Rais Samia Suluhu Hassan, umesahau Watanzania wanaitaka Katiba Mpya au ni hofu tu?

Watanzania gani wanataka katiba mpya? Nayashangaa sana haya yanayotuongelea wengine ambao hatujasema lolote. Rubbish. Katiba hainilishi wala kunivalisha. Sitaki katiba mpya.
Take that, take that!!
 

Attachments

  • twitter_20220322_213810.mp4
    663.1 KB
“Rais Samia Suluhu Hassan, umesahau watanzania wanaitaka katiba mpya au ni hofu tu?”

Katika nchi yoyote, msingi wa uendeshaji wa nchi unategemea Katiba. Katiba ni sheria kuu/sheria mama katika nchi yoyote. Sheria nyingine zote zinategemea au zinatungwa kwa mujibu wa Katiba. Wakati mwingine Katiba hutafsiriwa kuwa ni mkataba wa Kijamii kati ya Viongozi na Wananchi.

KATIBA ni makubaliano ya wananchi kuhusu utaratibu na kanuni za uendeshaji wa mambo mbalimbali katika nchi yao. Katiba ni muafaka wa kitaifa juu ya misingi mikuu ya kuendesha nchi. Anayeweza kupuuza mchakato wa katiba bora ni hawa viumbe wanaotaka kuishi kama wafalme na Sultan

Katiba ni Sheria ya msingi ambayo inaweka mfumo wa uendeshaji wa nchi. Katiba inafanya hivyo kwa kuainisha misingi ya taifa, mgawanyo wa madaraka na majukumu ya mihimili mikuu ya dola, usimamizi wake, mgawanyo na ukomo wa mamlaka ya vyombo mbalimbali vya dola.

Nchi ambazo zimefanya mabadiliko ya katiba, njia kuu zifuatazo huwa zinatumika:
(i) Rais kuanzisha mchakato wa mabadiliko ya kikatiba; (ii) Kuundwa Tume ya kuandaa Katiba kwa kupitia sheria zilizopo; na (iii) Bunge kutunga sheria maalum ya mabadiliko ya Katiba. Tuchague moja.

SSH, huamini tunataka Katiba Mpya?Ulipokuwa makamu mwenyekiti BUNGE la KATIBA, mlifanyia kazi RASIMU ya Jaji WARIOBA. Hukujua ni maoni ya WANANCHI? Kama watanzania hawataki katiba mpya, TUME ya Jaji Warioba iliyatoa wapi MAONI mliyoyafanyia kazi na kuleta KATIBA INAYOPENDEKEZWA?

Najaribu kukurejesha nyuma, tukumbushane masuala kadhaa. Safari ya mchakato wa kupata katiba mpya ya Tanzania ulianza tangu mwaka 2010, wakati Rais wa wakati huo, Jakaya Kikwete alipoamua kuutangazia umma dhamira na nia ya serikali ya kuanzisha mchakato wa kupata katiba mpya.

Baada ya mijadala kadhaa wa kadhaa na makongamano mfululizo ikishirikisha wanazuoni na umma, mchakato wa kuitafuta katiba mpya ukaanza rasmi mwaka 2011 kwa kutungwa kwa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba Na. 83/2011 na baadaye ikatungwa Sheria nyingine ya Kura ya Maoni Na. 11/2013.

Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ilitamka kuanzishwa kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba. Tume ikaundwa na Rais Kikwete, akateua wajumbe kwa kuzingatia makundi mbalimbali. Tume ya mabadiliko ya katiba, mwenyekiti wake akatajwa kuwa ni Jaji Joseph Sinde Warioba.

Tume ya mabadiliko ya katiba chini ya uenyekiti wa Jaji Joseph Sinde Warioba, ikaratibu mchakato wa kukusanya maoni ya wananchi kwa kuzunguka nchi nzima na kuandaa rasimu ya kwanza ya katiba ambayo kupitia uhariri wa Mabaraza ya Katiba ikapatikana Rasimu ya Pili ya Katiba.

Rasimu hii ya pili ya katiba ambayo ni maarufu kama ‘Rasimu ya Warioba’ ikawasilishwa kwenye Bunge Maalum la Katiba (BMK) ambalo kwa kiasi kikubwa lilikuwa na wajumbe wengi kutoka Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na wajumbe wa Baraza la Wawakilishi -Zanzibar.

Pia, kama ilivyotajwa na sheria ya mabadiliko ya katiba, Rais Jakaya Kikwete akateua wajumbe wengine (201) kwa namna ilivyoelekezwa, kuungana na wajumbe wengine ambao walikuwa wabunge wa bunge la Jamhuri ya muungano wa Tanzania na baraza la wawakilishi (Zanzibar).

Wajumbe kutoka katika kundi la wateule wa Rais walijulikana kama “kundi la mia mbili na moja”. wajumbe wanawake ni 100 na wanaume 101. vyama vya siasa vyenye usajili wa kudumu 21, jumla ya wajumbe 42 wakateuliwa. Hivyo kulikuwa na uwakilishi wa kila sekta. Rais SSH hakumbuki?

Uteuzi wa Wajumbe wa Bunge la Katiba ulitokana na Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Sura, 83 (The Constitutional Review Act, Cap 83). Sheria hii inaweka mamlaka ya uteuzi, masharti, taratibu, vigezo na mambo mengine yote yanayopaswa kuzingatiwa katika uteuzi wa Wajumbe wa Bunge la Katiba.

Sheria inatamka aina 3 za Wajumbe wa Bunge la Katiba kama ifuatavyo:- (i) Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano; (ii) Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar; na (iii) Wajumbe 201 kwa mujibu wa Kifungu Na. 22(1c) cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ambayo inaonyesha makundi mbalimbali 10 yanayohusika.

(i) Taasisi zisizokuwa za Kiserikali (20); Taasisi za Kidini (20); Vyama vyote vya Siasa vyenye Usajili wa Kudumu (42); Taasisi za Elimu (20); Watu wenye Ulemavu (20); Vyama vya Wafanyakazi (19); Vyama vinavyowakilisha Wafugaji (10); Vyama vinavyowakilisha wavuvi (10); Vyama vya Wakulima (20); Vikundi vya Watu wenye Malengo yanayofanana (20).

Rasimu ya Katiba ni miongoni mwa Nyaraka zilizoambatanishwa katika taarifa ya Tume kuhusu Mchakato wa Mabadiliko ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania waliyokabidhiwa wajumbe na Rais tarehe 30 Desemba, 2013 ikiambatana na nyaraka nyingine, nitazitaja;

(a) Taarifa ya Maoni ya Wananchi kuhusu Mabadiliko ya Katiba. Taarifa hii ina maoni ya Wananchi kuhusu maeneo mbalimbali ya kikatiba ambayo ndio msingi wa uandishi wa Rasimu ya Katiba;

(b) Taarifa ya Mabaraza ya Katiba ambayo inaainisha maoni ya Wananchi kuhusu Ibara zilizokuwemo katika Toleo la Kwanza la Rasimu ya Katiba na jinsi zilivyofanyiwa kazi;

(c) Taarifa ya maoni ya Wananchi kuhusu Sera, Sheria na Utekelezaji. Taarifa hii ina maoni ya wananchi kuhusu mambo ambayo yalihitaji kufanyiwa uamuzi wa kisera, kutunga au kurekebisha sheria zilizopo au utekelezaji wa kiutendaji;

(d) Taarifa ya Utafiti Kuhusu Masuala Mbalimbali ya Kikatiba, ambayo ilikuwa na taarifa nne ambazo ni:

(i) Utafiti Kuhusu Madaraka ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; (ii) Utafiti Kuhusu Maadili ya Viongozi na Uwajibikaji; (iii) Utafiti Kuhusu Masuala Yanayohusu Muungano wa Tanganyika na Zanzibar; na (iv) Ushauri Elekezi Kuhusu Mifumo ya Uchaguzi na Tume ya Uchaguzi, Tanzania (Final Report on the Review of Various Aspects of Electoral Systems and the Electoral Commission in Tanzania).

(e) Taarifa ya Takwimu za Ukusanyaji wa maoni ya Wananchi ambayo iliainisha maeneo makuu yaliyotolewa maoni, jinsi, elimu na kazi za watoaji maoni; na

(f) Viambatisho vya taarifa ambavyo viliainisha hatua mbalimbali za mchakato, uamuzi, hotuba za viongozi na miongozo mbalimbali iliyotolewa na Tume.

4. Taarifa ya Tume na baadhi ya Taarifa ziligawiwa kwa kila Mjumbe na Taarifa nyingine ziliwekwa katika Maktaba ya Bunge ili kuwawezesha Wajumbe kufanya marejeo.

Tume iliamini kwamba Taarifa zilizowasilishwa pamoja na maelezo hayo zingewasaidia Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba kujadili na kufanya uamuzi sahihi kwa kila Ibara iliyopendekezwa katika rasimu ile katiba kwa kuzingatia maslahi ya wananchi na Taifa kwa jumla.

Bunge Katiba, ambalo Makamu Mweyekiti wake alikua Samia Suluhu, ambaye ni ndiye Rais wa Tanzania kwa sasa, ndiko joto na mivutano mikali kuhusu masuala kadhaa yaliyomo kwenye katiba ilipoanzia. Baadhi ya wajumbe wa bunge hilo kutoka upinzani waliamua kujitoa na kususia mchakato.

Kwanini walisusia? Yapo masuala ya msingi karibu 70 yaliyokuwa maoni ya wananchi, yaliondolewa kiubabe kwa shinikizo la wajumbe wengi waliokuwa wanaunga mkono upande wa serikali ya Jakaya Kikwete na chama cha Mapinduzi (CCM). Wajumbe wengine wakagoma kuwa sehemu yake.

Wajumbe waliobaki (wengi wakiwa wabunge wa CCM na wajumbe wenye mrengo huo) waliendela na ikapatikana Katiba pendekezwa ambayo wengi waliiona kama imekosa muafaka na maridhiano ambayo yanaonekana kama ndio msingi wa kupata Katiba bora ya kitaifa yenye kukubalika na wengi.

Rais SSH alikuwa Makamu mwenyekiti wa Bunge la Katiba, lililochakata rasimu ya katiba (rasimu ya Warioba) na kupatikana Katiba pendekezwa kwa mujibu wa Sheria ya Kura ya Maoni na Maelekezo ya Tume ya Uchaguzi (NEC), zoezi la kura ya maoni lilipaswa kufanyika tarehe 30 Aprili 2015.

Mchakato wa kuitafuta katiba mpya ukaishia hapo, ikapatikana ‘katiba inayopendekezwa’ ambayo ipo katika kabati lisilojulikana, na hii ilikuwa mwaka 2014, na mpaka leo kumekuwa na mkwamo usiojulikana ni lini utakoma. Na sasa zimeamka kelele upya za kuitaka katiba mpya, mpya kweli.

Wakati wote huo, Samia Suluhu Hassan, ambaye sasa ni Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, ndiye aliyekuwa makamu mwenyekiti wa bunge maalum la katiba (BMK), na aliongoza wajumbe kufanyia kazi maoni ya wananchi yaliyowasilishwa bungeni na Jaji Warioba.

SSH anafahamu kinagaubaga mchakato huo, yakiwepo masuala yaliyoleta mijadala mikubwa BMK aliloliongoza mwenyekiti marehemu Samuel Sitta. Mchakato wa kuendelea/kutoendelea na mchakato wa Katiba utasalia kuwa jambo litakalozunguka kichwani kwake kwa muda wote atakaokuwa madarakani.

Sasa tukisikia SSH anasema wananchi hawataki katiba mpya, anatusikitisha wengi ambao tulikuwa watu timamu na tulitoa maoni yetu wakati ule, kwa njia ya maandishi na kwa njia ya mdomo. Sisi ndiyo wananchi wenyewe. Na wananchi walisema wanataka katiba mpya kabla ya 2015.

Zipo sababu nyingi za msingi za kwa nini nchi yetu inatakiwa kuandika upya Katiba yake, moja kubwa ni kupitwa kwa baadhi ya mambo ambayo hayaonekani kwenda na wakati wa sasa wa wananchi husika, lakini pia kujitokeza masuala ambayo yanahitaji kuwekewa misingi ya kikatiba.

Katiba iliyopo haijaweka misingi mingi haswaa ya haki za kiraia, uhuru wa watu, uwajibikaji, uchumi, misingi ya utumishi wa umma, udhibiti wa rasilimali za taifa, muundo wa uchaguzi, utawala bora wa sheria na masuala mengi ambayo watu wengi wanaendelea kufafanua.

Uchumi na Katiba bora ni kama ndugu wanaoendana, ukitaka kuwa na uchumi bora inakupaswa uwe na Katiba bora itakayoleta utulivu, itakayovutia wawekezaji na itakayosimamia mamlaka na rasimili mali za nchi. Sasa twende tukaipate katiba mpya, yenye ubora, tuweke hayo ndani yake.

Katiba ya sasa ya Tanzania ina umri wa karibu miaka 45 sasa, ilitungwa mwaka mwaka 1977. Kwa sababu Katiba hii na katiba zote tano zilizopita tangu katiba ya uhuru ya mwaka 1961, 1962, 1964, 1965 mpaka katiba ya kudumu ya mwaka 1977, na imefanyiwa marekebisho makubwa mara 14

Kumekuwa na malalamiko kwamba wananchi hawakushirikishwa kikamilifu kuzitunga katiba hizo zote 5, wakati zinahusu maisha yao. Huo ni ukweli. Hivyo 2011-2014 ukaundwa mfumo ambao ungeruhusu ushiriki wa wananchi katika kupata katiba bora ambao uliharibiwa na watawala.

KATIBA Mpya ni hitaji la lazima kwa sasa. Katiba ya nchi yetu ni waraka wa maridhiano na muafaka wa kisheria, kisiasa, kijamii, kiuchumi na kiutawala juu ya namna wanavyotaka nchi yao iongozwe na siyo itawaliwe. Katiba iliyopo haizalishi viongozi, bali watawala na wafalme.

Katiba bora ni msingi imara wa maendeleo endelevu ya watu. KATIBA bora inatakiwa kuweka msingi wa kiuchumi ambao ni shirikishi na unaoendana na wakati. Rais SSH, naendelea kusisitiza, bila Katiba mpya, siyo mpya tu, katiba mpya bora, hutaweza kujenga uchumi imara wa Tanzania.

Katiba ya sasa iliundwa wakati wa mfumo wa chama kimoja (baada ya serikali ya Mwl, Nyerere mwaka 1962 kuelekea 1963) kufuta mfumo wa siasa za vyama vingi baada ya safari yake ya China, akarejea na falsafa baadhi za rafiki yake, Mao Tse Tung. Akatoa tamko haramu.

lakini sasa nchi iko kwenye mfumo wa vyama vingi, katiba ya mwaka 1977 haiwezi kuwa muafaka wa kitaifa wa vyama vingi, kwa sababu ilisimamia misingi ya muafaka wa chama kimoja, CCM wakati huo, na hata msingi wake, katiba hiyo ya mwaka 1977, ulitengenezwa hivyo.

Ingawa, nafasi ya mamlaka ya chama (CCM) sheria ya 1984, Na. 15 ilitungwa wakati wa chama kimoja, [Ibara ya 10 ya katiba imefutwa na sheria Na.4 ya 1992]. Maana yake? CCM si mamlaka ya nchi tena, mwaka 1992 kikatajwa kuwa chama cha siasa (ingawa kimejinasibisha na dola sasa)

Lakini sasa kuna misingi ya vyama vingi, kuna mahitaji mapya ya kisiasa, kuna fikra mpya za kufanya siasa, mazingira mapya ya kisiasa na zipo changamoto mpya. Ni ngumu sana katiba ya mwaka 1977 kubeba taswira ya kimantiki ya mwaka 2022. Hizo ni sababu za msingi pia.

Kwa mantiki hiyo ili kuleta muafaka wa kitaifa, katiba mpya itakayopatikana inapaswa kuwa ndiyo medani ya kuleta muafaka wa kitaifa. Siyo porojo hizi za kuunda vikosi kazi za kulipana posho ili kubeba agenda za dola na watawala. Huo siyo muafaka wa kitaifa. Haukubaliki.

Rais SSH, kauli yako ya July 2021 “Nipeni muda tuimarishe uchumi kwanza kisha tuyashughulikie mambo ya katiba na mengine ya siasa” haikubaliki, tuliikata, kama ambavyo sasa tunaikataa kauli yako ya “wanaotaka KATIBA mpya ni watu wa mitandaoni”. Tunaikataa kwa sauti kubwa.

Je mchakato wa KATIBA mpya uanze upya kabisa? Kama utaanza upya mzigo wa gharama ataubeba nani? Je mchakato uanzie alipoishia Jaji Warioba, kwa kuileta rasimu ya Katiba na kuunda Bunge jipya la Katiba ili kuichakata na kupatikana upya kwa Katiba Pendekezwa?

Au mchakato uanzie lilipoishia Bunge maalumu la Katiba (BMK) alilolongoza Rais SSH (akiwa makamu mwenyekiti) na mwenyekiti wake Samuel Sitta, kwa kuitisha tu zoezi la kura ya maoni ili kuipigia kura Katiba pendekezwa iliyopendekezwa na bunge hilo mwaka 2014? Hayo yanajadilika!

Tanzania tunayo sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Sura ya 83, imeanzisha Tume ya Mabadiliko ya Katiba, ikaweka Hadidu za Rejea na kuipa Tume jukumu la kuratibu, kukusanya maoni ya wananchi, kuchambua na kutathmini maoni na kuandaa Ripoti na Rasimu ya Katiba.

Baadaye wananchi, kupitia Mabaraza ya Katiba, walipewa fursa tena ya kutoa maoni yao kabla ya Tume kufanya maboresho na kuiwasilisha rasimu ya katiba (rasimu ya Warioba) katika Bunge Maalum la Katiba; hatua ambayo tunaweza kuanza nayo bila kurejea mchakato wenye gharama.

Kama tukikubaliana kuanzia hapo, Baada ya Bunge Maalum kutoa Katiba inayopendekezwa, wananchi watapata fursa ya kufanya uamuzi wa mwisho kuhusu Katiba Mpya kupitia kura ya maoni, ilivyoelekezwa na Sheria ya Kura ya Maoni Na. 11 ya mwaka 2013.

Lakini kama yapo malalamiko ta wananchi kwamba mchakato wa awali haukuwa shirikishi, tunaweza kufanya masuala kadhaa ambayo LAZIMA tuafikiane kwa pamoja namna sahihi ya kuyafanya na kuyafikia, siyo kwa kauli ya dola au kuwatumia ‘vishoka’ ambao ni bendera za watawala

Mjadala wa kujenga muafaka wa kitaifa unapaswa kuutangulia mchakato wa kisheria wa kutunga katiba mpya. Mjadala wa Kitaifa ndio utakaoainisha: wigo wa uwakilishi wa makundi mbalimbali; sifa za wajumbe wa mkutano wa kitaifa wa katiba na kazi zake;

Sifa za wajumbe wa tume huru ya mabadiliko ya katiba na hadidu za rejea za tume hiyo ya mabadiliko ya katiba; sifa za wajumbe wa Bunge maalum la Katiba, muundo na kazi zake; na utaratibu wa kuandaa na kusimamia kura ya maoni baada ya uchambuzi wa maoni kukamilika.

Sasa, Ili huo mjadala uwe na tija, wananchi wanahitaji muda wa kutosha wa kujadiliana kwa namna zao na kukubaliana kwanza juu ya dira, misingi ya kisiasa na kiuchumi na maadili ya taifa lao. Sasa ni wajibu wa serikali kuacha kupiga marufuku mikutano ya hadhara na makongamano

Kazi ya kuandaa na kuratibu mjadala wa kitaifa inapaswa kufanywa na chombo huru kinachoundwa na wataalamu wenye misimamo thabiti (inayotambulika) na sio vyombo au taasisi za dola au hawa ‘vishoka’ hawa waliounda hiki tunachokiona na wamejiita ‘kikosi kazi’. Haipaswi kuwa hivyo.

Tungelikuwa na bunge linaloeleweka (siyo huu mkutano wa CCM), tungelitaka kutimiza wajibu wake wa kikatiba wa kuishauri serikali juu ya namna sahihi ya kuandaa na kuratibu mjadala wa kitaifa, wananchi wote waweze kushiriki kwa amani,utulivu na kuvumiliana.

Tungelikuwa na bunge (linalotokana na wananchi) lingepaswa pia kushirikiana na serikali katika kuweka mazingira muafaka ya kisiasa na kisheria ili mchakato wa kutunga katiba ukamilike kwa mujibu wa matarajio ya watanzania wote. Lakini hatuna bunge, tunao wanachama wa CCM bungeni

Ingawa, kuendelea kwa mchakato kwa kupigia kura katiba inayopendekezwa siyo sawa, haitokani na maoni ya wananchi, mambo kadhaa muhimu na yaliyopendekezwa na wananchi wengi yaliondolewa ama kubadilishwa kupitia Bunge maalumu la Katiba ambalo lilisusiwa na wajumbe wengine

Binafsi naamini,hakuna mshindi katika mchakato wa Katiba Mpya, hivyo hakuna maana watu wakavutana kiasi cha kutaka kuuathiri lolote linaloweza kuleta mchakato huo mezani tena, ambao awali umetumia mabilioni ya shilingi na ukaishia njiani bila kupata tulichohitaji.

Tuafikiane juu ya mfumo wa kuratibu mjadala wa kitaifa utakaoweka misingi ya kisiasa na kisheria ya kutunga katiba mpya. Tuafikiane juu ya muda wa mchakato wa kutunga katiba. Lakini siyo kupitia ‘vishoka’ hawa ambao wamebeba maslahi ya dola wanajiita ‘kikosi kazi’

Twende tuafikiane namna ya kutoa elimu kwa wananchi wote ili waweze kushiriki ipasavyo katika mchakato wa kutunga katiba. Bila kuanza kusema wanaotaka katiba mpya ni watu wa mitandaoni. Hao ni watanzania pia. Na takwimu za mwaka 2016 zinaeleza ni milioni 20, wapo mitandaoni.

Rais SSH, sasa lazima uone namna nzuri ya kushirikiana kuweka mazingira muafaka ya kisiasa yatakayowezesha wananchi wote kushiriki katika mchakato wa kutunga katiba mpya bila hofu au kuburuzwa na kundi la watu au taasisi yoyote au serikali. Katiba ni agenda ya wananchi.

Hivyo, Rais SSH, hili la KATIBA mpya, bora linasalia kuwa na karata yako muhimu ya turufu ya ama kufufua mchakato wa katiba ama kuuzika kabisa, hupaswi kupuuza kelele za ‘tunaitaka katiba mpya’ maana zina mantiki, zisikilize. Nafahamu, wafilisti hawataki katiba mpya.

MMM, Martin Maranja Masese
 
Ni hofu aliyonayo na mipango aliyojiwekea kuelekea 2025 hasa baada ya kusema 2025 ni zamu ya wanawake kumuweka mtu wao.

Alianza kwa kuwashughulikia aliohisi ni wapinzani wake ndani ya baraza lake la mawaziri, akawatosa kina Lukuvi na Kabudi kijanja, na kuwajaza watoto wa marafiki zake kwa kisingizio ndio timu yake ana imani nao watafanya kazi vizuri.

Baada ya hapo naamini anajua kikwazo kitachofuata kwake ni Katiba Mpya hasa ile rasimu ya Warioba, CCM wanajua fika hawakubaliki Tanzania hii wanachotegemea ni kuiba kura kwa kuwatumia polisi na Tume ya uchaguzi.

Hivyo lazima afanye kila awezalo kwa usalama wake kuelekea 2025, ndio maana sasa unawasikia Samia na ile tume yake feki ya kina Mukandala wanakwambia mchakato wa Katiba Mpya uanze baada ya 2025, hii maana yake wanataka angalau waibe kura kwa mara ya mwisho 2025 ili Samia arudi ikulu.

Heri angeacha mchakato wa katiba mpya ufuate mkondo wake.

Hataweza kuuzuia na utamgharimu.
 
Watanzania gani wanataka katiba mpya? Nayashangaa sana haya yanayotuongelea wengine ambao hatujasema lolote. Rubbish. Katiba hainilishi wala kunivalisha. Sitaki katiba mpya.
Watanzania wa upande wa bara ndiyo wanataka katiba mpya ili wazidi kuwaburuza Wazanzibari.
 
Akili yako haina akili kabisa kabisa. Unawaza kula tu kizazi cha hovyo.
Heshimu mawazo yangu vinginevyo wewe ni dikteta zaidi ya magufuli. Mkipata madaraka mtatopoteza akina saa nane wengi zaidi. Sitaki katiba mpya movement.
 
Ni sahihi. Hata mchakato wa 2011 hadi 2014 watu aina yako tulikuwa nao JF na kwingineko… hata 1992 wapo ambao hawakutaka kuona mfumo wa vyama vingi ukirejea. Ni bahati nzuri watu aina yenu tunafahanu lazima mtakuwepo na hamtazuia lolote kama dhamira za dhati za upatikanaji katiba mpya zitakuwepo. Tunapambana tukifahamu, wapo watu aina yako, na hata hakuna unachonufaika nacho isipokuwa upo kwenye denial status!
Umempa majibu ambayo hatokuja kusahau
 
Katiba Mpya ni sasa.
Anayeona sio sasa litamgarimu kwani tukumbuke Mzee Sitta alianza kuwazihaki viongozi wa Dini na wale waliokuwa tofauti ya mtazamo kwa hiyo tujitahidi kupima upepo unavyovuma la sivyo tupo nje ya muda na wakati.
 
Ni sahihi. Hata mchakato wa 2011 hadi 2014 watu aina yako tulikuwa nao JF na kwingineko… hata 1992 wapo ambao hawakutaka kuona mfumo wa vyama vingi ukirejea. Ni bahati nzuri watu aina yenu tunafahanu lazima mtakuwepo na hamtazuia lolote kama dhamira za dhati za upatikanaji katiba mpya zitakuwepo. Tunapambana tukifahamu, wapo watu aina yako, na hata hakuna unachonufaika nacho isipokuwa upo kwenye denial status!
Kaka acha kujidanganya hamna Kiongozi katika ndani ya hii Nchi anaweza badilisha Katiba ambayo anaona ina mfeva kwa 100%.Mwl.Nyerere na uzalendo wake wote alifahamu katiba ni mbovu na alikuwa na uwezo wa kubadili katika kipindi chake hakufanya hivyo.

Kama watu wanaona Katiba mpya itasaidia kutatua changamoto-kitu ambacho ni kweli ni lazima kuwalazimisha watawala kwa njia yoyote ile,hakuna mtawala atakuletea Katiba kwa maneno organise Wananchi kila Mkoa kila siku kukicha kukizama maengezi yawe ni Katiba (hapa damu zitamwagika ,watu watakufa maelf na maelf ndipo Katiba itapatikana).

Hii ya kuandika na maneno pasipo action yoyote ya kushinikiza utaandika mpaka siku unakwenda Mbinguni na Katiba mpya haitapatikana.
 
Back
Top Bottom