Riwaya: Hekaheka za Komando Zedi Wimba na Jasusi Honda huko Somalia

Kudo

JF-Expert Member
Nov 2, 2017
1,809
6,081
RIWAYA: URITHI WA GAIDI.

NA; BAHATI MWAMBA.

SIMU: 0758573660

Vitabu vilivyopita.

• Kikosi cha pili
• Dakika za mwisho
• Mpango wa Congo
• Mbwa wa geti
• Operesheni jicho la paka
• Sauti ya mtutu



1:HISABATI


Jua lilikuwa linaelekea magharibi na kuelekea kuzamia kabisa ili kutowesha nuru ilioanza kufifia kabisa na kuliacha anga likiwa jeusi na kiza juu yake.

Ilipata saa kumi na mbili kasoro dakika kadhaa!!

Ilikuwa ni furaha kwa watu kadhaa kuukaribisha usiku huku wengi wakiwa njiani kurejea makwao kujumuika na familia zao baada ya kutoka kuhangaika kutwa nzima. Wengine pia walifurahi kwa kuwa muda huu wa usiku kwao ndio ulikuwa muda sahihi kuingia mtaani na kutafuta riziki yao hasa wezi na vibaka lakini pia makahaba.
Furaha ya giza ilikuwa ni njema zaidi kwa watu wenye baa na kumbi za miziki mana kwao giza ndio riziki yao ya halali bila wizi kwa mtu.


Jioni hii haikuwa njema sana kwa mwanadada mrembo aliepata kuwa na miaka thelathini na mbili hadi na nne hivi. Alikuwa ni mdada mwenye familia ya mume na mtoto mmoja aliepata kuwa na miaka kama mitano hadi sita hivi. Lakini pia alikuwa na mume na maisha yao hayakuwa na tabu yoyote. Familia ilijaa upendo na amani lakini pia kipato kwao hakikuwa na utata.

Milo mitatu kamili ilikuwa ni kawaida kwao.

Hakika ilipendeza!!

Lakini hayo yote sasa yalikuwa yametoweka kwa miaka miwili.
Hakuwa na furaha kama ile aliokuwa nayo mwanzo wakati anaingia kwenye mahusiano na mume wake.

Kwanini!

Kwa sababu alikuwa anaishi yeye peke yake na mwanae zaidi ya miaka miwili na miezi kadhaa huku mume wake akiwa ameondoka kwenda kwenye kazi maalumu Nchi za mbali.

Kazi gani, Hakuzijua na hakupaswa kujua.

Ilikuwa ni ahadi ya kurejea kwa miezi sita tu ila sasa ilikuwa ni miaka miwili bila mume wake kurejea na kila aliemuliza hakuwa na jibu la kumpa akaridhika.

Amekufa?

Hata!!

Haiwezi kuwa rahisi hivyo.

Alijakatalia.


Jioni hii ilimkuta mwanadada huyu mwenye urefu na uzuri wa asili akiwa ndani ya gari akitoka Mwenge kurejea nyumbani kwake Kinondoni akitokea ofisini kwake. Ofisi alioianzisha miaka kadhaa nyuma ikiwa inajishugulisha na utafiti wa mambo ya kale.

Yeye alisomea fani hiyo katika chuo kikuu cha Dar es laam.

Alikuwa ni Archeologist.

Mawazo mengi yalikizonga kichwa chake hasa suala la mume wake kutokuwa na mawasiliano nae zaidi ya miaka miwili na ushee.

Je upendo umeisha! Au huko alikoenda kakutana na mabinti wazuri kumliko basi akaamua kulowea kabisa huko?

Haiwezi kuwa!!

Alijikatalia tena.

Mawazo yake yalizidi kumuumiza kichwa chake na kupelekea jasho jepesi limtoke licha ya gari lake kujitahidi kumpa kiyoyozi bila upendeleo.

Foleni nayo ilizidi kumchosha.

Licha ya kuchoka na foleni lakini kwake aliona ni heri zaidi kuliko kurejea nyumbani na kukutana na nyumba tupu isio kuwa na uchangamfu wowote mana ilikuwa ni yake peke yake kwa sababu mume hakuwepo na mwanae wa kiume alikuwa anasoma shule za kulala huko huko hivyo kwake alikuwa ni yeye kama yeye tu.

Karaha ilioje!!.

Alisonya huku fukuto la jaziba na wivu vikimsonga hasa alipofikiria namna mume wake huko aliko anavyowabambia wanawake wa kizungu au kiafrika huku lugha yao ikiwa ni kizungu ama kihindi ama kiarabu ambazo zote mume wake alizimudu vyema kabisa.

Akasonya tena.

***

Ilikuwa ni majira ya saa mbili usiku ndipo alipoingia nyumbani kwake Kinondoni B.O.B ni baada ya kuwa amepita kwa Bonita saloon kuweka Sawa nywele zake ambazo hakuwa amezijali kwa siku kadhaa hivi.

Alipita kuzifunga tu na kuelekea nyumbani kwake.

Alishuka ndani ya gari na kufungua geti kisha akarudi na kuingiza gari ndani ya uzio wa nyumba yake ya kifahali ambayo sasa aliiona kama jehanamu ya nafsi yake.

Ilikuwa ni bora kukaa nje kuliko kurudi nyumbani kwenye nyumba pweke namna ile.

Akachukua makabrasha yake ya kiofisi na kupiga hatua kadhaa kuingia ndani kwake.

Akawasha taa na kujitupa kwenye sofa huku macho yake yakitua ukutani na kujenga kibanda.

Alibaki akiikodolea picha ya mume wake iliokuwa imetundikwa ukutani pale. Mume wake alikuwa ndani ya vazi la kiofisi huku mabegani mwake akiwa amejaa beji tatu zilizotambulisha cheo chake.

Mume wake alikuwa ni ofisa mkubwa wa jeshi la polisi.

Yeye hakuwa anakodolea vyeo vile bali alikuwa anatazama tabasamu adhimu la mume wake pale kwenye picha. Tabasamu ambalo ni nadra kuliona kwenye uso wa mumewe.
Alitazama kidevu cha mumewe kilichokuwa kimejaa ndevu zilizochongwa kwa mtindo wa Timberland.

Hakika alimkumbuka mumewe.

Pembeni ya picha ile pia kulikuwa kuna picha ya mwanae ambae nae kama baba yake alikuwa na tabasamu safi la kitoto huku akiwa ameegemea kwenye mikono imara ya baba yake.

Mwanadada alifumba macho kwa hisia kali. Kisha akanyanyuka na kuelekea maliwatoni, huko alitumia dakika kadhaa kujiswafi na kurejea sebuleni ambapo napo hakukaa sana akaelekea jikoni ambako hakufanya lililompeleka akabaki akiwa amejishika kiuno tu na kulikodolea jiko lake kama mtumishi aliesusiwa upishi.

Uvivu!!

Uvivu wa kupika chakula chake mwenyewe ndio uliomsumbua.

Hakuona umuhimu wa kupika akaamua kufungua jokofu. Humo ndani akakuta chakula cha kopo akakichukua na kukipasha kisha akarudi sebuleni na kukaa kukila huku akishushia na mvinyo mwekundu.

Dakika kadhaa badae uchovu na msongo wa mawazo vikampelekea aelekee chumbani kwake kulala huku akisahau kufunga milango.

Akalala fofofo!.

Ilikuwa yapata usiku wa saa saba kwenda saa nane hivi, mwanamke yule alipata kuhisi kitu ndani ya nyumba yake. Mwanzo alitaka kupuuzia kile alichokihisi akiwa katikati ya usingizi mnene,lakini hisia za kutambua zilizidi kumsumbua.

Akafumbua macho kisha akatulia na kusikilizia kile kilichofanya aamke.
Masikio yake yalinasa mchakacho wa miguu ya kiumbe hai ndani ya nyumba yake.
Haraka nae akaingiza mkono chini ya mto na kuibuka na bastola na kwa kuwa alikuwa amelala na nguo,hivyo hakupata tabu kuinuka na kunyata kuelekea sebuleni.

Hakusikia kitu tena.

Akafumba macho na kutuliza hisia zake.

Bado hakusikia kitu.

Akanyata hadi mlangoni kisha akachungulia sebuleni.

Ajabu!!

Alibutwaika kwa sekunde kadhaa hivi hasa baada ya kugundua aliacha taa zikiwaka kote mle ndani na sasa zinawaka chumbani pekee huku sebuleni kukiwa giza.

Akagwaya!

Mwili ukamsisimka na hofu ikamjaa!.

Mwanamke akatetereka.

Kutoka pale alipokuwa aliendelea kusubiri zaidi ili kumhadaa aliezima taa sebuleni lakini akajishitukia baada ya kukumbuka kuwa pale chumbani kulikuwa kuna mwanga na sebuleni kiza hivyo yeyote ambae angelikuwa amelikaa sebuleni basi alikuwa akimuona yeye ama kivuli chake.

Hata!!

Haraka na kwa wepesi akanesa kwa kutumia ncha za vidole vya miguu na kufikia kiongoza taa na kuzima taa ya chumbani. Wakati akirudi mlangoni, alisikia mlango wa sebuleni ukibamizwa kwa nguvu kumaanisha kuna mtu katoka muda huo.
Kwa wepesi uliokusudiwa, mwanadada yule nae akapiga hatua ndefu na kufika sebuleni kisha kwa kasi ile ile akaufikia mlango wa sebuleni na kuufungua.

Hola!!

Hakuona mtu wala kivuli cha mtu na geti lilikuwa vilevile limefungwa kumanisha hakuna mtu aliepita muda mfupi uliopita.
Mwanadada yule akaona ajaribu kuzunguka nyumba nzima pengine atafanikiwa kuona mtu aliekuwa sebuleni ila alizunguka bila kuona lau dalili ya mtu.
Alibaki akiwa anatazama mlango wa kuingilia ndani na geti kubwa la kuingilia pale ndani.

Akamakinika na kitu na kumbukumbu zilimrejea vyema.

Akasonya kwa gadhabu!!

Hakuwa amemkumbuka askari anaelinda usiku nyumbani kwa kiongozi wake na pia alikumbuka wakati anaingia hakumuona wala kuhisi uwepo wake.

Hatari kabisa!

“Yani najiwaza hadi nasahau mlinzi” alijisemea huku akipiga hatua kwa makini kuelekea kwenye kibanda cha mlinzi.

“Afande! Afande!” aliita mara mbili na aliitikiwa na sauti yake mwenyewe iliokuwa inajirudia kutokana na utulivu wa kifo uliokuwa nyumbani pale. Akazidi kuukaribia mlango wa kibanda cha mlinzi na alipokifikia akatulia na kusikiliza endapo kungekuwa na harakati zozote ndani ya kibanda.

Kimya!!

Hakuna alichokisikia zaidi ya pumzi zake mwenyewe.
Akausukuma taratibu mlango wa kibanda kile kisha akaingia kwa fujo kidogo.

Hakuna alichokikuta!!

Hakukuwa na mlinzi wala dalili za kuwapo mlinzi ndani ya eneo lile na hiyo ilimaaisha kuwa mlinzi hakuwa amefika pale siku hiyo.

Kwanini!!

Hilo hakujua na wala hakutaka kuamini kama limewekwa makusudi ama vipi.

Lakini alibaki na swali moja kichwani ya kuwa inawezekana vipi nyumba ya ofisa mkubwa jeshini tena special operation asahaulike kuletewa mlinzi.

Hata!! Ni ngumu hilo kufanyika. Lakini sasa mlinzi yuko wapi ikiwa haonekani pale ndani?

Mwanadada alipagawa.

Haraka alirudi ndani na moja kwa moja alielekea mezani kulikokuwa na rununu yake ya mkononi na kulitafuta jina la mtu aliemhitaji na kupiga.

“Ndio nakusikiliza!!” iliunguruma sauti ya mtu aliepokea simu upande wa pili ambae alionekana kutoka usingizini.

“Afande leo mlinzi aliandikishwa kufika hapa kwangu?” aliuliza mwanadada.

Ukimya ukapita kidogo.

“Kuna mambo yamebadilika kidogo na mimi sipo ofisini tangu juzi hivyo sijui kama kuna mtu aliekuwa amepangiwa hapo kwenu!!” alijibu mtu yule baada ya kukaa kimya kwa sekunde kadhaa.

Mwanadada akavuta pumzi za kushindwa kuelewa kinachoendelea.

“Kwani kuna tatizo?” alihoji mtu yule baada ya kusikia ukimya ukiwa umetawala kwenye simu.

“Kesho nitakutafuta tuzungumze Afande!” alisema mwanadada.

“Ni ngumu kesho kunipata mana nasafiri kwenda Ufaransa kwenye kikao cha wakuu wa idara za usalama wa jumuia ya madola nikimuwakilisha Mkuu wa jeshi la polisi nchini” alifafanua yule mtu.

“lakini nahisi kuna tatizo, kwanini mlinzi hajafika hapa nyumbani leo!?” aliuliza yule mwanadada .

Mtu wa upande wa pili akavuta pumzi nyingi na kuzishusha kisha akasema.

“siwezi jua pengine nikupe namba za mtu anaeshugulikia hayo kwa sasa na ambae amekaimu nafasi yangu hadi nikirejea” alisema yule bwana huku akianza kuzitaja namba hizo na alipomaliza alikata simu bila kungoja maelezo zaidi.

Suala lile likamchanganya kidogo mwanadada yule na kumuacha na maswali mengi bila majibu. Ilikuwa ni tabia mpya kuoneshwa na mtu yule tangu amfahamu na pia alikuwa ni rafiki wa karibu wa familia yake licha ya mtu yule kuwa ni kiongozi wa mumewe kikazi.

Akaguna tu na kuendelea kujishugulisha kuipiga namba aliopewa dakika chache zilizopita.

Simu ilianza kuita kwa fujo na punde ikapokelewa.

“Remi Haji; nakusikiliza”

Ebanaee! Maajabu.

Remi alitamani kukata simu dakika hiyo na kutafakari upya alilosikia. Mtu yule aliekaimu alikuwa anamjua jina lake kwa ufasaha kabisa!

Alimjuaje sasa na kwanini amjue ikiwa yeye si mfanyakazi wa idara yoyote ya jeshi la polisi?

Hakika ni maswali yaliomuacha kinywa wazi na alijikuta akikosa la kusema kwa dakika moja nzima.

“Heloo Remi!!” mtu yule aliita kwa madaha jina la Remi baada ya kuona ukimya umetawala.

“aah nimepewa namba na Kamishina wa jeshi la polisi Zenge wa Zenge.” Aliongea kwa kirefu Remi.

“elekea kwenye suala lililokufanya upige simu tafadhali ninahitaji kupumzika!” mtu yule aliekaimu nafasi ya Zenge wa Zenge alisema kwa utulivu wa majivuno.

“Hapa kwangu hadi sasa sijaona mlinzi akifika wala kuripoti nilitaka kujua nini tatizo tafadhali” aliuliza Remi.

“Kabla ya kunipigia mimi usiku huu ulipaswa kuwapigia maafisa wanaoshugulika na malindo ya wakuu wao, mimi ni mtu mkubwa sana kuulizwa malindo usiku wa manani namna hii” aling’aka bwana yule.

“Nina sababu afande za kukutafuta wewe na…” alikatishwa kusema Remi.

“Hiyo sababu ilikuwa zamani ila sio sasa. Kwa sasa utaratibu unafuatwa kuanzia ngazi za chini binti” alisema yule bwana kwa ujivuni.

Remi alibaki akiwa amezubaa kwa fadhaa na simu sikioni.

Hakupata kuona mambo haya hapo kabla.

“Naomba kesho ufike ofisini kwangu nina ujumbe” alisema bwana yule na kukata simu.

Remi alibaki akiwa hana hamu na majibu ya ujivuni ya kamishina yule wa jeshi la polisi nchini.

Akaitoa simu sikioni na kulitafuta tena jina la Zenge wa Zenge ili apige lakini alikutana na jibu lililozidi kumuacha wazi kichwani.

Hakuwa akipatikana!

Haijawahi kutokea akazima simu tangu wafahamiane miaka kadhaa nyuma wakati akiwa katika misukosuko ya Ukimbizi ndani ya nchi ya Tanzania kisa ambacho kiliandikwa vyema na mwandishi wa riwaya Bwana Bahati Mwamba.

Sasa baada ya muda wote huo eti Kamishina anazima simu.

Kuna namna si bure.

****

Remi Haji Makame; usingizi ulimpaa na hapo akakumbuka kitu baada ya kushindwa kumtafakari vvyema Zenge wa Zenge.

Ujumbe!!

Alikumbuka mchana aliona ujumbe kutoka kwa mwandishi ambae pia aligeuka kuwa rafiki wa familia hasa baada ya kuwa anaandika mikasa mingi inayomhusu mume wake. Aliupokea ujumbe wa Davis Minja ila hakushugulika nao wakati ule.

Aliufungua!

“Siku ya sita sasa kuna gari silielewi nyuma yangu mumeo sikumpata!” ujumbe ulisomeka hivyo.

Sasa hii tena inakuwaje! Alijiuliza Remi na uso wake ulielekea juu ya ukutani na kuitazama saa.
Mishale iliendelea kuwa mashariki kumaanisha ni usiku wa maanani.
Alizima taa na kuacha usiku upite akiwa amekaa sebuleni kuongojea kuona kama mtu aliemtembelea usiku ule atarejea ili amjibu kwa nini alimtembelea kinyamela na alifuata nini.

Lakini kitu kimoja hakujua ni kuwa hesabu zake zilikuwa nyuma ya hesabu za mtu aliemvizia usiku na kumwacha bila kumduhuru.

Mtu yule hakurejea tena hadi mapambazuko.

Na yakawa ni mapambazuko ya Kihisabati; hesabu za akili.

****

Ahsubuhi ilimkuta Remi akiwa amelala kwenye sofa na bastola yake mkononi. Milio ya ndege waliokuwa juu ya miti ndio waliomsitua kutoka kwenye tope la usingizi wa mang’amung’amu.

Alijisonya bila sababu na kuelekea chumbani kwake ambapo moja kwa moja alielekea maliwatoni na kutumia dakika kumi na ushee kujiswafi kisha akarejea chumbani kwake ambapo hakumaliza muda murefu akawa tayari amekwisha kujiweka sawa na kuvaa suruali ya buluu mpauko na T-shirt nyeusi kisha akachukua mkoba wake wenye nyaraka za kiofisi na kuweka bastola yake kisha akaelekea sebuleni ambako alichukua funguo za gari na kutoka nje ambako alichukua gari lake jeusi aina ya Toyota Nadia na kisha akajifungulia geti na kutoka nje na alipokwisha kutoka akarudi tena kwa miguu na kulifunga kisha akaondoka kwa mwendo wa wastani tu.

Hakufika mbali kwa kupitia vioo vya gari ama side mirror akaona jambo.

Kutoka kwenye kona moja ya nyumba yake aliona mtu alievaa kofia akichepuka na kuivuka barabara kwa kasi na kupotelea kwenye nyumba za watu mtaani pale.

Akili yake ilimwambia mtu yule hakupita eneo lile kwa bahati mbaya au labda ni mkazi wa eneo lile.
Hakika akili yake ilikataa kukubaliana na hilo.

Alikuwa pale anafanya nini na kwanini akimbie kwa kujificha namna ile? Au ndie aliemtembelea usiku na…
Alibaki kutikisa kichwa tu bila kujua kama kuna kusudi baya juu yake ama ni akili yake tu.

Kamwe hakujua mana ya matukio yote yale yalioanza kumwandama siku kadhaa nyuma.

Aliendesha gari lake huku kila mara akitizama nyuma kuona kama kuna jambo lolote lisilo la kawaida.

Hakuona!!

Safari yake ilimfikisha hadi makao makuu ya jeshi la polisi na alipokwisha kufika akapaki gari lake eneo maalumu kisha akaomba kuonana Naibu kamishina. Alioneshwa zilipo ofisi zake.

Hatua zake zilimfikisha hadi kwenye korido pana iliokuwa na ofisi nyingi kushoto na kulia. Akasoma namba za ofisi zile na vitengo vyake hadi pale macho yake yaliponasa jina la ofisi alioihitaji. Ilikuwa ni ofisi ya kitengo maalumu yani special operesheni.
Akagonga mlangoni na kukaribishwa kuingia.

Alikaribishwa na uturi ghali ulionyanyasa pua zake kwa harufu kali. Lakini macho yake hayakuhadaika na na harufu za pua bali yalimakinika kumtazama mtu aliekuwa amekaa kwenye kiti nyuma ya meza na kibao kikiwa mbele yake kilichonasibisha jina lake.

Bwana yule aliitwa P. Kagoshima ambae ndie alikuwa Naibu kamishina wa jeshi la polisi kazi maalumu aliekaimu nafasi ya Kamishina Zenge wa Zenge. Bwana yule hakuonekana kuwa na umri wa kutisha ila umri wake aliukadiria kuwa kati ya miaka arobaini na nne hadi hamsini kasoro. Alikuwa ni mrefu wa wastani ila hakufikia urefu wa Mumewe ama Kamishina Zenge wa Zenge. Sura yake ilionesha ni mtu mjivuni sana lakini mbali na hayo Remi aliona kitu ndani ya macho ya yule bwana. Remi aliona tamaa ya kifisi imejaa kwenye mboni za macho ya Kagoshima ila hakujua ni tamaa ya nini, Pesa ama kitu kingine zaidi ila ilitosha tu kujua yule bwana ni mwenye ujivuni na tamaa.

“Naitwa Remi” alijitambulisha Remi.

“Ooh karibu bibie!” alisema Naibu kamishina Kagoshima huku akiachia tabasamu la upande na kuegemea kiti kilichopokea mwili wake wa kikakamavu.

“Nimeitikia wito Afande!!” alisema Remi huku akitizama saa yake ili kuhakikisha yupo ndani ya muda na sikuchelewa pale ofisini.

“OK! Bila shaka mumeo ni ofisa wa jeshi la polisi!” alihoji Kagoshima huku akijishugulisha kupekua makablasha kadhaa yaliokuwa mezani kwake.

Remi hakumjibu.

Kagoshima aliendelea..

“Na ndie Haji Makame!”

“Afande nadhani yote hayo unayajua na unapaswa kujikita kwenye mada tafadhali” alisema Remi kwa kukereka kidogo.

N. Kamishina alitabasamu kivivu huku akichukua kipande cha gazeti na kukitupia karibu na mikono ya Remi ambae alikuwa amekaa na kuweka mikono yake juu ya meza.

Remi alikichukua kipande kile ambacho kilikuwa ni cha ukurasa wa mbele wa gazeti la Daily News la Marekani. Remi alishuhudia picha mbili kubwa na picha moja ndogo. Picha ndogo ilikuwa ni ya mtu mgeni machoni pake na picha moja kubwa nayo hakuifahamu kabisa lakini picha nyingine ilikuwa ni picha ya mumewe Haji Makame licha ya kuwa na mabadiliko makubwa katika uso wake,lakini kamwe hakuwahi kumsahau mwanaume wa maisha yake.

Akasoma kichwa cha habari cha kipande kile cha gazeti ambacho kilikuwa kimeandikwa kingereza.

Mwili ukamwingia ubaridi kwa alichokielewa. Alimtizama Kagoshima; na alikutana na uso makini ukimtizama kisha akarejesha macho yake kwenye kipande kile.

Tafsiri Kiswahili.

“Tanzania yazidi kuzalisha magaidi, Wawili wasakwa na marekani na mmoja atoweka Guantanamo”

Yalikuwa ni maelezo machache lakini yenye kuchoma akili za watu.

“Sijaelewa Afande!” alisema Remi huku dhahiri akionekana kupagawa.
Naibu Kamishina P. Kagoshima alisogeza kiti huku akiguna kusafisha koo lake na mkono wake wa kushoto akikichukua kipande kile cha gazeti kutoka mikononi mwa Remi.

“Huyu anaitwa Ahmed Twalibu” alisema huku akinyooshea picha ndogo ya jamaa mweusi alieonekana kukomaa sura yake licha ya uso wake kuonesha umaridadi wake vyema.

“Na huyu anaitwa Aahmed Boka Ghailani” alionyeshea picha kubwa ya mwanaume ambae nae hakutofautiana sana na yule aliekuwa kwenye picha ndogo licha ya kuwa walionekana kuwa ni wanaume wawili tofauti.

“Na huyu ni Haji Makame” alisema tena huku akielekeza kidole kwenye picha ya mwanaume aliekuwa amenyoa upara na kuchonga ndevu zake kwa mtindo wa Timberland. Licha ya kunyoa ambayo si tabia alioizoea Remi; lakini ndevu zilimhakikishia yule ni mumewe kipenzi Haji Makame.

Gaidi!!

Ameanza lini ugaidi hadi kutafutwa na serikali ya Marekani!? Na kwanini ahusishwe na Ahmed Twalibu ambae siku za nyuma aliaminika ameuwawa kwenye shambulizi lililotekelezwa na Wataleban walishambulia chopa aliokuwamo?

Na vipi alipona na kuhusishwa tena na ugaidi sambamba na mumewe!?

Ebanae!!

Yalikuwa ni maswali bila majibu na hesabu ziligoma kuunganisha kachumbari ile kichwani mwa Remi ambae siku zote alijua mumewe ni mstari wa mbele kupigania masilahi ya taifa kwa kupambana na ugaidi ama uvunjaji wa sheria wa aina yoyote!

Hata haiwezekani.
Remi alijakatalia kata kata.

“eeh! Hapa kuna watu wawili wanafanana majina kwa kutamkwa ila herufi tofauti yani Ahmed na Aahmed .” Alisema tena Kagoshima huku akitoa picha nyingine kubwa kidogo ambayo nayo aliitupia kwenye meza na kuchukuliwa na Remi.

Picha ile ilifanana sawa sawa na picha ndogo ya mtu alieitwa Ahmed Twalibu aliesemekana kutoroka Guantanamo na sasa anatafutwa na serikali ya Marekani.

Remi alimtizama Kagoshima kwa macho ya kuuliza.

“Ok. Huyo bwana anaedaiwa kuitwa Ahmed Reality ambae unaona picha yake hapo,tumefuatilia na kugundua sio Ahmed Reality ila ni amewahi kuwa askari wa jeshi la polisi kitengo maalumu kama mumeo anaitwa Honda Makubi. Swali tunalojiuliza ni kwanini Marekani iseme ilikuwa nae gerezani kwake na ametoroka wakati miaka miwili nyuma alikuwa anahudumu hapa nchini? Lakini pia Ahmed wa kweli anaweza kuwa miongoni mwa hawa watatu yani huyu Aahmed Ghailani; Haji Makame ama Honda Makubi na hapa anaetafutwa sana ni Ahmed Twalibu ambae nasadiki ndie huyu Aahmed” alisema Naibu kamishina Kagoshima.

Remi alibaki akimtizama akiwa hajui ni kwanini anahusishwa katika jambo lile tena kwa kuelezwa kwa marefu na mapana na kiongozi mkubwa wa jeshi la polisi nchini.

“Kwanini unanambia yote haya na mimi nahusikaje na hili sakata!” alivunja ukimya Remi.

Kagoshima aliegemea kiti chake kisha akamtazama Remi kwa tuo huku akiwa amefumbata mikono yake pamoja.

“una hakika huhusiki?” aliuliza Kagoshima.

Jama!!

Remi alibutwaika kwa kauli ile ya ofisa yule wa jeshi la polisi.

“Nahusika vipi na mambo haya ambayo ni kama hadithi za kufikirika?” alihoji Remi.

“Inaonesha mumeo anashirikiana na magaidi muda mrefu kidogo na wewe yaezekana unajua hiko kitu na ndio mana unahusika katika sakata hili mwanamke!” alisema Kagoshima huku akilambalamba midomo yake kama wafanyavyo wasanii njaa wahojiwapo na vituo vya runinga.

“Huko ni kumkosea mume wangu kabisa na kamwe hajawahi kuwa gaidi. Yani mazuri yote alioyafanya leo mnamwita gaidi?” alisema Remi huku akivuruga nywele zake kichwani kwa mikono yake.
Alihisi kichwa kinawasha kwa taarifa zile.

“Kwanza nataka nikwambie mumeo hajawahi kuwa ofisa wa jeshi la polisi na hata katika rekodi zetu hayumo,hivyo inamaanisha hajawahi kuwa ofisa kabisa na hatumtambui Haji Makame na cheo chake na tunamhesabu kama mhujumu nchi tu aliejichomeka jeshini kutimiza matakwa yake ya kigaidi” Jibu la moto kwa Remi Makame.

“Hajawahi!? Inamaana, dah..” alishindwa kuelewa aseme nini katika dakika ile Remi. Alibaki akiwa ameachama mdomo akiwa hajui ama alie ama acheke ama tabasamu, mana hakuona kama kuna utani katika uso wa Kagoshima ambae ni ofisa mkubwa tu wa jeshi la polisi.

Sasa alielewa ni kwanini hakukuta mlinzi usiku wa jana nyumbani kwake.

“Mengine inabidi utuachie kama serikali tuyashugulikie ila kwa sasa taarifa hii inaweza kukuweka pabaya ama pazuri mrembo” alisema Kagoshima huku akikenua meno kama ngiri maji.

Haaa!!
Urembo tena unaingiaje katika sakata hili!

Remi alisimama kisha akauliza.

“kwanini inaweza niweka pabaya ama pazuri?”

“ukimficha mumeo na washirika wake itakuweka pabaya ila ukitoa taarifa utakuwa pazuri” alisema Kagoshima huku akitoa kadi mfukoni mwake na kumpa Remi.

“Ukiwa na shida utanipigia nami nitakusaidia muda wowote” alisema huku akiona Remi anaitazama ile kadi.

“sina hakika kama itafikia hatua ya kukuomba msaada” alisema Remi huku akiisunda kadi ile mkobani mwake.

“unahakika hutauhitaji msaada wangu?” alihoji Naibu Kamishina huku akitabasamu. Remi alimtizama bila kumjibu na kuondoka ofisini mule huku kichwa kikimuwaka moto kwa taarifa zile.

Hakika alichanganyikiwa.

Dakika kadhaa badae alikuwa ndani ya gari lake na lengo lilikuwa ni kuelekea Mwenge zilipo ofisi zake za utafiti wa mambo ya kale.

Tatizo hakujua huko nako ni moto mwingine utakao acha akili yake ikiwaka. Ila hakujua na angejua hakika angejirudia kwake tu akalale.

***

Nb; toa maoni yako kuhusu riwaya hii. Usiache kutupia maoni yako ambayo ni muhimu
 
RIWAYA; URITHI WA GAIDI

NA; BAHATI MWAMBA

SIMU; 0758573660


SEHEMU YA PILI.


Tatizo hakujua huko nako ni moto mwingine utakao acha akili yake ikiwaka. Ila hakujua na angejua hakika angejirudia kwake tu akalale.

***

Wakati Remi akiingia kwenye lango la ofisi yake alikutana na hekaheka ambazo hakujua chanzo ni nini. Ofisi zake zilikuwa ni kwenye nyumba ya kawaida tu ambayo ilijengwa maalumu kwa kazi za kiofisi na pembeni yake kulikuwa kuna gorofa kubwa lenye ofisi nyingine pia. Kampuni yake iliitwa REMI ARCH COMPANY LIMITED. Ilishugulika na utafiti wa mambo ya kale fani ambayo aliipenda sana.
Hekaheka zile zilianzia nje ambako kulikuwa kuna askari wa jeshi la polisi wenye silaha za moto ambao walipumuona wala hawakujali,waliendelea kuweka usalama eneo lile lakini pia alipoingia ndani alikuta wafanyakazi wake wote walikuwa wamekusanywa na kuwekwa pamoja huku kukiwa na maafisa kadhaa wa jeshi la polisi na wale wa ukusanyaji mapato yani TRA.
Alishindwa kuelewa kuna nini pale ofisini kwake licha ya kuona heka heka zile. Wafanyakazi wake nao walipomuona wakaelekeza macho yao kwake huku kila jicho likisadifu yalio myoyoni mwao.

Remi alielekea moja kwa moja kwa askari mmoja aliekuwa na cheo cha sajini na alionekana ndie kiongozi wa kundi na heka heka zile.

“Afande shida nini hapa!?” aliuliza kwa kihoro Remi.

Afande yule alimtizama kuanzia juu hadi chini kisha nae akauliza bila kutoa jibu.

“wewe ndie mkurugenzi hapa?”

“Ndio. Nieleze shida tafadhali!!” alisema Remi.

“Tusogee pembeni kidogo” alisema Sajini yule huku akimshika mkono Remi na kusogea nae pembeni.

“Kuna mambo mawili yanaendelea hapa. Mosi; inasemekana hujalipa kodi yako ofisi ya mapato kwa miaka kadhaa ila hilo silo lililotuweka hapa sisi maofisa wa polisi. Lilituweka hapa ni kuwa tulipigiwa simu ahsubuhi kabisa kwamba kumetokea mvurugano hapa ofisini kwako na kupelekea mwandishi wa riwaya Tanzania bwana Davis Minja kuchukuliwa na watu wasio fahamika na kuua mlinzi wako” alieleza Sajini aliejitambulisha kwa jina la Vengu.

E bana ee!!

Remi alihisi moyo unataka kuchomoka kwa kasi ya mdundo wa mapigo yake. Alitamani aangue kilio ili akinyamaza mauzauza yale yakatike ila haikuwezekana.

Nini sababu ya yote haya?

Mume gaidi na sasa anaambiwa mtu katekwa ofisini na mauaji kutendeka ofisini kwake na bado anadaiwa kodi na mawakala wa ukusanyaji na ofisi tayari zinapigwa kufuli.

Aah mkosi gani huu tena kwa Remi.

Hakika ni kipindi kigumu kuelezeka. Remi chozi lilimtoka.

“aah inapaswa tukuhoji kidogo dada kisha tukuache umalizane na maofisa wa TRA.” Alisema sajini Vengu.

Remi alipandisha pumzi na kuzishusha kwa mkupuo mara mbili kisha akayarudisha macho yake kwa Sajini.

“Eeh!! Unamahusiano gani na Davis Minja?” aliuliza Sajini.

“Ni rafiki wa familia”

“kwa muda gani”

“Muda mrefu”

“aliwahi kukwambia chochote kuhusu upande wa adui yake?”

“Hapana!!”

“unahisi kwanini ametekwa ofisini kwako?”


“siwezi kujua!”

“unahisi kwanini alikuwa hapa ahsubuhi sana badala ya kuja kwako!”

“sijui!”

“sawa sisi kwa sasa hatuna maswali mengi. Badae tutakuhitaji kituoni Mwinjuma uje kutoa maelezo zaidi lakini kwa sasa tutaendelea na utaratibu wa kipolisi kuukagua mwili wa mlinzi wako” alisema sajini huku akiondoka na kumuacha Remi akiwa amesimama bila kujua ni kipi cha kufanya.

Mambo yanayotokea yanachanganya.

Akiwa bado amesimama pale mara mtu mwingine aliekuwa amevaa suti akamfuata. Bila salamu akasema.

“Ofisi yako inakashifa ya kutokulipa kodi serikalini hivyo tutaziondoa kufuli na kukuacha uendelee na shuguli zako ukisafisha madeni yako”

Remi alimtizama bwana yule ambae hakuonekana kujali kutazamwa kule.

“wiki jana ndio nimetoka kufanya malipo ya makadirio ya kodi sasa inakuwaje nadaiwa?”

“kwa hiyo unataka kusema hapa sisi tumekosea kufika? Unadhani wewe ni mjanja kuliko serikali?” alibwata bwana kitambi yule alieonekana kuwa na mwili wa rushwa.


“Nyaraka zote ninazo sasa sijui nyie mna ofisi ngapi ambazo mnafanyia malipo hadi mshindwe kujua nimekuwa mlipaji tangu nisajili kampuni hii” Remi nae alimaka.

“Mwanamke angalia usije kujibia kituo cha polisi. Wewe ni sawa na mhujumu uchumi hivyo huna haki ya kuhoji lolote kwa sasa zaidi ya kuclear madeni yako na sisi tufungue ofisi zako” bwana kitambi alizungumza kwa majigambo makubwa.

“Nyaraka zipo aisee usinitishe na hili litakugarimu bazazi wewe” Remi nae alifoka,hakutaka kupelekeshwa kama tiara wakati ana uhakika kabisa amekuwa akilipa serikalini tangu aliposajili ofisi yake kuwa kampuni kwa ajili ya utafiti wa kujitegemea wa mambo ya kale.

Bwana kitambi alicheka kwa dhihaka kisha taratibu akasema kama vile asietaka wengine wasikie anachozungumza na Remi.

“Itakugarimu hiyo jeuri yako mwanamke na huna pa kukimbilia safari hii”

Ebana eeh

Huyu bwana anazungumza nini. Safari hii safari nyingine ilikuwa wapi!

Jama yakoje mambo haya?
Alijiuliza Remi huku ile sauti ya bwana kitambi ikijirudia kichwani mwake.

“Sauti hii nimepata kuisikia wapi?” alojiuliza mara nyingi bila kupata jibu na alipokuja kurudisha macho yake pale alipokuwa bwana kitambi hakumuona zaidi aliona wafanyakazi wake wakitoka pale walipokuwa na kuanza kumfuata. Askari polisi na maafisa wa mapato nao walikuwa wameanza kuondoka pale ofisini.

Hakika zilikuwa ni hesabu ambazo kamwe Remi hakujua njia ya kuzikokotoa.

Hisabati ilifanya kazi na hakika aliona anaenda kupata zero yenye masikio makubwa.

*****

Jambo la kwanza aliloona kwake linafaa ni kurudi nyumbani kwake kuzitafuta nyaraka za malipo ya kodi ili aelekee zilipo ofisi za mapato na kujua undani wa suala lile kwa marefu na mapana.
Alifungua geti na kuingiza gari kisha haraka akaelekea ndani ambapo moja kwa moja alielekea kwenye kabati maalumu la kuhifadhia nyaraka muhimu za kiofisi.

Kwa pupa aliokuwa nayo hakujihangaisha hata kudadisi nyumba yake,alipitiliza moja kwa moja kwenye chumba maalumu cha kuhifadhia nyaraka muhimu.

Alipofungua mlango wa chumba kile alishangaa kwa alichokiona.

Vitabu vilikuwa vimesambaratika hovyo, nyaraka zilizokuwa kwenye karatasi zilikuwa zimechanguka hovyo na kabati lilikuwa wazi.

Upekuzi ulifanyika!!

Ni nani sasa anaeweza kuingia ndani na kupekua kiasi hiki!

Alijiuliza bila kupata jibu.

Haraka akarejea sebuleni,na ndipo aliposhuhudia mtafaruku wa ajabu ambao alishindwa kuelewa wakati anaingia ni nini kilisababisha hakuona mambo yale. Kila sehemu ilikuwa imeguswa hovyohovyo na kupelekea baadhi ya mapambo kusambaratika hovyo mule ndani; sofa zilikuwa zimendolewa sehemu yake na kusogezwa pembeni na hata zulia zito lililokuwa chini nalo lilikuwa limebinuliwa. Alipotizama ukutani aliona picha zikiwa zimegeuzwa hovyo kabisa na moja ya picha zake ilikuwa inaamandishi madogo yaliomfanya amakinike. Akasogea taratibu na kwenda kuyasoma.

“it’s showtime!!” aliyarudia mara mbili maandishi yale na taratibu akaona kuna mchezo wa matukio yale na ule ni ujumbe maalumu kwake na hakika alikubali ile ilikuwa ni showtime kwake, lakini swali lilibaki linakizunguka kichwa chake.

Baada ya showtime ni nini kitafuata ama tukio gani? Na nini lengo hasa. Je ni ugaidi wa mumewe ama ni kisasi cha watu juu yake? Watu gani?.

Yalikuwa ni maswali mengi kwa mtu tofauti na Remi ila kwa Remi lilikuwa ni swali moja lenye jibu moja na vipengele vyake.
Remi nae aliandika kwa vidole vyake lile neno showtime kisha akaingiza mkono mfukoni na kuchukua kalamu ndogo ambayo huiweka kwa dharura na kuandika chini ya maandishi yale neno “mathematics; Hisabati” aliandka kwa kingereza kisha kiswahili. Alikuwa na maana ya kwamba wao watacheza mchezo wa kufurahisha na kukarahisha ila yeye atapiga hesabu kujua mbinu za mchezo wao. Remi hakuwa na akili za mtu wa kawaida; Remi aliamua kutulia na kufikiri zaidi, alijionya kuhamaki mana kungemtoa sadaka kwa wacheza mchezo wa utangulizi Showtime.

Akaiacha ile picha pale sebuleni na kurejea kwenye chumba kile cha kuhifadhia nyaraka.

Vilevile alivyokuta kumepekuliwa,nae akaamua kupekua kutafuta nyaraka za kampuni yake.

Kila alichogusa hakikuwa anachokihitaji.

Jama!!

Ziko wapi nyaraka hizo?

Alitafuta kila pahali bila kupata kile alichokitaka. Nyaraka hazikuwepo na hakuziona kabisa. Kumbukumbu zake zilimwambia aliweka mule kabatini na si sehemu nyingine. Hakuona hata risiti za malipo.
Haraka akatoka mle chumbani na kuelekea kwenye chumba chake cha kulala nako alikuta mkono wa mtu umepita na kufungua droo za kitanda na meza ya kujipambia. Remi alishika kiuno na alikubali kweli ilikuwa ni mchezo wa utangulizi. Waliamua kumkwamisha kwa kuchukua nyaraka za kampuni yake.

Lakini kwa nini?

Hakujua sababu ya yale yote ni nini na wala akili yake haikutaka kuyaunganisha na tuhuma za mumewe ambae kwa sasa lau alijua yu mzima na anatafutwa kwa tuhuma za ugaidi.

Ugaidi?

Hapana mume wangu hawezi kuwa gaidi. Alijikatalia.

Ooh shit!! Akamaka huku akitoka chumbani na kurudi sebuleni. Alikuwa amekumbuka matukio yaliotokea ofisini kwake.

Kwanza mauaji pili kutekwa kwa Davis Minja.

Kwanini ofisini kwangu na kwanini Davis alienda ofisini na si kunipigia simu ama kunijia hapa nyumbani?

Hakukuwa na wa kumjibu maswali yake na hesabu zake ziligoma kuyaunganisha matukio ili apate njia ya utatuzi, alibaki mshuhudiaji wa mchezo ule wa utangulizi huku akiwa hajui onyesho kamili litakuwaje.

Remi alitatizika.

****

Hakutaka kuendelea kukaa pale alitoka na kuingia kwenye gari yake na kuelekea zilipo ofisi za ukusanyaji mapato posta na jua lilikaribia saa nane alasiri.

Saa nane na dakika arobaini na tano; saa tisa kasoro dakika kumi na tano ilimkuta akiwa makao makuu ya kitengo cha ukusanyaji mapato na tayari mtu wa Tehama alikuwa anashugulikia swala lake kwenye vibarizi kadhaa vilivyokuwa mle ofisini.

“Dada tunasikitika taarifa zako hazionekani kabisa na inaonekana mara ya mwisho kulipia ni wakati unachukua leseni ya uendeshaji wa kampuni yako” alisema yule bwana huku macho yake yakiwa kwenye kibarizi(kompyuta).

Ajabu hii!!

“Lakini siku chache tu ndio nimetoka kufanya malipo na makadirio mapya!” alijitetea Remi.

“Hapana dada; takwimu zetu hazionyeshi jina la kampuni yako katika orodha ya walipaji ila lipo kwenye orodha ya watu wanaodaiwa na mamlaka ya mapato nchini” alifafanua yule bwana ambae kitambulisho chake kilimtambulisha kwa ubini wa Pius Kangwa.

Remi alivuta pumzi ndefu na kuzishusha kwa mkupuo.

“Unahisi kimefanyika nini hadi takwimu za kampuni yangu hazionekani?” hatimae Remi aliuliza.

“Ni ngumu kuelewa ila sina hakika kama ni mchezo umefanyika ili kukuhujumu, hatuna wafanyakazi wa aina hiyo katika ofisi zetu zote nchi nzima dada” alifafanua Pius.

“ Lakini nina uhakika na ninachokisema” alisema Remi.

“Kama unahakika,unazo risiti za malipo ya Bank na mhuri wa uthibitisho?” aliuliza Pius kangwa.

Lilikuwa swali muhimu na wakati muhimu ila hesabu za Remi hazikuwa na jibu la swali lile. Hesabu ziligoma.

“Hapana. Kwa sasa sina” alijibu kwa kubabaika Remi.

“Hauna kabisa Dada; na kama unazo njoo nazo kesho tafadhali” alisema kijana yule.

“kwani Bank nilikolipia hakujaunganishwa na mfumo wenu ili kutambua moja kwa moja walipaji?” alihoji Remi.

“Ukiona hapa hakuna takwimu za kumbukumbu,basi jua hata huko bank hakuna. Dada jaribu kuwa na muda wa kuwa unaleta mwenyewe usiwe unatuma watu” alishauri Pius.

“Nope!! Huwa naleta mwenyewe na nilifanya miamala mwenyewe” Remi alijibu.

“Basi utakuwa unaugua Schizophrenia dada angu, wahi hospital”
Alisema yule jamaa.

“Whaat! Umesema nini vile!” alimaka Remi na kumfanya Pius aruke juu ya kiti na kumkodolea macho Remi.

“Samahani dada,sikumanisha hivyo ulivyodhania ila nimekushauri tu mana ukiugua ugonjwa huu wa schizophrenia unakuwa unapoteza kumbukumbu” alifafanua kwa tabu Pius.

Remi alibaki akimtizama bwana mdogo yule huku akijiuliza maswali mawili kichwani bila kusema lolote.

Katamka bahati mbaya ama makusudi? Alijiuliza kimya kimya. Ugonjwa huo ndio uliomtesa kwenye mkasa ulioandikwa na Davis Minja; na sasa anatajiwa aina ya ugonjwa ule ule na kijana wa mamlaka ya ukusanyaji mapato nchini.

Kichwa kiliwaka moto na bila kusema lolote akachukua mkoba wake na kuutundika begani na kuanza kushuka chini akitokea ndani ya ofisi ile ya kusikiliza shida za wateja ndani ya mamlaka ile.

Wakati anamalizia ngazi ili atoke ndani ya ofisi zile, macho yake yalimuona Kitambi nae akikaribia pale.

Wote wakasimama.

“kama ulikuja kulipa ni heri ila kama ulikuja kuhakikisha madai yetu umekosea sana” alisema yule bwana kitambi waliekutana kwa mara ya kwanza ofisini kwake Mwenge.

Remi hakujibu tuhuma zile ila akili yake ilicheza kidalipo kuikumbuka sauti ile aliwahi kuisikiliza wapi kabla ya siku ile.

Kumbukumbu haikumpa ushirikiano licha ya kuhisi kabisa sauti ile si ngeni kwake.

Hakujishugulisha zaidi akamkwepa na kutaka kuendelea na safari.

“It’s showtime baby!!” Kitambi alitamka kwa madaha kama jingo ya radio free Africa mwanza.
Remi aliganda kama sanamu huku akizisikia hatua nzito za bwana Kitambi zikielekea juu alikotokea yeye.

Ebana eeh hili lilikuwa sawa na somo la hisabati gumu kulielewa na linahitaji utulivu na usikivu kulifaulu.

****

Tutaendelea usiku na sehemu inayofuata
 
RIWAYA; URITHI WA GAIDI

NA; BAHATI MWAMBA

SIMU; 0758573660


SEHEMU YA TATU



“It’s showtime baby!!” Kitambi alitamka kwa madaha kama jingo ya radio free Africa mwanza.
Remi aliganda kama sanamu huku akizisikia hatua nzito za bwana Kitambi zikielekea juu alikotokea yeye.

Ebana eeh hili lilikuwa sawa na somo la hisabati gumu kulielewa na linahitaji utulivu na usikivu kulifaulu.

****

MOGADISHU – SOMALIA.

Pembezoni kidogo mwa pwani ya mji wa Mogadishu ndani ya Somalia kulikuwa kuna tukio linaendelea kwa umakini wa hali ya juu bila kuwa na bughudha ama kelele yoyote. Kulikuwa kuna makundi mawili yaliokuwa yanafanya jambo katika barabara ya Old Mogadishu pembeni kidogo mwa fukwe ya Second Lido. Kutoka pahali fulani ndani ya hoteli ya Lugo kulikuwa kuna watu waliokuwa wamevaa kanzu za bei mbaya na vibandiko vya bei mbaya vile vile. Miongoni mwa watu wale kuna wawili waliokuwa wanakazi maalumu ambayo mmoja alikuwa na kiona mbali na kazi yake ilikuwa ni kuona mjongeo wa kile kilichowaweka pale. Lakini pia kulikuwa na mtu mwingine ambae alikuwa na mzigo mkubwa mgongoni ambao ulikuwa na mawimbi maalumu ya kupokelea simu za upepo kutoka kwa watu maalumu waliokuwa wamepandikwa kwenye barabara ile ya old Mogadishu.

Nyuma ya vijana wale kulikuwa kuna walinzi zaidi ya kumi ambao walihakikisha ulinzi eneo lile huku wakionekana kujali zaidi usalama wa watu wawili waliokuwa wamekaa kwenye viti ndani ya chumba kile cha gorofa tatu katika hotel ya Lugo.

Watu wale wawili walionekana kufuatilia kwa makini kila taarifa waliopewa na vijana wao kutokea nje ya eneo lile na kunaswa na mawimbi maalumu yaliokuwa katika mtambo uliokuwa umekaa sawia mwa kijana shababi aliekuwa mle ndani.

“Kabla ya dakika kumi ndege ataangusha YAI kiotani” ilisikika sauti kupitia simu ya upepo mle ndani na hapo mmoja ya watu waliokuwa wamekaa ambae alionekana ni kijana zaidi kuliko mwingine alinyanyuka na kuelekea dirishani kisha akanyoosha mkono na kijana aliekuwa na kiona mbali alimpatia nae akakipachika usoni mwake.

“Wapo ndege watatu, hatujui YAI lipo kwa ndege gani” Alisema yule jamaa kijana aliesimama dirishani na kiona mbali.

Hakuna aliemjibu nae hakujali akaendelea..

“Wamarekani ni wajanja sana,sina hakika kama watatupa YAI kamili”

Kauli ile ilimyanyua bwana aliekuwa amekaa peke yake nae akasogea karibu na dirisha na huku nyuma walinzi nao walisogea eneo lile kuhakikisha usalama zaidi.

“Unahisi wanaweza kutufanyia janja yao?” aliuliza yule mzee.

“Nahisi! Japo sina hakika” alisema yule kijana huku akishusha kiona mbali na kukirudisha mikononi mwa kijana aliekuwa nacho mwanzo.

“Kwani kuna anae mfahamu huyo Ahmed?” aliuliza yule kijana.

“Hapana! Na aliekuwa anamfahamu aliuwawa kwenye mashambulizi yaliotekelezwa na wamarekani mwaka 2006. Hivyo tunacheza pata potea japo ni muhimu sana kwetu huyu jamaa.” Alijibu Mzee wa kisomali.

“Mimi nakumbuka tu nilichokiona kwake wakati anaonana na Baba ila nimemsahau wajihi wake” alisema Kijana na jambo lile likafanya wote mle ndani wamakinike hasa yule Mzee.

“Nadhani ukiwakumbusha vijana ulichokiona itakuwa vyema zaidi ili tusipokee yai viza” alisema Mzee huku akijikuna kidevu chake kilichokuwa na ndevu ndefu wastani kama walivyo mashekhe wengi.

“Bwana alikuwa na kovu baya sijapata ona,Kovu lilianzia kifuani upande wa kushoto kuelekea upande wa mbavu za kulia likiwa limechora michirizi mingi huku lilipoanzia ni kama alijeruhiwa na mnyama mkali; Simba ama Chui” alisema kwa hisia kijana huku akijaribu kurekebisha kanzu yake ili imkae vyema.

Mara ileile taarifa ikatolewa kwa mapandikizi yalioko nje nayo yakaifanyia kazi.
*

Kundi lingine ndilo hasa lilikuwa linalengwa na kundi la kwanza lililoko Lugo Hotel. Kundi hili lenyewe lilijitenga katika viunga viwili. Kiunga cha kwanza kilikuwa upande wa mashariki mwa old Mogadishu na kilikuwa na watu wawili na Kiunga cha pili kilikuwa ndani ya magari matatu yaliokuwa na nembo za kikosi maalumu cha kulinda amani Mogadishu cha AMISOM(Africa Union Mission).
Ndani ya gari lililokuwa mbele kulikuwa kuna askari saba waliokuwa tayari kwa lolote na gari la nyuma pia lilikuwa na askari saba ila gari la katikati lilikuwa na askari komando watatu tu na mtu mwingine mmoja aliekuwa amefungwa minyororo mikono na miguu huku sura yake ikiwa imechakaa na mwili wake ukiwa umedhoofu sana.

Gari ya mbele ilionesha ishara kuwa wanapaswa kusimama eneo husika.

Magari yote yakasimama.

Kwenye gari la katikati, Komando mmoja alitoa kinasa sauti alichokuwa amekipachika sikioni mwake na kukipachika sikioni kwa yule mtu aliekuwa amefungwa kwa minyororo.

“Wanaweza kukujaribu kwa kila namna ili wathibitishe kama kweli wewe ndie Ahmed Twalibu sahihi,usije kutetereka na jukumu lako ni moja tu kuhakikisha tunajua maficho ya FLAMINGO kisha tutakupa utaratibu mwingine” ilisikika sauti kutoka kwa mtu aliekuwa kiunga cha kwanza mashariki mwa eneo lile.

“Nitawasiliana vipi na nyinyi kusubiri maelekezo?” aliuliza mtu aliekuwa amefungwa kwa minyororo.

“Siku mkipokea mzigo wa silaha hakikisha unatafuta risasi moja ambayo ni blanco hiyo itakuwa na ujumbe wako. Lakini kumbuka mwili wako ni mawasiliano na sisi Honda” ilisema sauti kutoka kiunga cha kwanza.

“Goda up kamanda!” ilisema sauti nyingine tofauti na ya awali iliokuwa upande wa kiunga cha kwanza.

“Goda up komredi” alijibu Honda p.a.k Ahmed Twalibu.

Kutokea nje ya gari walilokuwamo kukagongwa mara kadhaa na ikawa ni ishara kwao kushuka ndani ya gari huku Honda au Ahmed wa bandia akiwa amezingirwa na makomando watatu wa kikosi cha AMISOM. Na kutoka eneo lile lote ilikuwa limezingirwa na makomando kumi na saba kiujumla huku madereva wa magari yale wakiwa nao wametulia vyema kwenye gari zao tayari kwa lolote.

Ukimya ulikuwa wa kutisha kwenye barabara ile na makomando nao walikuwa kimya wakiwa makini na hatua zao wenyewe na mbele ya magari yao kulikuwa kuna gari dogo lililokuwa wazi na juu ya gari lile kulikuwa kuna kijana mdogo mwenye kupata umri wa miaka kumi hadi kumi na tano na alikuwa amebeba silaha ya kivita mikononi mwake bila wasiwasi wowote na ile ndio ilikuwa ishara ya kuwa pale ni eneo husika.

Wote wakiwa kimya,mara ukasikika mkoromo kutoka kwenye mifuko ya mmoja wa makomando waliokuwa wamemzunguka Ahmed Twalibu.

Komando yule alitoa simu ya upepo iliotoa mkoromo kuashiria kuna simu nyingine inayoingia.

“Mwacheni asogee mbele peke yake na nyinyi mrudi nyuma” iliunguruma sauti kutokea kwenye simu ile kwa lugha mbovu ya kingereza kwa lafudhi ya kihabeshi.

“Ni jicho kwa jicho komredi,tunaomba tuone upande wenu” Alisema komando wa kikosi kilichompeleka pale gaidi Ahmed.

Ukapita ukimya wa sekunde kadhaa.

“Anzeni nyie kisha tutawapeni wa kwenu” ilisema sauti kutoka upande wa pili.

Komando yule aliwaangalia wenzie ambao nao waliishia kutazama tu bila kusema kitu.

Akili zao zilikuwa zinapiga hesabu kali kukubaliana na jambo lile.

“Ok!!” alijibu kifupi komando yule na hapo komando wengine waligeuka na kutazamana kwa maamuzi yale ya kiongozi wao.

Dakika iliofuata walimpisha Ahmed asogee mbele kama ilivyotakiwa akiwa amefungwa vile vile minyororo mikononi na miguuni.

Honda; p.a.k Ahmed Twalibu alipiga hatua kivivu huku nae akiangaza macho yake kushoto na kulia taratibu bila papara.
Hatimae alifika kati kati ya gari lililokuwa wazi na juu kukiwa na mtoto aliebeba silaha na wale makomando ambao muda wote walikuwa kimya bila hata kupepesa macho yao.

Kutoka kwenye chumba ndani ya hotel ya Lugo; kijana yule aliekuwa na asili ya Saudia,alishusha chini kiona mbali na kuwageukia wenzie waliokuwa na asili ya kisomali.

“Anaweza kuwa ndie,mruhusuni tutamjua akiwa chini yetu” alisema huku akikabidhi tena kiona mbali kile kwa mtu aliekuwa nacho awali.

“Basi itifaki izingatiwe” alisema mzee wa kisomali huku akikuna msitachi wake.

Vijana walijua nini wanapaswa kufanya.

*

Kijana aliekuwa kwenye gari na mtutu wa bunduki,alisikia mlio wa mluzi mara mbili na hivyo alijua ni kipi cha kufanya wakati huo.

Haraka kutoka pale alipokuwa, akashuka kibabe utadhani ni mtu mzima. Akapiga hatua bila wasiwasi wowote na kumfikia Honda p.a.k Ahmed Twalibu.

Hakujishugulisha na pingu alizokuwa amefungwa Ahmed bali alibaki akimtizama usoni bila kupepesa. Honda aliona macho ya yule mtoto yalivyojaa ukatili ingali ni mdogo. Alikakamaa mithili ya wabeba mizigo bandarini.

Hakika ilihuzunisha.

Ila mtoto yule hakuonekana kujali.

Akachomoa kisu na kuiweka pembeni bunduki yake kisha akamfuata Ahmed.

Mtoto yule bila uoga alianza kurarua nguo za Honda p.a.k Ahmed Twalib gaidi aliesakamwa na makundi mbalimbali wakitaka ajiunge nao na sasa Ahmed yupo Somalia mbele ya kikundi cha kiharamia na kigaidi huku yakiwa ni makabidhiano maalumu na serikali ya Marekani.

Mtoto yule alieonekana ni fundi wa kutokea kutumia kisu,hakumaliza dakika moja tayari nguo za Ahmed zilikuwa hazitamaniki na yule mtoto akabaki akilikodolea kovu baya kifuani mwa Ahmed. Yule mtoto alishindwa kuelewa kovu limesababishwa na nini na ni binadamu gani anaweza kuhimili kuishi na kovu kubwa kiasi kile maishani mwake.

Hakika bwana mdogo aligwaya.

Bwana mdogo yule akabeba mtutu wake na kugeuka, lakini kama alisita hivi na kugeuka tena kulitazama kovu lile.

Kuna kitu kilipita akilini mwake.

Kovu gani hili? Mbona kama ni bandia? Aah!!” alijakatalia haiwezi kuwa maigizo katika mwili wa mtu.

Bwana mdogo aligeuka na kumpa ishara Ahmed amfuate. Ahmed akaanza kujivuta kivivu kumfuata huku makomando waliomfikisha pale wakiwa kimya na umakini wa hali ya juu.

Bwana mdogo yule alipiga mbinja kadhaa kisha akajipiga kifuan mara kadhaa. Ilikuwa ni ishara ya kukamilisha kazi yake na sasa wakubwa wake waendelee na utaratibu wao.

Wakati Ahmed anapakizwa kwenye gari na bwana mdogo yule, Makomando walishuhudia watu wengine watatu wakitokea kwenye jengo moja bovu lililokuwa pembezoni mwa barabara. Watu walionekana wakiwa wamedhoofu kupita maelezo na walizeeka kweli.

Walikuwa ni mateka wa kijeshi tangu miaka ya tisini baada ya vita kati ya kikundi cha kigaidi cha AIAI(Al-Itihaad Al-Islamiya).

Komando kiongozi aliona wahusika wa mabadilishano yale, akatoa ishara kwa makomando wale wa AMISOM nao wakaanza kuelekea kuwapokea watu wale walioonekana kudhoofu miili yao.

Lakini gafla ikasikika risasi moja hewani na makomando wote wakakoki silaha zao tayari kwa lolote.

Alikuwa ni bwana mdogo aliepiga risasi juu.

Akashuka kwenye gari na kumwacha Ahmed akiwa na dereva akawafuata wale makomando ambao walikuwa wamesimama bila kujua wafanye nini.

Akawafikia!!

“Oya!! atakaepiga hatua kusogea hapo alipo nitamvua chupi hadharani, nguruwe weupe nyie” alifoka bwana mdogo bila kuogopa macho ya kikazi ya makomando wale ambao mitutu yao ilikuwa sawia kifuani mwa bwana mdogo yule.

Walipigwa mkwara wakatulia.

Bwana mdogo akageuka kibabe na kuwafuata wazee waliokuwa wanakikokota kuwaendea wale makomando.

“Na nyie vibwenzi nitawatoa roho sasa hivi, mtaondokaje bila mi Mzee wenu kutoka hapa.” Bwana mdogo akaachia mkwara mbuzi wazee wale waliokuwa makimando miaka hiyo kabla ya dhahama iliowakumba na kujikuta wakiwa mateka miaka mingi.

Bwana mdogo alianza kuondoka kwa madaha huku akipiga mluzi wa wimbo asioujua,na kabla hajafika kwenye gari akawageukia wale wazee.

“Mnadhani na huo uzee mnaenda kufanya nini. Nendeni mshikishwe tunguli na Wamarekani vibwengo ninyi”

Alah!!!

Mtoto anatema mkwara kwa wakubwa.

Makomando wote walibaki wakiwa wameganda kama sanamu. Mtoto aliwashangaza kwa kujiamini kwake.

Na kweli walitulia hadi bwana mdogo alipoondoka pale ndipo na wao walipowahi kuwapokea wazee wale na kuwaingiza ndani ya magari yao na kuondoka eneo lile la Old Mogadishu.

Wao hesabu zao zilienda sawa siku hiyo na hesabu za kikundi kile ambacho hakikuwa na jina kubwa la ugaidi miaka ya karibuni, nacho kilijua kipo safi katika hisabati yao.

**

Bwana mdogo yule hakwenda mbali na mateka wake Ahmed. Walizunguka kona ya kwanza na ya pili wakaingia kwenye jumba lililoonekana kama ni karakana ya kutengenezea magari.

Humo ndani kulikuwa kuna magari mengi mabovu na mazima yalioonekana kupitia shuruba nyingi sana. Mbali na hayo pia kulikuwa kuna watu wengine wanne.
Kati ya watu hao wawili walikuwa na mitutu ya kivita huku mikanda ya risasi ikiwa imezunguka mabegani mwao, na wawili walikuwa ni wasichana wazuri wa kihabeshi wenye umri si zaidi ya miaka kumi na saba ambao walikuwa wamefungwa mikono kwa nyuma na vitambaa vyeusi machoni pao. Walionekana kupitia mateso mengi mana walidhoofu na miili yao kugandana na makovu mabichi.

Hakika ilitia huzuni.

Honda p.a.k Ahmed alitazama kwa huzuni wasichana wale.

Watekaji hawakujali.

Bwana mdogo yule alibaki akiwa anamtazama Honda kwa dakika kadhaa,kisha akaanza kumzunguka kwa madaha kama anaekagua kitu hivi kisha aliporidhika na tambo zake alisimama mbele ya Honda na kwa gafla akamtandika ngumi kali ya tumbo na kumfanya Honda ainame kwa maumivu makali yaliosambaa tumboni kwake.

Ngumi ya bwana mdogo ilikuwa ni ngumi ya mtu mzima hakika..

“Naitwa Sozi mfalme wa wajane hapa Somalia”alijigamba bwana mdogo huku akirekebisha mtutu wake begani na kuutia mikononi kisha akapiga mluzi na hapo akaja jamaa mwingine aliekuwa na zana za ufundi na alipofika bila kuelekezwa alianza kushugulika na vifyatuo vya minyororo iliokuwa mwilini mwa Honda.

Dakika nne baadae Honda alikuwa huru lakini hakuruhusiwa kupiga hatua hata moja.

“Ahmed; nataka ufanye kazi moja tu hapa” alisema Sozi bwana mdogo mtata au alivyopenda kuitwa mfalme wa wajane. Haijulikani wajane gani aliomaanisha huyu bwana mdogo.

Aliita wale vijana waliokuwa na wale mateka nao wakaanza kuwaburuza mabinti bila huruma na kuwafikisha pale walipokuwa Sozi na Honda au kama walivyomjua kwa jina la Ahmed.

“Hawa ni wahabeshi wa huko Ethiopia; mabwana zao walituchafua ndani ya nchi yetu sasa waliwaacha hapa na kifo kimefika na wewe ndo utawauwa” alisema Sozi huku akiikoki silaha yake na kitendo bila kutegemea akaachia risasi ilioenda kutua kichwani mwa binti mmoja na kumsambaratisha ubongo wake bila huruma.

Hakika Sozi alikuwa katili zaidi ya umri wake.

Akamgeukia Honda.

“wewe ni gaidi Ahmed; hivyo huoni huruma kwa hawa mende,piga risasi tu huyu aliebaki ili tujue kweli sifa unazopewaga ni za kweli.” Alisema Sozi huku akimpa mtutu wa kivita Honda waliemjua kwa jina la Ahmed.

Mmoja wa wasomali wale alimvua kitambaa yule binti. Binti alimlitizama Honda kwa huruma sana.

Honda alibaki akiwa hana la kufanya.

Ukitaka kumuua nyani usimtizame usoni.

Mfalme wa wajane alibaki akimtizama Ahmed na maamuzi yake.

Honda alikuwa katikati ya hisabati za Wasomali.

Hakujua aepuke vipi mtego wa hesabu ile, huruma ilikuwa kubwa karibu ibebe ujasiri wake.

Ataua?

***


Maoni yako ni muhimu sana katika kazi hii.karibuni
 
RIWAYA; URITHI WA GAIDI

NA; BAHATI MWAMBA

SIMU; 0758573660


SEHEMU YA PILI.


Tatizo hakujua huko nako ni moto mwingine utakao acha akili yake ikiwaka. Ila hakujua na angejua hakika angejirudia kwake tu akalale.

***

Wakati Remi akiingia kwenye lango la ofisi yake alikutana na hekaheka ambazo hakujua chanzo ni nini. Ofisi zake zilikuwa ni kwenye nyumba ya kawaida tu ambayo ilijengwa maalumu kwa kazi za kiofisi na pembeni yake kulikuwa kuna gorofa kubwa lenye ofisi nyingine pia. Kampuni yake iliitwa REMI ARCH COMPANY LIMITED. Ilishugulika na utafiti wa mambo ya kale fani ambayo aliipenda sana.
Hekaheka zile zilianzia nje ambako kulikuwa kuna askari wa jeshi la polisi wenye silaha za moto ambao walipumuona wala hawakujali,waliendelea kuweka usalama eneo lile lakini pia alipoingia ndani alikuta wafanyakazi wake wote walikuwa wamekusanywa na kuwekwa pamoja huku kukiwa na maafisa kadhaa wa jeshi la polisi na wale wa ukusanyaji mapato yani TRA.
Alishindwa kuelewa kuna nini pale ofisini kwake licha ya kuona heka heka zile. Wafanyakazi wake nao walipomuona wakaelekeza macho yao kwake huku kila jicho likisadifu yalio myoyoni mwao.

Remi alielekea moja kwa moja kwa askari mmoja aliekuwa na cheo cha sajini na alionekana ndie kiongozi wa kundi na heka heka zile.

“Afande shida nini hapa!?” aliuliza kwa kihoro Remi.

Afande yule alimtizama kuanzia juu hadi chini kisha nae akauliza bila kutoa jibu.

“wewe ndie mkurugenzi hapa?”

“Ndio. Nieleze shida tafadhali!!” alisema Remi.

“Tusogee pembeni kidogo” alisema Sajini yule huku akimshika mkono Remi na kusogea nae pembeni.

“Kuna mambo mawili yanaendelea hapa. Mosi; inasemekana hujalipa kodi yako ofisi ya mapato kwa miaka kadhaa ila hilo silo lililotuweka hapa sisi maofisa wa polisi. Lilituweka hapa ni kuwa tulipigiwa simu ahsubuhi kabisa kwamba kumetokea mvurugano hapa ofisini kwako na kupelekea mwandishi wa riwaya Tanzania bwana Davis Minja kuchukuliwa na watu wasio fahamika na kuua mlinzi wako” alieleza Sajini aliejitambulisha kwa jina la Vengu.

E bana ee!!

Remi alihisi moyo unataka kuchomoka kwa kasi ya mdundo wa mapigo yake. Alitamani aangue kilio ili akinyamaza mauzauza yale yakatike ila haikuwezekana.

Nini sababu ya yote haya?

Mume gaidi na sasa anaambiwa mtu katekwa ofisini na mauaji kutendeka ofisini kwake na bado anadaiwa kodi na mawakala wa ukusanyaji na ofisi tayari zinapigwa kufuli.

Aah mkosi gani huu tena kwa Remi.

Hakika ni kipindi kigumu kuelezeka. Remi chozi lilimtoka.

“aah inapaswa tukuhoji kidogo dada kisha tukuache umalizane na maofisa wa TRA.” Alisema sajini Vengu.

Remi alipandisha pumzi na kuzishusha kwa mkupuo mara mbili kisha akayarudisha macho yake kwa Sajini.

“Eeh!! Unamahusiano gani na Davis Minja?” aliuliza Sajini.

“Ni rafiki wa familia”

“kwa muda gani”

“Muda mrefu”

“aliwahi kukwambia chochote kuhusu upande wa adui yake?”

“Hapana!!”

“unahisi kwanini ametekwa ofisini kwako?”


“siwezi kujua!”

“unahisi kwanini alikuwa hapa ahsubuhi sana badala ya kuja kwako!”

“sijui!”

“sawa sisi kwa sasa hatuna maswali mengi. Badae tutakuhitaji kituoni Mwinjuma uje kutoa maelezo zaidi lakini kwa sasa tutaendelea na utaratibu wa kipolisi kuukagua mwili wa mlinzi wako” alisema sajini huku akiondoka na kumuacha Remi akiwa amesimama bila kujua ni kipi cha kufanya.

Mambo yanayotokea yanachanganya.

Akiwa bado amesimama pale mara mtu mwingine aliekuwa amevaa suti akamfuata. Bila salamu akasema.

“Ofisi yako inakashifa ya kutokulipa kodi serikalini hivyo tutaziondoa kufuli na kukuacha uendelee na shuguli zako ukisafisha madeni yako”

Remi alimtizama bwana yule ambae hakuonekana kujali kutazamwa kule.

“wiki jana ndio nimetoka kufanya malipo ya makadirio ya kodi sasa inakuwaje nadaiwa?”

“kwa hiyo unataka kusema hapa sisi tumekosea kufika? Unadhani wewe ni mjanja kuliko serikali?” alibwata bwana kitambi yule alieonekana kuwa na mwili wa rushwa.


“Nyaraka zote ninazo sasa sijui nyie mna ofisi ngapi ambazo mnafanyia malipo hadi mshindwe kujua nimekuwa mlipaji tangu nisajili kampuni hii” Remi nae alimaka.

“Mwanamke angalia usije kujibia kituo cha polisi. Wewe ni sawa na mhujumu uchumi hivyo huna haki ya kuhoji lolote kwa sasa zaidi ya kuclear madeni yako na sisi tufungue ofisi zako” bwana kitambi alizungumza kwa majigambo makubwa.

“Nyaraka zipo aisee usinitishe na hili litakugarimu bazazi wewe” Remi nae alifoka,hakutaka kupelekeshwa kama tiara wakati ana uhakika kabisa amekuwa akilipa serikalini tangu aliposajili ofisi yake kuwa kampuni kwa ajili ya utafiti wa kujitegemea wa mambo ya kale.

Bwana kitambi alicheka kwa dhihaka kisha taratibu akasema kama vile asietaka wengine wasikie anachozungumza na Remi.

“Itakugarimu hiyo jeuri yako mwanamke na huna pa kukimbilia safari hii”

Ebana eeh

Huyu bwana anazungumza nini. Safari hii safari nyingine ilikuwa wapi!

Jama yakoje mambo haya?
Alijiuliza Remi huku ile sauti ya bwana kitambi ikijirudia kichwani mwake.

“Sauti hii nimepata kuisikia wapi?” alojiuliza mara nyingi bila kupata jibu na alipokuja kurudisha macho yake pale alipokuwa bwana kitambi hakumuona zaidi aliona wafanyakazi wake wakitoka pale walipokuwa na kuanza kumfuata. Askari polisi na maafisa wa mapato nao walikuwa wameanza kuondoka pale ofisini.

Hakika zilikuwa ni hesabu ambazo kamwe Remi hakujua njia ya kuzikokotoa.

Hisabati ilifanya kazi na hakika aliona anaenda kupata zero yenye masikio makubwa.

*****

Jambo la kwanza aliloona kwake linafaa ni kurudi nyumbani kwake kuzitafuta nyaraka za malipo ya kodi ili aelekee zilipo ofisi za mapato na kujua undani wa suala lile kwa marefu na mapana.
Alifungua geti na kuingiza gari kisha haraka akaelekea ndani ambapo moja kwa moja alielekea kwenye kabati maalumu la kuhifadhia nyaraka muhimu za kiofisi.

Kwa pupa aliokuwa nayo hakujihangaisha hata kudadisi nyumba yake,alipitiliza moja kwa moja kwenye chumba maalumu cha kuhifadhia nyaraka muhimu.

Alipofungua mlango wa chumba kile alishangaa kwa alichokiona.

Vitabu vilikuwa vimesambaratika hovyo, nyaraka zilizokuwa kwenye karatasi zilikuwa zimechanguka hovyo na kabati lilikuwa wazi.

Upekuzi ulifanyika!!

Ni nani sasa anaeweza kuingia ndani na kupekua kiasi hiki!

Alijiuliza bila kupata jibu.

Haraka akarejea sebuleni,na ndipo aliposhuhudia mtafaruku wa ajabu ambao alishindwa kuelewa wakati anaingia ni nini kilisababisha hakuona mambo yale. Kila sehemu ilikuwa imeguswa hovyohovyo na kupelekea baadhi ya mapambo kusambaratika hovyo mule ndani; sofa zilikuwa zimendolewa sehemu yake na kusogezwa pembeni na hata zulia zito lililokuwa chini nalo lilikuwa limebinuliwa. Alipotizama ukutani aliona picha zikiwa zimegeuzwa hovyo kabisa na moja ya picha zake ilikuwa inaamandishi madogo yaliomfanya amakinike. Akasogea taratibu na kwenda kuyasoma.

“it’s showtime!!” aliyarudia mara mbili maandishi yale na taratibu akaona kuna mchezo wa matukio yale na ule ni ujumbe maalumu kwake na hakika alikubali ile ilikuwa ni showtime kwake, lakini swali lilibaki linakizunguka kichwa chake.

Baada ya showtime ni nini kitafuata ama tukio gani? Na nini lengo hasa. Je ni ugaidi wa mumewe ama ni kisasi cha watu juu yake? Watu gani?.

Yalikuwa ni maswali mengi kwa mtu tofauti na Remi ila kwa Remi lilikuwa ni swali moja lenye jibu moja na vipengele vyake.
Remi nae aliandika kwa vidole vyake lile neno showtime kisha akaingiza mkono mfukoni na kuchukua kalamu ndogo ambayo huiweka kwa dharura na kuandika chini ya maandishi yale neno “mathematics; Hisabati” aliandka kwa kingereza kisha kiswahili. Alikuwa na maana ya kwamba wao watacheza mchezo wa kufurahisha na kukarahisha ila yeye atapiga hesabu kujua mbinu za mchezo wao. Remi hakuwa na akili za mtu wa kawaida; Remi aliamua kutulia na kufikiri zaidi, alijionya kuhamaki mana kungemtoa sadaka kwa wacheza mchezo wa utangulizi Showtime.

Akaiacha ile picha pale sebuleni na kurejea kwenye chumba kile cha kuhifadhia nyaraka.

Vilevile alivyokuta kumepekuliwa,nae akaamua kupekua kutafuta nyaraka za kampuni yake.

Kila alichogusa hakikuwa anachokihitaji.

Jama!!

Ziko wapi nyaraka hizo?

Alitafuta kila pahali bila kupata kile alichokitaka. Nyaraka hazikuwepo na hakuziona kabisa. Kumbukumbu zake zilimwambia aliweka mule kabatini na si sehemu nyingine. Hakuona hata risiti za malipo.
Haraka akatoka mle chumbani na kuelekea kwenye chumba chake cha kulala nako alikuta mkono wa mtu umepita na kufungua droo za kitanda na meza ya kujipambia. Remi alishika kiuno na alikubali kweli ilikuwa ni mchezo wa utangulizi. Waliamua kumkwamisha kwa kuchukua nyaraka za kampuni yake.

Lakini kwa nini?

Hakujua sababu ya yale yote ni nini na wala akili yake haikutaka kuyaunganisha na tuhuma za mumewe ambae kwa sasa lau alijua yu mzima na anatafutwa kwa tuhuma za ugaidi.

Ugaidi?

Hapana mume wangu hawezi kuwa gaidi. Alijikatalia.

Ooh shit!! Akamaka huku akitoka chumbani na kurudi sebuleni. Alikuwa amekumbuka matukio yaliotokea ofisini kwake.

Kwanza mauaji pili kutekwa kwa Davis Minja.

Kwanini ofisini kwangu na kwanini Davis alienda ofisini na si kunipigia simu ama kunijia hapa nyumbani?

Hakukuwa na wa kumjibu maswali yake na hesabu zake ziligoma kuyaunganisha matukio ili apate njia ya utatuzi, alibaki mshuhudiaji wa mchezo ule wa utangulizi huku akiwa hajui onyesho kamili litakuwaje.

Remi alitatizika.

****

Hakutaka kuendelea kukaa pale alitoka na kuingia kwenye gari yake na kuelekea zilipo ofisi za ukusanyaji mapato posta na jua lilikaribia saa nane alasiri.

Saa nane na dakika arobaini na tano; saa tisa kasoro dakika kumi na tano ilimkuta akiwa makao makuu ya kitengo cha ukusanyaji mapato na tayari mtu wa Tehama alikuwa anashugulikia swala lake kwenye vibarizi kadhaa vilivyokuwa mle ofisini.

“Dada tunasikitika taarifa zako hazionekani kabisa na inaonekana mara ya mwisho kulipia ni wakati unachukua leseni ya uendeshaji wa kampuni yako” alisema yule bwana huku macho yake yakiwa kwenye kibarizi(kompyuta).

Ajabu hii!!

“Lakini siku chache tu ndio nimetoka kufanya malipo na makadirio mapya!” alijitetea Remi.

“Hapana dada; takwimu zetu hazionyeshi jina la kampuni yako katika orodha ya walipaji ila lipo kwenye orodha ya watu wanaodaiwa na mamlaka ya mapato nchini” alifafanua yule bwana ambae kitambulisho chake kilimtambulisha kwa ubini wa Pius Kangwa.

Remi alivuta pumzi ndefu na kuzishusha kwa mkupuo.

“Unahisi kimefanyika nini hadi takwimu za kampuni yangu hazionekani?” hatimae Remi aliuliza.

“Ni ngumu kuelewa ila sina hakika kama ni mchezo umefanyika ili kukuhujumu, hatuna wafanyakazi wa aina hiyo katika ofisi zetu zote nchi nzima dada” alifafanua Pius.

“ Lakini nina uhakika na ninachokisema” alisema Remi.

“Kama unahakika,unazo risiti za malipo ya Bank na mhuri wa uthibitisho?” aliuliza Pius kangwa.

Lilikuwa swali muhimu na wakati muhimu ila hesabu za Remi hazikuwa na jibu la swali lile. Hesabu ziligoma.

“Hapana. Kwa sasa sina” alijibu kwa kubabaika Remi.

“Hauna kabisa Dada; na kama unazo njoo nazo kesho tafadhali” alisema kijana yule.

“kwani Bank nilikolipia hakujaunganishwa na mfumo wenu ili kutambua moja kwa moja walipaji?” alihoji Remi.

“Ukiona hapa hakuna takwimu za kumbukumbu,basi jua hata huko bank hakuna. Dada jaribu kuwa na muda wa kuwa unaleta mwenyewe usiwe unatuma watu” alishauri Pius.

“Nope!! Huwa naleta mwenyewe na nilifanya miamala mwenyewe” Remi alijibu.

“Basi utakuwa unaugua Schizophrenia dada angu, wahi hospital”
Alisema yule jamaa.

“Whaat! Umesema nini vile!” alimaka Remi na kumfanya Pius aruke juu ya kiti na kumkodolea macho Remi.

“Samahani dada,sikumanisha hivyo ulivyodhania ila nimekushauri tu mana ukiugua ugonjwa huu wa schizophrenia unakuwa unapoteza kumbukumbu” alifafanua kwa tabu Pius.

Remi alibaki akimtizama bwana mdogo yule huku akijiuliza maswali mawili kichwani bila kusema lolote.

Katamka bahati mbaya ama makusudi? Alijiuliza kimya kimya. Ugonjwa huo ndio uliomtesa kwenye mkasa ulioandikwa na Davis Minja; na sasa anatajiwa aina ya ugonjwa ule ule na kijana wa mamlaka ya ukusanyaji mapato nchini.

Kichwa kiliwaka moto na bila kusema lolote akachukua mkoba wake na kuutundika begani na kuanza kushuka chini akitokea ndani ya ofisi ile ya kusikiliza shida za wateja ndani ya mamlaka ile.

Wakati anamalizia ngazi ili atoke ndani ya ofisi zile, macho yake yalimuona Kitambi nae akikaribia pale.

Wote wakasimama.

“kama ulikuja kulipa ni heri ila kama ulikuja kuhakikisha madai yetu umekosea sana” alisema yule bwana kitambi waliekutana kwa mara ya kwanza ofisini kwake Mwenge.

Remi hakujibu tuhuma zile ila akili yake ilicheza kidalipo kuikumbuka sauti ile aliwahi kuisikiliza wapi kabla ya siku ile.

Kumbukumbu haikumpa ushirikiano licha ya kuhisi kabisa sauti ile si ngeni kwake.

Hakujishugulisha zaidi akamkwepa na kutaka kuendelea na safari.

“It’s showtime baby!!” Kitambi alitamka kwa madaha kama jingo ya radio free Africa mwanza.
Remi aliganda kama sanamu huku akizisikia hatua nzito za bwana Kitambi zikielekea juu alikotokea yeye.

Ebana eeh hili lilikuwa sawa na somo la hisabati gumu kulielewa na linahitaji utulivu na usikivu kulifaulu.

****

Tutaendelea usiku na sehemu inayofuata
Kitu mulua kabisa

Sent using Jamii Forums mobile app
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom