Riwaya: Kikosi cha Kisasi

Willy Gamba akiwa amejipumzisha kwenye bwawa la kuogelea pamoja na Tete
20890a724f4f96b7eab8838ded342cc4.jpg

hahahahahah jamani unamsingizia siyo kweli ila kama vile ni kweli
 
SURA YA KUMI

MAPAMBANO BADO YANAENDELEA

III

Willy alisimamisha gari lake kwenye maegesho ya Memling Hoteli. Alitoa kadi aliyokuwa amepewa na Ntumba akasoma anwani ya nyumbani kwake Ntumba na kujitayarisha kwa maswali. Aliingia pale hotelini kama kwamba hana habari yoyote. Alipotaka kupanda ngazi za kwenda juu akasimamishwa na meneja wa hoteli.

"Wewe unaitwa Willy Chitalu?"

"Ndiyo", Willy alijibu.

"Samahani kidogo, ninakuhitaji ofisini", Meneja alimwambia Willy. Willy bila kubisha alimfuata meneja huyo. Alipoingia ofisini mwa meneja huyo alikuta mna watu wawili. "Karibu Bwana Chitalu. Samahani sikukujulisha hapo nje, mimi ndiye meneja wa hoteli hii na hawa mabwana wawili wanatoka kwenye idara ya polisi", Meneja alieleza. Willy alisalimiana na watu hawa kisha akavuta kitu akakaa. Wale jamaa wa polisi walitoa vitambulisho vyao kumhakikishia Willy kuwa kweli wao walikuwa polisi kutoka idara ya upelelezi ya makosa ya jinai.

"Bwana Chitalu, sijui kama una habari kuwa mfanyakazi wetu mmoja aliyekuwa anafanyakazi hapo mapokezi aitwaye Mwadi ameuawa?" Meneja aliuliza.

Willy alionyesha sura ya kushtuka sana na kushangaa kiasi kwamba hata polisi walidanganyika.

"Sina habari", alijibu taratibu kabisa.

"Basi hawa mabwana wana maswali machache ya kukuuliza. Usiwe na wasiwasi kwani wapangaji wetu wote inabidi waulizwe. Wewe mwenyewe unajua wakati kitendo kama hiki kikitokea lazima mambo kama haya yatokee". Meneja alijaribu kumtuliza.

"Hamna taabu", alijibu Willy kwa unyonge.

Polisi mmoja alitoa daftari tayari kwa kuandika malezo na mwingine akajitayarisha kwa kuuliza.

"Bwana Chitalu kama alivyokueleza Meneja, maswali yetu ni jambo la kawaida tatizo kama hili linapotokea, hivi unaombwa kueleza ukweli mtupu", yule polisi alimweleza.

""Hamna wasiwasi", Willy alijibu.

"Bwana Chitalu umefika hapa mjini lini?" Polisi aliuliza.

"Jumatatu", alijibu Willy.

"Ni mara yako ya ngapi kufika mjini Kinshasa?"

"Mara ya tatu", alijibu Willy.

"Huyu msichana Mwadi ulikuwa unamfahamu?"

"Ndiyo", alijibu Willy.

"Kwa muda gani umemfahamu?"

"Toka Jumatatu", alijibu.

"Je mmewahi kuwa na uhusiano wowote toka siku hiyo?"

"Ndiyo", alijibu Willy.

"Uhusiano wa namna gani?"

"Uhusiano wa kawaida tu wa mwanamke na mwanaume", alijibu Willy.

"Je, umewahi kufika kwake ama kwenda naye mahali popote?"

"Ndiyo", alijibu Willy.

"Lini na wapi mlitembelea?"

"Juzi usiku na tulitembelea Parafifi baa", Willy alijibu.

"Je jana jioni mlionana?"

"Hapana", Willy alijibu.

"Unaweza kutueleza jana kiasi cha saa kumi na moja jioni mpaka leo asubuhi ulikuwa wapi?"

"Nilikuwa nimekaribishwa mahali", alijibu.

"Mahali gani?"

"Kwa msichana mmoja," alijibu.

"Unaweza kututajia jina la huyo msichana?" Willy alisita kidogo kisha akasema, "Anaitwa Ntumba Akanda".

"Anakaa wapi?"

"Anakaa huko Matonge barabara ya Inzia nyumba nambari 26B ", Willy alijibu.

"Anafanya kazi?"

"Ndiyo."

"Wapi?"

"STK uwanja wa ndege", alijibu Willy.

"Una maana jioni yote ulikuwa huko na hukuondoka hata mara moja mpaka asubuhi?"

"Ndiyo", alijibu Willy.

"Una lolote unaloweza kutueleza juu ya mauaji ya Mwadi?"

"Nimesikitika sana", alijibu Willy.

Yule polisi aliyekuwa anauliza maswali alimwangalia mwenzake na mwenzake naye akaonekana kuwa hakuwa na swali zaidi.

"Asante sana bwana Chitalu. Tunalokuomba ni kwamba usiondoke hapa mjini bila kupasha habari kituo cha polisi cha 'Brigede Mobile'. Vile vile tunakuomba usihame kutoka hoteli hapa mpaka sisi tuwe tumepata habari", yule polisi alimweleza.

"Hamna wasiwasi", Willy alijibu.

"Unaweza kwenda".

"Asanteni sana," aliaga Willy na kutoka nje.

Wale polisi walichukua simu na kupiga moja kwa moja STK uwanja wa ndege. Walimuulizia Ntumba na walipompata walimuuliza kama alikuwa anamfahamu Willy Chitalu. Baada ya mazungumzo marefu aliwathibitishia kuwa alikuwa na Willy tokea saa kumi na moja jioni mpaka asubuhi. Waliridhika wakaondoka.

Willy alipoondoka ndani ya ofisi ya meneja aliitwa na kijana aliyekuwa mapokezi.

"Kuna msichana mmoja anaitwa Tete amekupigia simu zaidi ya mara nne, anasema umpigie," yule kijana alimweleza. Willy alimpa simu ya Tete na kumwambia. "Ukimpata niletee simu chumbani kwangu", Willy alipoingia chumbani kwake alikuta chumba chake kimepekuliwa kwa ustadi sana kiasi cha kwamba mtu wa kawaida asingeweza kujua. Aliangalia vitu vyake akakuta vyote salama. Yeye naye akakipekua kile chumba kuona kama wangeweza kuwa wameacha chombo chochote cha kunasa sauti hakukuta kitu. Mara kengere ya simu iliita.

"Hallo", Willy aliita.

"Zungumza na Tete", yule kijana wa mapokezi alimwambia.

"Hallo, Willy hapa".

"Tete, habari yako?" Tete alijibu kwa sauti ya chini sana.

"Nzuri, je wewe?" Willy aliuliza.

"Bado moyo wangu mzito sana kwa ajili ya kifo cha Mwadi," Willy alijibu.

"Tafadhali sana tuonane saa sita. Sasa hivi ni saa sita kasoro dakika ishirini, tafadhali fanya kila njia tuonane nina jambo la lazima," Tete alisema kwa sauti ya wasiwasi.

"Wapi?" Willy aliuliza.

"Mahali popote utakapoona pana usalama hata kama ni hapo hotelini kwako", Tete alijibu.

Willy alifikiria nini msichana huyu alikuwa anamtakia lakini, hakupata jibu. Alifikiria huenda akina Muteba walikuwa wamemuwekea mtego lakini akaamua ajaribu bahati yake. Hata yeye alikuwa na haja ya kuzungumza na msichana huyu lakini si kwa namna hii.

"Fanya hivi, ukitoka njoo na gari lako moja kwa moja na barabara ya 30 Juin halafu ingia kwenye maegesho ya Banque Comerciale Zairose, mimi nitakukuta hapo, sawa?" Willy alieleza.

"Sawa, saa sita", alijibu Tete.

"Saa sita", alijibu Willy huku Tete akiwa tayari ameisha kata simu. Baada ya kuweka simu chini, Willy alibadilisha nguo zake haraka haraka, halafu akatelemka chini mbio mbio. Aliingia ndani ya gari lake, akaondoka kuelekea kwenye ofisi za Agence Sozidime. Willy aliposimamisha gari lake katikati ya magari yaliyokuwa kwenye maegesho ya Cine Rac ilikuwa saa sita kasoro dakika tano.

Alitoka ndani ya gari na kuelekea upande mwingine wa barabara ambapo alibana kwenye sehemu ambapo alikuwa anaona moja kwa moja ndani ya lango la ofisi za Sozidime. Hakuwa hata hajajibanza vizuri alipomuona Tete akiwa anatoka ndani, akaingia ndani ya gari lake, akawasha moto na kuondoka. Mlinzi wa pale alimfungulia lango na gari la Tete likapita.

Willy alisubiri kuona kama kulikuwa na gari lolote linamfuata Tete. Lakini hakuona dalili. Alikimbia mpaka kwenye gari lake na kuondoka kwa mwendo mkali alimfuata Tete. Ni kwenye barabara ya 30 Juin alipomuona, alimfuata pole pole mpaka walipofika B.C.Z. Tete akaingia kwenye maegesho ya pale kama Willy alivyokuwa ameagiza. Willy huku akiwa amehakikisha kuwa hakukuwa na mtu aliyekuwa anawafuata naye aliingia kwenye maegesho ya B.C.Z. akafunga gari lake akafuata pale Tete alipokuwa ameegesha. Alipofika kwenye gari la Tete alimwambia.

"Sogea huko, mimi nitaendesha," Tete alisogea kwenye kiti cha abiria, Willy aliingia kwenye kiti cha dereva akawasha gari moto, wakaondoka.

"Mbona umeacha gari lako?" Tete alimuuliza.

"Napenda sana kuendesha gari aina ya sports", alitania Willy.

"Tunakwenda wapi sasa?" Tete aliuliza.

"Mahali penye usalama kama ulivyokuwa umesema", Willy alijibu. Willy alikuwa amekata shauri kuwa, mahali penye usalama pa kuweza kuzungumza na Tete palikuwa nyumbani kwa Robert tu, potelea mbali kama angegundua maficho yao, lakini alitumaini ya kwamba lilikuwa ni jambo la busara.

Walifika nyumbani kwa Robert na kukuta hakuna mtu. Willy alifungua gereji na kulificha gari la Tete ndani kwani alitegemea gari la msichana kama Tete lazima lingekuwa linafahamika mjini. Alimkaribisha ndani, akatayarisha kinywaji kwa ajili yao wote.

"Hapa ni nyumbani kwa nani?" Tete aliuliza.

"Kwa rafiki yangu" Willy alijibu.

"Mbona jana hukurudi nyumbani kwangu kama ulivyoahidi?" Tete aliuliza.

"Shughuli zilinizidi", Willy alijibu.

"Kwanza nataka kutoa shukrani zangu kwa kumlipizia rafiki yangu Mwadi kisasi", alisema Tete.

"Umejuaje kama nililipiza?" Willy aliuliza.

"Si uliniambia kuwa ungelipiza, na nikapata habari toka kwa Muteba kuwa Kabeya ameuawa hivi nikajua umelipiza," Tete alijibu.

"Muteba alikueleza saa ngapi?" Willy aliuliza.

"Alikuja nyumbani kwangu kiasi cha saa kumi za asubuhi. Kwanza tuache hayo tafadhali Willy nataka unieleze bila kunificha chochote wewe ni nani na uko hapa Kinshasa kwa ajili gani, halafu na mimi nitakueleza mambo ambayo ninaamini yatakuwa na manufaa kwako. Mpaka sasa hivi ninauza maisha yangu kwa ajili yako, tafadhali usinifiche", Tete alisema.

"Kwanini ujitolee kuuza maisha yako kwa ajili yangu?" Willy alimuuliza.

"Kwa sababu ile ile ambayo ilimfanya Mwadi auze maisha yake kwa ajili yako. Mwadi alikuwa rafiki yangu mpenzi sana, hivi niko tayari kuendeleza chochote alichoacha bila kumaliza," Tete alieleza.

"Mimi nitakuamini namna gani kukueleza mambo hayo unayotaka kuyajua?" Aliuliza Willy.

"Nafikiri itabidi uniamini au kama huniamini ubahatishe kuniamini, maana nadhani kama nilivyokueleza kuwa nina habari zinazoweza kuwa na manufaa," Tete alijibu.

"Wewe unaaminije kuwa niliyokueleza ni ya kweli?" Willy aliuliza.

"Mimi ninaamini lazima mtu kama wewe si wa kusema uongo," alijibu Tete.

Willy aliamua kujitosa na kumweleza msichana huyu kila kitu na ikiwa kama alikuwa ametumiwa kuja kumdadisi, hayo yalikuwa mambo ya kawaida katika kazi hivi angeweza kuyakabiri bila taabu.

"Nimeridhika Tete, hivi nitakueleza kwa kirefu. Mimi jina langu hasa ninaitwa Willy Gamba na kazi yangu mimi ni mpelelezi." Willy alimweleza. Tete alimwangalia kwa macho makavu bila kuonyesha mshangao wowote. Akiwa anavutwa na uzuri na ukali wa macho ya msichana huyu. Willy alimweleza kwa ufasaha kabisa mambo yaliyokuwa yamemleta hapa pamoja na wenzake na mambo yote waliyokuwa wameyafanya mpaka wakati huo. "Ulitaka kujua sasa umeshajua, nimekueleza kila kitu sikuacha kitu," Willy alimalizia.

"Sasa nimeelewa, nimeelewa kabisa kwanini mambo yako namna ile ofisini kwetu. Nilikuwa naona mambo mengi ya ajabu ajabu lakini sikuwa ninajua yana maana gani. Umenifumbua macho, nimekuwa kama kipofu ambaye amefumbuliwa macho. Wamekuwa wananitumia kwa mambo mengi bila mimi kujua," alieleza Tete akiwa kama anazungumza ndotoni.

"Uliniambia kuwa ungenieleza mambo ambayo yangekuwa na manufaa kwangu, nieleze".

"Mambo mengi umeshayaelewa kutokana na ulivyonieleza. Ni kweli kabisa kuwa Kampuni yetu inashughulika na mambo ya kijasusi sasa nimeona kwanini mambo yako hivyo. Mkurugenzi wetu anaitwa Fernand Barbier anajiita kuwa ni Mbelgiji lakini ni kaburu. Huyu Mkurugenzi wa 'Gereji Du Peuple', Pierre Simonard naye si Mbelgiji ni kaburu hata Jean Vergeance. Mambo haya niliwahi kuelezwa na Muteba siku moja wakati mapenzi yetu yalipokuwa moto sana. Nilimuuliza hawa wazungu alifahamiana fahamiana nao namna gani akanieleza kuwa alikuwa ameonana nao huku Afrika Kusini alipokwenda huko na askari wa kukodiwa baada ya kupigana na askari hao upande wa majeshi ya Tshombe huko jimbo la Shaba", Tete alinyamaza kidogo kuvuta pumzi kisha akaendelea.

"Nilipomuuliza kwa nini wanajiita kuwa ni Wabelgiji, alisema kuwa ingekuwa vigumu kwa makaburu kufanya biashara katika nchi huru ya Kiafrika kufuatana na siasa ya nchi za Kiafrika. Hii ndiyo alitoa kama sababu kwa nini watu hawa walikuwa wanatumia uraia wa bandia. Yule Maximilian leo uliyekuja kumuona, naye si Mbelgiji bali ni Mfaransa. Mpaka sasa nashindwa kujua kwa nini anatumia uraia bandia, Kwani Wafaransa hawakataliwi katika Afrika na wako chungu nzima hapa Zaire kwa shughuli mbali mbali", Tete alitua tena kuvuta pumzi kisha akaendelea.

"Huyu Max kama tunavyomuita aliwahi kunieleza mwenyewe akijitapa mbele yangu kuwa si Mbelgiji bali ni Mfaransa kamili." Tete alimwangalia machoni Willy, akasita kidogo kama kama kwamba anaona haya kueleza alichotaka kueleza, kisha akaangalia sehemu nyingine akaendelea. "Max ananipenda sana mimi, amekuwa ananitongoza kwa muda mrefu sana. Anamchukia sana Muteba kwa ajili yangu mimi. Katika kutaka kujionyesha alivyo na thamani kuliko Muteba na hawa watu wengine, amekuwa ananieleza mambo mengi sana. Anasema amewahi kuwa Meneja katika jeshi la Ufaransa kabla hajaweza kupewa kazi mbali mbali katika nchi mbali mbali zenye uhusiano na Ufaransa. Wakati fulani Fernand alikwenda Ulaya kwa likizo yeye akabaki ndiye Mkuu wa ofisi yetu. Siku moja Lucie alikuwa anaumwa mimi nikawa nafanya kazi ofisini kwake ilipofika saa za kufunga ofisi aliniambia nisiondoke kuna kazi. Wafanyakazi wengine wote waliondoka tukabaki mimi na yeye tu. Kisha akafunga milango ya kutokea nje ya ofisi akanijia nimfuate." Tete alitabasamu kidogo kisha akaendelea.

"Nilimfuata ingawaje kwa woga sana lakini nilitaka nijue nini nia yake. Tulienda mpaka kwenye ofisi ya Fernand akafungua tukaingia ndani akafunga. Akiwa sasa amenishika mkono tulienda mpaka kwenye ukuta ambao ulikuwa nyuma ya meza ya Fernand. Alinieleza kuwa nisiogope kwani alitaka kunionyesha milango inayoenda kwenye chumba cha siri ambako ndiko tungeweza kufanya mazungumzo yetu. Alienda kwenye pembe ya ukuta wa nyuma kulikuwa na kidude akakibonyeza mara ukuta ukaachana na kuwepo na mlango. Kumbe ukuta huo ulikuwa wa bandia ulikuwa wa mbao. Chini ya mlango kulikuwa na ngazi zinatelemka chini, aliwasha taa za kwenye ndazi hizi, na tulipokuwa kwenye uchochoro wa ngazi hizi za kutelemka chini alibonyeza kidude kingine, ukuta ule ukarudi sawa sawa. Tulitelemka chini tukakuta mlango akaufungua tukaingia ndani ya chumba kimoja kizuri ajabu, kilikuwa na kila kitu. Kitanda kikubwa, makochi mazuri, barafu, jiko la umeme, kusema kweli chumba hiki kilikuwa na kila kitu mtu anaweza kuhitaji. Vile vile mlikuwa na makabati mawili makubwa ya chuma. Max alinionya kabisa kuwa nisimweleze mtu yeyote juu ya chumba hiki na akasema ni yeye na Fernand tuu waliokuwa wanajua juu ya chumba hiki na kwamba mimi ndiye nilikuwa mtu wa tatu," Tete alimwangalia Willy, kisha akaendelea. "Kusema kweli Willy sijawahi kumwambia mtu ila ni wewe leo. Nilipomuuliza kwa nini iliwabidi wawe na nyumba ya namna hii, alijibu kuwa kwa ajili ya usala wao yakitokea machafuko, kwani Zaire ni nchi yenye machafuko mara kwa mara.

Nilimuuliza chumba kama hiki kilikuwa na usalama gani. Akaniambia kuwa nyumba hii ilikuwa ya Jenerali mmoja wa jeshi la Kibelgiji ambaye alijijengea kwa usalama wake wakati wa msukosuko. Alisema Jenereli huyo alikuwa amekitengenezea chumba hiki mlango ambao ulikuwa unatokea sehemu nyingine kabisa. Alienda kwenye sehemu nyingine ya ukuta akabonyeza kidude kama kile alichokuwa amebonyeza ofisini kwa Fernand mara ukuta ukaachana na nikajikuta naangalia ndani ya uchochoro wenye giza kubwa. Akaniambia kuwa uchochoro huu ulikuwa unatokea nyuma ya lile jumba refu liitwalo' Galleries Presidentielles', na kulikuwa na taa ndani ya uchochoro huu. Max alinieleza yote haya ili niweze kumtia maana kusudi niweze kumtimizia haja zake. Wanaume wana matatizo sana," Tete alinyamaza na kumwangalia Willy, lakini Willy aliendelea kumwangalia katika hali ile ile, "Sasa leo ndiyo nimejua kwa nini Sozidime ina ofisi za namna ile. Nimekubaliana kabisa Willy, ile ni ofisi ya majasusi ndiyo sababu iko vile", Tete aliendelea.

Maelezo yote haya yalimwingia Willy kama nyali za moto. Alijiona mtu mwenye bahati sana katika safari hii kwani alikuwa ameweza kupata habari za muhimu sana bila matatizo makubwa. "Je umewahi kwenda kuona pale kwenye uchochoro huo unapotokea?" Willy aliuliza.

"Kwa bahati nimewahi. Nilitaka kuhakikisha kama maneno ya Max ni kweli kwani mimi sikuamini kama kungeweza kujengwa njia ya chini kwa chini mpaka mahali pale aliposema. Hivyo siku moja nilimtania na kumwambia kuwa alikuwa ni mwongo, ilikuwa haiwezekani kuwa na njia ya namna hiyo. Kwa vile alikuwa hataki kuniacha hata mara moja alinipeleka pale mahali na kunithibitishia kwa hivi ninapafahamu. Pamefunikwa na mfuniko kama ule unaofunika mashimo ya vyoo, lakini unaingia sawa sawa pale kwenye shimo la mlango na kufungwa kwa funguo," Tete alijibu.

"Kwa hiyo na mimi utanionyesha hapo mahali?" Willy aliuliza.

"Bila wasiwasi", Tete alijibu.

"Endelea na maelezo yako", Willy alimwambia.

"Sasa tukiacha hayo mambo ya zamani, nataka kukueleza kuwa wao wameishagundua kuwa wewe si willy Chitalu bali Willy Gamba mpelelezi hatari sana," Tete alieleza.

"Wamejuaje?" Willy aliuliza.

"Zilikuja habari kwa telex, kutoka kwa hao wateja wao leo asubuhi zilizokuwa zinakuelezea wewe. Nilizipokea mimi lakini kama kawaida huwa zinafumbwa fumbwa zikiwa zinazungumzia mambo ya spea. lakini nilieleza kwa sababu niliona majina yako yote kwenye hiyo Telex. Nilipompelekea karatasi hiyo Max, alinieleza ya kwamba wewe ulikuwa mtu hatari sana katika mambo ya biashara na akanishukuru sana kwa kuweza kukufahamisha kwake", Tete alijibu.

"Ahaa," aliitikia Willy.

"Kisa hasa kilichonifanya nikate shauri kukuona na kuzungumza na wewe kinatokana na maneno aliyonieleza alipokuja leo asubuhi nyumbani kwangu. Muteba huwa haji kwangu wakati wa saa kama zile ila anapokuwa anakerwa na kitu.

Alikuja akionekana amechoka kabisa na akiwa amepoteza hata rangi ya sura yake. Aliniambia kuwa umemuua Kabeya na Charles na kwamba ulikuwa umelipua magereji yao yote isipokuwa gereji la Pierre. Alikulaani vikali sana na akaniapia kwamba lazima atakuua. Alinieleza pia kuwa Mwadi aliuawa na Kabeya sababu za kuficha siri zako na akanionya kuwa kama mimi ninajua kitu chochote juu yako ni afadhali niseme, maana kweli toka tufahamiane na Muteba sijamwona katika hali ile, na niliogopa hata kumuuliza swali lolote. Alilala kwa muda wa saa moja tu akaamka na kuondoka na kuaniambia tuonane naye mchana.

Maelezo haya yalinifanya nifikiri vitu viwili, cha kwanza wewe si mfanyabiashara kama ulivyosema, na pili kuwa Muteba naye alikuwa si mfanyabiashara tu kama alivyokuwa anafahamika ila alikuwa amejiingiza katika jambo fulani la kijambazi na wale wazungu na ndiyo sababu alikuwa katika hali aliyokuwamo. Tokea asubuhi nilikuwa nafikiria niwe upande upi, na baada ya kufikiria sana nikaona ikiwa Mwadi alikuwa anakufichia siri yako na kujitolea kufa basi wewe hukuwa mtu mbaya, Maana Mwadi ninamfahamu sana alikuwa msichana aliyejisitahi sana na hakuwa na uhusiano na watu hovyo hovyo. Hata mimi aliwahi kunionya juu ya urafiki wangu na Muteba, kwani alisema Muteba hakuwa anatembea na kundi zuri. Hivyo nikaona nikuone ili niweze kuwa na msimamo," Tete alimalizia na kuvuta pumzi ndefu.

"Sasa umepata msimamo?"Willy alimuuliza.

"Ndiyo, nina msimamo kamili tokea sasa mimi niko upande wako. Nitaanzia pale marehemu rafiki yangu alipoachia", alijibu Tete huku machozi yanamtoka.

Willy aliyekuwa amekaa karibu naye alimsogelea akatoa kitambaa akaanza kumfuta machozi. Tete alipitisha mikono yake mabegani kwa Willy na wakaanza kupeana busu moto moto, "Kazi na dawa", Willy alibwabwata.

ITAENDELEA
Haahaaa Willy kwa totoz
 
Mkuu kama hutaimaliza hapa useme kabisaa .

Kwa wanao hitaji kitabu cha
1 kikomo.

2; Njama

3; Umsolopagaus.

4; mashimo ya mfalme suleiman.
Anitafute.
Kaka salama?!! Nahitaji kitabu change machimbo ya mfalme Suleiman.. Nakupataje?! Asante
 
Anayetaka kitabu cha hofu cha msiba na kufa na kupona tubadilishane na chochote alicho nacho nichek DM ila kwa dar tu
 
Walikuwapo pia kina Hammie Rajab na vitabu vyake kama Sanda ya jambazi na Kamlete akibisha mripue.Kulikuwa na Simbamwene na vitabu vyake mauaji lodging,muuaji ni nani?,Pesa zako zinanuka.Huyu ndiye mwandishi aliyetunga riwaya nyingi sana hapa Tanzania.Hata baba yake Banana,Zahir Ali Zorro naye aliandika riwaya mbili kali Unyama wa mafia part 1&2 na Kabwe makanika.Enzi hizo kuna watu mitaani walijiita Willy Gamba,Inspector Forg,Kachelo Haji,Joram Kiango,Suresh Kanji,Elungata,Baruni mwasi,Mzee Ole nk.Yaani ilikuwa raha sana.
Dah nimekumbuka mbali sana nilikua darasa la tatu kuna inspector wingo Mwana mtama inspector ojiti ojoko wa Kenya na ageshi mwamba kama jambazi sugu
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom