Nyuma yako (Riwaya ya S. Mollel)

*NYUMA YAKO (MSIMU WA PILI) -- 31*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Lakini mwanamke huyo ingali akiwa hapo mahakamani alipata kumwona mwanaume ambaye alimtilia mashaka. Mwanaume huyo alikuwa amekaa kwenye viti vya nyuma akiwa amevalia miwani na ‘earphone’ nyeupe masikioni. Alikuwa ana nywele ndefu na kwa kipindi chote kesi ilipokuwa inaendelea hakupata kunyanyua uso wake.

Miss Danielle alimtazama bwana Charles na kumwambia amngoje kwani kuna mtu anataka kuongea naye. Aliporudisha uso wake kuangaza, hakumwona mtu huyo tena.

Alikuwa amepotea machoni.

ENDELEA

Akafanya kutafuta kwa kuangazaangaza ndani ya jengo pasipo mafanikio, miwshowe akatoka kwa kukimbilia nje napo alipotuma macho ikawa kazi bure, mwanaume yule hakuwa anaonekana. Akashika kiuno chake akijiuliza kama kile alichokuwa anakiona ni uhalisia ama ni mafumbo ya macho yake.

“Miss!” sauti iliita nyuma yake, lipogeuka akamwona Charles akiwa amebebelea faili lake anamsogelea. “Vipi? Kuna nini?” akauliza.

Miss Danielle akiwa amedaka kiuno chake akitupa macho huku na kule alafu akashusha pumzi ndefu na kusema, “Usijali, twende zetu!” wakajipaki kwenye gari na kuanza safari ya kutoka kwenye eneo la mahakama.

“Nini mipango yako sasa, miss?” akauliza bwana Charles. Yeye alikuwa abiria ingali Miss Danielle akiwa dereva. “Utarudi kazini kwako ama una mpango mwingine wa ziada?”

Baada ya Danielle kufikiria kidogo, akasema, “Sitaki kurejea tena kazini!” kauli hiyo ikamshtua kidogo bwana Charles, “kwanini?” akauliza akimtazama Danielle kwa macho ya kukodoa.

“Nataka nifanye mambo yangu mengine sasa,” akajibu Danielle. “Punde nitakapopata pesa, nitatazama fursa nyingine ambayo itaweka kichwa changu huru.”

Bwana Charles akatabasamu na kutia neno, “Ni jema. Unajua ni pesa nyingi sana utakayopata, ni juu yako kuamua la kufanya!” baada ya hapo kukawa kimya kidogo gari likienda.

Lakini kichwani mwa bwana Charles kulikuwa na kitu kinachomtatiza, mara kadhaa alimtazama miss Danielle na kujitahidi kufunga kinywa chake. Ingawa Danielle alikuwa anatazama mbele, bado alikuwa ana uwezo wa kumwona mwanaume huyo akimkodolea.

“Vipi, kuna tatizo?” akauliza.

“Hamna!” akawahi kujibu bwana Charles na kuongeza, “lakini nilitaka tu kufahamu jambo moja.”

“Lipi hilo?”

“Ni kweli ulikuwa na mahusiano na bwana Marshall?”

Swali hilo likamfanya Danielle amtazame bwana Charles kabla hajaurejesha uso wake mbele waendako.

“Kwanini umeuliza hilo?”

“Nataka tu kufahamu, hamna lolote kubwa.”

Miss akakaa kimya kwanza. Akamtazama tena bwana Charles na kuurejesha uso wake mbele.

“Hamna shida kama haujisikii kujibu,” alisema Charles kitahadhari. “Naelewa. Siku utakayojisikia kunambia unapajua pa kunipata.”

Miss Danielle hakuongezea neno, akaendelea kuendesha. Alipofika mahala pa kumtua Charles akafanya vivyo na kuendelea na safari yake moja kwa moja mpaka nyumbani.

Bado muda ulikuwa mwingi kumaliza siku, na kwakuwa alipata ushindi siku hiyo akaona ni vema akaenda kujipongeza fukweni, basi akapaki vitu vyake kwenye gari na kuanza safari ya kwenda huko.

Akiwa njiani, simu yake ikaita. Ilikuwa ndani ya mkoba kabisa hivyo kuipokea ikamlazimu aegeshe gari kando na kuitafuta. Alipoiweka mkononi na kutazama akabaini ni mkuu wa shirika la kipelelezi, FBI. Akashusha pumzi na kujiuliza aipokee simu ile ama aipuuzie?

Alipofikiri kwa sekunde chache akakata shauri kwa kupokea. Baada ya salamu tu mkuu huyo akamwomba radhi na kumpasha anamwitaji kazini aendelee na majukumu yake kama kawaida.

Kuhusu hilo, mis Danielle akakataa katakata akisema ni muda wake sasa kutazamia kufanya mengine. Japo mkuu alimsihi sana. Danielle hakutazama tena nyuma, alitaka aendelee. Hakutaka tena kurudi alipotoka. Akakata na simu.

Alipofika ufukweni, jua bado lilikuwa linawaka, akatandika kijimkeka chake kepesi mchangani na kujilaza hapo. Basi akiwa anapata upepo na kufurahia mwonekano, kichwani mwake akawa anawaza mambo mbalimbali, moja juu ya pesa yake na mipango, pili juu ya mkuu wake na maombi yake.

Mwili ulikua unapumzika ingali kichwa kinachemka.


**

“Ni dollar mia mbili tu,” alisema mhudumu akimtazama bwana Morris. Ni ndani ya ‘mall’ kubwa ambapo mwanaume huyo, mshirika wa bwana James Peak, alikuja kujipatia mahitaji yake kadhaa.

Mkononi alikuwa amebebelea mfuko wenye chapa ya jina la ‘mall’. amevalia shati jeupe aliyoikabia na mkanda mwembamba mweusi pamoja na suruali yake ya kitambaa na moka.

Basi baada ya mwanaume huo kuambiwa bei, akazama mfukoni na kukabidhi pesa kisha akaaga na kwenda zake kwenye gari.

Alikuwa yu mwenyewe. Gari lake lilikuwa upande wa pili wa barabara. Alitazama pande zote mbili kabla hajavuka kwenda kukuta chombo chake cha usafiri.

Akafungua kwanza mlango wa nyuma na kutia mzigo wake huko ndipo akaketi mbele na kutia gari moto. Alipochopoka, ikapita kama sekunde tano, gari lingine ambalo lilikuwapo karibu kwenye maegesha, nalo likachopoka kumfuata.

Bwana Morris pasipo kujua akaendelea na safari yake, na kwa kuondoa uchovu na kuboreka katika safari yake ndefu, akawasha radio na kuweka muziki. Basi akiwa anaendesha akawa anatikisa kichwa chake kwenda mbele na nyuma, kushoto na kulia.

Baada ya kupoteza lisaa barabarani, sasa bwana Morris akaanza kupata shaka kwamba huenda anafuatiliwa. Kwa kutazama vioo saidizi vya gari alipata kuona gari lile ambalo limemuungia mkia.

Basi kwa usalama wake, akaongeza kasi ya gari na akaona ni vema amtaarifu mwenzake juu ya jambo hilo ili kuona kama anaweza kumpatia msaada.

“Unaweza ukaniambia laonekaje na namba zake za usajili?” sauti ilimuuliza tokea kwenye simu.

“Hapana, lipo mbali kubaini namba, ila ni SUV nyeusi!”

“Sawa, kuwa mwangalifu. Nafanya jitihada za kusonga karibu.”

Bwana Morris alipoongeza kasi, ndani ya muda mchache, akawa ameipoteza gari ile iliyokuwa inamfuatilia, basi alipoligundua hilo, upesi akarejea kwenye barabara yake ya kuelekea nyumbani na kumpasha mwenzake kuwa yuko salama sasa.

“Nimempoteza, hamna haja ya kuja tena.”

Lakini bwana Morris hakuwa anafahamu kwamba gari yake ilikuwa inavuja mafuta, na swala hilo halikuwa limeanza karibuni, lah! Bali tokea alipotoka kwenye mall.

Lilikuwa ni jambo la muda tu kwa gari lake kusimama kwa kukaukiwa.

Akiwa amebakiza kama maili moja afike nyumbani kwake, gari likaanza kutoa ishara ya kukaukiwa mafuta.

Akiwa amestaajabu, akafikiria pengine gari lilikuwa limepatwa na maruhani, mbona alikuwa ametoka kulijaza muda si mrefu kabla ya kwenda kwenye mall kupata mahitaji yake?

Tena full tank!

Muda si mwingi gari likazima kabisa na kumfanya asiwe na msaada wowote, akiwa amekanganyikiwa, akashuka na kuanza kulikagua. Kidogo akabaini kuvuja kwa mafuta kutokana na kutobolewa kwa tenki! Kulikuwa na matundu mawili ya ukubwa wa msumari mdogo.

Ina maana wale waliokuwa wanamfuatilia walikuwa wametoboa tenki la mafuta? Alijiwazia kichwani. Kidogo, gari aina ya SUV likaja kwa kasi sana, hakuweza kulitambua likiwa mbali kutokana na uhafifu wa mwanga.

Liliposonga karibu, akawa na muda mchache sana wa kujiepusha. Kabla hajafanya kitu akawa amekula risasi tatu za kifuani, akadondoka akiwa anagugumia kifo.

Jamaa mmoja toka kwenye SUV, akashuka na kumjongea. Jamaa huyo alikuwa amevalia kofia na kinywa na pua yake akivifunika kwa kitambaa, koti refu na viatu vya kuendeshea farasi. Mkononi mwake alikuwa amebebelea bunduki inayotema moshi kwa moto wa hapo nyuma.

Akasimama kando ya Morris.

**
 
*NYUMA YAKO (MWISHO WA MSIMU WA PILI) -- 32*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

Liliposonga karibu, akawa na muda mchache sana wa kujiepusha. Kabla hajafanya kitu akawa amekula risasi tatu za kifuani, akadondoka akiwa anagugumia kifo.

Jamaa mmoja toka kwenye SUV, akashuka na kumjongea. Jamaa huyo alikuwa amevalia kofia na kinywa na pua yake akivifunika kwa kitambaa, koti refu na viatu vya kuendeshea farasi. Mkononi mwake alikuwa amebebelea bunduki inayotema moshi kwa moto wa hapo nyuma.

Akasimama kando ya Morris.

ENDELEA

Akamtazama mwanaume huyo akiwa anakufa, na basi kumwahisha safari akamwongezea risasi zingine nne kisha akarudi zake kwenye gari na kutimka akiacha maiti.

Baada ya muda kidogo habari za Morris zikamfikia bwana James Peak na washirika wake wengine, wakafika eneo la tukio. Polisi walikuwa wamejaa eneoni na pia waandishi wa habari kadhaa wakifyatua picha na kuandika maelezo.

Basi baada ya Bwana James kufika hapo akapekua sana eneo la tukio pasipo kubaini kitu cha maana, ni baada ya kuzungumza na maafisa waliowahi ndipo akabaini vitu vichache hususani kiatu alichokuwa amekivaa muuaji na pia maganda ya risasi.

“Vipi mmeweza kubaini aliyefanya tukio hili?”

“Hapana, ni mapema kwa sasa. Pengine baada ya kufanya upelelezi zaidi.”

Basi mwili wa Morris ukachukuliwa kupelekwa kwenye uchunguzi zaidi huku bwana James na washirika wengine wawili wakiwa wamebakiwa na maswali, ilikuwa ni tishio sasa kwa usalama wa maisha yao.

“Samahani, kama hautojali twaweza kuongea kidogo?” alikuwa ni mwandishi wa habari akinena na bwana James.

Bwana huyo akamtazama mwandishi kwa jicho la ukali, pasipo kusema kitu, mwandishi akajiondokea akiomba radhi.

“Mkuu, tunafanya nini?” akauliza mshirika mmoja, bwana Gerrard, akimtazama bwana James kwa jicho la mkanganyiko. Nyuso zao zilikuwa zimelowana hofu lakini pia mafikirio.

“Sijajua,” akasema James akitikisa kichwa. “Naona hili jambo linazidi kuwa kubwa zaidi na zaidi.”

“Vipi tukaomba msaada, mkuu. Huoni tunaweza kupukutika kabisa?” akauliza mshirika mwingine, kwa jina bwana Harold. Yeye huyu alikuwa ana hofu zaidi.

“Naombeni muda zaidi, sawa?” akasema James kisha akataka kuendea gari lake kabla hajageuka na kuwaambia wenzake, “Kuweni makini sana na hakikisheni tunakuwa kwenye mawasiliano muda wote, sawa?”

Aliposema hayo akajiendea zake kufuata gari alafu akatimka.

Kesho yake akiwa kazini akafikiria sana pasipo kikomo. Alitoka kwenda kuuona mwili wa Morris na kufanya taratibu za maziko, baadae akakutana na wale washirika wenzake wawili, bwana Gerrard na Harold wajadili hatma yao.

Kwenye kikao hicho cha dharura wakakubaliana kwamba, kama inawezekana, wafikishe azimio lao kwa mkuu wao wa kazi juu ya kuachia na kukabidhi kesi hiyo kwa FBI.

Walihofia usalama wao, haswa mabwana wale wawili, Harold na Gerrard. Upesi walitaka mkuu ahusishwe na kufikia hitma.

Basi baadae bwana James alipopata nafasi akaenda kuonana na mkuu wake na kumweleza juu ya makubaliano yao lakini asiseme kuwa wamehofia bali kupunguza ukubwa wa msukumo kwa jeshi la polisi ingali FBI wanashughulikia kesi inayorandana nayo.

Lakini si kheri, swala hilo likakataliwa katakata!

“Bwana James, sikudhani ungeweza kunifadhaisha kiasi hiki. Sisi kama jeshi la polisi tuna nafasi yetu na wao kama FBI wana nafasi yao. Kila mtu ana uwanja wake, hata kwenye hii kesi pia.

Wao wanamtafuta mtu anayehusika na kupotea kwa Raisi, sisi tunahusika na kumtafuta muuaji. Tutashirikiana katika hili kila mtu akicheza nafasi yake.

Kutopatikana kwake kwa wakati kusitufanye tukajiona hatufanyi kazi. Kwani hao FBI hawamtafuti? Wamempata? Si bado wanahangaika kama sisi?

Nakwambia James, endapo tukifanikisha hili, kila mtu atajenga imani zaidi kwa jeshi letu. Jua watu wamepoteza imani na FBI, CIA na hata USSS baada ya hili tukio la kupotea kwa Raisi. Hii ndo nafasi yetu!”

Baada ya maelezo hayo bwana James akawa hana cha kusema zaidi ya kuafiki. Alitoka akiwa ametingwa na mawazo akarejea kwenye kiti chake kabla ya muda si mrefu kutoka tena ofisini kwenda kusikojulikana.

**

“Nimeshatekeleza mpango mwingine,” alisema bwana William akiongea na Ian kwenye simu. Bwana huyo alikuwa kwenye gari yake, viti vya nyuma akiwa ameweka zile nguo alizotendea kazi; kofia, koti na viatu.

“Umehakikisha haujaacha kielelezo?” akauliza bwana Ian.

“Hapana, sijaacha kitu,” akasema William kwa uhakika.

“Willy, kumbuka huu ni mpango wa kando. Unapofanya hayo hakikisha hauachi kitu tusije tukavuruga na kujipa kesi nyingine. Sawa?”

“Usijali, mkuu.”

Simu ikakata.

Bwana Willy akampigia James, punde simu ikapokelewa na watu hao wakakubaliana kuonana mahali fulami mud si mwingi. Kabla Willy hajaenda huko, akamtumia ujumbe bwana Ian kwamba bila shaka anaenda kumaliza swala lao.

**

Saa nane mchana …

Bwana James alikuwa ameketi mahali patulivu akiwa anakula ‘bites’. Akiwa ameegesha gari lake pembeni, aliwasha muziki kwa mbali taya zikifanya kazi.

Alikuwa hapo akimngoja bwana William, tayari alishapoteza kama robo saa papo. Alitazama saa yake ya mkononi na alipotoa tu jicho lake kutazama mbele akaona gari likiwa linapaki. Bila shaka alikuwa ni William.

Mwanaume huyo alikuwa amebalia ‘form six’ nyeupe, suruali nyeusi ya kadeti na raba yeupe. Mkononi alikuwa amebebelea simu.

“Habari yako? Samahani kwa kukawia,” alisema bwana William akimpatia mkono James.

“Usijali, karibu.”

“Nashukuru sana. Nimeitikia wito wako mheshimiwa.”

“Nashukuru sana, lakini pengine sikuwa na habari nzuri kwako. Kama unavyoona mambo yanazidi kuwa magumu kila uchwao. Tunajitahidi pasi na matunda mauaji yakiendelea. Vipi kwa upande wenu mmepata jambo?”

Mazungumzo haya yakazongazonga mpaka pale ambapo bwana William aliamua kuvuta kwenye upande wake. Alikuwa pale kujua kama bwana James ameridhia ushauri wake ama lah.

“Nasikitika kukwambia haitawezekana,” akasema James. “Tutaendelea kushikilia hii kesi mpaka kikomo chake!”

Maneo hayo yakamkwaza sana William. Akamfokea bwana James kwa kumpotezea muda wake kisha akamsisitiza hatomtafuta tena, janga analolichuma atakula na wa kwake.

Aliposema hayo akaenda zake pasipo kuaga. Alipopiga hatua chache tu kuendea gari yake, bwana James akatoa kamera yake na kumchukua picha kadhaa.

William alipoyoyoma, James akashuka kwenye gari lake na kufuatilia nyayo za viatu vya bwana William. Akazipima na kuandika saizi yake kando kisha pia akazipiga picha na kujirejesha kwenye gari lake.

Akapiga simu.

“Nimepata saizi ya kiatu chake na pengine tutajua na kimo chake.” aliposema hayo akakata simu na kumpigia mtu mwingine akitimka.

Bwana huyo alishaanza kuhisi huenda bwana William ndiye yuko nyuma ya haya yote, na si Marshall kama wanavyodhani.

Tayari sori ya kiatu ilikuwa inaunga mkono hoja yao, bado vinginevyo.

“Harold, umemuona?” akauliza bwana James simuni.

“Ndio nimemwona,” sauti ikajibu simuni. “Na hapa nipo nyuma yake kwa hatua kadhaa nikimfuatilia.”

“Sawa, hakikisha haufanyi makosa,” James aliposema hayo akakata simu na kushusha pumzi.

Kwanini afanye hivi? Akajiuliza. Kwanini sikulifikiria hili tangu mwazo? Akaendelea kujiuliza. Hapa ndipo akakumbuka lile tukio la ajenti wa FBI kutupa risasi kabla ya agizo. Ina maana wapo pamoja na Willy?

Ina maana lengo lao ni kumuua Marshall?

Kwanini?

**
 
*NYUMA YAKO (CHOMBEZO LA MSIMU WA TATU)*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA

“Ndio nimemwona,” sauti ikajibu simuni. “Na hapa nipo nyuma yake kwa hatua kadhaa nikimfuatilia.”

“Sawa, hakikisha haufanyi makosa,” James aliposema hayo akakata simu na kushusha pumzi.

Kwanini afanye hivi? Akajiuliza. Kwanini sikulifikiria hili tangu mwazo? Akaendelea kujiuliza. Hapa ndipo akakumbuka lile tukio la ajenti wa FBI kutupa risasi kabla ya agizo. Ina maana wapo pamoja na Willy?

Ina maana lengo lao ni kumuua Marshall?

Kwanini?

ENDELEA

Baada ya Harold na Gerrard kutimiza walichoagizwa na inspekta James Peak, wakakutana majira ya usiku kujadili zaidi juu ya walichokipata. Kwa kuanza, walipata kufahamu wapi yalipo makazi ya bwana William lakini zaidi wakazidi kujengea kwenye hoja yao ya kumshuku bwana William kwa kuliona gari aina ya SUV likiwa kwenye sehemu ya maegesho ya makazi yake.

Basi baada ya hapo wakapanga kumtazama na kumfuatilia kwa ukaribu bwana huyo wakiwa wanawasiliana kwa ukaribu sana. Kila mmoja aweke namna ya kuwasiliana na mwenzake na wawe tayari muda wowote ule.

“Tumeelewana?” akauliza James.

“Ndio,” wakajibu washirika.

“Lakini pia tusisahau kumfuatilia mtuhumiwa wetu. Pengine tukimpata atatueleza zaidi kuwahusu hawa watu, sawa?”

“Sawa, mkuu.”

Maongezi yakakoma.

**

Usiku wa saa nne


Akiwa mpweke sebuleni mwake, Danielle alivuta rimoti na kubadili chaneli kwenye runinga. Alitazama chaneli ya kwanza, pili na kisha ya tatu ambayo ilimvutia, akatuama.

Mezani kulikuwa na sahani ya chakula ambacho amekibakiza baada ya kushiba. Chakula hicho kilikuwa kimekwishapoa, ungeweza kukibaini hata kwa macho tu. Danielle alikuwa yu bize akicheza na simu yake. Hata chaneli aliyoiweka hakuwa na muda nayo.

Akiwa anabofya, akasikia sauti ya kugonga mlangoni. Kidogo alishtuka maana hakusikia hodi tokea getini kabla ya kufika hapo mlangoni. Kwa mashaka, akauliza ni nani anayebisha huku akiwa anatazamia namna ya kujiimarishia usalama.

Sauti ikamjibu mlangoni kuwa ni Marshall! Akasimama kwa kuganda.

“Nani?” akauliza tena.

“Marshall!” sauti ikarudia tena mlangoni. Masikio yake yalitibitisha kweli sauti hiyo ilikuwa ni ya Marshall, basi upesi, asijue kwanini anafanya vivyo, akauendea mlango na kutazama.

Kweli alikuwa ni Marshall!

Mwanaume huyo alikuwa amevalia sweta la kijivu lenye kofia ya kufunika kichwa. Alimtazama Danielle machoni na upesi mwanamke huyo akamsihi aingie ndani.

“Ulikuwa wapi, Marshall? Upo salama?” Danielle aliropokwa na maswali. Alimtazama Marshall kana kwamba mzazi ambaye amempoteza mwanaye kwa majuma na sasa amerejea mikonoi.

“Niko salama, Danielle,” akasema Marshall kisha akamtaka Danielle azime taa yake ya sebuleni. Upesi Danielle akafanya vivyo kukawa kiza. Mwanga wa runinga ndiyo ambao ukawa unaangaza ndani ya sebule.

Na kufanya usikivu uwe bora, Danielle akazima na sauti ya runinga.

“Marshall,” Danielle akaita. Alikuwa anamtazama Marshall kwa mashaka lakini pia kukanganyikiwa. “Ulikuwa wapi muda wote huo?”

Kabla ya Marshall kusema jambo akamwomba Danielle ampatie maji ya kunywa. Danielle aliponyanyuka akamuuliza pia Marshall kama angehitaji na chakula.

“Hapana, nashukuru miss,” akasema Marshall akitazama chini, basi Danielle akaenda zake kumletea Marshall maji. Aliporejea akaketi pembezoni mwa mwanaume huyo na kuteta mambo kadhaa.

Marshall hakuwa muwazi sana. Ni kama vile alikuwa mtu mwenye haraka zake. Alimwambia Danielle kuwa amempoteza Katie na maisha yake yamebadilika zaidi. Anajihisi amekuwa mnyama zaidi kuliko binadamu.

Akiwa anaongea kuhusu Katie, macho yake yakawa mekundu zaidi. Danielle alipata kuona ni namna gani Marshall anavyoumia kuongelea hilo jambo.

Zaidi ya hilo, Marshall akamweleza Danielle juu ya nia yake kuwa sasa hana tena cha kupoteza na atamwangamiza kuanzia mtoa agizo mpaka yule ambaye amefanya Katie wake akapoteza uhai, kisha atafute ukweli kuhusu Raisi.

Akiwa anaongea, ungeweza kuona haja ndani ya maneno yake. Namna gani ambavyo uso wake unamaainsha kile anachokisema.

Danielle alimtazama mwanaume huyo kisha akamuuliza, “Marshall, ulikuwa ni wewe, sio? … pale mahakamani.”

Kabla ya Marshall hajajibu, Danielle akauliza, “kwanini haukutaka kungoja?”

“Hapakuwa mahala sahihi!” Marshall akamjibu akimtazama na macho yake mekundu kisha akampongeza mwanamke huyo kwa kushinda kesi.

“Kwahiyo vipi sasa kuhusu mpango wako baada ya hapo?” Marshall akauliza.

“Aaahmm, natazamia kufungua shirika langu,” Danielle akajibu kwa kujiamini,

“Shirika? Shirika la nini?”

“La upelelezi. Unajua Marshall napenda kitu ninachokifanya lakini naona sasa sipapendi tena mahali ninapofanyia shughuli hiyo. Nimekaa na kutafakari nimeona nifungue shirika lango binafsi la upelelezi.” baada ya Danielle kusema vivyo akamtazama Marshall na kumuuliza, “Unaonaje wazo langu?”

“Ni jema,” Marshall akamuunga mkono kisha akamwambia adhma yake, “Najua utapata pesa muda si mrefu, Danielle, nimekuja hapa kukuomba kiasi fulani cha pesa lakini nitakirejesha.”

“Unataka kufanya nini Marshall? - waweza kuwa muwazi zaidi kama hutojali?”

Marshall akamwambia kuhusu mpango wake kwa mke wa Raisi, bibie Mariettea Abbey. Anahitaji kiasi fulani cha pesa kwa ajili ya kumkamata mwanamke huyo na pale atakapotimiza hitaji lake basi atarejesha mara moja.

Basi Danielle akamtazama Marshall kwa mafikirio. Hakuwa anaona kama mpango huo utakuwa mwema kwa uhai wa Marietta. Aliamini fika Marshall atammaliza mwanamke huyo akishatimiza haja yake, kitu ambacho kwake hakikuwa sahihi.

Akamwambia Marshall,

“Unaonaje tukafanya kazi hii kwa pamoja?”

“Kivipi?” Marshall akatia shaka. “Sitaki kumwingiza yeyote katika matatizo yangu.”

“Usijali, Marshall,” Danielle akamtoa hofu. “Najua kupigania na kutetea uhai wangu, nadhani hata wewe unalifahamu hilo. Jambo lako ni kubwa sana, itakuchukua muda sana ama ugumu mkubwa kulifanikisha peke yako. Unaonaje tukaungana kulifanya kwa pamoja?

Shirika langu litakuwa changa, naamini tukifanya kazi hii kwa pamoja na tukafanikiwa kufumbua fumbo hili, utakuwa ni mwanzo mkubwa sana kwangu, na hata kwako pia. Waonaje?”

Kidogo Marshall akanyamaza maneno hayo yakiwa yanazama ndani yake. Alinyanyua glasi ya maji na kunywa mafundo mawili kisha akaendelea kuwa kimya kidogo akitafakari.

“Unahitaji hilo Marshall, unahitaji timu kufanikisha hili,” Danielle akaendelea kusisitiza. Alikuwa anamtazama Marshall machoni akiwa anaongea kwa sauti kuu.

“Unadhani hilo litasaidia?” Marshall akauliza kisha ndiyo akamtazama Danielle. Mwanamke huyo akamhakikishia, “Kwa asilimia zote.”

“Basi tufanye vivyo,” Marshall akaafiki. Danielle akatabasamu na kumwambia, “hutokuja kujutia hili.” kisha akaongezea, “lakini bado tunamhitaji mtu mmoja.”

“Nani huyo?” Marshall akauliza

“Jack Pyong!” Danielle akajibu kwa tabasamu alafu akauliza, “Hauoni akikaa kwenye tarakilishi tutamaliza mambo mapema?”

Marshall akajikuta akitabasamu kwa mara ya kwanza tangu alipoonana na Danielle.

**

- Nini kinafuata kwa Marietta Abbey?

- Nini kinamfuatia Ian Livermore na kundi lake?

- Nini hatma ya William mbele ya James Peak?

- Raisi yuko wapi?

- Nani anahusika haswa na kupotea kwake na kwanini?
 
*NYUMA YAKO (MSIMU WA TATU) -- 01*

*Simulizi za series*


ILIIPOISHIA

“Basi tufanye vivyo,” Marshall akaafiki. Danielle akatabasamu na kumwambia, “hutokuja kujutia hili.” kisha akaongezea, “lakini bado tunamhitaji mtu mmoja.”

“Nani huyo?” Marshall akauliza

“Jack Pyong!” Danielle akajibu kwa tabasamu alafu akauliza, “Hauoni akikaa kwenye tarakilishi tutamaliza mambo mapema?”

Marshall akajikuta akitabasamu kwa mara ya kwanza tangu alipoonana na Danielle.

ENDELEA

Zilipita siku nne kukiwa kimya kusiwe na habari yoyote ya kukamata vyombo vya habari. Kulikuwa shwari na amani japo bado watu walikuwa wakizungumza na kujadili matukio yaliyopita.

Jua lilikuwa likizama na kutuama kwa utulivu. Lakini katika hayo si kwamba watu walikuwa wamelala ama tuseme si wote walikuwa wanalala.

Watu hawa watatu: Marshall, Jack Pyong na Miss Danielle walikuwa macho karibia kila usiku. Walikuwa wakipanga na kupangua. Walikuwa wakiumba na kuvunja. Walikuwa wakiwaza na kuwazua, kuhesabu na kuhesabua.

Wote hawa walikuwa wanafanana kitu kimoja; ni watu wenye ujuzi wa kufundishwa darasani na vipaji binafsi. Wote wakiwa watu waliolitumikia taifa kwa njia kubwa na pana, tena kwenye vitengo nyeti kabisa vya usalama vya nchi.

Walipoona kila walilolipanga limekaa sawa, basi wakapumzika katika siku hii ya nne wakiwa wanangoja sasa utekelezaji.

Mipango yao hii haikuwa statiki, lah! Walikubaliana itakuwa inabadilika kutokana na matukio yanavyokwenda, kutokana na mambo yatakavyoenenda. Lengo kuu likiwa ni kuisaka haki popote pale lakini pia na kuufunua ukweli kwa hadhira.

Kulitimiza hilo kwa ufanisi, jamaa hawa wakawa wamekodisha eneo katikati ya jiji la New York maalumu kwa ajili ya kufanyia kazi zao ‘formal’ na zile ambazo ni za siri zaidi basi zitakuwa zikifanyiwa ndani ya nyumba maalum ambayo hii hawakuwa wameinunua katikati ya jiji bali mbali kabisa kwasababu za kiusalama.

Wakiwa huko itakuwa rahisi kumtambua adui awajiayeh tofauti na wakiwa mjini. Na kwa usalama zaidi, nyumba hiyo ilikuwamo na handaki lakini pia njia za kutokea ambazo hazikuwa nyepesi kuonekana.

Nyumba hii ambayo ipo mbali na jiji, itakuwa ikitumika kama ‘engine’. kama kitovu cha mambo yote yanayoendelea kwenye yale makazi ya kule jijini.

Humo kutakuwa kukikaliwa na tarakilishi kubwa zenye uwezo lakini pia vifaa kadha wa kadha vya kisayansi kusaidia upelelezi. Humo sasa watakaa wanaume wawili ambao wanatafutwa, yaani Marshall na Jack Pyong.

Watafanya kazi zao huko na pale itakapohitajika basi watatuma taarifa kwenye ofisi iliyokuwapo jijini, ambayo inakaliwa na Miss Danielle.

Kwahiyo kwa mpango huu basi, Miss Danielle atakuwa anatumika kama ‘cover up’ ya mambo yote hayo. Kwa kupitia ofisi yake atakuwa anafuatilia na kufunua mambo ambayo aidha anafikishiwa na wakina Marshall ama anayafunua mwenyewe kwa upelelezi.

Yale yote ambayo Marshall na Jack Pyong watakuwa wakiyapata, basi watakuwa wakimfikishia Miss Danielle kuyafikisha.

“Wamesema itachukua mwezi kukamilika,” alisema Danielle akiwaambia Marshall na Jack. Mwanamke huyo alikuwa ametoka kufuatilia tena usajili wa kituo chake cha upelelezi binafsi. Mambo hayakuwa yanaenda vibaya, lah! Ila ni jambo linalochukua muda kuhitimu.

“Lakini ni uhakika?” akauliza Jack.

“Hamna shida,” Danielle akamtoa hofu akinyoosha miguu yake kwa kiti. “Kila kitu kitakuwa sawa lakini si kwamba tungoje. Inabidi tuanze kutekeleza mipango mara moja!”

Basi ulipowadia wakati wa jioni wakakutana wote kwenye lile jengo ambalo lipo mbali na jiji. Huko wakakagua mdoli ambao ulikuwa umetengezwa maalum kwa ajili ya kujiveka bwana Marshall akienda kukutana na bibie Marietta.

Kila kitu kilikuwa sawa.

“Unaweza ukaujaribu,” akasema Miss Danielle. Mdoli huo ulikuwa unatengenezwa na mtu wao maalumu kwa hizo kazi, kwa jina Royal, mwanaume huyo alikuwa anahusika na kuwatengenezea midoli hiyo hata kwa shirika la CIA.

Na kama haitoshi, msanii huyo alikuwa ni mtaalamu haswa wa kufanya ‘makeup’, si tu kipaji bali pia na taaluma. Angeweza kubadilisha kabisa uso wako ukaonekana mtu mwingine tofauti.

Marshall akauvaa mdoli huo aliotengenezewa, na kila kitu kikawa sawa kabisa. Usingeweza kudhani kabisa kama ni Marshall bali ni mtu yule ambaye alikutana na Marietta na kukubaliana kupeana pesa kwa ajili ya taasisi yake ya watoto.

“Aiseee!” Jack alishangaa alipotazama kazi hiyo. Alimkagua Marshall na akajikuta akishindwa kabisa kupata walakini. Marshall alikuwa amebadilika kabisa usimtambua kwa namna yoyote ile.

“Ipo vipi?” Marshall akauliza akiwa amebadili sauti.

“Iko bomba,” Jack akajibu akionyesha ishara ya dole gumba. Alikuwa amefurahishwa na mabadiliko yale.

“Lakini kuna kitu cha ziada,” Marshall akawajuza wenzake. Wakaongozana mpaka chumbani ambapo aliwaonyesha chupa moja kubwa ya kioo, ndani yake kulikuwa na kimiminika chenye rangi ya maji.

“Ni nini hicho?” akauliza Danielle akisogea karibu kutazama.

“Ni Sodium Thiopental!” akajibu Marshall akiwa anatabasamu, Danielle akaachama kinywa, “Kweli?”

“Yah! Ndiyo yenyewe.”

“Umetoa wapi?” Jack akauliza akiwa anakodolea chupa hiyo.

“Ni story ndefu. Siku nikiwa na muda na nipo kwenye mood, nitawaeleza,” akasema Marshall akiwa anatabasamu kwa mbali, basi Daniell akampongeza kwa kufikiria hilo kwani litawasaidia sana kwenye kazi zao.

Lakini Sodium thiopental ni nini?

Hii ni ‘chemical composition drug’ yenye fomula C11H17Na02S ambayo ni mashuhuri kwa kusababisha ‘Anesthesia’. Anesthesia ni ile hali ya mtu kupoteza ufahamu ama kujitambua kwa muda (temporary loss of sensation).

Kemikali hii hutumika maalumu kwasababu ya kulazimisha kupata taarifa toka kwa mhanga. Kwa jina maarufu hujulikana kama ‘truth serum’ ambapo hufanya kazi kama kileo kwenye ubongo wa mhanga na hatimaye kumfanya aropoke kwa wepesi kile atakachokuwa anaulizwa.

Ila kisheria kitendo hiki ni kinyume na katiba ya Marekani ingawa kimekuwa kikitumika mara kadhaa kwenye maeneo kadhaa haswa taasisi za upelelezi, kwa siri.

“Itatusaidia kwa kuanza na Marietta,” alisema Marshall akifunga chumba. “Nitahakikishha napata kila taarifa aliyonayo kichwani.”

“Lakini vipi akaja kutambua?” akauliza Jack Pyong. Marshall akatabasamu na kumtoa shaka, “Jack, najua namna ya kuenenda naye. Hilo lisikupe tabu kabisa!”

Basi wakaketi sebuleni na hapo wakaendelea kuteta mambo kadhaa ikiwamo pia namna ambayo itakuwa inawaingizia pesa kwani watahitaji sana kwenye misheni zao.

Wakiwa wanajadili hilo wakakubaliana kufungua baadhi ya miradi, lakini katika namna kidogo ya ajabu Marshall akawaambia kuna mahali pengine pa kupatia pesa.

“Si kwa uhalifu, Marshall!” Danielle akaonya.

“Si kwa uhalifu,” Marshall akasema akimtazama mwanamke huyo kwa tabasamu alafu akahamishia macho yake kwa Jack Pyong. “Na nadhani njia hiyo itamfurahisha sana mmoja wetu hapa.”

“Njia gani hiyo?” Jack akapaliwa na swali.

“Msijali. Harakaharaka haina baraka. Tuanze kwanza na la huyu mwanamke, Marietta. Ama mwasemaje?” alisema Marshall kisha akajaribu kuvua mdoli wake aliokuwa ameuvaa.

Wenzake walikuwa wamejawa na shauku. Ungeona hilo kwenye nyuso zao.

**
 
*NYUMA YAKO (MSIMU WA TATU) -- 02*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Si kwa uhalifu,” Marshall akasema akimtazama mwanamke huyo kwa tabasamu alafu akahamishia macho yake kwa Jack Pyong. “Na nadhani njia hiyo itamfurahisha sana mmoja wetu hapa.”

“Njia gani hiyo?” Jack akapaliwa na swali.

“Msijali. Harakaharaka haina baraka. Tuanze kwanza na la huyu mwanamke, Marietta. Ama mwasemaje?” alisema Marshall kisha akajaribu kuvua mdoli wake aliokuwa ameuvaa.

Wenzake walikuwa wamejawa na shauku. Ungeona hilo kwenye nyuso zao.

ENDELEA

Basi ikapita siku moja tu na ndipo mwanaume mmoja akaonana na Marietta kwenye hoteli ya nyota tano ndani ya jiji la New York.

Marietta alikuwa amevalia suti nyeusi na skafu nyekundu shingoni ambayo aliifananisha rangi na mkoba wake. Kwa upande wa mwanaume yule mgeni, yeye alikuwa amevalia suti nyeusi kabambe na nywele zake amezilaza vema.

Mwanaume huyo alikuwa akifanania ipasavyo na ule mdoli ambao uliandaliwa na msanii Royal kwa ajili ya kazi ya Marshall. Mwanaume huyo alikuwa ni Marshall mwenyewe!

Lakini kwa jina la miungu nakwambia, usingeweza kumtambua mwanaume huyo kama ni Marshall hata tu kwa kuhisi. Si tu kwamba alikuwa hafananii, bali alikuwa haonekanii wala kusikika kama ni Marshall.

Sauti yake, umbo na mavazi yake yalimfanya aonekane ni mtu wa tofauti kabisa na ambavyo ungewaza kichwani. Hata Marshall mwenyewe alipojitazama kwenye kioo alikiri kujisahau kwa muda!

“Umewahi sana!” alisema Marietta akitazama saa yake ya mkononi. Uso wake ulikuwa umepambwa na tabasamu.

“Hamna, si sana, hata wewe upo ndani ya muda,” akasema Marshall, naye asinyime tabasamu la mbali.

Alimtazama Marietta ndani ya macho na kwa kiasi fulani mwanamke huyo akawa anaparanganyika. Umbo la Marshall si tu kwamba lilikuwa la kiume, bali pia matendo yake yalikuwa ya ki ‘gentleman’.

Alimsogezea kiti Marietta aketi. Alikuwa anatabasamu kwa kiasi. Alimpatia Marietta glasi ya kinywaji baada ya kummiminia, na muda wote wakati Marietta alikuwa anangea, mwanaume huyo akawa anamtazama ndani ya macho, kwa utulivu na uskivu mkubwa.

Kwa kiasi fulani, Marietta alijihisi mwanamke anayethaminiwa. Si kwamba wafanyakazi wake hawamtii na kumskiza, la hasha! Ile ilikuwa ni tofauti na muktadha wa aina hiyo.

Alicheka kidogo akamwambia Marshall,

“Hatukuwa tumemaliza maongezi siku zile, ulikuwa na kipi cha kunambia?” wakati anauliza alikuwa amesimamisha wima mikono yake na kuipinda apate kuweka ncha ya kidevu chake papo. Tayari alikuwa anamtazama Marshall kwa namna ya kipekee, naye Marshall alikwishalibaini hilo.

Akatafuna chakula chake kisha akajifuta na kitambaa na kusema kwa sauti ya chini, “Bibie Marietta, kwani una upesi sana?”

Kabla Marietta hajajibu, Marshall akaendeleza maneno, “Japo ni kwa muda mfupi, nimefurahi sana kukaa nawe hapa. Mimi ni mtu wa kutunza sana muda lakini nimejikuta nikipuuzia. Samahani kama nakukwaza.”

Marietta akatabasamu. “Hamna shida kabisa, hata nami nimefurahia sana. Sikuwa najua kama wewe ni mcheshi kiasi hiki!”

Wote wakatabasamu.

“Unajua muda mwingine kuna kitu huja pengine sababu ya nani uliyekaa naye karibu!” Marshall akadokeza.

“Ni kweli!” Marietta akaunga mkono. “Mimi sikuwa najua kama nitafurahia nitakapokuwapo hapa. Unajua siku zangu zimekuwa za kawaida sana, muda mwingine kutingwa na kazi kunasaidia kusogeza muda zaidi siku iishe.”

Basi mlango huu wa maongezi ukawafanya watu hawa waanze kuongelea mambo yao binafsi. Japo kwa uangalifu mkubwa kila mmoja akadokeza kile ambacho alikuwa anakiona kitampa ahueni dhidi ya mwenzake.

Muda ukiwa unaenda katika maongezi hayo Marshall akapata kujifunza kuwa Marietta amekuwa akiishi maisha ya upweke sana, na kwa kiasi fulani amekuwa ni mtu asiye na furaha kwa mawazo ama majuto.

Ndani ya lisaa limoja, Marshall akawa amefanikisha kabisa kumpeleka Marietta mpaka chumbani, mwanamke huyo akiwa hoi kwa pombe. Haikuwa kawaida yake kuwa hivi, yaani kulewa upesi, lakini hamadi alijikuta akiwa hajiwezi, kichwa kizito na anaropoka hovyo.

Marshall alikuwa amemtilia madawa - Sodium Thiopental - kwenye kinywaji chake.

Madawa hayo yalikuwa yakifanya kazi kama pombe kichwani mwa Marietta, hivyo kujumuisha na pombe ile ambayo alikuwa anakunywa, basi akajikuta hoi maradufu, taabani, dhoofu l’hali!

Marshall alimkokota na kumbwagia kitandani kisha akavuta kiti na kukaa pembezoni mwa mwanamke huyo akilenga kumchokonoa zaidi ajue kuhusu Raisi.

Lakini akiwa hapo kama dakika nane tu, mlango ukagongwa kwanguvu! Alishtuka kabla hajauliza ni nani yu mlangoni. Punde, sauti ya kiume ikamjuza, ni walinzi!

“Walinzi gani?” akapaza sauti kujongea mlango, kidogo, mwanaume kwa nje akamjibu kwa uwazi kuwa ni walinzi wa Miss Marietta Abbay! Alipochungua nje kweli akawaona wanaume wawili papo.

Akafungua mlango.

Wanaume hao wakaingia ndani upesi na waliporusha macho yao kitandani wakamwona ‘boss’ wao akiwa amejilaza hoi.

“Sidhani kama alikuwa anawahitaji,” alisema Marshall na kuongeza, “amepumzika!”

Lakini wanaume wale hawakumsikiza, wakawa wanajaribu kumnyanyua Marietta waende naye.

“Kwani kuna tatizo, maafisa?” Marshall akauliza akiwajongea. “Nadhani ni swala la kumuuliza mkuu wenu kama anahitaji kupumzika ama lah!”

Wakiwa wanajitahidi kumnyanyua Marietta, ndipo mwanamke huyo akapaza sauti iliyoelemewa na ulevi. Alikuwa anataka aachwe upesi!

Walinzi walijitahidi kumwelewesha lakini hakutaka kuwasikia abadani. Aliwafokea kama watoto akiwataka wamwache apumzike kwani hajawaita.

Basi walinzi wakajikuta hawana chaguzi bali kutii maagizo ya mkuu. Kishingo upande, wakaenda wakiwa wanamtazama Marshall kwa macho ya ndita. Mwanaume huyo akatabasamu akiwapungia mkono wa kwaheri.

Walipotoka, akaufunga mlango kwa komeo.

Walinzi wakashuka mpaka kwenye magari yao, wakajipaki na kungoja. Walikuwa na mashaka kabisa juu ya mwanaume yule, yaani Marshall, lakini hawakuwa na budi.

Waliona ni vema kungoja, na basi zitakapopita dakika kadhaa, mmoja wao ataenda tena kutazama usalama.

Basi zikapita dakika kumi, kumi na tano, ishirini, ishirini na tano. Zilipofika dakika thelathini, wanaume wale wakaona ni stara sasa kwenda tena kwenye chumba kutazamia usalama wa mkuu wao.

Hapa basi kugawanga majukumu, mmoja akaona aende na huku mwingine abaki kwenye gari pamoja na dereva.

Jamaa huyo mmoja akapandisha ngazi upesi na kwa ukakamavu. Hakukuwa na shida sana kwenye upande wa ulinzi maana ilikuwa inatambulika wako pale kwa ajili ya nani.

Alipofika kwenye chumba chenyewe, akabisha hodi.

Kimya.

Akabisha tena na tena. Kimya. Akaongeza nguvu kwenye mkono wake kwa kubisha zaidi na zaidi lakini bado matokeo yakawa yaleyale.

Kimya!

Kabla hajaamua kuchukua hatua yoyote, mara akasikia taarifa sikioni mwake kutoka kwa mwenzake. Taarifa ikimwambia,

“Yule mwanaume huyu huku chini!”

Upesi akamwambia mwenzake akimbize mwanaume huyo ilhali yeye anafanya namna akamwone mkuu anaendeleaje huko ndani. Baada ya muda mfupi, akawa ameshampata msimamiza na wakazama ndani.

Humo wakakumta Marietta amelala.

Yu salama salmini.

Lakini bado vifua vikiwa na hofu.

Nini kitakuwa kimetokea?


**
 
*NYUMA YAKO (MSIMU WA TATU) -- 03 & 04*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Upesi akamwambia mwenzake akimbize mwanaume huyo ilhali yeye anafanya namna akamwone mkuu anaendeleaje huko ndani. Baada ya muda mfupi, akawa ameshampata msimamizI na wakazama ndani.

Humo wakakumta Marietta amelala.

Yu salama salmini.

Lakini bado vifua vikiwa na hofu.

Nini kitakuwa kimetokea?

ENDELEA

Yule jamaa aliyemkimbiza bwana Marshall alikuwa anatota jasho na hakuwa amempata bwana huyo. Akiwa anajifuta na lesso aliteta akiwa anapambana kuhema.

Alitafuta kila kona, kila barabara akakimbilia lakini hakupata kitu. Kote kulikuwa kukavu. Moyo ulikuwa unamwenda mbio ingali hajamwona mlengwa wake.

Basi walichofanya ni kumbeba Marietta na kumweka kwenye gari kisha wakampeleka moja kwa moja hospitali kwa ajili ya uchunguzi zaidi. Huko baada ya vipimo ikabainika mwanamke huyo alikuwa amekunywa pombe nyingi tu, hakuna cha zaidi.

Hakuwa ameingiliwa wala kujeruhiwa kwa namna yoyote ile.

Lakini hayo kama hayatoshi, walinzi wale wakafanya jitihada kutambua ni nini kilimtokea Marietta kwani bado walikuwa na mashaka na mwanaume yule waliyemwona naye.

Basi kwa kupitia kamera za hotelini, wakanyaka uso wa mwanaume huyo na kuanza kusaka taarifa zake. Kwakuwa mwanaume huyo alikuwa amejitambulisha na kubebelea kitambulisho cha Umoja wa Mataifa, basi wakaanzia huko kumtafuta.

Wakasaka sana pasipo majibu. Taarifa za Marietta zikamfikia bwana Ian na basi akafanya jitihada za makusudi kwenda kuonana na mwanamke huyo.

Bwana Ian alikuwa amejawa na hofu. Akiwa njiani alipata kujiuliza sana ni nini ambacho kitakuwa kimemtokea mwanamke huyo kwani usalama wake upo mikononi mwake.

“Nilikuambia uwe makini, Mareietta!” alifoka Ian ambaye kwa Marietta alikuwa anatambulika kwa jina la Dick. “Umefanya nini sasa? Unaendaje kuonana na watu usiowajua na unafahamu fika, unafahamu wazi namna tulivyo, mazingira tuliyomo!”

Bwana Ian alikuwa amefura. Marietta alikuwa ameketi kwenye kochi akiwa ameegamia tama macho yanatazama chini. Alikuwa amenywea. Kichwa kilikuwa cha moto.

Bwana Ian akashika kiuno kisha akakiachia, akakishika tena akitembea kwenda mbele na kisha kukata kona kurudi nyuma, alafu tena anaenda mbele.

Uso wake ulikuwa umejawa na ndita. Hawezi hata kuhema vizuri, ni kana kwamba kiroba cha ndizi kimetuama juu ya kifua chake.

Akajaribu kuketi. Akanyoosha miguu kisha akaikunja tena. Akakunja mikono na kulaza mgongo wake kwenye kiti, mara akanyanyuka na kumtazama Marietta, “Unakumbuka mambo uliyoyasema?” akauliza.

Marietta akatikisa kichwa, “Sikumbuki nililofanya hata moja!”

“Na vipi kuhusu maelezo yake ya awali?”

“Alisema anafanya kazi Umoja wa Mataifa.”

“Kitengo gani?”

“Sikumbuki vema lakini ni kuhusu mambo haya ya watoto kama sikosei.”

“Huna uhakika!”

“Dick, tafadhali. Siko vizuri kwa sasa. Najua nimefanya nisivyotakiwa ila ndo’ kishatokea. Kama kuna cha kujadili hapa basi ni cha kufanya sio yaliyopita!”

Japo Marietta alieleza vema, bado bwana Ian hakuwa anaelewa. Aliendelea kuporomosha lawama kwa Marietta kwa uzembe wake na ukaidi, ikafikia kipindi sasa Marietta akashindwa kuvumilia, naye akaja juu wakiwakiana.

“Yote haya umesababisha wewe!” alifoka Marietta. “Wewe ni mwanaume gani, au kwasababu waona nimenyamaza basi wadhani ni mjinga, sio?

Dick, tangu mume wangu apotee, umeonana na mimi mara ngapi? Tumekuwa pamoja mara ngapi? Kila siku umekuwa mtu wa kusingizia umebanwa na kazi. Unakimbia huku na kule. Haujali kabisa kuhusu mimi!”

Alipofoka vivyo, akajikuta akiangua kilio. Alijifunika uso wake kwa viganja akamwaga machozi. Bwana Ian akamtazama lakini asimguse wala kuhangaika naye.

Marietta akaketi kwenye kiti na kuendelea kulia. Baada ya kama dakika nane, akatulia kimya. Alikuwa anavuta makamasi mepesi na kupiga kwikwi za kilio.

Kukawa kimya kwa kama dakika mbili. Bado bwana Ian alikuwa anamtazama Marietta pasipo kusema kitu, ila ndani yake alikuwa ni kama mtu anayejutia, pengine anakosa tu namna ya kuanza maongezi.

“Nimekuwa nikiishi maissha ya ajabu sana,” akasema Marietta. “Nimekuwa mwenyewe sasa, mpweke niliyetelekezwa. Si wewe Dick ambaye ulikuwa hapo awali. Umebadilika kabisa na ninajua kwanini, umeshapata ulichokuwa unakitaka.

Mimi sio mke wa Raisi tena. Sina thamani tena kwako, sio?”

“Marietta,” akaita Ian akimsogelea mwanamke huyo karibu. “Sikulenga kukuumiza, na si kama unavyoniwazia. Mambo hubadilika.”

Aliposema hayo Marietta akamtazama mwanaume huyo kwa macho yake mekundu yaliyolowana. Macho yake yalikuwa yamefichwa na ndita za mashaka na maulizo.

“Mambo hubadilika, sivyo?”

“Sijamaanisha hivyo unavyowaza!”

“Usijali, Dick. Nimekuelewa vema. Nadhani sasa ni muda wa kila mtu kutenda na kuenda na njia yake.”

“Marietta, umoja wetu ndiyo nguvu yetu.”

“Umoja upi huo? Mbona sikuwa nauona siku zote hizo?”

“Marietta, mimi na wewe tun--”

“Sitaki kusikia kitu! Nakuomba nyanyuka uondoke kwangu.”

“Tumefikaje huko?”

“Sijui ila ndiyo tumeshafika. Toka kwangu!”

Baada ya kuona Ian haelewi, Marietta akapiga kelele kuita walinzi na ndani ya muda mfupi walinzi wakafika na kumtaka bwana Ian aondoke kama alivyoelekezwa.

Kidogo bwana huyo akawa mkaidi kusikia. Walinzi walimshika na kumvuta, akawasukuma na kuwafokea ataenda mwenyewe pasipo bughudhi.

“Mkithubutu kunishika ..!” alifoka Ian akiwaonyeshea kidole walinzi, kisha akatengenezea koti lake la suti na kumtazama Marietta.

“Unajua wapi pa kunipata,” akasema kwa ngita kisha akaenda zake.


**

Marshall alizima kifaa cha kurekodia sauti, alafu akawatazama wenzake, Danielle na Jack Pyong, kwa tabasamu.

“Umesikia?” akauliza. Wenzake wakashusha kwanza pumzi ndefu kabla hawajatia neno. Mambo yalikuwa mazito haswa.

Kumbe mke wa Raisi, bibie Marietta Abbay, alikuwa kwenye mahusiano ya kimapenzi na bwana Ian Livermore, mahusiano hayo yakiwa yameanza kwa muda kipindi hicho bwana huyo akiwa anafanya kazi kama mlinzi wa Raisi!

“Lakini kwanini aliamua kufanya hivyo?” Danielle akauliza. Basi kwa kuepusha kupoteza muda, Marshall hakucheza tena sauti bali akawahadithia wenzake mkanda mzima.

Mkanda huo ni kama ifuatavyo.

Hapo kabla ya mumewe kuwa Raisi, Marietta alikuwa akiishi na familia yake vema. Mapenzi yalikuwa mengi sana na wakiwa wenye ndoto kubwa kwa hapo mbeleni.

Mume alikuwa ni seneta wa Florida kwa kupitia chama cha Democratic. Alikuwa ni mtu anayekubalika sana na watu na mwenye ushawishi mkubwa kwa wananchi wa ndani ya Florida na hata chamani.

Kwa muda wote huo bibie Marietta Abbay alikuwa pembeni ya mume wake akimuunga mkono, lakini pasi na kujua kumbe mwanaume huyo alikuwa na mahusiano ya siri na mwanamke mwingine.

Tena mcheza filamu za ngono!

Swala hilo likamuumiza sana Marietta. Akawa akilia akijifungia ndani na tangu hapo akawa haonekani akizunguka na mumewe kama ilivyokuwa hapo nyuma. Alijihisi mpweke na aliyesalitiwa.

Anaamini ni kwasababu hakuwa na uwezo wa kubeba mimba labda ndiyo maana mumewe akatafuta njia ya pembeni, lakini ni wapi wataweka nyuso zao ikibainika mtu mkubwa kama huyo amechepuka na mcheza filamu za ngono? Na kama haitoshi akambebesha na mimba?

Hasira zake zikamtuma kumchukia mumewe lakini pia mwanamke aliyezaa naye. Basi kwa kuapa akasema kwamba kwa mkono wake atamwangusha mwanaume huyo kama vile alivyofanya jitihada za kumnyanyua.

Pia atamsaka kwa namna yoyote mwanamke aliyezaa na mumewe na kumteketezea mbali.


****

*SEHEMU YA 04*

Baada ya mume kutambua dhamira ya mkewe, akafanya namna kumsafirisha ‘bibi wake mdogo’ pamoja na mwanaye kwenda Ulaya kwa usalama. Huko kwa siri akawalipia makazi na akawa anawatumia pesa za kujikimu.

Hivyo tokea alipokuwa Raisi akawa anatunza siri hiyo na akihangaika kwa gharama yoyote ile, isije ikavuja kuchafua jina lake na hata jina la taifa kubwa la Marekani!

Wakati huo mkewe akiwa anaishi kwa uchungu na sonona, ndipo akaanza kuingia kwenye mikono ya bwana Ian. Kwa mwanzoni si kwamba alikuwa anampenda bwana huyo bali kwasababu mbili kubwa: mosi, kulipiza kisasi kwa mumewe, pili, kukaa karibu na bwana huyo kutamfanya afahamu mambo ambayo mumewe anamficha.

Taratibu wakaanzisha mahusiano yao kwa siri, na ndani ya muda mfupi Marietta akapata kujua wapi alipo bibi mdogo wa Raisi pamoja na mwanaye. Ni huko jijini Brussels, Ubelgiji.

Baada ya kusema hayo, Marshall akaweka kituo. Wenzake wote walikuwa wanamtazama kwa hamu kweli, habari hiyo ilikuwa imewashika masikio na kupanua vinywa vyao.

Ilikuwa ni habari nyeti. Habari adimu.

“Kwahiyo alipojua, ikawaje?” akauliza Danielle. Alikuwa amepaliwa na hamu ya kujua.

Basi Marshall akaendelea kuwa baada ya Marietta kutambua habari hizo akaanza kupanga mkakati wa kummaliza Britney, mwanamke aliyezaa na mumewe, pamoja pia na mtoto wake!

Afanye vivyo sababu ya kupoza kifua chake dhidi ya chuki na uchungu alokuwanao lakini kabla hajaanza utekelezaji, bwana Ian akamtaka awe mtulivu kwani ana mpango kabambe kabisa.

Wakati huo mapenzi baina yao yalikuwa yamekolea haswa. Marietta alishakuwa kipofu kwa Ian kwani mwanaume huyo aliziba kabisa pengo la mumewe na kumpa faraja hivyo hakuona kama kuna haja ya kumpinga mpenzi wake.

Basi siku zilivyosonga ndipo bwana Ian akaja kumpa mpango mkubwa kwamba wasifanye vitu kwa hasira bali kwa faida. Japo mpango huo hakuwa anauelewa vema ila ulikuwa umejikita kwenye kutumia familia ya siri ya Raisi kumtumikisha mwanaume huyo kufanya jambo kubwa litakalowapa pesa kubwa sana.

Wakishapata pesa hiyo wataondoka na kwenda kuishi maisha kwenye ulimwengu mwingine wakila raha mpaka kufa kwao.

Marshall akakomea hapo.

“Sasa ni mpango gani huo?” Jack akauliza.

“Sijaujua bado. Taarifa zaidi atakuwa nazo bwana Ian, yeye ndo alikuwa anausuka mpango huo. Kwa nilivyoona, Marietta hakuwa anaelewa kwa undani kuuhusu ingawa alikuwa ameketi kungoja faida ya mpango huo.”

Kukawa kimya kidogo wakitafakari, kidogo Danielle akauliza, “Familia ya Raisi ilikuwa Ujerumani si ndio?”

“Ndio,” akajibu Marshall.

“Kwahiyo kama ni hivyo, itakuwa walikamatwa huko Ubelgiji, walipokuwapo mwanzoni, na kupelekwa Ujerumani!”

“Inawezekana,” Marshall akaunga mkono hoja.

“Kwanini walipelekwa Ujerumani?” Danielle akauliza lakini kabla ya yeyote kutoa hoja, akaendeleza soga,

“Unajua Raisi alipotea muda mfupi kabla ya kikao kikubwa cha kiuchumi duniani kufanyika Ujerumani. Pasipo shaka, kupotea kwa Raisi, kupelekwa kwa familia yake ya siri Ujerumani, na kile kikao kikubwa cha kiuchumi, vitakuwa na mahusiano!”

Danielle akawa ameng’amua fumbo moja kubwa sana. Marshall akamuunga mkono na kuwataka wafanyie utafiti zaidi kuhusu mkutano ule. Wakina nani walikuwa wahusika na ulikuwa unahusu nini.

Kuhusu mambo hayo ya kupembua rekodi, bwana Jack Pyong akaingia kazini kufukua kadiri anavyoweza ingali Marshall na Miss Danielle wakiwa wanapangilia zile taarifa ambazo bwana Marshall alikuwa amezipata toka kwa Marietta Abbay.

Walizitunza taarifa hizo kwenye maandishi na pia wakiambatanisha sauti na baadhi ya picha. Kazi hizo zikadumu kwa masaa, mpaka inawasili saa nane usiku ndipo kila kitu kikawa sawia, wakapumzika.

Kwakuwa muda ulikuwa umeenda sana, Danielle akaona ni vema akalala kwenye ile nyumba mbali na jiji. Alilala kwenye chumba chake binafsi ingali Jack Pyong na Marshall wakishea chumba kimoja.

Wakiwa wamelala, kuna muda Jack Pyong akajikuta akiamka. Alipofumbua macho yake kuangaza akaona mwanga ni mkali chumbani, hawakuwa wamezima taa.

Alipotazama kando, akamwona Marshall aliyekuwa amejilaza akiwa anatazama picha ya mwanamke. Alitahamaki mwanaume huyo kutokuwa amelala mpaka muda huo. Yalikuwa ni majira ya saa kumi na moja sasa!

Akarusha jicho lake kutazama ile picha aliyokuwa anaitazama Marshall, kisha asijali sana akajilalia.

Alipokuja kuamka jua likiwa limechomoza, akajikuta yu kitandani peke yake. Marshall hakuwepo chumbani wala ndani ya nyumba. Vilevile Danielle!

Alikuwa yu peke yake, mpweke.

“Hawa ni binadamu kweli!” akastaajabu akipiga mihayo. Asijali sana, akajiendea kukoga kisha kupata kifungua kinywa na kurejea mbele ya tarakilishi!


**


Baada ya hodi ya muda mfupi, bwana James Peak aliruhusu mtu anayegonga aingie ndani ya ofisi yake.

Alipotazama mlangoni, akamwona mwanamke Marietta Abbay. Mwanamke huyo alikuwa amevalia suti kama kawaida yake, na shingoni alikuwa amevalia skafu rangi ya manjano ambayo amaefananishia rangi na mkoba na viatu vyake.

Mwanamke huyo alikuwa ana macho mekundu na uso wake ulikuwa wa kichovu, ni kama vile mtu ambaye hajalala usiku wa kuamkia siku hiyo. Ungemtazama kwa umakini ungebaini macho yake yalikuwa yamevimba.

“Karibu sana, madam!” bwana James alimpatia mkono Marietta, mwanamke huyo akajibu kwa tabasamu la uongo kisha akaketi kitini.

Akasema amekuja papo kwa ajili ya kesi ya Marshall.

“Nadhani nimekutana na Marshall jana,” alisema mwanamke huyo akitazama chini. Alikuwa amekabwa kwa mawazo kichwani.

“Ulikutana naye wapi?” Bwana James akauliza. Kidogo Marietta akanyamaza kabla ya kuminya lips zake na kusema kwa sauti ya chini,

“Hotelini. Lakini akiwa na mwonekano tofauti!”

Baada ya hapo Marietta akafunguka ni namna gani alivyokutana na mwanaume huyo na kumwambia wanataka wafanye jambo kwa pamoja kuhusu watoto kabla hajamlewesha na kumpeleka chumbani.

“Sijui alinifanya nini, lakini nahisi sipo salama,” alihitimisha mwanamke huyo kisha akameza mate.

Bwana James akamtazama na kumuuliza, “Kwanini unajihisi haupo salama? Kwanini Marshall alikutafuta? Mlishawahi kuwa na mahusiano naye yoyote hapo kabla?”

Kabla ya kujibu, Marietta akamtazama bwana James machoni kwa kama sekunde tatu, kisha akaangusha macho yake chini na kusema kwa sauti ya kunyong’onyea,

“Sijawahi kumjua hapo kabla.”

“Sasa ulijuaje kama ni Marshall?” bwana James akauliza. Kidogo Marietta akabanwa na kigugumizi.


**
 
*NYUMA YAKO (MSIMU WA TATU) -- 05 & 06*

*Simulizi za series*


*ILIPOISHIA*

Bwana James akamtazama na kumuuliza, “Kwanini unajihisi haupo salama? Kwanini Marshall alikutafuta? Mlishawahi kuwa na mahusiano naye yoyote hapo kabla?”

Kabla ya kujibu, Marietta akamtazama bwana James machoni kwa kama sekunde tatu, kisha akaangusha macho yake chini na kusema kwa sauti ya kunyong’onyea,

“Sijawahi kumjua hapo kabla.”

“Sasa ulijuaje kama ni Marshall?” bwana James akauliza. Kidogo Marietta akabanwa na kigugumizi.

*ENDELEA*

Baada ya kujiumauma, Marietta akaeleza kwamba amedhania vivyo maana hana adui, mtu pekee ambaye angelenga kumtafuta na labda kummaliza ni bwana Marshall, kwani ndiye ambaye alikuwa anahusika na kumtafuta mumewe.

Basi bwana James akaandika maelezo hayo pembeni akiwa anamsikiza vema mwanamke huyo. Alipomaliza kufanya naye mahojiano akampatia namba ya simu mwanamke huyo kwa ajili ya maongezi zaidi hapo mbeleni.

Bibie Marietta akajikusanya na kwenda zake.

Alijiweka kwenye gari na kutimka, kama kawaida alikuwa akiongozana na walinzi wake wawili watiifu. Lakini pasi na kujua, kulikuwa na mwanaume mmoja aliyekuwa ndani ya gari akimtazama mwanamke huyo akiyoyoma.

Mwanaume huyo alikuwapo hapo tangu Marietta alipoingia ndani mpaka kutoka kwake.

Alipoona Marietta ameenda zake, naye basi akahepa akielekea uelekeo mwingine.


**

“Una uhakika?” aliuliza Ian. Mwanaume huyo alikuwa ameketi kwenye ‘kiti chake cha enzi’, ndani ya suti rangi nyeupe, shati jeusi na tai nyekundu. Mkononi alikuwa amebebelea sigara kubwa inayomwaga moshi, mdomo wake ulikuwa mkavu na vuguvugu kwa moto wa sigara.

Mbele yake alikuwa amesimama mwanaume yule ambaye alikuwa anamfuatilia bibie Marietta. Mwanaume huyo alikuwa amevalia koti la ngozi rangi nyeusi, mkononi alikuwa amebebelea funguo wa gari.

“Ndiyo nina uhakika, mkuu, nimemwona kwa macho yangu kabisa!” alisema huyo mwanaume kisha akaenda zake akimwacha bwana Ian anafikiri.

Kwanini Marietta ameenda kwa inspekta? Anataka kumwaga mchele ama? Anafahamu fika kuwa jambo hili la Marshall alitakiwi kufika polisi. Amefuata nini huko?

Alijiuliza maswali yasiyo na ukomo.

Alijiona yu hatarini na huenda Marietta akamgeuka hapa, basi kwanza akaamua kumpigia simu bwana Willy na kumtaka mwanaume huyo afike ofisini mara moja!

“Nipo mbali, mkuu,” akasema bwana Willy simuni.

“Willy!” bwana Ian akaita kwa kufoka kisha akabamiza meza. “Uwe mbali ama karibu, nakuhitaji hapa ofisini mara moja!” aliposema hivyo akakata simu yake na kuibamizia mezani.

Kisha akavuta pafu kama nane za sigara. Alikuwa yu moto haswa.

Kichwa kilikuwa kinamgonga, mkono aliobebelea sigara ukiwa unatetemeka.

Alinyanyua simu kumpigia Marietta lakini mwanamke huyo hakupokea. Alijaribu tena na tena lakini bado. Akaamua kumwandikia ujumbe.

Lakini kila alipouandika ujumbe, akaufuta kwa kuuona haufai. Alifanya hivyo takribani mara tatu mwishowe akaamua kuachana na zoezi hilo.

Akabaki kuvuta sigara tu kama mwehu.


**

“Kwahiyo nifanye nini, mkuu?” lilikuwa swali la kwanza baada ya bwana Ian kumweleza bwana Willy kilichotokea. Bwana huyo alitumia masaa matano mpaka kuja kukutana na Ian.

Wakati huo Ian alikuwa amekwishamaliza kama pakti tatu za sigara!

“Unaniuliza ufanye nini?” Ian akafoka. “Ina maana hujui cha kufanya?”

“Hapana mkuu!” bwana Willy akatanabaisha, “ni kwamba nilitarajia huenda ukawa na mawazo. Ila usijali, nitajua cha kufanya,” bwana Willy alivyosema vivyo akanyanyuka kumuaga bwana Ian.

“Willy!” Bwana Ian akaita na kusema, “Naomba kazi hiyo iwe nadhifu!”

Kazi nadhifu ni ile inayofanyika pasipo kuacha alama yoyote nyuma ya kutilia mashaka.

Bwana Willy akaitikia na kisha akaenda zake.

Alijipakia kwenye gari lake matata alafu akatimka upesi akielekea kwake. Alikuwa anafikiria kichwani juu ya mwenendo wake ujao na baada ya muda akaafiki kuwa anahitaji kwenda kuonana na bwana James.

Si kazini, hapana, bali kwake kwa wakati huo wa usiku.

Kwa mara ya kwanza alidhani itakuwa vema kama akienda kuonana na Marietta lakini baada ya kufikiria akakubaliana na kichwa chake kwamba mwanamke huyo hatoridhia kile ambacho ameenda kukisema, hivyo acha aanzie kwa bwana James.

Huyo akikubali ama akikataa, ni lazima afe! Ni wazi amekuwa mkaidi asiyesikia la wakuu.

Basi akafika nyumbani na kuoga vema kisha akaandaa nguo zake na vifaa vyake vya kazi. Nguo nyeusi, buti na barakoa. Bunduki na visu viwili vikubwa kwenye nyonga na nyuma ya mguu unaofunikwa na suruali.

Pia akabebelea na ‘spray’ ya kemikali kwenye begi lake dogo aliloliweka mgongoni.

Alipoona kila kitu kipo sawa, akajipaki kwenye gari lake na kuanza safari ya kuelekea kwenye makazi ya bwana James. Safari yake ikamchukua kama masaa mawili hivi.

Alipofika, asiwe na haraka, akajiweka kando akisoma kwanza mazingira. Alizima taa za gari na hata gari lenyewe kisha akakaa hapo kwa kama nusu saa hivi kabla hajawasha tena gari na kuliacha ‘stand by’.

Taratibu akasonga kuelekea nyuma ya nyumba ya bwana James, kwenye mlango wa nyuma akakomea hapo na kuzamisha mkono wake ndani ya begi.

Humo akatoa pini ndogo yenye kung’aa kama dhahabu, akaikunja pini hiyo kwa mikono yake iliyofunikwa na glovu alafu akaizamisha kwenye kitasa na kukorokochoa, punde mlango ukafunguka!

Kwa taratibu akausukuma na wenyewe haukutoa kelele hata kidogo. Alipoona kila kitu ni shwari, akazama ndani akitanguliza mguu wake wa kuume.

**

“Amekwishaingia!” sauti ilinong’ona.

Alikuwa ni Harold akiwa amesimama mbali kidogo na nyumba ya bwana James. Mwanaume huyo akiwa amesimama hapo alikuwa amebebelea hadubini ambayo aliitumia kumtazamia bwana Willy akizama ndani.

Pembeni ya Harold alikuwa amesimama bwana Gerrard, yeye mkononi alikuwa amebebelea bunduki ndogo na pia macho yake yakiwa yanatazama makazi ya bwana James Peak, mkuu wao.

Mabwana hawa wawili, katika namna ya kutoonekana, walimfuatilia bwana Willy tangu akitoka kwenye nyumba yake.

William hakuwa anafahamu hilo. Hakuwa anafahamu kama mabwana hawa walikuwa wameweka kambi kwenye makazi yake wala kama tayari ameshaundiwa kamati maalumu kwa ajili ya kumfuatilia kwa ukaribu.

Wakati wa majira ya mchana, baada ya bwana James Peak kuongea na Marietta, aliweka madhanio kuwa huenda bwana yule anayewafuatilia atafuata kujua taarifa hiyo kutoka kwa yeyote kati yao.

Hivyo wakachukua hatua.

Wakati Willy anazima gari kukagua eneo, wakina Harold nao wakawa wanazima gari wakiwa umbali wa kutosha dhidi yake katika eneo la maficho.

Wakati bwana Willy akishuka kwenda ndani ya jengo, Harold na Gerrard nao wakashuka kumtazama mwanaume huyo anafanya nini.

Na kwa wakati wote huo wakiwa wanawasiliana na James.

James ambaye yeye ndiyo yupo ndani ya jengo.

“Kuweni tayari muda wowote!” sauti ya James ilisikika kwenye kifaa cha sauti kisha kukawa kimya.

Harold na Gerrard wakawa wamesimama tenge kungoja agizo.


**

Basi bwana Willy, akiwa hana hili wala lile, akazidi kusonga ndani ya nyumba ya bwana James. Mkono wake wa kuume ulikuwa umebebelea bunduki, macho yamemtoka kukodoa na masikio yake yamesimama kuskiza.

Alikuwa jikoni. Jiko lilikuwa kubwa na la kuvutia lakini lisilo na matumizi kwa mwenyeji tangu atengane na familia yake. Alipomaliza kukatiza jikoni, akashika korido inayoelekea sebuleni na chumbani.

Hapo akasita kwanza kusikiza kama yu salama. Alipoona kimya, akapiga moyo konde na kusonga zaidi.


*SEHEMU YA 06*
Alisonga kushika korido ya kuelekea chumbani baada ya kuona sebule ni tupu. Alipopiga hatua kadhaa akawa amefikia chumba cha kwanza kati ya vinne.

Akajaribu kufungua chumba hicho kikafunguka. Kwa taratibu akausogeza mlango na kutazama ndani, kulikuwa kutupu, basi kaachana na chumba hicho na kusonga mbele zaidi.

Akakifikia chumba cha pili, lakini kabla hajakifungua, akasikia mlio wa mlango nyuma yake, akash’tuka! Upesi akatazama huko na kuona mlango wa chumba alichokipita ukiwa unachezacheza.

Akaurudia mlango huo na kuufunga taratibu kisha akaendelea na mlango wa mbele. Akaufungua taratibu na kutazama, hamna kitu! Chumba kilikuwa kitupu.

Mpaka hapo akawa ameshamaliza nusu ya vyumba, kumalizia vyote akageukia upande mwingine uliokuwa na milango miwili.

Akaufungua mlango wa kwanza na kutupa macho yake. Hakuona kitu. Lakini kabla hajatoa kichwa humo, akabaini juu ya kitanda kulikuwa na nguo, hiyo ilikuwa ni ishara ya mtu kuwapo humo!

Japo chumba hicho hakuwa anakitambua kama ni cha James, kumbuka alishawahi kuja hapo awali, lakini akavutiwa kuingia atazame zaidi.

Bwana huyu atakuwa wapi? Alijiuliza akisonga. Mbona kwenye chumba chake hayupo? Ina maana hajalala leo kwake? Aliendelea kujiuliza akiwa anasonga zaidi na zaidi.

Alipofikia kitanda akachukua nguo moja hapo na kuipeleka puani kunusa. Ilikuwa ni nguo iliyotoka kutumika muda si mrefu, pua yake ilitambua. Lakini kabla hajafanya kitu, akahisi kishindo cha mtu nyuma yake.

Alipogeuka akamwona mtu akimjia! Upesi akanyoosha mkono wake wenye bunduki lakini usimsaidie kitu, mkono ukapigwa akadondosha silaha chini na kubaki mikono mitupu!

“Nilikuwa natarajia ujio wako, Willy,” akasema mwanaume ambaye aliposonga kidogo mbele ukaonekana vema uso wa bwana James. Alikuwa amevalia sweta jeusi linalobana mwili pamoja na suruali nyepesi mithili ya ‘traki’, rangi nyeusi pia.

Basi Willy pasipo kutia neno, akajiweka sawa kwa jili ya pambano, naye bwana James akatanua miguu na kukunja ngumi, tayari kwa ajili ya kumpokea mgeni wake katika namna ya pili.

Pambano likazuka!

Bwana Willy alirusha ngumi nyepesi na za haraka. Alikuwa mwepesi sana lakini mashambulizi yake hayakuwa na madhara. Mara kwa mara bwana James alitabiri mwenendo wake na hivyo basi ikawa rahisi kumkabili adui yake.

Jambo ambalo bwana James hakuwa analifahamu ni kwamba, William alikuwa ana silaha zingine kwenye mwili wake, nazo ni visu. Na mwanaume huyo alikuwa mzuri zaidi kwenye matumizi ya silaha kuliko kombati ya kawaida.

Basi wakiwa wanaendelea kupimana ubavu, bwana Willy akanyumbulika kurusha teke sanifu. Ni kwa haraka sana, alimgeuzia mgongo bwana James na kisha akapaa kidogo kwa kama urefu wa futi tano toka ardhini alafu akajigeuza akiwa ametanua miguu yake.

Aliutanguliza ule wa kulia kwanguvu ukifuatiwa na wa kushoto!

James akafanya jitihada za kujikinga na shambulizi hilo, lakini pasipo kujua kuwa ingali Willy akiwa hewani alichomoa kisu toka kwenye mguu wake na sasa amekiweka mkononi.

Basi akiwa anajikinga na shambulio jingine, akatahamaki mkono wake umechanwa na unavuja damu.

“Ni bora ukatulia ukafa kifo cha taratibu, James,” akasema Willy na kuongezea, “Leo ni siku yako ya kufa!”

Kurupu akamfuata James, akarusha kisu, James akakwepa, alipotaka kurudisha mkono wake nyuma, usifike popote, James akauvutia na kuubana kwapani kwanguvu, alafu akauminya kuutengua.

Willy akapaza sauti kuu ya maumivu!

Akajaribu kuuokoa mkono wake kwa kuutuma mwingine lakini James akawa upesi zaidi kwa kuukita mkono huo ngumi nzito alafu akamshindilia Willy ngumi tatu za maana mbavuni na kumwachia huru.

Willy akashika mbavu zake akiugulia. Alikuwa anahisi maumivu makali sana. Alihisi pengine moja ama zaidi ya mbavu zake zitakuwa zimevunjwa. Alitema damu ikaishia kwenye barakoa.

Basi baada ya hapo akawa mdhaifu sana kupambana na James tena. Hata alipochomoa kisu kingine hakufua dafu kwani alikuwa anahisi maumivu makali mbavuni, hakuwa anaweza kutuma ngumi kwa ufasaha wala teke.

Kitu pekee anachokumbuka kabla ya kupoteza fahamu ilikuwa ni kumwona James akiwa hewani baada ya kumsulubu kwa teke la kianzio. Hilo teke lingine lililokuja baada ya hapo, hata hakujua maumivu yake kwani lilimziraisha mara moja!

**

“Sogeeni!” sauti ilisema kwenye chombo cha mawasiliano, bwana Harold akamtazama mwenziwe, Gerrard, na kumpatia ishara ya kichwa, wakajongea ndani ya nyumba ya James.

Walimkuta bwana huyo akiwa ameketi sebuleni anafunga jeraha lake kwa bandeji.

Harold akauliza,

“Yupo wapi?”

“Chumbani,” bwana James akajibu akiendelea na zoezi lake, Harold na Gerrard wakaenda chumbani kumwona bwana Willy ambaye alikuwa hajitambui.

Baada ya muda mfupi polisi wakafika eneo la tukio na bwana Willy akabebwa.

**

Asubuhi palipokucha tu, bwana Ian alipata taaria juu ya Willy. Aliyemfikishia taarifa hizo alikuwa ni moja ya mashushu wake waliokuwapo ndani ya polisi.

Habari hizo zikamvuruga sana bwana Ian na kumkosesha raha. Alivuta sigara kama hana akili nzuri lakini hakupata ahueni. Alihofia huenda Willy anaweza akamwaga mchele panapo banda la kuku!

Habari hazikuwa kificho tena. Kwenye majira ya mchana zilizidi kupamba moto na kushika karibia kila chombo cha habari Marekani, Ajenti wa FBI avamia nyumba ya inspekta na kutiwa nguvuni!

Ulikuwa mjadala mkubwa na mzito.

Mkuu wa FBI alijitokeza hadharani na kukana madai ya shirika lao kuhusishwa na tukio hilo akisema kuwa ameshangazwa na wao pia watalichukulia hatua.

Zaidi ya hapo kila mtu akawa anaumba tukio lake kichwani na kujipatia sababu. Nyingi zikiwa ni sababu zisizo na mantiki ama zikiwa zimeenda kombo!

“Unafikiria nini kuhusu hili?” Marshall alimuuliza Miss Danielle. Watu hawa wawili walikuwa kwenye gari wenyewe, Marshall akiendesha.

“Walitaka kumuua James,” Danielle akajibu akitazama nje ya dirisha. Kiuhalisia mwanamke huyu alikuwa ana uwezo mkubwa sana wa kuchanganua mambo. Kasi ya akili yake ilikuwa inatisha.

Jambo gumu angeweza kulifanya likawa jepesi kabisa kwa kulivunjavunja vipandevipande.

“Kwanini unadhani hivyo?”

“Ian hawezi akawa mwenyewe, ana timu yake udhalimu, bila shaka katika timu hiyo kuna huyo aliyekamatwa.”

“Sawa, kwanini unadhani wanataka kumuua James?”

“Wao na James wanashea kitu kimoja, wote wanakutafuta wewe. Ni swala la conflict of interest. Pengine James amepata kitu kuhusu wewe hivyo wanakitaka, ama wanataka swala hili la kukutafuta liwe binafsi kwenye mhimili mmoja ulio karibu nao, na si mwingine bali FBI.”

“Kwahiyo vipi kuhusu Marietta? Unadhani atakuwa kwenye hatari pia?”

“Bila shaka, kama tu watakuwa wamejua kuwa ulikutana naye.”

“Ni lazima watakuwa wanajua hilo!”

Basi Danielle akamtazama Marshall na kumwambia, “Kama ni hivyo, tutarajie Marietta kuuawa ama kupotea muda si mrefu.”


**

**
 
*NYUMA YAKO (MSIMU WA TATU) -- 07 & 08*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Wao na James wanashea kitu kimoja, wote wanakutafuta wewe. Ni swala la conflict of interest. Pengine James amepata kitu kuhusu wewe hivyo wanakitaka, ama wanataka swala hili la kukutafuta liwe binafsi kwenye mhimili mmoja ulio karibu nao, na si mwingine bali FBI.”

“Kwahiyo vipi kuhusu Marietta? Unadhani atakuwa kwenye hatari pia?”

“Bila shaka, kama tu watakuwa wamejua kuwa ulikutana naye.”

“Ni lazima watakuwa wanajua hilo!”

Basi Danielle akamtazama Marshall na kumwambia, “Kama ni hivyo, tutarajie Marietta kuuawa ama kupotea muda si mrefu.”

ENDELEA

Wakafika kwenye makazi yao mbali na jiji, huko wakapumzika wakiwa wamkutana na Jack alafu baada ya muda kidogo wakajumuika kwa pamoja kupata chakula cha usiku.

Wakiwa hapo wakawa wanajadili mambo kadhaa. Mambo ambayo yametokea na ambayo yanafuatia.

Lakini katika hayo swala la bwana Willy lilishika sana hatamu.

“Unadhani bwana James atakuwa anafahamu kuwa jamaa huyo aliyekamatwa anahusika na bwana Ian?” akauliza Jack Pyong akitafuna.

“Hataweza kujua,” akajibu Marshall baada ya kumeza. “Pengine kama atatumia njia mbadala ya kumlazimisha mwanaume huyo aongee kila kitu. Kitu ambacho ni ngumu sana kutokea!”

Kukawa kimya kidogo wakitafuna. Baada ya vijiko viwili vitatu, Jack akasema,

“Napata mawazo sana juu ya hili. Leo nimepekuwa magazeti kila moja na habari yake. Nimejiuliza, kama huyu bwana amekamatwa akiwa amejikamilisha kisilaha, yupo kwenye nyumba ya inspekta, vipi kuhusu maajenti wengine? Hamna ambao wapo pamoja naye pale shirikani?”

Akiwa anasema hayo alimtazama Danielle. Mwanamke huyo akangoja kwanza ameze nipi ajibu. Ni Jack Pyong peke yake ndiyo alikuwa anaweza kuongea na chakula mdomoni.

“Jack,” Danielle akaita na kugusia, “shirika ni kitu kikubwa chenye watu wengi. Ndani yake haiwezekani wote wakawa wema, kuna ambao ni mahasidi na kuna ambao wanalipigania taifa lao.”

Basi baada ya hapo kukawa kimya zaidi watu wakila na kunywa. Baada ya kumaliza wakaendelea na mjadala wao.

“Natazamia kama nitapata nafasi ya kuonana na rafiki yangu,” alisema Danielle na kuongeza, “pengine yeye atakuwa ananieleza ni nini kinaendelea kule shirikani.”

“Itakuwa vema,”Marshall akaunga mkono, “Nadhani kutakuwa na mtandao fulani kwenye shirika na FBI unaoongozwa na wadhalimu. Endapo tukibahatika kumpata mtu hata mmoja, basi atatusaidia sana kwenye upelelezi wetu.”

“Kabisa,” Danielle akaafiki. “Lakini pia wakati Jack anaongea kuhusu magazeti, nimejikuta napata wazo.”

“Lipi hilo?” Jack akawahi kuuliza.

“Mnaonaje kama tukaanzisha chombo cha habari?” Danielle akapendekeza.

“Danielle, huoni ni gharama sana? Tutawezaje kuendesha chombo hicho ikiwa kinahitaji pesa sana kwenye uwekezaji?” Jack akawahi kupinga hoja.

Lakini Marshall yeye alitulia. Alijua kuna kitu kichwani mwa Danielle hivyo akampa muda zaidi mwanamke huyo aongee.

“Si kama unavyowaza, Jack,” akasema Danielle. “Ni gazeti tu! Na gazeti hilo litakuwa limesajiliwa na ‘farm’ yetu ya upelelezi. Litakuwa linatoa habari kwa kina na matazamio ya mambo mbalimbali kisiasa, kijamii na hata kiuchumi.

Mitazamio ambayo itakuwa yakinifu na ya kiundani sana. Napata kuamini gazeti hilo litakuwa kubwa sana kutokana na habari zake, na hivyo basi litakuwa na wateja wengi, haswa kwenye kipindi kilichogubikwa na matukio kama hiki.

Au mnasemaje?”

Danielle akauliza akimtazama Marshall.

“Ni wazo jema!” Jack akapaza sauti. “Naunga mkono hoja!”

“Na vipi kuhusu wewe Marshall?” Danielle akauliza. “Wewe unalionaje hili?”

Marshall akakuna kidevu akifikiri, kidogo naye akaunga mkono hoja na kuongezea habari, “itapendeza kama mhariri na waandishi wa hilo gazeti wakawa watu wasiofahamika kwa ajili ya ishu za usalama.

Waandishi hao hawatakiwi kujulikana na jamii wala na vyombo vya usalama. Hilo pia litawafanya wafanye kazi kwa uhuru pasipo kuhofia.”

“Ni wazo jema!” Danielle akasema akiliza vidole vyake. “Kama ni hivyo basi, hamna haja ya kusema gazeti hilo linamilikiwa na ‘farm’ yetu ya upelelezi. Mnaonaje?”

“Ni wazo jema,” Marshall na Jack wakaunga mkono, lakini wakakubaliana kwamba jambo hilo litafuata baada ya kumaliza kwanza kusajili taasisi yao ya kipelelezi.

Muda ulikuwa umebakia mchache kukamilisha hilo na kila jambo lilikuwa limeshawasilishwa kwenye mamlaka husika.

Basi mjadala huo ukafungwa na sasa wajamaa hawa wakawa wamemwazima masikio bwana Jack ambaye alikuwa anaeleza yale ambayo ameyang’amua toka kwenye msako wake mitandaoni.

Haswa kwenye lile swala la mkutano wa kimataifa uliokuwa unafanyika kule Ujerumani. Mkutano ambao ulifanyika muda mfupi baada ya Raisi wa Marekani kupotea.

Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali, bwana Jack alipata kubaini kuwa jambo kubwa lililokuwa linangojewa kwenye mkutano huo kama ajenda kuu ni swala la mabadiliko tabia nchi na kivipi nchi zilizopiga hatua kubwa kimaendeleo zitachukua hatua kuhusu swala hilo.

Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali, Marekani ilikuwa radhi kuunga mkono jitihada za kupunguza idadi ya viwanda na haswa vinu vya nyuklia duniani, lakini si kila taifa lilikuwa linaunga mkono jambo hilo.

Na zaidi, kulikuwa na mjadala mkubwa juu ya soko la mafuta na ushawishi wa nchi zinazozalisha mafuta kwa wingi duniani.

Kwenye sakata hilo, Marekani alikuwa amesimama kidete kupinga mfumuko wa bei ya mafuta duniani na haswa vikwazo ambavyo amewekewa dhidi ya mataifa ambayo yanaongoza kuzalisha mafuta duniani.

Baada ya Jack kueleza hayo, Marshall na Danielle wakaanza kuchanganua taarifa hizo vichwani mwao kubaini wapi ulipotoka mkono uliompoteza Raisi.

Ni aidha kwenye mataifa ambayo hayaungi mkono jitihada za kukabili mabadiliko ya tabia nchi, ama kwenye swala la mafuta.

Japo walighani mawazo mbalimbali wawili hawa walikubaliana kwamba bwana Ian ndiye kipande cha fumbo kinachokosekana.

Huenda bwana huyo akawa na taarifa nyeti kwenye hili yeye kama mmoja watu waliohusika na kupeleka familia ya siri ya Raisi nchini Ujerumani.

Hawakuwa na budi kumtafuta kwa udi na uvumba kumtia mkononi, lakini swala hilo halikuwa jepesi. Bwana huyo amekuwa ni mtu wa kuhamisha makazi na ofisi yake mara kwa mara, kama vile baada ya kila miezi kadhaa.

Hata wafanyakazi wake baadhi hawajui ni wapi haswa alipo bwana huyu. Kitu pekee kinachowafanya waone uwepo wake ni kwa kupitia akunti zao za benki tu. Pesa inakuwa ikiingizwa kila mwisho wa mwezi.

Kwa wale wanaofahamu makazi yake na wapi anapopatikana, walikuwa hawazidi watano.

Yote hayo kwasababu za kiusalama.

Hata Marietta, mpenzi wake, hakuwa hafahamu lolote kuhusu wapi anapopatikana bwana Ian.

Kumpata iliwapasa watulie na kuja na mpango kabambe.

“Vipi, una wazo lolote?” Danielle aliuliza akimtazama Marshall. Baada ya Marshall kufikiri kidogo akasema, “Kuna njia mbili. Moja kwa kupitia Willy na nyingine kwa kupitia Marietta.”

Kisha akamalizia,

“Lakini kote kuna changamoto.”

Danielle akatabasamu na kusema,, “Changamoto ndiyo raha ya mchezo, Marshall.”


**

*SEHEMU YA 08*


Asubuhi ya saa nne …


“Sitasema kitu,” alibwabwaja bwana Willy akimtazama Inspekta James. Bwana huyo alikuwa amefungwa mikono na pingu iliyojishikiza mezani. Miguu yake pia ilikuwa imefungwa minyororo iliyozungushiwa kwenye kiti.

Hakuwa na uhuru.

Uso wake ulikuwa na majeraha, haswa upande wake wa kushoto ambapo ulikuwa na rangi ya zambarau kuonyesha amevilia damu.

Bwana huyo tangu ameketishwa hapo kwa ajili ya mahojiano, amekuwa mkaidi haswa. Hakuna swali hata moja alilojibu, muda mwingine alimtazama tu muulizaji pasipo kufungua kinywa.

“Nakuuliza kwa mara nyingine, kwanini ulikuwa unataka kunimaliza? Na kwanini ulikuwa unataka niachie kesi?”

Bwana Willy akamtazama inspekta kama mdoli. Hakutia neno.

“Ukaidi wako hautakupeleka kokote, ndugu. Na ninakuhakikishia, utasema kila kitu ambacho unakificha,” akasema James akinyanyuka. Bwana Willy akamtazama akimsindikiza na macho alafu akasema akitikisa kichwa,

“Kamwe!”

Inspekta akaachana naye ajiondokee lakini kabla hajaufikia mlango, Willy akamtahadharisha, “kuwa makini, inspekta. Maisha yako yako kwenye mstari.”

Inspekta asijali sana maneno hayo, akaenda zake nje.

Alikutana na Harold na Gerrard akawapa maagizo waende wakapekua kila kitu ambacho kipo huko, na chochote wanachoona kinaweza kuwasaidia kwenye upelelezi wao, basi wakilete mara moja kituoni.

Baada ya Harold na Gerrard kuondoka zao, inspekta akajirusdisha kwenye ofisi yake na kutazama baadhi ya mambo ya kazi. Muda kidogo akanyanyua simu yake na kumpigia Marietta. Alitumia namba ya simu ambayo ipo kwenye kadi ya biashara ya mwanamke huyo.

Simu ikaita mara mbili, ikapokelewa.

“Ni inspekta James Peak hapa,”

“Ndio, inspekta.”

“Habari yako?”

“Njema kabisa. Unaendeleaje?”

“Vizuri, nashukuru. Nimeona kimya nikaona nikutafute hewani. Vipi hauna jambo la kunishirikisha?”

Kukawa kimya.

“Madam Marietta …?”

“Ndio, inspekta.”

“Una chochote cha kunishirikisha?”

“Aahm, hapana, inspekta. Namba yako ninayo, nitakapopata jambo, usihofu nitakutafuta kama nilivyofanya awali.”

“Kweli?”

“Ndio, usijali.”

“Samahani, kama hutojali. Tangu ulipotoka hapa kituoni, haujakutana na kitisho ama maneno yoyote?”

Kukawa kimya kidogo.

“Madam Marietta,” inspekta akaita.

Mara tiiiiiiiii! Simu ikakata.

Inspekta akajaribu kumpigia tena mwanamke huyo pasipo mafanikio. Alikuwa hapatikani!

“Ana shida gani huyu?” inspekta James akajiuliza akiweka simu yake chini. Alitambua kutakuwa na tatizo na haja ndani yake ilimtuma amtafute mwanamke huyo kwa maongezi zaidi.

Kwenye ulimwengu wa kiitelijensia, kila mtu ni mtuhumiwa, hakuna wa kuaminika kwa asilimia zote.

Alifikiria jambo hilo la Marietta kwa muda kidogo kabla hajaachana nalo na kuendelea kupitia rekodi za bwana Willy kwenye shirika lake la kazi, FBI.

Ripoti hizo aliziomba toka huko shirikani na pasipo tatizo, wakampatia.

Likapita lisaa limoja akiwa anazipitia. Hakuwa anaona kama kuna jambo la kumtilisha maanani hivyo kidogo akaanza kuboreka, ila kwakuwa hana budi, akaendelea kupitia.

Kidogo akiwa katika zoezi lake hilo, hodi ikapigwa kwenye ofisi yake na kabla hajaitikia, akaingia afisa mmoja aliyemtazama kwa kukodoa,

“Mkuu, inabidi uone hili!”

Upesi bwana James akanyanyuka na kuongozana na afisa huyo mpaka mahali alipokuwa amehifadhiwa bwana Willy, selo.

Hapo aliporusha macho, akastaajabu kuona bwana huyo akiwa amelala, anavuja damu puani na mdomoni!

“Nini kimetokea?” inspekta akauliza akizama ndani. Mapigo ya moyo ya bwana Willy yalikuwa yanasikika kwa upole mno. Macho yake yalikuwa yanarembua akihema kwa uzito.

Basi upesi bwana huyo akanyanyuliwa na haraka akakimbiziwa kwenye gari la wagonjwa kuwahishwa hospitali. Pamoja naye, wakaongozana maafisa wawili wa polisi.

Bwana James akiwa amepigwa na butwaa, alishika kiuno akitazama gari la wagonjwa likitokomea. Alimtazama afisa yule aliyemletea habari, akamuuliza,

“Ni nini kimetokea?”

Bwana huyo akamwambia anadhani Willy ametiliwa sumu kwenye chai yake.

“Alianza kubadilika muda mfupi baada ya kunywa chai. Sikujua nini kilikuwa kinamtokea, alikuwa anagugumia na kujikunjakunja akishika tumbo. Ndani ya muda mfupi ndiyo nikamwona akiwa anatokwa damu, nikaja kukufuata!”

“Nani aliyempatia chai!” akauliza inspekta akitoa macho.

“Ni mimi, mkuu!” akajibu afisa. Uso wake ulikuwa umejawa na mashaka lakini pia woga. Alitoa macho yake kwa kukodoa na mdomo akiuachama.

Inspekta akamkwida nguo yake na kumsogeza karibu.

“Umetia nini kwenye chai?” akamuuliza akimkazia macho.

“Sijatia kitu mkuu. Kweli nakuapia!” akasema afisa kwa woga mkuu. Alikuwa amekunja ndita jasho likimchuruza.

“Nimetoa chai kantini nikamletea moja kwa moja baada ya kuniambia anahitaji kitu cha kupasha tumbo lake!”

Basi inspekta akaenda mpaka jikoni napo akauliza lakini hakupata majibu. Mpishi na watu wanahudumia walikana kabisa kuhusika na jambo hilo na hata kujaribu chai ile wao wenyewe kuthibitisha kwamba haina tatizo.

Inspekta akabaki akiduwaa.

Aliamua kurudi ofisini na kuketi huko akitafakari. Aliona ni vema akangoja majibu ya daktari kugundua nini haswa tatizo.

Lakini uvumilivu nao ukamshinda, akanyanyuka na kujieka koti lake, moja kwa moja akaelekea hospitalini yeye mwenyewe.

Alichukua kama lisaa kufika kutokana na foleni. Alipowasili na kujitambulisha akapewa habari kwamba bwana Willy amekwishafariki!

Bwana huyo alifariki njiani kabla hajafika hospitalini.

“Amefika hapa akiwa tayari ni mfu kwa kama robo saa!” alisema daktari. Alikuwa ni mwanamama mwenye makamo ya miaka thelathini na kitu hivi, macho yake madogo alikuwa ameyajaladia kwa miwani.

“Ni nini kimemuua?” James akauliza.

“Ni sumu kali ya kemikali!” akasema daktari kisha akajaribu kwa ufupi kumwelezea inspekta juu ya sumu hiyo. Ni mchanganyiko wa kemikali kadhaa ambazo huathiri mfumo wa hewa na wa chakula kwa muda mfupi mno!

“Yampasa mtu mtaalamu kutengeneza kitu kama hicho!” alisema daktari na kuongeza, “miligramu moja tu inatosha kabisa kumaliza uhai wa mtu!”

Inspekta akachoka.

**

“Nimekamilisha kila kitu,” alisema afisa wa polisi akiwa ananong’ona na simu. Afisa huyo alikuwa amejibana mahali na kwa kuzuia sauti isisambae, akawa ameziba mdomo kwa kiganja chake.

Afisa huyo alikuwa ndiye yuleyule ambaye alikuja kumpasha habari inspekta juu ya hali ya bwana Willy baada ya kunywa chai!

“Ndio, tayari amekwishakufa,” alisema bwana huyo na punde akakata simu na kutoka chooni alipokuwapo. Akachomekea vema sare yake na kuendelea na kazi zake.


**

“Mkuu!” sauti ilipaza kwenye simu ya inspekta James. Bwana huyo alikuwa akiongea na mtumishi wake, Harold, ambaye alimpigia akiwa kwenye mazungumzo na daktari.

Kwasababu mazungumzo yao ni faragha, akatoka ndani ya chumba cha daktari apate kuwa huru.

“Vipi Harold?”

“Tumezingirwa!” Harold akabwatuka. “Tumezungukwa nje ya jengo na watu waliobebelea silaha!”

“Serious?”

“Ndio! Wamekuja muda si mrefu. Ni sita kwa idadi!”

“Nakuja! Nakuja!”

Inspekta akaweka simu mfukoni kisha akanza kukimbia kama mwehu akielekea nje ya hospitali.


**
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom