Rais Mwinyi akimuwakilisha Rais Samia nchini Angola

Ojuolegbha

JF-Expert Member
Sep 6, 2020
722
471
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, akimwakilisha Rais Samia Suluhu Hassan, leo Alhamisi tarehe 15 Septemba, amejumuika na viongozi mbalimbali wa Afrika na wengine kutoka nje ya Afrika, katika sherehe za kuapishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Angola Mhe. Joao Manuel Gonclaves Lourenco, pamoja na Makamu wake wa Rais Mwanamama Esperanca Maria Eduardo Franscisco da Costa.

Viongozi hao wawili wa Angola waliapishwa na Rais wa Mahakama ya Katiba ya Angola Laurinda Cardoso.

Katika hotuba yake mara tu baada ya kuapishwa Rais huyo wa Angola Joao Manuel alieleza maeneo mbalimbali ya vipaumbele katika Kipindi hichi cha pili cha uongozi wake kwa kuendeleza mambo mbalimbali ambayo tayari ameshayaanza katika awamu yake ya mwanzo ya uongozi wa Taifa hilo.

Vile vile amegusia Sekta ya mafuta na Gesi, Ujenzi wa miundo mbinu, Huduma za jamii ikiwemo Afya, Elimu na Maji na kuelezea dhamira yake ya kupambana na vitendo rushwa na ubadhirifu wa Mali ya Umma.

Akigusia katika masuala ya kidiplomasia alisema atahakikisha anashirikiana na mataifa barani Afrika katika kukuza Uchumi pamoja na kuendeleza hali ya Amani na Utulivu.

Mbali na Rais Dk. Mwinyi, Viongozi mbalimbali kutoka mataifa Hamsini walihudhuria wakiwemo Marais kutoka Namibia, Guinea ya Ikweta, Cape Verde, DRC, Sao Tome, Zambia, Hispania, Ureno, Guinea-Bissau, Zimbabwe, Burundi, Kenya, Uganda, Malawi, Afrika Kusini na Msumbiji.

Rais Joao Manuel Goncalves Lourenco amechaguliwa kwa muhula wa pili katika uchaguzi ambao chama cha upinzani cha UNITA kilipinga matokeo na kupeleka kesi mahakamani ambayo Mahakama Kuu ya Angola iliitupilia mbali. Sherehe hizo zilifanyika katika uwanja wa wazi wa Praca da Republica Square na kupambwa na gwarida la vikosi vya ulinzi na usalama vya Angola. Jiji la Luanda lipo katika Ulinzi mkali wa wanajeshi na hali imekuwa tulivu kwa vile leo ni siku ya mapumziko.
IMG-20220915-WA0057.jpg
 
Back
Top Bottom