Prof. Mbele na hoja zake: Amfagilia JK

Sumaku

Member
Feb 17, 2009
53
1
i1473_jmbelebc.jpg


13 January 2010

Mimi ni m-Tanzania ambaye si mwanachama wa chama chochote cha siasa.

Sizuiwi na yeyote au chama chochote katika kutoa hoja na misimamo yangu. Wala sina sababu ya kumbembeleza au kumwogopa yeyote. Siwanii cheo kutoka kwa chama chochote, kwani si mwanachama na sitaki uanachama.

Kwa hali inavyokwenda, namwona Rais Kikwete ndiye amekomaa kisiasa kuliko wengi, na anafaa kuendelea kuwa rais.

JK Anajiamini, anatoa fursa kwa wapinzani

Profesa Joseph L. Mbele

BAADA ya makala yangu ya wiki iliyopita, kuhusu safari za Rais Kikwete nchi za Nje, ambayo imezua mjadala mkubwa, nimeamua kuongelea suala la Rais Kikwete na wapinzani. Nimeamua kuongelea suala hili kwa vile Rais Kikwete ameleta picha tofauti na ilivyozoeleka katika miaka ya karibuni Tanzania, chini ya utawala wa CCM.

Ninavyokumbuka, suala la uhusiano wa Rais Kikwete na wapinzani lilijitokeza kwa namna ya pekee siku Kikwete alipoapishwa kuwa rais wa Tanzania.

Sikuwepo uwanjani, lakini nilipata taarifa katika mitandao ya mawasiliano. Kitu cha pekee ni namna Kikwete alivyowaongelea wapinzani katika hotuba yake, baada ya yeye kuibuka mshindi katika kampeni ya kugombea urais. Aliwashukuru wapinzani kwa changamoto waliyotoa katika kampeni za uchaguzi, akisema kuwa changamoto yao iliiboresha kampeni.

Kauli hii ilinigusa. Kwanza, haikuwa tabia ya CCM kuutambua mchango wa wapinzani. Hatua aliyochukua Kikwete siku hiyo ni tofauti na jadi ya CCM. Kwa miaka mingi, CCM ilikuwa inawaona wapinzani kama maadui wa Taifa. Hali hii ilidhihirika zaidi katika Awamu ya Tatu ya uongozi Tanzania.

Wapinzani walikumbwa na hujuma nyingi zilizofanywa na vyombo vya dola, ambayo vilikiuka wajibu wake kama vyombo vya Taifa, vikawa vinafanya umachinga kwa CCM. Hayo yalibainishwa na taasisi huru za ndani na nje ya nchi, wakati wa uchunguzi wa vurugu zilizotokea Visiwani. Tanzania ilifedheheka kimataifa.

Pili, kauli ya Kikwete siku ile ilikuwa ni ishara ya busara na uungwana. Kiongozi anapaswa awe mwenye kuwajali na kuwaheshimu watu anaowangoza, wakiwemo wapinzani. Mtu anayejiamini, haogopi kuwapa sifa wengine. Ni ishara ya kujiamini, na kukomaa katika falsafa na saikolojia ya uongozi.

Kiongozi wa nchi anapowachukulia wapinzani kama afanyavyo Rais Kikwete anathibitisha kuelewa kuwa yeye ni kiongozi wa wote. Tumeshawaona wengine nchini mwetu ambao wanafanya vingine. Tumeshawaona ambao, siku ya kuapishwa, wanaendelea kuwabeza washindani wao, kama vile bado wako kwenye kampeni. Pengine sio sahihi kusema kuwa hao ni viongozi. Uongozi wa kweli si wa mbwembwe wala mabavu, bali unatokana na tabia njema. Unatokana na tabia inayowafanya watu wamkubali huyu mtu kwa hiari yao kuwa ni kiongozi.

Kama nilivyosema, alivyofanya Kikwete siku alipoapishwa ni tofauti na jadi ya CCM ya kuwabeza, kuwahujumu na kuwashambulia wapinzani. Napenda kurudi nyuma na kukumbushia kuwa jadi hii Mwalimu Nyerere alikuwa anajitahidi kuwakanya CCM waiache. Kwa mfano, wakati wanachama wa vyama vya upinzani walipokuwa wanasukuma magari ya viongozi wao kwa shangwe, na vyombo vya dola, kwa kutekeleza matakwa ya CCM, vikawa vinawazuia, Mwalimu Nyerere aliingilia kati na kusema watu waachwe na uhuru wao wa kusukuma hayo magari. Hivi ndivyo CCM ilivyokuwa, kwamba ilibidi Mwalimu awaelimishe jambo la wazi kama hilo, linalohusu uhuru na haki ya binadamu.

Baada ya kuingia madarakani, Rais Kikwete ameendelea kwenda njia tofauti na ilivyozoeleka, katika mahusiano yake na wapinzani. Amekuwa akiwashirikisha wapinzani katika shughuli za kiTaifa. iwe ni kuwakaribisha wageni wa nchi za nje Ikulu, au kuwa katika tume muhimu za kiTaifa. Vile vile, katika ziara zake za nchi za nje, Rais Kikwete anawajumuisha wapinzani. Hii haikuwa jadi ya CCM. Awamu ya Tatu, kwa mfano, sikuwahi kusikia wapinzani wamekaribishwa Ikulu.

Binafsi, nayatilia maanani hayo yote, hata kama baadhi yanaonekana madogo. Kwa ujumla wake, yanaonyesha kuwa Rais Kikwete ana moyo na mwelekeo tofauti na ule wa zamani. Kuwajumlisha wapinzani katika tume kama ile ya kuchunguza mikataba au tuhuma za kashfa ni ishara ya kuwa Rais Kikwete anatambua kuwa suala la maslahi ya Taifa ni suala la wote, si la chama tawala tu. Suala la kusafiri na wapinzani nje ya nchi linaweza kuonekana dogo, lakini mimi naliona kubwa. Nazingatia kuwa kusafiri ni fursa ya kujifunza na kupanua akili. Kusafiri ni kuelimika. Tangu enzi za mababu na mabibi, ilifahamika hivyo, hata wakatuachia methali: tembea uone. Kwa kuwajumuisha wapinzani katika misafara ya nje, Rais Kikwete anawapa fursa ya kujiimarisha kielimu na kimtazamo. Angekuwa mtu asiyejiamini, angeogopa kuwa wapinzani wakiimarika watakuja kuwa tishio kwenye kampeni za uchaguzi.

Jukumu nililojipa katika kuandika makala hii ni kuibua mjadala, na nategemea mjadala utakuwepo. Ninafahamu kuwa Rais Kikwete, kama kiongozi mwingine yeyote, hawezi kumridhisha kila mtu. Ninahisi kuwa hata haya niliyosema huenda watu wengine ndani ya CCM hawayapendi. Nafahamu kuwa katika uongozi wake kuna mapungufu, kama ilivyo katika uongozi wowote. Lakini mimi kama Mtanzania ambaye si mwanachama wa chama chochote cha siasa naona msimamo wa Rais Kikwete kuhusiana na suala la wapinzani ni mzuri na unastahili kutajwa kama nilivyofanya. Kwa namna fulani, kama nilivyodokeza, anayofanya Rais Kikwete ni mwendelezo way ale aliyoyawazia Mwalimu Nyerere, alipokuwa anawakingia kifua wapinzani.


–
Joseph L. Mbele
English Department
St. Olaf College
Northfield, MN 55057
Phone: (507) 786 3439


CHANZO: kwanzajamii.com
 
BRAVO PROFESA MBELE

Waswahili wana msemo 'Mnyonge mnyongeni lakini haki mpeni'
Tatizo letu sisi mara nyingi tunawacha hisia zetu zituteke nyara na kwa yule ambaye maamuzi juu ya siasa/uchumi etc yanatokana na tathmini halisi ya issues- Huwa anabandikwa label either pro ccm or upinzani.

Hata ukiangalia jinsi anavyo shughulikia matatizo ya wananchi mikoani kwa wanaofuatilia utagundua ni msikilizaji mzuri sana. Tatizo inawezekana kuwa aina ya uongozi wake ni tofauti na viongozi wengine [katika ustahamilivu] ikawa kwetu ni ishara ya udhaifu.

Wengi wamezungumzia safari zake za nje lakini kutokana umakengeza hawafuatilii matunda ya ziara hizo.

Nchi hii inahitaji watu makini wanaotathmini mambo na kutoa mapendekezo/utekelezaji wa uchambuzi huo bila kuingiza siasa za vyama kwenye issues za national interests.
 
Huyu Mbele naye ni Profesa?!! Afanye utafiti kwa nini Profesa mwenziwe amenyimwa mkataba wa kuendelea kufundisha pale Chuo Kikuu. Halafu jambo la Wapinzani kualikwa Ikulu afanye pia utafiti ili aweze kujua Ikulu inaendeshwaje kabla hajatoa maelezo ambayo anaonekana pamoja na u-profesa wake yanadhihirisha haelewi mambo yanayohusiana na utaratibu ama uendeshaji wa shughuli za Rais.
 
BRAVO PROFESA MBELE
Waswahili wana msemo 'Mnyonge mnyongeni lakini haki mpeni'
Tatizo letu sisi mara nyingi tunawacha hisia zetu zituteke nyara na kwa yule ambaye maamuzi juu ya siasa/uchumi etc yanatokana na tathmini halisi ya issues- Huwa anabandikwa label either pro ccm or upinzani.
Hata ukiangalia jinsi anavyo shughulikia matatizo ya wananchi mikoani kwa wanaofuatilia utagundua ni msikilizaji mzuri sana. Tatizo inawezekana kuwa aina ya uongozi wake ni tofauti na viongozi wengine [katika ustahamilivu] ikawa kwetu ni ishara ya udhaifu.
Wengi wamezungumzia safari zake za nje lakini kutokana umakengeza hawafuatilii matunda ya ziara hizo.
Nchi hii inahitaji watu makini wanaotathmini mambo na kutoa mapendekezo/utekelezaji wa uchambuzi huo bila kuingiza siasa za vyama kwenye issues za national interests.

Tatizo ni kuwa ameenda kutafuta Milioni 20 ambazo tunazipata kwa masharti na masimango kibao na kaacha kufanya kazi nzito na kukusanya hizo milioni 20 hapahapa Tanzania.

Umatonya ni too much na mtu anayekaa na kusifia umatonya kwa kweli ni kichekesho. Toa sadaka ameni, na bahati mbaya watoa sadaka wenyewe hata dini hawaamini. Wao hapendwi mtu ila pesa.
 
Haya ndiyo matatizo waliyonayo wenzetu walioko nchi za nje; hawayaoni mambo ya huku nyumbani kwa macho yale yale kama sisi tuliopo hapa nyumbani. Kuongoza ni kuonesha njia na huwezi kuonesha njia kama hujui unataka kwenda wapi.

Sasa huyu Prof. aliyeko Minnesota anaweza kutuambia VISION ya Kikwete toka ameingia madarakani ni kulipeleka Taifa hili wapi? Je kusafiri nchi za nje akiongozana na wabunge wa upinzani ni ujasiri wa aina gani?

Kikwete ni msanii na nyie mnaokaa nje mnategemea spin za magazeti kama source ya taarifa zenu as a result you make wrong conclusions. Safari za Kikwete za nje zimeleta matunda gani zaidi kuliko angetulia nyumbani na kuchunga maliasili za nchi zisiibiwe na mafisadi?

Kikwete angeonekana jasiri kama angewashikisha adabu marafiki zake ambao kuna ushahidi kuwa wamehujumu uchumi wa nchi yetu. Wadanganyika karibuni wengi wanajua jinsi Lowassa, Rostam, Karamagi, Chenge, Rashid Idris, Manji, Subash Patel etc walivyohusishwa na ufisadi uliokithiri nchini mwetu; angekuwa jasiri hawa wote wangekuwa Segerea wanabeba mitondoo!!

Kufuatana na mizengwe ya CCM, Kikwete atateuliwa na kuchaguliwa kuwa Rais muhula wa pili; lakini hatafanya lolote la maana bali kuliangamiza Taifa kwa kushirikiana na maswahiba wake kuzidi kupora rasilimali za nchi yetu. Uzoefu tulionao kwa awamu zilizopita ni kwamba Rais anapopata kuchaguliwa kipindi cha pili inakuwa ni lalasalama yao kwahiyo concentration yao inakuwa kujilimbikizia mali wao ndugu na marafiki zao!!

Mungu muumba unisamehe lakini ni dhahili Kikwete hata kuwa tofauti na waliomtangulia na dalili zinajionesha wazi na kama huamini maneno yangu nenda kijijini kwake Msoga ukajionee!!
 
Sina uhakika kama kuna anaebishana na Prof. Mbele. Ila nina uhakika kuwa Prof. Mbele hajaweka bayana mambo muhimu kwa Taifa.

Naomba msaada. Sifa za Rais au kiongozi zinapimwa kwa ukarimu tu?
 
Hukumu nililojipa katika kuandika makala hii ni kuibua mjadala, na nategemea mjadala utakuwepo. Ninafahamu kuwa Rais Kikwete, kama kiongozi mwingine yeyote, hawezi kumridhisha kila mtu. Ninahisi kuwa hata haya niliyosema huenda watu wengine ndani ya CCM hawayapendi. Nafahamu kuwa katika uongozi wake kuna mapungufu, kama ilivyo katika uongozi wowote. Lakini mimi kama Mtanzania ambaye si mwanachama wa chama chochote cha siasa naona msimamo wa Rais Kikwete kuhusiana na suala la wapinzani ni mzuri na unastahili kutajwa kama nilivyofanya. Kwa namna fulani, kama nilivyodokeza, anayofanya Rais Kikwete ni mwendelezo way ale aliyoyawazia Mwalimu Nyerere, alipokuwa anawakingia kifua wapinzani.
Style ya utawala wa JK inanikumbusha enzi za mzee "Ruksa". Mzee Ruksa used to just sit back and let things happen. Ruksa, ruksa. Style ya Kikwete ni "Ruksa" katika era ya sasa - which makes it very compromising. A president cant just sit back like that wakati millions of $$ zinakuwa plundered (EPA, Richmond - the list is endless!). There's no value eti kuwa "mvumilivu vs opposition" wakati core issues kama hizi haziwi addressed. My learned professor anaweza kuelezea kwa nini Tanzania (arguably the richest in resources in EA) ni moja ya nchi masikini sana duniani? Do you think kwa style ya uongozi wa JK tutaweza kujikwamua kutoka kwenye bracket hii? Nimuulize ndg prof ametembelea TZ vijijini kwa mara ya mwisho lini? Kama bado tafadhali take a stock on that and you will understand what am trying to say. Naongea haya kwa uchungu kwa vile mtu aliyeanzisha debate hii ni mtu msomi ambaye nilitegemea awe na microscopi vision kuliko sisi akina yakhe.
 
He is entitled to his opinion....na siyo lazima maoni ya msomi/wasomi yakubalike na watu wote mara zote.
 
Profesa Mbele ameamua kuchokoza mjadala; kimsingi anahoji sababu alizotoa zinatosha kumfanya JK agombee tena?
 
Siri kubwa ni kwamba Prof Mbele alisoma na JK so nadhani ni wakati wa yeye kutafuta ka mkate kake naye . Kama haombi kazi wala hana Chama mbona asione makubwa yanayo ikumba nchi yeye anaona JK kuwa mgombea mkomavu ? Kampimia nini huyu naye ? Mh haya Mbele nakusikiliza
 
Waswahili wana msemo "DEBE TUPU HALIACHI KUVUMA" nadhani huyu "Profesa" ni debe tupu!
 
Jamani huyu profesa ni wakuachana nae ana matatizo si bure!!!

Ananikera sana nachelea kusema huo uprofesa ni wa mashaka
 
15 January 2010

"We believe, in fact, that a second party will not need to grow provided that a broad two way channel of ideas and education is maintained through TANU between the people and the Government. It is the establishment and maintenance of this channel of communication which is the real problem of democracy in Tanganyika, not the establishment of an artificial opposition. " ( JK. Nyerere, Freedom And Unity, page 134).

Nimesoma maandiko hayo ya Mwalimu wakati nikitafakari hoja ya Profesa Mbele.

Maggid

Tunahitaji Vyama vya Siasa?
Joseph L. Mbele

Jamii yetu, kama jamii zingine, inatafuta namna ya kujenga na kuimarisha demokrasia. Katika harakati hii, uamuzi ulifikiwa kwamba tuwe na vyama vya siasa, badala ya chama kimoja. Watu wanavihangaikia vyama vya siasa karibu kila mahali, kwa imani kuwa ni njia muhimu ya kujenga demokrasia. Kama kuna nchi isiyo na vyama vya siasa, utawala wa nchi hiyo unahesabiwa kuwa si wa kidemokrasia.

Hii ndio hali ilivyo. Kwa hivi, kuuliza kama tunahitaji vyama vya siasa inaonekana ni suali la kipuuzi. Lakini mimi sioni kama ni suali la kipuuzi.

Demokrasia ni nini? Katika historia, zimekuwepo tafsiri kadhaa za dhana ya demokrasia. Kwa maoni yangu, demokrasia ni aina ya utawala ambamo umma umeshika hatamu.

Si utawala ambao unaendeshwa na kikundi cha watu, bali umma wa walio wengi. Demokrasia ni utawala unaowakilisha na kuendeleza matakwa na maslahi ya umma. Hii ndio maana ya demokrasia. Katika kufafanua zaidi, dhana ya umma ni dhana inayozingatia matabaka katika jamii. Umma ni tabaka la wafanyakazi na wakulima. Hao ndio wengi, katika nchi kama ya Tanzania.
Dhana ya vyama haiko kwenye tafsiri hii ya demokrasia, kwani sio msingi au uhai wa demokrasia. Ni namna gani demokrasia inaweza kujengwa? Ili demokrasia iwepo, ni lazima kuwe na vyama? Haya ndio masuali ya kujiuliza.

Watu wa Ulaya, katika historia yao na mazingira yao, waliamua kuwa mfumo wa vyama vya siasa ndio wanaouhitaji kwa kujengea na kuwezesha demokrasia. Huo ulikuwa uamuzi wao, kufuatana na hali halisi ya kwao.

Lakini je, wa-Tanzania tulikaa lini tukatathmini historia na mazingira yetu, hadi kufikia uamuzi kuwa, ili tuwe na demokrasia nchini mwetu, tunahitaji mfumo wa vyama? Tumefanya hiyo tathmini au tumeiga tu? Je, kinachofaa au kuhitajika Ulaya ni lazima kiwe hiki hiki hapa kwetu? Hakuna uwezekano wa kuwa na demokrasia bila vyama? Haya ni masuali muhimu.

Je, hatukuwa na historia na jadi yetu ambayo tungeweza kuitumia katika kujenga demokrasia yetu? Kwa nini tumeshindwa hata kuwazia jambo hilo? Mataifa yanayotutawala kiuchumi nayo yanatushinikiza tuwe na vyama vya siasa. Je, huu si ukoloni mambo leo, ambao watu kama Frantz Fanon waliuongelea?

Vyama vya siasa tumevipata, na huenda vikaongezeka. Je, vimetusaidia au vimetuletea matatizo? Ni wazi kuwa katika nchi yetu, vyama vya siasa vimeleta mfarakano, ambao unazidi kuota mizizi. Kampeni za uchaguzi zinaendelea kuwa na sura ya magomvi. Kadiri siku zinavyopita, amani inazidi kuharibika. Hayo yote yako wazi, lakini wazo la kuhoji umuhimu wa vyama vya siasa halisikiki. Hakuna anayetamka kuwa labda vyama vya siasa ni kipingamizi katika maendeleo ya nchi yetu.

Mtu anaweza kusema kuwa tunaweza kuendesha siasa ya vyama vingi kwa amani na utulivu.

Lakini hoja hii haitaivunja hoja yangu ya msingi kuwa wazo la vyama ni wazo tuliloiga tu, kikasuku, na pia tunashinikizwa na mataifa mengine. Kutokana na kasumba tuliyo nayo vichwani, wala hatuwazii kutumia uhuru wa kulichunguza upya suala la demokrasia na kutafuta njia nyingine.

Tunataka demokrasia. Hilo ni wazi. Ingekuwa bora iwapo tungetafuta mfumo tofauti wa kujenga na kuendeleza hiyo demokrasia, mfumo unaotufaa kwa mujibu wa historia, jadi na mazingira yetu. Mfumo huu ungekuwa ni wetu, usio na chembe ya kushinikizwa kutoka nje, kama ilivyo sasa.

Kuna tatizo gani, kwa mfano, kuwa na mfumo ambao ungetumia busara za wazee, kama ilivyokuwa katika jadi zetu tangu zamani? Ingewezekana kila kijiji, tarafa, au wilaya kuwachagua wazee wenye busara, wanaokubalika, wakawa ndio wawakilishi kwenye ngazi hizo na kwenye ngazi ya Taifa pia. Kwa busara zao, hao wangewasilisha maoni na mahitaji ya jamii zao, kuanzia watoto hadi wazee, wanawake kwa wanaume.

Katika maisha ya kila siku katika jamii zetu za ki-Afrika, mitaani na vijijini, wazee wanashika wadhifa huo. Mambo ya vyama vya siasa tumeiga na dosari zake zinaonekana.

Mbunge ambaye tunamchagua kwa mtindo huu wa vyama vya siasa anaweza kupotea muda mrefu, asionekane, hadi wakati wa uchaguzi ujao, lakini masuala ya jamii anayopaswa kuiwakilisha yanatatuliwa na wanajamii wenyewe kwa njia zao za asili. Kuna wabunge ambao ni kama watalii kwenye majimbo yao ya uwakilishi, lakini maisha ya wanavijiji kwenye majimbo hayo yanaendelea kwa utaratibu ambao si wa vyama. Utaratibu huo ni pamoja na jadi ya kuwatumia wazee.

Miaka ya karibuni, tumeona kitu cha aina hiyo kikifanyika katika kutafuta ufumbuzi wa masuala ya bara la Afrika. Wazee kama Askofu Desmond Tutu, Jimmy Carter, na Kofi Annan, wamepelekwa kushughulikia masuala kama yale ya Zimbabwe, ambako kumekuwa na mgogoro baina ya chama tawala cha ZANU na chama cha MDC.

Katika migogoro ya Somalia, mara kwa mara wazee wamekuwa ndio watafutaji wa suluhisho. Miezi kadhaa iliyopita, wazee hao walikusanyika Kenya, wakafanya mazungumzo ya muda mrefu kutafuta ufumbuzi wa matatizo ya nchi yao.

Hapa Tanzania, Rais Ali Hassan Mwinyi alikuwa na utaratibu wa kuongea na wazee wa Dar es Salaam kuhusu masuala muhimu ya ki-Taifa. Mzee Mwinyi alikuwa na upeo mzuri, ambao ungepaswa kufuatwa na kuimarishwa. Mifano hii yote inaendana na hoja ninayojaribu kujenga hapa, kuhusu umuhimu wa wa-Afrika kutafuta mifumo inayofaa kwa demokrasia katika mazingira yetu.

Utawala wa nchi si lazima uwe kwa mfumo wa chama cha siasa au vyama vya siasa. Nchi inaweza kutawaliwa bila chama au vyama. Kuwepo au kutokuwepo kwa demokrasia ni suala ambalo si lazima lihusishwe na vyama. Demokrasia ndio lengo letu, lakini vyama ni mfumo tu ambao unaweza kutumiwa kujenga na kudumisha demokrasia, lakini si mfumo pekee.

Tunaweza kuwa na demokrasia bila vyama, kama ilivyokuwa enzi za mababu na mabibi zetu, kabla ya kuja wazungu. Hapakuwa na vyama. Lakini, kama Mwalimu Nyerere alivyoandika, wazee walikuwa wanakaa chini ya mti na kujadiliana masuala hadi kukubaliana. Hii ilikuwa ni demokrasia, bila vyama.

Kinachohitajika ni sisi kufanya tafakari sisi wenyewe, si kudandia mambo ya Ulaya kama tunavyofanya. Uganda, chini ya Rais Yoweri Museveni, imeonyesha mfano. Ina mfumo ambao inaona unafaa katika nchi ile, kufuatana na historia na mazingira yake.

Mfumo waliochagua unaweza kuwa na dosari, lakini angalau ni matokeo ya tathmini yao wenyewe. Wanaweza kuubadili wakaunda mwingine, kufuatana na hali halisi, bila kuiga kikasuku. Hizi ni fikra za watu huru.

Kwa kutumia na kuthibitisha uhuru wa fikra na uamuzi, kila nchi katika bara letu ingeweza kujitungia mfumo wa aina yake, kwa mujibu wa hali halisi ya nchi ile. Kwa mtindo huu, tungejenga demokrasia ya kweli. Tungedumisha amani na mshikamano na kuleta maendeleo, sio hizi fujo tunazoziendekeza sasa, na mfarakano katika jamii, kwa kisingizio cha ushindani wa kisiasa.

Tunahitaji demokrasia, yaani mfumo wa utawala ambao chimbuko lake na nguvu zake ni umma, mfumo ambao unasimamia na kuendeleza maslahi ya umma. Lakini je, ili hayo yawepo, tunahitaji vyama vya siasa? Hili ndilo suali linalohitaji jibu.

-------------------------------------------------------
Profesa Joseph Mbele, m-Tanzania ambaye si mwanachama wa chama chochote cha siasa, alikuwa mwalimu wa Chuo Kikuu Dar, 1976-91. Makala yake hii imo katika kitabu kipya, kilicholengwa kwa wavijiji, wafanyakazi, na walalahoi, kiitwacho CHANGAMOTO:Insha za Jamii: http://www.lulu.com/content/8116223 .

CHANZO: KwanzaJamii.com
 
( Nimeyanasa maoni ya profesa kule kwanzajamii.com)

18 January 2010 13 views No Comment
Emma, Mimi niliongelea suala la uhusiano wa JK na wapinzani. Kama una kipingamizi kwa hoja nilizotoa kuhusu kipengele hiki, andika hoja zako tuzisome.
Mimi ni mwanataaluma, na taaluma haijui mipaka ya nchi. Mawazo yangu yamo kwenye vitabu na majarida mbali mbali, ambayo husomwa na yeyote duniani pote. Watu wanaotaka kujifunza kutoka kwangu wanawasiliana nami kutoka nchi mbali mbali. Mifano ya hivi karibuni ni Mexico, Afrika Kusini, Uingereza, na India, achilia mbali sehemu mbali mbali za hapa Marekani, sehemu ambako sijawahi hata kufika. Nawasiliana nao bila matatizo kwani dunia ya leo ni ya mtandao.
Watanzania amkeni. Tambueni kuwa dunia ya leo ina mawasiliano ya aina yake, na watu duniani wanabadilishana mawazo, na kufundishana kwa kutumia mtandao. Nyinyi mmekaa tu mnangojea wataalam warudi nchini, wakati wenzenu duniani wanajua kuwa dunia ya leo si kama ya miaka iliyopita.
Lakini, kama ni suala la mimi kuwepo nchini Tanzania, mimi ninakuwepo Tanzania kila mwaka, angalau kwa wiki kadhaa, na pengine miezi miwili hivi. Yeyote mwenye nia ya kweli ya kuniona ili kufuatilia taaluma, anayo fursa ya kufanya hivyo. Hapa nilipo ninajiandaa kuja tena Tanzania, miezi michache kuanzia sasa.
Jambo la zaidi ni kuwa mimi kama mwanataaluma, naandika vitabu na makala. Humo yamo mawazo yangu ambayo yanawafaidia wengi, si hapa Marekani tu bali sehemu mbali mbali za dunia. Watu wako Japan au Australia au Uingereza na wanafaidika. Wala hawatoi kisingizio kwamba niko mbali, kama wanavyofanya wa-Tanzania.
Hata hivi, ili kuwarahisishia, nimehakikisha kuwa vitabu vyangu vinapatikana Tanzania. Nimevileta hapa Dar es Salaam, simu namba 0717 413 073 au 0754 888 647. Kwa hivi, hakuna visingizio. Nendeni mkavinunue, mvisome, kama kweli mna hamu ya kujifunza kutoka kwangu.
Tatizo la wa-Tanzania nalifahamu sana, na nimeandika mara kwa mara kwenye blogu zangu na sehemu zingine. Hawavithamini vitabu. Mimi mwenyewe, nilisomea digirii ya juu huku Marekani, miaka ya 1980-86. Nilizingatia wajibu wangu wa kutafuta elimu ili nije Tanzania kuendelea kufundisha kwa kiwango cha juu kabisa.
Nilijizatiti kwa kununua vitabu sana. Nilitumia yapata dola 2000 kununulia vitabu. Nilipomaliza masomo, nilikuja hima Tanzania kuendelea kufundisha. Watanzania waliniuliza suali moja tu: je, umeleta “pick-up?” Walipoona kuwa sikuleta “pick-up” bali hivi vitabu, walinishangaa na kuniona nimechemsha. Ndivyo wa-Tanzania walivyo. Hawaoni kwa nini mtu uache kununua “pick-up” na badala yake ununue vitabu.
Sasa, pamoja na yote hayo, mimi napatikana Tanzania na pia nimewaleteeni vitabu vyangu. Vinunueni. Visomeni. Halafu, leteni masuali kwa kutumia barua pepe kama wanavyofanya watu wa nchi zingine wenye kutafuta elimu kutoka kwangu. Nitakuwa sambamba nanyi, kwani sibagui.
Umeongelea suala la kujenga nchi. Kila mtu anatoa mchango kutokana na uwezo au kipaji chake. Mimi si mhandisi wa barabara wala daktari wa mifugo. Mchango wangu katika kujenga nchi ni katika taaluma.
Nimeshatoa maelezo hapa juu, kuhusu mchango wangu. Na kusema kweli, ningeweza kuandika mengi zaidi kuhusu uzembe niliouona Tanzania, tangu wakati nilipokuwa nimeajiriwa hapo, hadi nilipoajiriwa na wa-Marekani. Wamarekani wanathamini taaluma. Na mimi napenda kuwa na watu wanaothamini taaluma. Napenda kuwa mahali ambapo mchango wangu unathaminiwa. Si mahali ambapo naonekana nimechemsha.
Lakini hata wa-Tanzania sijawasahau, pamoja na uzembe uliokithiri, wa kuendekeza sherehe na michango ya arusi badala ya kununua vitabu, uzembe wa kutoenda maktaba na kusoma, uzembe wa kutokuwa na vitabu majumbani, wakati pesa nyingi wanazitumia kwenye baa na kitimoto.
Mawazo uliyotoa ambayo yanaongelea masuala ya ulaji ni ushahidi wa uzembe ulioko vichwani mwa wa-Tanzania. Mimi ni mwanataaluma. Kwa miaka mingi nimeshaambiwa kuwa nikirudi Tanzania nitapata ulaji. Lakini mimi sina hamu ya huo ulaji. Mnaowazia au kutafuta ulaji endeleeni. Mimi natafuta elimu na shughuli yangu ni kuchangia taaluma.
CHANZO: Kwanzajamii.com
 
Back
Top Bottom