Ripoti ya madini kujadiliwa Bungeni!!!!!!

The Khoisan

JF-Expert Member
Jun 5, 2007
15,385
12,970
Ripoti ya madini moto

2008-07-10 11:49:49
Na Jackson Kalindimya, Dodoma


Bunge limekubali kupanga muda maalum wa kuijadili ripoti ya Kamati ya Rais ya Kupitia Mikataba ya Madini nchini iliyowasilishwa Bungeni na kupewa Wabunge ili ijadiliwe kwa kina kutokana na uzito wake.

Naibu Spika wa Bunge, Bi. Anne Makinda, alitoa msimamao huo jana, akiunga mkono shauku ya Wabunge wengi kutaka ripoti hiyo ijadiliwe kwa kina.

``Kwa sababu Wabunge wengi wameonyesha nia ya kutaka ripoti hii ijadiliwe na kutokana na uzito wake naona kuwa itapangiwa muda muafaka ili ijadiliwe,`` alisema Bi. Makinda na msimamo huo kuungwa mkono kwa makofi ya Wabunge wengi.

Hoja ya kutaka ripoti hiyo ijadiliwe, ilitolewa na Mbunge wa Mtera (CCM), Bw. John Malecela, ambaye aliwahi kushika nyadhifa za juu serikalini, ikiwemo Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais, ambaye aliliomba Bunge lipange muda maalum wa kuijadili ripoti hiyo waliyokabidhiwa juzi ili waipitie.

Naibu Spika, baada ya kuona Wabunge wengi wamesimama kuunga mkono hoja ya Bw. Malecela alisema kuwa hata wao waliona kuwa lina umuhimu wa kulijadili, lakini awali halikuwepo katika orodha ya mjadala wa kipekee.

Hata hivyo, aliahidi kupanga muda maalumu wa kuijadili ripoti hiyo. Hakutaja lini.

Hoja hiyo ilitolewa mara baada ya kipindi cha maswali kukamilika asubuhi na kabla hawajaanza kuijadili hotuba ya makadirio ya mapato na matumzi ya Wizara ya Nishati na Madini iliyowasilishwa na Waziri wake, Bw. William Ngeleja.

Wabunge wengi walioisoma ripoti hiyo, waliisifu kuwa ni nzuri na imeandikwa kwa upeo mkubwa wa kutatua matatizo yaliyoko katika sekta hiyo ya madini inayolalamikiwa sana.

Baadhi ya mambo yaliyosifiwa, ni mapendekezo ya kamati hiyo iliyoongozwa na Jaji Mark Bomani, inayotaka wageni wasiruhusiwe kuchimba madini ya vito, huku miongoni mwa maudhui ya ripoti ikitaja kuwepo usimamizi duni wa rasilimali hiyo ya taifa.

Kwa mujibu wa Wabunge, kamati hiyo pia imebainisha vitendo vya udhalilishaji katika migodi mikubwa, ikiwa ni pamoja na wafanyakazi kukaguliwa na miale ya x-ray, jambo ambalo ni hatari kiafya na udhalilishaji.

Mbunge Malecelea akitoa hoja bungeni, alisema ripoti hiyo ni muhimu ikajadiliwa na Wabunge kabla ya kwenda katika hatua nyingine ya utekelezaji. Kamati hiyo iliundwa na Rais Jakaya Kikwete, mwishoni mwa mwaka jana.

Baada ya kutolewa hoja hiyo, Anne, aliyekuwa akiongoza kikao jana asubuhi, aliridhia hoja hiyo na kufafanua kuwa hata Spika Samwel Sitta, baada ya kupata ripoti, alitaka ipewe muda wa kuujadili.

Katika ratiba ya vikao vya bunge vinavyomalizika mwezi ujao suala hilo halikuwepo Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Nishati yalipitishwa jana jioni.

Akichangia mjadala huo mbunge wa Vunjo (CCM), Bi. Aloyce Kimaro, aliungana na wenzake wanaounga mkono ripoti ya Jaji Bomani na kutaka hatua zaidi zichukuliwe ili kuanza utekelezaji.

Naye Mbunge wa Tabora (CCM), Bw. Siraju Kaboyonga, alisema hakuna sababu ya serikali kuendelea kusubiri, kwani baadhi ya mambo yaliyomo kwenye ripoti hiyo si ya kisheria, akirejea kauli ya Waziri Bw . Ngeleja, aliyesema kua sheria na sera mpya ya madini itakamilika ifikapo Aprili mwakani.

Alitahadharisha kwamba, hadi sheria mpya itakapoanza, tayari yatakuwepo mabadiliko makubwa yatakayoliingizia taifa hasara kubwa hasa ikizingatiwa kuwa wazalishaji hao wanafanyakazi kwa saa 24 na bei ya madini inapanda kila kukicha.

Bw. Kaboyonga, alitoa mfano kwamba, madini ya almasi katika kipindi kifupi kilichopita kipimo cha wakia (once) moja ilikuwa dola za Marekani 250 na sasa imepanda hadi kufikia dola 900, hali inayoashiria ongezeko la bei kwa kasi kubwa.

Ripoti ya kamati imeshauri kuwa baadhi ya mambo kama vile vivutio vya kodi viondolewe kwa wewekezaji wa madini na mirahaba wanayotozwa wachimbaji ipande.

Miongoni mwa changamoto zilizoko katika ripoti ya kamati hiyo ambayo yanatakiwa kufanyiwa kazi ni uharibifu wa mazingira, migogoro baina ya wawekezaji na matokeo ya uzalishaji wa madini hauna matunda mazuri kiuchumi ikiwa pamoja na kuwepo uhusiano mbaya baina ya wachimbaji wadogo na wakubwa.

Karibu wabunge wote waliochangia kutoka chama tawala na vyama vya upinzani waliisifia ripoti hiyo.

Ripoti hiyo iliyoongozwa na Jaji Mark Bomani ilifanya tatmini ya mapitio katika migodi yote mikubwa nchini, ikiwemo iliyopo katika mikoa ya Shinyanga, Mwanza,Mbeya, Tabora na Mara.

Kamati hiyo, pia ilisafiri katika nchi kadhaa kuangalia namna gani sekta ya madini inavyoendeshwa ikiwa pamoja na kupitia mikataba mbalimbali ya uwekezaji.

SOURCE: Nipashe
 
Back
Top Bottom