Raza: CCM itatue kasoro Z'bar

Rutashubanyuma

JF-Expert Member
Sep 24, 2010
219,470
911,173
na Betty Kangonga na Bakari Kimwanga

CHAMA cha Mapinduzi (CCM) kimetakiwa kuchukua hatua za haraka kutatua mapungufu yaliyojitokeza visiwani Zanzibar wakati wa kipindi cha uchaguzi vinginevyo kuna uwezekano wa kupoteza dola katika uchaguzi wa mwaka 2015.

Pia kimetakiwa kuhakikisha kinafanya tathmini ya Uchaguzi Mkuu uliopita na kuangalia sababu zilizochangia viongozi wastaafu kushindwa kupewa nafasi wakati wa kampeni.

Kauli hiyo ilitolewa jana jijini Dar es Salaam na Mfanyabiashara maarufu visiwani humo, Mohamed Raza, alipozungumza na waandishi wa habari na kuongeza kuwa viongozi wa juu wa CCM wanapaswa kuyafanyia kazi masuala hayo, ili kuwatoa hofu wananchi.

Alisema kamwe kundi fulani haliwezi kuongoza visiwa hivyo na wala ndani ya chama hicho hakuna bwana wala mtu maarufu bali kinachompa haki ya kuongoza ni chama hivyo viongozi wawe wazi kuzungumzia suala hilo kwa wananchi.

Raza alisema kipindi cha kampeni mpaka uchaguzi kulikuwa na mapungufu hatua iliyosababisha CCM kuwa na ushindi wa tofauti na mwaka 2005, hali ambayo inatoa taswira ya kutopata nafasi katika uchaguzi ujao wa 2015.

Alisema inasikitisha kipindi cha kampeni viongozi wastaafu walishindwa kushirikishwa huku wakiachwa kando jambo ambalo limeonekana kutoa taswira mbaya kwa wananchi hali iliyosababishwa na kukosekana mshikamano na uzalendo wa pamoja miongoni mwa wanachama.

“Wapo hata viongozi wastaafu walioamua kujipeleka wenyewe katika kampeni za chama hicho tena pale Kibanda Maiti ambapo kwa sasa panaitwa Kibanda Uhai na wananchi walishangilia walipomuoa Komandoo (Dk. Salmin Amour),” alisema.

Alisema kuwa kiongozi huyo mstaafu hakupewa hata nafasi ya kuwasalimia wananchi waliokuwa katika mkutano huo licha ya kujipeleka kitendo ambacho hakipaswi kunyamaziwa.

Alisema kutokana na hali hiyo Chama cha Mapinduzi (CCM), kina kazi kubwa ya kutibu majeraha hasa kutokana na baadhi ya viongozi wastaafu wa serikali kutoshirikishwa na hata majina yao kuondolewa katika ratiba za kampeni katika Uchaguzi Mkuu uliopita.

“Mimi bado nitaendelea kuwa mwanachama mwaminifu wa CCM, ila ninatumia uhuru wangu kwa kuionya CCM ni lazima iangalie hali na kujua ni nini kinasababisha kukosekana umoja kwani 2015 tunaweza kujikuta tukiambulia nafasi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar,” alisema Raza.

Alisema ilipoingia serikali ya awamu ya sita visiwani humo ilifika hatua ya kuwanyang’anya magari pamoja na ulinzi baadhi ya viongozi wastaafu waliotangulia kuongoza serikali ya Zanzibar.

Kada huyo, alisema ni lazima viongozi watambue CCM inaongozwa kwa busara na sio mtu na kutoa wito kwa viongozi wa Halmashauri Kuu kuangalia katiba ya chama juu ya umuhimu wa viongozi wastafu wa serikali na nafasi zao.

Raza, ambaye alikuwa mshauri wa masuala ya michezo wa Rais wa Awamu ya Tano, Dk. Salmin Amour, alisema kamwe CCM haiwezi kuzuia upepo wa kisiasa uliopo sasa Zanzibar kama wataendelea kufumbia macho hatua ya kutowapa kipaumbele wastaafu wa serikali hasa waliohudumu katika nafasi ya juu ya urais.

Kuhusu wabunge wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kukacha hotuba ya Rais Jakaya Kikwete, alisema hakuna budi vyama vikakutana na kuzungumza kwa kuhakikisha maslahi ya wananchi yanawekwa mbele.
 
Dhambi ya ubaguzi yaitafuna CCM Zanzibar


Na Emmanuel Kwitema

MFANYABIASHARA maarufu na kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) visiwani Zanzibar, Bw. Mohamed Raza amekitahadharisha chama hicho kuwa kitatoweka visiwani humo endapo hakitarekebisha mapungufu yaliyojitokeza katika Uchaguzi Mkuu wa
Oktoba 2010.

Alisema hayo alipokutana na waandishi wa habari, Dar es Salaam jana wakati akitoa tathmini yake kuwa ushindi wa chama hicho katika uchaguzi huo haukuwa wa kishindo kama walivyotarajia, kwani asilimia 50 na nukta kidogo walizopata ni dalili mbaya.

Alitoa mfano kuwa miaka ya nyuma CCM kilikuwa na majimbo Pemba, sasa hakuna hata moja na pale Zanzibar hivi sasa majimbo manne yamechukuliwa na wapinzani wao na kuongeza kuwa kama chama hakitakuwa wazi kuelezea yaliyojiri, basi Uchaguzi Mkuu ujao wa 2015 kwa upande wa Zanzibar wasishangae majimbo zaidi yakaangukia upinzani kitendo kitakachofanya chama chao kuambulia nafasi ya Makamu wa Kwanza wa Rais.

"Kwa kuwa Uchaguzi Mkuu ujao hauko mbali, basi ni vyema chama kikakaa chini na kufanya tathmini ya kina na kwa uwazi kikihusisha Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya chama hicho ili kurekebisha mapungufu yaliyojitokeza", alisisitiza Bw. Raza.

Bw. Raza alionesha kushangazwa na kutoshirikishwa kwa viongozi wastaafu wa Zanzibar katika mchakato mzima wa uchaguzi. Alisema tangu ufunguzi wa kampeni za uchaguzi visiwani humo hadi kumalizika hakuna kiongozi aliyepewa nafasi kuhutubia mikutano hiyo.

Alisema hata kiongozi aliyepangwa katika ratiba kuhutubia moja ya mikutano hiyo, ratiba hiyo ilifutwa na viongozi wenyewe wa CCM bila sababu za msingi.

Aliutaka uongozi wa chama hicho visiwani humo kuwaeleza wanachama wao kwa nini walifanya hivyo na kusisitiza kuwa viongozi wastaafu wana nafasi zao.Akizungumzia usawa, Bw. Raza aliitaka CCM na SMZ kutenda haki kwa viongozi wote wastaafu, kinyume cha hivyo kitakuwa kinatayarisha na kuunda matabaka ya viongozi hao.

Alisema haoni sababu kwa nini kati ya viongozi hao wastaafu wengine wawe na magari ya kuwaongoza na wengine wasiwe nayo; wengine wapewe magari aina ya benz na wengine wasipewe.Alisisitiza kuwa katika CCM hakuna bwana mkubwa wala umaarufu wa mtu, bali chama wanachokitumikia na kusisitiza kwamba asingetaka kuiona Zanzibar yenye matabaka ya wastaafu na ili kuondokana na hilo katiba ya nchi na sheria zifuatwe katika kuteleza usawa huo.

Awali, Bw. Raza alitoa shukrani na pongezi kwa ushindi wa CCM katika Uchaguzi Mkuu wa 2010 na hasa Zanzibar ambako baadaye kuliundwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa iliyojumuisha Chama cha Wananchi (CUF).Bw. Raza alisema serikali hiyo isibezwe wala kupuuzwa ili kudumisha hali ya amani na utulivu visiwani humo.

 
Ni uamuzi mzuri kuonyesha hisia zake kwa chama.lakini, kama yeye ni mwanachama wa chama cha mapinduzi (ccm) ni vema haya yote angeyatoa kwenye vikao halali vya chama ili kuepuka mgawanyiko kwenye chama.Hapa mimi naona hajaitendea haki CCM.Hli hii inafanana sana na vituko vya Zitto kwa CHADEMA.Nafikiri wanasiasa watanzania wanatakiwa wabadilike na kuelewa wajibu wao kwa vyama vyao na si kuropokaropoka kwenye vyombo vya habari.
 
Back
Top Bottom