Ongezeko la kodi kwenye Miamala ya Fedha: Serikali imekosea

Mwanahabari Huru

JF-Expert Member
Mar 9, 2015
14,243
34,899
Kumekuwepo na mjadala mpana katika jamii na kwenye vyombo vya habari kuhusiana na utaratibu mpya ulioanzishwa na serikali wa kukata kodi katika miamala ya fedha kwa njia ya mitandao ya simu na benki.

Katika bunge la bajeti lililomalizika mwezi jana, serikali ilitangaza kuanza kukusanya ushuru kupitia miamala yote ya fedha inayofanywa kwa benki au kwa mitandao ya simu.

Kwenye hotuba ya Waziri wa fedha Dr.Philip Mpango alisema hivi:

"Serikali imekusudia kutoza ushuru wa bidhaa wa asilimia 10 kwenye ada zinazotozwa na watoa huduma (benki na makampuni ya simu) katika kutuma na kupokea fedha... Katika utaratibu wa sasa, baadhi ya kampuni zinazotoa huduma zimetumia mwanya huo kuhamishia sehemu kubwa ya ada hizo kwenye kupokea fedha na hivyo kuwa nje ya wigo wa kodi."

#UFAFANUZI
Kupitia utaratibu huu mpya, serikali itatoza jumla ya asilimia 28% ya gharama za kutuma na kutoa fedha kwa njia ya simu au benki. Asilimia 28% inatokana na 10% ya ushuru wa bidhaa/huduma na 18% ya kodi ya ongezeko la thamani (VAT).

Maana yake ni kwamba kwa utaratibu huu mpya ukituma fedha kwa mtu kupitia simu au benki utakatwa 28% ya gharama za kutuma, na yule anayeenda kutoa atakatwa 28% ya gharama za kutoa.

Kabla ya July 1, ulikua ukituma pesa kwa mtu yeyote hakukuwa na kodi kwenye gharama za kutuma wala za kutoa.

Kwa mfano kama gharama za kutuma Shilingi Milioni 3 kwa MPesa/tigopesa au Airtel money ilikua shilingi 8,000/= na anayeenda kutoa anakatwa 20,000/= faida yote ilikua inaenda kwa mtoa huduma ambaye ni kampuni ya simu. Na benki vivyo hivyo.

Lakini kuanzia tarehe 1 July, serikali imeona ni vizuri faida inayopatikana ilipiwe kodi of which ni jambo zuri lakini linalohitaji mjadala mpana kabla ya serikali kuamua kuendelea nalo au kusitisha.

Kwa hiyo kwenye 8,000/= uliyokua ukikatwa ukituma milioni 3, serikali itachukua 28% ya 8,000/= ambayo ni 2,240/=. Halafu yule uliyemtumia akienda kutoa atakatwa 28% ya 20,000/= ambayo ni 5,600/=. Kwahiyo jumla serikali itakuwa imechukua 7,840/= kwenye "transaction" ya Shilingi Milioni 3.

#MKANGANYIKO;
Katika hali inayoonesha serikali haikujipanga kuhusu suala hili, kumetokea mkanganyiko wa namna ya ulipaji wa kodi hii. Taasisi mbili nyeti za serikali zimetofautiana hadharani (contradiction).!

Benki kuu (BOT) imesema ongezeko la kodi litalipwa na Mtumiaji wa huduma (beneficiary) lakini Mamlaka ya mapato (TRA) imesema kodi hiyo italipwa na mtoa huduma (Service Provider) yani makampuni ya simu au mabenki. Hali hii imeleta mtafaruku mkubwa na kuibua sintofahamu katika jamii.

Kufuatia tamko la BOT, Mabenki yalianza kuwatoza wateja wao zidio la 28% maana walipewa maelekezo kwamba zidio hilo litalipwa na wateja. Baadae TRA ikatoa ufafanuzi kupitia kwa Kamishna wake Mkuu Ndg.Alfred Kidata kuwa kodi hiyo italipwa na mtoa huduma na sio mteja.

#Kwa_Mujibu_Wa_BOT
Kwa maelezo ya BOT, kodi husika ilipaswa ilipwe na mteja. Kwahiyo mchanganuo ungekuwa kama ifuatavyo.

Ukituma milioni 3 unakatwa 8,000 plus 28% ya hiyo 8,000 ambayo ni 2,240/=. Kwahiyo ili utume Milioni 3 utakatwa jumla 10,240/=. Na yule uliyemtumia akienda kutoa atakatwa 20,000/= plus 28% ya hiyo 20,000/= ambayo ni 5,600/=. Kwahiyo jumla atakatwa 25,600/=. Haya ndio maelekezo yaliyotolewa na BOT.

#Kwa_Mujibu_Wa_TRA
Kwa mujibu wa TRA kodi husika italipwa na mtoa huduma (service provider) yani kampuni ya simu au benki. Kwa hiyo ukituma milioni 3 kwa calculation za TRA wewe uliyetuma utakatwa 8,000/=. Halafu katika hiyo 8,000/= kampuni husika ya simu itatozwa 28% ambayo ni 2,240/= kama kodi ya serikali. That means kampuni itabakiwa na faida ya 5,760/= badala ya 8,000/= waliyozoea.

Na yule unayemtumia atakatwa 20,000/= kama kawaida, halafu serikali itachukua kodi ya 28% ambayo ni 5,600/=. Kwahiyo kampuni ya simu itabaki na faida ya 14,400/= badala ya 20,000/= waliyozoea. Haya ndio maelekezo yaliyotolewa na TRA.

#Je_Nani_Sahihi_Kati_Ya_BOT_na_TRA?
Kutofautiana kwa maelekezo kati ya taassi hizi mbili kubwa za fedha nchini kumeleta sintofahamu na kufikia watu kuhoji nani yupo sahihi kati ya TRA na BOT?

Lakini baadae Waziri Mpango katika mahojiano na vyombo vya habari akasema kuwa kodi iliyotajwa itatozwa kwa "mtoa huduma" na sio "mteja". Maana yake ni kwamba Serikali ilimaliza ugomvi wa ndugu wawili yani TRA na BOT. Na kwa maelezo hayo inamaanisha kuwa TRA ndio wapo sahihi na BOT "walikurupuka" (kwa mujibu wa serikali).

#Maswali_Ya_Msingi
1. Je ni sahihi kodi tajwa kukatwa kwa mtoa huduma badala ya mteja?

2. Je makampuni ya simu na mabenki yalipaswa kulipa kodi hii lakini yakawa hayalipi?

3. Je kwa kumkata mtoa huduma serikali imemsaidia mwananchi?

4. Je athari zake ni kiuchumi ni zipi?

#MAJIBU;
1. Si sahihi serikali kumkata mtoa huduma kodi ambayo ni "Customer oriented". Hii ni kwa sababu mtoa huduma nae ana kodi zake lukuki anazolipa serikalini.

Kwa mfano makampuni ya simu na mabenki yanalipa kodi mbalimbali serikalini kama Corporate tax, SDL, WCF etc ndizo zinazowagusa moja kwa moja. Sasa kwanini walazimishwe tena kumlipia mteja 28% ya VAT na ushuru wa huduma?

Logically serikali imetumia "unsound economic approach" kutatua suala hili. Yani serikali imelazimisha makampuni yalipe ili kukwepa lawama za wananchi. Kwahiyo maamuzi ya serikali ni "political oriented" sio ya kiuchumi. Kiuchumi aliyetakiwa kubeba mzigo huu ni mwananchi.

2. Je makampuni ya simu na mabenki yalipaswa kulipa kodi hii lakini yakawa hayalipi?

Biashara ya mabenki au fedha kwa njia ya simu ni biashara kama zilivyo biashara nyingine. Na unapoanzisha biashara kuna mambo ya msingi ya kuzingatia. Mojawapo ni kitu kiitwacho "Debut" yani mkakati wa kuipeleka product yako sokoni (go-to-market strategy). Hapa vitu vingi huangaliwa na mojawapo ni kodi; kwa sababu imposition ya kodi inaweza kuathiri biashara yako sokoni kwa namna hasi au chanya.

Kwahiyo wakati makampuni ya simu na mabenki yanaweka viwango vya ada walizingatia kodi zile zinazowahusu tu (kama kama Corporate tax, SDL, WCF etc). Hili chagizo la 28% kwenye ada halikua sehemu ya kodi walizopaswa kulipa kwa sababu serikali haikuwahi kuwaambia walipe.

Kwahiyo isionekane kuwa mabenki na makampuni ya simu yalikuwa korofi na kukataa kulipa kodi hii, la hasha.! Serikali ndio ilikuwa dhaifu kushindwa kudai kodi hii mapema. Kama serikali ingewadai mapema, basi nao "wangefix" viwango vyao vya ada mapema ili kukabiliana na ongezeko hilo.

3. Je kwa kumkata mtoa huduma badala ya mteja serikali imemsaidia mwananchi? Jibu ni Hapana. Kumkata mtoa huduma hakutamsaidia mwananchi kwa sababu makampuni ya simu na benki yatatafuta njia nyingine ya kufidia hasara hiyo. Hakuna kampuni wala benki itakayokubali kupata hasara kwa "uzembe" wa serikali.

Kwa mfano mabenki yanaweza kuongeza gharama za riba katika mikopo yao kama sehemu ya kufidia hasara hii. Kwa upande wa makampuni ya simu yanaweza kupunguza vifurushi vya internet, au muda wa maongezi ili kufidia hasara. Kama kwa shilingi 1,000/= ulikua unapata MB 500 utaanza kupata MB 300. Au kama kifurushi cha 1000/= ulikua unapata dakika 30, utaanza kupata dakika 20. Hizi ni baadhi ya "alternatives" zinazoweza kutumiwa kufidia hasara. Kwahiyo mwishowe mhanga wa mwisho anabaki kuwa mwananchi. Mzigo wote unarudi kwa mwananchi.

4. ATHARI ZAKE NI NINI?

#Athar_ya_Kwanza;
Ni kama nilivyoeleza hapo juu; yani kuongezeka kwa gharama za huduma nyingine zitolewazo na mabenki au makampuni ya simu kama njia ya kufidia hasara. Kwahiyo tutegemee kupanda kwa gharama za huduma mbalimbali za kibenki na makampuni ya simu.

#Athari_ya_Pili;
Kudorora kwa biashara ya fedha kwa mitandao ya simu. Kwa kuwa makampuni ya simu ambao ndio watoa huduma (service providers) wamelazimishwa kulipa gharama zote za kodi na ushuru, lazima watapunguza mrabaha (commision) kwa mawakala wao.

Yani kama wakala alikua anapata commision ya 1,000/= mtu akitoa laki 5, sasa hivi atapata commission ndogo zaidi, may be 5,00/=. Makampuni ya simu yatalazimika kupunguza kiwango cha commision kwa mawakala wao ili waweze kulipa 28% ya kodi iliyoongezwa.

Kwa kuwa mawakala watapunguziwa "commission", wafanyabiashara wengi wenye vibanda vya kutuma fedha watafunga biashara hii. Hakuna mtu atakayekua tayari kuinvest milioni moja halafu apate mgawo wa elfu moja. Wengi watafunga biashara za Mpesa/tigopesa/Airtel Money etc na kupeleka mitaji yao kwenye biashara nyingine zinazoweza kuwapa faida nzuri zaidi.

Maana yake ni kwamba tutegemee vibanda vingi vya kutuma na kupokea pesa kwa njia ya simu vitafungwa. Kwa wale wananchi wa vijijini ambapo unakuta kibanda cha Mpesa/tigopesa ni kimoja watapata shida zaidi vibanda hivyo vikifungwa, maana watalazimika kwenda mjini kutafuta huduma.

Kwahiyo kama ulikua ukimtumia mzazi wako/ndugu yako laki moja, akawa anaitoa palepale kijijini, saivi itabidi umtumie laki moja plus hela ya nauli ya kwenda mjini kutoa kwa sababu kibanda alichokua anakitegemea kijijini kitafungwa. Hapo kuna hasara mbili. Hasara ya kutuma fedha zaidi na hasara ya kupoteza muda.

#Athari_Ya_Tatu;
Ongezeko kubwa la ukosefu wa ajira. Kwa kuwa huduma za kutuma na kupokea fedha kupitia mitandao zimeajiri watu wengi, zikidorora means watu wengi watakosa ajira pia. Na hii ni hatari sana kwa maendeleo ya nchi kwa sababu inaweza kuchochea vitendo vya kihalifu. Jiulize ni watu wangapi wamejiajiri kupitia Mpesa/tigopesa /Airtel money etc. Jiulize biashara hii ikidorora wataenda wapi? Jiulize serikali imetengeneza njia gani mbadala kwa watu hawa kujikwamua kiuchumi?

#NINI_KIFANYIKE;
Zipo njia nyingi ambazo serikali inaweza kuzitumia kutatua suala hili. Lakini leo nitaeleza njia moja yenye manufaa zaidi (kwa serikali na kwa wananchi). Njia yenyewe ni serikali kufuta ongezeko hili la kodi la 28% kwenye charges haraka iwezekanavyo. Faida za kufuta kodi hii ni nyingi kuliko hasara zinazoweza kujitokeza.

Kuna watu watasema tuache serikali ikusanye kodi. Well.! Hata mimi nasema ni jambo zuri serikali kuongeza wigo wa kukusanya kodi lakini ni vizuri ipime kodi hiyo inawezaje kuathiri ustawi wa maisha ya wananchi wa kawaida (Economic and Social welfare).

Kwenye uchumi kuna approach mbili zinazoweza kutumika kuelezea suala hili. Moja ni "Absolute Advantage Economic Approach" na nyingine ni "Relative Advantage Economic approach."

#Absolute_Advantage;
Hapa faida hupatikana "vertically". Serikali inaweza kukusanya mapato makubwa lakini kwa kuumiza wananchi. Kwa mfano serikali inaweza kukusanya Trilioni 2 kwa mwezi lakini biashara nyingi zikawa zimedorora, nyingine zimekufa, kampuni zimepunguza wafanyakazi etc. Kwa kifupi serikali inapata lakini wananchi wanaumia.

#Relative_Advantage;
Hapa faida hupatikana "horizontally". Serikali inakusanya mapato bila kuumiza wananchi. Kwa mfano badala ya kukusanya Trilioni 2 kwa mwezi inakusanya Trilioni 1.5, lakini biashara binafsi zinastawi, kampuni zinazaliwa kila siku, ajira zinaongezeka etc. Kwa kifupi serikali inapata na wananchi wanapata.

Serikaki kukusanya kodi ni jambo zuri. Hata mimi naunga mkono, lakini ni vizuri serikali ijipime na ijue inatumia approach gani. Ni absolutely au ni relatively?

Hakuna maana yotote kama serikali itakusanya mapato makubwa lakini watu wanapoteza ajira, kampuni zinakufa, watu wanashindwa kuanzisha biashara, ofisi zinashindwa kupandisha mishahara kwa watumishi etc.

Kwa hiyo ni vizuri serikali ikajitafakari upya katika hili. Najua Rais ana washauri wazuri wa uchumi, sijui kwanini hawamshauri haya. Kuna madai kuwa wanamuogopa. Sijui kama madai haya ni ya kweli, lakini mimi (Malisa) ningekua mshauri wa Rais ningemshauri bila kupepesa macho kwamba aondoe haraka ongezeko la kodi (28%) katika miamala ya fedha kwa njia ya simu na benki kwa sababu athari zake "relatively" ni kubwa sana. Ni heri anichukie kwa kumwambia ukweli utakaomsaidia, kuliko anipende kwa kumuambia uongo utakaomletea shida badae.

Serikali inaweza kuongeza wigo wa mapato kwa kutoza kodi hii lakini athari zake ni kubwa sana kiuchumi. Mwisho wa siku atakayeumia na kubebeshwa mzigo wote ni mwananchi masikni ambaye ndiye "final consumer".

Hata hivyo sioni sababu ya serikali kung'ang'ania kodi hii na kumuumiza mwananchi masikini wakati kuna vyanzo vingi vya mapato vinavyoweza kulisaidia taifa kupiga hatua kimaendeleo.

Hadi leo makampuni yanayochimba madini nchini yanalipa mrabaha wa 04% tu serikalini na yenyewe yanachukua 96% ya mapato. Ghana makampuni ya madini yanachukua 70% na serikali inachukua 30%. Botswana wawekezaji wanachukua 60% na serikali 40%. Kwanini kwetu wawekezaji wachukue 96% na serikali ichukue 04% tu??

Haya ndio mambo ambayo serikali inatakiwa kushughulika nayo, sio kung'ang'ania kodi za vibanda vya Mpesa, tigopesa au Airtel money. Nilitegemea Rais baada ya kuingia madarakani angefanya review ya mikataba yote ya madini na gesi. Kama mkataba haunufaishi nchi auvunje au aagize ufanyiwe marekebisho.

Lakini kuacha makampuni ya madini yalipe 04% tu ya mapato wakati huohuo wananchi masikini wakinyonywa 28% ya makato kwenye miamala ya fedha ni kichekesho. Huwezi kuwafumbia macho watu wanaovuna madini yetu bila nchi kupata faida ya kueleweka, halafu uje kukimbizana na mawakala wa Mpesa na tigopesa. Serikali makini inapaswa kukusanya kodi kwenye vyanzo vikubwa vya mapato sio vichochoroni.

Mwalimu Nyerere aliwahi kuusema "..serikali makini duniani inakusanya kodi, hasa kwenye vyanzo vikubwa vya mapato. Lakini serikali uchwara haiwezi kukusanya kodi. Serikali uchwara inaogopa wafanyabiashara wakubwa, kwahiyo itakimbizana na wafanyabiashara wadogo barabarani lakini kamwe haiwezi kuwagusa wafanyabiashara wakubwa"

Nawashauri watendaji wa serikali ya JPM wasikilize vizuri hotuba hiyo ya Mwalimu Nyerere na iwape mwongozo. Waache kukimbizana na vibanda vya M-pesa na Tigopesa mtaani, wakimbizane na wachimbaji wa madini, na gesi ambao mikataba yao haijulikani kwa wananchi. Kwa kufanya hivyo watasaidia taifa hili kupiga hatua.

JIPU LIMEPASUKA, SIWEZI KUWA ADUI KWA KUSEMA UKWELI.!

Malisa GJ || Your Partner In Critical Thinking.!
 
Serikali inajua hizo service charges za bank ni mapato ya bank usidanganyike na hilo jina hivyo wanastahili kulipa wao kodi zote mbili, Hawa kina tigopesa watapangiwa ada elekezi ndipo vat italipwa na mlaji.Mkuu servicecharges ni biashara usilaghaike
 
hawa walivyochanganyikiwa wakijenga viwanda vitalipuka kwa mawenge.
 
Back
Top Bottom