Pinda,Ghasia wazidi kubanwa bungeni

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,299
33,080
Ezekiel%20Wenje.jpg

Mbunge wa Nyamagana, Ezekia Wenje,(Chadema)


Wabunge wameendelea kuwang’ang’ania kooni Waziri Mkuu Mizengo Pinda, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, (Tamisemi), Hawa Ghasia wakiwataka wasisubiri kutimuliwa bali wapumzike nyadhifa zao kistaarabu kwa kushindwa kuwajibika.

“Inatakiwa kabla ya Mkutano huu wa Bunge kumalizika, mawaziri kadhaa hapa hawastahili kuwapo kwa kushindwa kuwajibika katika nafasi zao na hivyo kusababisha ufisadi na ubadhirifu kwa fedha za umma,” alisema Mbunge wa Muhambwe, Felix Mkosamali (NCCR-Mageuzi), wakati akichangia mjadala wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa, Kamati ya Bunge ya Bajeti na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali jana.

“Huwezi kila mwaka wabunge wanakulalamikia waziri kuhusu rushwa katika wizara yako halafu hakuna hatua zozote zinazochuliwa kudhibiti hali hiyo…unastahili kuondolewa.

Alisema hata wafadhili waliotoa fedha zao Tamisemi kiasi cha Sh. milioni 600 na zikatafunwa wanamtaka Rais Jakaya Kikwete, amfukuze waziri kwa kushindwa kuwajibika.
“Sasa kama haya yote ya rushwa yanafanyika katika wizara yake, yeye (waziri) anafanya kazi gani, kwanini asipigiwe kura ya kutokuwa na imani naye.

“Spika unapaswa kuliongoza Bunge kumfukuza Waziri Mkuu kwa mujibu wa Ibara ya 52 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania…Waziri Mkuu anapaswa kupumzika kistaarabu sasa, Waziri Ghasi pia naye anapaswa kupumzika, lakini wakishindwa kufanya hivyo wenyewe hawa wote ni kupiga nje, kufukuza tu,” alisema.

Mbunge wa Viti Maalum, Pauline Gekul, (Chadema), alisema ni vizuri Waziri Mkuu Pinda akaondoka mapema na mawaziri wake, lakini akaonya kwamba siyo vizuri kuwaondoa hao kwani hakutakuwa na wengine wenye nafuu kwa sababu ya mfumo uliowaweka madarakani ni huo huo, hivyo unapaswa kuondolewa.

“Hata tukiwaondoa hawa, tatizo linabaki pale pale, mfumo. Hawa wote hawafai, wananuka rushwa.…Dawa yao ni Watanzania kuwaondoa kwenye masanduku ya kura za uchaguzi,” alisema.

Alisema kwa mfano, vitabu 2,546 vya makusanyo ya kodi mbalimbali katika halmashauri havijareshwa na ni fedha kiasi gani ambazo zimekusanywa kupitia vitabu hivyo, lakini kila wakati serikali inasema chakula hakitoshi kwani sungura mwenyewe ni mdogo.

“Hivi ni kweli Watanzania waangalie tu fedha zao zinavyoliwa…tatizo siyo kwamba fedha zetu ni chache ila ni chama ambacho kimekufa ganzi…kwanini waziri asiwajibike.

Lakini alisema, “haya yote yanavumilika ila wapo baadhi yetu ambao wameamua kuichagua CCM, sasa ni vema wakafanya maamuzi magumu…nchi yetu siyo maskini kiasi hicho, lakini siyo vizuri kuwaondoa hawa, tatizo ni mfumo wenyewe.”

Baada ya Pauline kumaliza kujadili kamati hizo, Mnadhimu Mkuu wa Bunge, William Lukuvi, ambaye ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera na Uratibu) alisimama na kusema, “nimemsikiliza mheshimiwa kwa muda mrefu, sikupenda kumkatisha nilitaka amalize kwanza mchango wake, lakini mchango wake wote umejaa matusi na lugha ya kuudhi, tunataka afute kauli yake.”

Hata hivyo, Mbunge wa Nyamagana, Ezekia Wenje, (Chadema), aliposimama na alimtetea Pauline akisema katika mchango wake hakutoa matusi yoyote ingawa maneno yake yanachoma sana kwa upande mmoja wa CCM.

“Lukuvi ni mwongo na athibitishe na siyo vizuri kwa mzee kama yeye kutoa uongo bungeni,” alisema na kutaka mwongozo wa Naibu Spika Job Ndugai, ambaye hata hivyo aliahidi kutolea ufafanuzi/majibu mwishoni mwa kikao hicho, lakini hakuweza kufanya hivyo.

Mbunge wa Mufindi Kaskazini, Mahmood Mgimwa, (CCM), alikiri kwamba kuna udhaifu na ubadhirifu serikalini na akataka hatua za msingi za kumaliza tatizo hilo zichukuliwe.

“Ni kweli kwenye matumizi mabaya ya fedha, Serikali ya CCM tunalalamikiwa,” alisema.





CHANZO: NIPASHE

 
Ghasi si shemeji ? Ndiyo maana kiburi mingi na ni mwenzetu kwa upande ule ? Pinda mh naona sasa kinanuka lakini wanao lia lia ni wapinzani CCM hawana utamaduni wa kuwaunga mkono sijui kama kuna lolote .
 
Back
Top Bottom