yetu kutoka huko mpaka hapa Malosha. Vijana hao pamoja na mzee huyo waliweza kumuingiza mtegoni binti wa Kiarabu akaanza kufanya nao biashara pia, ilikuwa rahisi kwa sababu binti wa Kiarabu alikuwa akichukua mzigo wake toka nchi hiyo na jinsi mtego ulivyosukwa haikuwa rahisi kushituka"

David Samson alikuwa makini sana kumsikiliza Amani Collence, muda wote akiwa amepiga magoti. Amani Collence aliona umuhimu wa David Samson kuinuka, alimwamuru kuinuka na kukaa kwenye kiti cha plastiki kilichokuwa ndani ya chumba hicho. David Samson akatimiza maagizo ya bosi wake. Amani Collence akaendelea kutoa ufafanuzi wake

"Ingawa ilikuwa rahisi lakini haikuwa rahisi sana kumuaminisha binti wa Kiarabu kukubali kufanya biashara na watu asiowafahamu. Tuliandaa mpango wa kumuaminisha binti huye. Tulifatilia nyendo za biashara zake tukagundua ratiba yake ya kuendea mzigo Afrika Kusini. Tuliandaa mpango wa kuwakamata watu wake watakaoenda kuchukua mzigo wa madawa ya kulevya Afrika Kusini. Tuliandaa polisi feki waliofanikiwa kuwakamata watu wa kundi lake wakiwa na mzigo wa madawa ya kulevya tayari kwa kuondoka kurejea Malosha”

Kitendo kile kilimaanisha jela tena ughaibuni, vijana wale walifadhaika sana. Walifungwa pingu kisha wakaingizwa kwenye gari la polisi feki tuliowaandaa lakini kabla gari lile halijaondoka mahala pale pa maficho ambapo hutumika kufanyia biashara ya madawa ya kulevya ghafla gari tatu zikiwa mwendo kasi zilivamia eneo lile, zikafanikiwa kulizuia gari la polisi lililowateka vijana wa binti wa Kiarabu. Walishuka vijana zaidi ya nane wakiwa na silaha za moto za kisasa. Polisi walishurutishwa kushuka ndani ya gari lao. Polisi hawakuwa na jinsi, walishuka kama walivyoamuriwa. Wakaambiwa wachague kufa au kutimua mbio. Hakuna polisi aliyejibu, muda huo walikuwa wakitimua mbio. Vijana waliokamatwa na polisi awali wakawa mikononi mwa vijana walioenda kutoa msaada. Makundi yote mawili yalikuwa hayafahamiani kabisa kwa sura lakini vijana walioenda kutoa msaada walikuwa na taarifa za kutosha kuhusu vijana waliotoka nchini Malosha. Mmoja wa vijana walioenda kutoa msaada akaongea

"Hakuna haja ya kujiuliza mara mbili, hamtufahamu hata kidogo lakini sisi tunafahamu kuwa ninyi ni Wamalosha mnaojishughulisha na biashara ya madawa ya kulevya. Msihofu, hiyo ni biashara yetu pia"

Akapumzika kidogo akawatazama wenzake waliokuwa kimya huku wamevaa sura za kazi. Kijana yule akaendelea kutoa maelekezo kwa vijana waliookolewa toka mikononi mwa polisi

"Mpo mikono salama, wala msiwe na hofu wala shaka yoyote. Nyie ni mwenzetu. Wote tuonafanya biashara moja na tuna uaduni na polisi na Serikali kwa ujumla. Tuligundua polisi walifahamu nyendo zenu tukaamua kufatilia ili tutoe msaada endapo ukihitajika. Tumefanikiwa kwa asilimia mia moja"

Japokuwa ufafanuzi uliendelea lakini vijana waliosaidiwa toka mikononi mwa polisi hawakuwaamini waliotoa msaada kwa sababu hawakupewa sababu za msingi za kusaidiwa na watu wasio wafahamu, vile vile hawakuachwa huru waondoke bali walichukuliwa wakapelekwa kwenye ngome ya waokoaji, ngome iliyo Casino kwa muonekano lakini ina siri nzito ndani yake. Ilikuwa ni ngome ya kitajiri yenye kila aina ya ufuska. Wacheza kamari, wasagaji, wanawake malaya wachezea fimbo pamoja na mambo mengine ya anasa yaliendelea kama kawaida. Waliingizwa ndani ya Casino hiyo kisha wakaingizwa kwenye chumba cha siri, hata baadhi ya wafanyakazi wa Casino hiyo hawafahamu uwepo wa chumba hicho. Chumba hicho kinafahamika kwa watu wachache sana, watu ambao wanafahamu uwepo wa gwiji wa madawa ya kulevya ndani ya Casino hiyo. Chumba hicho kipo chini ya jengo la Casino. Mlango wa siri wa kuingilia chumbani humo unapatikana kwenye choo kimojawapo kati ya vyoo vya Casino hiyo. Siyo rahisi mtu kufahamu uwepo wa mlango huo wa siri. Choo hicho hutumiwa na Mr Casino na watu wake wachache, kati ya watu hao wachache ndio siri ilipo.

Chumbani humo walikutanishwa na mzee wenye umri zaidi ya miaka sitini, mzee alijitambulisha mbele yao kwa jina Masiya akimaanisha kuwa yeye ni mkombozi aliyeletwa duniani makusudi kuwatetea wanyonge na masikini. Aliwaeleza kuwa yeye ndiyo msambazaji nguli wa madawa ya kulevya barani Afrika. Hakika aliweza kujielezea kwa vijana wale. Mwisho wa siku, mzee Masiya aliwahakikishia ulinzi na usalama. Siku iliyofuata aliwasafirisha kwa njia za panya zaidi ya njia walizokuwa wakizifahamu wakafanikiwa kufika nchini Malosha pasipo kipingamizi chochote. Hakika walijihakikishia kuwa mzee yule ni nguli katika biashara ya madawa ya kulevya. Kilichowashangaza zaidi hawakuporwa mzigo wao wa madawa ya kulevya wala fedha nyingi walizokuwa nazo bali waliongezewa ulinzi na usalama wa safari yao. Mzee Masiya alikuwa wa ajabu sana vichwani mwao. Nafikiri walijiuliza

"Inakuwaje muuza madawa ya kulevya akuache uondoke na madawa pamoja na pesa nyingi kiasi hiki?"

Lakini walipoufikiria utajiri wa mzee yule waliamini aliamua kuwaacha kwa sababu alijiita mtetezi wa wanyonge na masikini. Taarifa za mzee Masiya walimfikishia bosi wao, binti wa Kiarabu. Zilikuwa taarifa za kumshitusha sana lakini baada ya kuwasiliana na mzee Masiya kupitia mawasiliano aliyowapa vijana wake hofu ya binti wa Kiarabu iliisha kabisa. Hapo ndipo urafiki wa kazi kati ya binti wa Kiarabu na mzee Masiya ulipoanza, walifanya biashara kwa kuaminiana sana. Mzee Masiya alimuhakikishia binti wa Kiarabu kuwa anamjali kama mwanae wa kumzaa, hakika kauli hiyo aliithibitisha kupitia uhusiano wao.

Japokuwa wapo mbali na hawajawahi kuonana lakini wanawasiliana sana kama watu walio ndani ya mkoa mmoja. Binti wa Kiarabu alifungiwa mzigo wake, ukapewa na ulinzi na kukwepa vipingamizi vyote kwa nguvu ya mzee Masiya. Biashara ilileta hali ya uaminifu zaidi ya undugu, uaminifu huo ulijengwa na binti wa kiarabu dhidi ya mzee Masiya, akahitaji kufahamiana zaidi. Binti wa kiarabu alimuomba mzee Masiya waweze kuonana nchini Malosha, aende maana amemuandalia zawadi anayohisi itamfaa. Lakini mzee Masiya alimsisitizia binti wa Kiarabu kuwa umri wake ni mkubwa sana, hashauriwi kusafiri safiri sana hasa umbali mrefu maana akifanya hivyo anahatarisha afya yake. Mzee Masiya akamwambia binti wa Kiarabu kuwa atamtuma kijana wake aende kuonana nae na kumpokelea zawadi hiyo. Kauli hiyo ilikuwa nzuri katika masikio ya binti wa Kiarabu, lakini aliomba kitu kingine zaidi.

Binti yule alimwambia mzee Masiya kuwa angependa mwanae abaki ndani ya kundi lake ili aratibu biashara vizuri zaidi, alimuhakikishia kuwa uwepo wa mtoto wake ndani ya kundi lake utarahisisha mambo mengi yanayomuhitaji mzee Masiya
Kauli hiyo ilimaanisha kijana wa mzee Masiya aje nchini Malosha kuchukua zawadi ya baba yake, arudi nchini kwao kumpelekea mzee wake kisha aje mara ya pili nchini Malosha kujiunga na kundi la binti wa Kiarabu ili wafanye kazi kwa ukaribu zaidi. Kauli hiyo ilikuwa tamu sana masikioni mwa mzee Masiya, aliona amepatikana mwaya wa kumuingiza kijana wetu katika himaya ya binti wa Kiarabu. Mzee Masiya alinieleza kila kitu, akaniambia nimuingize kijana makini katika himaya ya binti wa Kiarabu ili tuweze kumsambaratisha mara moja. Kijana huyo amepatikana, kijana huyo ni wewe David. Lazima uingie kwenye himaya ya binti wa Kiarabu kama mtoto wa mzee Masiya. Sasa amenasa mtegoni. Binti huyo wa Kiarabu anaitwa Nasrat Abdul al Aziz"

Amani Collence aliweka kituo kikubwa katika ufafanuzi wake. Sasa David Samson alilitambua jina la binti wa Kiarabu kuwa ni Nasrat Abdul al Aziz lakini utambuzi wa jina hilo haukumsaidia chochote wakati huo. Yeye aliufikiria mpango ulioandaliwa, mpango wa kumuingiza kwenye imaya ya Nasrat Abdul al Aziz kama mpelelezi kisha akafikiria kazi aliyopewa na binti huyo wa Kiarabu, kazi iliyomuweka mtoto wake dhamana. David Samson alibaki njia panda.

ITAENDELEA
MATEKA%20COVER.jpg
 
RIWAYA: MATEKA
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890

(KIPANDE CHA NNE)

Ilikuwa furaha na nderemo kwa binti wa Kiarabu, Nasrat Abdul al Aziz. Alikuwa akimsubiri kwa hamu mtoto wa mzee Masiya, aliamini akimpata mtoto huyo utakuwa mwanzo mzuri wa safari yake ya matumaini. Alitabasamu baada ya kuona anaweza kuua ndege wawili kwa wakati mmoja. Ilikuwa ni siku nzuri sana kwa Nasrat Abdul al Aziz, aliona jinsi alivyokuwa akielekea kushinda vita ya kujiongezea utajiri mkubwa alioachwa na marehemu baba yake, mzee Abdul al Aziz.

Vile vile aliamini lazima atapata mwanga wa kuchunguza mpango wake wa siri aliouandaa dhidi ya kila mtu au himaya aliyoitilia mashaka kuhusu familia yake. Muda huo alikuwa ndani ya jakuzi akioga maji ya uvugu vugu pasipo haraka yoyote. Aliyafikiria majibu ya mzee Masiya, majibu yaliyomdhihirishia ujio wa mtoto kipenzi wa mzee huyo, gwiji wa madawa ya kulevya barani Afrika. Alijisemea moyoni kuwa lazima afanye mbinu zake zote amteke kimapenzi mtoto huyo ili awe karibu zaidi ya mzee Masiya na ikiwezekana ateke utajiri wake wote. Alipanga mbinu za kumfilisi. Hiyo ndiyo ilikuwa kazi ya Nasrat Abdul al Aziz, ulikuwa ukiingia kwenye mtego wake lazima ufilisike na ukijifanya unajua kuzitetea mali zako lazima utangulie mbele ya haki. Lazima uzikwe futi sita ardhini.

Hakika haikuwa rahisi mtu kukwepa mtego wa Nasrat Abdul al Aziz kwa sababu alikuwa binti mrembo sana wa Kiarabu, binti aliyewatoa macho vijana wengi waliomuona katika majumba ya starehe, walimtongoza na kumuhitaji kimapenzi lakini hakuna walichoambulia. Hawakujua kipindi hicho alikuwa kazini, alikuwa na ahadi za kukutana na mtu katika maeneo hayo, ahadi ambazo mwisho wa siku alikuwa mshindi.
Jina la Nasrat Abdul al Aziz halikuwa chafu mahali popote, hakuwa na rekodi chafu popote. Alifahamika kama mwanamitindo aliyependwa zaidi na wanaume. Hakuwa maarufu sana, hapana, bali jina lake lilikuwa likikuwa siku hadi siku katika tasnia hiyo ya mitindo na ulibwende.

Nasrat Abdul al Aziz aliinuka toka ndani ya jakuzi alilokuwa akioga ndani yake, akachukua taulo na kujifuta maji yaliyokuwa yakitiririka toka mwilini. Alijifuta taratibu huku akijiangalia kwenye kioo kilichokuwa kikipatikana ndani ya bafu lake la kuogea, hakika alijidhihirishia alikuwa mrembo. Alilitazama umbile lake la kibantu kisha nywele ndefu zilizofika mpaka mgongoni. Hakuacha kusifia macho, kifua na midomo yake. Ngozi nyeupe iliyong`aa iliendelea kuakisi urembo wake. Hakika aliamini lazima amteke mtoto wa mzee Masiya, alijisemea moyoni

“Lazima niendelee alipoishia baba, lazima nipambane kurudisha heshima ya mzee Abdul al Aziz. Lazima nipambane”

Alitembea akiwa amevaa nguo zake za ndani mpaka chumbani kwake, akajiandaa taratibu mithili ya kinyonga mpaka akamaliza. Alivyojiona yupo vizuri akaitazama saa yake aliyoivaa mkononi, ilimuonesha ilikuwa saa nane na dakika arobaini na mbili mchana. Akatabasamu baada ya kuona masaa ya kuwasili mtoto wa mzee Masiya yamekaribia. Zilikuwa zimebaki dakika ishirini na nane ndege itue kwenye uwanja wa ndege wa Rwama Mwanzo. Nasrat Abdul al Aziz alichukua gari lake aina ya Toyota Land Cruiser V8 kisha akashika barabara kuelekea uwanja wa ndege, moyoni alikuwa na furaha sana ya kwenda kumpokea mtoto wa mzee Masiya.

Alipanga kumfikishia nyumbani kwake apumzike kisha ampeleke kwenye ngome yake, aliamini ndani ya siku hizo za mapumziko ataweza kumshawisha hata kidogo kijana yule wa mzee Masiya. Alijiapinza kichwani kuwa hata mtongoza kwa mdomo lakini vitendo vitachukua nafasi hiyo. Alijiamini katika mitego aliyotega. Alikuwa tayari kupoteza usichana wake kwa lengo la kumnasa kijana huyo. Njiani alipigiwa simu na mzee Masiya kupitia njia ya ‘WhatsApp’, mzee yule alimueleza kuwa mtoto wake ameshafika uwanja wa ndege anamsubiri ili utaratibu mwingine uendelee. Mzee Masiya alimfafanulia Nasrat muonekano wa mwanae pamoja na mavazi aliyovaa siku hiyo ili wasije kuchengana. Mtoto wa mzee Masiya na Nasrat Abdul al Aziz hawakuwa na mawasiliano hivyo basi mzee Masiya aliratibu mazungumzo yote kwa niaba ya mwanae.

Mzee Masiya alifanya hivyo kwa lengo la kutimiza mpango aliousuka dhidi ya adui yake, adui hakutilia shaka yoyote. Nasrat Abdul al Aziz aliongeza kasi ya gari, ndani ya dakika sita alikuwa nje ya uwanja wa ndege. Akaangaza mahali alipoambiwa atamkuta mtoto wa mzee Masiya. Kweli alifanikiwa kumuona kijana aliyevaa kofia aina ya kepu akiwa na begi dogo la mgongoni. Hakujiuliza mara mbili, alijihakikishia kuwa yule ndiye mgeni wake kwa sababu mavazi aliyovaa yalifanana kabisa na maelezo aliyopewa na mzee Masiya. Kwa mwendo wa madaha, Nasrat Abdul al Aziz alipiga hatua kuelekea alipokuwa mgeni wake, alitembea akihisi miguu ikitaka kugongana yenyewe kwa furaha aliyokuwa nayo moyoni. Aliona mambo yake yalivyokuwa yakimnyookea kirahisi sana.

Laiti kama angelijua mgeni aliyekuwa akimsubiri angelibaki nyumbani kwake na kumuamuru amfuate mwenyewe. Muda wote mgeni wake alikuwa ameinama chini huku macho akitazama kioo cha simu yake, moyoni alikuwa akitetemeka kama mtoto mdogo kila alipojihakikishia aliyekuwa akimfuata kwa bashasha alikuwa ni Nasrat Abdul al Aziz. Alihisi akiishiwa nguvu miguuni lakini alijikaza kiume, alikuwa tayari kupambana kwa lolote alilohisi lingeweza kutokea, alikuwa tayari kujiteketeza mwenyewe lakini siyo kumkosa mtoto wake. Alitaka kurudisha furaha katika sura ya mpenzi wake. Nasrat Abdul al Aziz alifika mbele ya David Samson aliyekuwa ameinama kama kobe atungaye sheria. Sauti nyororo ikaongea kwa lugha ya kiingereza

“Hello, my name is Nasrat Abdul al Aziz” (Habari, jina langu ni Nasrat Abdul al Aziz)

David Samson alitamani kufungua mdomo ili ajibu salamu ya Nasrat Abdul al Aziz lakini ukawa mzito. Akajikaza kiume akainua kichwa chake, sura yake ikakutana na macho mazuri ya mwenyeji wake yakimtazama kwa makini. Sasa ilikuwa ni zamu ya Nasrat Abdul al Aziz kushikwa na bumbuwazi. Akili yake ikashindwa kuamini kama aliyekuwa mbele yake ni David Samson, kijana aliyemuagiza kuingia ndani ya kundi la maadui zake kwa lengo la kudukua taarifa zao. Akili ya Nasrat Abdul al Aziz ikashindwa kuelewa na kuamini kilichokuwa kikiendelea, alishindwa kumuhusianisha David Samson na mzee Masiya. Vile vile alishindwa kuhusianisha kundi alilokuwa akilifanyia kazi David Samson na mzee Masiya.

Sasa aliamini alikuwa mtegoni, mtego alioutega mwenyewe aliona ukimrudia. Hakuongea chochote, alimshika mkono David Samson kisha akaanza kupiga naye hatua haraka haraka kuelekea alipoegesha gari lake, Toyota Land Cruiser V8. Kila mmoja alikuwa amechanganyikiwa lakini Nasrat Abdul al Aziz alichanganyikiwa zaidi. Akili yake iliwaza jinsi ya kupambana vita iliyokuwa mbele yake. Hakika aliiona vita hiyo, siyo vita ya taifa bali vita ya kimataifa. Hatua zao zilifanikiwa kuingia ndani ya gari. Walikaa viti vya mbele kisha Nasrat Abdul al Aziz akawasha gari, alihisi kushindwa kuliongoza gari lake mwenyewe. Kichwa kilikuwa kizito kupita kawaida. Akamwambia David Samson ashike usukani wa gari, David Samson hakuwa na jinsi zaidi ya kukubali lakini hakujua walipaswa kuelekea wapi. Alikuwa hapajui alipokuwa akiishi Nasrat Abdul al Aziz wala ilipokuwa ngome yake kwa sababu siku aliyoingizwa kwenye ngome ile alifumbwa macho. Akamuuliza Nasrat Abdul al Aziz kwa sauti ya kitetemeshi

“Tunaelekea wapi?”

Nasrat alielewa vizuri swali na David Samson, alimjibu pasipo kumtazama
“Tunaelekea nyumbani kwangu, nakaa Bungero jirani kabisa na kambi ya jeshi”
David Samson alikuwa akipafahamu vizuri Bungero lakini alishangaa kusikia msichana huyo akikaa jirani na kambi ya jeshi inayopatikana maeneo yale. Aliuona ujasiri wa binti yule jambazi mwenye sura nzuri. Alijihakikishia kuwa Nasrat Abdul al Aziz hakuwa mtu wa kawaida kabisa. Alibaki na swali moja kichwani kwake

“Anakaa Bungero au na ngome yake ipo Bungero?”

Lilikuwa swali lililokosa jawabu lakini kwakuwa ulikuwa ndiyo uelekeo waliokuwa wakielekea wakati huo, aliamini majibu yote yatapatikana mbele ya safari. Kipindi akiendelea kutafakari na kujiuliza maswali yasiyo na majibu huku mikono yake ikiwa imeshikilia usukani wa gari, ghafla alisikia swali likipita sikioni kwake, lilikuwa swali toka kwa binti wa Kiarabu

“Kwanini upo mahali hapa?”

Lilikuwa swali gumu zaidi katika maisha ya David Samson. Alifikiria majibu kadhaa lakini yote akaona hayafai kusikika katika masikio ya binti wa Kiarabu. Ukimya ukatawala. Nasrat Abdul al Aziz alielewa ugumu alioupata David Samson katika swali alilomuuliza, hakutaka kumfokea wala kumpanikisha chochote, alienda nae taratibu. Akabadilisha swali

“Mbona upo mtaani, umeshapata taarifa nilizokutuma?”

David Samson aligeuza kichwa akamtazama Nasrat Abdul al Aziz aliyekuwa pembeni yake kisha akarudisha kichwa kutazama walipokuwa wakielekea. Sasa aliona hakuwa na namna zaidi ya kuongea, aliamini akiongea ukweli anaweza kupata ahueni ya maisha yake na mwanae. Akamwambia Nasrat Abdul al Aziz

“Ngome inayoongozwa na Amani Collence ina uhusiano mkubwa na ngome ya mzee Masiya, wanafanya biashara kwa kushirikiana kwa miaka mingi”

Kauli hiyo ilikuwa tata katika masikio ya Nasrat Abdul al Aziz aliyekuwa ameshavurugwa na kauli za awali. Alikumbuka uhusiano alioujenga na mzee Masiya, uhusiano aliohisi ungekuwa na mafanikio mbele yake kumbe ulikuwa uhusiano utaopelekea kumteketeza kabisa. Nasrat akamuhoji David Samson

“Kivipi?”

David Samson alimuelezea Nasrat Abdul al Aziz mpango mzima ulivyosukwa mpaka akaingia kwenye mtego wa mzee Masiya, mtego ulioandaliwa kama kisasi kwake. Kichwa kilizidi kumuuma Nasrat Abdul al Aziz, akajaribu kutafakari kwa haraka lakini akaona uzito wa mawazo yaliyojenga kichwani kwake. Hakuwa na jinsi zaidi ya kuendelea kuilazimisha akili kufikiri na kutengeneza majibu ya maswali aliyokuwa akijiuliza. Sasa aliona njia pekee aliyohisi itakuwa njia ya ushindi, aliona jinsi kundi la Amani Collence linashirikiana na mzee Masiya lilivyokuwa likimtumia David Samson kumteketeza. Akatabasamu. Roho ngumu aliyofunzwa katika mafunzo yake ya siri ikamwingia mwilini. Alipata njia ya kuwateketeza maadui zake, hakika alijihakikishia itakuwa njia bora sana. Nasrat Abdul al Aziz akamwambia David Samson

“Ngome zao zinaamini wewe upo upande wao na zitaamini kila kitu utakachoongea kwao kwa sababu wamekupandikiza kama mtoto wa mzee Masiya katika himaya yangu…”

Kabla Nasrat Abdul al Aziz hajamaliza kuongea ghafla simu yake ikaita, akaitazama akaona jina My Love. Aliitazama simu ikiita mpaka ikakata. Mpigaji alipiga kisha akapiga tena pasipo kupokelewa simu yake, mara ukaingia ujumbe wa maandishi

“My love, why don’t you answer the phone? What’s the problem?” (Mpenzi wangu, kwanini hupokei simu? Kuna tatizo gani?)

Nasrat Abdul al Aziz aliitazama ujumbe ule kutoka kwa mwanaume aliyemkabidhi moyo na mwili wake, mwanaume aliyekuwa kila kitu katika maisha yake lakini muda huo hakuhitaji kuongea nae. Aliamini kazi iliyokuwa mbele yake haikuhitaji faraja ya mapenzi bali roho ngumu. Alijisemea moyoni

“I will call you my love, I am on a special mission. Work of life and death” (Nitakupigia mpenzi wangu, nipo kwenye kazi maalumu. Kazi ya uhai na kifo)

Jumbe na simu za mpenzi wake ziliendelea kuingia kwa fujo lakini Nasrat Abdul al Aziz hakubadilisha msimamo wake. Muda huo alisahau kabisa habari za mapenzi, akili yake yote ilikuwa kazini, kazi maalumu isiyojulikana kwa mpenzi wake aliyemkabidhi moyo wote pasipo kubakiza sehemu hata ndogo ya kumuweka mwanaume mwingine kama mchepuko. Nasrat Abdul al Aziz akaendelea na maongezi yake yaliyozidi kumchanganya David Samson

“Mzee Masiya amekuleta kwangu kama mtoto wake, hakika na mimi nakupokea hivyo. Ipo siku wataelewa kuwa wao ndiyo hawaujui ukweli. Siku watakayojua watakuwa wameshateketea. Utakaa kwangu kwa muda wa siku mbili, siku ya tatu utaanza safari ya kuelekea Afrika Kusini kumpelekea mzee Masiya zawadi niliyomuahidi, lazima umpelekee zawadi hiyo ili aamini kuwa kila kitu kimeenda sawa kama alivyohitaji kiwe. Ukifika Afrika Kusini utachunguza vitu vya misingi utakavyoweza kuvijua kwa muda utakaokuwa ndani ya himaya yake ili atakapokurudisha katika himaya yangu ushirikiane nami kama mwanae tuwe na mwanzo mzuri wa kuanzia. Kuhusu himaya ya Amani Collence tutajua cha kufanya utakaporudi nchini…nafikiri ukifanya hivyo utampata mtoto wako akiwa salama kabisa”

David Samson alichanganyikiwa kwa maelekezo aliyopewa, alitamani asimamishe gari amuhoji vizuri Nasrat Abdul al Aziz lakini aliamini haitasaidia chochote. Aliona anavyozidi kuingizwa kwenye mipango mikubwa ya kihalifu, mipango iliyomaanisha mchezo wa kifo au kupona. Alitamani kukataa kufanya kazi hiyo lakini taswira ya mtoto wake mchanga ikamjia kichwani, akaikumbuka sauti yake akilia. Sauti aliyoisikia siku aliyomshika ndani ya ngome ya Nasrat Abdul al Aziz. Aliamini asipojitoa sadaka mtoto wake anaweza kuwa sadaka ya kuteketezwa. David Samson alijisemea moyoni

“Hakuna cha maana zaidi ya uhai wa mwanangu”

Akili ya David Samson iliendelea kutafakari hatima yake, lakini ilikuwa kazi bure kwa sababu hatima ya maisha yake ilikuwa mikononi mwa binti wa kiarabu aliyechafukwa moyo na roho, binti aliyekuwa akipanganisha mawazo kichwani kama mvua ya mawe inavyoshambulia bati la mlala hoi. Dakika kadhaa zilipita kama zikisukumwa na upepo, wakafanikiwa kufika kwenye makazi ya binti wa kiarabu. Japokuwa palikuwa pembezoni kidogo mwa mji lakini nyumba ya Nasrat Abdul al Aziz ilionesha utajiri aliokuwa nao. Aliishi kwenye nyumba ya kisasa, nyumba yenye vigezo vyote vya kuitwa ya kisasa. Mlinzi wa geti alifungua mlango wa geti haraka kisha gari likafanikiwa kuingia ndani ya uzio. David Samson alifanikiwa kuyaona magari mengine mawili yakiwa yameegesha katika sehemu maalumu iliyoandaliwa kwa kazi hiyo. Akajisemea moyoni

“Hakika binti huyu ni tajiri mtoto”

Walifungua mlango wa gari, kila mmoja upande wake kisha wakaelekea sebuleni. David Samson alipokelewa na sebule kubwa iliyopambwa na kupambika kwa picha mbalimbali za wana mitindo wa walimbwende maarufu nchini na duniani kwa ujumla. Macho yake yaliendelea kutambaa juu ya vitu vya thamani vilivyoenea kila kona ya sebule ile. Alizidi kujihakikishia utajiri wa Nasrat Abdul al Aziz. Binti wa Kiarabu alikaa juu ya sofa akiendelea kutafakari hatima ya mambo yaliyotokea, lakini kipindi akiendelea kusumbuliwa na mawazo ghafla simu yake ikaita kwa fujo. Simu iliita mpaka ikakata, ikaita tena na tena pasipo mafanikio ya kupokelewa. Binti wa Kiarabu hakuthubutu hata kuitazama kwa sababu aliamini aliyekuwa akipiga ni yule yule mpenzi wake. Simu haikuchoka kuita, iliita zaidi ya mara sita pasipo kuitikiwa hata kauli moja, ikaamua kukaa kimya. Baada ya dakika moja na sekunde kadhaa ukasikika mlio wa ujumbe katika simu yake, akashawishika kuusoma ujumbe ule. Nasrat Abdul al Aziz akachukua simu yake iliyokuwa upande wake wa kushoto, juu ya sofa aliyokuwa amekalia kisha akautazama ujumbe ule. ulionesha umetumwa na Zimwi, akausoma

“Tumefanikiwa kuupata mzigo aliokuwa nao kijana wa miraba minne, mzigo aliopewa na David Samson”

Tabasamu hafifu likashambulia mashavu ya Nasrat Abdul al Aziz baada ya kuona mipango yake ikienda vizuri. Akili yake ikamtuma aangalie namba iliyokuwa ikimpigia mfululizo. Hakika alijithibitishia kuwa alikuwa mpumbavu wa akili, aliyekuwa akipigia simu mfululizo hakuwa mpenzi wake kama alivyofikiria awali bali alikuwa Zimwi. Moyo ulimuuma Nasrat Abdul al Aziz, akaona jinsi mapenzi yanavyoweza kuhatarisha misingi na misimamo ya kazi yake. Kauli ya marehemu baba yake mkubwa ikamjia kichwani

“Mixing love and work never works”

Alijihakikishia ukichanganya mapenzi na kazi huwezi fanikiwa katika mipango yako, lakini atafanya nini kumuepuka mwanaume aliyemkabidhi moyo wake. Mwanaume aliyevutiwa nae tangu siku ya kwanza aliyokutana nae katika mashindano ya kumtafuta Miss Rwama Mwanzo miezi minne iliyopita. Mwanaume mrefu, mweupe na aliyejengeka mwili kwa ratiba nzuri ya mazoezi ya viungo. Mwanaume aliyemfahamu kama mchongaji wa vinyago na mchoraji mwenye kipaji cha ajabu, mwenye uwezo wa kuchora picha mithili ya kivuli (photocopy). Nasrat Abdul al Aziz alijitambulisha kwa mwanaume yule aliyemfahamu kwa jina la Derrick Edward kuwa anajishughulisha na masuala ya ulimbwende na mitindo. Kwa upande wake aliamini haikuwa kazi ngumu kumuaminisha Derrick Edward suala hilo kwa sababu mara kadhaa alizofanikiwa kuingia nyumbani kwake alikaribishwa na mandhari yaliyoakisi ulimbwende na mitindo. Penzi lao lilikuwa na kasoro moja tu, kasoro waliyoijadili kila siku pasipo kuipatia majibu, kasoro iliyowaumiza vichwa lakini mwisho wa siku walikubaliana kila mmoja abaki na upande wake ili wadumishe penzi lao. Kasoro yao ilikuwa ni dini.

Nasrat Abdul al Aziz alikuwa muislamu safi mbele ya macho ya kila mmoja aliyemtazama lakini Derrick Edward alikuwa mkristo safi wa Kikatoliki. Kikwazo kilichobaki kilikuwa kuhusu watoto watakaowapata, watakuwa wakristo au waislamu? Walikubaliana watazungumzia jambo hilo watakapofanikiwa kuwapata watoto hao. Penzi zito liliendelea kumea mizizi kama kawaida. Japokuwa Nasrat Abdul al Aziz alikuwa na pesa nyingi zaidi ya Derrick Edward lakini hazikuleta utofauti wala kikwazo katika penzi lao. Derrick Edward alisimama kama mwanaume shupavu anayejipambania na kutafuta pesa zake na siyo kutegemea pesa za mwanamke.

Suala hilo lilimfurahisha sana Nasrat Abdul al Aziz akajikuta akizidi kumpenda zaidi Derrick Edward na kumboreshea sanaa yake ya uchongaji na uchoraji kwa kumnunulia vifaa vya kisasa. Kazi ya Derrick Edward ilimpa umaarufu sana tofauti na pesa alizokuwa akipata, umaarufu wake ulipaa siku hadi siku. Alishirikishwa kwenye matamasha mengi ya uchoraji, matamasha yaliyomkutanisha na watu wengi maarufu na matajiri nchini na nje ya nchi. Matamasha yaliyomkutanisha na wasichana warembo wa kila aina lakini hakuna hata mmoja aliyefanikiwa kuuteka moyo wake kwa sababu kila sehemu aliyokuwa akienda akuchoka kumsifia mpenzi wake.

Jina la Nasrat Abdul al Aziz lilikuwa kama kiitikio katika wimbo mzuri unaomsifia msichana mrembo mwenye asili ya Kiarabu. Hali ilikuwa tofauti kwa Nasrat Abdul al Aziz, yeye hakumzungumzia kabisa Derrick Edward mahali popote na mara chache alizoulizwa kuhusu Derrick Edward alijibu majibu ya mafumbo yaliyowaacha midomo wazi waulizaji. Hali hiyo haikumaanisha chochote katika penzi lao, walipanga kuwachanganya wanaowafatilia. Hakika walifanikiwa kuwachanganya.
Binti wa Kiarabu alikuwa akiumiza kichwa namna atakavyompeleka David Samson katika himaya ya mzee Masiya, siyo kwamba alikosa njia, la hasha, bali aliifikiria zawadi gani anayostahili kumpelekea mzee yule mwenye utajiri mkubwa Afrika Kusini. Zawadi zilipangika kichwani kwake lakini bado akaona hazina maana yoyote mbele ya tajiri yule. Hakuchoka kufikiria jawabu sahihi. Mtafutaji hachoki na akichoka ujue kapata alichokuwa akikitafuta, ndivyo ilikuwa kwa Nasrat Abdul al Aziz. Sasa alikuwa amechoka baada ya kupata jawabu sahihi, jawabu lililomuhusisha mpenzi wake katika kazi hiyo ya kihalifu. Nasrat Abdul al Aziz aligeuza shingo akamtazama David Samson aliyekuwa akiendelea kushangaa sebule kisha akamwambia

“Kabla hujaenda Afrika kusini kwa mzee Masiya lazima tuandae zawadi utakayompelekea, zawadi hiyo ndiyo itakayokuweka karibu zaidi na yeye”

David Samson alikuwa kamtumbulia macho binti wa Kiarabu aliyekuwa akiendelea kufafanua kauli yake

“Ninakurushia picha ya mzee Masiya kwa njia ya ‘WhatsApp’, kisha leo saa kumi jioni utaenda Kabutuka katika ofisi ya mchoraji na mchongaji anayeitwa Derrick Edward. Utamwachia picha hiyo aichore na kuichonga haraka iwezekanavyo kwa gharama yoyote ile atakayokwambia. Anaweza kukuhoji kwanini unahitaji picha ya mzee Masiya iliyochongwa na kuchorwa? Mzee huyo ni maarufu sana nchini Afrika Kusini kwa sababu alishiriki katika uchaguzi wa Rais mwaka jana lakini bahati haikuwa kwake, alishindwa kwa asilimia chache na Rais wa sasa. Utamjibu kuwa unavutiwa sana na siasa za mzee huyo wa kusini mwa bara la Afrika…Usitaje jina langu mbele ya mchoraji huyo, namaanisha anatakiwa kujua kuwa wewe ndiye kila kitu kwenye kazi hiyo na siyo vinginevyo. Msisitize afanye kazi hizo haraka iwezekanavyo ili tuandae mpango wetu mapema na wewe umpate mtoto wako haraka”

David Samson alimfikiria mchoraji anayefanya shughuli zake mtaa wa Kabutuka, aliyeambiwa anaitwa Derrick Edward, halikuwa jina geni hata kidogo kwa sababu alikuwa mchoraji na mchongaji maarufu sana, mwanasanaa mwenye sifa kemkem mpaka nje ya mipaka ya Rwama Mwanzo. Lakini David Samson alikuwa hajawahi kuongea nae wala kuingia katika ofisi yake hata mara moja, siku zote hakuwa na sababu ya msingi ya kumkutanisha na kijana mwenye kipaji cha ajabu cha uchoraji na uchongaji. David Samson aliyafikiria maneno ya Nasrat Abdul al Aziz, maneno yaliyomsisitiza asitaje jina lake mbele ya mchoraji yule, Kauli hiyo ilimpa udadisi akabaki akijiuliza

“Kuna nini kati ya binti wa Kiarabu na mwana sanaa wa ajabu?”

Alikosa jibu la swali lake lakini alijihakikishia kuwa lazima atajuwa kila kitu kilichojificha nyuma ya pazia la chuma, aliamini kama kitaweza kumsaidia kumpata mtoto wake kwa uharaka lazima atakisimamia ipasavyo lakini akigundua hakina maana yoyote atakipuuza. Laiti kama David Samson angelijua alikuwa akiendelea kutumbukizwa shimoni angelilia na kusaga meno kwa wakati mmoja. Masaa yalisogea haraka, David Samson akafanikiwa kufika mtaa wa Kabutuka katika ofisi ya Derrick Edward, ofisi ya kisasa haswa iliyofahamika kwa jina la UCHORAJI NA UCHONGAJI. Aligonga mlango kisha akaingia ndani ya ofisi hiyo. Alimkuta kijana mrefu, mweupe na aliyejengeka kwa mazoezi akiendelea na shughuli zake za uchoraji, alikuwa akipaka rangi picha ya mrembo mwenye asili ya Kiarabu.

Baada ya salamu, David Samson aliikazia macho picha iliyokuwa ikipakwa rangi, hakika alishindwa kuyaamini macho yake, alihisi yakimdanganya kwa asilimia mia moja kumbe yeye ndiye aliyekuwa akijidanganya. Macho yalikuwa sahihi kwa asilimia zote. Ilikuwa picha ya binti wa Kiarabu akitabasamu na kuruhusu meno yake mazuri kuonekana barabara. Picha ya Nasrat Abdul al Aziz. David Samson alibabaika kidogo lakini akajikaza kiume, akakaa kwenye kitu alichoambiwa akae na mwenyeji wake, lakini kabla hajaongea shida iliyompeleka mahali pale alifanikiwa kuiona picha kubwa ya Nasrat ikiwa imebandikwa kwenye moja ya kuta za ofisi hiyo, picha hiyo haikumshangaza sana bali maandishi yaliyoambatanishwa chini ya picha hiyo ndiyo yaliyomuacha mdomo wazi. Maandishi yale yalisomeka

“Nakupenda Nasrat – Derrick”

David Samson aliitazama mara mbili mbili picha ile akihisi ikiendelea kumdanganya lakini mwisho wa siku alijihakikishia alikuwa sahihi kwa asilimia zote. Aligeuza kichwa chake na kumtazama Derrick Edward aliyekuwa bize akisafisha mikono yake kwa kitambaa chepesi, alikuwa akijifuta rangi iliyoathiri mikono yake. Alimkazia macho kisha akakumbuka alishawahi kusikia kuwa kuna msichana wa Kiarabu anayejihusisha na masuala ya ulimbwende na mitindo yupo katika mahusiano ya kimapenzi na mchoraji huyo mwenye sifa kemkem nchini. Sasa aliamini msichana huyo aliyekuwa akizungumziwa alikuwa Nasrat Abdul al Aziz. Awali alishindwa kufahamu kuhusu suala hilo kwa sababu hakuwa mtu anayefatilia mambo ya mitindo na ulimbwende. Derrik Edward alisogea mpaka kwenye kiti cha plastiki kilichokuwa jirani zaidi ya David Samson kisha akamchangamkia mgeni wake

“Karibu Bro, utanisamehe nilikuwa bize kidogo. Sasa naweza kukusikiliza vizuri”

Kauli hiyo ilitoka kwenye mdomo wa Derrick Edward huku akiambatanisha na tabasamu mororo, lilikuwa tabasamu la kuonesha ukarimu kwa mteja. Hakika alijua jinsi ya kuwakarimu wateja wake ndiyo maana alisifika kila kona kwa kila mgeni aliyewahi kuhudumiwa naye. Kichwa cha David Samson kiliendelea kutengeneza maswali mengi hasa baada ya kukumbuka kauli ya Nasrat Abdul al Aziz, kauli iliyomsisitiza asitaje jina lake kwa mchoraji huyo. Akajiuliza

“Kwanini hataki ajulikane kwa mpenzi wake? Kuna nini kilichojificha?”

Yalikuwa maswali yaliyokosa majibu halisi, alisahau mazungumzo yalikuwa yameshaanza kati yake na Derrick Edward. Ukimya ulitawala pasipo kujibu, alizama mawazoni. Hali hiyo ilimpa taswira mpya Derrick Edward, alimfikiria mteja wake kwa jicho la pili, jicho ambalo hulitumia kuwatazama watu wachache sana hasa anapokuwa nje ya taaluma ya uchoraji na uchongaji. Jicho ambalo huwa lipo kazini zaidi ya kazi iliyomtambulisha kwa jamii iliyomzunguka. Akatamka kwa mara ya pili, safari hiyo aliongeza umakini kwa mteja wake

“Karibu kaka, naweza kukusikiliza”

David Samson alishituka toka katika dimbwi la mawazo, sasa aliisikia kauli ya Derrick Edward. Alijichekesha kinafiki kuonesha kuwa alikuwa makini toka awali lakini kicheko chake hakikuweza kumuhadaa Derrick Edward aliyekuwa ameshatambua mteja wake alikuwa mbali kimawazo. David Samson akajibu haraka

“Asante kaka. Kuna picha ipo katika simu yangu nataka uichore na kuichonga haraka iwezekanavyo, nachomaanisha haraka namaanisha haraka kweli”

Kauli hiyo ilitoka mdomoni mwa David Samson huku akimkabidhi simu na kumuonesha picha husika Derrick Edward, ilikuwa picha ya mzee Masiya kama alivyoagizwa na binti wa Kiarabu. Sasa ilikuwa zamu za Derrick Edward kushangaa baada ya kuiona kazi aliyokabidhiwa na mgeni wake, alishanga kuona akipewa kazi ya kumchora mzee Masiya, kiongozi imara wa chama cha upinzani na mwenye nguvu kubwa ya umma nchini Afrika Kusini. Aligeuza kichwa chake kisha akamtazama David Samson, akamuuliza swali la kichokozi

“Naona unataka picha ya mpinzani wa Afrika Kusini, kuna nini ndugu yangu?”

Lilikuwa swali rahisi sana katika akili ya David Samson kwa sababu aliambiwa mapema na Nasrat Abdul al Aziz kuwa anaweza kuulizwa swali la namna hiyo, swali hilo hilo rahisi kwa David Samson lilikuwa swali la maana sana kwa Derrick Edward aliyekuwa ameshatengeneza hali ya hofu na mashaka kwa mteja wake. Macho ya Derrick Edward yalikuwa makini kutazama umakini wa sura ya David Samson, alitaka kuisoma lugha ya picha ya sura yake kuliko maneno atakayotoa mdomoni. Hakika Derrick Edward alikuwa kazini, kazi yakuhitaji kumfahamu vizuri mteja wake aliyemtilia mashaka. David Samson alikuwa makini sana kwa sababu halikuwa swali geni katika masikio yake, umakini wake uliweza kuhadaa matarajio ya Derrick Edward aliyekuwa akiipeleleza sura yake. Kauli ya Nasrat Abdul al Aziz ikajirudia kichwani kwake

“…Anaweza akakuhoji kwanini unahitaji picha ya mzee Masiya iliyochongwa na kuchorwa. Mzee huyo ni maarufu sana nchini Afrika Kusini kwa sababu alishiriki katika uchaguzi wa Rais mwaka jana lakini bahati haikuwa kwake, alishindwa kwa asilimia chache na Rais wa sasa. Utamjibu kuwa unavutiwa sana na siasa za mzee huyo wa kusini mwa bara la Afrika”

Alimjibu kama alivyoelekezwa na Nasrat Abdul al Aziz, majibu hayo hayakubadilisha utafiti wa Derrick Edward aliyekuwa makini dhidi ya mteja wake. Derrick Edward akauliza swali ya pili dhidi ya David Samson

“Unataka kuzitumiwa wapi picha hizo?”

David Samson hakutegemea kuulizwa swali hilo, sasa alibabaika kidogo usoni akitafakari jibu la haraka la kumjibu Derrick Edward aliyekuwa makini akisubiri. David Samson hakujuwa kama alikuwa akichunguzwa na mchoraji yule

“Kama nilivyokwambia navutiwa na siasa za kizalendo za mzee Masiya, hivyo nikipata picha zake zitakuwa kumbukumbu kwangu na kwa kizazi changu”

David Samson alidhani amefanikiwa kumlaghai Derrick Edward lakini hakujuwa umakini wa mchoraji huyo katika usomaji wa sura za watu. Derrick Edward alielewa fika kuwa jibu alilopewa na David Samson halikuwa sahihi kabisa, aliamini nyuma ya jibu hilo la uongo kuna siri nzito iliyojificha. Alibaki akijiuliza kichwani kwake

“Kwanini anataka picha za mzee huyu, mafia wa kuuza madawa ya kulevya? Kijana huyu atakuwa anafanya kazi chini ya nani?”

Alikosa majibu ya maswali yake, lakini alijihakikishia lazima afatilie mpaka afahamu kila kilichojificha. Aliuona mwanga wa kazi iliyokuwa mbele yake, ulikuwa ni mwanga wenye giza totoro mbele. Mwanga wenye vita vya kupigania uhai au kuacha uhai upotee na lichimbwe kaburi la futi sita. Waliongea machache yaliyohusu kazi iliyokuwa mezani, Derrick Edward alimwambia David Samson kuwa arudi baada ya siku kumi kuchukua kazi zake zote mbili. Suala la malipo halikuwa shida kwa David Samson, hakubisha gharama aliyoambiwa na mwana sanaa. Kitendo kile kilizidi kumpa mashaka Derrick Edward dhidi ya mteja wake, alijihakikishia uhatari wa mteja wake.

Siku kumi ziliisha, David Samson alikabidhiwa kazi yake. Hakuamini macho yake alivyoona ubora wa hali ya juu wa kazi alizompatia Derrick Edward, alikubali kuwa mwana sanaa huyo ana kipaji cha ajabu. Alichukua kazi zake na kuondoka. Nyuma ya mgongo aliacha maswali mengi kwa Derrick Edward, maswali yaliyozidi kujitengeneza siku hadi siku. Laiti kama David Samson angelijua alichokifanya Derrick Edward katika picha zile asingelizipokea kamwe.

ITAENDELEA
1382476836.jpg
 
RIWAYA: MATEKA
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890

(KIPANDE CHA TANO)

MIEZI KADHAA NYUMA
Upepo mwanana uliendelea kupepea, haikuwa kawaida kwa upepo wa namna ile kupepea majira kama yale, saa mbili na nusu usiku. Mapazia ya sebule ya mkuu wa kitengo cha kupambana na kudhibiti madawa ya kulevya nchini Malosha yalikuwa yakipepea ovyo. Mapazia yale yalielezea tabu yaliyokuwa yakiipata toka kwenye upepo ule wa ajabu. Upepo ule haukuwa na maana yoyote mbele ya vijana wawili waliokuwa kazini, japokuwa hayakuwa masaa ya kazi lakini walikuwa wakijadili masuala ya kazi. Hawakuwa na muda wa kusubiri usiku huo upite, ilikuwa kazi ya haraka sana. Kijana aliyepewa kazi ya kuwa mkuu wa idara ya kupambana na kudhibiti wauza madawa ya kulevya nchini Malosha alimwita kijana mwenzake ili ampe kazi, kazi aliyoamini itakamilika endapo ikiwa mikononi mwa kijana huyo.

Maongezi yao yalikuwa ya siri sana na hawakutaka watu wengine wafahamu usiri huo. Kiongozi yule aliamua kumchukua kijana huyo ili ampe kazi nzito, kazi ya kulipigania taifa la Malosha. Kiongozi yule aliyefahamika kwa jina la Ibrahim Shadidy alimwambia kijana wake aliyefukuzwa kazi katika kitengo chake, ulikuwa mpango maalumu kati ya kiongozi huyo na kijana wake kuwa lazima watengeneze mazingira ya kumfukuzisha kazi mbele ya watu kisha apewe kazi ya siri ya kuchunguza mambo yaliyojificha. Hakika mpango wao ulifanya kazi. Kiongozi Ibrahim Shadidy alimtazama mtumishi wake aliyemfukuzisha kazi kwa mpango maalumu, mtumishi aliyezoea kumuitwa kwa jina moja la Derrick kisha akamwambia

“Nimekutoa kwenye idara yangu ili uwe mtu huyu, nataka ufanye kazi iliyowashinda watu wengi. Nataka tung`oe kila kizuizi kilichowashinda baba na babu zetu”

Akaweka kituo kikubwa kisha akasimama, akaanza kutembea tembea sebuleni kwake huku akijipiga piga kichwani kwa kutumia mkono wake wa kulia, akarudi alipokuwa awali kisha akaendela

“Najua una kipaji cha ajabu cha uchoraji na uchongaji, nataka nchi nzima ya Malosha ikufahamu kama mwana sanaa na siyo mpelelezi. Naamini kupitia uwezo wako wa sanaa utaweza kupenya katika sehemu ambazo mwingine hawezi, naamini utaweza kufanya kazi vizuri kwa asilimia zote. Hakika naamini katika uwezo wako…acha jamii na wana idara wenzako wajue umefukuzwa kazi, acha wafikirie hivyo lakini mimi na wewe tunajua tunachokifanya”

Derrick Edward kama vyeti vyake vya masomo vilivyomtambulisha aliinamisha kichwa chini kisha akaitafakari kazi mpya aliyokabidhiwa usiku huo, alijihakikishia ilikuwa kazi ngumu na nzito. Kipindi akiendelea kutafakari juu ya kazi hiyo, kiongozi Ibrahim Shadidy akaendelea kutoa ufafanuzi.

“Yakupasa kwenda mkoani Rwama Mwanzo, mkoa wa Magharibi ulio mpakani. Biashara ya madawa ya kulevya imeshamiri sana mkoani humo. Madawa yanaingia na kutoka kama kawaida…Kuna mwanamitindo wa Kiarabu anahisiwa kushiriki biashara hiyo, inasemekana yu miongoni mwa magwiji wa biashara haramu. Tulishajaribu kumpeleleza kwa siri lakini hakuna tulichoambulia, mbaya zaidi kila aliyempeleleza alifariki kifo cha ajabu kabda hajakamilisha kazi aliyotumwa”

Yalikuwa maneno makali sana toka kwenye kinywa cha kiongozi Ibrahim Shadidy, maneno yaliyoelezea ugumu wa kazi iliyokuwa mbele ya Derrick Edward, maneno yaliyomtaka Derrick Edward kumpeleleza kwa umakini wa hali ya juu binti wa Kiarabu ili asije kutangulizwa mbele ya haki kama walivyofanywa wapelelezi wenzake. Mwisho wa siku Derrick Edward alikubali kwa mikono miwili kuipokea kazi hiyo. Aliwaaga rafiki zake wote wa mkoani Rwama Mwisho, akamwaambia anaelekea Rwama Mwanzo kutafuta maisha mapya baada ya kufukuzwa kazi. Wote waliamini kauli ya Derrick Edward lakini hawakujua nyuma ya pazia alikuwa akielekea mkoani Rwama Mwanzo kupambana na wauzaji na wasambazaji wa madawa ya kulevya, hawakujua alikuwa akielekea mkoani Rwama Mwanzo kumpeleleza binti wa Kiarabu aliyedhaniwa kuwa gwiji wa kuuza na kusambaza madawa ya kulevya. Hakika hawakujua chochote.

Derrick Edward alifanikiwa kuingia mkoani Rwama Mwanzo kwa usafiri wa treni. Kichwani kwake alifikiria jambo moja tu, namna ya kuwa karibu na Nasrat Abdul al Aziz, mtoto wa Kiarabu. Baada ya wiki kadhaa Derrick alifanikiwa kufungua ofisi yake ya kufanyia kazi zake za sanaa, kazi ilimtangaza hasa kutokana na ubora aliozalisha siku hadi siku. Alisifika kila kona ya mtaa, mkoa na akaanza kuvuka mipaka ya nchi. Kazi zake zilisambaa mpaka nchi za jirani. Muda wote alikuwa akiwasaliana na kiongozi wake bwana Ibrahim Shadidy, katika mawasiliano yao walipanga mipango mingi itakayowezesha kumuweka karibu Nasrat Abdul al Aziz. Mwanzo walikubaliana amfatilie binti yule wa Kiarabu kimya kimya mpaka afanikiwe kupata taarifa zake. Mbinu hiyo iligonga mwamba na ilikuwa ngumu sana kufanikiwa kwa sababu ratiba ya maisha ya Nasrat Abdul al Aziz ilikuwa ngumu kufahamika.

Miezi kadhaa ilisogea pasipo kujua nini cha kufanya lakini Mungu siyo Athumani, na ukihitaji msaada wake lazima akupatie pindi anapohitaji. Derrick Edward alipata wazo la kujihusisha kimapenzi na Nasrat Abdul al Aziz ili aweze kufahamu mambo mengi ndani ya muda mfupi, lilikuwa wazo zuri lakini gumu kufanikiwa. Alimshirikisha kiongozi Ibrahim Shadidy, naye aliafiki wazo hilo, akamwambia endapo likifanikiwa litafanikisha kazi ndani ya muda mfupi. Wazo hilo lilikuwa na unafuu wa kumpata Nasrat Abdul al Aziz kwa sababu lilihitaji kumuongelesha binti yule popote pale atakapoonekana, tofauti na wazo la kwanza lililohitaji kumchunguza kimya kimya.

Suala la kumchunguza mtu linakuhitaji umakini zaidi ili asije kubaini lakini suala la kumtongoza mtu alihitaji umakini huo. Mapenzi ni hisia. Kwakuwa walielewa Nasrat Abdul al Aziz alipendelea kujihusisha na masuala ya mitindo na ulimbwende wakaamini lazima wamuingize katika mtego wao, walikubaliana lazima waanzishe matamasha mbalimbali ya urembo na ulimbwende ili waweze kumsogeza katika rada yao. Hakika walijipanga kumnasa mtoto wa Kiarabu.

Kiongozi Ibrahim Shadidy alijiingiza rasmi kwenye masuala ya kusaka vipaji vya urembo na ulimbwende, siyo kwamba jamii ilifahamu kuwa yeye ndiye aliyeanzisha harakati hizo za kisanaa, la hasha, bali alimtumia kijana wake wa kazi aliyefahamika kwa jina la Daniel Magesa. Daniel Magesa alikuwa kijana aliyeajiriwa kuchukua nafasi ya Derrick Edward baada ya kufukuzwa kazi, alikuwa hafahamiki na watu wengi ndiyo maana bwana Ibrahim Shadidy akaamua kumtumia kama ngao yake. Daniel Magesa alikuwa hajui mipango ya bwana Ibrahim Shadidy na Derrick Edward, yeye alijua ameaminiwa na bosi wake kusimamia sanaa hiyo aliyoianzisha kwa jina lake, hakujua nyuma ya matamasha aliyosimamia kulikuwa na mpango madhubuti wa kumchunguza binti wa Kiarabu. Hakika hakujua. Alichoambiwa kuhusu Derrick Edward ni suala moja tu, aliambiwa ampatie nafasi ya kutangaza biashara zake za uchoraji na uchongaji katika matamasha hayo.

Daniel Magesa hakuwa na kinyongo chochote ingawa alikuwa ameshaambiwa kuhusu suala la Derrick Edward kufutwa kazi kwa sababu za utoro na nidhamu, aliamini suala la yeye kuambiwa amsaidie kijana mwenzie kutangaza sanaa yake katika matamasha atakayosimamia ilikuwa ni njia ya kumnusuru na umasikini mwenzao.
Matamasha yalianzishwa kama uyoga ndani ya mkoa wa Rwama Mwanzo, katika matamasha hayo Derrick Edward alipata wasaa wa kutangaza bidhaa na ofisi yake. Derrick Edward alihudhuria matamasha yote ya awali lakini hakufanikiwa kumuona Nasrat Abdul al Aziz, aliona jinsi mpango wao ulivyokuwa ukienda kombo. Alimshirikisha kiongozi Ibrahim Shadidy kila hatua aliyopiga pasipo mafanikio. Walipatwa na kigugumizi katika harakati zao. Mwanzo matamasha yao yaliegemea kusaka vipaji wilayani, walitegemea ikifika zamu ya wilaya ya Rwama Mjini wataweza kumuona Nasrat Abdul al Aziz akishiriki lakini hali haikuwa hivyo. Hawakufa moyo waliendelea kusaka vipaji wilaya zote za mkoani Rwama Mwanzo, walipomaliza kuwakusanya washiriki wote wa kila wilaya, ikatangazwa siku ya fainali ya kumtafuta Miss Rwama Mwanzo na mwanamitindo bora wa mkoa huo. Upande wa mwanamitindo iliwahusisha wasichana na wavulana.

Siku ilifika, ukumbi wa Rwama hoteli uliotumika katika tamasha hilo ulijaa sana, watu toka mikoa mbalimbali walifurika kuona nani atafanikiwa kushinda taji la Miss Rwama Mwanzo na wanamitindo bora wa mkoa huo. Miongoni mwa watu hao alikuwemo Nasrat Abdul al Aziz. Nasrat Abdul al Aziz alienda kutazama mashindano yake huku moyo ukimuuma sana, siyo kwamba moyo ulimuuma kwa kupenda, hapana, moyo ulimuuna kwa sababu aliamini hakujitendea haki kwa kutoshiriki mashindano hayo makubwa mkoani huo. Siyo kwamba hakupenda kushiriki, la hasha, bali ratiba zake za uuzaji na ushambazaji wa madawa ya kulevya ndizo zilizoingiliana na ratiba za mashindano hayo. Hivyo basi, ikamlazimu kutimiza majukumu yake aliyoachiwa na marehemu baba yake, suala la ulimbwende na mitindo lilikuwa mwamvuli wa kufichia maovu yake.

Shindalo lilipamba moto huku wasanii wa mkoani Rwama Mwanzo wakipewa nafasi ya kuwaburudisha watazamaji waliofika mahali pale. Miongoni mwa wana sanaa waliopewa nafasi ya kupanda jukwaani alikuwa Derrick Edward. Alipendeza sana siku hiyo, aling`aa kama kijana aliyekuwa kwenye mashindano ya mitindo. Awali kila mtazamaji alifikiri ni mwanamitindo lakini walipomtazama vizuri waligundua alikuwa wana sanaa ya uchoraji na uchongaji mkoani humo. Derrick Edward aliwasalimia watu wote kisha akajielezea kama jinsi alivyokuwa akifanya katika matamasha na mashindano mengine yaliyokuwa chini ya Daniel Magesa.

Baada ya salamu alimpandisha kijana aliyekuwa ameshika picha kubwa mkononi pamoja na kinyago kilichochongwa kwa mbao aina ya mninga. Ilikuwa ni kawaida kwa Derrick Edward kupanda jukwaani kujitambulisha kisha kumpandisha kijana wake mwenye kazi zake za mikono, kijana yule alimkabidhi kazi zile kisha akashuka. Derrick Edward akawaonesha waliohudhuria eneo lile. Kila mmoja hakuamini uchoraji ule wenye viwango vya juu, alichora picha ya mpigania uhuru wa nchini India anayefahamika kwa jina la Mahatma Gandhi. Chini ya picha hiyo aliandika moja ya msemo maarufu wa Mahatma Gandhi, msemo uliosema

“Hate the sin, love the sinner” (Chukia dhambi, mpende mtenda dhambi)

Vile vile aliwaonesha kinyago alichochonga, hakikuwa kinyago cha mtu mwingine bali kilikuwa cha yule yule mwana harakati wa nchini India, Mahatma Gandhi. Picha iliyochongwa haikuwa tofauti hata kidogo na picha iliyochorwa. Ilikuwa picha ile ile, utofauti ulikuwa mahali ilipowasilishwa na ujumbe ulioambatanishwa. Picha iliyochongwa kinyago iliambatanisha na msemo mwingine maarufu wa mwana harakati yule wa nchini India, msemo uliosomea

“Where there is love, there is life” (Palipo na upendo, kuna maisha)

Baada ya kutambulisha kazi zake, alishuka jukwaani. Umati ulipiga makofi ya kuafiki kipaji chake, miongoni mwa watu waliopiga makofi kwa nguvu alikuwemo Nasrat Abdul al Aziz. Nafikiri Nasrat Abdul al Aziz alifurahishwa zaidi na kazi za Derrick Edward kwa sababu hakuishia kuangalia picha na kinyago tu bali hata ile misemo ilimaanisha kitu kwake, hasa msemo uliokuwa kwenye picha ya iliyochorwa. Alijiona mwenye dhambi lakini aliyehitaji kupenda na kupendwa. Ingawa Derrick Edward alikuwa maarufu lakini umaarufu wake ulikuwa haujafika kwenye kichwa cha Nasrat Abdul al Aziz. Nasrat Abdul al Aziz alikuwa akisikia taarifa zake lakini hakuna siku hata moja aliyoshawishika kumfahamu mtu huyo kwa sababu walikuwa ni watu wawili tofauti. Nasrat Abdul al Aziz hakuona umuhimu wa kumfahamu mchoraji na mchongaji wakati yeye sanaa yake haikuwa upande huo.

Siku hiyo baada ya kumuona Derrick Edward jukwaani aliona jinsi alivyokuwa akijiongopewa, aliuona uwezo wa ajabu katika mikono ya kijana aliyevutia kuanzia sura mpaka mavazi. Alihisi akihitaji kumfahamu zaidi Derrick Edward. Nasrat Abdul al Aziz alisimama toka mahali alipokaa akaanza kuangaza kwenye meza moja baada ya nyingine akimtafuta Derrick Edward. Vijana kwa wazee wa makamo walimshangaa kwa urembo alikuwa nao, hakuuficha urembo huo kwa sababu alivaa nguo fupi iliyoonesha sehemu kubwa ya mapaja yake. Hakujali macho ya watu, yeye aliendelea kumuangaza Derrick Edward. Vijana wenye tamaa za kimwili walijaribu bahati yao kwa kumsimamisha ili wapate walau hata namba yake ya simu lakini hali ilikuwa tofauti, hakugeuza hata shingo kuwatazama. Alifanikiwa kumuona Derrick Edward akiwa na kijana wake katika meza moja iliyojitenga kabisa na umati ule, Nasrat Abdul al Aziz alipiga hatua mpaka mahali pale kisha akasalimia kwa sauti nyonyoro

“Habarini”

Sauti yake ilipenya barabara katika masikio ya vijana waliokuwa wamezunguka meza ile. Awali Derrick Edward hakumuona Nasrat Abdul al Aziz na alifikiri binti ule wa Kiarabu hakuwa miongoni mwa watu waliohudhuria siku hiyo kama alivyofanya katika matamasha yaliyopita. Suala la Derrick Edward kumuona Nasrat Abdul al Aziz hasa akiwa mbele ya meza yake lilimchanganya zaidi, akabaki kamkodolea macho kama mtu aonavyo jambo la ajabu. Nasrat Abdul al Aziz alielewa Derrick Edward hakuamini kuona mrembo yeye amemfuata kwenye meza yake, aliamini hivyo kwa sababu wanaume wote waliojaribu kumjumuisha katika meza zao walishindwa kumpata. Hakika Nasrat alielewa tofauti, na hayo hayakuwa mawazo ya Derrick Edward, mpelelezi aliyevaa kalamu ya uchoraji na uchongaji. Nasrat Abdul al Aziz akavunja ukimya baada ya kuona hajibiwi na wenyeji wake

“Samahani, naweza kukaa?”

Lilikuwa swali la ajabu katika masikio ya Derrick Edward, alitamani akubali haraka lakini akili yake ilikuwa bado ikikinzana kuamni kama aliyekuwa mbele yake ni Nasrat Abdul al Aziz, msichana aliyemtega kwa muda mrefu pasipo mafanikio. Kijana aliyekuwa meza moja na Derrick Edward alivyoona hali ya bosi wake akaamua kuchukua maamuzi ya kumkarimu mgeni wao. Kijana yule aliyefahamika kwa jina la Nasibu Kaoneka aliongea kwa sauti ya heshima

“Waweza kukaa mrembo”

Hakika hakukosea kumuita mrembo, alikuwa mrembo hasa mwenye ngozi ya Kiarabu na umbile la Kibantu. Nasrat Abdul al Aziz alikaa kwenye kiti, katikati ya vijana wale kisha akamtazama Derrick Edward aliyekuwa upande wake wa kulia kisha akamwambia

“Naitwa Nasrat Abdul al Aziz, jina langu ni ndefu kidogo lakini waweza kiita Nasrat kupunguza msongamano wa maneno”

Baada ya kauli hiyo iliyojaa utani akaachia tabasamu mororo, tabasamu lile lilikuwa kama kilevi kwa Derrick Edward, aliamini anaelekea kushindwa kufanya kazi iliyompeleka Rwama Mwanzo, aliona namna moyo wake ulivyoanza kumpokea Nasrat Abdul al Aziz haraka kwa kasi ya ajabu. Aliiambia akili yake itulie ili ifanye kazi. Derrick Edward akatulia na akili yake ikarudi mahala pake, akajitambulisha kama alivyojitambulisha jukwaani kisha akamtambulisha kijana wake. Hawakuwa na maongezi mengi, la hasha, bali Nasrat Abdul al Aziz alimwambia Derrick Edward kuwa anahitaji kumfahamu zaidi. Derrick Edward hakuwa na kikwazo chochote, walibadilishana namba za simu kisha Nasrat Abdul al Aziz akatimka zake. Alisindikizwa na macho ya Derrick Edward mpaka alipotokomea katika umati wa watu waliohudhuria. Kila mmoja alibaki na mawazo yake kichwani, Nasrat Abdul al Aziz alimfikiria Derrick Edward kama mwanaume aliyekuwa akimtafuta, mwanaume wa sifa zake. Upande wa Derrick Edward hakuisha kuusifia uzuri wa Nasrat Abdul al Aziz mbele ya Nasibu Kaoneka, hakika alimsifia kuanzia utosi mpaka unyayo wa miguu. Siku mbili zilipita pasipo Nasrat Abdul al Aziz kumtafuta Derrick Edward. Derrick Edward alitamani kumpigia simu lakini moyo wake ukamsisitiza

“Subiri akutafute, yeye ndiye aliyesema ana shida ya kukufahamu zaidi”

Akili ya Derrick Edward ikamkumbusha dhumuni la yeye kwenda Rwama Mwanzo, hakika alikumbuka alikuwa mkoani humo kwa lengo la kuchunguza nyendo za Nasrat Abdul al Aziz. Sasa aliamini akisubiri mpaka atafutwe atakuwa hafanyi kazi yake. Akachukua simu kisha akatafuta namba ya Nasrat Abdul al Aziz kisha akapiga, simu iliita na ndani ya sekunde chache ikapokelewa

“Hallo Derrick”

Derrick aliitikia salamu ya Nasrat Abdul al Aziz lakini kabla hajaongeza kauli yoyote Nasrat Abdul al Aziz aliendelea kufafanua ukimya wake

“Samahani sana Derrick, nilikuwa bize kidogo na mambo yangu…leo nakualika uje kwangu kula usiku kama hutojali. Nitafurahi ukifika”

Mapigo ya moyo wa Derrick Edward yakaongeza kasi maradufu, alihisi kama ndoto kukaribishwa chakula cha usiku katika nyumba ya mrembo yule, alihisi kumpenda lakini alipofikiria kazi aliyotumwa akakinzana na upendo huo. Hakuwa na kipingamizi chochote zaidi ya kukubali kwenda katika nyumba ya mrembo wa Kiarabu, aliamini atakuwa amepiga hatua kubwa katika upelelezi wake dhidi ya mrembo huyo. Waliongea mengi lakini yote yaliegemea namna ya Derrick Edward atakavyoweza kufika katika nyumba ya Nasrat Abdul al Aziz. Derrick Edward hakuyafahamu yalipokuwa makazi ya Nasrat Abdul al Aziz, hivyo basi Nasrat Abdul al Aziz alimwambia ataenda kumchukua ofisini kwake. Nasrat Abdul al Aziz hakutaka kumtuma mtu yeyote kumchukua Derrick Edward. Hakuhitaji kujitangaza kuwa atakuwa na mwanaume nyumbani kwake. Derrick Edward ndiye aliyependekeza afatwe ofisini kwake kwa sababu hakutaka Nasrat Abdul al Aziz afahamu alipokuwa akiishi. Ilikuwa kawaida kwa Derrick kufunga ofisi yake ya sanaa saa mbili mpaka tatu usiku, hivyo basi suala la kumwambia Nasrat Abdul al Aziz amfuate ofisini kwake baada ya kumuelekeza mahali ilipokuwa lilikuwa sahihi kwake.

Masaa yalisogea kama yakisukumwa, ilipofika saa moja jioni giza la usoni lilikuwa limeanza kuweka kiwingu katika macho ya watu, lakini giza hilo halikuwa kitu katika ofisi ya Derrick Edward kwa sababu mataa ghari yaliendelea kutoa mwanga wa kutosha. Gari dogo aina ya Toyota Tudra lilisimama jirani kabisa ya ofisi ya Derrick Edward kisha akashuka msichana aliyevaa mavazi yaliyoficha kabisa muonekano wake, alivaa vazi maarufu ambalo huvaliwa na wanawake au wasichana wengi wenye imani kali ya dini ya kiislamu, alivaa Niqab, hivyo basi hakuna mtu aliyeweza kufanikiwa au kutambua aliyeshuka garini alikuwa nani. Vazi lilikuwa ndefu likafunika mpaka miguu yake, kitu pekee kilichoonekana katika mwili wake yalikuwa macho tu. Msichana yule alienda moja kwa moja mpaka ndani ya ofisi ya Derrick Edward pasipo kupiga hodi, alimkuta mwana sanaa akichora picha ya mwanamke. Mwana sanaa alikuwa amempa mgongo akiendelea na shughuli yake kama kawaida. Derrick Edward hakufanikiwa kumuona msichana yule kipindi akipoingia, vile vile hakufanikiwa kusikia hata sauti iliyozalishwa na gari kipindi alipofika kwa sababu ya mziki uliokuwa ukizalishwa na redio ofisini kwake.

Kwakuwa Derrick alikuwa amempa mgongo mgeni wake aliyeingia kimya kimya hivyo basi mgeni yule alifanikiwa kuiona vizuri picha iliyokuwa ikichorwa na Derrick Edward. Kitendo cha kuiona picha ile kilimuongezea umakini na udadisi wa kuendelea kuitazama ili kujihakikishia alichokiona. Hakika alikuwa sahihi, ilikuwa picha yake akiwa kwenye mavazi aliyovaa siku ya kwanza aliyokutana na mchoraji huyo katika ukumbi wa Rwama Mjini. Nasrat Abdul al Aziz alizidi kukubali kuwa Derrick Edward alikuwa na kipaji cha ajabu sana kwa sababu siku ile hakupiga naye picha yoyote hivyo basi Derrick Edward alikuwa akichora picha yake kutoka kwenye taswira aliyoihifadhi siku ile waliyoonana ana kwa ana. Nasrat Abdul al Aziz alishindwa kuvumilia, akaamua kuvunja ukimya kwa kuuliza swali pasipo kusalimia

“Huyo unayemchora ni mimi?”

Kauli hiyo ilimshitua sana Derrick Edward, aligeuka haraka akakutana na muonekano alioshindwa kuutambua lakini alijihakikishia alikuwa mwanamke. Alitambua hilo kwa sababu ya maumbile na mavazi aliyovaa mgeni wake aliyekuwa amesimama wima kama mlingoti wa umeme. Sauti haikuwa ngeni lakini alishindwa kujihakikishia kuwa ilikuwa ya nani. Aliweka vifaa vyake chini kisha akasimama wima kama mgeni wake alivyokuwa, akamjibu

“Kama wewe ni Nasrat Abdul al Aziz hakika u wewe katika picha hii, lakini kama siyo Nasrat Abdul al Aziz hakika siyo wewe katika picha”

Ilisikika sauti nyororo ikicheka, sasa Derrick Edward alijihakikishia alikuwa ni Nasrat Abdul al Aziz, mrembo wa Kiarabu mwenye umbile la Kibantu. Pasipo kuchelewa akaendelea na maongezi yaliyohitaji ufafanuzi

“Umenishitua sana Nasrat, nimeshangaa kusikia sauti ikiongea nyuma yangu. Kwanini lakini umeingia kimya kimya? Utakuja kuniua kwa presha”

Derrick Edward akaachia tabasamu, lilikuwa tabasamu la kinafiki kwa sababu hakujisikia kucheka lakini aliamua kujilazimisha ili ionekane alikuwa kwenye hali nzuri ya kimwili na akili. Derrick Edward alikuwa na hofu kubwa akitafakari kipi alitakiwa kutekeleza kati ya kazi na mapenzi, aliona mapenzi yakiwa na nguvu zaidi ya kazi lakini alijilazimisha kuwa lazima atekeleze kazi kwa manufaa ya taifa nzima la Malosha. Nasrat Abdul al Aziz hakujibu swali la Derrick Edward bali aliongea

“Yatupasa kuondoka sasa hivi kabla hajaingia mgeni mwingine”

Derrick Edward akamtazama Nasrat Abdul al Aziz aliyekuwa akionekana macho pekee kisha akamwambia

“Ngoja nijiweke sana kidogo, nipunguze uchafu wa rangi mwilini”

Nasrat Abdul al Aziz hakupepesa macho hata kidogo, alimtazama Derrick Edward moja kwa moja usoni kisha akaongea kauli iliyozua taharuki katika masikio ya Derrick Edward, Nasrat Abdul al Aziz alisema

“Unahisi kwangu hakuna maji ya kujisafisha? Utaoga, utakunywa na hata ukitaka kulala utalala”

Derrick Edward aliona namna Nasrat Abdul al Aziz alivyodhamiria kumteka kimapenzi. Aliamini huko aendako hakuna ukaka na udada bali kuna asilimia kubwa ya kuanza kwa mahusiano mapya ya kimapenzi. Picha ya urembo Nasrat Abdul al Aziz akiwa kwenye mavazi ya kichokozi ikamjia kichwani, akajithibitishia urembo wa msichana yule. Kichwa cha Derrick Edward kikawa kizito. Akahisi endapo akiacha kutimiza matakwa ya Nasrat Abdul al Aziz atakuwa ameacha kutimiza matakwa ya moyo wake, alijisemea moyoni

“Potelea mbali, kila kitu kitafahamika mwisho wa safari”

Alikubali kauli ya Nasrat Abdul al Aziz. Akafunga ofisi yake, wakapanda ndani ya gari la Nasrat Abdul al Aziz kisha safari ya kuelekea Bungero kwenye makazi ya Nasrat Abdul al Aziz ikaanza. Ilikuwa safari ya kimya kimya, kila mmoja akitafakari juu ya yatakayoenda kutokea mbele ya safari. Baada ya robo saa walifika katika nyumba ya Nasrat Abdul al Aziz. Kama kawaida Nasrat Abdul al Aziz alishuka garini akafungua geti la nyumba yake kisha akarudi ndani ya gari na kuingia uwani. Nyumba haikuwa na mlinzi kwa kipindi hicho. Derrick Edward alishangaa kupokelewa na nyumba ya kifahari. Alibaki akijiuliza maswali mengi sana, maswali yote yalihusu umiliki wa nyumba hiyo. Aliona siyo rahisi kwa binti mdogo kama Nasrat Abdul al Aziz anayejihusisha na masuala ya urembo wa ulimbwende kumiliki nyumba ya gharama kama ile, alijihakikishia kuwa lazima nyuma ya pazia atakuwa akijihususha na mambo mengi ya siri.

Sasa aliamini kauli ya bosi wake, kauli iliyomshuku Nasrat Abdul al Azi kuwa mwanachama wa wauzaji na wasambazaji wa madawa ya kulevya nchini huo. Mshangao haukuishia kwenye uzuri wa nje wa nyumba hiyo bali mpaka ndani. Alikutana na thamani za kutosha. Sebule ilipambwa ikapambika haswa. Picha za wanamitindo na walimbwende wa ndani na nje ya nchi ya Malosha zilitapakaa ukutani. Kitendo kile kilimuaminisha Derrick Edward kwa asilimia mia moja kuwa Nasrat Abdul al Aziz ni mwanamitindo haswa. Mitindo na ulimbwende vipo ndani ya damu yake lakini haikumaanisha kuwa hajihusishi na biashara haramu ya madawa ya kulevya. Derrick Edward alikaribishwa kwenye kiti kisha kauli nyororo ya Nasrat Abdul al Aziz ikaongea, kauli ya kumtoa nyoka pangoni

“Nafikiri ukaoge kwanza ndiyo mambo mengine yafuate, kumbuka umetoka ofisini ukiwa hujajiandaa kwa chochote”

Derrick Edward alihisi akiota, aligeuza kichwa akamtazama Nasrat Abdul al Aziz aliyekuwa bize akivua Niqab yake. Alivua akabaki amevaa suruali ya jinzi iliyomchonga maumbile yake ya kichokozi, juu alibakia amevaa tisheti nyepesi iliyochonga maumbile ya matiti yake. Hakika alidhamiria kuchukua umakini wa Derrick Edward. Derrick Edward aliweweseka akakosa jibu la kutoka. Macho yake yaliendelea kuukagua mwili wa mrembo aliyekuwa mbele yake akimkodolea macho malegevu. Akili ya Derrick Edward iliwaza mbali sana, akafikiria labda Nasrat Abdul al Aziz ameshatambua kuwa alipenyezwa mkoani Rwama Mwanzo ili ampeleleze ndiyo maana anaamua kumfanyia vimbwanga ili aingie katika mtego wake. Lakini akili hiyo hiyo ilikataa katakata ikiamini Nasrat Abdul al Aziz haelewi chochote kuhusu ujio wake. Wazo la pili ndilo alilolipa nguvu, alijikuta akizama kwenye mtego wa mapenzi wa Nasrat Abdul al Aziz. Alijikuta akitabasamu pasipo kufahamu.

Moyo ulihisi kupata sehemu sahihi ya kupumzika. Hakuna alichobisha, alipelekwa bafuni akaoga kisha akapelekwa chumbani kwa ajili ya kubadilisha nguo. Alikuta nguo mpya kitandani, hapo ndipo alipoamini Nasrat Abdul al Aziz alijiandaa kumkarimu kimwili na kiakili. Alivaa kisha wakaanza kuongea, maongezi yao yaliegemea maswala ya mapenzi na siyo kazi, waliongea mengi sana yaliyopelekea kulala kitanda kimoja mpaka asubuhi. Derrick Edward hakuamini alichoshudia usiku ule, alihisi kuokota embe dodo mchangani. Alichanganywa zaidi na kauli za binti yule, kauli zilizomsisitiza kuwa amemuamini awe mwanaume wa maisha yake. Kichwa cha Derrick Edward kilijaa mawazo kikaanza kukinzana na majukumu aliyopewa, kichwa kilimuuma sana akahisi kama ameibeba dunia. Mwisho wa siku aliamini maamuzi aliyoyachukua awali yalikuwa sahihi, maamuzi ya kumpenda Nasrat Abdul al Azizi kwa kila hali. Alijisemea moyoni

“Nitamchunguza kimya kimya mpaka nielewe kila kitu anachohusishwa nacho, lakini sidhani kama kuna ukweli ndani yake”

Penzi jipya lilichanua kwa kasi, haikuwa siri tena walipendana kichwa kuuma lakini kila mmoja alikuwa na mawazo ya kazi yake, yalikuwa mawazo tofauti kwa sababu hata kazi zao zilikuwa tofauti. Kipindi Derrick Edward akimchunguza kimya kimya Nasrat Abdul al Aziz na yeye alikuwa akimchunguza kimya kimya na Nasrat Abdul al Aziz ili ajiridhishe kama alikuwa kwenye mikono salama. Ilikuwa vita baridi, vita ya wapenzi waliopendana kwa dhati. Japokuwa Nasrat Abdul al Aziz alimpenda kwa dhati Derrick Edward lakini haikumaanisha alikuwa tayari kumuelezea Derrick Edward kila kitu kilichozunguka maisha yake, alitaka amsogeze karibu zaidi ili apime kama angeweza kumuingiza katika mfumo wake wa madawa ya kulevya au aendelee kuishi naye kimya kimya mpaka siku atakayopata ufumbuzi yakinifu. Kuna kipindi alihisi kujuta kumuamini sana Derrick Edward mkapa akampa mamlaka ya mwili wake, mamlaka yaliyompa uhuru Derrick Edward kutimiza haja zake za mapenzi kama mke amtimiziavyo mume wake.

Upande wa Derrick Edward hali iliendelea kuwa mbaya zaidi hasa alivyofikiria maagizo ya mkuu wake wa kazi, kiongozi Ibrahim Shadidy. Alihisi kuchanganyikiwa. Siku hadi siku alizidi kumpenda Nasrat Abdul al Aziz, walistarehe kila walipohitaji kufanya hivyo. Penzi la Nasrat Abdul al Aziz lilipumbaza kabisa akili ya Derrick Edward, akili ikalala usingizi wa pono. Derrick Edward akaona kazi aliyopewa ilikuwa haina maana yoyote. Kwakuwa alikuwa mtu maarufu taarifa za uhusiano wake zilisambaa kwenye vichwa vya watu ingawa Nasrat Abdul al Aziz hakuwa mzungumzaji wa jambo hilo. Mapenzi yao ilikuwa furaha kubwa kwa mkuu wa kazi wa Derrick Edward, kiongozi Ibrahim Shadidy. Aliamini mpango aliopanga na kijana wake lazima utimie, mpango waliokubaliana kuwa lazima Derrick Edward atafute namna ya kumpata kimapenzi Nasrat Abdul al Aziz ili aweze kumchunguza vizuri.

Hakika mpango ulikuwa umefanikiwa kwa asilimia mia moja, lakini mpango huo uliingia dosari ambayo awali hawakuifikiria kabisa. Dosari hiyo ilisababisha Derrick Edward atoe taarifa za uongo kila alipoulizwa na mkuu wake wa kazi, Derrick Edward alikuwa akimwambia mkuu wake kuwa hajaona kitu chochote kinachoweza kumuunganisha au kumuhusisha Nasrat Abdul al Aziz na masuala ya madawa ya kulevya. Lakini haikuwa kweli, Derrick Edward hakumchunguza wala kumpeleleza kwa undani zaidi mpenzi wake, hakutaka kujua kitu chochote ambacho kingeweza kuleta dosari katika penzi lao. Alijikuta akichunguza masuala ya mahusiano tu na siyo masuala ya kazi aliyotumwa na kiongozi wake. Hakika aliamua kuisaliti kazi aliyotumwa, alijisemea moyoni

“Acha nifurahie maisha na penzi la Nasrat”

Kwakuwa Derrick Edward hakujihusisha kwa undani zaidi juu ya suala la kumchunguza mpenzi wake hivyo basi hata Nasrat Abdul al Aziz baada ya kumpeleleza sana Derrick Edward hakupata jawabu lolote ambalo lingeweza kumpa mashaka au walakini, alimuona Derrick Edward akiwa mwanasanaa mwenye mipango mikubwa sana na sanaa yake. Suala hilo lilimpa moyo na furaha sana Nasrat Abdul al Aziz. Aliapa moyoni na mbele yake kuwa lazima apambane juu chini kutimiza ndoto za mpenzi wake. Suala la pesa za Nasrat Abdul al Aziz halikuwa kikwazo sana kwa Derrick Edward kwa sababu Nasrat Abdul al Aziz alimuaminisha kuwa alirisishwa pesa hizo na marehemu baba yake aliyekuwa akifanya biashara za madini. Derrick alioneshwa baadhi ya nyaraka zilizoonesha uhalisia kuwa mzee Abdul al Aziz alikuwa mfanya biashara mkubwa wa madini barani Afrika.
Nasrat Abdul al Aziz alionesha upande mmoja wa marehemu baba yake, upande wa biashara ya madini aliokuwa akiutumia kama kiini macho mbele ya jamii na maafisa wa serikali.

Nasrat Abdul al Aziz alidhamiria kumdanganya Derrick Edward, hakika alifanikiwa kufanya hivyo. Mapenzi yakamtia upofu Derrick Edward, akaamini kila kauli ya mpenzi wake na kuona jinsi alivyokuwa akihusishwa na masuala ya madawa ya kulevya. Kuna kipindi alitamani amwambie kuwa yeye ni afisa wa serikali wa siri aliyeingizwa mkoani humo kwa lengo la kumchunguza lakini akaona wakati wa kumwambia haujafika, alitamani kumwambia hivyo baada ya kujihakikishia kuwa Nasrat Abdul al Aziz hahusiki kabisa na mtandao wa wauzaji na wasambazaji wa madawa ya kulevya katika nchi ya Malosha.
Suala la upofu wa Derrick Edward lilimpa mashaka sana mkuu wake wa kazi, kiongozi Ibrahim Shadidy alihisi kuna kitu hakikuwa sawa kwa kijana wake aliyemuamini siku zote mpaka akaamua kuingiza kwenye mpango wa siri. Alihisi Derrick Edward akimficha baadhi ya mambo kuhusu Nasrat Abdul al Aziz, aligundua hivyo baada ya kumpatia kazi Daniel Magesa kufatilia nyayo za Nasrat Abdul al Aziz.

Daniel Magesa alifatilia nyayo za Nasrat Abdul al Aziz chini ya kivuli chake kile kile cha kuanzisha matamasha makubwa ya ulimbwende na urembo. Katika baadhi ya matamasha hayo alimshuhudia Nasrat Abdul al Aziz akifanya mazungumzo ya siri na watu waliokuwa wakiwafatilia kwa kuwahusisha na biashara haramu ya madawa ya kulevya. Hawakuwa wengine bali alikuwa Amani Collence na wenzake. Daniel Magesa aliwasilisha taarifa hiyo kwa kiongozi wake wa kazi, mkuu wa kazi akamwambia aendelee kufatilia nyayo za Nasrat Abdul al Aziz. Hakika alifanikiwa kushuhudia namna Nasrat Abdul al Aziz alivyofanya biashara haramu na kundi la Amani Collence kisha akawageuka na kuchukua kila kitu. Alishuhudia namna Nasrat Abdul al Aziz na vijana wake walivyochukua pesa na mzigo wa madawa ya kulevya mbele ya kundi la Aman Collence kisha wakaondoka eneo la tukio. Taarifa hiyo iliibua maswali mengi katika kichwa cha mkuu wa kazi wa Derrick, bwana Ibrahim Shadidy, alijiuliza maswali

“Kwanini Derrick ashindwe kufahamu uchafu wa Nasrat wakati yupo naye karibu zaidi? Kwanini Daniel Magesa amefanikiwa kufahamu mambo mengi ndani ya muda mfupi? Kwanini…Nafikiri Derrick atakuwa amenasa kwenye mtego wa mapenzi tuliomtegea Nasrat”

Kiongozi Ibrahim Shadidy na Daniel Magesa walikubaliana wamfatilie Derrick Edward kimya kimya kwa lengo la kubaini kama ameingizwa kwenye biashara haramu ya madawa ya kulevya. Mipango ya kazi ikabadilika, Derrick Edward akawa hapewi maelekezo yoyote na mkuu wake wa kazi, akili ikamtuma labla kiongozi Ibrahim Shadidy ameelewa maelezo yake. Alifurahi sana na kuamini uongo wake umekuwa ukweli kwenye akili ya mkuu wake. Hakujua alikuwa akijidanganya mwenyewe, hakujua alikuwa akitafutiwa mtego utakao muweka mtu kati na kukosa pa kukimbilia, hakujua alikuwa akitazamwa kama msaliti. Hakika hakujua kilichokuwa kikiendelea dhidi yake.

ITAENDELEA
1982132253.jpg
 
RIWAYA: MATEKA
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890

(KIPANDE CHA SITA)

Upepo wa kiangazi uliendelea kuchafua mazingira, ulichukua takataka toka sehemu moja na kupeleka sehemu ya pili. Hali hiyo haikuwapendeza raia wengi wa mkoa wa Rwama Mwanzo hasa akima mama waliokuwa na majukumu ya kudumisha usafi majumbani kwao. David Samson alikuwa ndani ya gari alilokabidhiwa na Nasrat Abdul al Aziz ili afanyie mizunguko ya kukamilisha kazi aliyompatia Derrick Edward. Lilikuwa gari la Zimwi lakini hakutambua hilo, yeye alijua lilikuwa gari la Nasrat Abdul al Aziz. Nasrat Abdul al Aziz alimkabidhi gari la Zimwi kwa sababu alihofia akimpa gari lake lazima Derrick Edward angelifahamu na kutilia shaka zaidi.

David Samson alikuwa njiani akirudi kwa Nasrat Abdul al Aziz baada ya kukabidhiwa kazi na mwana sanaa wa ajabu. Akilini kwake alikuwa akifikiria safari iliyokuwa mbele yake, safari ya kuelekea nchini Afrika Kusini kwa mzee Masiya.
Hakuwa mbishi kwenda kwa sababu aliamini akithubutu kufanya hivyo atakuwa amehalalisha kifo cha mtoto pamoja na mpenzi wake. Aliendesha gari huku machozi ya hasira yakimtoka. Aliamini akifika Afrika Kusini lazima apokelewe kama mfalme kwa sababu mzee Masiya pamoja na kundi la Amani Collence litaamini limefanikiwa kumuhadaa Nasrat Abdul al Aziz, hakika alichokiwa ndicho kilichokuwa kikifikiriwa na mzee Masiya na Amani Collence. Wao waliamini ulikuwa mpango madhubuti wa kumtokomeza Nasrat Abdul al Aziz, hawakujua mpango huo ulikuwa hatari kwao. Hawakujua silaha waliyokuwa wakiitumia kumteketeza Nasrat Abdul al Aziz ilikuwa imeelekea kwao, ilikuwa tayari kuwateketeza wenyewe. Hawakujua David Samson alipandikizwa kuwapeleleza.

Upande wa pili, Derrick Edward alikuwa akimfikiria mteja wake aliyempatia picha na kinyago chenye taswira ya mzee Masiya, mfanya biashara nguli wa madawa ya kulevya aliyejificha kwenye kivuli cha siasa. Alihisi kuna uwezekano mkubwa wa mteja huyo kujihusisha na madawa ya kulevya au kuwa kwenye mipango ya mzee Masiya. Derrick Edward alipanga kutambua hilo. Alipachika ‘microchip’ ndani ya kinyago alichochora, lengo la kuweka ‘macrochip’ lilikuwa ni kufahamu kila kitu kitakachoendelea. ‘Microchip’ huweza kuchukua mawimbi ya sauti pamoja na picha za watu au vitu vilivyo zaidi ya kifaa hicho.
Baada ya kufanikiwa kupachika ‘microchip’ alielewa fika kuwa lazima atafahamu kama mteja wake ni mwema au anajihusisha na biashara haramu.

Japokuwa hakujihusisha na masuala ya kumchunguza mpenzi wake lakini haikumaanisha aliacha kuwachunguza watu wengine aliohisi walihusika kwa namna moja au nyingine katika biashara haramu za madawa ya kulevya. Vile vile, hakuchoka kutoa taarifa za watu hao kwa mkuu wake wa kazi, bwana Ibrahim Shadidy. Baadhi ya taarifa alizompatia mkuu wake wa kazi zilipofatiliwa zilionekana kuwa na ukweli asilimia mia moja. Suala hilo lilimchanganya sana kiongozi Ibrahim Shadidy, kwa sababu aliona juhudi ya Derrick Edward katika jukumu wa kuwafichua wahalifu wa madawa ya kulevya. Hakika kiongozi Ibrahim Shadidy alibaki njia panda, na kichwa chake kilizidi kutengeneza maswali mengi siku hadi siku.
Derrick Edward alikuwa hafahamu kama David Samson alitumwa na Nasrat Abdul al Aziz, hakujua kuwa suala la picha zile liliratibiwa na mpenzi wake aliyemuweka kwenye mpango wa siri wa kufunga naye pingu za maisha. Ulikuwa mpango wa siri kwa sababu hakumshirikisha mkuu wake mpango huo.

Ulikuwa mpango wake na Nasrat Abdul al Aziz, walipanga kufunga ndoa ya Kiserikali ili kuepuka kikwazo cha dini na vizuizi vya jamii iliyowazunguka. Walikuwa kwenye mipango mizito ya kuishi pamoja lakini hawakujua nyuma ya mipango yao kulikuwa na mipango dhidi yao. Derrick Edward aliamini akimshirikisha mkuu wake angeweza kuzua taharuki na maswali mengi yasiyokuwa na majibu sahihi, alifanya siri.
Wakati David Samson akiendelea kusonga barabara ya kuelekea kwa Nasrat Abdul al Aziz ili akabidhi kazi iliyotoka kwa Derrick Edward hakujua kama alikuwa akifuatiliwa muelekeo wake, Derrick Edward alikuwa amefunga ofisi yake huku macho yake yakiwa kwenye kompyuta aliyoiunganisha na ‘macrochip’ aliyoipandikiza kwenye kinyago alichompatia David Samson. Alikuwa makini akifatilia uelekeo wa David Samson. Alitega mtego sahihi lakini hakujua alikuwa akimtega nani, hakujua nyuma ya David Samson kulikuwa na sura ya msichana mrembo mwenye akili kama mchwa. Hakujua mtego alioutega ulimkamata mwenyewe. Hakika, Derrick Edward hakujua alijichimbia shimo mwenyewe.

Nasrat Abdul al Aziz alikuwa makini sana na kazi yake, kwakuwa hakumuamini David Samson tangu siku ya kwanza aliyomteka kisha kumpeleka katika kundi la Amani Collence kwa ajili ya kuwachunguza lakini hali ikawa tofauti kwa sababu David Samson alirudishwa katika ngome yake kama mtoto wa mzee Masiya. Kitendo kile kilimpa hofu sana Nasrat Abdul al Aziz, japokuwa alihisi ni ushindi upande wake lakini hakuamini kwa asilimia mia moja. Aliamini hata David Samson anaweza kuwa msaliti kwa namna moja ama nyingine ili ampate mtoto wake. Hivyo, aliandaa namna ya kumdhibiti David Samson pamoja na mtandao wote uliomzunguka. Nasrat Abdul al Aziz alipachika ‘macrochip’ katika simu ya David Samson pasipo David Samson kufahamu lolote, kitendo kile kilimuwezesha kufahamu kila hatua aliyoipiga David Samson.

Vile vile kiliweza kunasa sauti na kupiga picha za maeneo aliyotembelea. Ilikuwa ngao kwa Nasrat Abdul al Aziz, ngao ya kumdhibiti mtumishi wake aliyemtilia mashaka. Kipindi David Samson alipokuwa akikabidhiwa kazi alizompa Derrick Edward hakuelewa mchezo aliokuwa akiufanya Derrick Edward. Derrick Edward alikuwa kategesha simu yake katika kona nzuri, simu ilichukua video namna alivyokuwa akimkabidhi David Samson picha na kinyago cha mzee Masiya. Haikuishia kuchukua video hiyo tu, la hasha, bali ilifanikiwa kuchukua mazungumzo yote yaliyofanyika kipindi cha makabidhiano.

Kabda siku hiyo kufika, Nasrat Abdul al Aziz alikuwa ameshaandaa mtego mwingine wa kujihakikishia usalama wake, alimuandaa kijana wake amfatilie David Samson kimya kimya ili ashuhudie zoezi zima la makabidhiano, aliona ‘microchip’ aliyoweka kwenye simu ya David Samson haitoshi kukamilisha uchunguzi wake. Aliona ushahidi wa video toka kwa kijana wake utakuwa bora sana kuliko picha zitakazopigwa na ‘microchip’ iliyotegeshwa. Nasrat Abdul al Aziz alifikiria suala la kumpandikiza mtu kufatilia kazi iliyokuwa ikiendelea kwa sababu alipata mashaka sana na toka katika maswali ya Derrick Edward, aliyomuuliza David Samson siku ya kwanza walipokabidhiana kazi. Mashaka yale pamoja na picha zilizopigwa na ‘microchip’ iliyokuwa kwenye simu ya David Samson viliongeza udadisi na walakini katika akili yake, aliiona sura ya Derrick Edward ilivyokuwa na mashaka juu ya mteja wake, mashaka makubwa baada ya kupewa kazi ya kuchora na kuchonga taswira ya mzee Masiya, mzee aliyejificha kwenye kivuli cha siasa.

Kipindi makabidhianao ya kazi na malipo yalipokuwa yakifanyika hawakufahamu kama kulikuwa na mtu wa tatu akichukua video tukio zima, mtu huyo alipitisha kamera ndogo mithiri ya kishikizo (kifungo) cha shati katika mlango wa ofisi ya Derrick Edward, mtu yule alibaki nje kama mteja aliyekuwa akisubiri huduma ya ofisi. Siyo kwamba hawakujua kama nje ya ofisi kulikuwa na mtu, hapana, walifahamu hilo lakini hawakumtilia mashaka kabisa kwa sababu alikaa nje kama mteja aliyekuwa kwenye foleni ya kupata huduma, na ndivyo ilivyokuwa. Baada ya Derrick Edward na David Samson kukamilisha makabidhiano yao, David Samson aliondoka kisha kijana yule akaingia ofisi kama mteja. Aliuliza alichojisikia kuuliza kisha akaaga, akatokomea zake. Derrick Edward na David Samson hawakuelewa chochote kilichotokea. Kamera ya kijana yule ilifanikiwa kuchukua tukio zima la Derrick Edward kutegesha simu iliyokuwa ikichukua tukio lote la makabidhiano ya kazi, hakika kamera yake ilikuwa kazini kama ilivyokusudiwa kuwa. Baada ya kukamilisha suala lake la kuchukua video alimtumia Nasrat Abdul al Aziz kisha akamwambia

“Huyu ndiye mwanaume uliyemkabidhi moyo wako, mwanaume anayekufatilia pasipo wewe kujua. Kama picha za awali zilivyokuonesha jinsi mwanaume wako alivyokuwa makini kumchunguza David, ndivyo hivyo hivyo video hiyo inavyoonesha jinsi alivyomrekodi David”

Kauli pamoja na video toka kwa Zimwi vilimchanganya sana Nasrat Abdul al Aziz, aliamini alikuwa kwenye vita kali na mwanaume aliyemkabidhi mwili wake. Nasrat Abdul al Aziz hakuwa tayari kufa wala kuharibiwa mipango yake, alikuwa tayari kufanya lolote ili atimize kazi aliyoianza. Alijiona mkosaji mbele ya kijana wake, Zimwi, akili ilifanya kazi haraka sana kwa sababu alielewa akichelewa kuchukua maamuzi lazima Derrick Edward afahamu kuwa yeye ndiye aliyekuwa akiratibu mambo yote, alipata mashaka juu kazi iliyoandaliwa na Derrick Edward. Aliamini Derrick Edward atakuwa mpelelezi yakinifu aliyejivisha vazi la sanaa, alifikiria hilo baada ya kuhusisha suala la Derrick Edward kurekodi video ya makabidhiano kwa siri na kazi aliyokuwa akiifanya, aliona hakuna ulazima wa kumrekodi mteja wako kwa siri. Swali lilibaki, kwanini amerekodi video? Hapo ndipo ukakasi ulipoanzia, ukakausi huo ulikuwa mkubwa zaidi baada ya kuhusianisha na maswali ya Derrick Edward aliyomuuliza David Samson. Alihusianisha akaona kuna kitu kilichojificha. Simu ilikuwa sikioni kipindi mawazo hayo yakishambulia kichwa yake, akakumbuka kuendelea na mazungumzo na Zimwi. Akamwambia kijana wake wa kazi aliyemuamini tangu tangu na tangu

“Yakupasa kumpigia simu David na kumwambia asimame alipo ili uende kukagua picha alizopewa, nina mashaka na kazi hiyo. Inaweza kuwa imewekewa vitu hatari kwetu”

Ilikuwa akili ya ajabu ya Nasra Abdul al Azizt, akili iliyoweka kukwepa mtego wa Derrick Edward. Zimwi hakuwa na maneno mengi, alitekeleza kauli ya bosi wake. David Samson alimsubiri njiani kama maagizo alivyoyapokea. Alikuwa amefika kwenye kituo kikuu cha mabasi yaendayo mikoani, njia iliyoelekea katika makazi ya Nasrat Abdul al Aziz. Zimwi hakuchukua muda mrefu kufika mahali alipoegesha gari David Samson, alifika na kifaa maalumu ‘microchip scanner’ cha kukagua kama picha au kinyago kilipandikizwa kifaa chochote cha kielektoniksi kinachoweza kuchukua taarifa kutoka sehemu moja kwenda nyingine. Baada ya salamu aliingia ndani ya gari aliloegesha David Samson akachukua picha na kinyago kisha akaanza kuvikagua kupitia kifaa kile cha kuskani. Aliiskani picha, hakugundua chochote lakini alipokiskani kinyago kifaa kilianza kupiga kelele huku kikiwaka taa nyekundu. Kitendo kile kilimaanisha kinyago kilikuwa kimepandikizwa ‘microchip’, GPS au kifaa kingine cha kielektoniksi. Akaongeza umakini katika kinyago kile, akarudia mara ya pili ili kufahamu sehemu husika iliyo na pandikizi hilo, alifanikiwa kupaona. Aliibandua ‘microchip’ kisha akashuka ndani ya gari, akaivunja vunja kwa mawe yaliyokuwa yamezagaa eneo la tukio. Alirudi ndani ya gari kisha akamwambia David Samson

“Sasa waweza kumpelekea mzigo huu”

David Samson alibaki mdomo wazi asiamini alichoshuhudia dakika chache zilizopita, alimfikiria Derrick Edward kisha taswira ya Nasrat Abdul al Aziz ikamjia kichwani. Alichanganyikiwa sana baada ya kuiona vita ya watu waliokuwa wakipendana kwa dhati, alidhihirisha ilikuwa vita kali baada ya kuona namna Derrick Edward alivyopandikiza ‘microchip’ katika mzigo ule. Sasa alielewa kwanini Nasrat Abdul al Aziz hakutaka Derrick Edward aelewe chochote kuhusu kazi ile, alielewa Nasrat Abdul al Aziz hamuamini mpenzi wake kwa asilimia zote. Alibaki akijiuliza mwenyewe

“Derrick ni nani haswa? Kwanini Nasrat aliamua kujihusisha kimapenzi na mwanaume asiyemuamini?”

Alijiuliza maswali mengi pasipo kupata jawabu kamili. Alikumbuka kauli ya Zimwi, kauli iliyomwambia anaweza kuendelea na safari yake ya kupeleka mzigo kwa Nasrat Abdul al Aziz. Alikubali kauli ya Zimwi kwa kichwa kisha akawasha gari tayari kwa kuondoka, Zimwi alishuka na kupanda gari aliloenda nalo eneo lile kisha akatokomea mbali na macho ya David Samson. Muda wote gari alilopanda David Samson lilikuwa likinguruma tayari kwa kuondoka, aliruhusu mafuta kisha safari ya kuelekea kwa Nasrat Abdul al Aziz ikaanza. Ilikuwa safari ya kimya kimya lakini iliyojaa kelele nyingi kichwani, alipanganisha mawazo na maswali pasipo majibu sahihi. Kichwa kilikuwa kizito pasipo kawaida. Upande wa Derrick Edward hali ilikuwa tofauti na matarajio yake lakini aliamini aliongeza kitu katika upelelezi alioutega, muda huo ‘microchip’ aliyoitega kwenye kinyago cha mzee Masiya ilikuwa haisomi kabisa. Hakushangazwa na tukio hilo kwa sababu alisikia mazungumzo yote yaliyofanywa kati ya David Samson na kijana mtanashati, Zimwi, mazungumzo yaliyomsisitiza David Samson asimamishe gari kisha amsubiri. Vile vile ‘michochip’ ilifanikiwa kuchukua picha za Zimwi.

Dakika kadhaa baada ya Zimwi na David Samson kukutana alishangaa kutoendelea kupata matukio ya picha, mandhari na mazungumzo yaliyokuwa yakisafirishwa na ‘microchip’, kitendo kile kilimuhakikishia kuwa ‘michochip’ ilivunja pale pale njiani baada ya watu wale kukutana. Akili ya Derrick Edward iliwaza mbali sana kuhusu Zimwi, iliona namna David Samson alivyokuwa akitumika na mtu au watu wale. Aliamini nyuma ya Zimwi kulikuwa na mtu mwingine, na mtu huyo atakuwa ndiye muhusika wa mipango yote kwa sababu kipindi Zimwi alipompigia simu David Samson amsubirie alimwambia kuwa mzigo ule haukuwa salama kufika kwa bosi wao pasipo kuukagua kwanza, kauli ile ilimaanisha kuna mtu mwenye mamlaka mbele ya vijana wale. Derrick Edward aliapa kumfahamu mtu huyo, kwakuwa alipata picha ya Zimwi na David Samson aliamini atakuwa kwenye hatua nzuri ya upelelezi wake. Ingawa hakujuwa watu wale walikuwa wakijihusisha na mambo gani lakini kitendo cha watu hao kuhitaji picha ya mzee Masiya kilisababisha Derrick Edward awahusishe na masuala ya madawa ya kulevya. Alijihakikishia suala hilo baada ya kusikia nyuma ya watu hao kuna bosi wao, hapo ndipo alipojiuliza

“Bosi wa nini kama hawapo kwenye mtandao wa madawa ya kulevya?”

Derrick Edward akafikiria kumfahamisha kiongozi Ibrahim Shadidy suala hilo, na ndivyo alivyofanya. Alimsimulia kisa chote kilichotokea mpaka upelelezi wake ulipofika. Ilikuwa habari mpya na ngeni katika masikio ya kiongozi Ibrahim Shadidy. Mkuu yule alimwambia Derrick Edward amtumia picha za wahusika alizofanikiwa kuzinasa, Derrick Edward alitimiza kauli ya mkuu wake wa kazi. Picha ya Zimwi haikuwa ngeni katika macho ya kiongozi Ibrahim Shadidy, picha yenye sura kama ile aliwahi kutumiwa na kijana wake aliyempa kazi ya kipelelezi chini ya mwamvuli wa kusimamia matamasha ya urembo na ulimbwende, siku aliyofanikiwa kumuona Nasrat Abdul al Aziz akiongea kisha kufanya biashara ya madawa ya kulevya na Amani Collence. Biashara iliyoishia kwa kugeukana wao kwa wao. Sasa kiongozi Ibrahim Shadidy alishindwa kumuelewa Derrick Edward, alishindwa kuelewa alikuwa upande gani kwa sababu taarifa alizompatia aliona zilikuwa na wazi kabisa kusafisha njia ya kumkamata Nasrat Abdul al Aziz. Kiongozi Ibrahim Shadidy alifikiria mara mbili mbili akaona labda kuna mtego katikati ya jambo hilo, lakini alivyozidi kufikiria kwa undani zaidi hakuuona mtego huo. Aliamini kijana wake amerudi kundini, katika kuamini huko alijihakikishia kutakuwa na mpasuko wa kimapenzi kati ya watu hao.

Japokuwa alipata taarifa kamili toka kwa Derrick Edward lakini hakumuamini asilimia mia moja kama kijana wake sahihi wa kazi, aliamini kama aliweza kumficha suala la Nasrat Abdul al Aziz wakati lilikuwa ndiyo mpango kazi basi anaweza kumficha hata mambo mengine yenye faida nyingi upande wake kuliko taifa. Kiongozi Ibrahim Shadidy aliandaa mpango kazi, mpango uliokuwa macho dhidi ya Derrick Edward. Kipindi kiongozi Ibrahim Shadidy akifikiria namna ya kupambana na matukio yaliyokuwa yakiendelea, upande wa pili Derrick Edward alijihakikishia kuwa lazima afanye juu chini kubaini uchafu wote uliokuwa nyuma ya David Samson na kijana mwenye rasta fupi, Zimwi. Aliamini endapo akibaini nyendo za vijana hao atakuwa amebaini kila kitu kuhusu mipango yao na kuhusu kila nguvu iliyo nyuma yao. Derrick Edward alijidhatiti haswa kusafisha jina lake alilohisi lilianza kupotea baada ya kuona mkuu wake wa kazi akiacha kumshirikisha mambo mengi. Hakuwa tayari kupoteza imani hiyo, aliamini endapo akifanikiwa kupambana ipasavyo mpaka wakakamatwa wauzaji na wasambazaji wa madawa ya kulevya nchini Malosha atakuwa ametimiza kazi yote iliyompeleka mkoani Rwama Mwanzo kutoka Rwama Mwisho.

Hakujua kundi la David Samson na Zimwi lilikuwa chini ya mpenzi wake. Derrick Edward alijipa moyo kuwa kwakuwa alifanikiwa kuchukua sura ya David Samson kwa jina ya video ingekuwa rahisi sana kumtafuta mtaani, aliamini atatumia video ile kufanyia upelelezi wake uliokuwa mezani. Vile vile alikuwa na picha ya kijana mwenye rasta, picha iliyonaswa na ‘microchip’ aliyoipachika kwenye kinyago cha mzee Masiya kabla hakijavunjwa. Aliamini huo ulikuwa mwanzo mzuri wa kuwabaini na kuwakamata wahalifu wote, aliamini hilo kwa sababu alikuwa ameshapata njia ya kuanzia Hakujua nyuma ya njia aliyoipata kulikuwa na msitu mnene, msitu mwenye kila aina ya wanyama wakali.

Upande wa Nasrat Abdul al Aziz hali ilikuwa tofauti, kichwa kiliwaza kumwaga damu, hakuona sababu ya Derrick Edward kubaki na uhai. Aliamini uhai wa Derrick Edward unamaanisha kifo au kukamatwa na kuwekwa gerezani. Akili ilipanga kufanya mauaji kwa mkono wake mwenyewe lakini moyo ulikataa, moyo ulikuwa umemuhifadhi Derrick Edward katika vyumba vyote vinne, moyo haukuwa tayari kumuua Derrick Edward. Nasrat Abdul al Aziz alichukua chupa ya pombe ghari ya Hennessy VS kisha akamimina kwenye glasi iliyokuwa ikimtazama kisha akapeleka mdomoni, alimeza funda moja baada la lingine huku kichwa chake kikiendelea kutafakari maamuzi sahihi ya kuchukua, maamuzi yaliyoegemea kuchukua uhai wa Derrick Edward au kulitetea penzi lake. Aliinuka, akatembea tembea ndani ya sebule yake huku kichwa kikishambuliwa kwa kelele za mabishano ya mawazo kichwani kwake. Wazo moja likashinda, akaona huo ndiyo muda muafaka wa kulitekeleza wazo lake. Tabasamu laini likashambulia midomo yake, aliiona njia ya kufuata ili akamilishe utata uliokuwa mbele yake. Akatafuta jina alilolihifadhi katika simu yake, alipoliona akapiga kisha akaweka sikioni. Simu iliita sekunde kadhaa, aliyepigiwa akapokea kisha Nasrat Abdul al Aziz akaongea kwa sauti ya kutoa amri bila hata ya kuona umuhimu wa kutoa salamu

“Kabla siku ya leo haijaisha nataka Derrick akamatwe na kupelekwa katika himaya yangu”

Zimwi hakuwa na kauli zaidi ya kukubali kauli ya bosi wake, aliafiki kwa kumuhakikishia kula lazima Derrick Edward akamatwe kama maagizo yalivyotolewa. Baada ya maagizo simu ilikatwa. Japokuwa Nasrat Abdul al Aziz alitoa agizo la kumkamata Derrick Edward lakini moyo uliendelea kukataa, mapigo ya moyo yaliongeza kasi akajiona akiishiwa nguvu. Siyo kwamba pombe aliyokunywa ilishababisha hivyo, hapana, kiwango alichokunywa kilikuwa kidogo sana kulingana na hali aliyokuwa nayo muda huo, bali mawazo ndiyo yaliyomtesa. Akahisi kama fahamu zikimtoka, mwili ukamlegea, machozi yakatengeneza mifereji katika mashavu yake. Nguvu zikamuisha kabisa. Hofu ikapanda, akajitahidi kuinuka alipokaa akashindwa. Akili ikamtuma ampigie daktari wake, hakujiuliza mara mbili. Akampigia daktari kisha akamsisitiza afike kwake haraka iwezekanavyo. Na ndivyo ilivyokuwa. Daktari alifika akamtuliza Nasrat Abdul al Aziz kama afanyavyo siku zingine, lakini siku hiyo hali ilikuwa tofauti Nasrat Abdul al Aziz hakutulia kabisa. Ilikuwa kawaida kwa Nasrat Abdul al Aziz kumuita daktari huyo kila alipohisi hali tofauti katika mwili wake. Nasrat Abdul al Aziz alimuogopesha daktari wake. Alitapika mfululizo kisha maumivu chini ya kitovu yakamshambulia pasipo huruma. Hali ilikuwa mbaya zaidi, alianza kuhisi hali ya unyevunyevu usio wa kawaida ukeni. Macho yalimtoka akamtazama daktari kwa umakini kama mtu anayemwambia kitu fulani, daktari alielewa hali hiyo. Akamwambia Nasrat Abdul al Aziz

“Nimekuja kwa ajili yako, waweza sema unavyojisikia zaidi ya ulivyoniambia awali”

Nasrat Abdul al Aziz hakuwa na jinsi zaidi ya kumwambia ukweli daktari Johnson, ingawa alieleza kwa shida sana lakini alifanikiwa kumuelewesha. Daktari Johnson alielewa kazi zote zilizokuwa zikifanywa na baba Nasrat Abdul al Aziz zimebaki mikononi mwa binti yake. Daktari huyo alikuwa sehemu ya kundi la Nasrat Abdul al Aziz, alikuwa kitu kimoja na binti huyo wa Kiarabu kwa sababu walitoka kwenye historia moja iliyoandamwa na visasi. Alikuwa daktari tajiri tofauti na madaktari mwengine kwa sababu alijihusisha na makundi haramu. Alimtumikia Nasrat Abdul al Aziz kwa siri kubwa, wawili hao walikuwa na siri ya maisha yao. Awali daktari Johnson aliajiriwa na serikali lakini alihisi akibanwa. Akaacha kazi kisha akafungua hospitali yake chini ya msaada wa wahalifu. Daktari Johnson alikuwa kama kaka mkubwa kwa Nasrat Abdul al Aziz, lakini ukaka huo huokuweka mipaka ya kidaktari. Nasrat Abdul al Aziz alikuwa wazi kumuelezea kila alichojisikia katika mwili wake hata kama yakiwa magonjwa ya wanawake au sehemu zake za kike. Daktari Johnson alimkazima macho Nasrat Abdul al Aziz kisha akamwambia

“Vua nguo yako ya ndani nithibitishe hali yake”

Nasrat Abdul al Aziz alikuwa amevaa gauni lefu lisilochonga mwili wake, halikumbana hata kidogo hivyo basi suala la kuvua chupi halikuwa gumu. Alielewa fika kuwa akishavua nguo hiyo lazima daktari amtazame sehemu zake za siri ili kubaini chochote cha kitabibu, hakuwa na jinsi zaidi ya kuiambia akili yake kukubali kila kitu atakachoambiwa. Alikuwa na mawazo tofauti na daktari. Aliingiza mikono pasipo kufunua mwili wake kila akavuta chupi yake nyeupe, ilikuwa imechora ramani nyekundu. Hali ile ilimaanisha alikuwa akivuja madone ya damu ukeni. Hofu ilizidi moyoni, mapigo ya moyo yakaongeza kasi. Akamtazama daktari, daktari alikuwa akitabasamu kama mtu aliyefurahishwa na hali ile. Ilikuwa lugha ya picha ya kumtuliza mgonjwa wake. Alielewa akionesha hali ya hofu atamuogopesha zaidi Nasrat Abdul al Aziz. Tabasamu la daktari Johnson lilimshangaza kidogo Nasrat Abdul al Aziz, akabaki na bumbuwazi. Daktari Johnson alimwambia

“Naomba hiyo nguo”

Nasrat Abdul al Aziz alimkabidhi daktari Johnson chupi chake, daktari akaitazama vizuri ilivyochakaa kwa matone ya damu. Vile vile aliona ute mweupe kama maziwa ulivyosambaa katika chupi ile. Kwa akili ya kidaktari alihisi kitu. Alifungua begi lake akatoa kopo dogo kisha akamuinua Nasrat Abdul al Aziz kwa nguvu, alimbeba mpaka chooni akampatia lile kopo kisha akamwambia

“Jitahidi upatikane mkono katika kopo hilo”

Nasrat Abdul al Aziz alifanya alichoambiwa kisha akamwita daktari Johnson. Alifika akambeba kama awali, safari hiyo alimpeleka chumbani kwake na siyo sebuleni. Alimlaza vizuri kisha akarudi sebuleni na lile kopo la mkojo. Alichukua vipimo vyake akapima alichokusudia kupima, alisubiri baada ya muda kadhaa kupita kisha akapata majibu. Alitabasamu kisha akarudi chumbani kwa Nasrat Abdul al Aziz. Nasrat Abdul al Aziz alikuwa macho kitandani akisubiri majibu ya daktari wake. Daktari Johnson hakuwa na maneno mengi bali aliongea maneno machache yaliyobadili mtazamo na fikra za mgonjwa wake. Maneno yaliyompa furaha na huzuni kwa wakati mmoja, maneno yaliyompa kigugumizi na kumuacha njia panda. Maneno ya daktari yalikuwa

“Hongera mdogo wangu, una ujauzito”

Daktari Johnson alikuwa akitabasamu kama kawaida yake, lakini hali ilikuwa tofauti kwa mgonjwa wake. Nasrat Abdul al Aziz alishindwa kuelewa acheke au alie. Alijihakikishia kuwa mtoto aliye tumboni ni wa Derrick Edward, ofisa upelelezi aliyejificha kwenye kivuli cha sanaa. Machozi yalitengeneza mifereji katika mashavu yake, hayakuwa machozi ya furaha wala huzuni. Alibaki njia panda pasipo kujua njia kuu.

ITAENDELEA
IMG-20220328-WA0004.jpg
 
RIWAYA: MATEKA
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890

(KIPANDE CHA SABA)

Toyota Probox nyeupe ilifunga breki jirani kabisa na nyumba aliyopanga David Samson na mpenzi wake, kisha msichana wa makamo anayekadiriwa kuwa na miaka ishirini na saba akashuka kwa utaratibu uliotukuka, msichana yule hakuwa na papara wala haraka yoyote. Alikuwa makini akiamini alichokuwa akienda kukifanya. Msichana huyo alivaa gauni la bluu lililofanana rangi na viatu vyake vya mchuchumio. Alistahili kuitwa mrembo. Alikuwa na kazi ngumu lakini aliamini lazima afanikiwe kwa namna moja ama nyingine. Alitazama saa yake ya mkononi ikamuonesha ilikuwa saa kumi na moja na robo jioni, akatabasamu baada ya kuona alikuwa ndani ya muda. Akafungua mkoba wake ghari kisha akachomoa kioo kidogo akajitazama usoni, akajifuta jasho kwa leso kisha akarekebisha nywele zake alizohisi zilitawanyika kidogo. Alipohakikisha yupo sawa, akafunga mlango wa gari lake kisha akaanza kupiga hatua kuelekea katika nyumba aliyoikusudia. Alifika uwani, akawakuta akina mama wawili, mmoja akiwa anasuka mwingine akiwa anasukwa. Baada ya salamu aliuliza

“Nafikiri hapa ndipo anapokaa David Samson?”

Wale akina mama walimkazia macho yule mgeni kisha aliyekuwa akisukwa nywele za uzi akamjibu mrembo aliyekuwa mbele yao

“Wala hujakosea mtoto, gonga mlango ule waweza pata majibu zaidi”

Yule mama alimuelekeza mgeni wao mlango wa kugonga, ulikuwa mlango wa nyumba aliyopanga David Samson na mpenzi wake. Mgeni alielewa maana ya kuambia agonge mlango alioelekezwa, lakini kuna kitu kilimshangaza, kitu kile kilimuongezea swali la udadisi. Alijiuliza mwenyewe

“Kwanini walitazamana baada ya kuwauliza kuhusu David? Kuna nini kinachoendelea!”

Alihisi kuna kitu kipo nyuma ya mlengwa wake, kwakuwa alienda kwa ajili ya David Samson alielewa lazima atajua kila kitu ili kazi aliyokabidhiwa aikamilishe kwa wakati husika. Hakika akijipumbaza mwenyewe, hakujua ugumu uliokuwa mbele ya kazi yake, hakujua kabisa. Alifika kwenye mlango alioambiwa agonge, alikaribishwa na pazia leupe lenye mchanganyiko wa maua mekundu na kijivu. Hali ya hewa iliyoathiriwa na kiupepo cha jioni ilimsaidia kuipeperusha pazia ile na kufanikiwa kuuona mlango umefungwa, awali hakujua kama ulikuwa umefungwa na funguo au ulikuwa umeegeshwa. Aligonga mlango kama alivyoagizwa, hali ya ukimya ilitawala. Hakusikia sauti yoyote toka ndani ikiitikia. Akaongeza nguvu ya ugongaji wa mlango, hakika nguvu iliongezeka maradufu kwa sababu alivisikia vidole vyake vikimwambia apunguze nguvu, aliviumiza. Bado ukimya uliendelea kutawala, akadhani labda ndani hapakuwa na mtu yeyote lakini akili ikakataa baada ya kukumbuka kauli ya mwanamke aliyekuwa akisukwa

“Wala hujakosea mtoto, gonga mlango ule waweza pata majibu zaidi”

Kauli ile ilimaanisha muhusika aliyestahili kumjibu alikuwa ndani, lakini kwa nini ukimya ulitawala? Kilikuwa kitendawili kilichomsumbua. Akili ikamwambia arudi kwa wale akina mama kwakuwa wao walikuwa wenyeji basi awatumie kumpata mwenyeji aliyemfuata, lakini kabla hajapiga hatua hata moja kuondoka mbele ya mlango uliofungwa ghafla alishuhudia ukifunguliwa kisha akakutanisha uso na msichana aliyeonekana kuchoshwa na usingizi, alilitambua hilo kwa sababu muonekano wake ulijieleza vizuri. Sura ilikuwa na makunyazi ya usingizi, vile vile alikuwa amevaa kanga juu na chini kitu kilichomaanisha alijitanda haraka ili aende kumsikiliza aliyekuwa akigonga mlango wake. Msichana aliyetoka usingizini aliongea kwa sauti dhaifu

“Karibu dada, sijui nikusaidie nini?”

Kauli hiyo ilimtoka akiwa katikati ya kizingiti cha mlango, kitendo hicho kilimaanisha alitaka kumaliza shida ya mgeni wake mahali pale pale na siyo kumuingiza ndani mtu asiyemjua. Mgeni alielewa kila kitu, alimkazia macho mwenyeji wake kisha akamjibu kwa nidhamu iliyotukuka

“Nimekuja kuongea na David, nafikiri wewe utakuwa mkewe au nimekosea?”

Swali hilo lilipita vizuri katika masikio ya Winnie Ngocho na hakika alilisikia vizuri kabisa lakini lilimshangaza, yaani msichana mrembo anamuulizia David Samson nyumbani kwake? siyo kwamba alihisi atakuwa mwanamke wa mpenzi wake, hapana, bali alihisi kuna mchezo alikuwa akichezewa kuhusu matukio yaliyokuwa yakiendelea kuhusu mpenzi wake. Hali ya uchovu wa usingizi ikamruka maradufu, makunyazi yakapotea kabisa, akawa Winnie Ngocho aliyezoeleka, Winnie Ngocho mwenye kisura cha kitoto. Winnie Ngocho alimtazama mgeni wake kuanzia chini mpaka juu, akaona jinsi alivyopendeza, kupendeza kule hakukumpa mashaka sana bali mashaka aliyapata baada ya kuthaminisha vito vya thamani alivyokuwa amevaa mgeni wake, alijihakikishia alikuwa amevaa vitu vya gharama sana. Akili yake ilimuaminisha kuwa mgeni huyo atakuwa miongoni mwa watu wanaomsumbua kipenzi chake. Mapigo ya moyo yakaongeza kasi, akaona jinsi walivyokuwa wakiendelea kuishambulia familia yake. Alishindwa kujizuia kuruhusu machozi yatengeneze njia katika mashavu yake baada ya kumkumbuka Lucia wake, mtoto wake wa pekee aliyechukuliwa na wafanya biashara haramu ya madawa ya kulevya. Kitendo cha kuruhusu machozi yapite katika mashavu yake kilimshangaza sana mgeni aliyekuwa akisubiri kupatiwa majibu ya swali alilouliza. Winnie Ngocho alijitahidi kupambana na hisia zilizosababisha aendelea kutoa machozi lakini alishindwa, machozi yaliendelea kuteremka bondeni kutoka juu ya kilima kilicho jirani ya pua. Mgeni akauliza kwa haraka

“Kuna shida gani mdogo wangu?”

Hakika alistahili kumuita mdogo wangu kwa sababu umbile lilimthibitishia hilo, Winnie Ngocho alijikaza kwa shida sana kisha akajibu

“Wewe ni nani na kwanini unamuulizia David?”

Lilikuwa swali lepesi sana kwa mgeni lakini hakupenda kulijibu akiwa amesimama wima namna ile, alitamani apate sehemu ya kukaa ili waulizane maswali kinaga ubaga. Kipindi mambo hayo yakiendelea wale akina mama waliokuwa kwenye ususi walikuwa makini kuangalia kila kilichokuwa kikiendelea. Mgeni alielewa hilo, ikabidi amwambie Winnie Ngocho

“Sijui nikwambie mimi ni nani ili uniamini kwa haraka, lakini kabla sijajielezea chochote ningependa unikaribishe ndani ili tufahamiane vizuri”

Kauli ya mgeni ilisikika vizuri sana katika masikio ya Winnie Ngocho lakini ilizidi kumchanganya sana, alishangaa kuona namna mgeni alivyokuwa akijiamini namna ile. Eti akaribishwe ndani ili waongee zaidi! Ulikuwa mshangao wa namna yake. Winnie Ngocho alimkazia macho mgeni wake lakini mgeni hakuwa na hofu wala wasiwasi, alikuwa akitabasamu. Hakika lilikuwa tabasamu bandia, tabasamu la kujaribu kuuhadaa msimamo wa Winnie Ngocho. Kwa kweli mgeni alifanikiwa kwa hilo, Winnie Ngocho aliamua kuchukua maamuzi magumu. Akamkaribisha mgeni ndani. Baada ya kukaa katika kiti cha sofa kilichokuwa na kitambaa kilichochoka, Winnie Ngocho hakuhitaji mgeni apumzike hata sekunde kadhaa, yeye alihitaji ufafanuzi zaidi. Mgeni hakuwa mbishi bali alianza kwa kujitambulisha

“Naitwa Olivia Komba, mwandishi wa habari kutoka kituo cha redio ya taifa tawi la hapa mkoani”

Winnie Ngocho alikuwa makini kumsikiliza mgeni wake aliyekuwa akiongea kwa kujiamini sana, mgeni hakuwa na dalili ya hofu wala wasiwasi wa aina yoyote. Kitendo kile hakikumuaminisha Winnie Ngocho kauli ya mgeni wake, alikumbuka namna alivyowahi kumpokea mgeni akisema alitumwa na mama yake mzazi baada ya kusikia amejifungua mtoto lakini baadae alipofungua zawadi aliyoletewa na mgeni huyo aligundua alidanganywa kama mtoto mdogo. Vile vile alikumbuka namna David Samson alivyomsimulia kisa kilichomtokea, jinsi alivyotekwa na watu waliojitambulisha kwake kuwa ni maofisa wa jeshi la polisi lakini mwisho wa siku alijikuta katika mikono ya wauza madawa ya kulevya. Winnie Ngocho akatabasamu baada ya kuona mgeni wake akiichezea akili yake, akamwambia

“Jua nimekatisha usingizi wangu nikusikilize, sasa usiniletee habari nisizozielewa. Kama na wewe umetumwa sema ulichotumwa”

Mrembo aliyejitambulisha kwa jina la Olivia Komba aliisikia vizuri kauli ya jeuri ya Winnie Ngocho, siyo kwamba ilimuudhi, la hasha, bali ilimuongezea maswali ya udadidi. Alijikuta akijiuliza maswali akilini

“Eti kama nimetumwa? Na nani?”

Alitamani kuuliza swali lakini alikuwa amechelewa, Winnie Ngocho aliendelea kumshambulia kwa maneno yaliyodhihirisha alimtilia mashaka Olivia Komba

“Eti mwandishi wa habari! Mwandishi gani usiye na kifaa chochote cha kuchukulia Habari? Unafikiri mimi ni mjinga kiasi hicho!”

Ujasiri wa ajabu ulikuwa moyoni mwa Winnie Ngocho, alijikuta akiropoka maneno makali mbele ya mgeni wake. Alielewa mgeni ule alikuwa miongoni mwa watu hatari walioiweka familia yake kizuizini. Alitamani kupiga kelele za kumfukuza lakini alielewa haitasaidia chochote. Alisimama wima tofauti na awali, kwa sauti ya upole alimwambia Olivia Komba

“Waweza kuondoka dada yangu”

Olivia Komba aliiona sura ya Winnie Ngocho ilivyokuwa ikimaanisha kauli aliyoitoa, sura nzuri ilikuwa na makunyanzi ya hasira kitu kilichotafsiri hakuhitaji kuendelea kuiona sura ya mgeni wake. Olivia Komba alisimama wima kisha akamwambia Winnie Ngocho

“Hakika upo sahihi, mimi siyo mwandishi wa habari wa kituo chochote cha televisheni, redio wala magazeti. Sihusiki na watu hao, mimi ni askari mpelelezi kutoka makao makuu. Nimekuja hapa kupata maelezo ya kutosha kuhusu mpenzi wako kwa sababu kuna kijana wetu tulimpachika mkoani hapa kupambana na masuala ya madawa ya kulevya lakini mwisho wa siku ameungana nao”

Kauli ya Olivia Komba ilikuwa ndefu sana lakini haikuwa na kizuizi chochote cha kueleweka, Winnie Ngocho alisikia vizuri maneno yale lakini alihisi akipigiwa kelele. Baada ya kuruhusu funda mbili za mate kulainisha koo lake, Olivia Komba aliruhusu mwayo uliotoa hewa aliyoiingiza mwilini muda mfupi uliopita kisha akaendela

“Nasikia mume wako alishawishika kujiunga katika biashara hizo na mpaka sasa anashirikiana na kijana wetu katika biashara hiyo haramu. Nimekuja hapa ili nifahamu kila kitu ili nifahamu wapi pa kuanzia”

Kipindi akiongea kauli hiyo alikuwa akikagua mkoba wake kisha akachomoa kitambulisho chake cha kazi akamkabidhi Winnie Ngocho aliyekuwa amesimama kama mlingoti wa umeme. Winnie Ngocho alikipokea kisha akasoma jina kwa sauti ya chini, sauti iliyosikika vizuri ndani ya sebule yake

“Olivia Komba”

Kitambulisho kilijieleza kuwa Olivia Komba alikuwa polisi kutoka idara ya CID (Criminal Investigation Department). CID ni idara maalumu ya upelelezi katika jeshi la polisi. Maofisa wa polisi katika idara hiyo hupaswa kupeleleza mambo makubwa ya jinai kama makosa ya udanganyifu, ulaghai, wizi, unyang`anyi wa kutumia silaha, uhujumu uchumi, ugaidi, kugushi nyaraka na uhalifu mwingine wa aina yoyote unaoweza kuathiri taifa au mataifa. Winnie Ngocho aliinua kichwa chake kisha akamtazama mrembo aliyekuwa akiendelea kutabasamu, kipindi Winnie Ngocho akitafakari kauli aliyotaka kuongea, Olivia Komba alimuwahi kutoa kauli, Olivia Komba aliendelea kutoa ufafanuzi

“Inspekta Jenerali wa Polisi (Inspector General of Police – IGP) ndiye aliyetoa amri nifatilie suala hili mpaka nihakikishe limepatiwa ufumbuzi yakinifu”

Kauli ya Olivia Komba ilimshangaza sana Winnie Ngocho, kauli iliyosema Olivia Komba alikuwa kazini kwa amri ya IGP. Winnie Ngocho aliona ukubwa wa tatizo hilo kwa sababu IGP ndiye kiongozi wa ngazi ya juu wa jeshi la polisi nchini, kiongozi ambaye husaidiwa kazi zake na makamishna wa polisi pamoja na wakuu wa polisi wa mikoa. Winnie Ngocho alianza kumuamini Olivia Komba aliyekuwa akimtazama usoni, alimuuliza

“Inawezekanaje uje kumchunguza polisi mwenzako?”

Olivia Komba alitabasamu kidogo, akaruhusu meno yake yaliyoathiriwa na dhahabu kuonekana. Aliyavisha dhahabu ili kuficha uhalisia wake, alijiweka kama mrembo wa kisasa kumbe nyuma ya urembo huo alikuwa mpelelezi mwenye viwango vya juu. Akamjibu Winnie Ngocho huku akipokea kitambulisho chake toka kwenye mkono ya mwenyeji wake

“Sote ni polisi wa taifa la Malosha lakini tupo idara tofauti, huyo aliyekengeuka anatoka idara inayopambana na madawa ya kulevya, idara ya mkoa huu. Mimi natokea idara ya upelelezi. Tupo sehemu mbili tofauti, ingawa jeshi la polisi ni moja…suala langu ni siri kubwa, hakuna polisi mwingine anayejua nimepachikwa kufatilia jambo hili. Anayejua ni CID aliyetoa kazi na kiongozi wa idara ya upelelezi pekee”

Winnie Ngocho alikuwa kimya, hakuwa na uwelewa wa kutosha kuhusu jeshi la polisi. Alimuacha mwenye uwelewa adadavue kinaga ubaga. Hakika alidadavua. Olivia Komba aliendelea, kitendo kile cha kuendelea ndicho kilichozua taharuki katika kichwa cha Winnie Ngocho. Olivia Komba alisema

“Ulishalisikia jina la Alimas Jumbe? Nasikia siku hizi anajiita Zimwi na amefuga rasta fupi”

Jina la Zimwi halikuwa geni katika masikio ya Winnie Ngocho, alikumbuka alishawahi kulisikia sehemu. Alifikiria muonekano wa rasta fupi, alikumbuka kitu. Alikumbuka kipindi alipokuwa hospitali aliambia alilipiwa gharama za matibabu na kijana aliyejitambulisha kwa jina hilo, kijana mwenye rasta fupi aliyemwambia nesi kuwa alikuwa mdogo wake wa mwisho. Mshangao uliteka taswira ya Winnie Ngocho lakini kabla hajastaajabu zaidi suala hilo alizidi kuchanganywa na kauli ya Olivia Komba

“Kijana anayejiitwa Zimwi ndiye polisi aliyetusaliti”

Winnie Ngocho alikosa jibu la kutoa, alimkodolea macho Olivia Komba, macho yalieleza fika kuwa alishangazwa na taarifa hiyo. Alihisi akiishiwa nguvu, kizunguzungu kikaanza kumnyemelea kama mwindaji amnyemeleavyo windo lake. Akakaa kwenye kiti kisha akainua sura yake kumtazama mgeni aliyekuwa bado amesimama wima tayari kwa kuondoka. Winnie Ngocho aliuona umuhimu wa Olivia Komba katika matatizo yaliyokuwa yakisumbua familia yake. Akamwambia

“Olivia, waweza kukaa tuongee vizuri”

Olivia Komba hakutengeneza mazingira ya ubishi wowote kwa sababu lilikuwa ndiyo kusudio lililompeleka, alifika ili apate nafasi ya kuonana mtu atakayempatia taarifa kamili kuhusu David Samson. Alikaa kwenye sofa kisha akasubiri kauli ya mwenyeji wake. Winnie Ngocho alimkazia macho Olivia Komba kisha akamuuliza kwa kuhamaki

“Umesema kijana anayeitwa Zimwi ni polisi mpelelezi?”

Lilikuwa swali la kitoto kwa sababu lilikuwa limeshatolewa ufafanuzi toka awali. Kitendo cha Winnie Ngocho kuuliza akiwa kwenye hali iliyoonesha wazi kuchanganyikiwa kilisababisha Olivia Komba afahamu kuna uwezekano mkubwa Winnie Ngocho akawa anafahamu kitu au vitu vinavyoweza kuwa mwangaza katika kazi yake ya kipelelezi. Hakujibu swali la Winnie Ngocho wala hakusubiri kauli nyingine kutoka kwake bali aliuliza swali, aliamini kupitia swali lake angeweza kupata majibu yakinifu. Na ndivyo ilivyokuwa

“Unafahamu chochote kuhusu mtu huyo? Namaanisha Zimwi”

Winnie Ngocho hakujiuliza mara mbili wala hakufikiria sana kuhusu jibu la kutoa bali alitigisa kichwa juu chini akimaanisha kukubali kuwa alifahamu mambo kumuhusu Zimwi. Kitendo kile kilimuongezea umakini Olivia Komba, siyo kwamba alisahau kabisa kuuliza kuhusu masuala ya David Samson, hapana, lakini alifahamu akijua mambo kuhusu Zimwi atakuwa amefahamu baadhi ya mambo kuhusu David Samson. Hivyo basi aliamini utakuwa mwanzo mzuri wa kuuwa ndege wawili kwa wakati mmoja. Olivia Komba alirudisha macho katika taswira ya Winnie Ngocho kisha pasipo kuchelewa akauliza swali, swali lililohitaji ufafanuzi wa ishara ya kichwa aliyoionesha

“Unaelewa nini kuhusu Zimwi?”

Kipindi Winnie Ngocho akifikiria wapi alistahili kuanzia katika maelezo yake, Olivia Komba alikuwa akisogea mahali alipokaa awali kisha akakaa kitako akisubiri majibu kutoka kwa mwenyeji wake. Hali ya ukimya ikaendelea pasipo kutegemea, kitendo kile kilimshangaza sana Olivia Komba akashindwa kuelewa kwanini Winnie Ngocho alikuwa na kigugumizi cha kuongea. Winnie Ngocho alifungua mdomo wake, ufunguzi huo wa mdomo haukujibu swali aliloulizwa bali alitoa ufafanuzi mwenye mashaka ndani yake. Alisema kwa sauti ya kitetemeshi

“Najua David na mwanangu wapo mikononi mwa kijana huyo anayejiita Zimwi, najua kabisa. Suala la wewe kutaka taarifa za Zimwi kutoka kwangu ni kutaka kuangamiza familia yangu endapo mtu huyo akifahamu mimi ndiye chanzo cha taarifa hizo. Nafikiri natakiwa kutafuta njia nyingine ya kuisaidia familia yamgu”

Maneno ya Winnie Ngocho yalisikika vizuri katika masikio ya Olivia Komba, japokuwa yalionesha hali ya pingamizi lakini yalimfunulia kitu mpelelezi yule. Awali hakujui kama David Samson alikuwa na mtoto, na mtoto huyo yupo mikononi mwa watu wabaya. Sasa alipata picha na kuelewa kwanini Winnie Ngocho alitengeneza hofu, lengo la hofu lilikuwa kuilinda familia yake. Olivia Komba aliona jinsi Winnie Ngocho alivyojitahidi kuilinda familia hiyo lakini kwa njia ya kitoto. Olivia Komba aliamini Winnie Ngocho alitakiwa kumchangamkia kwa kutoa taarifa pasipo kuangalia upande hasi kuliko upande chanya. Olivia Komba aliuliza swali ili ahakikishiwe taarifa aliyoisikia

“Unasema mwanao yupo mikononi mwa Zimwi?”

Winnie aliitikia kwa kichwa akimaanisha kukubaliana na swali hilo. Kitendo kile kilimuhakikishia Olivia Komba kuwa David Samson atakuwa mikononi mwa watu waovu siyo kwa matakwa yake bali kwa shinikizo ili aokoe maisha ya mtoto wake. Aliamini sio rahisi mtu kuingia katika kundi la kigaid akiwa na mwanao, aliona namna mtoto wa David Samson alivyotumika kama ngao. Olivia Komba akakumbuka kitu, akaamua kuuliza haraka

“Mwanao alichukuliwa lini? Na ana miaka mingapi?”

Ilikuwa zamu ya Winnie Ngocho kufafanua kila kitu, hakuna alichoficha. Alieleza kila kitu kuhusu mahusiano yake na David Samson, alieleza jinsi familia zao zilivyowatenga kwa sababu walilazimisha kuishi pamoja pasipo idhini ya familia zao. Hakuna alichoficha kuhusu mkasa uliokuwa ukiwaandama wana familia hao. Namna David Samson alivyoshawishiwa na rafiki yake kujiingiza kwenye biashara ya madawa ya kulevya, namna David Samson alivyokamatwa na watu waliojitambulisha kwake kuwa maofisa wa jeshi la polisi. Mwisho wa simulizi yake alifafanua alivyonyang`anya mtoto wake wa pekee na vijana wawili waliokuwa na misuli iliyosambulia miili yao. Alieleza mtoto wake alikuwa chini ya mwezi mmoja, mtoto anayehitaji malezi kamili ya mama na baba yake. Maelezo ya Winnie Ngocho yalimtoa machozi Olivia Komba, alitoa kitambaa katika mkoba wake kisha akafuta chozi taratibu huku akifikiria kauli stahiki aliyostahili kuongea. Aliongea kwa sauti nyororo

“Maisha yako yapo matatani, usifikiri kama upo salama hata kidogo”

Winnie Ngocho alimkazia macho Olivia Komba baada ya kusikia kauli kuwa maisha yake yalikuwa matatani, siyo kwamba alipingana na kauli hiyo, la hasha, bali alihitaji ufafanuzi zaidi aweze kujikinga na matata hayo. Macho ya Winnie Ngocho yalijieleza kwa kiasi kikubwa, yalitoa picha ya kuhitaji ufafanuza. Olivia Komba alielewa hali ya mwenyeji wake, haikuwa kazi ngumu kufahamu hali hiyo kwa sababu alikuwa na mafunzo ya kutosha ya kumsoma mtu anayeongea naye. Akafafanua kauli yake

“Kama ulivyosema, David yupo mikononi mwa watu wanaojifanya wanapambana na wauza madawa ya kulevya lakini watu hao wamemchukua mtoto wako kama ngao ya kumtumikisha mpenzi wako. Yakupasa kufikiria kwa makini kwa sababu hakuna polisi anayeweza kutumia mbivu hiyo ili aweze kupata taarifa, mbinu gani ya kumtoa mtoto katika titi la mama yake. Haiwezekani. Hao ni majambazi wazoefu”

Olivia Komba alijinyoosha kama mtu aliyetoka usingizini. Akamtazama Winnie Ngocho aliyekuwa ameinamisha kichwa chini lakini masikio yakiwa makini kama kinasa sauti cha mpelelezi kinapokuwa kazini. Olivia Komba akaendelea kutoa ufafanuzi

“Najua David anatafuta njia ya kumuokoa mtoto wenu toka kwa maharamia, endapo akifanikiwa kutoroka lazima maharamia waangalie sehemu nyingine ya kumdhibiti ili waweze kumpata kirahisi. Sehemu hiyo ni wewe”

Winnie Ngocho aliinua kichwa chake akamtazama Olivia Komba aliyekuwa akiendelea kufuta machozi yaliyotengeneza mifereji katika mashavu yake. Sio kwamba Olivia Komba alikuwa akimlilia David Samson au Zimwi aliyewasaliti, hapana, bali alikuwa akimlilia mtoto Lucia, mtoto wa David Samson na Winnie Ngocho, mtoto aliyeingizwa kwenye adha za dunia akiwa na umri chini ya mwezi mmoja. Kitendo cha Winnie Ngocho kuona mifereji ya machozi katika mashavu ya mgeni wake kilimuongezea hisia kali juu ya familia yake, alijikuta akilia, tena siyo kilio cha lele mama bali kilio kilichoambatana na kwikwi. Sasa ilikuwa kazi ya Olivia Komba kumtuliza Winnie Ngocho, alimnyamanzisha kama mama afanyavyo kwa mtoto wake wa pekee. Ilimchukuza zaidi ya dakika mbili kutuliza kilio cha mwenyeji wake. Winnie Ngocho hakuwa na jinsi zaidi ya kunyamanza kwa sababu alisikia kauli ya Olivia Komba, kauli iliyomwambia kuwa kilio chake hakitamsaidia kuokoa familia yake bali ujasiri wake ndiyo unaohitajika. Hakika aliamini alistahili kuwa jasiri, na aliapa mbele ya Olivia Komba kuwa atakuwa jasiri kuhakikisha familia yake inakuwa salama. Alijikuta akiongea hivyo kwa ujasiri lakini hakujua atafanya nini ili kufanikisha maneno aliyoongea, hakika hakujua chochote. Kauli ya Olivia Komba ikajirudia kichwani kwake

“Najua David anatafuta njia ya kumuokoa mtoto wenu toka kwa maharamia, sasa endapo akifanikiwa kutoroka lazima maharamia waangalie sehemu nyingine ya kumdhibiti ili waweze kumpata kirahisi. Sehemu hiyo ni wewe”

Alikuwa Winnie Ngocho mpya, siyo Winnie Ngocho aliyelia kama mtoto dakika chache zilizopita. Alikuwa tayari kuelewa kila kitu ili awe sehemu ya kufanikisha zoezi la kuipata familia yake. Aliitafakari kauli hiyo akahisi bado ilikuwa na utata kichwani kwake, akaomba kupewa ufafanuzi yakinifu. Olivia Komba hakuwa mbishi hata kidogo, atakuwa vipi mbishi wakati alihitaji ushirikiano wa Winnie ili aweze kupata njia sahihi ya kupita? Olivia Komba alifafanua

“Hawatakuwa tayari kumpoteza David kama mpango wao haujakamilika, hivyo basi watamtafuta kwa udi na uvumba ili wampate. Unafikiri watamchukua nani kama siyo wewe? Yakupasa kuwa makini na jambo hilo”

Winnie Ngocho alielewa maana ya Olivia Komba lakini bado alitengeneza swali lingine kichwani kwake na aliona haitakuwa vizuri akiacha swali hilo liendelee kumsumbua, akaamua kuuliza ili apate maelezo zaidi

“Unasema yanipasa kuwa makini, kivipi?”

Olivia Komba alitabasamu, sio kwamba alikuwa na furaha juu ya swali la Winnie Ngocho, hapana, tabasamu lake halikuhusiana na swali la Winnie Ngocho bali aliamua kurudisha sura angavu usoni kwake ili kuruhusu akili yake kufanya kazi kwa ufanisi. Akajibu swali aliloulizwa

“Ndiyo, unahitaji umakini haswa. Lazima makazi yako yasifahamike ili kujiweka mbali na maharamia. Lazima uwe mafichoni”

Macho yalimtoka Winnie Ngocho baada ya kusikia alitakiwa kuhama makazi yake, alimtazama Olivia Komba akiwa mdomo wazi, mtazamo wake ulidhihirisha hakuamini alichokisikia. Alijaribu kumuuliza Olivia Komba kuhusu kauli hiyo lakini hakuwa kilichobadilika, Olivia Komba alisisitiza suala la Winnie Ngocho kuwa mafichoni. Winnie Ngocho alifikiria atajificha wapi akakosa kwa sababu hakuwa na upande wa familia uliokuwa ukimuunga mkono, hasa baada ya tukio la mtoto na David Samson kupotea katika mazingira ya kutatanisha. Ndugu wa pande zote mbili walimuona mzembe hasa baada ya kukosa majibu ya maswali waliyomuuliza. Ilibidi Winnie Ngocho afafanue tena kuhusu mtihani huo wa kifamilia, Olivia Komba alielewa kwa asilimia zote na alikuwa tayari kutatua tatizo hilo. Olivia Komba alimwambia Winnie Ngocho

“Nitajua wapi pa kukuweka?”

Winnie Ngocho hakuwa na neno lolote zaidi ya kukubali kauli ya Olivia Komba. Walipanga iwe siri kati yao. Hakuna aliyeagwa katika makazi aliyokuwa akiishi Winnie Ngocho. Maisha mapya yalianza, maisha yaliyoambatana na visa na mikasa ya kutisha.

ITAENDELEA
 
RIWAYA: MATEKA
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890

(KIPANDE CHA SABA)

Toyota Probox nyeupe ilifunga breki jirani kabisa na nyumba aliyopanga David Samson na mpenzi wake, kisha msichana wa makamo anayekadiriwa kuwa na miaka ishirini na saba akashuka kwa utaratibu uliotukuka, msichana yule hakuwa na papara wala haraka yoyote. Alikuwa makini akiamini alichokuwa akienda kukifanya. Msichana huyo alivaa gauni la bluu lililofanana rangi na viatu vyake vya mchuchumio. Alistahili kuitwa mrembo. Alikuwa na kazi ngumu lakini aliamini lazima afanikiwe kwa namna moja ama nyingine. Alitazama saa yake ya mkononi ikamuonesha ilikuwa saa kumi na moja na robo jioni, akatabasamu baada ya kuona alikuwa ndani ya muda. Akafungua mkoba wake ghari kisha akachomoa kioo kidogo akajitazama usoni, akajifuta jasho kwa leso kisha akarekebisha nywele zake alizohisi zilitawanyika kidogo. Alipohakikisha yupo sawa, akafunga mlango wa gari lake kisha akaanza kupiga hatua kuelekea katika nyumba aliyoikusudia. Alifika uwani, akawakuta akina mama wawili, mmoja akiwa anasuka mwingine akiwa anasukwa. Baada ya salamu aliuliza

“Nafikiri hapa ndipo anapokaa David Samson?”

Wale akina mama walimkazia macho yule mgeni kisha aliyekuwa akisukwa nywele za uzi akamjibu mrembo aliyekuwa mbele yao

“Wala hujakosea mtoto, gonga mlango ule waweza pata majibu zaidi”

Yule mama alimuelekeza mgeni wao mlango wa kugonga, ulikuwa mlango wa nyumba aliyopanga David Samson na mpenzi wake. Mgeni alielewa maana ya kuambia agonge mlango alioelekezwa, lakini kuna kitu kilimshangaza, kitu kile kilimuongezea swali la udadisi. Alijiuliza mwenyewe

“Kwanini walitazamana baada ya kuwauliza kuhusu David? Kuna nini kinachoendelea!”

Alihisi kuna kitu kipo nyuma ya mlengwa wake, kwakuwa alienda kwa ajili ya David Samson alielewa lazima atajua kila kitu ili kazi aliyokabidhiwa aikamilishe kwa wakati husika. Hakika akijipumbaza mwenyewe, hakujua ugumu uliokuwa mbele ya kazi yake, hakujua kabisa. Alifika kwenye mlango alioambiwa agonge, alikaribishwa na pazia leupe lenye mchanganyiko wa maua mekundu na kijivu. Hali ya hewa iliyoathiriwa na kiupepo cha jioni ilimsaidia kuipeperusha pazia ile na kufanikiwa kuuona mlango umefungwa, awali hakujua kama ulikuwa umefungwa na funguo au ulikuwa umeegeshwa. Aligonga mlango kama alivyoagizwa, hali ya ukimya ilitawala. Hakusikia sauti yoyote toka ndani ikiitikia. Akaongeza nguvu ya ugongaji wa mlango, hakika nguvu iliongezeka maradufu kwa sababu alivisikia vidole vyake vikimwambia apunguze nguvu, aliviumiza. Bado ukimya uliendelea kutawala, akadhani labda ndani hapakuwa na mtu yeyote lakini akili ikakataa baada ya kukumbuka kauli ya mwanamke aliyekuwa akisukwa

“Wala hujakosea mtoto, gonga mlango ule waweza pata majibu zaidi”

Kauli ile ilimaanisha muhusika aliyestahili kumjibu alikuwa ndani, lakini kwa nini ukimya ulitawala? Kilikuwa kitendawili kilichomsumbua. Akili ikamwambia arudi kwa wale akina mama kwakuwa wao walikuwa wenyeji basi awatumie kumpata mwenyeji aliyemfuata, lakini kabla hajapiga hatua hata moja kuondoka mbele ya mlango uliofungwa ghafla alishuhudia ukifunguliwa kisha akakutanisha uso na msichana aliyeonekana kuchoshwa na usingizi, alilitambua hilo kwa sababu muonekano wake ulijieleza vizuri. Sura ilikuwa na makunyazi ya usingizi, vile vile alikuwa amevaa kanga juu na chini kitu kilichomaanisha alijitanda haraka ili aende kumsikiliza aliyekuwa akigonga mlango wake. Msichana aliyetoka usingizini aliongea kwa sauti dhaifu

“Karibu dada, sijui nikusaidie nini?”

Kauli hiyo ilimtoka akiwa katikati ya kizingiti cha mlango, kitendo hicho kilimaanisha alitaka kumaliza shida ya mgeni wake mahali pale pale na siyo kumuingiza ndani mtu asiyemjua. Mgeni alielewa kila kitu, alimkazia macho mwenyeji wake kisha akamjibu kwa nidhamu iliyotukuka

“Nimekuja kuongea na David, nafikiri wewe utakuwa mkewe au nimekosea?”

Swali hilo lilipita vizuri katika masikio ya Winnie Ngocho na hakika alilisikia vizuri kabisa lakini lilimshangaza, yaani msichana mrembo anamuulizia David Samson nyumbani kwake? siyo kwamba alihisi atakuwa mwanamke wa mpenzi wake, hapana, bali alihisi kuna mchezo alikuwa akichezewa kuhusu matukio yaliyokuwa yakiendelea kuhusu mpenzi wake. Hali ya uchovu wa usingizi ikamruka maradufu, makunyazi yakapotea kabisa, akawa Winnie Ngocho aliyezoeleka, Winnie Ngocho mwenye kisura cha kitoto. Winnie Ngocho alimtazama mgeni wake kuanzia chini mpaka juu, akaona jinsi alivyopendeza, kupendeza kule hakukumpa mashaka sana bali mashaka aliyapata baada ya kuthaminisha vito vya thamani alivyokuwa amevaa mgeni wake, alijihakikishia alikuwa amevaa vitu vya gharama sana. Akili yake ilimuaminisha kuwa mgeni huyo atakuwa miongoni mwa watu wanaomsumbua kipenzi chake. Mapigo ya moyo yakaongeza kasi, akaona jinsi walivyokuwa wakiendelea kuishambulia familia yake. Alishindwa kujizuia kuruhusu machozi yatengeneze njia katika mashavu yake baada ya kumkumbuka Lucia wake, mtoto wake wa pekee aliyechukuliwa na wafanya biashara haramu ya madawa ya kulevya. Kitendo cha kuruhusu machozi yapite katika mashavu yake kilimshangaza sana mgeni aliyekuwa akisubiri kupatiwa majibu ya swali alilouliza. Winnie Ngocho alijitahidi kupambana na hisia zilizosababisha aendelea kutoa machozi lakini alishindwa, machozi yaliendelea kuteremka bondeni kutoka juu ya kilima kilicho jirani ya pua. Mgeni akauliza kwa haraka

“Kuna shida gani mdogo wangu?”

Hakika alistahili kumuita mdogo wangu kwa sababu umbile lilimthibitishia hilo, Winnie Ngocho alijikaza kwa shida sana kisha akajibu

“Wewe ni nani na kwanini unamuulizia David?”

Lilikuwa swali lepesi sana kwa mgeni lakini hakupenda kulijibu akiwa amesimama wima namna ile, alitamani apate sehemu ya kukaa ili waulizane maswali kinaga ubaga. Kipindi mambo hayo yakiendelea wale akina mama waliokuwa kwenye ususi walikuwa makini kuangalia kila kilichokuwa kikiendelea. Mgeni alielewa hilo, ikabidi amwambie Winnie Ngocho

“Sijui nikwambie mimi ni nani ili uniamini kwa haraka, lakini kabla sijajielezea chochote ningependa unikaribishe ndani ili tufahamiane vizuri”

Kauli ya mgeni ilisikika vizuri sana katika masikio ya Winnie Ngocho lakini ilizidi kumchanganya sana, alishangaa kuona namna mgeni alivyokuwa akijiamini namna ile. Eti akaribishwe ndani ili waongee zaidi! Ulikuwa mshangao wa namna yake. Winnie Ngocho alimkazia macho mgeni wake lakini mgeni hakuwa na hofu wala wasiwasi, alikuwa akitabasamu. Hakika lilikuwa tabasamu bandia, tabasamu la kujaribu kuuhadaa msimamo wa Winnie Ngocho. Kwa kweli mgeni alifanikiwa kwa hilo, Winnie Ngocho aliamua kuchukua maamuzi magumu. Akamkaribisha mgeni ndani. Baada ya kukaa katika kiti cha sofa kilichokuwa na kitambaa kilichochoka, Winnie Ngocho hakuhitaji mgeni apumzike hata sekunde kadhaa, yeye alihitaji ufafanuzi zaidi. Mgeni hakuwa mbishi bali alianza kwa kujitambulisha

“Naitwa Olivia Komba, mwandishi wa habari kutoka kituo cha redio ya taifa tawi la hapa mkoani”

Winnie Ngocho alikuwa makini kumsikiliza mgeni wake aliyekuwa akiongea kwa kujiamini sana, mgeni hakuwa na dalili ya hofu wala wasiwasi wa aina yoyote. Kitendo kile hakikumuaminisha Winnie Ngocho kauli ya mgeni wake, alikumbuka namna alivyowahi kumpokea mgeni akisema alitumwa na mama yake mzazi baada ya kusikia amejifungua mtoto lakini baadae alipofungua zawadi aliyoletewa na mgeni huyo aligundua alidanganywa kama mtoto mdogo. Vile vile alikumbuka namna David Samson alivyomsimulia kisa kilichomtokea, jinsi alivyotekwa na watu waliojitambulisha kwake kuwa ni maofisa wa jeshi la polisi lakini mwisho wa siku alijikuta katika mikono ya wauza madawa ya kulevya. Winnie Ngocho akatabasamu baada ya kuona mgeni wake akiichezea akili yake, akamwambia

“Jua nimekatisha usingizi wangu nikusikilize, sasa usiniletee habari nisizozielewa. Kama na wewe umetumwa sema ulichotumwa”

Mrembo aliyejitambulisha kwa jina la Olivia Komba aliisikia vizuri kauli ya jeuri ya Winnie Ngocho, siyo kwamba ilimuudhi, la hasha, bali ilimuongezea maswali ya udadidi. Alijikuta akijiuliza maswali akilini

“Eti kama nimetumwa? Na nani?”

Alitamani kuuliza swali lakini alikuwa amechelewa, Winnie Ngocho aliendelea kumshambulia kwa maneno yaliyodhihirisha alimtilia mashaka Olivia Komba

“Eti mwandishi wa habari! Mwandishi gani usiye na kifaa chochote cha kuchukulia Habari? Unafikiri mimi ni mjinga kiasi hicho!”

Ujasiri wa ajabu ulikuwa moyoni mwa Winnie Ngocho, alijikuta akiropoka maneno makali mbele ya mgeni wake. Alielewa mgeni ule alikuwa miongoni mwa watu hatari walioiweka familia yake kizuizini. Alitamani kupiga kelele za kumfukuza lakini alielewa haitasaidia chochote. Alisimama wima tofauti na awali, kwa sauti ya upole alimwambia Olivia Komba

“Waweza kuondoka dada yangu”

Olivia Komba aliiona sura ya Winnie Ngocho ilivyokuwa ikimaanisha kauli aliyoitoa, sura nzuri ilikuwa na makunyanzi ya hasira kitu kilichotafsiri hakuhitaji kuendelea kuiona sura ya mgeni wake. Olivia Komba alisimama wima kisha akamwambia Winnie Ngocho

“Hakika upo sahihi, mimi siyo mwandishi wa habari wa kituo chochote cha televisheni, redio wala magazeti. Sihusiki na watu hao, mimi ni askari mpelelezi kutoka makao makuu. Nimekuja hapa kupata maelezo ya kutosha kuhusu mpenzi wako kwa sababu kuna kijana wetu tulimpachika mkoani hapa kupambana na masuala ya madawa ya kulevya lakini mwisho wa siku ameungana nao”

Kauli ya Olivia Komba ilikuwa ndefu sana lakini haikuwa na kizuizi chochote cha kueleweka, Winnie Ngocho alisikia vizuri maneno yale lakini alihisi akipigiwa kelele. Baada ya kuruhusu funda mbili za mate kulainisha koo lake, Olivia Komba aliruhusu mwayo uliotoa hewa aliyoiingiza mwilini muda mfupi uliopita kisha akaendela

“Nasikia mume wako alishawishika kujiunga katika biashara hizo na mpaka sasa anashirikiana na kijana wetu katika biashara hiyo haramu. Nimekuja hapa ili nifahamu kila kitu ili nifahamu wapi pa kuanzia”

Kipindi akiongea kauli hiyo alikuwa akikagua mkoba wake kisha akachomoa kitambulisho chake cha kazi akamkabidhi Winnie Ngocho aliyekuwa amesimama kama mlingoti wa umeme. Winnie Ngocho alikipokea kisha akasoma jina kwa sauti ya chini, sauti iliyosikika vizuri ndani ya sebule yake

“Olivia Komba”

Kitambulisho kilijieleza kuwa Olivia Komba alikuwa polisi kutoka idara ya CID (Criminal Investigation Department). CID ni idara maalumu ya upelelezi katika jeshi la polisi. Maofisa wa polisi katika idara hiyo hupaswa kupeleleza mambo makubwa ya jinai kama makosa ya udanganyifu, ulaghai, wizi, unyang`anyi wa kutumia silaha, uhujumu uchumi, ugaidi, kugushi nyaraka na uhalifu mwingine wa aina yoyote unaoweza kuathiri taifa au mataifa. Winnie Ngocho aliinua kichwa chake kisha akamtazama mrembo aliyekuwa akiendelea kutabasamu, kipindi Winnie Ngocho akitafakari kauli aliyotaka kuongea, Olivia Komba alimuwahi kutoa kauli, Olivia Komba aliendelea kutoa ufafanuzi

“Inspekta Jenerali wa Polisi (Inspector General of Police – IGP) ndiye aliyetoa amri nifatilie suala hili mpaka nihakikishe limepatiwa ufumbuzi yakinifu”

Kauli ya Olivia Komba ilimshangaza sana Winnie Ngocho, kauli iliyosema Olivia Komba alikuwa kazini kwa amri ya IGP. Winnie Ngocho aliona ukubwa wa tatizo hilo kwa sababu IGP ndiye kiongozi wa ngazi ya juu wa jeshi la polisi nchini, kiongozi ambaye husaidiwa kazi zake na makamishna wa polisi pamoja na wakuu wa polisi wa mikoa. Winnie Ngocho alianza kumuamini Olivia Komba aliyekuwa akimtazama usoni, alimuuliza

“Inawezekanaje uje kumchunguza polisi mwenzako?”

Olivia Komba alitabasamu kidogo, akaruhusu meno yake yaliyoathiriwa na dhahabu kuonekana. Aliyavisha dhahabu ili kuficha uhalisia wake, alijiweka kama mrembo wa kisasa kumbe nyuma ya urembo huo alikuwa mpelelezi mwenye viwango vya juu. Akamjibu Winnie Ngocho huku akipokea kitambulisho chake toka kwenye mkono ya mwenyeji wake

“Sote ni polisi wa taifa la Malosha lakini tupo idara tofauti, huyo aliyekengeuka anatoka idara inayopambana na madawa ya kulevya, idara ya mkoa huu. Mimi natokea idara ya upelelezi. Tupo sehemu mbili tofauti, ingawa jeshi la polisi ni moja…suala langu ni siri kubwa, hakuna polisi mwingine anayejua nimepachikwa kufatilia jambo hili. Anayejua ni CID aliyetoa kazi na kiongozi wa idara ya upelelezi pekee”

Winnie Ngocho alikuwa kimya, hakuwa na uwelewa wa kutosha kuhusu jeshi la polisi. Alimuacha mwenye uwelewa adadavue kinaga ubaga. Hakika alidadavua. Olivia Komba aliendelea, kitendo kile cha kuendelea ndicho kilichozua taharuki katika kichwa cha Winnie Ngocho. Olivia Komba alisema

“Ulishalisikia jina la Alimas Jumbe? Nasikia siku hizi anajiita Zimwi na amefuga rasta fupi”

Jina la Zimwi halikuwa geni katika masikio ya Winnie Ngocho, alikumbuka alishawahi kulisikia sehemu. Alifikiria muonekano wa rasta fupi, alikumbuka kitu. Alikumbuka kipindi alipokuwa hospitali aliambia alilipiwa gharama za matibabu na kijana aliyejitambulisha kwa jina hilo, kijana mwenye rasta fupi aliyemwambia nesi kuwa alikuwa mdogo wake wa mwisho. Mshangao uliteka taswira ya Winnie Ngocho lakini kabla hajastaajabu zaidi suala hilo alizidi kuchanganywa na kauli ya Olivia Komba

“Kijana anayejiitwa Zimwi ndiye polisi aliyetusaliti”

Winnie Ngocho alikosa jibu la kutoa, alimkodolea macho Olivia Komba, macho yalieleza fika kuwa alishangazwa na taarifa hiyo. Alihisi akiishiwa nguvu, kizunguzungu kikaanza kumnyemelea kama mwindaji amnyemeleavyo windo lake. Akakaa kwenye kiti kisha akainua sura yake kumtazama mgeni aliyekuwa bado amesimama wima tayari kwa kuondoka. Winnie Ngocho aliuona umuhimu wa Olivia Komba katika matatizo yaliyokuwa yakisumbua familia yake. Akamwambia

“Olivia, waweza kukaa tuongee vizuri”

Olivia Komba hakutengeneza mazingira ya ubishi wowote kwa sababu lilikuwa ndiyo kusudio lililompeleka, alifika ili apate nafasi ya kuonana mtu atakayempatia taarifa kamili kuhusu David Samson. Alikaa kwenye sofa kisha akasubiri kauli ya mwenyeji wake. Winnie Ngocho alimkazia macho Olivia Komba kisha akamuuliza kwa kuhamaki

“Umesema kijana anayeitwa Zimwi ni polisi mpelelezi?”

Lilikuwa swali la kitoto kwa sababu lilikuwa limeshatolewa ufafanuzi toka awali. Kitendo cha Winnie Ngocho kuuliza akiwa kwenye hali iliyoonesha wazi kuchanganyikiwa kilisababisha Olivia Komba afahamu kuna uwezekano mkubwa Winnie Ngocho akawa anafahamu kitu au vitu vinavyoweza kuwa mwangaza katika kazi yake ya kipelelezi. Hakujibu swali la Winnie Ngocho wala hakusubiri kauli nyingine kutoka kwake bali aliuliza swali, aliamini kupitia swali lake angeweza kupata majibu yakinifu. Na ndivyo ilivyokuwa

“Unafahamu chochote kuhusu mtu huyo? Namaanisha Zimwi”

Winnie Ngocho hakujiuliza mara mbili wala hakufikiria sana kuhusu jibu la kutoa bali alitigisa kichwa juu chini akimaanisha kukubali kuwa alifahamu mambo kumuhusu Zimwi. Kitendo kile kilimuongezea umakini Olivia Komba, siyo kwamba alisahau kabisa kuuliza kuhusu masuala ya David Samson, hapana, lakini alifahamu akijua mambo kuhusu Zimwi atakuwa amefahamu baadhi ya mambo kuhusu David Samson. Hivyo basi aliamini utakuwa mwanzo mzuri wa kuuwa ndege wawili kwa wakati mmoja. Olivia Komba alirudisha macho katika taswira ya Winnie Ngocho kisha pasipo kuchelewa akauliza swali, swali lililohitaji ufafanuzi wa ishara ya kichwa aliyoionesha

“Unaelewa nini kuhusu Zimwi?”

Kipindi Winnie Ngocho akifikiria wapi alistahili kuanzia katika maelezo yake, Olivia Komba alikuwa akisogea mahali alipokaa awali kisha akakaa kitako akisubiri majibu kutoka kwa mwenyeji wake. Hali ya ukimya ikaendelea pasipo kutegemea, kitendo kile kilimshangaza sana Olivia Komba akashindwa kuelewa kwanini Winnie Ngocho alikuwa na kigugumizi cha kuongea. Winnie Ngocho alifungua mdomo wake, ufunguzi huo wa mdomo haukujibu swali aliloulizwa bali alitoa ufafanuzi mwenye mashaka ndani yake. Alisema kwa sauti ya kitetemeshi

“Najua David na mwanangu wapo mikononi mwa kijana huyo anayejiita Zimwi, najua kabisa. Suala la wewe kutaka taarifa za Zimwi kutoka kwangu ni kutaka kuangamiza familia yangu endapo mtu huyo akifahamu mimi ndiye chanzo cha taarifa hizo. Nafikiri natakiwa kutafuta njia nyingine ya kuisaidia familia yamgu”

Maneno ya Winnie Ngocho yalisikika vizuri katika masikio ya Olivia Komba, japokuwa yalionesha hali ya pingamizi lakini yalimfunulia kitu mpelelezi yule. Awali hakujui kama David Samson alikuwa na mtoto, na mtoto huyo yupo mikononi mwa watu wabaya. Sasa alipata picha na kuelewa kwanini Winnie Ngocho alitengeneza hofu, lengo la hofu lilikuwa kuilinda familia yake. Olivia Komba aliona jinsi Winnie Ngocho alivyojitahidi kuilinda familia hiyo lakini kwa njia ya kitoto. Olivia Komba aliamini Winnie Ngocho alitakiwa kumchangamkia kwa kutoa taarifa pasipo kuangalia upande hasi kuliko upande chanya. Olivia Komba aliuliza swali ili ahakikishiwe taarifa aliyoisikia

“Unasema mwanao yupo mikononi mwa Zimwi?”

Winnie aliitikia kwa kichwa akimaanisha kukubaliana na swali hilo. Kitendo kile kilimuhakikishia Olivia Komba kuwa David Samson atakuwa mikononi mwa watu waovu siyo kwa matakwa yake bali kwa shinikizo ili aokoe maisha ya mtoto wake. Aliamini sio rahisi mtu kuingia katika kundi la kigaid akiwa na mwanao, aliona namna mtoto wa David Samson alivyotumika kama ngao. Olivia Komba akakumbuka kitu, akaamua kuuliza haraka

“Mwanao alichukuliwa lini? Na ana miaka mingapi?”

Ilikuwa zamu ya Winnie Ngocho kufafanua kila kitu, hakuna alichoficha. Alieleza kila kitu kuhusu mahusiano yake na David Samson, alieleza jinsi familia zao zilivyowatenga kwa sababu walilazimisha kuishi pamoja pasipo idhini ya familia zao. Hakuna alichoficha kuhusu mkasa uliokuwa ukiwaandama wana familia hao. Namna David Samson alivyoshawishiwa na rafiki yake kujiingiza kwenye biashara ya madawa ya kulevya, namna David Samson alivyokamatwa na watu waliojitambulisha kwake kuwa maofisa wa jeshi la polisi. Mwisho wa simulizi yake alifafanua alivyonyang`anya mtoto wake wa pekee na vijana wawili waliokuwa na misuli iliyosambulia miili yao. Alieleza mtoto wake alikuwa chini ya mwezi mmoja, mtoto anayehitaji malezi kamili ya mama na baba yake. Maelezo ya Winnie Ngocho yalimtoa machozi Olivia Komba, alitoa kitambaa katika mkoba wake kisha akafuta chozi taratibu huku akifikiria kauli stahiki aliyostahili kuongea. Aliongea kwa sauti nyororo

“Maisha yako yapo matatani, usifikiri kama upo salama hata kidogo”

Winnie Ngocho alimkazia macho Olivia Komba baada ya kusikia kauli kuwa maisha yake yalikuwa matatani, siyo kwamba alipingana na kauli hiyo, la hasha, bali alihitaji ufafanuzi zaidi aweze kujikinga na matata hayo. Macho ya Winnie Ngocho yalijieleza kwa kiasi kikubwa, yalitoa picha ya kuhitaji ufafanuza. Olivia Komba alielewa hali ya mwenyeji wake, haikuwa kazi ngumu kufahamu hali hiyo kwa sababu alikuwa na mafunzo ya kutosha ya kumsoma mtu anayeongea naye. Akafafanua kauli yake

“Kama ulivyosema, David yupo mikononi mwa watu wanaojifanya wanapambana na wauza madawa ya kulevya lakini watu hao wamemchukua mtoto wako kama ngao ya kumtumikisha mpenzi wako. Yakupasa kufikiria kwa makini kwa sababu hakuna polisi anayeweza kutumia mbivu hiyo ili aweze kupata taarifa, mbinu gani ya kumtoa mtoto katika titi la mama yake. Haiwezekani. Hao ni majambazi wazoefu”

Olivia Komba alijinyoosha kama mtu aliyetoka usingizini. Akamtazama Winnie Ngocho aliyekuwa ameinamisha kichwa chini lakini masikio yakiwa makini kama kinasa sauti cha mpelelezi kinapokuwa kazini. Olivia Komba akaendelea kutoa ufafanuzi

“Najua David anatafuta njia ya kumuokoa mtoto wenu toka kwa maharamia, endapo akifanikiwa kutoroka lazima maharamia waangalie sehemu nyingine ya kumdhibiti ili waweze kumpata kirahisi. Sehemu hiyo ni wewe”

Winnie Ngocho aliinua kichwa chake akamtazama Olivia Komba aliyekuwa akiendelea kufuta machozi yaliyotengeneza mifereji katika mashavu yake. Sio kwamba Olivia Komba alikuwa akimlilia David Samson au Zimwi aliyewasaliti, hapana, bali alikuwa akimlilia mtoto Lucia, mtoto wa David Samson na Winnie Ngocho, mtoto aliyeingizwa kwenye adha za dunia akiwa na umri chini ya mwezi mmoja. Kitendo cha Winnie Ngocho kuona mifereji ya machozi katika mashavu ya mgeni wake kilimuongezea hisia kali juu ya familia yake, alijikuta akilia, tena siyo kilio cha lele mama bali kilio kilichoambatana na kwikwi. Sasa ilikuwa kazi ya Olivia Komba kumtuliza Winnie Ngocho, alimnyamanzisha kama mama afanyavyo kwa mtoto wake wa pekee. Ilimchukuza zaidi ya dakika mbili kutuliza kilio cha mwenyeji wake. Winnie Ngocho hakuwa na jinsi zaidi ya kunyamanza kwa sababu alisikia kauli ya Olivia Komba, kauli iliyomwambia kuwa kilio chake hakitamsaidia kuokoa familia yake bali ujasiri wake ndiyo unaohitajika. Hakika aliamini alistahili kuwa jasiri, na aliapa mbele ya Olivia Komba kuwa atakuwa jasiri kuhakikisha familia yake inakuwa salama. Alijikuta akiongea hivyo kwa ujasiri lakini hakujua atafanya nini ili kufanikisha maneno aliyoongea, hakika hakujua chochote. Kauli ya Olivia Komba ikajirudia kichwani kwake

“Najua David anatafuta njia ya kumuokoa mtoto wenu toka kwa maharamia, sasa endapo akifanikiwa kutoroka lazima maharamia waangalie sehemu nyingine ya kumdhibiti ili waweze kumpata kirahisi. Sehemu hiyo ni wewe”

Alikuwa Winnie Ngocho mpya, siyo Winnie Ngocho aliyelia kama mtoto dakika chache zilizopita. Alikuwa tayari kuelewa kila kitu ili awe sehemu ya kufanikisha zoezi la kuipata familia yake. Aliitafakari kauli hiyo akahisi bado ilikuwa na utata kichwani kwake, akaomba kupewa ufafanuzi yakinifu. Olivia Komba hakuwa mbishi hata kidogo, atakuwa vipi mbishi wakati alihitaji ushirikiano wa Winnie ili aweze kupata njia sahihi ya kupita? Olivia Komba alifafanua

“Hawatakuwa tayari kumpoteza David kama mpango wao haujakamilika, hivyo basi watamtafuta kwa udi na uvumba ili wampate. Unafikiri watamchukua nani kama siyo wewe? Yakupasa kuwa makini na jambo hilo”

Winnie Ngocho alielewa maana ya Olivia Komba lakini bado alitengeneza swali lingine kichwani kwake na aliona haitakuwa vizuri akiacha swali hilo liendelee kumsumbua, akaamua kuuliza ili apate maelezo zaidi

“Unasema yanipasa kuwa makini, kivipi?”

Olivia Komba alitabasamu, sio kwamba alikuwa na furaha juu ya swali la Winnie Ngocho, hapana, tabasamu lake halikuhusiana na swali la Winnie Ngocho bali aliamua kurudisha sura angavu usoni kwake ili kuruhusu akili yake kufanya kazi kwa ufanisi. Akajibu swali aliloulizwa

“Ndiyo, unahitaji umakini haswa. Lazima makazi yako yasifahamike ili kujiweka mbali na maharamia. Lazima uwe mafichoni”

Macho yalimtoka Winnie Ngocho baada ya kusikia alitakiwa kuhama makazi yake, alimtazama Olivia Komba akiwa mdomo wazi, mtazamo wake ulidhihirisha hakuamini alichokisikia. Alijaribu kumuuliza Olivia Komba kuhusu kauli hiyo lakini hakuwa kilichobadilika, Olivia Komba alisisitiza suala la Winnie Ngocho kuwa mafichoni. Winnie Ngocho alifikiria atajificha wapi akakosa kwa sababu hakuwa na upande wa familia uliokuwa ukimuunga mkono, hasa baada ya tukio la mtoto na David Samson kupotea katika mazingira ya kutatanisha. Ndugu wa pande zote mbili walimuona mzembe hasa baada ya kukosa majibu ya maswali waliyomuuliza. Ilibidi Winnie Ngocho afafanue tena kuhusu mtihani huo wa kifamilia, Olivia Komba alielewa kwa asilimia zote na alikuwa tayari kutatua tatizo hilo. Olivia Komba alimwambia Winnie Ngocho

“Nitajua wapi pa kukuweka?”

Winnie Ngocho hakuwa na neno lolote zaidi ya kukubali kauli ya Olivia Komba. Walipanga iwe siri kati yao. Hakuna aliyeagwa katika makazi aliyokuwa akiishi Winnie Ngocho. Maisha mapya yalianza, maisha yaliyoambatana na visa na mikasa ya kutisha.

ITAENDELEA

Safi sana mwendelezo mkuu
 
RIWAYA: MATEKA
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890

(KIPANDE CHA NANE)

Giza lilianza kuufukuza mwanga taratibu, mwanga haukuwa na ubishi wowote kwa sababu ulikuwa umeshatawala kipindi chake cha kuanzia asubuhi mpaka jioni. Sasa ulikuwa usiku, zamu ya ndugu yake giza, ndugu asiyeweza kuchangamana nae hata siku moja. Undugu wa giza na mwanga ni kama undugu wa ardhi na mbingu. Sina hakika kama unastahili kuitwa undugu au uadui. Kijana mmoja kati ya wawili waliokuwa ndani ya gari lililoegesha jirani kabisa na ofisi ya Derrick Edward, alitazama saa yake ya mkononi ikamuonesha ilikuwa saa moja na dakika thelathini jioni. Akatabasamu kisha akamwambia mwenzake.

“Hatuna muda wa kupoteza, yatupasa kufanya kilichotuleta kabda mlengwa hajatoka ofisini kwake”

Kijana mwenzake aliyekuwa nyuma ya usukani wa gari aina ya Toyota Crown Athletic aliitikia kwa sauti ndogo, sauti iliyoafikiana na mwenzake. Kijana aliyekuwa nyuma ya usukani wa gari akaingiza mkono katika mfuko wa suruali ya jinzi aliyovaa, mfuko wa upande wa kulia kisha akachomoa bastola ndogo yenye asili ya Urusi iitwayo Strizh. Akaitazama ukamilifu wa risasi zake kwa kufungua sehemu ya risasi. Zilikuwa sawa kama alivyohitaji. Sasa alielewa kauli ya jamaa yake iliyosema hawakuwa na muda wa kupoteza, alijihakikishia usemi huo baada ya kuona ukamilifu wa silaha zao. Akamtazama mwenzake aliyemfahamisha kuhusu muda, aliyekuwa pembeni yake akitazama kisu chake kirefu alichozoea kufanyia matukio ya mauaji, kisu kilichozoeleka kutengenezwa nchini Russia, kinachofahamika kwa jina la Kindjal Dolch. Kisu kilikuwa ndani ya ghala lake la kuhifadhi lakini kilikuwa tayari kwa kufanya tukio lililokuwa mbele yake. Kijana aliyekuwa nyuma ya usukani akajibu kauli ya mwenzake

“Nafikiri hatuna cha kusubiri”

Walifungua milango ya gari na kuelekea nje, kila mmoja alifungua mlango uliokuwa upande wake. Silaha zilirudi mafichoni, bastola ilikuwa kiunoni kwa kijana aliyekuwa nyuma ya usukani wa gari awali, vile vile kisu cha kijasusi kilikuwa kiunoni kwa kijana aliyekuwa pembeni ya dereva. Walikuwa tayari kutimiza jukumu lao, maagizo waliyopewa yalikuwa yakijirudia mara kwa mara. Maagizo yaliyosema wajaribu kumkamata mlengwa wao akiwa mzima lakini endapo ikitokea hali ya hatari juu yao wafanye lolote litakalowezekana, kauli hiyo ilimaanisha waliruhusiwa kumuua muhusika wao endapo akijaribu kuwashambulia. Vijana wale hawakuwa na cha kupoteza, wao waliamini katika kumwaga damu, kauli ya kwanza haikuwa na maana sana kwao, wao waliamini katika kauli ya pili, kauli iliyowapa ruhusa ya kuondoa roho ya muhusika wao. Wao walizoea kuua kuliko kuteka. Walipiga hatua taratibu kuelekea katika ofisi ya Derrick Edward.

Kipindi hatua zikiendelea, Derrick Edward pasipo kujua chochote kilichokuwa kikiendelea alionekana akitoka ndani ya ofisi yake kisha akafunga mlango wa ofisi tayari kwa kuondoka. Hakujua kama alikuwa mawindoni, hakujua vijana waliokuwa wakielekea uelekeo wake walikuwa tayari kuchukua uhai ulikuwa ndani ya mwili wake. Lakini hali ilikuwa tofauti, hali haikuwa sawa na mpangilio wa wauaji waliokuwa kazini kwa sababu kipindi wakiendelea kupiga hatua uelekeo wa Derrick Edward walishuhudia gari aina Brevis likiwa mwendo kasi na kuelekea uelekeo ule ule. Kitendo kile kiliwashangaza vijana waliojiandaa kuua, walihamaki wakataka kuchomoa silaha zao kwa ajili ya kushambulia lakini walikuwa nyuma ya muda, walishangaa kuona wakishambuliwa wao. Kitendo kile kilisababisha wakimbie haraka na kujifika nyuma ya mti mkubwa wa mwembe uliokuwa jirani ya ofisi ya Derrick Edward. Derrick Edward alihamaki kwa mshtuko mkubwa baada ya kushuhudia milio ya risasi ikirindima kama ngoma mbele yake, alitamani kukimbia kwa sababu hakujua chochote kilichokuwa kikiendelea, akili ilikufa ganzi, akili yake ilimsaliti.

Laiti kama angeliweza angelikimbia mbio kama mshale kuliko kuendelea kushangaa eneo lile. Gari aina ya Brevis lilipiga breki mbele ya Derrick Edward aliyekuwa ametumbua macho kama mjusi aliyebanwa na mlango kisha vijana watatu kila mmoja akiwa na silaha ya moto aina ya SMG wakashuka na kumshurutisha kupanda gari lao. Japokuwa Derrick Edward hakuelewa kilichokuwa kikiendelea lakini alielewa ilikuwa hali ya hatari, alielewa ilikuwa vita dhidi yake lakini hakuwajua maadui zake. Hakubisha kauli ya vijana mwenye silaha kwa sababu aliamini akifanya hivyo atakatisha maisha yake. Alipanda gari kama alivyoamuriwa kisha safari ya mwendo kasi ikaanza huku nyuma ikiacha vumbi kubwa.

Vijana waliokuwa na kusudio la kuondoa uhai wa Derrick Edward, waliojificha nyuma ya mwembe walivyoshuhudia gari la washambuliaji likiondoka eneo lile walijaribu kulishambulia kwa risasi lakini walichelewa, hata ushambuliaji wao haukuwa na nguvu kwa sababu walikuwa na bastola moja, mwingine alikuwa na kisu. Mwenye kisu alibaki akilitazama gari kwa macho mawili pasipo kujua cha kufanya. Gari liliwaachia vumbi. Hawakujiandaa kwa vita kali kama ile kwa sababu waliamini watamkuta Derrick Edward ofisini kwake kisha wafanye tukio walilokusudia. Hawakujua washambuliaji wale walitoka wapi na walikuwa akina nani lakini wao walichojua walikuwa maadui zao. Kwa mbali walisikia ving`ora vya polisi zikisogea eneo lile, suala lile lilikuwa hatari kwao kwa sababu walielewa endapo wakikutwa na polisi eneo lile ingekuwa hatari zaidi. Wakaamua kuondoka pasipo kupata majibu ya maswali yaliyokuwa vichwani mwao. Japokuwa maswali yalikuwa mengi yaliyokosa majibu lakini kuna maswali yaliwasumbua zaidi, maswali hayo yalikuwa

“Kwanini wavamizi hawakutushambulia baada ya kumchukua Derrick? Walijuaje kama sisi tulikuwa maadui wao au maadui wa Derrick?”

Hakika yalikuwa maswali magumu sana kujibika, kila wapojaribu kufikiria majibu bado walirudi katika maswali magumu. Walikuwa ndani ya gari wakirudi katika ngome ya bosi wao, waliamini lazima wapewe adhabu kubwa kwa kushindwa kutimiza kazi ndogo, kwao ilikuwa kazi ndogo kutimizwa kwa sababu walikuwa wameshashiriki kwenye kazi nyingi ngumu na za hatari zaidi. Walijiandaa kwa lolote lingeloweza kutokea. Gari aina ya Toyota Crown Athletic lilisimama katika eneo linalofahamika kwa jina la Kazengagu kisha kijana mmoja kati ya wawili waliokuwa ndani ya gari hilo akasogea katika mlango wa geti ulioshikiriwa na ukuta mnene kisha akaponyeza kitufe cha kengele (alarm) kwa lengo la kumfahamisha mlinzi wa jumba hilo la kifahari afungue mlango.

Kitendo cha kubonyeza kitufe cha kengele ili mlinzi afahamu uwepo wako hakikumaanisha kuwa ulinzi wa eneo hilo ulikuwa wa lele mama, hapana, bali ulikuwa ni utaratibu uliowekwa na mmiliki wa ngome hiyo ngumu kuingilika. Ngome hiyo ilifungwa kamera kila upande ili kubaini kila kilichokuwa kikiendelea jirani na eneo hilo, hivyo basi hata ujio wa vijana hao ulionekana hata kabla hawajabonyeza kitufe cha kingele. Kwa nje ngome ilionekana kama makazi ya kifahari ya mtu kumbe ndani ilikuwa imejaza vijana wachapakazi mwenye hali na shauku ya kufanya kila linalowezekana kufanikisha zoezi la uuzaji na usambazaji wa madawa ya kulevya unafanyika kwa ufanisi na weledi wa hali ya juu.

Jamii haikujua chochote kuhusu yaliyokuwa yakiendelea ndani ya jumba hilo la kifahari, wao waliona magari ya kifahari yakiingia na kutoka kila wakati. Baadhi ya raia wachache walisikika wakisema mmiliki wa jumba hilo alikuwa mmiliki wa mashimo ya dhahabu lakini walishindwa kufafanua mashimo hayo yalikuwa mkoa gani. Kauli na imani hiyo walijengewa na vijana waliokuwa wakifanya kazi ndani ya ngome hiyo, vijana hao walijipenyeza kwa siri katika mikusanyiko ya watu na kuvumisha uvumi huo. Jamii ikabaki ikiamini kauli hiyo pasipo kujua hata waliovumisha walikuwa washiriki wakubwa wa nyumba ile ya kifahari. Endapo jamii ingelifahamu kama ndani ya jumba lile ndiyo kulikuwa kukifanyika mipango yote ya kuuza na kusambaza madawa ya kulevya ingelipambana usiku na mchana kuisambaratisha nyumba ile.

Vijana wale wawili walioshindwa kutimiza kazi ya mkuu wao wa kikosi cha kigaidi waliingia moja kwa moja mpaka katika sebule ya nyumba ile, waliwakutwa vijana wanne wakiwa makini wakitazama taarifa ya habari iliyokuwa ikirushwa katika kituo maarufu cha televisheni nchini Malosha. Waliposikia habari ile haikuwa ngeni kabisa masikio kwao, ilikuwa ni habari iliyowahusu moja kwa moja. Habari ile ilikuwa ikifafanua tukio la uvunjwaji wa amani na utulivu katika mkoa wao wa Rwama Mwanzo, habari ile ilisema juu ya kikundi cha kigaidi kilichoshambulia ofisi ya mwana sanaa maarufu nchini na nje ya mipaka ya nchi kisha kikafanikiwa kumteka na kuondoka naye kusiko julikana. Habari ile ilionesha wazi hata uongozi wa mkoa wa Rwama Mwanzo na serikali kwa ujumla ilishindwa kuelewa ni akina nani waliomteka Derrick Edward. Kilibaki kuwa kitendawili.

Vijana walioshindwa kutimiza kazi ya kumkamata au kumuua Derrick Edward walikuwa wakitazamana macho kwa macho na vijana wanne waliowakuta sebuleni, sura za wale vijana wanne waliokuwa sebuleni zilikuwa zimekunjamana mithili ya mtu aliyekula kitu kichungu. Hawakuhitaji kufafanuliwa kuhusu suala la kazi waliyopewa wenzao kwa sababu muda mfupi uliopita walisikia na kuona katika televisheni kitendo cha Derrick Edward kuchukuliwa na watu wengine. Walielewa tangu awali kuwa waliofanikiwa kumkamata Derrick Edward hawakuwa wenzao kwa sababu mashuhuda wa tukio walisema walishuhudia vijana watatu wakiwa na silaha za moto wakimshurutisha Derrick Edward kupanda gari, kitendo cha mashuhuda kusema walishuhudua vijana watatu wakifanya tukio hilo kiliwaamisha wana ngome ngumu kuwa watu wao waliowatuma wakamkamate au kumuua Derrick Edward siyo waliofanya hilo tukio kwa sababu wao waliwatuwa wawili wenye bastola moja na kisu, lakini mashuhuda walisema watekaji walikuwa watatu na wenye silaha za moto kila mmoja. Mmoja kati ya vijana wanne waliopata taarifa kupitia televisheni alichukua simu yake ya mkononi akatafuta jina alilolihitaji, alipolipata akapiga. Simu iliita ikakata. Alipiga zaidi ya mara tatu pasipo kupokelewa lakini hakuchoka kupiga. Alikuwa na dhamira ya kuongea na aliyekuwa akimpigia simu hiyo. Alivyopiga mara ya nne simu ikapokelewa, baada ya salamu aliongea

“Vijana waliokwenda kwa Derrick wameshindwa kazi, Derrick ameangukia kwenye mikono isiyo fahamika”

Ilikuwa kauli ya kugadhabisha sana kwa aliyekuwa upande wa pili wa simu, alihisi kama amesikia vibaya lakini aliyempatia taarifa hizo alimsisitiza kuwa alikuwa sahihi wala hajakosea. Hasira zilimjaa sana baada ya kuona mipango yako ikivurugika kizembe. Aliona ni uzembe wa hali ya juu kwa watu wasio julikana kumchukua Derrick Edward mbele ya vijana wake. Hakuwahi kuruhusu lindo lake kupotea machoni kwake hata siku moja, siku hiyo ilikuwa mara ya kwanza. Alimpa maagizo kijana wake aliyempigia simu, yalikuwa maagizo magumu lakini rahisi sana katika kundi hilo. Simu ilikatwa na kiongozi aliyepigiwa, hakika alichanganyikiwa kwa sababu alikata simu ambayo hakupiga yeye. Kijana aliyepewa maagizo sekunde chache zilizopita akawageukiwa vijana wenzake walioshindwa kazi waliyopewa kisha akawaambia

“Wekeni silaha zenu juu ya meza”

Hakuna aliyebisha, waliweka silaha zao kama walivyoagizwa. Meza ilipokea bastola na kisu vyote vyenye asili ya Urusi. Walipoinua vichwa vyao baada ya kuweka silaha zao mezani walikutana na mdomo wa bastola ndogo iliyofungwa kizuia sauti. Macho yaliwatoka, wakaanza kubabaika kwa hofu ya kuuliwa lakini hawakupewa hata sekunde moja ya kujielezea. Risasi ilipenya katika paji la uso la kila mmoja wao. Waligeuka maiti ndani ya sekunde chache zilizofuata
***
Ilipita siku moja na masaa kadhaa tangu Derrick Edward atekwe na watu wasiojulikana, hali ya hewa ilikuwa mbaya sana kwa sababu hakuna aliyefahamu kama alikuwa bado yu hai au alishauliwa na watekaji. Kitendo cha watekaji kuendelea kuwa kimya kiliongeza hofu kwa raia na taifa kwa ujumla. Taifa lilitamani watekaji wajitokeze kwa namna yoyote waseme watakacho au kusudio la kumteka Derrick Edward ili ifahamike namna ya kumtoa katika mikono yao. Ukimya uliendelea kama kawaida. Hofu ilipamba nchini hasa katika mtaa ulikuwa na ofisi ya sanaa ya Derrick Edward. Watu walipunguza kutembea ovyo bila sababu ya msingi na waliotembea walirejea majumbani mapema kabla giza halijawa totoro. Waliamua kufanya hivyo kwa sababu hawakujua nani atakuwa wa pili kutekwa.

Olivia Komba alikuwa ndani ya chumba chake cha mazoezi, alikuwa amemaliza kufanya mazoezi mepesi ya viungo. Alizoea kuyaita mazoezi mepesi kwa sababu yalikuwa sehemu ya maisha yake lakini mazoezi hayo hayo mepesi kwa mwingine ni mazoezi magumu tena yasiyopaswa kujaribiwa kwa puta. Sasa alikuwa akisafisha moja ya silaha zake za moto, alikuwa akisafisha bastola aina ya Revolver aliyokuwa akiiandaa kufanyia kazi siku hiyo. Alipomaliza kuisafisha aliipanga na kuifunga vizuri. Ilikuwa bastola tayari kwa kufanya matukio ya kipelelezi. Alichukua taulo akajifuta jasho kisha akaondoka eneo lile na kuelekea bafuni huku kichwa kikifikiria juu ya kazi ya kipepelezi aliyoianza. Ndani ya chumba chake cha mazoezi kulikuwa na vifaa vingi vya mazoezi ya viungo, hilo halikua jambo la ajabu hata kidogo.

Jambo la ajabu lilikuwa moja, ndani ya chumba hicho alibandika picha za watu waliokuwa sehemu ya upelelezi wake, maadui pamoja na watu wengine aliohisi walikuwa sehemu ya msaada katika kufanikisha jambo alilokusudia. Ukuta ulichakazwa kwa picha za Winnie Ngocho, David Samson, Zimwi, Nasrat Abdul al Aziz pamoja na wengine aliohisi walifaa kuwa kwenye orodha hiyo. Picha ya Derrick Edward haikuwa sehemu ya picha hizo kwa sababu kipindi alipoanza shughuli yake hakujua uwepo wa mtu huyo katika matukio yalikuwa yakiendelea, lakini baada ya tukio la kutekwa kwa Derrick Edward alifikiria kubandika picha yake. Ukiachana na picha hizo, kulikuwa na picha moja ya mtu wa makamo aliyevaa soksi usoni, soksi ile ilisababisha kutofahamika kwa mtu huyo.
Japokuwa Olivia Komba ndiye aliyebandika picha zote lakini hata yeye hakumfahamu kabisa mtu huyo mwenye soksi usoni. Kila siku alijitahidi usiku na mchana ili kumbaini lakini hakuna alichoambulia.

Aliamini mtu huyo atakuwa nyuma ya matukio mengi ya kihalifu. Imani hiyo ilimjaa maradufu siku aliyokabidhiwa kazi ya kupeleleza mtandao mzima unaojihusisha na masuala ya madawa ya kulevya mkoani Rwama Mwanzo. Siku hiyo ndiyo alikabidhiwa picha ya mtu mwenye soksi usoni na mkuu wake wa kazi aliyemwambia kuwa hata yeye alikabidhiwa na Inspekta Jenerali wa Polisi (Inspector General of Police – IGP). Maagizo ya IGP yalisisitiza kutafutwa kwa mtu huyo aliyekuwa nyuma ya soksi ili atambulike mapema kwa sababu iliaminika mtu huyo alikuwa ndiyo kila kitu katika mtandao wa wauzaji na wasambazaji wa madawa ya kulevya pamoja na vikundi vingine vya kigaidi vinavyofanya biashara haramu. Ilikuwa kazi ya Olivia Komba kumbaini mtu huyo. Suala la Olivia Komba kufuatilia kisa cha David Samson na askari polisi aliyesaliti kazi yake, Zimwi, aliamini kupitia njia hiyo angeweza kumbaini mtu mwenye soksi usoni. Aliamini akifanikiwa kumdhibiti Zimwi atakuwa amepiga hatua kubwa ya kumfahamu mzee wa makamo aliyekuwa nyuma ya soksi, hakika ulikuwa mtazamo yakinifu aliouamini sana.

Olivia Komba alipanga nyumba kubwa ya kisasa katika mtaa uliochangamka sana, mtaa unaofahamika kwa jina moja ya Bugare. Mtaa huo ni moja ya mitaa mipya katika mkoani Rwama Mwanzo, awali lilikuwa eneo lililojaa miti, kwa lugha nyepesi huitwa msitu. Ongezeko la watu lilisababisha kuvamia na kujenga eneo hilo lililo jirani zaidi na zima Kuu, ziwa lenye sifa ya kupitiwa na bonde la ufa. Mtaa wa Bugare huitwa mji mpya kutokana na muda wake mfupi tangu uanzishwe. Japokuwa ni mji mpya lakini ni miongoni mwa maeneo lenye sifa ya nyumba za kisasa, hivyo basi limehifadhi matajiri wengi. Ukiacha suala la kuwa na nyumba za kisasa na huduma bora za kijamii, watu hupenda sana kuishi eneo hilo kwa sababu lipo jirani na ziwa Kuu hivyo huweza kupata upepo wa ziwa pasipo shida ya aina yoyote.

Olivia Komba hakuiishi peke yake, aliishi na Winnie Ngocho katika makazi yake. Alitaka kumuweka Winnie Ngocho katika makazi salama ili asiweze kudhurika kirahisi na vita iliyokuwa ikiendelea. Alifanikiwa kwa kiasi kikubwa kwa sababu nyumba ile ilikuwa maficho tosha kwa Winnie Ngocho. Nyumba yenye ukuta wa geti na vioo visivyoruhusu mtu wa nje kuona ndani, kwa kweli ilikuwa nyumba yenye ulinzi wa kutosha. Ukiacha uimara wa nyumba hiyo bado getini kulikuwa na walinzi watatu. Olivia Komba aliwaajiri wamasai watatu wadumishe ulinzi katika nyumba aliyopanga. Wamasai hao hawakufahamu kama ndani ya nyumba kulikuwa na mtu mwingine zaidi ya Olivia Komba. Siku zote Winnie Ngocho aliishi kwa usiri sana, na mara chache aliyotoka ndani ya nyumba hiyo kuelekea mtaani alikuwa ndani ya gari ya Olivia Komba. Mara zote walitoka ndani ya gari yenye vioo nyeusi iliyozuia watu wa nje kuwaona watu wa ndani.

Ndani ya wiki moja walikuwa wameshakuwa kama ndugu, waliongea mambo mengi ya kimaisha pasipo kusahau mpango wa Olivia Komba, mpango wa kupeleleza chochote kilichokuwa mbele yake. Olivia Komba hakuchoka kumsisitiza Winnie Ngocho kuwa atafanya juu chini kufanikisha anampata mtoto wake. Aliamini mtoto wake lazima atakuwa kwenye maisha safi kwa sababu alikuwa akitumika kama ngao ya kumshurutisha David Samson. Olivia Komba alikuwa na uhakika kuwa mtoto yule lazima awe hai mpaka siku ya mwisho, lazima awe hai ili David Samson akubali kutumikishwa kama mbwa. Olivia Komba alishindwa kumuhakikishia Winnie Ngocho usalama wa mpenzi wake, alishindwa hilo kwa sababu aliamini baadhi ya wahalifu hufanya mauaji ya watu endapo wakihisi hawana msaada tena kwao, hivyo Olivia Komba aliamini ingewezekana David Samson akauliwa na wahalifu wale pindi wakihisi wamefanikisha malengo yao dhidi yake. Vile vile majambazi hufanya hivyo ili kutunza siri zao, lakini siyo rahisi kumuua mtoto asiyejua chochote.

Olivia Komba aliendelea kumsisitiza Winnie Ngocho kuwa, mara kadhaa majambazi huwalea watoto kama hao ili wawatumie katika mipango yao ya kijambazi. Watoto hao huwa na roho ngumu ya mauaji kwa sababu ulelewa katika mazingiza ya namna hiyo. Wakati mwingine Watoto hao hupewa historia ya uongo kuhusu familia zao, huambiwa wazazi wao waliuliwa na kikundi ambacho kina upinzani nao, lengo likiwa kupandisha na kuchochea chuki dhidi ya kikundi hasimu na pingamizi kwao. Maneno ya Olivia Komba yalimuingia sawa sawa Winnie Ngocho na aliyaelewa kwa asilimia moja. Ingawa alihakikishiwa kumpata mtoto wake lakini upande wa pili wa akili yake uliamini endapo mpango wa kumpata mwanae ukigonga mwamba, mwanae atawatumikia majambazi. Roho ilimuuma sana, akaona anaweza kuwa amezaa mtoto atakayeingizwa roho za kijambazi na kuwa jambazi sugu atakayelisumbua taifa la Malosha. Machozi yalimtoka lakini hayakumsaidia chochote zaidi ya kulowanisha nguo aliyovaa.

Jioni ya siku hiyo ilikuwa maalumu sana kwa Olivia Komba, ilikuwa jioni aliyohisi ingekuwa na hatua moja au mbili katika harakati zake za kutafuta ufumbuzi wa mafumbo yaliyoenea kila kona ya ubongo wake. Jioni hiyo ilikuwa ya tofauti kwa sababu ya taarifa aliyopata, alitumiwa ujumbe wa meseji kwa namba mpya. Ujumbe ule ulimwambia

“Najua wewe ni mpelelezi uliyetukuka, mpelelezi unayelipigania taifa. Nataka kukwambia kuwa leo usiku katika Kasino ya ‘Just Your body’ itafanyika biashara haramu ya madawa ya kulevya”

Alipojaribu kuipigia namba ile alijibiwa na mtandao kuwa haipatikani, hakuchoka kuipigia kila baada ya dakika tatu mpaka tano lakini jibu lilikuwa lile lile lisiloridhisha. Kabla hajaanza kusafisha silaha yake ya moto aliipigia tena namba ile, iliita pasipo kupokelewa. Alipojaribu kwa mara nyingine alijibiwa na mtandao kuwa namba ile haipo, hapo ndipo alipopata jawabu kuwa mwenye namba ile ameifutia usajili ndani ya muda mfupi uliopita. Alipata shauku ya kutaka kujua alikuwa nani haswa lakini alikosa pa kuanzia. Akaamua kumpigia simu mkuu wake wa kazi ili ampae ushauri. Hakika alipata ushauri yakinifu, ushauri ulioongeza maswali yasiyo na majibu.

ITAENDELEA
FB_IMG_1652590582916.jpg
 
RIWAYA: MATEKA
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890

(KIPANDE CHA NANE)

Giza lilianza kuufukuza mwanga taratibu, mwanga haukuwa na ubishi wowote kwa sababu ulikuwa umeshatawala kipindi chake cha kuanzia asubuhi mpaka jioni. Sasa ulikuwa usiku, zamu ya ndugu yake giza, ndugu asiyeweza kuchangamana nae hata siku moja. Undugu wa giza na mwanga ni kama undugu wa ardhi na mbingu. Sina hakika kama unastahili kuitwa undugu au uadui. Kijana mmoja kati ya wawili waliokuwa ndani ya gari lililoegesha jirani kabisa na ofisi ya Derrick Edward, alitazama saa yake ya mkononi ikamuonesha ilikuwa saa moja na dakika thelathini jioni. Akatabasamu kisha akamwambia mwenzake.

“Hatuna muda wa kupoteza, yatupasa kufanya kilichotuleta kabda mlengwa hajatoka ofisini kwake”

Kijana mwenzake aliyekuwa nyuma ya usukani wa gari aina ya Toyota Crown Athletic aliitikia kwa sauti ndogo, sauti iliyoafikiana na mwenzake. Kijana aliyekuwa nyuma ya usukani wa gari akaingiza mkono katika mfuko wa suruali ya jinzi aliyovaa, mfuko wa upande wa kulia kisha akachomoa bastola ndogo yenye asili ya Urusi iitwayo Strizh. Akaitazama ukamilifu wa risasi zake kwa kufungua sehemu ya risasi. Zilikuwa sawa kama alivyohitaji. Sasa alielewa kauli ya jamaa yake iliyosema hawakuwa na muda wa kupoteza, alijihakikishia usemi huo baada ya kuona ukamilifu wa silaha zao. Akamtazama mwenzake aliyemfahamisha kuhusu muda, aliyekuwa pembeni yake akitazama kisu chake kirefu alichozoea kufanyia matukio ya mauaji, kisu kilichozoeleka kutengenezwa nchini Russia, kinachofahamika kwa jina la Kindjal Dolch. Kisu kilikuwa ndani ya ghala lake la kuhifadhi lakini kilikuwa tayari kwa kufanya tukio lililokuwa mbele yake. Kijana aliyekuwa nyuma ya usukani akajibu kauli ya mwenzake

“Nafikiri hatuna cha kusubiri”

Walifungua milango ya gari na kuelekea nje, kila mmoja alifungua mlango uliokuwa upande wake. Silaha zilirudi mafichoni, bastola ilikuwa kiunoni kwa kijana aliyekuwa nyuma ya usukani wa gari awali, vile vile kisu cha kijasusi kilikuwa kiunoni kwa kijana aliyekuwa pembeni ya dereva. Walikuwa tayari kutimiza jukumu lao, maagizo waliyopewa yalikuwa yakijirudia mara kwa mara. Maagizo yaliyosema wajaribu kumkamata mlengwa wao akiwa mzima lakini endapo ikitokea hali ya hatari juu yao wafanye lolote litakalowezekana, kauli hiyo ilimaanisha waliruhusiwa kumuua muhusika wao endapo akijaribu kuwashambulia. Vijana wale hawakuwa na cha kupoteza, wao waliamini katika kumwaga damu, kauli ya kwanza haikuwa na maana sana kwao, wao waliamini katika kauli ya pili, kauli iliyowapa ruhusa ya kuondoa roho ya muhusika wao. Wao walizoea kuua kuliko kuteka. Walipiga hatua taratibu kuelekea katika ofisi ya Derrick Edward.

Kipindi hatua zikiendelea, Derrick Edward pasipo kujua chochote kilichokuwa kikiendelea alionekana akitoka ndani ya ofisi yake kisha akafunga mlango wa ofisi tayari kwa kuondoka. Hakujua kama alikuwa mawindoni, hakujua vijana waliokuwa wakielekea uelekeo wake walikuwa tayari kuchukua uhai ulikuwa ndani ya mwili wake. Lakini hali ilikuwa tofauti, hali haikuwa sawa na mpangilio wa wauaji waliokuwa kazini kwa sababu kipindi wakiendelea kupiga hatua uelekeo wa Derrick Edward walishuhudia gari aina Brevis likiwa mwendo kasi na kuelekea uelekeo ule ule. Kitendo kile kiliwashangaza vijana waliojiandaa kuua, walihamaki wakataka kuchomoa silaha zao kwa ajili ya kushambulia lakini walikuwa nyuma ya muda, walishangaa kuona wakishambuliwa wao. Kitendo kile kilisababisha wakimbie haraka na kujifika nyuma ya mti mkubwa wa mwembe uliokuwa jirani ya ofisi ya Derrick Edward. Derrick Edward alihamaki kwa mshtuko mkubwa baada ya kushuhudia milio ya risasi ikirindima kama ngoma mbele yake, alitamani kukimbia kwa sababu hakujua chochote kilichokuwa kikiendelea, akili ilikufa ganzi, akili yake ilimsaliti.

Laiti kama angeliweza angelikimbia mbio kama mshale kuliko kuendelea kushangaa eneo lile. Gari aina ya Brevis lilipiga breki mbele ya Derrick Edward aliyekuwa ametumbua macho kama mjusi aliyebanwa na mlango kisha vijana watatu kila mmoja akiwa na silaha ya moto aina ya SMG wakashuka na kumshurutisha kupanda gari lao. Japokuwa Derrick Edward hakuelewa kilichokuwa kikiendelea lakini alielewa ilikuwa hali ya hatari, alielewa ilikuwa vita dhidi yake lakini hakuwajua maadui zake. Hakubisha kauli ya vijana mwenye silaha kwa sababu aliamini akifanya hivyo atakatisha maisha yake. Alipanda gari kama alivyoamuriwa kisha safari ya mwendo kasi ikaanza huku nyuma ikiacha vumbi kubwa.

Vijana waliokuwa na kusudio la kuondoa uhai wa Derrick Edward, waliojificha nyuma ya mwembe walivyoshuhudia gari la washambuliaji likiondoka eneo lile walijaribu kulishambulia kwa risasi lakini walichelewa, hata ushambuliaji wao haukuwa na nguvu kwa sababu walikuwa na bastola moja, mwingine alikuwa na kisu. Mwenye kisu alibaki akilitazama gari kwa macho mawili pasipo kujua cha kufanya. Gari liliwaachia vumbi. Hawakujiandaa kwa vita kali kama ile kwa sababu waliamini watamkuta Derrick Edward ofisini kwake kisha wafanye tukio walilokusudia. Hawakujua washambuliaji wale walitoka wapi na walikuwa akina nani lakini wao walichojua walikuwa maadui zao. Kwa mbali walisikia ving`ora vya polisi zikisogea eneo lile, suala lile lilikuwa hatari kwao kwa sababu walielewa endapo wakikutwa na polisi eneo lile ingekuwa hatari zaidi. Wakaamua kuondoka pasipo kupata majibu ya maswali yaliyokuwa vichwani mwao. Japokuwa maswali yalikuwa mengi yaliyokosa majibu lakini kuna maswali yaliwasumbua zaidi, maswali hayo yalikuwa

“Kwanini wavamizi hawakutushambulia baada ya kumchukua Derrick? Walijuaje kama sisi tulikuwa maadui wao au maadui wa Derrick?”

Hakika yalikuwa maswali magumu sana kujibika, kila wapojaribu kufikiria majibu bado walirudi katika maswali magumu. Walikuwa ndani ya gari wakirudi katika ngome ya bosi wao, waliamini lazima wapewe adhabu kubwa kwa kushindwa kutimiza kazi ndogo, kwao ilikuwa kazi ndogo kutimizwa kwa sababu walikuwa wameshashiriki kwenye kazi nyingi ngumu na za hatari zaidi. Walijiandaa kwa lolote lingeloweza kutokea. Gari aina ya Toyota Crown Athletic lilisimama katika eneo linalofahamika kwa jina la Kazengagu kisha kijana mmoja kati ya wawili waliokuwa ndani ya gari hilo akasogea katika mlango wa geti ulioshikiriwa na ukuta mnene kisha akaponyeza kitufe cha kengele (alarm) kwa lengo la kumfahamisha mlinzi wa jumba hilo la kifahari afungue mlango.

Kitendo cha kubonyeza kitufe cha kengele ili mlinzi afahamu uwepo wako hakikumaanisha kuwa ulinzi wa eneo hilo ulikuwa wa lele mama, hapana, bali ulikuwa ni utaratibu uliowekwa na mmiliki wa ngome hiyo ngumu kuingilika. Ngome hiyo ilifungwa kamera kila upande ili kubaini kila kilichokuwa kikiendelea jirani na eneo hilo, hivyo basi hata ujio wa vijana hao ulionekana hata kabla hawajabonyeza kitufe cha kingele. Kwa nje ngome ilionekana kama makazi ya kifahari ya mtu kumbe ndani ilikuwa imejaza vijana wachapakazi mwenye hali na shauku ya kufanya kila linalowezekana kufanikisha zoezi la uuzaji na usambazaji wa madawa ya kulevya unafanyika kwa ufanisi na weledi wa hali ya juu.

Jamii haikujua chochote kuhusu yaliyokuwa yakiendelea ndani ya jumba hilo la kifahari, wao waliona magari ya kifahari yakiingia na kutoka kila wakati. Baadhi ya raia wachache walisikika wakisema mmiliki wa jumba hilo alikuwa mmiliki wa mashimo ya dhahabu lakini walishindwa kufafanua mashimo hayo yalikuwa mkoa gani. Kauli na imani hiyo walijengewa na vijana waliokuwa wakifanya kazi ndani ya ngome hiyo, vijana hao walijipenyeza kwa siri katika mikusanyiko ya watu na kuvumisha uvumi huo. Jamii ikabaki ikiamini kauli hiyo pasipo kujua hata waliovumisha walikuwa washiriki wakubwa wa nyumba ile ya kifahari. Endapo jamii ingelifahamu kama ndani ya jumba lile ndiyo kulikuwa kukifanyika mipango yote ya kuuza na kusambaza madawa ya kulevya ingelipambana usiku na mchana kuisambaratisha nyumba ile.

Vijana wale wawili walioshindwa kutimiza kazi ya mkuu wao wa kikosi cha kigaidi waliingia moja kwa moja mpaka katika sebule ya nyumba ile, waliwakutwa vijana wanne wakiwa makini wakitazama taarifa ya habari iliyokuwa ikirushwa katika kituo maarufu cha televisheni nchini Malosha. Waliposikia habari ile haikuwa ngeni kabisa masikio kwao, ilikuwa ni habari iliyowahusu moja kwa moja. Habari ile ilikuwa ikifafanua tukio la uvunjwaji wa amani na utulivu katika mkoa wao wa Rwama Mwanzo, habari ile ilisema juu ya kikundi cha kigaidi kilichoshambulia ofisi ya mwana sanaa maarufu nchini na nje ya mipaka ya nchi kisha kikafanikiwa kumteka na kuondoka naye kusiko julikana. Habari ile ilionesha wazi hata uongozi wa mkoa wa Rwama Mwanzo na serikali kwa ujumla ilishindwa kuelewa ni akina nani waliomteka Derrick Edward. Kilibaki kuwa kitendawili.

Vijana walioshindwa kutimiza kazi ya kumkamata au kumuua Derrick Edward walikuwa wakitazamana macho kwa macho na vijana wanne waliowakuta sebuleni, sura za wale vijana wanne waliokuwa sebuleni zilikuwa zimekunjamana mithili ya mtu aliyekula kitu kichungu. Hawakuhitaji kufafanuliwa kuhusu suala la kazi waliyopewa wenzao kwa sababu muda mfupi uliopita walisikia na kuona katika televisheni kitendo cha Derrick Edward kuchukuliwa na watu wengine. Walielewa tangu awali kuwa waliofanikiwa kumkamata Derrick Edward hawakuwa wenzao kwa sababu mashuhuda wa tukio walisema walishuhudia vijana watatu wakiwa na silaha za moto wakimshurutisha Derrick Edward kupanda gari, kitendo cha mashuhuda kusema walishuhudua vijana watatu wakifanya tukio hilo kiliwaamisha wana ngome ngumu kuwa watu wao waliowatuma wakamkamate au kumuua Derrick Edward siyo waliofanya hilo tukio kwa sababu wao waliwatuwa wawili wenye bastola moja na kisu, lakini mashuhuda walisema watekaji walikuwa watatu na wenye silaha za moto kila mmoja. Mmoja kati ya vijana wanne waliopata taarifa kupitia televisheni alichukua simu yake ya mkononi akatafuta jina alilolihitaji, alipolipata akapiga. Simu iliita ikakata. Alipiga zaidi ya mara tatu pasipo kupokelewa lakini hakuchoka kupiga. Alikuwa na dhamira ya kuongea na aliyekuwa akimpigia simu hiyo. Alivyopiga mara ya nne simu ikapokelewa, baada ya salamu aliongea

“Vijana waliokwenda kwa Derrick wameshindwa kazi, Derrick ameangukia kwenye mikono isiyo fahamika”

Ilikuwa kauli ya kugadhabisha sana kwa aliyekuwa upande wa pili wa simu, alihisi kama amesikia vibaya lakini aliyempatia taarifa hizo alimsisitiza kuwa alikuwa sahihi wala hajakosea. Hasira zilimjaa sana baada ya kuona mipango yako ikivurugika kizembe. Aliona ni uzembe wa hali ya juu kwa watu wasio julikana kumchukua Derrick Edward mbele ya vijana wake. Hakuwahi kuruhusu lindo lake kupotea machoni kwake hata siku moja, siku hiyo ilikuwa mara ya kwanza. Alimpa maagizo kijana wake aliyempigia simu, yalikuwa maagizo magumu lakini rahisi sana katika kundi hilo. Simu ilikatwa na kiongozi aliyepigiwa, hakika alichanganyikiwa kwa sababu alikata simu ambayo hakupiga yeye. Kijana aliyepewa maagizo sekunde chache zilizopita akawageukiwa vijana wenzake walioshindwa kazi waliyopewa kisha akawaambia

“Wekeni silaha zenu juu ya meza”

Hakuna aliyebisha, waliweka silaha zao kama walivyoagizwa. Meza ilipokea bastola na kisu vyote vyenye asili ya Urusi. Walipoinua vichwa vyao baada ya kuweka silaha zao mezani walikutana na mdomo wa bastola ndogo iliyofungwa kizuia sauti. Macho yaliwatoka, wakaanza kubabaika kwa hofu ya kuuliwa lakini hawakupewa hata sekunde moja ya kujielezea. Risasi ilipenya katika paji la uso la kila mmoja wao. Waligeuka maiti ndani ya sekunde chache zilizofuata
***
Ilipita siku moja na masaa kadhaa tangu Derrick Edward atekwe na watu wasiojulikana, hali ya hewa ilikuwa mbaya sana kwa sababu hakuna aliyefahamu kama alikuwa bado yu hai au alishauliwa na watekaji. Kitendo cha watekaji kuendelea kuwa kimya kiliongeza hofu kwa raia na taifa kwa ujumla. Taifa lilitamani watekaji wajitokeze kwa namna yoyote waseme watakacho au kusudio la kumteka Derrick Edward ili ifahamike namna ya kumtoa katika mikono yao. Ukimya uliendelea kama kawaida. Hofu ilipamba nchini hasa katika mtaa ulikuwa na ofisi ya sanaa ya Derrick Edward. Watu walipunguza kutembea ovyo bila sababu ya msingi na waliotembea walirejea majumbani mapema kabla giza halijawa totoro. Waliamua kufanya hivyo kwa sababu hawakujua nani atakuwa wa pili kutekwa.

Olivia Komba alikuwa ndani ya chumba chake cha mazoezi, alikuwa amemaliza kufanya mazoezi mepesi ya viungo. Alizoea kuyaita mazoezi mepesi kwa sababu yalikuwa sehemu ya maisha yake lakini mazoezi hayo hayo mepesi kwa mwingine ni mazoezi magumu tena yasiyopaswa kujaribiwa kwa puta. Sasa alikuwa akisafisha moja ya silaha zake za moto, alikuwa akisafisha bastola aina ya Revolver aliyokuwa akiiandaa kufanyia kazi siku hiyo. Alipomaliza kuisafisha aliipanga na kuifunga vizuri. Ilikuwa bastola tayari kwa kufanya matukio ya kipelelezi. Alichukua taulo akajifuta jasho kisha akaondoka eneo lile na kuelekea bafuni huku kichwa kikifikiria juu ya kazi ya kipepelezi aliyoianza. Ndani ya chumba chake cha mazoezi kulikuwa na vifaa vingi vya mazoezi ya viungo, hilo halikua jambo la ajabu hata kidogo.

Jambo la ajabu lilikuwa moja, ndani ya chumba hicho alibandika picha za watu waliokuwa sehemu ya upelelezi wake, maadui pamoja na watu wengine aliohisi walikuwa sehemu ya msaada katika kufanikisha jambo alilokusudia. Ukuta ulichakazwa kwa picha za Winnie Ngocho, David Samson, Zimwi, Nasrat Abdul al Aziz pamoja na wengine aliohisi walifaa kuwa kwenye orodha hiyo. Picha ya Derrick Edward haikuwa sehemu ya picha hizo kwa sababu kipindi alipoanza shughuli yake hakujua uwepo wa mtu huyo katika matukio yalikuwa yakiendelea, lakini baada ya tukio la kutekwa kwa Derrick Edward alifikiria kubandika picha yake. Ukiachana na picha hizo, kulikuwa na picha moja ya mtu wa makamo aliyevaa soksi usoni, soksi ile ilisababisha kutofahamika kwa mtu huyo.
Japokuwa Olivia Komba ndiye aliyebandika picha zote lakini hata yeye hakumfahamu kabisa mtu huyo mwenye soksi usoni. Kila siku alijitahidi usiku na mchana ili kumbaini lakini hakuna alichoambulia.

Aliamini mtu huyo atakuwa nyuma ya matukio mengi ya kihalifu. Imani hiyo ilimjaa maradufu siku aliyokabidhiwa kazi ya kupeleleza mtandao mzima unaojihusisha na masuala ya madawa ya kulevya mkoani Rwama Mwanzo. Siku hiyo ndiyo alikabidhiwa picha ya mtu mwenye soksi usoni na mkuu wake wa kazi aliyemwambia kuwa hata yeye alikabidhiwa na Inspekta Jenerali wa Polisi (Inspector General of Police – IGP). Maagizo ya IGP yalisisitiza kutafutwa kwa mtu huyo aliyekuwa nyuma ya soksi ili atambulike mapema kwa sababu iliaminika mtu huyo alikuwa ndiyo kila kitu katika mtandao wa wauzaji na wasambazaji wa madawa ya kulevya pamoja na vikundi vingine vya kigaidi vinavyofanya biashara haramu. Ilikuwa kazi ya Olivia Komba kumbaini mtu huyo. Suala la Olivia Komba kufuatilia kisa cha David Samson na askari polisi aliyesaliti kazi yake, Zimwi, aliamini kupitia njia hiyo angeweza kumbaini mtu mwenye soksi usoni. Aliamini akifanikiwa kumdhibiti Zimwi atakuwa amepiga hatua kubwa ya kumfahamu mzee wa makamo aliyekuwa nyuma ya soksi, hakika ulikuwa mtazamo yakinifu aliouamini sana.

Olivia Komba alipanga nyumba kubwa ya kisasa katika mtaa uliochangamka sana, mtaa unaofahamika kwa jina moja ya Bugare. Mtaa huo ni moja ya mitaa mipya katika mkoani Rwama Mwanzo, awali lilikuwa eneo lililojaa miti, kwa lugha nyepesi huitwa msitu. Ongezeko la watu lilisababisha kuvamia na kujenga eneo hilo lililo jirani zaidi na zima Kuu, ziwa lenye sifa ya kupitiwa na bonde la ufa. Mtaa wa Bugare huitwa mji mpya kutokana na muda wake mfupi tangu uanzishwe. Japokuwa ni mji mpya lakini ni miongoni mwa maeneo lenye sifa ya nyumba za kisasa, hivyo basi limehifadhi matajiri wengi. Ukiacha suala la kuwa na nyumba za kisasa na huduma bora za kijamii, watu hupenda sana kuishi eneo hilo kwa sababu lipo jirani na ziwa Kuu hivyo huweza kupata upepo wa ziwa pasipo shida ya aina yoyote.

Olivia Komba hakuiishi peke yake, aliishi na Winnie Ngocho katika makazi yake. Alitaka kumuweka Winnie Ngocho katika makazi salama ili asiweze kudhurika kirahisi na vita iliyokuwa ikiendelea. Alifanikiwa kwa kiasi kikubwa kwa sababu nyumba ile ilikuwa maficho tosha kwa Winnie Ngocho. Nyumba yenye ukuta wa geti na vioo visivyoruhusu mtu wa nje kuona ndani, kwa kweli ilikuwa nyumba yenye ulinzi wa kutosha. Ukiacha uimara wa nyumba hiyo bado getini kulikuwa na walinzi watatu. Olivia Komba aliwaajiri wamasai watatu wadumishe ulinzi katika nyumba aliyopanga. Wamasai hao hawakufahamu kama ndani ya nyumba kulikuwa na mtu mwingine zaidi ya Olivia Komba. Siku zote Winnie Ngocho aliishi kwa usiri sana, na mara chache aliyotoka ndani ya nyumba hiyo kuelekea mtaani alikuwa ndani ya gari ya Olivia Komba. Mara zote walitoka ndani ya gari yenye vioo nyeusi iliyozuia watu wa nje kuwaona watu wa ndani.

Ndani ya wiki moja walikuwa wameshakuwa kama ndugu, waliongea mambo mengi ya kimaisha pasipo kusahau mpango wa Olivia Komba, mpango wa kupeleleza chochote kilichokuwa mbele yake. Olivia Komba hakuchoka kumsisitiza Winnie Ngocho kuwa atafanya juu chini kufanikisha anampata mtoto wake. Aliamini mtoto wake lazima atakuwa kwenye maisha safi kwa sababu alikuwa akitumika kama ngao ya kumshurutisha David Samson. Olivia Komba alikuwa na uhakika kuwa mtoto yule lazima awe hai mpaka siku ya mwisho, lazima awe hai ili David Samson akubali kutumikishwa kama mbwa. Olivia Komba alishindwa kumuhakikishia Winnie Ngocho usalama wa mpenzi wake, alishindwa hilo kwa sababu aliamini baadhi ya wahalifu hufanya mauaji ya watu endapo wakihisi hawana msaada tena kwao, hivyo Olivia Komba aliamini ingewezekana David Samson akauliwa na wahalifu wale pindi wakihisi wamefanikisha malengo yao dhidi yake. Vile vile majambazi hufanya hivyo ili kutunza siri zao, lakini siyo rahisi kumuua mtoto asiyejua chochote.

Olivia Komba aliendelea kumsisitiza Winnie Ngocho kuwa, mara kadhaa majambazi huwalea watoto kama hao ili wawatumie katika mipango yao ya kijambazi. Watoto hao huwa na roho ngumu ya mauaji kwa sababu ulelewa katika mazingiza ya namna hiyo. Wakati mwingine Watoto hao hupewa historia ya uongo kuhusu familia zao, huambiwa wazazi wao waliuliwa na kikundi ambacho kina upinzani nao, lengo likiwa kupandisha na kuchochea chuki dhidi ya kikundi hasimu na pingamizi kwao. Maneno ya Olivia Komba yalimuingia sawa sawa Winnie Ngocho na aliyaelewa kwa asilimia moja. Ingawa alihakikishiwa kumpata mtoto wake lakini upande wa pili wa akili yake uliamini endapo mpango wa kumpata mwanae ukigonga mwamba, mwanae atawatumikia majambazi. Roho ilimuuma sana, akaona anaweza kuwa amezaa mtoto atakayeingizwa roho za kijambazi na kuwa jambazi sugu atakayelisumbua taifa la Malosha. Machozi yalimtoka lakini hayakumsaidia chochote zaidi ya kulowanisha nguo aliyovaa.

Jioni ya siku hiyo ilikuwa maalumu sana kwa Olivia Komba, ilikuwa jioni aliyohisi ingekuwa na hatua moja au mbili katika harakati zake za kutafuta ufumbuzi wa mafumbo yaliyoenea kila kona ya ubongo wake. Jioni hiyo ilikuwa ya tofauti kwa sababu ya taarifa aliyopata, alitumiwa ujumbe wa meseji kwa namba mpya. Ujumbe ule ulimwambia

“Najua wewe ni mpelelezi uliyetukuka, mpelelezi unayelipigania taifa. Nataka kukwambia kuwa leo usiku katika Kasino ya ‘Just Your body’ itafanyika biashara haramu ya madawa ya kulevya”

Alipojaribu kuipigia namba ile alijibiwa na mtandao kuwa haipatikani, hakuchoka kuipigia kila baada ya dakika tatu mpaka tano lakini jibu lilikuwa lile lile lisiloridhisha. Kabla hajaanza kusafisha silaha yake ya moto aliipigia tena namba ile, iliita pasipo kupokelewa. Alipojaribu kwa mara nyingine alijibiwa na mtandao kuwa namba ile haipo, hapo ndipo alipopata jawabu kuwa mwenye namba ile ameifutia usajili ndani ya muda mfupi uliopita. Alipata shauku ya kutaka kujua alikuwa nani haswa lakini alikosa pa kuanzia. Akaamua kumpigia simu mkuu wake wa kazi ili ampae ushauri. Hakika alipata ushauri yakinifu, ushauri ulioongeza maswali yasiyo na majibu.

ITAENDELEA View attachment 2225110

Safi sana….Tuongeze mzigo Mkuu
 
RIWAYA: MATEKA
MTUNZI: EMMANUEL PHIRI
NAMBA: 0758 195 890

(KIPANDE CHA TISA)

Baada ya kumuelezea mkuu wake wa kazi aliambiwa amtumie namba hiyo ili wajaribu kufanya mawasiliano na makao makuu ya mtandao huo wa laini za simu. Waliamini kwakuwa laini nyingi zilisajiliwa kwa alama za vidole wangeweza kupata taarifa zake japokuwa amefutwa usajili. Haikuwa kazi rahisi kupewa jina la aliyekuwa mmiliki wa laini ile ya simu, kwakuwa ilikuwa oda ya mkuu wa polisi, wamiliki wa mtandao ule wa simu wahakuwa na jinsi zaidi ya kutoa jina la mhusika aliyesajili na kuifunga laini ile muda mfupi uliopita.

Jina la mtu huyo ndilo lililoleta utata kwa kila mmoja aliyelisikia. Halikuwa jina lingine bali Abdul al Aziz. Kila mmoja alipatwa na mshangao mkubwa kwa sababu hakuna aliyekuwa hajui kuhusu taarifa ya kifo cha mtu huyo, mtu aliyefariki miaka mingi iliyopita kwa ajali ya gari. Sasa kitendo cha laini iliyosajiriwa kwa alama za vidonge kufungiwa na mtu lilizua utata kwa sababu anayeweza kuifunga laini ya namna hiyo ni aliyeisajiri pekee na siyo vinginevyo. Hii ilimaanisha kuwa hata kama kuna mtu alibaki na laini za simu za marehemu Abdul al Aziz, mtu huyo hawezi kuzifunga laini hizo mwenyewe kwa sababu lazima ahitajike alama za vidole kufanikisha zoezi hilo. Maswali yaliibuka

“Inakuwaje laini yenye jina la Abdul al Aziz aliyekwisha fariki ifungwe leo? Au yupo hai? Atakuwaje hai wakati ilithibitishwa alizikwa na kaburi lake linafahamika lilipo?”

Yalikuwa maswali yaliyowasumbua Olivia Komba na mkuu wake wa kazi. Awali alivyotumiwa ujumbe ule wa meseji alishindwa kuuelewa kabisa. Siyo kwamba hakuelewa ulimaanisa nini, hapana, alishindwa kuelewa aliyemtumia ujumbe huo alijuaje kama yeye ni mpelelezi, vile vile alijuaje kuwa yupo mkoani Rwama Mwanzo kwa sababu Olivia Komba hakuwa mwenyeji wa mkoa huo bali aliingia kwa kazi maalumu. Kitendo kile kilimuongezea udadisi sana. Mkuu wake alimsisitiza asiende katika Kasino hiyo akiamini waweza kuwa ni mtego. Hata Olivia Komba aliamini kauli ya kiongozi wake lakini akili yake ilimsisitiza aende, akili ilimwambia

“Unakuwaje mpelelezi alafu uogope kupeleleza suala hili? Yakupasa kwenda ufahamu mbivu na mbichi. Ikitokea umekufa utakuwa umefia kazini. Nenda”

Alikubali maagizo ya akili yake na kupinga kauli ya mkuu wake wa idara, aliona haita kuwa sawa alipomjulisha mkuu wake msimamo aliojiwekea. Haikuwa kazi ngumu kukubaliwa kwenda lakini alisisitizwa kuwa makini awapo eneo hilo, asisitizwa asimuamini mtu yeyote atakayemfuata kuanzisha mazungumzo naye. Alikubali maagizo ya mkuu wa idara. Saa tano usiku alikuwa ndani ya kasino ya ‘Just Your body’, kasino iliyojaa kila aina ya anasa. Alivaa sketi fupi ya jinzi nyeusi iliyogawa mapaja sehemu mbili, nusu ya mapaja ilizibwa na sketi lakini nusu nyingine ilikuwa wazi ikipunga upepo. Juu alivaa tisheti fupi nyeupe yenye chapa ya adidas iliyoacha wazi sehemu ya kitovu kuruhusu shanga alizovaa kuonekana. Chini alivaa viatu vyeusi vyenye kisigino kirefu vyenye rangi sawa na sketi aliyovaa. Watoto wa mjini huita mchuchumio. Viatu vya aina hiyo vilikuwa sehemu ya maisha yake, alikuwa akivivaa kila wakati aendapo kwenye matukio aliyohisi alihitaji kuchukua utayari wa watu. Mkononi alibeba mkoba mweusi uliohifadhi bastola na leso tatu kama alivyozoea kutembea nazo. Hakuwa tofauti sana na wanawake wanaojiuza.

Awali kasino ile ilikuwa ikiitwa ‘Paradize Zone’ lakini kulingana na uchafu uliokuwa ukiendelea wakaona jina la ‘Paradize Zone’ halikufaa hata kidogo, wakaamua kuiitwa ‘Just Your body’ wakimaanisha wanahitaji mwili wako pekee na siyo vinginevyo, na ndivyo ilivyokuwa. Wasichana wadogo wenye miaka kumi na nane mpaka ishirini na tano walikuwa nusu uchi ndani ya kasino hiyo, wengine wakichezea fimbo kimahaba. Walikuwa sokoni. Soko la hapo halikuwa lele mama, wasichana ndani ya kasino hiyo waliuzwa bei ghari sana tofauti na sehemu zingine, kuuzwa kwao ghari hakukuwa kitu kwa vijana wenye pesa za kula ujana. Waliwatumia kila walipojisikia kufanya hivyo. Olivia Komba alikaa kaunta akinywa kinywaji baridi huku macho yake yakipepesa kulia na kushoto pasipo kuona kitu kilichompeleka mahali pale. Hakufa moyo kwa sababu aliamini aliyempa taarifa lazima atakuwa ndani ya kasino hiyo. Alijisemea moyoni

“Naweza nisione chochote nilichoambiwa lakini nikimfahamu aliyenipa taarifa hii inaweza kuwa hatua nzuri kwangu, ajitokeze nimjue”

Aliamini aliyempa taarifa alikuwa raia mwema au kama siyo raia mwema basi atakuwa mwanachama wa kundi la magaidi mwenye nia ya kuwageuka wenzake. Aliendelea kupiga fundo moja baada ya lingine. Kipindi kichwa kikiendelea kutengeneza maswali na koromeo likindelea kumeza fundo za kinywaji ghafla alisikia kama akishikwa bega na mtu kutoka mgongoni, aligeuka kwa haraka sana ili kumbaini mhusika. Hakutegemea kabisa, alikutana na ngumi nzito iliyompata kichwani, akapepesuka kutoka juu ya kiti cha kaunta na kuanguka chini. Alijaribu kuinuka haraka kwa lengo la kujibu mashambulizi lakini alichelewa, alikutana na mdomo wa bastola ukimtazama. Aliyeshika bastola alipiga risasi juu, kitendo kile kilileta taharuki kubwa, watu wakaanza kukimbia mbio ovyo kwa lengo la kuokoa maisha yao.

Kipindi watu wakiendelea kukimbia eneo lile kuelekea nje, vijana wengine walikuwa wakielekea mahali alipokuwa Olivia Komba na kijana aliyemshambulia kwa ngumi kali. Vijana wale walikuwa wameshika bastola aina moja na kijana aliyemshambulia Olivia Komba, kitendo kile kilimaanisha kilikuwa kikundi kimoja chenye lengo la kumdhibiti Olivia Komba. Na ndivyo walivyofanya. Mmoja kati ya vijana wale alimbeba begani Olivia Komba aliyekuwa akiona nyota kwa ngumi iliyosalimia sura yake dakika kadhaa zilizopita. Walitoka ndani ya kasino ya ‘Just Your Body’ kisha wakaingia ndani ya gari lililokuwa likiwasubiri nje ya jengo hilo, lilikuwa gari aina ya Toyota Noah. Safari ya kuondoka ikaanza kwa mwendo kasi. Ndani ya gari Olivia Komba alifungwa kamba miguuni, mikononi, akafungwa kitambaa cheusi usoni kisha akazibwa mdomo kwa plasta. Walimdhibiti kweli kweli. Ilikuwa safari ya kimya kimya kila mmoja akitafakari mambo yake, kichwa cha Olivia Komba kiliwaza ujinga aliofanya wa kwenda eneo la tukio kwa kujiamini namna ile, aliona ni ujinga wa kujiamini kupita kiasi. Alifikiri ilikuwa bora angetuma mtu wa kupepeza kabla hajachukua uamuzi wa kwenda. Wazo hilo alilipinga pia, aliipinga kwa kujiuliza

“Ningemtuma nani? Wakati sina mtu mwingine katika mpango”

Alijipa moyo na kuamini lazima apambane ipasavyo kubaini kila kitu, akili yake ilifikiria zaidi na kuona umuhimu wa kukamatwa kwake. Aliamini lazima atatambua kitu chochote mbele ya safari, aliamini suala la kukamatwa kwake ni hatari sana lakini endapo akifanikiwa kutoka mikononi mwa magaidi hao atakuwa na taarifa itakayompa mwanga juu ya kazi yake. Hakika alijipa moyo. Mawazo yalikata baada ya kusikia sauti kali ikimshurutisha kushuka ndani ya gari, kauli ile ilimaanisha walikuwa wamefika walipokuwa wakielekea. Walimfungua Kamba za mikononi na miguuni ili kuruhusu mwili wake kujongea. Kwakuwa alikuwa amefungwa kitambaa usoni hakuweza kushuka peke yake bila msaada wa mtu, alishikwa mkono na mmoja wa vijana wale waliomkamata kisha wakaanza kumuongoza njia taratibu pasipo haraka. Alipiga hatua kadhaa, mara aambiwe akate kushoto mara kulia. Baada ya mwendo wa dakika kadhaa ulioambatana na kona nyingi alisimamishwa sehemu kisha akasikia sauti ikipenya katika masikio yake

“Karibu sana Olivia Komba, karibu katika himaya takatifu”

Ilikuwa sauti ya kiume yenye hadhi ya kuitwa sauti nyenyekevu au pole. Masikio ya Olivia Komba yalithibitisha ilikuwa sauti ya kijana wa makamo mwenye miaka chini ya arobaini. Olivia Komba hakujibu kauli ya kijana yule, aliendelea kusimama kama alivyoamuriwa awali. Kijana aliyemkaribisha akatoa amri kwa vijana wake waliomfikisha mbele yake, amri ile ilisikika vizuri kwa kila mmoja aliyekuwa eneo lile

“Mfungue kitambaa, nataka tuonane ana kwa ana”

Vijana walitimiza kauli ya mkuu wao, walimfungua kitambaa Olivia Komba ili kuruhusu macho yake kusabahi eneo lile. Walitazamana ana kwa ana kati ya Olivia Komba na kijana aliyetoa amri. Haikuwa sura ngeni kwa Olivia Komba, ilikuwa sura iliyotiliwa mashaka toka miaka ya nyuma kuwa ilihusishwa na biashara haramu za kuuza au kununua madawa ya kulevya. Lakini miaka ilivyosogea ilisafishwa kisiasa na kuonekana alionewa katika taarifa za awali. Faili lake lilikabidhiwa katika kitengo maalumu cha kupambana na kudhibiti wauzaji na wasambazaji wa madawa ya kulevya, kitengo kile kiliamua kuchukua faili lile ili kumfatilia mtu huyo kimya kimya. Waliamini mtu huyo alisafishwa kienyeji na mamlaka iliyotoa tamko, waliamini kulikuwa na siri nzito iliyojificha katika ya tamko hilo. Olivia Komba alijitahidi kukumbuka jina la kijana huyo lakini kichwa kilikataa kabisa, kipindi akiendelea kufikiria ghafla alisikia sauti ya kijana yule akijitambulisha

“Nadhani unanifahamu vizuri lakini ni jambo la kheri kama nikijitambulisha tena…Naitwa Amani Collence, mtoto wa muasisi wa eneo hili”

Olivia Komba aliafiki akilini kwake, hakika alikuwa Amani Collence kama alivyojitambulisha. Muda wote Olivia Komba alikuwa amesimama wima katikati ya vijana wanne. Olivia Komba alitabasamu kwa kitendo cha Amani Collence kujitambulisha mbele yake, hakika alifurahishwa na kitendo kile kwa sababu aliamini amepiga hatua moja katika upelelezi wake. Akili yake ilimuhakikishia kuwa Amani Collence ni mwanachama wa kundi la kigaidi kama alivyodhaniwa awali lakini akasafishwa kienyeji. Kitendo kile kilimuaminisha ndani ya kitengo cha kupambana na masuala ya madawa ya kulevya kulikuwa na wanachana wa Amani Collence. Aliendelea kutabasamu baada ya kuamini amemfahamu adui namba moja, tabasamu lile halikuwa chochote mbele ya macho ya Amani Collence kwa sababu aliamini mateka wake alijaribu kumuhada na kucheza na akili yake, aliamini hakuwa na sababu ya msingi ya kutabasamu. Olivia Komba alijibu kauli ya Amani Collence akiwa amesimama wima kama awali

“Nafurahi kwa kunithibitishia kila tulichokifikiria juu yako kilikuwa na kipo sahihi”

Ilikuwa zamu ya Amani Collence kutabasamu, alitabasamu huku akitembea tembea ndani ya sebule ile iliyojaa vito vya thamani. Haikuwa sebule ya kitoto, wala haikuhitaji nguvu kubwa kumuelezea mtu kama ilikuwa imetumia pesa nyingi kupendezeshwa. Amani Collence alimwamuru Olivia Komba akae kwenye sofa lililokuwa jirani yake. Alikaa kama alivyoamuriwa. Kauli ya Amani Collence ilivunja ukimya baada ya Olivia Komba kukaa kwenye kiti

“Nilitaka tuonane Olivia. Tuna mengi ya kuzungumza, hakika ni mengi”

Olivia Komba hakujibu chochote bali aliendelea kumtumbulia macho Amani Collence aliyeandamwa na tabasamu kila muda. Amani Collence alitoa kauli, kauli iliyozidi kuonesha namna alivyokuwa na nguvu katika himaya yake

“Mpelekeni alipo yule kijana”

Vijana waliokuwa wima muda wote hawakujiuliza mara mbili, walimpa amri Olivia Komba ainuke toka kitini kisha akaongozwa njia kufuata korido ndefu iliyofuata baada ya kutoka sebuleni. Waliongozana kimya kimya mpaka mwisho wa korido hilo. Olivia Komba aliona kitu kilichomshangaza zaidi. Chumba cha mwisho katika korido hiyo ndefu kilikuwa na muundo sawa gereza. Kijana mmoja kati ya vijana walioongozana na Olivia Komba alifungua kufuri la gereza lile la ndani kisha akamuamuru Olivia Komba kuingia, hakuwa mbishi aliingia kama alivyoagizwa. Vijana walifunga kufuri lile kisha wakaondoka pasipo kuangalia walipotoka. Ndani ya gereza kulikuwa na kijana mwingine aliyeinamisha kichwa chini muda wote, kijana yule hakuwa na habari yoyote ya binti aliyeingia katika chumba hicho cha gereza. Aliendelea kuinama kama alivyokuwa awali. Gereza lilikuwa safi tena lenye kupendeza lakini lisilo na kiti wa kitanda cha kulala, sakafu pekee ndiyo iliyokuwa ikisubiri kuustiri mwili wa Olivia Komba. Olivia Komba alimkazia macho kijana aliyekuwa ndani ya chumba hicho, alijiuliza mara mbili kuhusu mtu yule akakosa majibu. Aliamini atakuwa mateka kama yeye alivyotekwa, kitu alichojiuliza kilikuwa

“Kwanini ametekwa? Anajihusisha na nini?”

Maswali yalimsumbua Olivia Komba. Alisogea katika kona ya pili toka alipokuwa kijana aliyeinamisha kichwa chake kisha akakaa chini kama kama kijana yule. Aliendelea kumtazama kijana aliyeinama, shauku ya kumfahamu ikapanda. Haiba ya upelelezi ilimkaa kichwani haswa, akatamka

“Habari rafiki! Naitwa Olivia Komba, sijui mwenzangu waitwa nani?”

Swali lilipita vizuri katika ngoma ya sikio ya kijana aliyeinama, alielewa lengo la msichana yule lilikuwa kufahamiana kisha maongezi mengine yaendelee. Aliendelea kuinama chini kama alivyokuwa awali, hakujali kabisa kauli ya binti aliyekuwa kwenye kona ya mbele yake. Hakutaka kuinua sura yake kumtazama ili amtambue, hakuona umuhimu huo. Yeye akili yake ilikuwa ikitafakari juu ya mkasa wake, alikuwa akiwaza namna ya kutoka eneo hilo na kupambana ipasavyo ili kuliokoa taifa katika jambo alilohisi aliweza kulitimiza. Olivia Komba hakuchoka kumsemesha kijana yule, alivyoona hajibiwi aliinuka taratib akaanza kupiga hatua kuelekea katika kona aliyokaa kijana yule. Hakufikiria kama angeweza kushambuliwa, hakuogopa suala hilo kwa sababu alijiamini sana kwenye mapambano ya ana kwa ana. Aliamini endapo kijana yule akianzisha vurugu lazima amdhibiti ipasavyo. Olivia Komba alipofika katika kona aliyokaa kijana yule akachuchumaa kisha akamshika bega, akamwambia

“Waweza sema neno lolote kijana mwenzangu”

Hakika alistahili kumwita kijana mwenzake kwa sababu alikuwa kijana kama yeye, tofauti ilikuwa jinsia. Kijana aliyeguswa bega aliinua kichwa chake, akakutana na sura ya mrembo ikimtazama kwa bashasha na tabasamu kama vile walikuwa kwenye eneo lenye bahari ya amani na utulivu. Olivia Komba alishangaa sana alipoona sura ya kijana yule, ilikuwa sura ya mwanasanaa aliyetekwa na magaidi siku chache zilizopita. Sasa aliamini alikuwa chumba sahihi, aliamini uwepo wa mwanasanaa huyo ndani ya chumba kile ungemuwezesha kufahamu kila kitu kuhusu mwanasanaa huyo. Aliamini atafahamu sababu zote zilizosababisha mwanasanaa huyo kutekwa nyara. Hakujua kama mwanasanaa huyo alikuwa mpelelezi aliyetoka katika idara ya kupambana na wauzaji na wasambazaji wa madawa ya kulevya nchini Malosha. Olivia Komba akamuuliza swali

“Kama sijakosea, nafikiri unaitwa Derrick Edward”

Derrick Edward aliitikia kwa kichwa akimaanisha kuwa binti yule alikuwa sahihi. Kipindi matukio hayo yakiendeela, akili ya Derrick Edward ilifikiria kwa kasi sana juu ya uwepo wa binti yule ndani ya gereza lile alilohisi lilikuwa maalumu kwa wanaume. Akafikiri labda amepandikizwa na magaidi ili amuhadae kutoa taarifa alizogoma kutoa. Alipanga kuwa makini na ulimi wake, katika mipango yake alijihakikishia kuwa lazima apeleleze maswali ya binti yule ili amfahamu kiundani. Sura ya Olivia Komba ilikuwa ngeni machoni mwa Derrick Edward. Siyo kwamba Olivia Komba hakufahamu kama Derrick Edward alikuwa mpenzi wa Nasrat Abdul al Aziz, binti wa Kiarabu ambaye baba yake alihusishwa na biashara za madawa ya kulevya kabla ya kifo chake, hapana, alielewa kabisa suala hilo.

Picha ya Nasrat Abdul al Aziz ilikuwa miongoni mwa picha za watu hatari aliopanga kuwafatilia ili atimize jukumu lake la kuusambaratisha mtandao wote wa wauza madawa ya kulevya alioamini ulikuwa ukiongozwa na mzee wa makamo aliyejificha nyuma ya soksi nyeusi. Mzee waliyejaribu kutafuta uhalisia, taswira na taarifa zake pasipo mafanikio. Awali Olivia Komba hakutaka kabisa kumsumbua Derrick Edward kwa sababu aliamini Derrick Edward alinasa kwenye penzi la mtuhumiwa wa biashara haramu pasipo kujua mpenzi wake alikuwa mwanaharamu. Olivia Komba aliamini Derrick alikuwa mwanasanaa haswa asiye muhalifu. Olivia Komba alitaka kumpeleleza Nasrat Abdul al Aziz kimya kimya pasipo kumuhusisha Derrick Edward, aliamini endapo ikitokea ulazima wa kumuhusisha Derrick Edward angefanya hivyo.

Suala la kumkuta Derrick Edward ndani ya gereza bubu lilimuongezea hamasa ya kujua zaidi, alihisi labda alikuwa akihusika moja kwa moja na masuala ya Nasrat Abdul al Aziz ndiyo maana akakamatwa na maharamia hao. Hakuona sehemu yoyote ya sanaa ingeyoweza kumchonganisha na watu hao. Sasa Olivia Komba alijithibitishia kuwa Derrick Edward alishirikiana na mpenzi wake kwa siri alafu akajifanya mwanasanaa kumbe kilikuwa kiini macho mbele ya watu. Sasa alijiona mjinga kwa kutomuhusisha kijana yule katika orodha ya wauza madawa ya kulevya aliowabandika katika ukuta wa chumba chake cha mazoezi. Aliamini kupitia uwepo wa Derrick Edward ndani ya chumba kile angeweza kupata taarifa za mzee wa makamo aliye nyuma ya soksi nyeusi, lakini aliamini lazima atapata pingamizi.

Aliamini siku zote majambazi huwa na roho saba, roho ya paka katika kufanya maamuzi ya usaliti au kuvujisha siri. Ilikuwa vita ya mawazo pande zote mbili, Derrick Edward alimkazia macho Olivia Komba akagundua alikuwa mkakamavu aliyezoea kufanya mazoezi ya viungo. Muonekano huo ulizidi kumpa hofu dhidi ya msichana yule, alijihakikishia moja kwa moja kuwa alikuwa mbele ya msichana hatari sana. Alitabasamu moyoni na kujihakikishia lazima acheze na akili ya msichana huyo. Macho yake yaliendelea kutambaa juu ya Olivia Komba aliyevaa mavazi ya kichokozi, mavazi yale yalizidi kumuhakikishia Derrick kuwa mrembo yule alipandikizwa makusudi katika chumba kile ili amuhadae kimapenzi kwa lengo la kupata taarifa zitakazowasaidia maharamia wenzake. Waliendelea kutazamana kama mabubu, lakini Olivia Komba hakuridhishwa na hali ile, alikuwa kazini muda huo. Aliendeleza kazi yake ya kipelelezi lakini hakujua aliyekuwa akimpeleleza alikuwa na mtazamo tofauti juu yake

“Derrick, kwanini upo humu?”

Derrick Edward aliamini Olivia Komba ameanza chokochoko za kupata taarifa. Aliapa kutotoa taarifa yoyote bali alidhamiria kupata taarifa kutoka kwa msichana huo. Derrick Edward alimkazia macho Olivia Komba kisha akamjibu, jibu la Derrick Edward lilimshangaza sana Olivia Komba

“Hivi hamjaridhika na kamera mliyoitega mpaka utumwe kunipeleleza ndani ya chumba hiki? Kawaambie wenzako kuwa hutapata kitu toka kwangu”

Olivia Komba alibaki mdomo wazi, macho yalimtoka huku yakitazama sura ya Derrick Edward aliyekuwa makini akiendelea kuukagua mwili wake. Kauli ya Derrick Edward ilimuhakikishia Olivia Komba kuwa ndani ya chumba kile kulipandikizwa kamera iliyokuwa ikiendelea kuchukua matukio na kuyasafirisha mpaka kwa wahalifu. Vile vile, aliamini Derrick Edward amemtambua yeye kama jambazi aliyepandikizwa kumpeleleza kisha kupeleka taarifa hizo kwa maharamia. Olivia Komba alisimama kisha akacheka kwa sauti, kicheko kile hakikumshitua wala kumshangaza Derrick Edward aliyejiaminisha kuwa mrembo yule alikuwa jambazi sugu. Olivia Komba hakuongeza kauli yoyote, aliangaza kila pande ya chumba kile. Alikuwa akikagua kamera iliyosemwa na Derrick Edward. Aliiona kamera ikiwatazama toka kona moja ya chumba kile, ilikuwa wazi kabisa pasipo kufichwa. Olivia Komba alisogea mpaka mbele ya kamera ile kisha akaongea kwa sauti kubwa iliyojaa hasira

“Nafikiri hamtafanikiwa katika mpango wenu”

Derrick Edward aliisikia kauli ya Olivia Komba lakini hakuitilia maanani, aliamini itakuwa kauli ya kucheza na akili yake. Ilikuwa zamu ya Derrick Edward kucheka, alisimama wima kama alivyosimama Olivia Komba kisha akaanza kutembea tembea ndani ya gereza lile huku ameinamisha kichwa chini. Kitendo kile kilidhihirisha alikuwa akitafakari jambo fulani lakini kabla hajaongea chochote kati ya tafakari yake ghafla walishangaa kuwaona vijana wawili kati ya wale vijana waliomuingiza Olivia Komba wakifungua mlango wa gereza lile. Mmoja kati ya vijana waliofika mbele ya mlango wa gereza alimuamuru Derrick Edward kutoka ndani ya chumba cha gereza. Ilikuwa kauli ya kushangaza lakini haikutoa nafasi ya kuulizana maswali, Derrick Edward alifanya kama alivyoagizwa kisha gereza likafungwa. Olivia Komba alibaki peke yake ndani ya chumba kile cha gereza. Vijana wale waliongozana na Derrick Edward hatua moja mpaka nyingine, wakafanikiwa kuingia katika chumba cha nne kutoka chumba cha gereza. Derrick Edward alisambaza macho yake katika chumba kile akakikagua haraka haraka, ukaguzi wake ulimthibitishia kilikuwa chumba cha mateso.

Kilikuwa na mazingira yaliyomtisha kidogo, kilining`inia minyororo, suala hilo lilimdhihirishia minyororo ile hutumika kuwafunga mateka kipindi cha kuwapa adhabu. Katikati ya chumba kile akiliona kiti cha chuma kikimtazama kwa hamu kubwa, kiti kile kilikuwa na pingu sehemu ya mbele ya miguu na sehemu ya juu yenye uwezo wa kuifunga mikono. Alijihakikishia kiti kile hutumika wakati wa kumpiga shoti ya umeme mateka wao, vile vile pingu zile hutumika kumfunga mateka wao ili asifurukute kipindi umeme ukipita katika mwili wake. Vijana wale walimpeleka Derrick Edward mpaka kwenye minyororo iliyokuwa ikining`inia kwa hamu kubwa ya kumfunga mateka. Walimfunga mikono na miguu katika minyororo, akawa kama mtu aliye msalabani. Miguu yake iliachanishwa kwa sentimeta thelathini. Derrick Edward alikuwa mpole kipindi akifanyiwa matukio hayo, hakuweza kubisha kwa sababu wahusika walikuwa na silaha za moto aina ya AK 47 zenye risasi za kutosha. Aliamini bora nusu shari kuliko shari kamili. Vijana walipojihakikishia mateka wao amefungwa barabara kwa minyororo ile waliondoka pasipo kusema neno. Derrick Edward alielewa ulikuwa umefika wakati wa mateso, wakati wa kulazimishwa kuongea kupitia kipigo na mateso. Alitabasamu kisha akaongea kwa sauti dhaifu kama akimnong`oneza mtu

“Tatizo maswali wanayoniuliza sina majibu yake kabisa. Wataniua bure”

Kipindi sura yake ikiendelea kushambuliwa na tabasamu ghafla alimuona Amani Collence akiingia ndani ya chumba kile akiwa ameongozana na vijana wawili walio vifua wazi. Miili ya vijana wale ilivimba kwa mazoezi waliyokuwa wakiyafanya kila siku. Akili ya Derrick Edward ilithibitisha kuwa kazi ya vijana wale ilikuwa kumpiga mpaka aongee walichotaka kusikia, hakika alikuwa sahihi. Amani Collence alisimama mbele ya Derrick Edward, upande wake wa kushoto na kulia wakiwa wamesimama vijana wale wenye mbavu za tembo. Akamwambia mateka wake

“Nafikiri sasa utaongea, nilitumia demokrasia ukagoma kusema chochote. Sasa natumia njia ya vita, utasema utake usitake”

Baada ya kauli hiyo alisogea akakaa katika kiti cha chuma kilichofungwa pingu kila upande kisha akawaambia vijana wenye mbavu za tembo

“Anzeni kazi yenu”

Vijana wale walimshambulia Derrick Edward kama nyuki waliochokozwa mzingani. Alipigwa ngumi za uso, mbavu, mgongo na kila mahali walipohisi pangemlainisha kuongea lakini hali ilikuwa tofauti, Derrick hakuwa na cha kuongea. Kwa kipigo alichokipata alijisemea moyoni kama angelikuwa akijua chochote alichoulizwa angeliongea ili wamuache, bahati mbaya alikuwa hajui chochote. Kitendo kile kiliwaaminisha wahalifu kuwa Derrick Edward alikuwa akibisha na kuweka kiburi cha kuongea. Amani Collence alisimama wima kisha akapiga hatua mpaka mbele ya Derrick Edward, akamuuliza kwa mara nyingine

“Kwani unajificha katika kivuli cha sanaa wakati unashirikiana na Nasrat Abdul al Aziz?”

Derrick Edward alishindwa kujibu kwa sababu alikosa kauli aliyohisi ingeweza kumuweka huru, alikuwa akigugumia kwa mauvimu makali huku kichwa chake kikimfikiria Nasrat Abdul al Aziz. Alijuta kujiingiza kwenye mapenzi na mwanamke aliyekuwa hamjui vizuri. Alijiona mjinga alivyozama kwenye penzi la binti wa Kiarabu. Sasa aliamini Nasrat Abdul al Aziz atakuwa alimtegea mtego wa mapenzi ili afanikishe mambo yake. Derrick Edward aliendelea kumkodolea macho Amani Collence aliyekuwa akitabasamu kila muda, Amani Collence alivyoona ajibiwi swali lake akaongea

“Sababu kuu ya kukukamata ni kutaka kumnyoosha Nasrat, alijifanya mjanja kuchukua mzigo wetu kisha akatugeuka. Akakupachika kwenye sanaa ili uwahadae raia ili msafirishe biashara zenu kirahisi”

Kauli za Amani Collence zilizidi kumchangaya Derrick Edward aliyekuwa hawezi hata kuuhimili mwili wake, alikuwa amesharegea mithili ya mlenda. Mwili wake ulizuiliwa kwa nguvu ya minyororo. Derrick Edward aliendelea kukaa kimya, aliona jinsi alivyoingizwa kwenye uchafu wa Nasrat Abdul al Aziz. Kimya cha Derrick Edward hakikusababisha Amani Collence aache kuongea. Aliongea kila kauli aliyohisi alistahili kuongea mbele ya Derrick Edward. Kati ya kauli hizo kuna kauli moja ilimchangaza zaidi Derrick Edward, kauli ambayo ilimuacha Derrick Edward mdomo wazi, kauli ile ilisema

“Nasikia mtoto wa mzee Masiya yupo katika himaya yenu, na mna mpango wa kwenda Afrika Kusini”

Kauli hiyo ilimkumbusha Derrick Edward kijana aliyefika ofisini kwake akihitaji picha ya mzee Masiya iliyochorwa na kuchongwa. Alikumbuka namna alivyomtilia mashaka kijana yule mpaka akamtegea kamera katika kinyago kwa lengo la kubaini kijana yule alikuwa akifanya kazi chini ya nani lakini hakufanikiwa. Alikumbuka alivyofanikiwa kupata picha ya kijana mtanashati mwenye rasta fupi. Aliunganisha matukio, akaona jinsi Nasrat Abdul al Aziz alivyokuwa nyuma ya mchezo mchafu aliokuwa akichezewa pasipo kujua. Alidhihirisha kuwa Nasrat Abdul al Aziz atakuwa ndiye bosi wa vijana wale kwa sababu gari lililobeba kazi zile za sanaa lilikuwa likielekea uelekeo wa makazi ya Nasrat Abdul al Aziz kabla hajapoteza mawasiliano nalo. Kabla ‘microchip’ haijapoteza mawasiliano. Aliamini Nasrat Abdul al Aziz ndiye aliyehitaji kazi zile za sanaa. Swali lililobaki likimsumbua Derrick Edward lilkuwa

“Anawezaje kufanya mambo haya kwa siri namna hii?”

Alikosa jibu, akajikuta akitabasamu. Kitendo cha kutabasamu kilitafsiriwa tofauti na Amani Collence. Amani Collence alihisi akidharauliwa na mateka wake. Aliwapa amri vijana wenye mbavu ya tembo wamshughulikie. Hakika walimshughulikia ipasavyo. Alipiga kelele za kuomba msaada lakini ilikuwa kazi bure, alikuwa akiwapigia mbuzi gitaa. Alipigwa mpaka akapoteza fahamu. Mwili wake ukabaki ukining`inia kwenye minyororo. Wapigaji walipothibitisha fahamu hazikuwa sehemu ya mwili wa Derrick Edward walimfungua toka kwenye minyororo wakamuacha sakafuni, kisha kwa amri ya Amani Collence wakaondoka ndani ya chumba kile. Upande wa pili ndani ya gereza, Olivia Komba alisikia namna Derrick Edward alivyokuwa akilalamika kwa maumivu kipindi alipokuwa akishambuliwa na wale vijana wenye mbavu za tembo. Olivia Komba alijisemea moyoni

“Hakika wafanya biashara haramu hawapendani”

Mawazo ya Olivia Komba yalienda mbali sana, aliamini Derrick Edward alikuwa mfanya biashara haramu toka kundi tofauti na kundi la watekaji. Aliamini kitendo cha kupigwa namna ile kilitokana na kugeukana kati ya makundi yao. Mawazo yake yalienda mbali zaidi akaamini siku za kupigwa kwake zinahesabika, alijua lazima ahojiwe na endapo akiwa mbishi lazima magaidi watumie njia haramu kulazimisha kupata taarifa kutoka kwake. Alijiandaa kwa lolote alilohisi lingeweza kutokea. Masaa yalisogea kama yakisukumwa na upepo wa kiangazi, giza la usoni lilianza kulazimisha watembea kwa miguu kuwasha tochi zao za simu au kifaa chochote cha kuzalisha mwanga kwa lengo la kurahisisha mjongeo wao. Wenye vyombo vya moto hawakusumbuka sana, waliwasha mataa ya vyombo vyao, yote hayo yalifanywa kwa lengo la kupambana na giza lililozalishwa katika sura ya nchi.

Ndani ya jengo lililokuwa chini ya Amani Collence hali ilikuwa tofauti kidogo, wao hawakujali hali ya giza lililozalishwa katika eneo lao, akili zao zilikuwa juu juu kama tiara iliyokata kamba. Hali hiyo iliwavaa baada ya kuona hali ya Derrick Edward ikiendelea kuwa mbaya kila muda ulivyozidi kwenda, hali ile ilimaanisha Derrick Edward angeweza kufa mbele yao kama wasipochukua hatua za haraka za kuokoa maisha yake. Amani Collence hakuhitaji kuona maiti ya Derrick Edward, alihitaji Derrick Edward kuwa hai ili aweze kumtumia kama ngao ya kumuadhibu Nasrat Abdul al Aziz. Aliamini uhai wa Derrick Edward ulikuwa na maana kubwa katika harakati zake za kimapambano. Derrick Edward alibebwa haraka haraka mpaka katika chumba kilichoandaliwa kwa shughuli za kitabibu.

Chumba hicho kilikuwa kikubwa chenye vitanda vitatu maalumu kwa kulaza wagonjwa ndani ya ngome hiyo. Kilizungukwa na vifaa mbalimbali za kitabibu pamoja na dawa zilizohifadhiwa katika ubora uliotukuka. Kilikuwa chumba kimoja chenye hadhi ya wodi na famasi. Derrick Edward alilazwa kwenye moja ya vitanda vile, alikuwa hajui kilichokuwa kikiendelea. Fahamu zake zilikuwa mita mia kutoka ulipokuwa mwili wake. Hofu iliendelea kumtafuna Amani Collence, alitafuta jina haraka haraka katika simu yake, alipolipata alipiga. Simu iliita sekunde kadhaa kisha aliyepigiwa akapokea. Pasipo hata salamu za kujuliana hali, Amani Collence aliongea haraka haraka kwa sauti ya kitetemeshi, sauti iliyojielezea hakuwa sana hata kidogo

“Dokta! nakuomba mara moja katika ngome yangu, kuna dharura. Nakuhitaji dokta”

Amani Collence hakusubiri jibu la daktari, alikata simu kisha akakaa juu ya kitanda alicholazwa Derrick Edward. Aliitazama sura ya Derrick Edward iliyokuwa haitamaniki kwa kipigo alichopata, tabasamu likapita katika sura yake, tabasamu lililokinzana na hali ya moyo wake. Alishangaa kwanini alitabasamu wakati alikuwa katikati ya dimbwi la mawazo ya kupigania uhai wa Derrick Edward. Kipindi akiendelea kupambana na mawazo yake alishitushwa na mlio wa simu yake, alipoitazama aliona jina la mlinzi kiongozi wa ngome hiyo. Aliipokea haraka sana kisha akaiweka sikioni. Mlinzi kiongozi akamsalimia bosi wake kwa heshima kisha akampa taarifa ili apate ruhusu yake

“Nimepewa taarifa na vijana wangu wa getini kuwa daktari Johnson anataka kuingia, vipi una taarifa ya ujio wake?”

Japokuwa mlinzi kiongozi alimfahamu daktari Johnson na alielewa daktrai huyo hutumika kutoa huduma za kitabibu katika ngome hiyo lakini halikumaanisha kumruhusu kuingia pasipo kauli ya bosi. Ilikuwa desturi au sheria mtu asiye mwanachama wa moja kwa moja wa ngome hiyo kuruhusiwa kuingia kwa kauli ya bosi tu, na siyo vinginevyo. Taarifa ya mlinzi kiongozi ilifufua matumaini ya uhai wa Derrick Edward. Amani Collence hakusita kutoa jawabu la ruhusa, jawabu lake lilimpa nguvu mlinzi kiongozi kuwaruhusu vijana wake kumruhusu daktari Johnson kuingia. Daktari Johnson aliingia haraka haraka mpaka kwenye chumba alicholazwa Derrick Edward, alimkuta Amani Collence akimsubiri. Alikaribishwa kwa uchangamfu.

Siku zote Amani Collence alikuwa mchangamfu kwa daktari huyo, uchangamfu huo ulikuwa na lengo la kudumisha mshikamano kati yao. Daktari Johnson alisogea alipolazwa Derrick Edward, alimtazama vizuri mgonjwa wake.
Hapo ndipo alipogundua dunia ni ndogo, dunia ni kama kiganja cha mkono. Japokuwa sura ya Derrick Edward ilikuwa imeharibika kwa kiasi kikubwa lakini hakuisahau hata kidogo, aligundua ilikuwa sura ya mwanasanaa maarufu. Hicho hakikumshangaza hata kidogo, kilichomshangaza ni suala la mwanasanaa huyo kuwa mikononi mwa Amani Collence, alishindwa kuelewa lakini kwa akili ya ajabu aliweza kuhusianisha uadui wa Amani Collence na Nasrat Abdul al Aziz. Hapo ndipo alipopata sababu ya kumuona Derrick Edward katika hali ile, alielewa Derrick Edward alikamatwa ili atumike kama shinikizo la kumuadhibu Nasrat Abdul al Aziz. Daktari Johnson alikumbuka alivyompima Nasrat Abdul al Aziz na kugundua alikuwa mjamzito, vile vile alikumbuka harakati zake na Nasrat Abdul al Aziz. Harakati za kulipa kisasi cha ndugu na jamaa zao. Aliapa kuwa bega kwa bega na Nasrat Abdul al Aziz katika mazingira yoyote, kwake Nasrat Abdul al Aziz alikuwa kama mdogo wake wa damu.

Amani Collence hakujua uhusiano wa daktari Johnson na Nasrat Abdul al Aziz, hakujua watu hao walikuwa kwenye mpango mmoja wa kulipa kisasi cha ndugu zao. Muda wote daktari Johnson alikuwa akitumiwa na makundi ya kigaidi kama daktari wao, kipindi chote hicho alichota taarifa na siri zao kisha kuziwasilisha kwa Nasrat Abdul al Aziz. Hakuna kundi lingine lililofahamu kama alikuwa akitumika katika makundi tofauti. Waliamini daktari Johnson alikuwa daktari wao pekee, hawakujua kama alitumika katika himaya za maadui zao. Kila kundi lililofika kuomba msaada wake, alilipokea kwa mikono miwili na kulitumikia kila lilipohitaji. Alikuwa jasiri, hakuogopa kuuliwa kama akigundulika na makundi hayo, yeye aliwaza kusafisha njia ili wafanikishe kulipa kisasi. Daktari Johnson alimtazama kwa makini mgonjwa wake aliyekuwa nje ya fahamu zake, alimpa huduma za kitabibu kama kawaida. Muda wote daktari Johnson alikuwa makini bila hofu wala wasiwasi wa aina yoyote, alielewa endapo Amani Collence akigundua kitu kilichokuwa akilini kwake lazima angekatishwa maisha. Hakuwa tayari kufa kizembe, namna ile. Baada ya kutoa huduma za kitabibu, daktari Johnson alimwambia Amani Collence

“Mgonjwa amepoteza damu nyingi. Nimechukua sampuli ya damu naenda kuipima ili nifahamu kundi lake, nikifahamu nitakuja na damu hiyo haraka ili tuokoe uhai wa kijana huyu”

Amani Collence hakuwa na kauli yoyote mbele ya daktari Johnson, hakuwa mbishi hata kidogo kwa sababu hakuwa na uelewa wowote wa kitabibu. Yeye mwambie masuala ya madawa ya kulevya na mauaji. Alimruhusu daktari Johnson kuondoka na sampuli aliyoichukua, alimsindikiza mpaka nje ya jengo. Daktari Johnson akapanda gari lake kisha akaondoka kwa mwendo wa wastani.

ITAENDELEA
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom