Ombwe la elimu ya ujinsia na mimba za wanafunzi 980 katika siku 180 wilayani Kidondo: Sera ya Elimu Tanzania inakidhi mahitaji?

Mama Amon

JF-Expert Member
Mar 30, 2018
2,021
2,478


Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mwanaidi Ali Khamis akiongea na wananchi na viongozi Wilayani Kibondo

Taarifa kwamba huko mkoani Kigoma, kila siku ya miezi sita iliyopita, angalau wanafunzi 5 walio chini ya miaka 18 walikuwa wanafanya ngono ya jenitalia kwa jenitalia bila kutumia kingamimba wala kingamaradhi, zimenikumbusha malumbano juu ya mbinu mwafaka za kupambana na janga la ukimwi katika enzi za miaka ya 1980.

Mwaka 1981 kesi ya kwanza ya janga la ukimwi ilirekodiwa nchini Tanzania. Na mwaka 1984, Padre Bernard Joinet aliandika kitabu kiitwacho "The Challenge of AIDS in East Africa". Sehemu ya kwanza infafanua "Basics Facts" na sehemu ya Pili inahusu "Prevention and Survivors".

Maandiko ya Padre Joinet yalithibitisha ukweli kwamba ili kujadili chanzo cha ukimwi ilikuwa ni lazima kujibu maswali yauatayo:

Kwa nini watu wanapata ukimwi? Kama ni kwa sababu ya uzinzi, kwa nini watu wanazini? Kama ni kwa sababu ya uasherati, kwa nini watu wanafanya uasherati? Kama ni kwa sababu ya ubakaji, kwa nini watu wanafanya ubakaji?

Kwa ujumla, swali likawa ni: kama ni kwa sababu ya ngono pasipo ndoa (non-marital sex), kwa nini watu wanafanya ngono pasipo ndoa?

Katika utafiti wake, Padre Joinet aliorodhesha sababu zifuatazo, kati ya zingine, kama jawabu kwa swali hili: kutafuta kipato, kuonyesha ukarimu, kutafuta mtoto, kutafuta anasa ya kingono, kutuliza mawazo, kufanya udadisi kuhusu maumbile, kutafuta utambulisho ndani ya kundi rika, na kadhalika.

Hii maana yake ni kwamba, safari hii Waafrika tulikuwa hatuna namna ya kuendeleza mila yetu ya kuongelea maisha ya ngono faraghani badala ya hadharani.

Kwa maana sasa ilikuwa wazi kwamba, wagonjwa wengi wa ukimwi walikuwa ama ni wazinzi au waasherati au vyote viwili.

Padre JOinet alianzisha kampeni ya mashua tatu, yaani mashua ya tekinolojia, mashua ya uaminifu na mashua ya useja. Aliitaja kama programu ya ABC, yaani Abstinence, Bening Faithful and Condoms.

Programu hii ilimfanya akosane na Askofu wake, Kardinali Pengo, na hatimaye Joinet akalazimika kuhama Tanzania.

Hali kama hii inaweza kutokea tena huko mkoani Kigoma, wilaya ya Kibindo. Huko kuna wanafunzi wengi ambao ama ni wazizi au waasherati au wabakwaji au vyote kwa pamoja.

Huko Kibindo kuna tabia tatu kubwa za iingono. Kwanza, kuna tabia ya kufanyika kwa ngono kati ya watu wawili, ambapo wahusika hawajaoana, na kati yao, angalau mtu mmoja amefunga ndoa na mtu baki (uzinzi kwa mujibu wa kanuni za kimaadili).

Pili, kuna tabia ya kufanyika kwa ngono kati ya watu wawili, ambapo wahusika hawajaoana, na kati yao hakuna mtu amefunga ndoa na mtu yeyote baki (uasherati kwa mujibu wa kanuni za kimaadili).

Na tatu, kuna tabia ya kufanyika kwa ngono kati ya watu wawili, ambapo wahusika hawajaoana, na kati yao kuna mwanamke ambaye, japo amebalehe kwa maana ya kupevuka kibayolojia, lakini bado yuko chini ya miaka 18, kwa maana kwamba hajafikia umri wa kujitawala kama mtu mzima (uasherati kwa mujibu wa kanuni za kisheria).

Kwa mujibu wa taarifa za kiserikali zilizopatikana hivi karibuni, kati ya Januari na Juni 2021, watoto wa kike wapatao 980 walipata mimba na kuacha masomo kwa sababu hiyo.

Taarifa hizo zilikabidhiwa kwa Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mwanaidi Ali Khamis, alipokuwa wilayani humo kwa ajili ya kukagua kazi za utoaji wa huduma za ustawi wa Jamii na masuala ya maendeleo ya jamii.

Taarifa kwamba kumekuwepo na matukio ya mimba za wanafunzi 980 katika siku 180 wilayani Kidondo zinamaanisha kuwa kila siku angalau wanafunzi 5 walio chini ya miaka 18 hufanya ngono bila kuwa na ujuzi wa kufanya menejimenti ya rutuba ya uzazi.

Kisheria, wanafunzi hawa wanabakwa. Lakini ukweli ni kwamba sheria haijawasaidia na huenda isiwasaidie hivi karibuni, kwani kijamii na kibayolojia wanafunzi hawa hawaonekani kwamba wamebakwa.

Kama ni hivyo, sera ya Elimu ya Tanzania inakidhi mahitaji kadiri kipengele cha elimu ya ujinsia kinavyohusika? Kama hapana kitu gani kinakosekana ili kitafutwe? Kama ni ndiyo, tatizo linaanzia wapi, na kitu gani kifanyike? Kuna haja ya kujibi maswali haya na kuchukua hatua stahiki.

Napendekeza kwamba sera ya elimu iboreshwe kwa kuboresha maudhui yanayohusu stadi za maisha katika kipengele cha elimu ya jinsi na ujinsia. Nitajenga hoja hiyo kupitia bandiko hili kwenye aya zitakazofuata hapa chini.

1626962198510.png

Profesa Joyce Ndalichako, Waziri wa Elimu Tanzania

Profesa Kitila Mkumbo (2009), katika andiko lake liitwalo "Content analysis of the status and place of sexuality education in the national school policy and curriculum in Tanzania," lililochapishwa katika Jarida la "Educational Research and Review," Chapisho la 4, Toleo la 12, ukurasa wa 616-625, alifanya uchambuzi wa maudhui ya mtaala wa elimu ya sekondari na kubaini kwamba, kwa ujumla, maudhui na mpangilio wa elimu ya ujinsia havikidhi mahitaji ya Watanzania. Katika hitimisho lake, Kitila alisema:

"This study has established that a substantial amount of sexuality education is covered in the Tanzanian national school curriculum, especially in the secondary school syllabi. However, most of the topics related to sexuality education that are covered in the national school curriculum appear to be somewhat disorganised and scattered across four subjects [namely Social Studies, Science, Civics and Biology] to the extent that they can hardly be said to constitute a meaningful sexuality education programme." (p. 624).

Pamoja na hitimisho lake zuri, napenda kuongeza kwamba, urefu na upana wa topiki na vijitopiki alivyobaini kwenye mitaala yetu vinaonyesha kuwa maudhui yaliyopo kwa sasa yanatoa marifa ya juu juu kuhusu ujinsia wa binadamu.

Kwa kuangalia changamoto za leo, ni wazi kuwa kuna haja ya kuyapanua maudhui ili kuwawezesha wanafunzi kupata dozi iliyokamilika kuhusu ujinsia wa binadamu katika milenia ya tatu.

Kwa hiyo, sasa napendekeza kwamba wataalam wa Taasisi ya Elimu Tanzania, yaani Tanzania Institute of Education (TIE), wafanye kazi ya kuboresha mtaala wa elimu ya msingi na sekondari kusudi maudhui ya kisasa yafuatayo yawe sehemu yake, kama somo moja lenye kitabu kimoja cha kiada:

Kwa marejeo zaidi, maktaba ya kidijitali ifuatayo inafaa sana: Maktaba
Pia, kamusi ya ujinsia ifuatayo inafaa sana: sexology dictionary

Naweza kubaini mapingamizi kadhaa dhidi ya pendekezo hili. Nitayajbu hapa hapa hivi punde.

cc. Profesa Joyce Ndalichako, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi.

1626899865832.png

Prof Kitila Mkumbo, mtaalam wa saikolojia na mtafiti wa masuala ya ujinsia wa binadamu
 
Back
Top Bottom