RAI: Vipimo 12 kwa mbunge ‘feki’; Makala- Mbunge safi, mwajibikaji, mwadilifu na asiyenunua ubunge

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
*Rai inatueleza jinsi ya kumuona Mbunge ni feki au safi anayependa nchi yake kwa moyo zaidi - miaka ya nyuma makala zao zilikuwa za kubeba mafisadi - this is a big U-TURN


Na Joseph Sabinus



BAADA ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 31, mwaka jana, sasa tunazungumzia matunda ya uchaguzi kama ni machungu, au ni matamu kama jamii ilivyotarajia maana watu hawapendi mti na mara nyingi wanapenda matunda.

Miongoni mwa matunda ya Uchaguzi Mkuu uliopita, ni wabunge tulio nao sasa katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Uchaguzi huo, umewapa Watanzania wawakilishi mbalimbali wakiwamo madiwani, wabunge na Rais.

Makala haya, yatajikita katika kuionyesha jamii ili kila mtu mwenyewe apime kuwa kura yake imezaa tunda tamu, au tunda chungu kwa kumpata mbunge ambaye ni mzigo.
Hapa, nitazitaja sifa au vipimo 12 kwa mujibu wa watu mbalimbali, ambavyo humpambanua mbunge safi miongoni mwa wabunge “mizigo”.

Uhusiano uliopo baina ya jimbo na taifa ni sawa na ule wa Mungu na Yesu aliyesema, “… Anionaye, amemuona Mungu.” “Mtu hawezi kufika kwa Baba (Mungu) bila kupitia kwangu maana yeye yu ndani yangu, nami ni ndani yake.”

Nimetumia maneno haya ambayo si nukuu halisi, kujaribu tu kuonyesha na kusisitiza kwamba, kwa gharama yoyote iwayo, mbunge; hasa mbunge wa kuchaguliwa anazo ngazi kuu nne za kuwajibika na huyo anayezizingatia, ndiye mbunge; ndiye mbunge wangu; mbunge wetu anayetufaa; tutamchagua hata akirudi mara 10.

Ngazi ya kwanza ya uwajibikaji wa mbunge, ni kwa taifa zima. Mbunge anayelitambua hilo na kulifanyia kazi kwa dhati, ni mbunge safi. Hii inamanisha kwamba mbunge yeyote anayetaka kuwa mbunge safi, lazima awe tayari kutetea kwanza, hata wale wasio wa jimbo lake ili mradi tu, anafanya hivyo kwa maslahi ya taifa; kwa maslahi ya Watanzania.

Kikiwa ni moja ya vipimo kati ya 12 vya mbunge asiye feki, mbunge pia baada ya kutambua wajibu wake kwanza kwa taifa zima, sasa atambue ngazi ya pili kuwa ni kwa jimbo lake zima la uchaguzi.

Ijulikane wazi kuwa, mbunge wako akitanguliza maslahi ya chama kabla ya maslahi ya taifa na jimbo kwa jumla, huyo si mbunge, huyo ni mzimu wa mbunge ni “dude” tu, lililoandikishwa na kupewa nafasi ya kiti pale bungeni.

Ninayajadili haya maana kumalizika kwa uchaguzi huu, ndiyo kuanza kwa maandalizi ya uchaguzi mwingine ujao hivyo, huu ni wakati sahihi wa kuwasoma, kuwachambua, kuwatafakari na hata kuwaelewa wabunge feki na wale orijino.

Hii itatufanya tukae mkao wa kula tukiwasubiri wakati ukifika, waje tena na “sera zao za mtoni” kutudanganya maana wamerithishana imani kuwa sisi ni wadanganyika wa kudumu. Hivi wanadhani watatudanganya kwa lipi tena wakati tunaona sera zao zilivyo za kutetea chama badala ya watu (taifa na jimbo)?

Kipimo cha pili, ni namna mbunge huyo alivyo tayari kupunguza mshahara au kupoteza hata ikibidi, marupurupu yake na maslahi mengine mradi tu, asikubali kufungwa kufuli mdomoni ili eti asiseme ukweli; eti akubali kuyumbishwa kifikra ili atengue msimamo wake wa kutetea maslahi ya umma. Mbunge safi haruhusu hilo litokee; yuko tayari kutetea maslahi ya umma kwa gharama yoyote hata kwa chozi la damu.

Mbunge kama huyo atapambana mpaka mwisho; posho na marupurupu si mambo ya msingi na kipaumbele kwake, kiasi cha kuusaliti umma. Huyo ndiye mbunge; mbunge safi. Wenye mbunge wa namna hiyo, wamelamba dume, lakini kinyume chake, jimbo hilo na taifa kwa jumla limelamba galasa.

Huyo ndiye mbunge safi; asiye feki wala kanyaboya la mbunge; kanyaboya lililokaririshwa usiku kucha namna ya kupokea sauti zinazoliita “mheshimiwa…”

Kipimo cha tatu, ni mbunge kutokuwa mnafiki kwa viongozi wa chama chake na wale wa Serikali ili eti apewe cheo; labda eti awe naibu wazi au waziri kamili.

Shirika la Ugavi wa Umeme Tanzania (TANESCO), limetangaza mgawo mkali wa umeme nchi nzima kwa siku 30 tangu Mei 19 hadi Juni 18, mwaka huu kutokana na kuzimwa kwa mitambo ya visima vinavyotumiwa na kampuni ya Pan African Energy vinavyozalisha gesi ya songosongo kwa ajili ya kufanyiwa ukarabati.

Hili si pigo la kwanza katika sekta ya umeme kwa Watanzania. Tatizo la umeme hasa wa gridi ya taifa ni ugonjwa “uliokula chumvu nyingi” na umeanza kupata hata wajukuu.

Wabunge wetu wamegeuza suala hilo kuwa mtaji wa kisiasa na kiuchumi; wanauzungumzia sana, lakini hakuna anayeonesha tiba mbadala hasa kwa taasisi muhimu zilizo maeneo ya vijijini ambako umeme wa gridi ya taifa ni ndoto kufika.

Mbunge wa Isimani, William Lukuvi na kampuni wakandarasi wa umeme utokanao na mionzi ya jua ya Ensol Tanzania Limited iliyopo Ubungo Dar es Salaam, wao wameonyesha mfano wa kuigwa.

Wameshirikiana kuona kuwa kupitia msaada, baadhi ya shule za sekondari ikiwamo ya Idodi mkoani Iringa iliyopata ajali ya moto na kupoteza maisha ya wasichana 12 kutokana na ukosefu wa umeme, zinapata nishati hiyo mbadala kutokana na mionzi ya jua.

Mbunge mwenye ubunifu na kujali kama huyo hata asipopiga kelele bungeni ili atazamwe kwenye runinga; asikike redioni na kusomwa magazetini, ni mbunge safi na kamwe si “zigo la mbunge”.
Kipimo kingine cha kumjua mbunge “aliyeoza” ni namna anavyotetea na kufurahia matumizi ya mashangingi huku usafiri jimboni kwake ukiwa msamiati kwa kuwa barabara za jimbo lake hazitumiki hata kwa bajaji; huyo ni mbunge anayejiona mungumtu anapowapita wapiga kura wake wakiwa wamebeba wagonjwa au maiti kwenye machela wakipiga kwata umbali mrefu bila usafiri kwa kuwa tu, barabara hazipitiki.

Huyo, atatumia muda na nguvu nyingi kutetea shangingi, badala ya kutetea matengenezo ya barabara. Mbunge anayetetea shangingi badala ya huduma muhimu za umma, ni sumu; aogopwe.

Mbunge safi, mwajibikaji, mwadilifu na asiyenunua ubunge, utampima na kumjua kwa matendo yake ikiwa ni pamoja na tofauti iliyopo kati ya hali yake ya maish na watu anaowawakilisha.
Kama familia ya mbunge ni ya akina “bonge” tupu huku wananchi wake wamekondeana mithili ya namba 1 (moja), kama ni familia inayokula hadi kuvimbewa na kukaribia kutapikia soksi huku familia nyingine zikiwa hazina uhakika wa mlo hata mmoja kwa siku, hapo kuna tatizo na mbunge huyo. Huenda mbunge huyo ni “chuma ulete” kwa njia moja au nyingine.

Ni mbunge chumaulete kama vitega uchumi vya eneo lake amevishikilia yeye, kisha anataka awe Mungu au mfalme anayetaka kutumikiwa badala ya kutumikia; anayekuwa mbabe kiasi kwamba ndiye mlalamikaji, ndiye makataji, ndiye shahidi na ndiye hakimu wa mambo mbalimbaliikiwa ni pamoja na kuchapa watu makofi.

Hii ni kusema kuwa, maisha ya mbunge feki au ambaye ni chuma ulete, utayajua namna yalivyo tofauti kubwa kabisa na yale ya wananchi anaowaongoza na huyo, si rahisi kuwakomboa watu wake, bali atawatumia tu kama daraja la kuvuka kwenda kwa chumaulete wa ngazi za juu. Huyo, matatizo ya watu wake, huyahesabu kama ushindi kwake.

Mbunge feki ni bubu asiyeweza kusema hata kama anaona watu wake wanaonewa na kufa ovyovyo kwa kukosa hospitali, kituo cha afya wala zahanati. Inapotekea hivyo vikawapo jimboni kwake, basi vinakuwapo kwa sura ya majengo na jina tu, sio ubora wa huduma zake kwa kuwa hakuna waganga, wauguzi wala dawa.

Si ajabu katika mazingira hayo, kukawa na mradi wake, ndugu yake au wa rafiki yake ambaye atauza dawa na huku akiitwa “dokta” hata kama hajui A, B wala C ya fani ya uuguzi na dawa na pengine hasa, hata kodi wala ushuru halipii.

Kama ilivyo kwa huduma za afya, huduma za elimu (shule) ni kipimo kingine. Mbunge safi hakubali wala kuruhusu shule katika jimbo lake zikawa majengo yenye wapangaji aina ya popo wasiolipa kodi ya mwezi.

Hakubali magofu ya majengo yaitwe shule wakati hakuna walimu, hakuna vitabu wala huduma nyingine muhimu za kufundishia. Anayeridhika na hali hiyo, ni mbunge mnyonyaji kama kupe; mtena mbunge juha kama alivyo mfalme juha.

Hii ni kwa kuwa muda mwingi anautumia kufukuzia posho na tenda za biashara na miradi yake binafsi hivyo, hajui matatizo ya wananchi wake. Huyo, hajui namna ukosefu wa mabweni unavyoathirti taaluma na hasa pia kwa maisha ya watoto wa kike wanaopata mimba na kukosa muda wa kujisomea.

Licha ya barabara niliyoitaja kwa njia isiyo ya moja kwa moja, jimbo lenye mbunge ovyo hata kama watu watafanyakazi kwa juhudi na maarifa, matunda ya juhudi hizo yataishia kwa wachache ambao ni walanguzi na wachuuzi wa bidhaa mbalimbali yakiwamo mazao.

Hii ni kwa kuwa, mbunge amelala kuliko hata maiti kiasi kwamba watu hawana hata soko; nao wachuuzi wanaendelea kunyonya kwa kujipangia bei ya mazao bila kujali gharama za uzalishaji.
Kwa ukosefu wa soko, hata wananchi wenyewe licha ya kuuza mazao yao kwa bei ya kutupa, wao wananunua bidhaa mbalimbali kwa bei isiyobebeka. Hayo ni mateso makubwa kupata mbunge vuvuzela, lakini masikini wa vitendo. Mbunge wako yukoje?

Mbunge mwema, asiye mzigo utamtambua kwa namna nyingi maana tausi hahitaji mapambo ili apendeze. Hii ni pamoja na namna mbunge huyo anavyowasiliana mara kwa mara na kwa njia sahihi hususan ya vikao na wapiga kura wake ili kupanga mipango ya maendeleo, kubaini matatizo, vyanzo vya matatizo na namna ya kuyakabili matatizo na changamoto zilizo mbele yao.
Mbunge safi si yule anayeonekana siku ya kutangazwa mshindi kwenye uchaguzi, kisha akaondoka na kuwakilisha wananchi wake kwa “remote control” hadi siku ya kampeni ya uchaguzi mwingine.

Kwamba huyo awe mbunge mithili ya njiwa anayekula chini na kulala juu; jimbo lake liko Mashariki, yeye anaishi Magharibi. Hapana, akiwa hivyo si mbunge wetu; ni mbunge chuma ulete.

Huyo tutampima pia kiwango cha uwajibikaji wake kwa kuangalia kiwango cha vitendo vya uhalifu katika eneo lake. Hii ina maana kwamba, kiongozi mwema, hukaa na watu wake kujadili namna nzuri ya kufichua na kuzuia uhalifu na wahalifu kwa kushirikiana na vyombo vya sheria, bila kujichukulia sheria mkononi.

Mbunge mwema, mzuri na safi, si mdau na wala hana ushirika wala mgawo kwa wahalifu; kwamba atoe taarifa kwa wahalifu ili wafanikishe uhalifu kisha katika mikutano, ajidai kukemea kumbe mchana anawamulika wananchi wake na usiku anawachoma!

Huyo si mbunge tunayemtaka. Ni vigumu kuamini kwamba wapo wabunge na viongozi wengine wa namna hiyo, lakini huo ndio ukweli maana kwenye msafara wa mamba, kenge hawakosekani.
Hivi mbunge wako umekwishamchunguza na kujua anaangukia wapi katika vipimo hivi 12 ambavyo ni miongoni mwa vipimo vya kumjua mbunge orijino au mbunge feki?
Tanzania itajengwa na wenye moyo.
sabinus55@yaoo.com
0788 007070
 
Back
Top Bottom