Pamoja na madudu haya, mkulo kwake ni upepo tu, ...atapeta

builddontbreak

New Member
May 4, 2012
2
0
Wana jamii, nadhani si vema mkapitwa na habari hii kama ilivyoandikwa na gazeti la Jamhuri wiki hii:

Mkulo alivyopiga dili

Ijumaa, Mei 04, 2012


*Siri nzito zavuja alivyoishinikiza CHC iwauzie kiwanja Mohammed Enterprises
*Katika kumlinda Katibu Mkuu akanusha maelekezo aliyotoa Mkulo hotelini
*Soma mgongano wa kauli na nakala za mashinikizo ya Wizara ya Fedha kwa CHC


Siri nzito na zenye kuitia aibu Serikali juu ya mgogoro wa uuzaji wa kiwanja Na. 10 kilichopo Nyerere Road kwa kampuni ya Mohammed Enterprises Tanzania Limited (METL) zimeanza kuvuja.

Uchunguzi uliofanywa na Gazeti la Jamhuri kwa wiki tatu sasa na kufanikiwa kupata nyaraka nzito kutoka ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG), zinafanana kwa kila hali na nakala ya nyaraka zilizopo Wizara ya Fedha, unashitua.

Mwishoni mwa wiki bila kujua kuwa Jamhuri linazo nyaraka za siri, Wizara ya Fedha na Uchumi imetoa tangazo katika baadhi ya magazeti kwa lengo la kumsafisha Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo, katika kashfa ya kuuza Kiwanja Na. 10 kwa kampuni ya Mohammed Enterprises, lakini uhalisia wamemvua nguo.

Mkulo amefanya uamuzi wa ajabu kwa kuwashinikiza watendaji wa serikali kumuuzia kiwanja hicho Mohammed Enterprises.

Mgogoro wa kiwanja hiki una historia ndefu inayoanzia miaka 1990 pale kampuni kadhaa zilipokinyemelea ila zikashindwa kukinunua. Mgogoro huu ulikua zaidi baada uamuzi wa Kampuni ya Kurekebisha Mashirika ya Umma (PSRC) kumuuzia Mohammed Enterprises kiwanja Na. 192 mwaka 2003.

Kiwanja hiki Na. 192 au Na. 11 kama kinavyojulikana sasa, kilikuwa kinatumia barabara moja na kiwanda Na. 191 kilichokuwa kinatumiwa na Kampuni ya Biashara Dar es Salaam (DRTC). Katika mazingira yasiyoeleweka DRTC iliuziwa kiwanda Na. 191 na kikaamua kuziba njia inayokwenda kiwanja cha nyumba yake ambacho ni cha METL.

Mnunuzi wa kiwanja Na 191 aliyekuwa Meneja wa DRTC, Mery Msira, alikwenda Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam na kupewa kibali cha kuyatoza magari ya METL Sh 500,000 kila siku ya Mungu, kwa kutumia barabara inayokatiza kwenye kiwanja chake kama ilivyokuwa awali kabla ya wawili hao kuuziwa viwanja hivi.

METL waliamua kwenda mahakamani na wakapata hati ya zuio, inayomzuia Msira kufunga hiyo njia. Alichokuwa akilalamikia Msira ni kwamba magari ni makubwa na yanamkosesha raha katika biashara na wateja wake, hivyo kufidia bughudha wanayopata ni heri wafidiwe Sh 500,000 kila siku kama ushuru wa kutumia kipande hicho cha barabara kisichofikia mita 20.


PSRC waagizwa wamlipa Msira
Katika kipindi ambacho mgogoro huo ulikuwa unaendelea miaka ya 2000, aliyekuwa msaidizi wa Waziri wa Mipango wakati huo, Dk. Juma Ngasongwa, aliandika barua PSRC kushinikiza imlipe Msira fedha hizo alizoingia mkataba na Jiji la Dar es Salaam, kuwa magari ya METL yakikatiza kwenye kiwanja chake yalipa Sh 500,000 kila siku.

Fedha hizo hazikupata kulipwa kwani baada ya PSRC kuvunjwa, shughuli zake zikahamishiwa kwa Shirika Hodhi la Mashirika ya Umma (CHC), wao waligoma kumlipa na deni hilo ndilo linaloonekana kwenye vitabu vya CAG kuwa DRTC inaidai Serikali Sh bilioni 2.34.

METL wajaribu kununua kiwanja Na 10
Mwaka 1999 METL walipeleka ofa ya kununua kiwanja hiki Na 10 kwa PSRC na wakaahidi kuwa wangeweza kulipa dola 300,000 lakini PSRC ilikataa kuwauzia kiwanja hiki kwa maelezo kuwa fedha walizoahidi kutoa ni kidogo, hivyo waongeze bei hadi dola 500,000.

Kumbukumbu zinaonyesha kuwa baada ya pendekezo hilo pande zote mbili zilikaa kimya hadi mtaalamu Mkulo alipokutana na uongozi wa METL Juni 8, 2010.


Mkutano wa Mkulo na METL

Juni 8, 2010 zikiwa ni siku chache kabla ya Baraza la Mawaziri kuvunjwa na kuingia kwenye mchakato wa Uchaguzi Mkuu, Mkulo alianzisha mchakato wa kumuuzia kiwanja hicho METL kwa kuitisha mkutano kati yake, watendaji wa CHC wakiongozwa na Metusela Mbajo na Ridhiwani Masudi aliyemwakiliza Msajili wa Hazina.

Katika mkutano huo walirejea historia ya mgogoro wa kiwanja, na ndani ya siku tatu, METL waliandika baraua kwa Msajili wa Hazina yenye Kumb. Na. METL/PLOT/2010/10-06 ya Juni 20, 2010 ikimweleza kuwa Waziri wa Fedha Mkulo alikuwa amekabidhi suala la kiwanja kwake (Msajili wa Hazina), na mambo makuu ya msingi yalikuwa mawili.

Kwamba walijadili suala la mgogoro wa kiwanja Na 192 kutokuwa na njia uliodumu kwa muda mrefu na kuwakosesha uwezekano wa kupata Hati ya Kiwanja (kwa mujibu wa sheria kiwanja kisicho na njia hakipatiwi hati). Suala la pili katika barua hiyo iliyosainiwa na G. Dewji, wakasema sasa wapo tayari kukinunua kiwanja hicho kwa bei iliyopendekezwa na PSRC mwaka 1999 ya dola 500,000.

Katika mkutano na Mkulo METL waliihakikishia Serikali kuwa pamoja na nia yao ya kununua kiwanja Na 10, METL ilikuwa tayari kulipa gharama yoyote, iwe ya kesi au itakayotokana na uamuzi huo wa kuuziwa kiwanja hicho.


Jeetu Patel awawekea ngumu METL

Mfanyabiashara maarufu wa jijini Dar es Salaam, Jeetu Patel, wakati mgogoro huu unaendelea yeye ndiye aliyekuwa mpangaji katika kiwanja Na 10 kupitia kampuni yake ya Noble Azania Investment (NAIL). Kampuni hii ilipinga wazo lililokuwa limetolewa kuwa sehemu ya kiwanja Na 10 imegwe na kumtengenezea barabara METL. Ilifungua kesi mahakamani na kupewa hati ya zuio.

Kuona hivyo, METL iliamua kununua kiwanja hicho Na 10 kwa Sh bilioni 2.046 na akasubiri kampuni ya Jeetu Patel imalize muda wake wa upangaji afanye marekebisho atakayo. Ikumbukwe kiwanja hiki kilikuwa mali ya TANGOLD, kampuni ya kuchonga madini iliyoishia kuvunjwa kwa aibu kubwa, ila mitambo yake iliendelea kubaki kwenye kiwanja hicho.


Shikizo la Mkulo lilivyoanza

Baada ya barua hii ya METL waliojitoa muhanga, Msajili wa Hazina kwa niaba ya Katibu Mkuu, katika barua aliyoiandika Julai 5, 2010 na kusainiwa na Ridhinwani Masudi, alimwandikia Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa CHC Mbajo, akimtaka atekeleze yaliyomo katika barua ya METL ama kwa kumuuzia kiwanja Na 10 kwa kumpatia njia ya kufika kwenye kiwanja chake Na 11. Barua hii ina Kumb. TYC/A/290/13.

Mkulo alipoona agizo lake halijatekelezwa kwa miezi mitatu, ilipofika Oktoba 1, 2010 zikiwa ni siku 30 kabla ya uchaguzi, Wizara ya Fedha kupitia kwa Msajili wa Hazina, Geofrey Msella, kupitia barua yenye Kumb. Na TYC/C/180/85/59, iliandika barua yenye kichwa cha habari kisemacho:-

Yah: Uuzwaji wa Kiwanja Namba 10 Nyerere Road kwa Mohammed Enterprises Tanzania Limited. Barua hiyo iliendlea kusema: "Tafahdali, rejea maelekezo ya Wizara ya Fedha na Uchumi kuhusiana na mchakato wa kutatua suala la maingiliano kati ya DRTC Trading Company Limited na METL.

"Wizara ya Fedha na Uchumi ingependa kupata taarifa ya utekelezaji wa suala la Mohammed Enterprises Limited la KUUZIWA kiwanja Na. 10 Nyerere Road ili kumuwezesha kupata njia ya kuingilia kwenye Godowns zake bila kupitia Kiwanja Na. 192 Nyerere Road kinachomilikiwa na DRTC Trading Company Limited.

"Pamoja na kukutaka kumaliza mzozo wa siku nyingi uliopo, unatakiwa pia kuhakikisha kwamba wote waliouziwa maeneo wanapewa hatimiliki kwa maeneo yao husika.

"Nashukuru kwa ushirikiano wenu.
G. M. K. Msella.
Kaimu Msajili wa Hazina"

CHC baada ya kupata barua hiyo walifanya uthamini na waliwaeleza Hazina kuwa kumuuzia Mohammed Enterprises kiwanja hicho ilikuwa ngumu, kwani kulikuwapo na kesi mahakamani, lakini pia kwa kufuata sheria ya ununuzi wa umma, ilibidi kutangaza kiwanja hicho na kuwashindanisha wazabuni.

Hata hivyo, shinikizo lilizidi kuwa kali ikabidi Bodi ya Wakurugenzi wa CHC ikutane Aprili 2, 2011. Tena walikutana siku ya Jumamosi, ambapo walikutana wajumbe wa Bodi wakiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi wakati huo, Profesa Hamisi Mahigi, Geoffrey Msella, ambaye ni Msajili wa Hazina, Dk. Raphael Chegeni, Aloyce Kimaro na Alhaj Shaweji Abdallah.

Watendaji waliohudhuria kikao hicho ni Metusela Mbajo (Ag. DG – CHC), Joseph Hellela, Albert Semng'indo, Dome Masolosha na Germana Ibreck.

Ajenda ilikuwa ni kujadili uuzaji wa Kiwanja Na 10. Kikao kilipokea taarifa ifuatayo:- "Moja, kumekuwa na mgogoro wa muda mrefu wa kutokuwa na barabara ya kuweza kufika katika Kiwanja Na 11 kinachomilikiwa na METL bila ya kupitia katika Kiwanja Na. 192 kinachomilikiwa na DRTC.

"Mbili, METL amekuwa akitumia barabara inayopita katika kiwanja cha DRTC ili kufika katika maghala aliyouziwa na Serikali kupitia PSRC; tatu, hali hii imezua mgogoro kati ya DRTC na METL na pia kuihusisha Serikali; nne, Kufuatia uchambuzi kuhusu mgogoro huu, Waziri wa Fedha alishauriwa akubali na akaagiza CHC kukiuza kiwanja Na. 10 kwa METL kwa bei ya soko na kwa kuzingatia sheria na taratibu; na tano, agizo hilo linalenga kutatua mgogoro uliopo kati ya DRTC na METL."

Baada ya wajumbe kupokea taarifa hiyo na kuijadili, Bodi ya Wakurugenzi iliamua yafuatayo:- "Bei ya Kiwanja kwa METL iwe ni ile iliyobainishwa katika "valuation" kama thamani ya soko inayozingatia kutoa njia ya barabara; mbili, Serikali isihusike tena na mgogoro wa barabara kati ya METL na DRTC mara baada ya METL kuuziwa kiwanja Na. 10; tatu, Kiwanja husika kiuzwe haraka ili Serikali iondokane na hasara inayotokana na mgogoro uliopo kati ya DRTC na METL.

"Tatizo la kisheria kati ya Serikali na Noble Azania Food Limited kuhusu ukodishwaji wa kiwanja hicho litakuwa limetatuliwa kwa sababu METL amekubali kuchukua matatizo yote (all encumbrances) yanayohusu kiwanja husika; tano Waziri wa Fedha ashauriwe kuhusu maelezo ya kikao ili kupata ushauri/uamuzi wake kulingana na mapendekezo ya Bodi na mwisho, menejimenti ishughulikie na kumaliza suala hili haraka iwezekanavyo."


Bodi yawasiliana na Mkulo

Baada ya uamuzi huo, Mwenyekiti wa Bodi Profesa Mahigi alimpigia simu Mkulo siku hiyo ya Aprili 2, 2011 na Mkulo akamwambia wakutane Morogoro kwani alikuwa anaelekea bungeni Dodoma.

Baada ya kauli hiyo, Profesa Mahiga na Mbajo walifunga safari na kwenda Morogoro. Walikutana katika Hoteli ya Morogoro na Mkulo akawaagiza wauze kiwanja hicho kwa Mohammed Enterprises.

Kutokana na maagizo hayo yalikuwa ya mdomo, Mbajo alimuomba Mwenyekiti wa Bodi amwandikie kwa maandishi maagizo hayo, naye akamwandikia hivi:-

"Yah: Maagizo ya Bodi ya Ufafanuzi wa Waziri wa Fedha, Mh. Mustafa Mkulo (MB).

"Tafadhali rejea mazungumzo ya kikao cha Bodi ya tarehe 2/4/2011 ambapo Bodi ilielekeza kwamba Shirika/Mwenyekiti wa Bodi (CHC) lipate ufafanuzi kutoka kwa Mh. Waziri wa Fedha kuhusu bei ya Soko/ya mthamini.

"Mimi kama Mwenyekiti wa Bodi na wewe kama Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa CHC tulionana na Mh. Waziri wa Fedha, akafafanua kuwa katika mazingira ya kiwanja Na. 10, bei inayopaswa kutumika ni ya mthamini wa kiwanja na hakuna haja wala umuhimu wa kutangaza.

"Kwa sababu Mh. Waziri wa Fedha amefafanua hilo, ninakuelekeza kwamba utekeleze uamuzi wa Bodi wa kumuuzia kiwanja Na. 10 METL kwa masharti kwamba yeye atahusika na matatizo yote ya kiwanja hicho bila kuhusisha serikali. Na kwamba yeye (METL) anauziwa kiwanja tu bila mashine/mitambo iliyopo ndani ya jengo.

"Tafadhali tekeleza.

Asante."


Mkulo amkwepa CAG

Kutokana na barua hii, katika ukaguzi maalumu uliofanywa na CAG, Ludovick Utouh, ndani ya CHC, Utouh alitaka kumhoji Mkulo hivyo akampigia simu kuomba miadi au kupanga utaratibu wa jinsi ya kukutana naye, lakini badala yake kusubiri aandikiwe barua ya kuhojiwa mara tu alipopigiwa simu na CAG Mkulo alichachawa.

Haraka haraka aliandika barua kinyume na taratibu za Serikali yenye Kumb. Na. TYC/B/70/2/03 na kuisaini yeye mwenyewe Mkulo huku akiigonga mihuri minne ya SIRI. Barua hiyo ya Oktoba 8, 2011 ilisema hivi:-

"Yah: Ukaguzi wa Consolidated Holding Corporation

"Tafadhali rejea mazungumzo yetu ya simu (UTOUH/MKULO) ya tarehe 07/10/2011 na ujumbe wa simu (SMS Message) wa tarehe 05/10/2011.

"Napenda kuthibisha niliyoyasema kwenye simu, "kwa maandishi" kwamba mimi kama "Waziri wa Fedha" sijawahi kutoa KIBALI kwa Mwenyekiti wa Bodi ya CHC, kumpa madaraka ya kuuza kiwanja au nyumba zinazomilikiwa au kutunzwa na CHC bila kufuata taratibu za zabuni au sheria ya manunuzi. Kama Mwenyekiti wa Bodi aliamuru Kaimu Mkurugenzi Mkuu na Bodi ya Wakurugenzi kuuza kiwanja cha Shirika bila kufuata taratibu za zabuni, alifanya hivyo kwa ridhaa yake mwenyewe na si kwa maagizo ya Waziri wa Fedha.

"Wizara ya Fedha ina utaratibu maalumu wa kushughulikia masuala yote yanayohusu mashirika ya umma. Kisheria huanzia kwa Msajili wa Hazina, kupitia kwa Katibu Mkuu – Hazina (PST/PMG) hadi kumfikia Waziri wa Fedha kwa uamuzi. Hivyo utaratibu uliotumiwa na Mwenyekiti wa Bodi na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa CHC ni kinyume na kanuni za utendaji kazi ndani ya Wizara ya Fedha na pia ni kinyume na kanuni za manunuzi.

"Nakushukuru sana kwa kunijulisha jambo zito ambalo sikuwa nikilifahamu. Natumaini kwa maelezo haya ya maandishi, ofisi yako sasa inaweza kukamilisha ukaguzi wa CHC.

"Mustafa Haid Mkulo (Mb.) Waziri wa Fedha."


Barua hiyo kama zilivyo nyingine, ilipelekwa nakala Ikulu, CHC na kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Msajili wa Hazina.

Kinachosikitisha, tangazo ambalo Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Ramadhani Khijjah ametoa magazetini Aprili 28, 2012 kumsafisha Mkulo pamoja na mawasiliano yote hayo na maelekezo kutoka katika wizara yake bila kutaja vikao alivyokutana na Profesa Mahigi na Mbajo, anasema halijui suala hilo. Je, nani mkweli, ni Mkulo au nyaraka rasmi zilizopo kwenye majadala ya serikali zinazoonyesha ushiriki wa Mkulo katika kushinikiza METL auziwe kiwanja Na. 10?

Ripoti ya CAG inasema Mkulo ameingilia mchakato wa uuzwaji wa kiwanja hiki, ila wizara yake inakanusha ripoti hii, pamoja na maelezo haya yasiyotiliwa shaka.
 
Hii nayo kali... napita tu hapa nitarudi saa 11 baada ya baraza jipya la mawaziri kutangazwa
 
Tanzania inatakiwa ijipange upya, kama sisi wazee tumeshindwa, tuanze na watoto wetu kuwafundisha kwa umakini kuhusu umuhimu wa kuwa waaminifu kwa madogo na makubwa, kuwa waadilifu, kuwa accountable kwa matendo yetu, kuwa WAZALENDO na hatimaye kuipenda kwanza NCHI yetu na siyo mtu wala chama/club. Pia MFUMO MZIMA una hitaji ku overhaul kupitia KATIBA MPYA.
 
Hilo dude lenye kipara ilitakiwa jumatatu liwe segerea yametuibia sana
 
Back
Top Bottom