Rais ni jalala, kama sivyo, taka zende wapi?

Dotto C. Rangimoto

JF-Expert Member
Nov 22, 2012
1,985
1,282
maguuu.jpg


Kama admin wa page hii nasikitika kwa Tundu Lissu kuwekwa Rumande kwa kutokana kauli zake, lakini nasikitika zaidi na lugha zinazo tumika kumkosoa rais.

Rais kama mzazi anakosoleka na haiwezi kuwa kosa kumkosoa rais, lakini tunatumia lugha gani sasa? Unapo mkosoa baba au mama yako kwa vyovyote vile huwezi kutumia lugha ya kuudhi na yenye kuashiria dharau.

Ukitumia lugha ya dharau au ya kuudhi mkosolewa hatashughulishwa na makosa uliyo yaona na kuyabainisha, bali ataanza kushughulishwa na dharau zako dhidi yake, maudhi yako dhidi yake, na ndicho kilichotokea kwa Lissu, serikali inashughulishwa na dharau za Lissu dhidi ya rais na si hoja nzito yenye mashiko ya Lissu ilobebwa na lugha ya kuudhi.

HATAHIVYO
Rais wetu ajue yeye ndio baba wa watanzania wote, ambao miongoni mwetu tuko watu wa hulka mbalimbali, na kwasababu hiyo ndio maana ikasemwa mkubwa jalala, hata kama likijaa, litapakuliwa na kuendelea kutumika tena.

Rais wetu lazima baadhi ya mambo afuate nyayo za mtangulizi wake, Dkt Kikwete. Alitake jeshi la Polis lisihangaike na watu wanao mtukana na kumkashifu, bali jeshi lihangaike zaidi na wahalifu wengine kama majambazi, akaunti fake kwa majina ya watu maarufu zinazo tumika kutapeli, nk

Rais wetu akubali kupokea matusi, kashfa, na lugha za kuudhi kama vile anavyo pokea pongezi na sifa. Matusi ni jinai lakini rais kama baba, hana budi kuyapokea, na kwake yeye yawe chachu ya kumfanya awajibike zaidi ili wale watukanaji waone ni kwa namna gani wamemkosea lakini kubwa umma uone kwa jinsi gani rais wetu anaonewa.

Hata hili la kufanya mikutano ya kisiasa na mambo ya kufananayo, pia lazima rais aige kwa mtangulizi wake. Maandamano na mikutano ni haki ya kikatiba, lakini itakuwa vurugu kama watu wataamua kila wiki kuandamana, au nchi nzima kuandamana au kila siku kutwa zima makongamano na mikutano ya kisiasa.

Lakini pia haikubaliki haki hiyo kwa upande wa wanasiasa waipate mwaka mmoja kwa kila miaka mitano, tena mwaka wenyewe uwe mwaka wa uchaguzi kwa miezi ya uchaguzi tu! HAIKUBALIKI.

Lazima rais azungumze na vyama vya siasa wakubaliane namna ya kuliendea suala hili, ili watu wasinyimwe haki yao ya kikatiba lakini pia rais asikwamishwe juhudi zake za maendeleo. Sababu maandamano na mikutano inahitaji watu, lakini pia maendeleo yanahitaji watu, sasa vyama vya siasa na serikali wakae wakubaliane utaratibu.

SISHANGAI RAIS KUTUKANWA.

Narejea kusema rais ni jalala, achape kazi, wanao tukana na watukane, wanao kashifu na wakashifu, lakini mwishowe hulala na siku huendelea. Na kwasababu hiyo mimi sishangai rais kutukanwa nashangaa hatua wanazo chukuliwa watukanaji.

Mosi
Viongozi wakubwa katika nchi mbalimbali hupuuza watu wanao watukana na kuwakashifu. Sababu wanajua madaraka ya kuwa juu kuliko watu wote katika nchi yahitaji uvumilivu. Usipokuwa mvumilivu, ulio washinda katika uchaguzi watakutoa katika reli sahihi uliyopanga kuitumia.

Pili.
Hivi mathalani katika mitandao anayetukanwa ni rais tu? Mbona tunaona matusi na kashfa kwa viongozi wa upinzani? Mbona watu maarufu nchini wanatukanwa sana kama ukifuatilia mitandao? Kwakuwa wanajua umaarufu una gharama, na gharama yake kubwa ni kashfa na matusi, na kwa kulijua hilo ndio maana hawaripoti polis wala hawafungui kesi.

Sasa nashangaa mtu maarufu kuliko wote nchini, mtu mkubwa kuliko wote, mtu ambaye angepaswa kuvumilia matusi na kashfa kuliko watu wote nchini ndiye mtu anayeteswa na matusi na kashfa. Mwenzenu nashangaa.

MWISHO.
Wote mnaosoma andiko hili, na mtumiaji wa mtandao, kabla ya kuposti kitu kinacho mtaja rais Magufuli, kisome mara tatu na ikibidi kwanza mtumie rafiki yako inbox akipitie, ukijiridhisha kiko sawa ndio uposti.

Lakini kama post yako inamtaja Lowassa, usipate tabu ya kuhariri wala kujiuliza kama hili tusi kwa Lowassa au sio, sababu kwanza Polis hawafuatilii kama Lowassa na wapinzani wanatukanwa.

Pili, Lowassa mvumilivu, ukimtukana hata kujibu na wote mashahidi, CHADEMA walimtukana Lowassa kwa miaka isiyopungua nane. Gazeti la Mwanahalisi lilimtukana sana Lowassa lakini sasa hivi CHADEMA na bosi wa mwanahalisi wanafanya kazi pamoja.

Mikutano ya CCM ya kampeni hasa ya Mwanza, kupitia utenzi na kupitia hotuba za baadhi wa viongozi wa CCM Lowassa alitukanwa, Lowassa alikashifiwa, lakini mzee wa watu hakuwajibu zaidi ya kumshukuru MUNGU.

Tangu Lowassa atukanwe na akashifiwe, kama matusi yangekuwa mkuki basi Lowassa yupo kaburini siku nyingi sana. Anajua matusi hayachubui, anajua hayatii joto, anajua umaarufu una gharama, ndio maana HAJIBU TUSI KWA TUSI, Ukimya siku zote ndio jibu la Lowassa na katika hili yeye na Dkt Kikwete mwalimu wao mmoja. Atukanaye hana dhara midhali hana mawe mkononi.

SIASA MJUE NJIA, MAAMUZI KUFIKIA.

Nimezama mwituni, kumtafuta mnyama,
Mwenye nguvu duniani, leo na kesho kiama,
Atajwa msikitini, kanisani wa msema,
Haliwi jambo mwituni, bila ya huyo mnyama.
Siasa mjue njia, maamuzi kufikia.

Naanzia shuleni, watoto wanaposoma,
Wanao soma vyuoni, na shahada za heshima,
Ngumbaru ipo kundini, unyago akina mama,
Elimu yetu nchini, huongozwa na mnyama.
Siasa mjue njia, maamuzi kufikia.

Uende sipitalini, na walipo wakulima,
Kwenye sekta ya madini, na kwa wapiga ngoma,
Utalii wa mbugani, uchezaji wa sinema,
Kote huko tambueni, mratibu ni mnyama.
Siasa mjue njia, maamuzi kufikia.

Siasa ndio mnyama, Lutumbo katuambia,
Siasa ni kitu chema, katika yetu dunia,
Siasa njia ya umma, maamuzi kufikia,
Siasa si kama sima, bali maji nawaambia.
Siasa mjue njia, maamuzi kufikia.

Siasa kitu lazima, katu huwezi kimbia,
Waweza ikacha sima, maji huwezi susia,
Hata ngazi ya boma, siasa waitumia,
Siasa ukiitema, jua umeangamia.
Siasa mjue njia, maamuzi kufikia.

Kuna siasa ya chama, kimwe kwa wote raia,
Kila shauri la umma, chama hujiamulia,
Bunge huwa maamuma, muhuri hushikilia,
Jambo lipite kwa Chama, bunge lalishadidia.
Siasa mjue njia, maamuzi kufikia.

Zipo za demokrasia, vyama vingi hutumia,
Mfano za Tanzania, na uingereza pia,
Vyama hushindania, magogoni kuingia,
Rais kwa Tanzania, waziri kwa malikia
Siasa mjue njia, maamuzi kufikia.

Siasa ndani ya vyama, huko hazikuanzia,
Ilianza toka zama, kabla ya hino dunia,
Furkani nimeisoma, sikuiacha biblia,
Malaika na Karima, pia wanaitumia,
Siasa mjue njia, maamuzi kufikia.

Siasa za huko ahera, kiongozi ni Jalia,
Huongoza msafara, waja wakafuatia,
Mwenye kufanya harara, jeuri akajitia,
Atakuwa ni asira, wa shetani nawambia.
Siasa mjue njia, maamuzi kufikia.

Muumba ndio kinara, wa mbinguni na dunia,
Maisha huyachora, na njia hutupangia,
Hupata njema ijara, mwenye kumsujudia,
Hupata kubwa hasara, mwenye kupuuzia.
Siasa mjue njia, maamuzi kufikia.

Nani alipiga kura? Munguwe kumchagua,
Mjibu pasi kufura, kweli mpate ijua,
Hapana si masihara, si punde mtagundua,
Tena sifanye papara, siasa kuchambua.
Siasa mjue njia, maamuzi kufikia.

Siasa za kifalme, mfano za Saudia,
Mwana hasa wa kiume, kiti ndio hukalia,
Koo iloshika kome, dola huishikilia,
Mfalme ndio sime, na pia huwa pazia.
Siasa mjue njia, maamuzi kufikia.

Zipo za kidikteta, kama zile za Mobutu,
Wengine panga hufuta, pia wapo wa mtutu,
Umma wote hufyata, mbele ya miungu watu,
Kila mwenye kutukuta, ni mbwa mbele ya chatu.
Siasa mjue njia, maamuzi kufikia.

Dikteta awe katili, mbona mtaumwa sana,
Siombe awe jahili, mtapoteza amana,
Tena akiwa bahili, wananchi hukondeana,
Kiongozi bahaluli, asiaminiwe tena.
Siasa mjue njia, maamuzi kufikia.

Samaki awape nyoka, mkate awape mawe,
Nani kashindwa ondoka, kisa halina mauwe?
Ya msingi wanataka, viongozi waelewe,
Wakichoka kuboboka, watawapopoa mawe.
Siasa mjue njia, maamuzi kufikia.

Dikteta awe rahimu, ndipo mtanufaika,
Rasini awe timamu, na tena mshaurika,
Mtakula keki tamu, mafurushi mtashika,
Libya imaamumu, Gaddafi yamkumbuka,
Siasa mjue njia, maamuzi kufikia.

Nikitazama chupani, sioni kitu jamani,
Wino wangu wa thamani, ya manjano zafarani,
Niko mengi rasini, wino umetufitini,
Mwenye nao sinihini, anifae si utani,
Mmeshindwa nidhamini, ujiti naweka chini.

Ahsanten kwa kuwa pamoja.

Dotto Chamchua Rangimoto (Njano5)
Call/whatspp 0622845394
Morogoro Tanzania.
 
Back
Top Bottom