Polisi Dar yatangaza vita dhidi ya majambazi

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,790
288,005
Polisi Dar yatangaza vita dhidi ya majambazi

• Yasema hakuna jambazi atakayeponyoka

na Happiness Katabazi
Tanzania Daima~Sauti ya Watu

JESHI la Polisi, Kanda Maalum ya Dar es Salaam, limetangaza vita dhidi ya majambazi na kuwataka wananchi wazidi kutoa ushirikiano kwa kuwapa taarifa za siri ili kufanikisha kukabiliana na matukio ya ujambazi yanayorejea kwa kasi jijini.

Kauli hiyo ya polisi imetokana na tukio la juzi ambapo majambazi walivamia kituo cha mafuta cha Gapco, kilichopo karibu na makutano ya Barabara ya Kawawa na Mandela na kupora zaidi ya sh milioni 200 pamoja kusababisha kifo cha mhasibu wa kituo hicho aliyeuawa kwa kupigwa risasi na majambazi hayo.

Kaimu Kamanda Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Evarist Mangalla, alisema katika mkutano wake na waandishi wa habari jana kuwa jeshi lake limejipanga kukabiliana na hali hiyo na kuwaonya watakaojihusisha na matukio ya ujambazi kuwa lazima watakamatwa.

“Jeshi la polisi linazidi kutoa pongezi kwa raia wema wanaolisaidia jeshi hilo kwa kutoa taarifa ambazo zinaleta mafanikio katika kuutokomeza mtandao wa ujambazi, tunaahidi tutaendelea kusimama imara ili kukabiliana na majambazi hayo,” alisema Kamanda Mangalla.

Alisema taarifa za siri kutoka kwa wananchi, ndizo zilizoisadia polisi juzi kuzima tukio lingine la ujambazi, lililopangwa kufanyika katika kiwanda cha Cello Plastick, kilichopo barabara ya Mbozi, eneo la Chang’ombe ambapo majambazi watatu waliuawa.

ACP-Mangalla alisema walifanikiwa kuzima tukio hilo kwa sababu Octoba 5 mwaka huu, walipata taarifa kutoka kwa raia wema kwamba kuna kikundi cha majambazi kimekula njama za kutaka kuvamia na kupora fedha kiwandani hapo.

“Baada ya taarifa hizo, polisi wetu walianza kufuatilia ili kubaini kundi hilo la majambazi na kuweka mtego wa kuwanasa na walifanikiwa,” alisema Kamanda Mangalla.

Alisema katika ufuatiliaji zaidi, polisi walibaini mpango wa uporaji huo; uporaji huo ungelifanyika juzi asubuhi na baada ya taarifa hizo kubainika, waliandaa mtego kuwanasa.

“Kweli, juzi saa 5:45 majambazi yaliyotarajiwa kufika katika eneo hilo, yalifika yakiwa na magari mawili na moja kati ya magari hayo namba zake zilisomeka T.619 AMD na jingine halikuweza kusomeka namba kwani baada ya kugundua wamezingirwa, walitoa bunduki walizokuwa nazo na kuanza kuwafyatulia askari ili wawadhuru na wapate nafasi ya kutoroka,” alisema Mangalla.

Alisema polisi kuona maisha yao yako hatarini, walijibu mapigo na kuyafyatulia risasi majambazi hayo na kuyajeruhi; yalikufa yakiwa njiani kuelekea katika hospitali ya Amana.

Alisema majamabzi hayo yalipopekuliwa, yalikutwa na bunduki aina ya bastola yenye namba 016080 aina ya Browning iliyotengenezwa nchini Czechoslovakia.

Aidha alisema gari aina ya Toyota Chaser iliyokuwa inatumiwa na majambazi hayo ilibandikwa namba za bandia zilizosomeka T.989ATB na zilipobanduliwa namba za juu, ndani zilikutwa namba nyingine zilizosomeka T.447 AKM.

Kati ya majambazi hao, wawili wametambuliwa kwa majina ya John Philipo Komba ambaye alikutwa na shahada ya kupigia kura mfukoni mwake iliyotolewa Desemba 3 mwaka huu.

Hata hivyo alisema katika tukio hilo, hakuna askari aliyejeruhiwa kwa risasi isipokuwa askari watatu walipata maumivu kutokana na msukosuko wa kujigonga kwenye magari waliyopanda wakati wa mapambano hayo.

Aliwataja askari hao kuwa ni D.2927 D/SGT Joseph,D.8408 D/CPL Peter na F.5371 D/C Issa ambao walitibiwa na kuruhusiwa na hali zao zinaendelea vizuri.

Tukio hilo lilitokea siku moja na lile la uvamizi wa kituo cha mafuta cha Magomeni. Uvamizi huo, ni wa kwanza kwa ukubwa kutokea tangu Kamanda Suleiman Kova akabidhiwe Kanda Maalum ya Dar es Salaam, na kusababisha kifo cha mfanyakazi mmoja wa kituo hicho.

Mapema wiki hii polisi mjini Arusha walipambana na majambazi kwa zaidi ya saa 6 katika nyumba moja walimokuwa wamejificha na kusababisha vifo vya majambazi wawili, huku polisi mmoja akijeruhiwa na kushonwa nyuzi sita kichwani.
 
Watanzania tumechoshwa na mwenendo wenu polisi wa kupambana na majambazi pale tu wimbi la ujambazi linapoongezeka nchini badala ya kuifanya kazi hiyo 24/7 na kwa siku 365. Kampeni hizo huchukua mwezi au sana sana miezi miwili ambapo majambazi huamua kuweka silaha zao chini na kusubiri kuona ulinzi mnaopaswa kuwapa Watanzania na mali zao umezorota na wao hurudi tena na nguvu mpya na kuziweka juu roho za Watanzania.

Kitu kingine kinachoshangaza ni huu mtindo wenu wa kutangaza hadharani kampeni dhidi ya majambazi ambazo zinawapa faida majambazi hao na kuamua kukaa pembeni wakati polisi 'wakiendelea na kampeni' zao za kupambana na majambazi. Hivi hamuwezi kufanya kampeni dhidi ya majambazi kimya kimya bila kutangaza katika vyombo vya habari ili kutowapa faida majambazi hao!?

Watanzania pia wanakufa kwa ajali za kutisha barabarani kutokana na ajali nyingi ambazo zinaweza kabisa kuzuilika lakini kutokana na uzembe mkubwa na ulaji rushwa wa polisi ajali hizo mmeshindwa kuzuia na matokeo yake ni kupoteza maisha kwa Watanzania wengi, kupata vilema vya maisha na uharibifu wa mali.

Badala ya kuhakikisha usalama wa Watanzania barabarani ni mwaka mzima, mna wiki yenu moja mliyoipa jina 'wiki ya usalama barabarani' ambayo kazi mnayopaswa kuifanya mwaka mzima huwa mnaifanya kwa wiki hiyo moja. Katika wiki hiyo huwa mnaangalia kama maderena wana leseni zinazowaruhusu kuendesha, magari yao yana hadhi ya kuwa barabarani, abiria hawajazidi uwezo wa gari n.k. pamoja na hayo bado polisi ambao ni wala rushwa hutumia wiki hiyo kujitajirisha kwa kuhakikisha wale wote wanaoptikana na kosa moja au zaidi basi hutoa rushwa na kuachiwa huru.

Kuna haja ya kuangalia utendaji wenu wa kazi kila siku ili kuhakikisha usalama wa ria na mali zao badala ya kufanya kampeni kwa wiki moja tu kama 'wiki ya usalama barabarani' au kusubiri mpaka wimbi la ujambazi liongezeke nchini ndiyo muingie kazini kupambana na majambazi. Mnalipwa mishahara kwa mwaka mzima, hivyo wakati umefika sasa wa kulisafisha jeshi la polisi ili kuongeza ufanisi wa jeshi hilo na wale wahuni ndani ya jeshi hilo wanaoshirikiana na majambazi wafukuzwe mara moja.
 
Vita dhidi ya majambazi haistahili kutangazwa maana inatakiwa kuendelea 24/7/365/366! Hizi kampeni hazina maana kwa sababu kila kampeni ina mwisho wake na vita hii haipaswi kuwa na mwisho!

Amandla........
 
Vita dhidi ya majambazi haistahili kutangazwa maana inatakiwa kuendelea 24/7/365/366! Hizi kampeni hazina maana kwa sababu kila kampeni ina mwisho wake na vita hii haipaswi kuwa na mwisho!

Amandla........

Tatizo lililopo baadhi ya polisi ni washiriki wa huo ujambazi, hasa kwa kutoa habari zinazowasaidia majambazi, pia majambazi wakiandaa kuiba mahali fulani huwajulisha washirika wao(baadhi ya polisi), na polisi baada ya kupewa hiyo deal wanachofanya ni kuwa mbali na eneo la tukio ili ujambazi ufanyike bila vikwazo. hata wakuu wa mikoa wa polisi wamewahi kuhisiwa kujihusisha au kulinda ujambazi kiasi mmoja wapo alikutwa na Tshs 200,000,000 kwenye account yake. swali alizipata wapi??. jibu ndo hilo, ujambazi hautaisha iwapo baadhi ya hao polisi wataendelea na mwenendo huo
 
Wanatakiwa waangaliane wenyewe polisi maana majambazi wengi wemedumu kutokana na kushikiliana na polisi.
 
Back
Top Bottom