Orijino Comedi Matatani, Wakanywa

Sophist

Platinum Member
Mar 26, 2009
4,484
3,400
Wekezeni, acheni kiburi cha umaarufu na fedha

Kwenu wadogo zangu.

Masanja, Joti, Mpoki, Wakuvwanga, McRegan, Seki na Vengu.

Nianze kwa kuwakumbusha msemo wa Kiingereza usemao "You can not be a champ for life, one day you will go off and some else will come" sikumbuki vizuri msemo huu kwa mara ya kwanza ulisemwa na nani lakini ni wa zamani hapa duniani na maana yake haichuji kila siku ni mpya, kwamba huwezi kuwa bingwa milele lazima uondoke bingwa mwingine aje!

Najua mlitarajia kwa jambo mlilonifanyia ningeibuka na kisasi, mimi si mtu wa aina hiyo, mwenzenu Dudubaya aliwahi kupewa saa nzima kwenye kipindi cha Nani ni Nani Channel Ten, akanitukana matusi yote aliyoyafahamu lakini sikulipa kisasi, baadaye alipowekwa ndani akikaribia kufungwa ni mimi niliyemtoa mahabusu! Sikufanya hivyo kwa kutafuta sifa bali kutimiza kile kisemacho Wasamehe waliokukosea, leo hii Godfrey Tumaini ni rafiki yangu mkubwa...

Uamuzi niliouchukua si kupigana nanyi, maana ugomvi wa sisi kwa sisi hautasaidia chochote, bali nimeamua kuwapeni ushauri ili mfahamu kwamba kila enzi ina mabingwa wake, leo hii ninyi ni mabingwa lakini mfahamu kwamba wengine watakuja ninyi mtaondoka hivyo badala ya kuwacheka na kuwatukana watu, ni vizuri mkawekeza.

Enzi zile za Hitler aliyeua Wayahudi milioni sita duniani kote hakuna binadamu aliyewahi kuwaza eti siku moja angekuja kutokea mtu aitwaye Osama Bin Laden autingishe ulimwengu kwa mauaji na kusakwa bila mafanikio! Enzi zile za tajiri John D. Rockerfeller hakuna mwanadamu aliyewahi kufikiri atakuja mtu aitwaye Bill Gates au Warren Buffet na kuwa tajiri namba moja.

Enzi zile za Pele hakuna binadamu aliyewahi kufikiri atakuja kutokea mtu aitwaye Christiano Ronaldo au Messi, enzi zile za Mohamed Ali akiwa bingwa wa Ndondi wa dunia hakuna mtu aliyewahi kufikiri atakuja kutokea mtu aitwaye Mike Tyson na katika enzi za King Majuto, Mzee Small au Jangala aliyetuweka kila siku usiku tumezunguka redio kusikiliza michezo ya kuigiza, hakuna Mtanzania aliyewahi kufikiri kwamba ipo siku mngekuja kutokea ninyi. Kweli kila enzi na watu wake.

Mmekuja na mtapita kama walivyopita wengine wengi waliotangulia kabla yenu, ambao leo hii ukiwatafuta utashangazwa na maisha wanayoishi ingawa waliwahi kutingisha Taifa letu na wengine Dunia, baadhi wanateseka wakisubiri kusaidiwa! Kwenu hivi sasa jua linawaka lakini giza linakuja.

Mifano niliyoitoa ya watu niliowaongelea hapo juu inaonesha kwamba hakuna binadamu anayeweza kubaki bingwa siku zote, lazima aondoke ili kutoa nafasi kwa mabingwa wengine, tutake tusitake ni lazima tuondoke hivyo ni lazima kufanya mambo sahihi wakati huu tukiwa katika ubingwa wetu. Huu ndiyo ujumbe wangu kwenu leo.

Swali linalowasumbua watu wengi duniani na ambalo kila mtu mwenye akili timamu ni lazima ajiulize ni hivi siku nitakayotupwa nje nitafanya nini? Itakuwaje siku nitakayokuwa siwezi kucheza soka? Nitafanya kitu gani siku nitakayokuwa siwezi kuchekesha luningani na watu kunishangilia kila ninakopita? Kama binadamu mwenye akili timamu ambaye umaarufu haukupagawishi ni vizuri kujiuliza maswali haya kwani kila mmoja wetu siku moja atajikuta yupo nje ya mchezo.

Wadogo zangu,
Ilikuwa niwaandikie Waraka huu tangu wiki mbili zilizopita baada ya kunitoa kwenye kipindi chenu cha Orijino Comedi na rafiki yangu mpendwa aliyewahi kuwa mshindani wangu wa Biashara huko nyuma Mashaka Matongo au Abiola! Ingawa hamkututaja majina yetu lakini kila mtu aliyekiona kipindi hicho alielewa mliwalenga nani na nani na nina uhakika aliyetoa wazo hilo ni Sekioni David kwa sababu yeye ndiye aliwahi kuwa rafiki wa karibu sana na Mashaka Matongo enzi hizo wakiigiza pamoja katika kikundi cha MAMBO HAYO, pia akiwa mfadhili wake mkubwa.

Kwa wale ambao hawakubahatika kukiona kipindi hicho nitawasimulia kidogo; kilichotangazwa na vijana hao maarufu hivi sasa nchini Tanzania wakitembelea magari ya kifahari na kufanya kila aina ya starehe wanayoona inafaa ni kumwonyesha Bw. Mashaka Matongo ambaye huko nyuma aliwahi kumiliki magazeti kadhaa Pendwa akiwa amefilisika vibaya! Kazi yake hivi sasa eti ni kunyoa nywele huko Sinza na kuomba misaada kwa watu! Wakanionesha mimi kama mtu aliyefanikiwa ‘sana' kuliko Mashaka Matongo katika kazi hiyo na kumcheka wakimfanya mjinga.

Inawezekana kwa kunionesha mimi niko juu na mwenzangu akiwa amefilisika mlifikiri ningefurahishwa na kitendo hicho, naomba niwaeleze wazi kwamba mimi si mtu wa aina hiyo, wanaonifahamu wanaelewa na kitendo hicho hakikunifurahisha hata kidogo, sipendi umaarufu wa bei nafuu (Cheap popularity) napenda ninapopewa sifa iwe ni halali na ya kutolea jasho. Mpaka leo ninapowaandikia makala hii binafsi sielewi mwenzangu alijisikiaje baada ya dhihaka hiyo kurushwa na TBC 1 ambayo Mkurugenzi wake ni mtu ninayemheshimu sana katika fani hii, Tido Mhando.

Kilichonituma niandike makala hii ni kuwakumbusha wadogo zangu wa Orijino Komedi kwamba, maisha ni safari ndefu. Kwa kuonekana kwenye luninga kila Alhamisi na Jumapili, kupita huku na kule wakishangiliwa, wasijione wamefika kwenye kilele cha mafanikio na kuanza kucheka wenzao, ninachofahamu mimi na uelewa wangu mdogo juu ya mafanikio ni kwamba safari kwao ndiyo kwanza imeanza.

Safari ya maisha ni ndefu wadogo zangu, hakuna sababu ya mtu kumcheka mwenzake. Mzee mmoja aliwahi kuniambia ni kama safari ya kwenda umbali wa kilometa elfu moja kwa miguu, kila mtu ataondoka kwa staili yake. Mwingine atakimbia mwingine atatembea au kutambaa zote hizo ni safari lakini hakuna mwenye uhakika kwamba atafika mwisho wa safari yake salama kiasi cha kuwacheka wenzake, hiki ndicho ninachotaka kuwaeleza wadogo zangu wa Orijino Komedi.

Ninachojua mimi hakuna anayeweza kukimbia umbali wa kilometa elfu moja bila kupumzika, lazima mahali fulani mbele ya safari atachoka na kuketi chini ya mti ili kuwapisha wengine wapite na pengine huo ndiyo ukawa mwisho wa safari yake huku uliowaacha nyuma wakitembea taratibu wakipita na kukuambia "Mzee tunatangulia" huu ni ukweli.

Inavyoonekana kwa hivi sasa wadogo zangu wa Orijino Komedi mmeanza safari yenu kwa kukimbia kiasi cha kujiona ni wajanja kuliko wanaotembea hata kufikia hatua ya kuwacheka kama mlivyofanya kwa Mashaka Matongo ambaye huko nyuma alimlisha na kumtunza Sekioni! Mmesahau kwamba mbele ya safari ni lazima mahali fulani mtapumzika na waliokuwa wakitambaa na kutembea wakaja na kuwapita mkiwa chini ya mti, nimekwishawaeleza hapo juu kwamba binadamu huwezi kuwa bingwa milele lazima siku moja utoke na wengine waingie, kumbukeni walikuwepo mzee Majuto na Small kabla ninyi hamjaja.

Kibaya zaidi na kinachositikisha ni kwamba mmeanza hata kuwatukana watu waliowasaidia kufika mlipo leo! Hiki ni kitendo cha ukosefu wa shukrani cha kiwango cha juu kabisa ambacho nimewahi kukiona chini ya jua. Kila Mtanzania anafahamu mlipotokea, namna ambavyo mtu kama Reginald Mengi na vyombo vyake vya habari amesaidia kuwafikisha ninyi kwenye mwanga, ambaye hakika hamuwezi kusimama mahali popote duniani kutoa historia yenu mkaacha kutaja jina lake, lakini huyu ndiye amekuwa mtu wa kutukanwa kila siku katika vipindi mnavyofanya! Hili ni jambo la kusikitisha sana.

Najua mnatiwa kiburi na utajiri wa fedha na umaarufu ambao hivi sasa mnao! Mmethibitisha ile kauli kwamba hakuna kitu kigumu duniani kwa mwanadamu kuwa na fedha au mafanikio halafu akabaki yule yule! Fedha na umaarufu ni shetani, huwabadilisha watu na kuwapa tabia ambazo huko nyuma hazikuwahi kuonekana, sitaki kuwahukumu wadogo zangu lakini jambo hili limethibitika kwa matendo mnayoyafanya hivi sasa.

Najua mnatumiwa na watu kutimiza malengo yao, mambo mnayoyafanya si yenu yote, baadhi ni ya kuwafurahisha watu wanaowaweka mjini! Lakini kumbukeni mfano wa Mzee Kijiti aliyesafiri kwenda miji ya mbali akimwacha mke wake nyumbani, akiwa huko ashki ya tendo la ndoa ilimshika na kujikuta akitafuta mwanamke wa kuondoa haja yake.

Akifahamu kuna gonjwa la Ukimwi mzee huyo alilazimika kutafuta mpira wa kujikinga na gonjwa hilo. Kwa mahali alipokuwa ilikuwa kazi kidogo kupata mpira huo, akazunguka huku na kule kwenye vibanda bila mafanikio, mwili wake ukiwaka tamaa ya ngono. Mwisho mhudumu wa nyumba ya wageni aliyofikia alimpa mpira mmoja, akafurahi na kuingia chumbani ambako alifanya shughuli yake mpaka kufikia tamati akauvua mpira na kuutupa sakafuni tena akasikia kinyaa na kujilaumu kwa kitendo alichokifanya kusaliti ndoa yake.
"Ichukue" Akamwambia mwanamke aliyekuwa naye.

"Ichukue wewe" Mwanamke akakataa.
Baadaye wote wawili waliondoka na kuuacha mpira huo sakafuni, sasa wakiwa na akili timamu kondomu haikuwa na umuhimu tena, ilishawasaidia kuwaepusha na Ukimwi basi ilikuwa inatosha, kazi yake ilishakwisha.
Wadogo zangu,

Kwa mfano huu wa Mzee Kijiti naamini mtakuwa mmenielewa vizuri, jiepusheni sana na kutumiwa na watu wenye malengo yao ambao mwisho wa siku yakitimia watawatupa kule kama Kondomu na hawatawajali tena. Mkilijua hili mtafanya mambo mawili, la kwanza ni kuwekeza na la pili ni kujiepusha na matusi kwa watu waliowasaidia kufika mlipo kwani kesho ni lazima mtarudi kwao kuwashika mikono, hivyo ndivyo Mungu anavyofanya kazi.

Jiepusheni na starehe na kulewa umaarufu, jua haliwaki siku zote, kuna mchana na usiku. Muda huu mkiwa juu, ni vizuri kujiuliza giza litakapoingia na mwanga kupotea, au siku tutakapotupwa tutaishi vipi? Anasa hazina mwisho, zipo tu, mlizikuta, mtaziacha na wengine watazikuta na kuziacha hivyo ni vizuri kuwa makini katika kipindi hicho ambacho neema bado ipo, maana mchekaji huwa mchekwaji kesho na mchekeshaji huwa mchekeshwaji kesho kutwa.

Mmekwishanitukana mimi mara nyingi lakini mimi sijali, nimekwishazoea, katika miaka kumi na moja niliyofanya kazi hii ngumu ninao maadui wanaoweza kufanya chochote ili wanichafue, kinachoniuma sana ni kitendo mnachokifanya kwa mzee Mengi ambaye bila yeye TBC1 wasingewaona, kwa umri wake mzee huyu ni sawa na mzazi wenu na mnachokifanya ni utovu wa nidhamu wa hali ya juu sababu tu mmelipwa!

Inawezekana mkawa hamfahamu kwamba umaarufu wenu unapotezwa na kitendo hiki, Watanzania hawapendi watu wenye maringo na kujisifu tabia ambayo hivi sasa imewagubika ninyi mkiwa mwanzo tu mwa safari ya maisha! Mnakumbuka kilichowapata uwanja wa Taifa siku ile mlipopigwa kwa chupa na makopo ya soda? Hilo linapaswa liwe fundisho ili mjiangalie upya, mimi naamini mnaweza kurejesha hali mliyokuwa nayo zamani kwa kujiepusha na matusi kwa watu waliowasaidia.

Mkiendelea na tabia hii si tu mtachukiwa bali mtailetea TBC1 matatizo makubwa sana ya kulipa watu mabilioni ya fedha jambo ambalo najua kabisa TBC1 hawatakuwa tayari kulifanya, hivyo kuamua kujiepusha nanyi! Hata kama TBC1 ni chombo cha serikali, inaelewa kabisa kuna mahakama na hakuna aliye juu ya sheria, kitendo cha wao kuwaruhusu ninyi kuendelea kutukana watu kwa maneno ya uongo, kitakuja kuwaingiza kwenye matatizo makubwa ambayo hatimaye yatavunja ndoa yenu.

Najua maneno yangu yatawaumiza lakini naomba msikasirike kwani tiba ya ugonjwa siku zote inauma lakini mwisho wa siku inaponyesha! Naomba mnivumilie na myafanyie kazi yale mtakayoona yanafaa, binadamu hatujatimia, tunayo mapungufu mengi na kila siku tunafanya kazi kurekebisha sehemu mbalimbali maishani mwetu, nanyi nawasihi mchukue hatua hiyo. Mtu hahitaji kuwa na elimu kubwa sana kuelewa kitakachowapata kama mkiendelea na mtiririko huu mnaokwenda nao.

Sisi sote ni Watanzania tuacheni kuchekana bali tuwatie moyo waliovunjika na tuwasaidie kusimama walioanguka! Matendo hayo ndiyo yatakuwa akiba yetu mara giza litakapoingia hawa mnaowacheka na kuwatukana leo si ajabu ndiyo watakaowasaidia ikitokea siku moja kigogo anayewafadhili sasa akawa hafanyi kazi na ninyi tena jambo ambalo si ajabu kutokea.

Naomba niseme neno moja natumaini sitamuudhi mtu. Watanzania tuna tatizo ambalo ni lazima tulishughulikie kama kweli tunataka kupata mafanikio ya kweli maishani mwetu, tuna tabia ya kuridhika mapema hata kwa mafanikio kidogo. Hapo mlipo wadogo zangu wa Orijino Komedi tayari mmesharidhika, lakini kumbukeni kufika Uingereza au kuendesha ‘Haria' peke yake haitoshi, kuna mambo mengi sana ya kufanya, kama kufika nje na kuendesha gari ingekuwa kila kitu basi watu wangekwisha acha kufanya kazi.

Hili ni kosa kubwa sana ambalo sisi Watanzania tunalifanya, mafanikio kidogo tu yanatulewesha na kuanza kutukana watu bila kujua kwamba kuna kesho, hata Orijino Komedi mtakubaliana nami katika hili! Wadogo zangu mmelewa sifa mapema, kila mahali mnapoingia mnataka huduma ya VIP? Kumbukeni wanaojikweza hushuswa bali wanaojishusha hukwezwa! Chapeni kazi wadogo zangu, bado hamjafika popote, mafanikio ni safari ndefu mnahitaji sana watu kuliko mnavyohitaji fedha.

Nimeongea mengi sana wadogo zangu, lakini huu ndiyo Waraka wangu kwenu sisi ni ndugu lazima tuelekezane kwa maneno ya ukweli na si visasi, ni vizuri mkakumbuka mlikotoka badala ya kujisikia mmefika mwisho na kuanza kuwatukana watu waliowasaidia kufika juu! Ni vizuri kuelewa hamtakuwa mabingwa siku zote, pengine mtakapokuwa mnaporomoka hawa mnaowatukana leo watakuwa bado wako juu na mtahitaji msaada wao.

Naomba niishie hapo.

Jipu limepasuka siwezi kuwa adui kwa kusema kile ninachoamini ni ukweli. POLE SANA MASHAKA MATONGO, MANENO YA ORIJINO KOMEDI YASIKUVUNJE MOYO, PAMBANA TU HATIMAYE UTAFIKA JUU, YOTE YAWEZEKANA, IF THEY CAN, YOU CAN!
 
Hii mku ipo tayari watu tumesha jadili sana,Mods ipelekeni kule kwenye nyingine
 
hii inachosha kuona wanabodi wanaokurupuka kuanzisha threads bila kufanya utafiti kama zipo tayari.
Mods naomba muiunganishe hii na ile orijino
 
Halafu kunaibuka watu wanasema umaarufu wao umepungua..thubutu threads kumi kumi hata kama ni kurudia kwa vichwa vipya twende kaziii...nyoa hadi vimalaika
 
Orijino Komedi hawana jipya wanatumiwa tuu,ila waangalie kwani rafiki wa leo ndio adui wa kesho.
 
Orijino Komedi hawana jipya wanatumiwa tuu,ila waangalie kwani rafiki wa leo ndio adui wa kesho.

Nani anawatumia kama hawana jipya? tusidanganyane hao wanaowatumia ni kwa sababu wanajua wapo juu..hilo wanalijua kwani walikuwa marafiki wa EATV muda mfupi wamegeuka maadui kwa hiyo uskonde.Madogo wanasaka karatasi nyekundu hayo mengine kwao ni njia tu
 
hehehehe
naona kuna wadau wakiona kichaka basi mboji hujisogeza mlangoni kabsaaa.
si mchangie ktk ile thread ya orijino komedy? maana mtoa hoja amepest kutoka ktk source ile ile ambayo tushaijadili
 
Lete mengine, sio mbaya tukiwasifia kwa kituko cha Mwalimu kuwanywesha wanafunzi bia ili waelewe kienglish.
 
Ilisha semwa hawa jamaa ,orijino komedi ni kama prostitutes,changudoa. Na wana act hivyo hivyo.Ukiwalipa vizuri watakune.... kisawasawa.
Actually they bore!
 
ukweli ni kwamba siku hizi wanabore..not interesting anymore...zamani nyumbani kwangu ikifika alhamisi muda wa ze komedy kila kitu kina simama...siku hizi wala hakuna anaeangalia wala kujishughulisha...
 
Back
Top Bottom