Polisi pemba si wajinga kabisa waumiao ni ndugu zao pia

Lunyungu

JF-Expert Member
Aug 7, 2006
8,873
1,894
Date::9/7/2009CCM yapoteza imani na polisi kisiwani Pemba
broken-heart.jpg

Salma Said, Zanzibar

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimesema kuwa hakina imani na askari wa Jeshi la Polisi Kisiwani Pemba kikidai kuwa idadi kubwa ya watumishi hao wa chombo cha dola wamejiingiza katika siasa kwa kushabikia CUF, kitu ambacho kinawafanya washindwe kuwajibika kikamilifu kwa umma.

Tuhuma hizi zimetolewa na mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM (Nec), Zainab Khamis Shomari alipokuwa akizungumza ofisini kwake Kisiwani hapa jana. Alisema polisi wengi wamejawa na itikadi za kisiasa ndani ya mioyo yao hivyo inakuwa vigumu sana kufaya kazi kwa haki.

Mjumbe huyo wa Nec kutoka mkoa wa Kusini Pemba na ambaye pia ni katibu wa CCM wilayani Chake Chake alisema kwa muda mrefu sasa wamekuwa wakifanya kazi kwa misingi ya itikadi za kisiasa.

"Hakuna siri tena ni jambo ambalo kila aliye Pemba analijua; polisi wamekuwa mashabiki wakubwa wa CUF na ndio maana utendaji wa kazi zao unakuwa mgumu kwa kuwa wanaingiza ushabiki wa kisiasa katika kazi," alisema mjumbe huyo.

Katibu huyo alisema kwamba ni jambo la kusononesha kuona watumishi wa polisi wametingwa na siasa huku wakitelekeza majukumu ambayo kimsingi hawapaswi kujiingiza katika masuala hayo na kumtaka Mkuu wa Polisi, Inspekta Jenerali Said Mwema kuichukulia hali hiyo kwa umakini wa hali ya juu.

"Wananchi wa Pemba imani yao imebakia kwa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania(JWTZ)... sio tena kwa polisi. Huwezi kuwategemea askari ambao ni manazi wa siasa katika hali kama ya Pemba," alisema Zainab ambaye aliwahi kuwa Naibu Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii Zanzibar katika kipindi cha mwaka 2000 hadi 2005.

Mjumbe huyo wa Nec alishauri serikali kufanya kila iwezalo kutafutia ufumbuzi tatizo hilo ikiwa pamoja na kuwahamisha askari ambao wanajishughulisha na siasa kwenda mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara , ili kupunguza na kuondoa kabisa ubovu wa polisi wasiofuata maadili ya kazi zao.

Shomari alitoa mfano wa wakati wa zoezi la uandikishaji wapigakura katika daftari la kudumu katika mkoa wa Kaskazini Pemba ambako polisi waliokuwa kazini walishindwa kuwaondoa wafuasi wa CUF, waliokuwa wakijikusanya katika baadhi ya vituo vya uandikishaji licha ya sheria kueleza kwamba, hakuna mtu anayeruhusiwa kuingia au kukaa ndani ya mita 200 ikiwa hausiki na uandikishaji.

"Sheria iko wazi... inasema kwamba hakuna mtu atakayeruhusiwa kukaa ndani ya mita 200 katika kituo cha uandikishaji, lakini tumeshuhudia watu wakiwa ndani ya mita tano hadi kumi lakini polisi wanawatazama na unapowaendea kuwaeleza wanasema wao hawana vya kuwafanya," alilalamika Zainab.

Alisema kwamba katika tukio lililotokea hivi karibuni wafuasi wa CUF walijikusanya kwenye ofisi ya mkuu wa wilaya ya Chake Chake kwa nia ya kushinikiza kusajiliwa, kupatiwa vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi na ilibidi askari wa JWTZ kuwatawanya wafuasi hao.
"Ni mara ngapi JWTZ itasaidia wakati ina majukumu mazito ya kulinda mipaka ya nchi na kazi nyinginezo. Jeshi la Polisi ndilo lenye majukumu hasa ya kulinda usalama wa raia na mali zao... nafikiri ipo haja kwa IGP (Said Mwema) kulipanga upya katika uwajibikaji hasa kisiwani Pemba," alisema kada huyo wa CCM.
Tuma maoni kwa Mhariri
 
Back
Top Bottom