Papa na Nyangumi: Nani atawavua tuwale?

Rev. Kishoka

JF-Expert Member
Mar 7, 2006
4,526
1,529
Papa na Nyangumi: Nani atawavua tuwale?
Katika bahari, kuna samaki wakubwa wawili, Papa na Nyangumi. Samaki hawa wanaogopewa kwa kuwa ni wakubwa na wana uwezo wa kudhuru kila kilicho karibu yao.

Tumeshasikia simulizi nyingi za watu kuuawa na kuliwa na Papa Yule anayeitwa kwa Kiingereza Great White, tunajua kuwa Nyangumi ni mkubwa kama Lori la Scania na mlo wake ni mkubwa.

Lakini pamoja na sifa zote za hawa samaki, bado Mwanadamu ana uwezo wa kuwavua kama samaki wengine, kwa kutumia mitego mikubwa na maarifa kuwazidi akili. Kwa hiyo dhana ya kuwa Papa na Nyangumi hawawezi kuvuliwa ni batili! Wanavulika kirahisi tuu, na hivyo ubabe wao ndani ya Bahari hauna nguvu yeyote pale panapokuwa na dhamira ya kuwavua!

Kwa muda wa wiki mbili hivi, Taifa letu limekumbwa na malumbano kati ya Wafanyabiashara kadhaa, wakinyoosheana vidole vya nani kati yao ndie mhujumu au fisadi, nani kati yao ni Papa na Nyangumi amb aye hula kila kilichomo baharini.

Nasi kama Taifa, tumegeuka na kuyumbishwa na malumbano hayo, kama ushabiki wa Simba na Yanga.

Lakini katika haya yote yanayosemwa na kudaiwa kati ya wafanyabiashara hawa, Mchungaji anajiuliza, je wale wenye Mamlaka ya kulinda Sheria na Haki Tanzania wako wapi?

Je wamekaa mguu pande wakipagawa kutokana na mlipuko wa mabomu Mbagala? Au Wanatahayari kutokana na Rais wa Zanzibar Karume kushindwa kuhudhuria sherehe za kuadhimisha miaka 45 ya Muungano?

Kinachonishangaza mimi ni jinsi kila mmoja wa hawa wafanyabiashara wakubwa nchini mwetu alivyo na habari kuhusu mwenzake. Kila mmoja wao anajua undani wa biashara za mwenzake mpaka nambari za akaunti za Benki au mkopo jambo ambalo kwa mujibu wa kanuni za Kibenki, ni kati ya Benki na Mteja au Serikali pindi inapokuwa inafanya upelelezi.

Bwana Mengi, alianzisha hii Sandakalawe, akatamka kuna Mafisadi Papa, akawataja majina, sikumbuki ni ushahidi wa namna gani aliutoa, lakini alitaja majina na watu wa Serikali na Chama Tawala, wakakasirika.

Si mara ya kwanza kwa Reginald Mengi kutoa tuhuma kubwa namna hiyo, ni jambo ambalo kalifanya miaka nenda rudi.

Waliotuhumiwa na Mengi, nao wakarudi mapigo, Maji kafungua kesi ya madai, somaiya anajiandaa kufungua kesi, lakini Rostam Aziz akaamua kumjibu Mengi kwa kutumia mkutano wa waandishi, ambapo alitoa vielelezo vingi kana kwamba yeye ndiye benki zilizotoa mkopo kwa Mengi au yeye ndiye Serikali mwenye mamlaka kumchunguza Mengi kama si mkusanyaji madeni aliyeombwa akamate mali za mengi zitaifishwe.

Kilichonishangaza sana ni katika orodha ya Rostam ya kuutaja Unyangumi wa Mengi, alitoa maelezo ya kina ya mambo ambayo Mengi alikumbana na ama wafanya biashara wenzake au waliomo Serikalini pale Mengi alipolalamika kuwa kadhulumiwa au hakutendewa haki.

Rostam kawataja Lowassa, Mramba, Masha, Manji, Somaiya, na Malima kati wengi aliodai wamefanyiwa visa na Mengi kama vile wameonewa, kinachoniudhi kwa hawa sita waliotajwa kuonewa, wao wenyewe hawana rekodi nzuri na wanatuhuma nyingi mno ambazo mpaka leo hazijatatuliwa.

Najiuiliza tena, inakuwaje leo Mtuhumiwa mkuu wa Ufisadi, ushahidi wake ni kuwataja watuhumiwa wenzake na si kujisafisha yeye kwanza?

Kitendo cha kuwepo kwa Masha katika orodha ya Rostam kujitetea au kumuumbua Nyangumi, kinanipa tatizo, Masha ambaye ni waziri wa Mambo ya Ndani, ana uwezo mkubwa sana kisheria kufanya alilofanya Rostam kwa kutamka wazi masuala binafsi ya Kibenki kama akaunti namba, na si Rostam.

Swali linakuja tena, Rostam alipata wapi namba za akaunti za Mengi? Je mabenki yote ambayo Mengi alikopa ni mali ya Rostam?

Nikigeuka kwa Mengi, naye katoa tuhuma nyingi, kana kwamba ana ushahidi tosha. Lakini hata pamoja na kuwa Rostam hana mamlaka yeyote (huenda anayo, ni mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM!), lakini madai ya Rostam kuhusu vitendo vya Mengi si ya kupuuziwa hata kidogo!

Je Mengi pamoja na kudai kalipa madeni , iweje kila siku yeye ndiye analia moto, samba na nyuki? Kwa nini Mengi anakuwa mzito kuwajibika inavyopaswa, kama kulipa madeni au kutojiingiza katika vitendo vichafu huku akijifanya ni mtakatifu?

Nashukuru hawaPapa na Nyangumi wanajitoa hadharani tuwaone, lakini lengo langu leo ni kuuliza, wale wenye mamlaka ya kuongoza nchi yetu wako wapi?

Mabenki yanafanyia usailiwa kihasibu, ni lini yamemfikisha Mengi mahakamani kwa kushindwa kulipa mikopo na kukimbilia kuuza habari za Mengi kwa Rostam?

Je Serikali yetu iko wapi? Tuhuma hizi kutoka kila upande ni kubwa sana na si za kupuuziwa, je Serikali yetu imefanya nini kupata ufumbuzi wa mambo haya ya uhujumu uchumi wan chi yetu yanaofanywa na Papa na Nyangumi?

Ni lini Serikali itakuwa mvuvi stadi iweze kuwavua hawa samaki wakubwa wanaosemekana ni hatari? Ili tuweze kula nyama zao na mafuta yao kututengenezea mishumaa na sabuni?

Tumechoka kusikia maigizo na ngonjera, tunataka Serikali inayofanya kazi, Serikali itakayohakikisha kuwa mazingira ya haki na sheria yanafuatwa na kuthaminiwa na kila mtu aliye ndani na nje ya nchi yetu.

Ni aibu sana kusikia malumbani kama haya, na cha kujiuliza ni hivi, ikiwa haya tunayoambiwa ni ya Mengi , Rostam, Somaiya, Manji na wachache, je Wafanyabiashara wengine wote nao ni mchezo huo huo?

Je leo tutashangaa Benki zetu kushindwa kufanya kazi kutokanana mikopo isiyolipwa kutokana na mianya iliyotengenezwa kukidhi mahitaji ya Wafanyabiashara mashuhuri? Leo hii pesa zinapohujumuwa Benki Kuu na kila mtu anakana, na mpaka Taifa linagundua tunaingia hasara, ni wajibu wa nani kuhakikisha kuwa tabia kama hizi haziiendelei?

Je tunamwambia nini Mtanzania mfanyakazi na Mkulima ambaye kila siku anavuja jasho na akitaka kuinua ubora wa maisha yake, hata kupata mkopo kulipia matibabu, elimu ya watoto, kujijengea nyumba, kununua gari, kununua zana za kilimo na pembejeo au kupata mtaji wa kujianzishia biashara, Mtanzania huyu anapigwa dana dana na kunyimwa mkopo, lakini tuna kundi la watu maarufu ambao wakiingia Benki au kupiga simu tu, mkopo unatolewa bila masharti na malipo ni mpaka siku watakapoamua kulipa?

Imekuaje tumefika hapa tulipo ambapo tuna taifa la wanaojifanyia kila wanalotaka kutokana na nguvu na umaarufu wao na si kufuata kanuni na maadili?
Serikali ambaye ni Mvuvi Mkuu, nasubiri kauli yako rasmi itakayoandamana na vitendo na si manung'uniko ya chini chini kama ya Sophia Simba!
 
mkuu umekuwa nyutro,
safi sana ,nchi hii haina serikali, wote wezi kaka,
 
Mkuu Rev,

Majuzi kuna mwanasiasa mmoja alitamka hadharani kwa kujiamini kabisa kwamba ukiacha Dk Shein, wote serikalini ni mapapa na manyangumi.

Mpaka sasa sijasikia mtu yeyote serikalini akikanusha hii tuhuma.

Wavuvi (watu wenye nia ya dhati ya kukomesha ufisadi) wapo wengi ila wanakosa zana muhimu za kuvulia kama meli, drag nets, harpoon guns nk (yaani maarifa).

Haya masamaki makubwa yanatumia akili sana kufanikisha mambo yao. Inabidi wavuvi nasi kwa ujumla wetu tutumie maarifa na tuweke mikakati imara ya kuyavua haya masamaki makubwa. Kuonesha hasira tu haitoshi.

Corruption fights back.
 
Tatizo siyo kuwavua hawa papa na nyangumi. Tatizo muongoza meli anaelekeza meli kule wasiko ili tusiwavue. Politics za bongo ndizo hizo by June tutakuwa na jambo jingine la kuzungumzia then life goes on!!!!!!!!!!!!!!
 
Mchungaji,

such a well articulated analysis...kinachoshangaza kweli ni hawa wakubwa wetu wakiongozwa na Kikwete mwenyewe hadi kwa Pinda,kina Mwema na Manumba sijui wanafanya nini...achana na kina Sofia Simba na Mkuchika wasiokuwa na lolote...au ndo tukubali nchi imeshawekwa rehani?

Nasikia watu wanasema eti Pinda ndio ana msimamo,mbona yuko kimya mpaka sasa?
 
Tatizo siyo kuwavua hawa papa na nyangumi. Tatizo muongoza meli anaelekeza meli kule wasiko ili tusiwavue. Politics za bongo ndizo hizo by June tutakuwa na jambo jingine la kuzungumzia then life goes on!!!!!!!!!!!!!!

Kweli kabisa lakini pia Dr. Shein ambaye ndio anaonekana mwenye uwezo wa kuvua hao samaki maskini meli yake MV. VP sio ndefu enough kuwafikia papa na nyangumi... hawa samaki hukaa kina kirefu sana. Wanahitaji ile meli MV Presida... kuvuliwa.
 
Hivi kati ya Papa na Nyangumi yupi mwenye thamani kiliko mwenziwe
Halafu nasikia bei ya supu ya fins za papa zina bei mbaya sana kwa wenzetu
check picha







File:DSC_7334.JPG
 

Attachments

  • nyangumi.jpg
    nyangumi.jpg
    55.8 KB · Views: 43
  • papa.jpg
    papa.jpg
    6 KB · Views: 37
..wengi tunamangamanga kuukimbia ukweli.

..hebu tujiulize: kati ya Rostam na Mengi nani amemsetiri na kumkirimu Raisi wetu kumzidi mwenzake?

..mnafikiri Raisi wetu ana muunga mkono nani kati ya Mengi na Rostam.

..kwa taarifa yenu huu ufisadi wa sasa hivi hauwezi kushughulikiwa na serikali iliyopo madarakani.

..wale mawaziri[sophia simba,mkuchika] wa wizara nyeti walipotoa matamshi yale dhidi ya Reginald Mengi msifikiri hawana akili timamu wale.

..kwa kifupi ufisadi huu hauwezi kushughulikiwa na Raisi na serikali iliyopo madarakani.
 
Rev. Kishoka,
Ahsante sana kwa mchango wako mzuri.

Nadhani tumepata vielelezo vya kutoka kwa Rostam dhidi ya Mengi na taarifa za magazeti zinasema kuwa ameuwasilisha katika taasisi husika kwa ajili ya uchunguzi.

Sasa nadhani Mengi naye awe muungwana awasilishe ushahidi kwa yale madai aliyoyatoa kwenye press conference yake siku chache zilizopita. Nimeona juzi ametuma wanasheria wake kujibu baadhi ya tuhuma zilizotokana na Press Conference ya Rostam. Kimsingi majibu ya tuhuma hizo ayawasilishe kule ambako tayari tuhuma zake zimepelekwa.
Jambo lingine ambalo ningependa Mengi alifanye ni kuthibitisha madai yake dhidi ya Rostam na wala si kumuuliza maswali juu ya mahusiano yake na Kagoda, Dowans na Richmond kwani maswali hayo si mageni yaliulizwa mara kadhaa na amekanusha. Mengi atusaidie kutueleza kiushahidi kuwa hayo mahusiano ushahidi wake ni huu hapa na si vinginevyo. Kwa kufanya hivyo atakuwa amefungua box ambalo halijawahi kufunguliwa kwa maana ya ushahidi thabiti.

Mwisho, ninaungana na wewe kabisa kuwa serikali inatakiwa iwaelekeze hawa wawili kufanya mambo yao kwa kufuata na kuzingatia sheria halali kwani hakuna ambaye yuko juu ya sheria baina yao. Kuendelea kuwaacha kutumia press kunazidi kuchanganya wananchi hasa pale maneno ya kiuchochezi yanapotumika.
 
Punda na wenzako wengi mlioko huku jukwaani ambao maoni yenu ni kuhakikisha kuwa wana wa nchi hawajadili kimakini hoja za ufisadi!!!!

Naomba nichukue nafasi hii kuwahakikishia kuwa saa ya kupambana kwa uwazi dhidi ya ufisadi imefika. yale yaliyokuwa ndoto miaka mitano iliyopita sasa yanawezekana.
  1. Nani aliwaza kuwa ingewezekana kutaja majina ya viongozi wa serikali wanaoiibia nchi hadharani na mtajaji asikamatwe wala kushitakiwa?
  2. Nani aliwaza kuwa ingewezekana kumjiuzulisha Waziri Mkuu, tena mwenye nguvu na utukufu kama Lowasa?
  3. Nani aliwaza kuwa Rostam na kiburi chake angelazimika kuita waandishi wa habari na kujibu tuhuma dhidi yake hata kama kwa kejeli.
  4. Nani angeamini kuwa iko siku mawaziri wastaafu, makatibu wakuu, na makada wa CCM wangetinga Kisutu kujiba mashitaki ya rushwa na ufisadi dhidi yao?
Kwa mabadiliko na mwendo kama huo ninapenda nikuhakikishie Punda na wenzako kwamba MAMBO BADO. Yanakuja mengine mengi.

Wakati wa kunyamaza kwa uchungu kwa kuwa tu mkosaji ni Kada wa CCM umepita.
Wakati wa kunyamaza kwa kuwa tu mkosaji ni mfadhili mkuu wa CCM umapita.

Na nyakati zaja zenye makubwa zaidi ambapo watanzania wataanza kuheshimiwa kwa utu wao.

Mnalo hilo!!!!!!!!!!!
 
Kila jambo na majira na sababu zake. Wakati wa Mkapa alibana uhuru kiasi kuwa haya yasingekuwa wazi kiasi hiki. Haya yanayoibuka sasa yaliffanyika nyakati zilizopita.

Hili anguko halina budi kutimia kwani pale kiongozi mkuu mtawala wa nchi anapotumia ofisi yake vibaya basi maptokeo yake ndiyo kama haya ya kuinuka kwa rushwa kubwa na mwenyewe kushindwa kuituliza hali. Labda, tunashuhudia hii hali Tanzania sasa ikiwa ndio njia ya mpito kutoka utawala mkongwe wa ccm kuelekea utawala ambao watanzania watakuwa na sauti na mustakabali wa nchi yao.

Ili mbegu imee na izae mazao mengi haina budi kuoza..
 
Back
Top Bottom