Mag3
Platinum Member
- May 31, 2008
- 13,037
- 22,728
Dk Rashid awekasharti la kurudi Tanesco !
Na Sadick Mtulya - Mwananchi.
ALIYEKUWA Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme (Tanesco), Dk Idris Rashid ametoa sharti la kurudi kwenye nafasi hiyo nyeti baada ya kupendekezwa na bodi ya wakurugenzi.
Nafasi ya mkurugenzi mkuu wa Tanesco imekuwa wazi tangu Dk Idris alipostaafu baada ya kumaliza kipindi chake. Kustaafu wake kuliacha msuguano mkubwa baina ya bodi hiyo na menejimenti, na baadaye bodi ilipendekeza gavana huyo wa zamani wa benki arejeshwe kwenye kiti hicho.
Habari zilizolifikia gazeti hili zimeeleza kuwa Dk Rashid, ambaye mpango wake wa kununua jenereta za kampuni binafsi ya Dowans Tanzania Limited ulipingwa vikali na Bunge, sasa anataka wanasiasa wasimuingie kwenye kazi yake iwapo atarejea kuliongoza shirika hilo.
Kwa mujibu wa habari hizo, bodi ya Tanesco imefikia hatua ya kupendekeza Dk Rashid arudi Tanesco baada kuwepo na mgogoro wa kiutendaji baina yake na menejimenti ya shirika hilo.
"Kutokana na mvutano uliopo wa kiutendaji na matatizo yanayolikabili shirika kwa sasa, bodi inaamini Dk Rashid ndiye anayeweza kumudu hali hiyo," chanzo cha habari kililidokeza gazeti hili.
"Lakini moja ya masharti aliyotoa ni kutaka asiingiliwe kiutendaji na wanasiasa"
Mwenyekiti wa bodi ya wakurugenzi ya Tanesco, Peter Ngumbuli jana hakutaka kuthibitisha suala hilo na kueleza kwa kifupi kuwa, bodi imeshamaliza kazi yake na kuiachia serikali.
"Ninachoweza kukuambia ni kuwa Bodi imeshatoa mapendekezo yake na kuyakabidhi serikalini kupitia Wizara ya Nishati na Madini," alisema Ngumbuli bila ya kufafanua.
Hata hivyo, Ngumbuli alisema kutokana na unyeti wa nafasi hiyo, bodi iliamua kuunda kamati ndogo kutoka nje ya Tanesco iliyoratibu mchakato mzima, ikiwemo kupitia majina ya watu waliojitokeza kuomba nafasi hiyo.
"Bodi ilipotangaza kazi ya nafasi ya mkurugenzi mtendaji mpya, ilikabidhi majukumu yote kwa kamati ndogo iliyoundwa nje ya Tanesco na yenyewe ndiyo iliratibu mchakato mzima ikiwemo kupitia majina ya watu wote waliojitokeza kuomba nafasi hiyo," alisema Ngumbuli.
Awali chanzo cha habari kilieleza kuwa mgogoro ndani ya Tanesco unatokana na kila upande- bodi shirika hilo na menejimenti- kutaka kuwa na nguvu katika uamuzi wa mkurugenzi mtendaji atakayeteuliwa kushika wadhifa huo.
Habari za kuaminika kutoka ndani ya Tanesco zinaeleza kuwa watendaji wa ngazi za ukurugenzi waliandika barua za kuomba nafasi hiyo ya Dk Idris.
Mgogoro wa kiutendaji uliopo Tanesco ulibainishwa hivi karibuni na Kamati ya Bunge ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC).
Kutokana na hali hiyo, POAC iliwapa onyo watendaji hao kuacha makundi na kuwasisitizia waongeze jitihada katika utendaji ili waliokoe shirika hilo, ambalo limeelezwa kuwa liko hatarini kufilisika.
POAC, iliyo chini ya uenyekiti wa Zitto Kabwe, ilitoa onyo na maagizo hayo Aprili 6 mwaka huu katika kikao kilichofanyika kwenye ofisi ndogo za Bunge jijini Dar es Salaam. Kikao hicho kilikuwa baina ya kamati hiyo na watendaji wakuu Tanesco na kiliitishwa kujadili matumizi ya fedha ya mwaka 2008.
Katika kikao hicho, Ngumbulu alikiri kuwepo kwa matatizo ya kiutendaji ndani ya shirika hilo na kusema ndiyo yanayosabisha kwa kiasi kikubwa shirika hilo kutetereka
Ni mara chache nakosa la kusema lakini leo hakika sina la kusema, niseme nini ? Ni mtu mmoja tu Tanzania anayeweza kuiendesha TANESCO hata kama mtu huyo kachafuka namna gani ! Jamani kuendesha nchi si mchezo, Mungu inusuru Tanzania !