Othman Masoud: Maendeleo ya Zanzibar yatakuja kukiwa na amani, Umoja na utawala bora

ACT Wazalendo

JF-Expert Member
May 5, 2014
609
1,540
Maendeleo ya Zanzibar yatakuja kukiwa na amani, Umoja na utawala bora - Othman Masoud

Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha ACT Wazalendo, ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Mheshimiwa Othman Masoud, ameendelea na siku ya tatu ya ziara yake katika mikoa ya kichama ya kisiwani Unguja kwa kutembelea mkoa wa Kusini.

Ziara hiyo iliyowakutanisha wanachama wa Chama cha ACT Wazalendo ngazi ya mikoa, majimbo na matawi yenye lengo la kutambuana na kuzungumza na wanachama hao imefanyika katika viwanja vya ofisi ya Mkoa wa Kusini (kichama) iliyopo Kilimani, Makunduchi.

Akizungumza katika kikao hicho, Mheshimiwa Othman alisema ni muda muafaka sasa kuungana kuitetea Zanzibar kwa kurudisha mamlaka kamili, kwani nchi hii ilipaswa kuwa na mafanikio makubwa zaidi.

"Raia wa Zanzibar hawana mfarakano, bali kuwepo kwa baadhi ya viongozi wasiowajibika, kunapelekea hali kuwa mbaya pamoja na kuleta mitafaruku. Hivyo jambo la msingi zinapotokea chaguzi ziwe za ukweli, uhuru na uwazi ili kupatikana viongozi wazuri, wanaofaa na wawajibikaji", alisema Mheshimiwa Othman.

Wakati huo huo, Mheshimiwa Othman ametoa kadi kwa wanachama wapya waliojiunga na chama hicho.

Kabla ya hapo, Makamu Mwenyekiti wa Chama hicho, Ndugu Juma Duni Haji, aliwataka wananchi wa Makunduchi na viunga vyake kujitokeza kuchukua vitambulisho vyao vya Mzanzibari Mkaazi kwenye vituo vya mawilaya, kwani ni haki ya kila Mzanzibari aliyetimiza vigezo.

Aidha, Mjumbe wa Kamati Kuu ya chama hicho, Ndugu Ismail Jussa, amewakumbusha wanachama wa kusini kutokusahau malengo yao makuu ikiwemo kupiga vita ubinafsi na ubaguzi.

"Tunapaswa kumpinga yeyote atakayeleta ubinafsi na utengano baina ya Wazanzibari, kwani hizo sio silka na hulka za Wazanzibari, na badala yake tusimamie umoja, ukweli na kinaa (kukinai). Hiyo ndiyo njia ya mafanikio yetu".

Akiisoma taarifa ya utendaji kazi wa mkoa huo kichama, Katibu wa Oganaizesheni na Wanachama wa ACT Wazalendo, Omar Ali Shehe, alisema awali mkoa wa kusini ulikuwa ni mkoa mgumu ambao wananchi walikuwa hawaielewi dhamira ya chama hicho, ila kwa sasa mkoa huo ndio umekuwa miongoni mwa mikoa bora kichama na imekuwa ni eneo bora kisiasa.

Mheshimiwa Othman aliendelea na ziara yake katika mkoa wa Kati (kichama) kwa lengo la kujitambulisha na kuzungumza na viongozi na wanachama wa chama hicho ambapo alikutana na wanachama wenzake katika ofisi ya mkoa huo iliyopo Dunga.

IMG-20210531-WA0036.jpg
 
Back
Top Bottom