Nyuma yako (Riwaya ya S. Mollel)

*NYUMA YAKO – 18*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Tulipofika pakavu, nikamtazama mtoto na kubaini alikuwa amejigonga kwenye jiwe ingali tu mtoni. Na kwa namna alivyokuwa anatoka damu, inabidi ifanyike namna upesi ya kumsaidia, la sivyo alikuwa anatuacha!
Nikamwambia mama yake, “gandamizia mahali pa jeraha, nakuja!” mimi nikaenda kutafuta majani yatakayoweza kumsaidia jerahani.
ENDELEA
Nilifahamu ndani ya msitu ule sitakosa ninachotaka. Nikakimbia upesi na kufanya jitihada za kuangaza macho yangu nikitumia stadi niliyonayo juu ya madawa ya asili. Tulifunzwa hii. Tulifunzwa namna ya kudumu na kumudu kwenye hali mbalimbali kama hizi.
Ndani ya muda mfupi, nikapata kuona kichaka chenye majani membamba na ncha kana kwamba sindano. Nikajongea hapo na kuchuma majani kadhaa na kuyatia mdomoni kutafuna alafu nikaanza kurudi upesi kule kwa yule mwanamama na mwanaye.
Nilipofika majani mdomoni mwangu yalikuwa tayari yashalainika vya kutosha. Nilikunja sura kwa uchungu wake mithili ya shubiri. Nikayatema na kumpachika yule mtoto eneo lake la jeraha alafu nikachana sehemu ya shati langu kutengeneza bandeji, nikamfungia hapo kichwani na kumweka mtoto huyo begani tuendelee na safari.
Tukiwa tunatembea, nikapata sasa wasaa wa kumuuliza maswali kadhaa. Niliona huu ni muda muhimu wa kufanya hivyo maana lolote linaweza kutokea muda wowote. Basi likitokea, angalau niwe nimetimiza robo ya haja yangu.
“Wewe ni nani? Kwanini watu hawa wamekuteka?” Niliuliza nikimtazama mwanamke huyo ambaye alikuwa akitembea kwa ukakamavu. Alikuwa na ushupavu ndani yake.
Akanitazama na kunyamaza kwanza akipiga hatua. Alipovuta pumzi ndefu ndipo akanijibu pasipo kunitazama, “Nilidhani utakuwa unanijua ndo’ maana ukaja kuntafuta.” Kisha akaniuliza, “Ajenti, umekujaje kumtafuta mtu ambaye humjui?”
“Umejuaje kama mimi ni ajenti?”
Akatabasamu. “Anayeweza kuyafanya yote haya, ni raia wa kawaida?” kabla sijanena akaendelea kunena, “Umefanya kazi kweli kujua wapi nilipo. Hata sasa kuwa hai unastahili pongezi.”
Nikamtazama na pasipo kuongea nikarudisha macho yangu mbele tuendako nikitarajia mwanamke huyo ataendelea kunena.
“Mimi ni raia wa kawaida kabisa. Ni mmarekani ninayeishi Ujerumani pamoja na mwanangu. Sina shida nyingine na mtu!”
“Huku Ujerumani unafanya nini? Na kwanini Ujerumani?”
“Una maswali mengi sana. Sidhani kama nipo kwenye mood ya kukata kiu chako. Pengine baadae nikiwa nimetulia.”
“Wamekufanya lolote ulipokuwa chini yao?”
Akatikisa kichwa. “wasingeweza kunifanya kitu.”
Nikamtazama kwa maulizo pasipo kusema kitu. Nadhani yeye mwenyewe akajiongeza na kunijibu swali langu la kimya. “Bado wananihitaji. Mimi ni asset kwao. Hawawezi kunidhuru.”
“Unamaanisha nini wewe ni asset?”
“Nimekuambia una maswali mengi. Najua. Tutakapotulia nitakuambia, pengine nitakata kiu chako.”
“Hauwezi ukanambia hata machache?”
“Naitwa Britney. Ni raia wa Marekani. Nadhani hayo yanakutosha.”
Sikutaka kusumbuana naye. Niliona ninyamaze kimya, kweli hayupo kwenye mood, japo kifuani mwangu nilikuwa nalaumu sana kutokujua kinachoendelea ingali tulipokuwa kitu chochote kingeweza kujiri.
Tukatembea kwa kama dakika kumi, akantazama kisha asiseme kitu akatazama zake mbele. Nadhani alikuwa anajiuliza maswali kichwani. Baada ya sekunde kadhaa, akasema, “Naomba umtazame mwanangu. Yeye ndo’ kitu pekee nilichonacho kwa sasa.” Kisha akasimama na kun’tazama. Nami nikasimama. Akaniambia, “Niahidi hilo … niahidi mtoto wangu atakuwa salama.”
“Nakuahidi,” nikasema kwa sauti ya kutikisika. Akaniuliza, “Unaniahidi?”
“Ndio, nakuahidi,” saa hii nikasema kwa kujiamini. Basi akaridhika tukaendelea na safari. Akaniambia kama tukitembea kwa takribani robo saa tutakuwa tumefika barabarani.
Tukatembea kwa kama dakika sita, yeye mwenyewe akaanza kuongea. “Nimemkumbuka sana mama yangu,” sauti yake ilikuwa ya mtu anayekaribia kulia.
“Kama ningalifuata alichonambia, nisingalikuwa hapa.”
Nikamtazama nisimsemeshe kitu. Nilihofia maneno yangu yangeweza kumkatiza. Nilimwacha afanye vile alivyokuwa anataka.
Akavuta makamasi mepesi kisha akaendelea, “Sasa nimekuwa mkimbizi nisiye na makazi. Toka kwenye kamera za mwanga mpaka kujificha chini ya uvungu na nyuma ya milango. Ama kweli maisha huweza badilika ndani ya sekunde moja tu!
Ndani ya sekunde moja mtu akawa kilema. Akapoteza alivyovipata kwa masaa. Ndani ya muda huo mchache akawa amebadili mwelekeo wa maisha yake.”
Nikaendelea kumtazama pasipo kutia neno. Niliona uso wake ukiwa umebadilika rangi kuwa mwekundu. Alikifikicha pua yake na kumwaga tena maneno, “Hakuna anayejua kesho yake, sio? … mimi sikudhani kama siku moja ntakuja kuwa na familia. Sikuwa nawaza hilo jambo kabisa, labda kwasababu ya aina ya maisha niliyoyachagua.
Maisha yalonifanya ninyooshewe kidole kila nilipopita nikionekana laana, mchafu na niliyelaaniwa. Sikutaka mwanangu aje kushea laana yangu. Ashindwe kupita mtaani kwasababu ya mama yake. Ni adhabu. Najua ukubwa wa adhabu hiyo maana nimeibeba mgongoni kwa muda mrefu. Inachosha na kuumiza.
Watamani kukaa mbali na walimwengu ambao ni wepesi wa kuhukumu na wachoyo wa fadhila. Lakini ajenti, wawezaa kukaa mbali na dunia?”
Aliniuliza akintazama. Nikamtikisa kichwa kukataa pasipo kutia neno. Basi akatabasamu kwa mbali na kisha akakaa kimya kidogo. Tukatembea kwa kama dakika moja asinene jambo ila nikiamini ataendelea tu kusema.
Nilihisi ana kitu kifuani. Atajihisi mwepesi endapo atakitoa.
Akajifuta machozi na mikono ya sweta lake alafu akatazama juu kwenye matawi ya miti, pembeni na kisha mbele.
“Hata kama niki –”
“Shhh!” nikamzuia upesi nikimwonyeshea ishara ya kidole mdomoni. Kuna kitu nilihisi. Tulisimama tukatulia tuli na kutazama kushoto na kulia. Masikio yangu yalinambia nimesikia sauti ya watu wakiteta. Na sikuwa nimekosea, lah! Nyuma yetu kwa umbali, tukawaona wanaume wawili waliokuwa wamevalia nguo nyeusi na mikononi mwao wana bunduki ndefu!
Wanaume hawa hawakuwa na usafiri, bali wakitumia miguu yao.
Haraka nikamtaka Britney akimbie na mie kabla sijafungua miguu yangu nikafyatua risasi kuwalenga wanaume wale kuwapumbazisha kwa muda kidogo.
Tukakimbia na kukimbia. Nao wale wanaume wakawa wanaendelea kutukimbiza, wakawa pia wanatupa risasi wakijaribu kunilenga.
Nikiwa nimembebelea mtoto, nikakimbia kwa kasi na kwanguvu mpaka kumwacha Britney nyuma. Si kwamba alikuwa anakimbia taratibu, hapana! Na wala hakuonekana mtu anayehitaji msaada. Alikuwa anajimudu kukimbia.
Hatukudumu muda mrefu mbioni, nikasikia risasi ya karibu zaidi na kisha sauti ya kike ikilalama! Kutazama, nikamwona Britney akidondoka chini!
“Shit!” nikamsikia mmoja wale wajamaa wanaotukimbiza akilaani, kisha kwa punde akamlaumu mwenzake kwa kumfyatulia risasi Britney. Hapa nikatumia nafasi hiyo upesi kuwamiminia risasi na kuwalaza chini.
Nikamtazama Britney. Alikuwa amelengwa kwenye shina la nyuma la shingo. Risasi ilivunja uti wake wa mgongo! Ilikuwa ngumu kwake kupona. Damu zilimtiririka. Macho yake yalimwaga machozi akinishika kwanguvu na kung’ata meno yake.
“Ajenti, mtazame vema mwanangu,” akasema akikwamakwama. Kisha akaninong’oneza, “Naitwa Juliette Simpson. Natumai utakuwa unanijua.” Alafu akajifia.
Akafa mbele ya macho yangu. Akafa mwanaye akiwa bado hajitambui.
Nikawaendea wale wanaume niliowaua na kuwapekua. Sikuwakuta na kitu zaidi ya bunduki na risasi kadhaa. Nikazichukua. Nilipomrudia Britney ambaye kabla hajafa alinipa jina lingine, naye nikampekua kama ana kitu. Alikuwa mtupu.
Nikapata maswali juu ya nini cha kufanya. Haraka nikatoa simu yangu na kumchukua picha kadhaa, nashukuru simu yangu haikuwa simu inayoingiza maji.
Nikiwa nimempiga picha mbili tu, nikasikia tena sauti ya watu, hiyo ikawa ishara kuwa sitakiwi kukaa hapo tena. Nikaanza kukimbia. Huko nyuma nikasikia, “Yule!” na vishindo vya watu vikinifuata kwa kasi!
Nikakimbia sana lakini nguvu zangu hazikuwa kama za hapo awali, nilichoka mno. Kumbeba mtu kwa muda wote ule huku nikikimbia na kutembea haikuwa jambo jepesi. Hivyo basi nikaanza kupunguza kasi ya mwendo wangu na kupelekea wale maadui wanikaribie zaidi!
Wakatupa risasi kadhaa. Nashukuru miti ilinikinga. Nilisikia zikipasua na kugotea mitini. Nilipoona maji yanazidi kupiku unga, nazidi kukaribiwa na hali ni mbaya, nikakimbilia mtoni na kujitosea humo!
Nilizama maana kina kilikuwa kirefu. Risasi zikatumwa kunifuata ndani ya maji, zikanipitia kupunyua, lakini kwakuwa maji yalikuwa na nguvu na mengi ya kutosha kunipeleka, yakaniepushia na balaa!
Yakanisomba kunisafirisha.

***
 
*NYUMA YAKO – 19*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Nilizama maana kina kilikuwa kirefu. Risasi zikatumwa kunifuata ndani ya maji, zikanipitia kupunyua, lakini kwakuwa maji yalikuwa na nguvu na mengi ya kutosha kunipeleka, yakaniepushia na balaa!
Yakanisomba kunisafirisha.
ENDELEA
Maji yalipotuama, tukiwa tumesafiri kwa kama robo saa, nikachoropoka toka mtoni kuitafuta barabara.
Haikuwa safari ndefu sana. Sidhani kama nilichukua zaidi ya dakika kumi, nikawa tayari nimefika kwenye lami ambapo niliomba msaada na upesi nikapatiwa. Nadhani ilikuwa ni sababu ya mtoto niliyekuwa nimembeba. Mama mmoja ambaye alikuwa anasafiri na mbwa wake, alisimamisha akiwa ananitazama kwa huruma kisha akaniuliza naelekea wapi kabla hajaniruhusu niingie ndani na kuendelea na safari.
Nikiwa ndani akawa ananidadisi nini kimenitokea, na kwasababu sikutaka kumsababishia taharuki, nikamlaghai kuwa tumepata ajali. Akanipeleka mpaka mjini kabisa na kuniacha hospitalini. Mtoto akatazamwa jeraha na kupatiwa dawa za kumsaidia dhidi ya maumivu na kumkausha jeraha.
Baada ya hapo nikatafuta mahali pa kupumzikia. Nikamlaza mtoto na mimi kufanya utaratibu wa chakula maana njaa nayo ilikuwa inauma. Kila kitu kilipokuwa sawa, nikajilaza kitandani nikiwa nawaza.
Mwanamke yule aliyefia mikononi mwangu, mtoto huyu ambaye yupo pembeni, watu wale waliokuwa wanatufukuza na mahusiano yao na Raisi! Nilihisi mambo yamechangamanaa sana.
Sikudhani kama msako wangu wa Raisi ungenisafirisha ukubwa huo. Nikanyanyua simu na kumpigia Jack Pyong kumweleza yote yaliyojiri. Naye akashangaa sana lakini lile la Britney likamshangaza zaidi. Akanisihi nimtumie picha za mwanamke huyo na kisha jina lake hilo la mwisho ambalo alilisema kabla hajafariki, yaani Juliette Simpson.
Nikafanya hivyo, akaniambia nimpatie muda kidog basi atanirejeshea majibu. Nikaendelea kujilaza kitandani. Kama baada ya dakika tano, mtoto yule akaamka akilalamikia maumivu makali kichwani.
Nikampatia dawa na kumhasa apumzike zaidi. Lakini kabla hajafanya hivyo, akaniuliza mama yake yupo wapi? Hapa nikapata kigugumizi.
“Unaitwa nani?”
“Henessy,” akanijibu akiwa ananitazama kwa kufinya macho.
“Henessy, Mama ametangulia Marekani. Marekani si ndo’ nyumbani?”
Akasita kisha akaniuliza, “Kwanini ameenda mwenyewe?” kisha macho yake yakalowana machozi. “Kwanini ameniacha?’
“Hajakuacha,” nikasema nikimkodolea macho. Nikamfuta machozi na kumpoza, “ilibidi atangulie kwenda huko maana ndege ilijaa. Nasi tutamfuata, usijali.”
Akan’tazama kwa maulizo. Akafuta machozi kwa mgongo wa kiganja chake kisha akaniuliza kwa sauti ya kubashiri, “Tutaenda lini?”
“Usijali, tutaenda. Kuna mambo kadhaa namalizia kama kesho ama keshokutwa. Sawa?” akatikisa kichwa kuafiki lakini kishingo upande. Kidogo simu yangu ikaita, alikuwa ni Jack Pyong, nikapokea akaanza kunambia nini amepata.
“Tony,” akaanza kwa kuniita jina. Sauti yake ilikuwa ya chini na msisitizo. Akanambia, “Huyo mdada ni mwigiza picha za ngono!”
“Yupi?”
“Huyo Juliette! Namaanisha Juliette Simpson!”
“Huyo niliyekutumia picha?”
“Acha basi kuniuliza maswali ya kijinga. Kwani tumetoka kuongelea nini hapa muda si mrefu?”
“Kuna mtu mwenye maujinga kama wewe?”
“Nitaacha kukwambia! Ohoo!”
“Sema basi. Unajua credit inaenda!”
“Sasa nikitaka kusema wewe unaanza mambo yako. Tulia kama unanyolewa.”
“Sawa, nimetulia. Kwahiyo unanambia—” kabla sijamalizia nikamtazama yule mtoto, sikutaka asikie. Nikasonga kando kidogo.
“…kwahiyo Juliette huyo ni pornstar?” Pornstar maanaye mcheza sinema za ngono.
“Ndio. Ni maarufu tu. Sikuwa najua hilo mpaka nilipoingia mtandaoni!”
“Sasa Jack, mcheza sinema za ngono atakuwa ana mahusiano gani na kupotea kwa Raisi?”
“Tony, hiyo ni kazi yako. Unanipachikia mimi sasa?”
“Sasa we fala, huko mtandaoni ulikuwa unafanya nini?”
“Nakutafutia huyo mtu wako. Ebu sikia, kesho kama nikipata muda nitaenda kwenye kampuni aliyokuwa anafanyia kazi. Pengine nitapata baadhi ya majibu. Baadae!”
Akakata simu na kuniachia maswali lukuki kichwani. Niliona mambo yanazidi kuwa magumu. Nikazama mtandaoni na kuandika jina la yule mwanamke, punde nikaona majibu ya ajabu. Kweli mwanamke yule alikuwa mcheza sinema za ngono.
Lakini kwa taarifa zaidi, alikuwa mstaafu! Lakini kwa kazi hii kuna mstaafu kweli ilhali video zake bado zipo hewani na watu wanaweza kuzipakua na kuzitazama?
Nilipofuatilia zaidi nikabaini na hiyo kampuni aliyokuwa akifanyia kazi. Kwa jina, LEXANDER PLEASURE ikiwa inasimamiwa na mwongozaji mwenye asili ya kilatini aitwaye jina la utani, Bomboclat!
Hapa sasa nikapata kujua kwanini mwanamke yule alishangaa nilipomwambia simfahamu. Huenda alidhani umaarufu wake kwenye michezo hiyo ungelinigusa hata mimi. Lakini pia nikafahamu kwanini alinipatia majina mawili, mosi Britney, pili Juliette. Ina maana Britney lilikuwa ni jina lake la uhalisia wakati Juliette Simpson likiwa ni la ‘kazini’.
Nikashusha pumzi ndefu nikimtazama yule mtoto. Nilikuwa nawaza kama atakuwa anajua kuwa mama yake huko mtandaoni yupo uchi. Nikajikuta natikisa kichwa kisha nikaanza kusuka tu mipango ya kurudi Marekani maana sikuwa na cha ziada cha kukifanya tena hapa Ujerumani.
Hivyo nikaona ni stara kufunga safari, kesho asubuhi na mapema, kwenda jiji la Berlin ambapo ndipo kuna ubalozi wa Marekani.
Siku hiyo nipumzike tu kwakweli. Nilikuwa nimechoka mno. Shurba nilizopitia zilikuwa zatosha kunifanya nijilaze.

**

Kesho yake …

Berlin, Ujerumani.

Nilitoka ndani ya balozi nikiwa na uhakika wa safari yangu jioni. Na kwakuwa nilijitambulisha na kuthibitisha humo ndani kuwa mimi ni ajenti wa CIA, basi mambo hayakuniwia sana ‘ugumu’.
Nikaongozana na Henessy mpaka mgahawani kujipatia chakula. Hapo tukakaa kwa muda wa kama nusu saa kabla hatujajiweka kwenye basi na kwenda mpaka beach. Nilitaka angalau nifurahie ujio wangu hapo Ujerumani japo ulikuwa ni wa kikazi.
Walau nipate muda wa ‘kuenjoy’ kabla sijaacha ardhi hiyo kurejea nyumbani. Nikiwa hapo nikapata nafasi ya kuzoezana na Henessy ambapo tulicheza na kufukuzana pamoja tukiwa tunapigwa na pepo ya bahari.
Tukiwa tumechoka, tukawa tunatembeatembea tu fukweni. Lakini kama baada ya hatua zetu kadhaa, paliongokea mwanamke mmoja ambaye amevalia ‘casual’. Uso wake ulikuwa umefichwa na miwani meusi na miguu yake imebanwa na jeans iliyopauka. Begani ananing’iniza mkoba mdogo uliobana kwapa lake.
Mwanamke huyo akiwa anapunga mkono wake na kutabasamu, aliita, “Heneessyy!” tukageuka wote kutazama. Alikuwa anatokea upande ilipo barabara kuu.
Nikamuuliza Henessy, “Unamjua huyo mwanamke?”
Henessy hakunijibu, badala yake akawa anamtazama kwa umakini mwanamke huyo pengine akumbuke kama alishawahi kumwona mahali. Hivyo kabla hajanipa majibu, mwanamke huyo, kwakuwa alikuwa anakimbia na kutembea kwa kasi, akawa ametufikia.
Akan’salimu kwa upesi, akitumia kiingereza, kisha akainama kumtazama Henessy akitabasamu. “Hujambo Henessy? … unaendeleaje muda wote huo?”
Henessy akamjibu lakini bado akiwa anamtazama kwa macho yaliyokaza. Nikamuuliza mwanamke huyo, “Tafadhali unaweza kujitambulisha?”
“Oow!” akasema akivua miwani yake. Macho yake yalikuwa ya paka yakiwa na uchangamfu ndani yake. Akatabasamu na kunipatia mkono, “Naitwa Jolene! Ni rafiki yake na Britney.”
“Oooh! Nimefurahi kukujua,” nikamjibu nisiongezee mengi. Akaniuliza, “na wewe? Wewe ni nani?”
“Naitwa Rodney. Ni rafiki pia wa Britney!”
Akaangaza kushoto na kulia. “Britney yupo wapi?”
“Hayupo. Hatujaja naye hapa!”
“Ooh! Yupo wapi kwa sasa. Ni muda sijawasiliana naye. Hata sasa imenichukua muda sana kumtambua Henessy!”
“Ni simulizi ndefu kidogo,” nikamjibu na kumwomba, “tunaweza tukapata dakika kadhaa za kuongea?”
Akaridhia baada ya kutazama saa yake ya mkononi. Tukasonga kwenda mahali fulani tulivu kwenye eneo hilohilo la ufukweni, hapo tukapata vinywaji laini na kupiga soga nikitaka kufahamu machache juu ya Britney lakini nikiwa nimemlaghai kuwa mimi na Britney ni mtu na mchumba wake. Tumekutana na akanieleza mambo kadhaa, ikiwamo kujihusisha na kucheza sinema za ngono.
Kwa kufanya hivyo nilitarajia kumpa mwanya mwanamke huyo wa kutonificha kitu. Kumtengenezea mazingira ya yeye kuwa huru kunielekza lolote maana hata lile ambalo lingeweza kuwa siri, mimi tayari nalifahamu.
“Umemjua Britney kwa muda gani?”
“Miaka mingi tu. Alikuwa ni rafiki yangu toka High school!”
“Kwahiyo ulikuwa unafahamu juu ya yeye kujihusisha na ile kazi?”
“Yah! Ni rafiki yangu, nitashindwaje kujua hilo?”
“Mlikuja kupotezana naye muda gani?”
“Aaahmm kama mwaka mmoja na nusu hivi uliopita.”
“Kwanini mkapotezana? Hakukuaga kama anakuja Ujerumani?”
“Hakunambia! Nilistaajabu amepotea. Simu yake nayo haikuwa inapatikana.”
“Lakini ulikuwa unajua kuwa ameenda Ujerumani?”
Akabinua mdomo. “Napo nilikuwa sijui.”
“Kwahiyo huku Ujerumani umekuja kufanya nini, Jolene?”
“Kwenye matembezi yangu tu. In fact, kuna ndugu yangu anaishi huku. Nimekuja kumsalimu.”
Akanywa juisi na kisha akaniuliza, “Vipi na wewe? Ni Mmarekani, sio?”
“Ndio.”
“Kwahiyo ndiyo uko na Britney huku?”
“Ndio. Nipo naye.”
“Unatokea wapi Marekani na unajihusisha na nini?”
“Mimi ni mwalimu High school! Natokea California.”
“Ulikutanaje na Britney? Hakuwahi kunambia kuhusu wewe.”
Nikatabasamu. “Nadhani kwasababu ulipotezana naye.”
Akapandisha mabega. “Labda!” kisha akaniuliza, “So mtakuwa huku kwa muda gani?”
“Si muda mrefu sana, tutarudi Marekani.”
“Ooh! Basi si mbaya kesho mkaja nyumbani kwetu. Kuna tafrija ya siku yangu ya kuzaliwa. Nadhani Britney atakuwa anakumbuka hilo.”
“Samahani, hatutaweza kuja.”
“Kwanini?”
“Kuna mahali tutaenda. Sidhani kama tutapata muda.”
Akamtazama Henessy kisha akarudisha uso wake kwangu. “Mnaenda Marekani, sio?”
“Hapana, si Marekani,” nikamjibu. “Ni hapahapa ndani ya Ujerumani.”
“Ndiyo mkose muda wa kuja kuniona? Kweli? Sidhani kama Britney atakuwa amenisahau na kutonijali kiasi hiko!”
Nikanyamaza nikikosa cha kumjibu. Nikanyanyua glasi ya juisi na kunywa fundo moja. Nikamwona yule mwanamke akifungua mkoba wake na kutoa simu. Akabonyeza kidogo na kuweka sikioni, “Njoo unichukue!” kisha akarejesha simu mkobani na kutoa bunduki! Akaninyooshea na kuniambia, “Ukifanya lolote la kipumbavu ntakugeuza mzoga!”

**
 
*NYUMA YAKO – 20*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Nikanyamaza nikikosa cha kumjibu. Nikanyanyua glasi ya juisi na kunywa fundo moja. Nikamwona yule mwanamke akifungua mkoba wake na kutoa simu. Akabonyeza kidogo na kuweka sikioni, “Njoo unichukue!” kisha akarejesha simu mkobani na kutoa bunduki! Akaninyooshea na kuniambia, “Ukifanya lolote la kipumbavu ntakugeuza mzoga!”
ENDELEA
“Nyoosha mikono juu!” akaniamuru. Nami nikatii ikiwemo pia na Henessy naye akanyoosha mikono yake juu. Na mwanamke huyo akiwa ameiminyia silaha mbavuni mwangu katika namna ambayo haionekani na mtu mwingine, akaniamuru nielekee nje ya eneo hilo kuelekea moja kwa moja kule lami.
Nikatii, tukatoka tukitembea kwa ukakamavu kuelekea huko. Tukiwa njiani mwanamke yule akawa anaangazaangaza huku na kule kuhakikisha usalama wake, nami kichwani mwangu nikifikiria namna gani ya kujichoropoa.
Tukasonga mpaka mahali ambapo kwa mahesabu tulikuwa tumebakiza umbali mfupi kufikia ule usafiri ambao mwanamke yule anatupelekea. Ghafla, nikiwa hata sijui kinachoelekea kutokea, Henessy akachoropoka toka kwenye mikono ya mwanamke yule mtekaji na kukimbilia miongoni mwa watu waliokuwa wamejaa huko ufukweni!!
Mwanamke yule, akiwa amechanganyikiwa, akamnyooshea bunduki Henessy, mara akapata fahamu kuwa hawezi kumfyatulia risasi hapo, basi akataka kurejesha bunduki kwangu, hapo nikakataa kwa kuudaka mkono wake kisha kuutegua kistadi, akaachia bunduki!
Nikamnyooshea na kumwamuru atulie kama maji mtungini. Nikamtaka anyooshe mikono yake juu na kisha twende kule alipokuwa anataka kunipeleka. Akatii.
Nikamwita Henessy na kumtaka akae mahali kuningojea, naja muda si mrefu. Naye akatii. Nikaongozana na mwanamke yule mpaka garini, Van nyeupe yenye vioo vyeusi. Hapo nikagonga mlango, punde ukafunguliwa na mwanaume mwenye kuvalia kapelo.
Nikamkaba vema mwanamke yule niliyekuja naye kisha bunduki nikamwelekezea yule jamaa mwenye kapelo. Tukazama ndani ya gari.
Swali la kwanza nikawauliza wametumwa na nani. Hapo nikiwa nimehakikisha kuwa uso wangu unaogofya.
“Hamna mtu aliyetutuma,” akasema yule jamaa. “Ni sisi wenyewe ndiyo tumekuja hapa.”
“Kufuata nini?”
Kabla jamaa hajanijibu akamtazama kwanza mwenzake. Hapo nikaongezea nguvu kwenye kumkaba mwanamke huyo mpaka kusikia akikoroma.
“Tulikuwa tumemfuata Henessy!” akaropoka jamaa. Nikamuuliza, “Mnamtakia nini na mumpeleke wapi?
Jamaa yule akanyamaza akiwa anantazama. Nikarudia kumuuliza swali langu, hakunijibu, badala yake akaniuliza, “Wewe ni ajenti wa CIA, sio?”
“Jibu nilichokuuliza!” nikamwamuru. Lakini hakuonyesha sura ya hofu, hata akatabasamu na kuendelea na maneno yake, “Hautafanikiwa kwenye hili,” akasema. “Una kazi ngumu sana, ajenti.”
“Nami ndizo hizo ngumu napenda!” nikamjibu kisha nikamfyatulia risasi kuparaza sikio lake la kushoto. Haraka akalidaka sikio lake hilo akilalama kwa maumivu makali! Yule mwanamke nikamgonga na kitako cha bunduki chini ya kisogo chake, akazirai!
Nikamfuata yule mwanaume na kumkwida shati, bado akiwa analalama kwa maumivu makali sikioni, nikamwamuru anijibu maswali yangu!
“Ajenti!” akaniita. “hata kama nikijibu maswali yako haitasaidia kitu.”
“Mambo ya kunisaidia au kutonisaidia nayajua mwenyewe. Nijibu kabla sijazibua sikio lako jingine!”
Bado akawa mgumu. Nikageuza kitako cha bunduki na kumtwanga nacho kwanguvu kwenye shina la pua. Akapiga kelele za maumivu akidaka pua yake ambayo ilikuwa inachuruza damu.
“Mmetumwa na nani?” nikafoka kumuuliza. Alikuwa analalama kwa maumivu mikono yake iliyoziba pua ikijawa na damu lakini bado akawa mbishi! Hakutaka kusema.
Nikabana mikono yake na kumkandika tena kitajo cha bunduki kwenye pua yake yenye maumivu. Damu zikamruka akilalamika kwa maumivu makali. Akalia sasa kama mtoto uso wake ukiwa umefunikwa na damu nyingi.
Nikarudia kumuuliza, “Mmetumwa na nani!”
Bado akawa hasemi. Akalia na kulia tu kwa maumivu anayoyapata. Basi nikamkamata tena mikono yake ili nikamndike tena pua. Hapa akapiga kelele kali, “nasema! Nasema!”
“Sema!” nikamkaripia.
“Tumetumwa na Adolfo!”
Hapa nikamkumbuka yule jamaa niliyemkamata na kumtesea kule hotelini. Kabla hajazirai alisema jina la Rodolfo. Ina maana ndiye huyu Adolfo? Nilipomuuliza huyu jamaa zaidi akasema ni Adolfo. Basi nilikuwa nimesikia vibaya toka kwa jamaa yule siku ile.
Ila Adolfo ni nani haswa? Na kwanini anatufuatilia? Nilipomuuliza hilo, akashindwa kujibu. Nadhani nilikuwa nimemkandika sana. Nilimwona amelegea. Na hatimaye akazirai macho yakiwa hayajafumba vema.
“Shit!” nikapiga dashboard. “Sasa nitapata wapi taarifa za Alfonso?”
Kwa muda kidogo nikapata kufikiri. Nilihitaji sana kumjua huyu Alfonso.

**

Nadhani ilikuwa imepita lisaa tangu tutoke ufukweni mimi na Henessy kwa kutumia van ya wale wavamizi waliokuja kututeka.
Tulipoenda ilikuwa mbali na mji, mbali na purukushani za watu, na huko nyuma ya gari tulikuwa tumewabebelea wale watu wawili, mwanamke na yule mwanaume ambao bado hawakuwa wamepata fahamu.
Basi tukiwa hapo, nikawa nateta na Henessy nikimdadisi kwa maswali kadhaa kadhaa juu yake na mama yake. Hapo ndiyo nikapata kujua kuwa hata alipokuwa kwenye mikono ya watekaji, yeye pamoja na mama yake, alikuwa akipewa simu acheze ‘game’ lakini kwa uangalizi maalumu.
Game alipendalo, Subway Surfers. Hata hapo aliniuliza kama simu yangu ina credit apate kulipakua toka mtandaoni.
Laiti kama wale watekaji wale wangelijua kuwa game hilo ndilo lilikuwa njia ya kuwapata, wasimgeruhusu Henessy ashike simu yao.
“Kuna muda nilikuwa naboreka sana,” alisema Henessy. “Ningekaa kwenye kona nikiwa sina raha, basi angekuja mmoja wao na kuniambia shika ucheze!”
Nikatabasamu nikimwangalia. Alikuwa mtoto mchangamfu na mwenye akili. Hakustahili kupitia yote haya. Kweli dunia haina usawa. Nilimfinya shavu lake nikimchekea kisha nikampatia simu yangu acheze game lake.
“Baba yako yuko wapi, Henessy?”
“Hayupo!” akanijibu akibofyabofya simu.
“Yuko wapi?”
Akapandisha mabega pasipo kunena jambo.
“Henessy, unamjua baba yako?”
“Ndio. Mama aliwahi kunionyesha picha zake.”
“Hujawahi kumwona kwa macho?”
“Aaahm!” akatulia kidogo. Kuna kitu kilikamata macho yake kwenye simu. Alipotulia akaendelea kunena, “Baba yangu ni mtu wa kusafiri sana. Anashinda muda mrefu akiwa kwenye ndege na kwenye mabasi, hivyo amekuwa akija nyakati za usiku nikiwa nimelala tayari. Mama huwa ananiambia.”
“Mara yako ya mwisho kumwona ilikuwa lini?” Akatulia kama hajanisikia. Alikuwa akitazama simu kwa umakini. Punde akanionyeshea kioo cha simu akiniambia, “ona alama zangu!” kisha akacheka. Nikamtazama nikitabasamu. Alikuwa anafurahia sana kile anachokitazama na kukicheza simuni, nikaona maongezi yetu hayatafika popote pale. Acha nimwache acheze baadae tutaongea.
Kidogo, nikasikia mtu akijigeuza garini. Kutazama nikamwona yule mwanamke akirejea fahamuni. Alipotazama vema akanikuta ni mbele yake nikimnyooshea mdomo wa bunduki. Sura nimekunja kibabe, na nikasema maneno machache kwa kumaanisha,
“Umeona kilichomtokea mwenzako?” akageuza shingo kutazama mwili wa mwenzake kando. “kitakutokea na wewe endapo utaleta ujuaji.”
Akakunja uso wake kwa hofu akisema, “mimi sijui kitu!”
Nikatabasamu kikebehi, “acha kunifanya mjinga. Kwahiyo ulitufuata kwa bahati?”
Nikamdaka mkono na kumvuta kumketisha kitako. Nikamwambia, “Mwanamke, sina mzaha na wewe. Ni aidha unambie ama nikulaze hoi. Chaguo ni lako!”
Macho yake yakajawa na machozi. “Nini unataka kufahamu toka kwangu?” akaniuliza.
“Kila kitu unachodhani nastahili kujua!”
“Mimi si rafiki yake Britney. Nilikuongopea tu.”
“Kwanini uliniongopea? Nani alikutuma?”
Akanionyeshea yule mwanaume aliyelala hajitambui pale kando.
“Kwanini alikutuma?”
“Sijui! Alinambie nimteke huyo mtoto.”
“Alafu?”
“Nimpatie!”
“Mlijuaje kama tupo pale ufukweni?”
“Tulikuona ukitokea ubalozini. Walikuwepo hapo wakijua utafika tu.”
“Wakina nani hao?”
“Huyu jamaa na wenzake! … mimi sihusiki. Kweli nakwambia!”
Nikamtazama kwa macho makali kwa sekunde tatu alafu nikamuuliza, “Alfonso ni nani?”
Alipotaka kusema hajui, kabla hajamalizia kauli yake, nikamkita na kitako cha bunduki pembeni ya jicho lake la kushoto, “Shenzi!”
Akalia kwa maumivu. Alivuja damu. Nikamdaka nywele zake kwanguvu na kumuuliza tena, “Alfonso ni nani?”

***
 
*NYUMA YAKO – 21*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Nikamtazama kwa macho makali kwa sekunde tatu alafu nikamuuliza, “Alfonso ni nani?”
Alipotaka kusema hajui, kabla hajamalizia kauli yake, nikamkita na kitako cha bunduki pembeni ya jicho lake la kushoto, “Shenzi!”
Akalia kwa maumivu. Alivuja damu. Nikamdaka nywele zake kwanguvu na kumuuliza tena, “Alfonso ni nani?”
ENDELEA
Jicho lake la kushoto lilivilia damu. Kweli aliumia. Ila sikumwonyesha uso wa huruma bali ule uonyeshao kuwa mengi yanafuata hapo mbele endapo akiwa mkaidi.
Akalia kwa muda kidogo. Na mafua akapata. Akan’tazama na kunambia kwa uso mtakatifu, “Simjui Alfonso mimi!”
Nikamdaka nywele zake kwanguvu sana kisha nikamuuliza amemjuaje Britney? Na zile soga alizokuwa ananipa je? Akasema alidanganya! Yeye si rafiki wa Britney kama alivyosema. Yote aliyosema alidanganya.
Na vipi kuhusu Henessy? Alimjuaje? Nikapata swali. Nacho akaniambia hakuwa anafahamu lolote lile kumhusu. Yote hayo alipandikiziwa mdomoni akayaseme.
“Nani alikupandikizia hayo?” nikamuuliza.
“Huyu!” akaninyooshea kidole yule jamaa aliyelala kando. “Ni huyu hapaa!”
Lakini hapana! Mimi haikuniingia akilini kuwa mwanamke huyu hajui lolote kumhusu Alfonso. Ni kwamba tu nguvu yangu haikutosha kuondoa gamba lake alimojifichia.
Hivyo nikaona kuna haja ya mimi kuongeza ‘pressure’ kidogo niuone uhalisia. Endapo akifaulu jaribio hilo basi ningemwacha huru.
Nikadaka mkono wake wa kulia na kuvunja kidole chake cha mwisho! Kat! Akapiga yowe kwa maumivu makali. Sikumwonea huruma, nikadaka tena kidole kinachofuata akiwa anajitetea kujikomboa, nacho nikakiminya kukivunja, akapiga kelele, “Najua!”
“Unajua nini?” nikamuuliza nikiendelea kubinya kidole hicho karibu na kukivunja.
“Namjua Alfonso! Tafadhali niachie!” nikamwachia na kumwambia, “Enhe, ni nani na wapi alipo?”
Akatetema kwanza kwa kilio akitazama kidole chake kilichokuwa kimepinda. Akajaribu kukishika, akaishia kulalama kwa maumivu. Akavuta makamasi na kun’tazama kwa hasira na ghadhabu yenye maumivu ndani yake, “wewe ni mnyama!” akasema.
“Mwanamke, sina muda wa kupoteza na wewe,” nikamwonya. “naweza kuwa mnyama wa kupeti ama wa kukutafuna kutokana na mienendo yako. Sasa utasema ama tuendelee kumalizia vidole?”
Akajifuta makamasi na mkono wake wa kushoto kabla hajaanza kusema,
“Alfonso ni bosi wetu, anaishi huku Berlin, Ujerumani. Anatulipa vizuri sana, na ametuahidi kutulipa zaidi tutakapomaliza kazi yetu.”
“Kazi gani hiyo?”
“Sikia, ajenti. Mimi sijui mengi sana, na ukinilazimisha niseme hivyo hivyo nitaishia kukudanganya. Ninachojua ni kwamba, Alfonso anamhitaji huyo mtoto, Henessy. Ndiye pekee aliyebakia baada ya mama yake kufariki.”
“Kwanini anawahitaji hao watu? Wa kitu gani?”
“Kwasababu ya Raisi! Raisi wa Marekani. Hii ni familia yake Raisi. Henessy ni …” nikamsihi apunguze sauti yule mtoto asisikie. “Henessy ni mtoto wa Raisi!”
“Unatania, sio?”
“Unauona huu ni muda wa matani, ajenti? Nikiwa nimevunjwa kidole na kubabuliwa kichwa?”
“Umejuaje kama hii ni familia ya Raisi? Hamna mtu anayelijua hilo!”
“Ndio ujue sasa kuwa ajenti hakumaanishi kujua kila kitu kuhusu Marekani. Hata Secret Service hawaitambui siri hii. Hii ni familia ya siri!”
“Lakini …”
“Sikia, unafahamu kuwa Britney alikuwa ni pornstar, mcheza picha za ngono maarufu, unadhani Raisi gani angebeba sifa hiyo? Tena amezaa naye! Angemwambia nani juu ya hilo? Huoni ni kujichafua, kuchafua chama, kuchafua taifa? … ndiyo maana ni familia ya siri! … Raisi alikuwa ana mahusiano na Britney! Mcheza sinema za ngono!”
Habari hii haikuwa ya kawaida. Lilikuwa ni jambo kubwa tena likisemwa ndani ya van ya kawaida, nchi ngeni! Likikuwa ni jambo nyeti la kuteka vichwa vya habari ulimwengu mzima!
“Una uhakika na unachoongea?”
“Ajenti, kwa akili yako unadhani kuna haja gani ya kusumbuka na mcheza ngono? Sisi si ISIS au Boko Haram useme tunateka raia yeyote wa Marekani!”
“Sasa kwanini Alfonso anataka hii familia? Na Raisi yupo wapi?”
Nilikuambia awali, mimi sijui mengi. Na hata huyu uliyemziraisha hapa, hatokueleza kipya. Wote tunachojua na tulichopewa kufanya ni kutafuta familia hii na kuiweka mikononi mwetu. Hayo mengine, anayajua Alfonso tu!”
“Niambie wapi anapatikana.”
Kabla hajasema akasita kidogo.

***

Basi safari yangu ya kurudi Marekani jioni ya hii siku ilibidi niifute ili nipate kufuatilia haya yaliyojiri.
Nikiwa nimevalia nguo nyeusi ambazo nilizikwapua toka kwa yule jamaa wa kwenye van, nikashuka toka garini na kusonga kuifuata nyumba fulani kubwa inayopatikana upande wa magharibi wa jiji la Berlin.
Nyumba hii ndiyo ambayo nimeelezwa kuwa ya Alfonso kwa mujibu wa mateka wangu. Kwahiyo nilikuwapo hapa nikiwa natarajia kupata majibu ya maswali yangu mawili, mosi, kwanini Alfonso anawinda familia hii ambayo nimeambiwa ni ya Raisi, na pili, Raisi yupo wapi? Niliamini atakuwa ana fahamu!
Nikaudaka ukuta huu mrefu na kuukwea, kisha nikatumbukia ndani. Kwa ufupi, labda tuepushe kupoteza muda, nilitumia kama dakika nane kufika nilipokuwa natakiwa kuwapo. Na huku safari yangu hiyo ikiwa imegharimu maisha ya watu watano.
Ilikuwa ni usiku wa saa tano, na tofauti na nilivyokuwa nawaza, nikamkuta huyu jamaa ambaye niliamini kuwa ni Alfonso, amelala akikoroma!
Nikamuwekea silaha kichwani na kumnong’oneza aamke kwani nina maongezi naye machache. Alipoamka akashtuka kuonana na sura ngeni. Japo sikuwasha taa, tulikuwa tunaonana vizuri kwasababu ya mwanga wa taa za nje.
Mwanaume huyu alikuwa wa makamo ya hamsini kwa umri japo nywele zake hazikuwa na tembe ya mvi. Mnene kwa umbo lakini anayejiweza. Alikuwa anazungumza kiingereza vizuri kwa lafudhi ya kimarekani hivyo nikajua moja kwa moja ni wa nyumbani..
Akajivuta akiketi kitako kisha akan’tazama, pasi na woga, akaniuliza, “Unataka nini kwangu muda huu?”
Kabla sijamjibu, yeye akaendelea kunena, “Sikia, ajenti.” Sijui alijuaje kama mimi ni ajenti. Pengine kwa namna nilivyozama ndani. Akiwa ananinyooshea kidole, akawa anasema, “kama umekuja hapa kwa kudhani nina majibu ya maswali yako na ya nchi yako …” akabinua mdomo, “hesabu umefeli!”
“Maswali gani unayoyaongelea wewe?” nikamuliza. Akagunia kifuani. “Sijui Raisi wa Marekani alipo, sawa?’ akanambia akin’kodolea macho. “Kama wewe tu, sijui Raisi wenu alipo! Kama umekuja hapa kuniuliza hilo, basi umefeli.”
Nikaketi kitandani. Sikuamini anachokisema, najua hata mwizi ni ngumu kukiri alhali umemkamata na ngozi.
“Alfonso, haujui Raisi alipo ila unafahamu familia yake. Sio?”
“Ajenti, nimefanya kazi na namiliki klabu nyingi za usiku jijini Los Angeles na Miami. Huko wanawake wanacheza uchi na wengine kujiuza. Britney alikuwa ni mfanyakazi wangu kwa miaka mitano. Unadhani kipi ambacho nisingekijua?”
“Kwanini ukamteka? Yeye pamoja na mwanae!”
Akatikisa kichwa na kusema, “Ungeniuliza kwanza kwanini nipo Ujerumani?”
Kabla sijamuuliza hicho alichosema nimuulize, akakijibu yeye, “Nipo huku toka Marekani, ajenti. Kwasababu ya sera za mbovu za Raisi wako juu ya wawekezaji. Amenifilisi sana. Ameniangusha kiuchumi na sikudhani kama ningekuja kusimama tena. Kwa miaka yake miwili tu, ilitosha kunidhoofisha haswa. …
Ajenti, unadhani nilikuwa tayari kurudi nilipotokea baada ya miaka mingi ya kujenga mfuko wangu?” akatikisa kichwa. “Hapana, siko tayari kupoteza yote ndani ya mfumbo mmoja wa macho. Kumteka kwangu Britney na mwanaye, ni kutaka pesa yangu irudi! Arudishe yale yote ambayo amenipotezea.”
“Kwahiyo umeshapata baada ya hapo?” nikamuuliza.
“Aaaahmm .. kidogoo!” akanijibu akifumba jicho lake moja. “Ila si kama nilivyokuwa nikitarajia. Kama unavyojua, Raisi amepotea. Wapi nitapata pesa?”
Sikumwamini maelezo yake. Niliona kuna haja ya kumsafirisha nimpeleke Marekani akatoe maelezo zaidi. Lakini akanitahadharisha, “Nikirudi Marekani, kila mtu atajua Raisi alitembea na kuzaa na mcheza sinema za ngono maarufu. Nadhani unajua itakuwa ni aibu kiasi gani!”
Nikamtazama mwanaume huyo kisha nikamuuliza, “Alfonso, Raisi yuko wapi?”
Akanipandishia mabega, “sijui! Ajenti, sifahamu hilo!” akasema akin’tolea macho. “mimi mwenyewe natamani apatikane nipate pesa yangu!”
Hapa nikajikuta nanyong’onya. Nilidhani hatua hii itakuwa ya karibu kufikia lengo, kumbe nalijidanganya. Bado nipo mbali!
Sasa na wale waliokuwa wanawashambulia wakina ajenti Daniele kule Marekani, kumuua pia O’Neil, ni watu wengine? Watu wasiohusiana na Alfonso?
Kwa muda nikajikuta nikisahau kama nipo kwenye nyumba ya maadui.

**
 
*NYUMA YAKO --- 22*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Sasa na wale waliokuwa wanawashambulia wakina ajenti Daniele kule Marekani, kumuua pia O’Neil, ni watu wengine? Watu wasiohusiana na Alfonso?
Kwa muda nikajikuta nikisahau kama nipo kwenye nyumba ya maadui.
ENDELEA
Nilipomulikwa usoni ndipo nikagutuka na kurudisha akili tukioni. Nikakuna kichwa. Hapa nikambana Alfonso na kumtumikisha twende naye nje kwa usalama wangu. Lakini bwana huyu hakutaka katu hata kunitaka nimuue lakini hatatii agizo langu!
Akacheka.
“Bwana mdogo, hutoweza kutoka hai hapa. Ni bora uka surrender!” akanambia kwa kebehi. Nami nisitake maneno mengi, nikafyatua risasi mbili za upesi pembeni na kichwa chake. Nikamtengenezea maumivu makali sikioni, na kama haitoshi nikamtwanga risasi ya mguuni kisha nikaketi kando yake.
“Haya sasa tukae, utakufa taratibu kwa kupungukiwa na damu!”
Bwana huyo akawa analalama sana kwa maumivu. Huku masikioni na kule miguuni. Alivumilia sana na hakukuwa na wa kumsaidia kwani walinzi wake wasingeweza kuzama ndani kwa kuhofia nitammaliza kabisa mkuu wao.
Nami nisiwe na habari yoyote, nikatoa risasi zangu toka kwenye bunduki, nikibakisha tatu, kisha nikizirudisha tena ndani ya bunduki. Nilipofanya mchezo huo kwa dakika kama tano, nikasimama na kuanza kupekua chumba cha Alfonso.
Alfonso akaniita na kuniambia, “Ewe ajenti, nipeleke hospitali kabla sijafia hapa. Huoni kitanda changu kimefurika damu?”
Nikamtazama na kisha nikaendelea na msako wa mule chumbani. Nikamjibu pasipo kumtazama, “Ulijifanya mkaidi, endelea kukaa hapo mpaka utakapoona kuna haja hiyo!”
Akanisihi, “sikia, mruhusu mmoja wa vijakazi wangu twende nikuonyeshe njia ya kupita chini kwa chini tuondoke hapa. Nakuhakikishia utakuwa salama. Ila uniahidi kunipeleka hospitali!”
Nikamtikisia kichwa, “Hapana, siwezi fanya hivyo. Hamna mtu mwingine yoyote atakayeongozana na sisi. Ni sisi peke yetu tu!”
Akaleta ubishi kidogo hapa ila alipoona hali inazidi kuwa mbaya, akakubali. Nikamnyanyua na kutoka naye ndani ya chumba kuelekea chumba kinachofuata ndani ya nyumba hiyo, humo tukazama na kuuelekea mlango mdogo wa sakafuni, nikaufungua na kuzama humo.
Ilikuwa ni njia ya kutokea nje kisiri. Na mlango huu unawekwa maalumu kwa ajili ya kipindi cha mashambulizi. Hivyo mkiwa mnashambuliwa inakuwa rahisi kwa mkazi kutoroka.
Tukatembea humo na ndani ya kama dakika nane, tukawa tumefika mahali ambapo niliona kuna mwanga wa kutokea nje. Tukakazana, hapo nikiwa namburuta bwana huyu ambaye hakuwa anajiweza. Alikuwa mdhaifu sana na anayehisi maumivu.
Lakini kwa namna alivyokuwa amechoka, hakuwa analalamika tena. Alikuwa ameachama kinywa wazi, anatokwa na jasho jingi. Kwa namna nilivyomwona hakuwa anaweza kudumu baada ya lisaa. Ilinipasa nikazane zaidi kama ningelitaka awe hai.

**

Nilishamkabidhi mtoto ubalozini na safari yangu nikiwa nimeisogeza mbele kwa siku mbili.
Alfonso alikuwa hospitalini akipata matibabu, lakini chini ya uangalizi wa kiusalama. Na mimi … nilikuwa hapa mgahawani nikipata chakula cha mchana. Niliagiza kuku wa kuchoma na vegies.
Si kwamba napendelea sana aina hiyo ya chakula, hapana, ila ndo’ chakula ambacho niliona naweza nikala hapa na kujihesabia nimekula.
Nilipomaliza, nikaagiza sharubati na kunywa taratibu nikiwa natafakari baadhi ya mambo huku nikitazama picha kadhaa kwenye simu yangu, picha ambazo nilizipiga kwenye baadhi ya vitu vya Alfonso kule kwenye nyumba yake.
Nikiwa nakaguakagua, simu yangu ikapigwa tokea ubalozini. Nilipopokea ilikuwa ni sauti ya kike ambayo iliteta maneno machache, “Fika ubalozini.”
Nikalipia bili yangu ya chakula kisha nikaelekea huko upesi. Nikakutana na ‘director’, bwana Phillip, akaniambia baadhi ya mambo ambayo wameyapata toka kwa Alfonso.
Watu hawa niliwaachia kazi kidogo ya kuulizia na kufuatilia nyaraka halali za bwana Alfonso hapa Ujerumani, ikiwemo pia na akaunti zake ili tuone uingizaji na utokaji wa pesa zake tangu Raisi alipopotea.
Basi bwana huyu, Phillip kwa jina, akanambia kuwa wamefanikiwa kupata taarifa nilizoagiza. Jambo hili lilikuwa jepesi kwakuwa niliwapatia baadhi ya picha za kadi zake za benki ambazo mimi nilizitolea kule kwenye chumba cha Alfonso.
Na kwa mujibu wa maelezo ya bwana Phillip, Alfonso alianza kupokea dola laki nane za kimarekani kila mwezi baada ya Raisi kupotea. Hivyo swala hili likanipa tena nguvu kuwa Alfonso atakuwa anajua wapi Raisi alipo. Au basi kama hajui, atakuwa anamjua mtu ambaye anajua.
Kidogo akili yangu ikaanza kuwandawanda kabla sijaituliza kuskiza maneno ninayopewa.
“Ni nani ambaye anamwingizia pesa hizo Alfonso?’ nikauliza.
Bwana Phillip akakuna kidevu alafu akapekua karatasi zake na kunambia, “Anaitwa Payne! Payne Cluster.”
“Umepata taarifa zake?”
“Hapana! Tumejitahidi lakini swala hilo limekuwa gumu. Bado tunalifanyia kazi.”
“imekuaje limekuwa gumu na jina la mwenye akaunti mnalo?”
“Tatizo hatumii akaunti moja,” akasema Bwana Phillip. “Jina ni moja lakini amekuwa akitumia akaunti tofauti tofauti. Na kunaa …” akachomoa tena karatasi na kuitazama, kisha akanambia, “Ila mara ya mwisho, pesa zilitoka kwenye akaunti yenye jina la Katie Rodwell.”
“Huyo mmepata taarifa zake?” nikawahi kuuliza. Akabinua mdomo na kutikisa kichwa. “Hapana. Tangu alipotuma pesa hiyo akaunti yake ikafa. Haipo tena!”
Basi nikaona nisipoteze muda sana, nikachukua taarifa hizi na za maeneo ya uwekwaji wa hizo pesa kisha nikaondoka zangu.
Kilinichomishangaza ni kwamba, maeneo matatu ya mwisho kwa Alfonso kuwekewa pesa ilikuwa ni Ujerumani! Yaani watu waliomwekea hiyo pesa walitumia benki za hapahapa Ujerumani. Inamaanisha watu hawa wapo hapahapa nchini!
Sasa nitawapatia wapi? Nikajiuliza. Njia nyepesi ilikuwa ni kwa kupitia Alfonso mwenyewe. Hivyo nikapanga kwenda kumwona.
Baadae majira ya jioni nikawa hospitalini pembeni ya kitanda cha Alfonso. Baada ya kumjulia hali, nikamuuliza maswali yangu, ni nani Payne na yule Katie ambaye walikuwa wanamwekea pesa kwenye akaunti yake?
Akakohoa kwanza kisha akaniambia, “ajenti, nikikuambia siwafahamu utaamini?”
Kabla sijasema jambo, akasema, “Siwafahamu hao watu. Na kama nilivyokueleza hapo kabla, nilikuwa napokea pesa kwa kuwa na familia ya Raisi. Mtu anayeniwekea pesa, mimi sijali. Najali pesa kuingia kwenye akaunti tu!”
“Alfonso,” nikaita na kuuliza, “mara mbili za mwisho kuwekewa pesa zilitokea Ujerumani. Unanambiaje huwafahamu? Ina maana haukukutana nao?”
“Sikukutana nao,” akanijibu kwa sauti ya chini. “Siwafahamu kabisa, ajenti. Mimi nalikuwa napokea pesa tu na si kingine.”
Nikanyamaza nikimtazama. Naye akan’tazama kwa sekunde kadhaa kabla hajaniomba simu yangu aongee na mtu aliyemtambulisha kama binti yake wa pekee. Anahitaji kumwambia juu ya hali yake. Anadhani atakuwa amefanya jema kumjuza.
“Yuko wapi huyo binti?” nikamuuliza.
“Marekani,” akanijibu na kuongezea, “Anasoma huko. Yeye hana makosa na sitaki ahusishwe na mambo yangu. Nataka asome na aendelee na maisha yake kwa amani.”
Mimi, pasipo ajizi, nikampatia simu yangu akapiga. Nikiwa nimesimamishaa masikio, nikasikia, “Halo, Perry. Unaendeleaje? … vipi shule? … Kuna shida yoyote? … nimekumiss sana mwanangu, natazamia kukuona karibuni, naona kuna haja hiyo … hamna shida, kuwa salama mpenzi wangu … niko sawa … kweli … nimepata majeraha kidogo, nikaja hospitali, Berlin … nitakuwa sawa, si kitu kikubwa. Kwaheri … nakupenda.”
Akanikabidhi simu yangu akitabasamu kwa mbali. Nami nikamuaga na kwenda zangu nikiwa nimeshapanga kufuatilia namba ile alozungumza nayo kwa kumtumia ajenti Daniele.
Nikiwa njiani, ili nisisahau hilo jambo, nikamtafuta ajenti Daniele na kumjuza juu ya Perry na namba yake. Nikamwamchia kazi hiyo anipatie majibu baadae. Nikaelekea kwenye makazi yangu, kisha nikaanza kujiandaa kwenda kule nyumbani kwa Alfonso. Nilihisi kule kutakuwa na kitu ambacho kitanisaidia kujua wapi pakuanzia kutafuta wale watu ambao walikuwa wanamtumia pesa.
Mule chumbani, hamtakosekana nyaraka elekezi.
Basi nikafika huko baada ya nusu saa tu, na kwasababu nilikuwa najua mlango ule wa siri, nikauzamia na kuibukia ndani kisha moja kwa moja chumbani mwa Alfonso.
Nilifanya kila jambo kwa utulivu na ukimya kweli. Sikutoa hata punje ya sauti. Nikiwa nasakasaka, nikapata baadhi ya makabrasha ambayo niliyapiga picha kwa simu, ila kidogo nikasikia sauti ya gari ikiingia eneoni.
Nikasonga dirishani na kuchungulia nje. Huko nikaoma BMW x6 nyeusi. Toka kwenye gari hiyo, wakashuka wanaume watatu waliovalia suti. Mmoja wao, hakuwa mgeni machoni pangu.
Nilihisi nimeona vibaya, ila nilipozidi kuangaza nikagundua nilikuwa sahihi. Bwana huyo hakuwa mgeni machoni pangu! Bwana huyo alikuwa ni yule ajenti ambaye alikuwa anahusika na kumlinda Raisi kisha akapotea kwa kusemekana amefia ndani ya nyumba yake iliyoungua moto!
Kumbe yu hai!
Kumbe wanajuana na Alfonso!

**
 
*NYUMA YAKO 23*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Nilihisi nimeona vibaya, ila nilipozidi kuangaza nikagundua nilikuwa sahihi. Bwana huyo hakuwa mgeni machoni pangu! Bwana huyo alikuwa ni yule ajenti ambaye alikuwa anahusika na kumlinda Raisi kisha akapotea kwa kusemekana amefia ndani ya nyumba yake iliyoungua moto!
Kumbe yu hai!
Kumbe wanajuana na Alfonso!
ENDELEA
Nikapata hamu ya kujua zaidi. Nikiwa nimejibana humo ndani watu wale wakaingia ndani ya jengo, na moja kwa moja wakaketi sebuleni huko wakiongea na kupanga mipango yao.
Chumba nilichomo hakikuwa mbali sana na sebule hivyo nikawa nasikia baadhi ya mambo. Na watu hawa walikuwa wakizungumza kwa lugha ya kiingereza, tena kile cha Marekani.
Wakaongea kwa muda mchache sana, kama dakika tano tu, kisha kikao kikakata, nilichokiambulia kikiwa ni haya machache: mosi, kumhusu Alfonso. Hapa waliteta kwa maneno mawili tu, kuwa wamkute, na baada ya hapo wakagusia swala la malipo, pesa itakuja, na mwisho nikiwa nimegundua kuwa bwana yule ambaye ni ajenti wa Secret Service akiitwa jina la PKP.
Kidogo, gari lile BMW x6 likawashwa na watu wale watatu wakajikwea kwenye gari lao ma kuondoka. Hapo ndipo baada ya kama dakika mbili tu, simu yangu ikaita. Sauti ilikuwa kubwa kidogo ukizingatia na ule ukimya uliokuwepo. Nikapokea na kunena kwa kunong’ona. Alikuwa ni bwana wa ubalozini.
Akasema, “Ajenti, Alfonso ametoroshwa hospitalini!”
Sikutaka maelezo zaidi maana sikuwa eneo zuri kuwasiliana hivyo nikapokea habari hiyo na kurudisha simu mfukoni. Kidogo tu, nikasikia mtu akija. Nikahisi mtu huyo atakuwa amesikia ule mlio wa simu yangu. Haraka nikajificha nyuma ya mlango, na punde tu, mlango ukafunguliwa!
Kutazama, bwana huyo hakuingia ndani, aliangaza kwanza kwa kama sekunde nne, na nadhani alipoona cha kutilia shaka, ndipo akazama ndani. Nilipomtazama nikamwona akitazama kule kwenye droo, mojawapo ilikuwa wazi. Akasonga akitupa mlango kwanguvu ujifunge.
Bahati hakutazama nyuma, akasonga kwenda mbele. Hapo ndipo mimi nikatumia hiyo nafasi kumfuata bwana huyo kwa ukimya wa hali ya juu. Nilipomkaribia, akageuka, ila akawa amekawia kwani nilimdaka shingo yake na kumtuliza pia nikambana kinywa.
Alafu kwa usalama wangu zaidi, nikaufunga mlango kwa funguo.
“Nijibu maswali yangu nami nitakubakizia uhai wako,” nikamwambia bwana yule niliyemuweka kwenye himaya yangu. Naye kwasababu alikuwa amebanwa hakuwa na uwezo wa kunena, ikabidi nimwache kidogo.
Akahema kwanguvu sana akitoa macho. Nikampatia kama sekunde nne tu, kisha nikamuuliza, “Yule PKP ni nani yenu?”
Bwana yule akaleta ukaidi. Nami nisifanye ajizi, nikamkaba tena kwanguvu mpaka nilipohisi amepata adabu ndipo nikamwacha na kumuuliza tena, akanijibu ni mshirika mwenzao! Kabla sijapata muda wa kuminya zaidi majibu toka mwilini mwake, huko nje ya chumba nikasikia wakimuulizia bwana huyu. Naye akanambia, “Watakuwapo hapa muda si mrefu na utakuwa mwisho wako!”
Basi nikawa sina muda wa kupoteza tena hapa, nikamziraisha bwana huyu na kutoka humo ndani upesi. Nikaelekea kile chumba kinachofuata ambacho ndipo penye tundu la kuzamia chini kwa chini kutokea nje. Lakini kufika mlangoni hapo, nikaukuta umefungwa! Nilijaribu kuufungua pasipo mafanikio. Sikuelewa nani ameufunga na kwa muda gani! Na wakati huohuo, nikiwa nasikia sauti ya watu wakija huu uelekeo wangu!
Hapa nikaona nichukue maamuzi ya upesi. Nikauvunja mlango huu kwa teke la nguvu kisha nikazama ndani na kuukimbilia mlango ule wa dharura. Nikaufungua na kudumbukia humo alafu upesi nikaanza kukimbia.
Kidogo huko nyuma nikasikia sauti ya watu wakiteta na kufoka, na masikio yangu yakiwa sahihi, watu hao wakazama ndani ya ile chemba ya chini itokayo nje, humo ambapo mimi nilikuwamo!
Nikakimbia sana. Punde sauti za risasi zikaanza kuvuma kuniwinda. Hata niliposhika ngazi kupanda juu, zingine zikagonga ngazi ile ya chuma na kusababisha kelele kali!
Nilipotoka nikaendelea kukimbia, kidogo nikawa nimewahepuka maadui zangu nao hawakunikamata tena!

**

“Hamna mtu huyo!” sauti ya Daniele ilinguruma kwenye simu.
“Una uhakika?” nikamuuliza kwa mashaka. “Jina lake ni Perry!”
“Hayupo huyo mtu!” Daniele akasisitiza. “Tumefuatilia hiyo namba na kubaini haipo huku Marekani ingawa ina ‘code number’ za huku.”
Hapa ndipo nikajiona mjinga. Alfonso alinizidi maarifa. Yule mtu aliyeongea naye hakuwa mwanaye kama alivyosema, bali mtu wake wa kazi. Na kwa kuongea naye akabaini wapi mwanaume huyo alipo na wakaja kumkomboa!
Nikawaza sana. Na hapa ndipo nikajenga hoja kuwa Bwana yule ambaye alikuwa ni ajenti wa Secret Service, ndiye ambaye atakuwa anamtumia pesa huyu Alfonso. Asili ya jina lake hilo, yaani PKP, ni Payne, Katie na Perry! Hayo ni majina yake ya kujificha nyakati za haja.
Hivyo basi, PKP ndiye ‘mastermind’ wa yote haya. Na kwakuwa alikuwaa ajenti anayehusika na kumlinda Raisi basi ni wazi atakuwa anafahamu wapi Raisi alipo!
Ni lazima PKP atafutwe na kukamatwa popote pale kwa gharama yoyote ile. Pengine akiwa mikononi mwangu nitaelewa mtiririko wa yote haya.
Nikafika hospitali na kisha ubalozini, nikapata maelezo juu ya namna ambavyo Alfonso alivyotoroshwa. Watu hao wavamizi walifika hapo hospitali kama majambazi kisha wakawaweka watu chini ya ulinzi na kumkwapua mtu wao!
Hakukuwa na mtu aliyetambulika maana waliziba nyuso zao kwa barakoa. Na tukio hilo lilidumu kwa takribani dakika sita tu, wakawa wameshapotea!
“Sasa tunafanyaje, ajenti?” akaniuliza director. Nikamwomba simu yake na kufanya mawasiliano na Daniele. Nikamjuza mwanamke huyo atafute kila taarifa anayoijua kumhusu ajenti yule wa Secret Service ambaye alipotea kwenye mazingira ya kutatanisha!
Aliponiuliza sababu, nikamwambia kwa ufupi tu, bwana huyo yu hai na yupo Ujerumani.
“Kweli?”
“Ndio, na anashirikiana na Alfonso.”
“Sawa. Nitalifanyia kazi!” akamalizia Daniele kisha akakata simu.

**

Nikiwa nimeamka na kuoga, Daniele akanipigia simu na kunipatia taarifa zote ambazo amezipata toka kwa yule ajenti. Kumbe jina lake ni Ian Livermore. Amefanyia kazi USSS kwa takribani miaka sita.
Kuhusu familia yake, haikuwa inajulikana. Hakuwa na mke wala mtoto, wazazi wake inasemekana walishafariki miaka kadhaa huko nyuma.
Na kuhusu akaunti zake nazo zilishafungwa. Hakuna rekodi yoyote ya kuingia wala kutoka kwa pesa tangu iliposemekana kuwa amekufa!
Mambo hayo kidogo yakanivunja moyo. Sikuona mwanya wa kupata chochote kitu hapo, ila kwa mwishowe Daniele akanipa tumaini. Anamfuatilia rafiki yake na bwana huyo Ian akitarajia kupata kitu toka kwake.
“Mpaka jioni ntakuwa na la kukwambia!” akamalizia vivyo kabla ya kukata simu.
Nami kuendeleza upelelezi wa hilo jambo, nikaanza kutulia kuangaza yale makabrasha ambayo niliyapiga picha kule kwenye nyumba ya Alfonso. Nikitazama na kukagua vema, kuvuta picha kwa ukubwa na kwa udogo.
Mojawapo ya nyaraka hizo nikagundua ni mkataba. Mkataba huu aliusaini ndugu mmoja anayeitwa Bevin Casen na Alfonso Lundergan. Ulikuwa ni mkataba wa mashirikiano kwa makubaliano ya kulipwa ujira wa takribani dola za kimarekani milioni moja kila mwezi!
Huyu Bevin Casen ni nani? Nikapata maswali. Nikaendelea kupekuapekua na kuja kubaini kuwa pia kulikuwa na mawasiliano ya bwana Ian. Hapa nikajikuta natabasamu. Angalau nilipata pa kuanzia kumtafuta mtu yule.

**

“Ndipo hapa!” akasema dereva uber. Nami kabla sijafanya lolote nikatazama eneo hilo kwa wepesi alafu nikalipia na kutoka ndani ya gari.
Nikatembea kuvuka barabara. Ila hamaki, gari likaja kwa upesi mno likilenga kunizoa! Nikalikwepa upesi ila likanisukumia kando kwanguvu mno! Sijajikusanya, risasi zikatupwa kwa fujo kunifuata! Moja ikajeruhi paja langu la kushoto!
Nikajitahidi kunyanyuka, nikipuuzia maumivu, nikakimbia kidogo, ila napo kabla sijafika popote, nikadungwa risasi ya mgongo. Nikapoteza nguvu na kuanguka.

**
 
*NYUMA YAKO – 24*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Nikatembea kuvuka barabara. Ila hamaki, gari likaja kwa upesi mno likilenga kunizoa! Nikalikwepa upesi ila likanisukumia kando kwanguvu mno! Sijajikusanya, risasi zikatupwa kwa fujo kunifuata! Moja ikajeruhi paja langu la kushoto!
Nikajitahidi kunyanyuka, nikipuuzia maumivu, nikakimbia kidogo, ila napo kabla sijafika popote, nikadungwa risasi ya mgongo. Nikapoteza nguvu na kuanguka.
ENDELEA
Sikufahamu nini kiliendelea baada ya hapo, wala sikujua nilikuwa siko fahamuni kwa muda gani, nilikuja kuamka nikiwa eneo la giza! Sikuwa naona mbele wala nyuma yangu, kushoto wala kulia!
Nikiwa nahema kwanguvu, nikakodoa lakini haikusaidia. Nilikuwa nimefungiwa kitini nisiweze kunyanyuka wala kujitetea. Na kiti chenyewe kilikuwa kimesimikwa chini kiasi cha kutoweza kukinyanyua!
Nikajaribu kukumbuka nini kilitokea mara ya mwisho, sikuambulia kitu bali maumivu ya kichwa. Sikuwa nakumbuka jambo lolote. Kitu pekee nilichoambulia ni kuhisi maumivu kwenye paja langu la kushoto. Nilikuwa na jeraha hapo, nilihisi hilo, lakini sikuweza kugusa sababu ya mikono yangu kufungwa. Na pia, nilikuwa nahisi maumivu mgongoni.
Mengine hayo sikuwa naweza ku … mara mlango ukafunguliwa na kusababisha mwanga mkali kuzama ndani na kunichapa usoni. Haraka nikafunga macho yangu na kuyaminya kwanguvu kujitetea na mwanga ule mkali hivyo sikupata kumwona aliyeingia. Lakini nikajua muda ule ulikuwa ni mchana.
Mlango ulipofungwa, taa zikawashwa kufukuza kiza kile ndani. Hapo ndipo nikamwona mtu yule aliyekuja kunisabahi. Alikuwa mwanaume mrefu mwenye mwili mpana. Alivalia suruali ya jeans, koti la ngozi jeusi, na tisheti ya bluu kwa ndani ikiwa imeandikwa maneno ya njano – “GO https://jamii.app/JFUserGuide YOURSELF!”
Mwanaume huyo akasonga karibu yangu akivuta kiti alichokitwaa konani. Akakigeuza kiti hicho na kuketi akin’tazama. Alikuwa ni mwanaume mwenye miba ya ndevu mashavuni na kidevuni. Nyusi zake pana na lips zake nyembamba, kidogo zikiwa zimemezwa na hii miba ya ndevu.
Hapa kabla mwanaume huyo hajasema jambo, nikafahamu kinachoenda kutokea. Mazingira haya hayakuwa mageni kwangu. Nimeshapitia mazingira kama haya maishani mwangu, kama si mara nne basi tano. Angalau nikaanza kuvuta kumbukumbu. Na kumbukumbu zangu hizo zikanambia kuwa mazingira hayo huwa hatarishi.
Huwa yanaambatana na maumivu ya mateso kumlazimisha mtu kuongea kitu ambacho aidha anakijua ama hakijui. Anachohusika nacho ama lah! Lakini sasa mimi nitaeleza nini na kumbukumbu zangu bado hazikuwa zimenijia kichwani?
Si hicho kilichokuwa kinanipa hofu, bali pia hali ile nlokuwamo ilikuwa ni tishio kwa usalama wangu kwani naweza jikuta nikitoa taarifa ambazo hazitakiwi kutolewa kwa adui!
Unajua kabla ya kutumia ujuzi wa kudanganya na kulaghai lazima kwanza uwe unaujua ukweli ili ufahamu namna gani ya kuumba katika njia nyingine ya tofauti ambayo inafanana nayo. Sasa mimi sikuwa naujua huo ukweli. Nilitaraji bwana huyu angenitesa sana kuutoa mwilini mwangu, lakini angeambulia damu tu.
Ila … mawazo haya yalikuwa kinyume. Bwana yule baada ya kunitazama, akaniuliza, “Unanikumbuka?”
Nikatikisa kichwa, “Hapana.” Akatabasamu kisha akapitisha ulimi wake kusafisha meno. Ungepata kuuona ulimi huo kwenye lips zake ukiwa unatembea.
Akaniuliza tena, “Unakumbuka mara yako ya mwisho ulikuwa wapi?”
“Hapana,” nikamjibu.
“Nini unakumbuka?” akaniuliza.
“Mazingira haya,” nikamjibu. “Nadhani sio mageni.”
“Yapi?”
“Haya ya kufungwa kamba kitini, na mtu kukaa mbele yangu.”
Akan’tazama kidogo alafu akanyanyuka aende zake. Nikamwita, “Tafadhali niambie hapa nipo wapi na nafanya nini?”
Akan’tazama asiseme kitu alafu akaenda zake. Akaufungua ule mlango na kupotea ila saa hii akiwa ameacha taa zinawaka. Nikaangaza huku na huko ndani ya mahali nilipo. Hakukuwa na kitu isipokuwa meza na kiti upande wangu wa kulia, tena kwa mbali.
Chumba kilikuwa cheusi na kisicho na dirisha. Ila kulikuwa na na viyoyozi ambavyo vilikuwa vinamwaga kipupwe cha baridi. Nikajiuliza hapa ni wapi? Kabla sijapata majibu, tena hata sijachukua sekunde tano, mlango ukafunguliwa akaingia mwanaume mwenye kimo cha kati akiwa anaongozana na mijibaba miwili kwa nyuma.
Mwanaume huyo alikuwa na mustachi mweupe kama nywele zake za kichwani. Amevalia miwani ya jua na mkononi mwake ameshikilia sigara kubwa. Suruali nyeusi na buti kubwa huko chini.
Akasimama karibu yangu, kiti na ile meza vikasogezwa karibu naye. Hapa ndiyo nikajua kumbe vitu vile vilikuwa vimetengwa kwa ajili yake. Lakini mbona hakuja yeye mwanzoni na badala yake akaja yule mwanaume mwingine?
Akili yangu ikaniaminisha kuwa bwana yule alikuwa ametumwa aje kun’tazama kwanza kama najua jambo lolote, kama nakumbuka kitu, na alipoona hilo limefaulu ndipo akaja huyu.
Kwahiyo hawa ndiyo watakuwa wanahusika na kupotea kwangu kwa kumbukunbu, nikaamini hilo. Nikamtazama bwana yule, naye akintazama akaketi. Akanyonya sigara yake kubwa alafu akantemea moshi pasipo adabu!
Akaita, “Kijana!” nami nikamtazama pasipo kumsemesha.
“Najua haukumbuki jambo, nami nipo hapa kukupatia machaguzi mawili ambayo ni juu yako kuchagua.” Aliposema hayo akavuta tena sigara, na tena pasipo adabu, akanipulizia usoni mwangu. Nilimtazama kwa hasira sana na kama ningekuwa na uwezo ningemdaka na kumfunda nidhamu!
“Moja, ufanye kazi na sisi ukapate nyumba ya kukaa, ama mbili, tukuache ukarande mtaani ukiwindwa kama swala!”
Nikashangazwa na hiyo kauli. Kwani wanadhani sina pa kwenda? Nikajiuliza. Wanadhani mimi ni mzururaji au? Wanadhani sina makazi wala kazi ya kufanya?
Nikawauliza, “ninyi ni wakina nani na kwanini mmenikamata?”
Bwana yule akaniambia, “Sipo hapa kwa ajili ya kuulizwa maswali na wewe. Nipo hapa kukupatia nafasi ya pili, kama uko tayari, sema, na pia kama haupo tayari.”
“Nitakubalije kitu nisichokifahamu?” nikawauliza. Yule bwana hakujali swali langu, akanyanyuka na kwenda zake kuufuata mlango. Nikapaza sauti, “Ngoja!” akasimama pasipo kunitazama akiendelea kuvuta sigara yake.
“Nimekubali,” nikamjibu. “Nimekubali kufanya kazi nanyi!” basi bwana huyo akarejea pale kitini kisha akazamisha mkono wake ndani ya mfuko wa koti na kutoa kikopo kidogo chenye tembe nyeupe, akasema, “Unaona hiki?” akitikisa hiko kikopo. “Ni dawa ya kurejesha kumbukumbu zako, na ukifanya kazi yetu kwa takribani juma moja tu, kazi moja tu, utapewa tembe hizi ukaendelee na maisha yako na pesa nyingi mkononi.”
Aliposema hayo akavua miwani yake, hapo ndipo N jicho moja lililobovu, la kulia, na pia tattoo ya chozi jicho la kushoto.
“Deal?” akaniuliza.
Mimi nikamjibu kwa kumtikisia kichwa.

**

Leo nilikuwa najua ni siku gani na muda gani tofauti na ile jana yake. Nilipewa chai nzuri na muda wa kupumzika kwenye chumba ambacho ni ‘luxury’ chenye kila kitu akitakacho binadamu. Na pia jeraha langu lilipewa dawa na kufungwa bandeji.
Sasa ningeweza kutembea, na nadhani hata kukimbia, kwani nilihisi maumivu kwa mbali, na nilitambua kuwa jeraha hilo halikuwa lililonichimba sana. Kama ndani ya majuma mawili ama matatu laweza likawa limepona kabisa.
Nikiwa hapa sebuleni, baada ya kunywa chai, nikaendelea kuwazia kitu ambacho bado sikuwa nakipatia majibu. Hapa nipo wapi? Hawa watu ni wakina nani? Wanataka nini kwangu?
Na kubwa zaidi MIMI NI NANI?
Nikaja tu kuamini kuwa kujiuliza maswali hayo ni kupoteza muda tu maana nisingepata majibu abadani. Inabidi nipate zile tembe. Tembe za kumbukumbu. Lakini sasa nita ….
Ngo! Ngo! Ngo! Sijajibu, mlango ukafunguliwa, akaingia yule mwanaume aliyekuja kunipa chaguzi jana yake kwenye kile chumba. Kama kawaida alikuwa anaongozana na wanaume wawili waliojaza misuli, akaketi kwenye kochi litazamanalo na langu kisha akaniuliza, “Unaendeleaje?”
“Naendelea vizuri,” nikamjibu pasipo kutia neno lingine.
“Sasa upo tayari kwa kazi yetu?” akaniuliza.
“Kazi gani hiyo?” nami nikamuuliza. Akan’tazama kwanza kabla hajavua miwani yake.

***
 
*NYUMA YAKO – 25*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
“Naendelea vizuri,” nikamjibu pasipo kutia neno lingine.
“Sasa upo tayari kwa kazi yetu?” akaniuliza.
“Kazi gani hiyo?” nami nikamuuliza. Akan’tazama kwanza kabla hajavua miwani yake.
ENDELEA
“Kumuua balozi!” akaniambia kwa sauti kavu. Nikatoa macho, “balozi gani?”
“Balozi wa Marekani!” akanijibu kana kwamba ni kazi ya kumuua kuku kisha akanipatia na muda, “ndani ya siku tatu kazi hiyo inabidi iwe imeshakwisha kufanyika.”
Mimi nikatikisa kichwa. “sitaweza.”
“Unasema?”
“Sitaweza!” nikarudia kauli yangu. Basi bwana yule akazamisha mkono wake ndani ya koti na kutoa kile kijichupa cha tembe na kunambia, “Ni uchaguzi wako, kufanya kazi yetu ama kwenda ukawe mbwa huko mtaani!”
“Ni sawa!” nikawajibu kwa kiburi. “Niachieni huru ila siwezi kwenda kumuua mtu ambaye sijui sababu yake ya kifo!”
Basi bwana yule akan’tazama kwa kukunja ndita alafu akawatazama wale wenzake wawili. Akanyanyuka akitaka kwenda zake.
“Niambie mimi ni nani!” nikamwomba.
Akanitazama pasipo kunisemesha kitu, akaondoka akiniacha na wale wanaume wawili waliojaza miili. Wanaume hao wakanisomba na kwenda kunitupia nje ya nyumba, huko barabarani, alafu kabla hawajaondoka mmoja wao akanambia, “akili itakapokukaa kichwani, unajua pa kurudi!”
Sikumjali nikaenda zangu.
Nikatembea ndani ya jiji la Berlin likiwa jipya kabisa machoni mwangu, sijui wapi pa kwenda wala pa kuelekea. Nikazunguka kwa kama masaa matatu kabla sijajikuta ufukweni nikiwa nimechoka.
Sikuwa nakumbuka kitu! Nilidhani nitakumbuka lolote kwa kutazama watu na majengo lakini haikuwa kama nilivyowaza. Sikukumbuka hata tone ya jambo. Nikawaza niende hospitali na kuwaelezea shida yangu pengine watanisaidia lakini mfukoni sikuwa na pesa. Ni vipi watanielewa?
Hapo ndipo nikakumbuka hata pesa ya chakula sikuwa nayo. Na nilipokumbuka hayo tu, nalo tumbo likanguruma! Nikaona nifanye stara kutafuta kazi yoyote ile ambayo itanipatia hata vijisenti kabla jua halijazama na kiza kutawala.
Nikatafuta kwa kupita huku na huko, ila sikufanikiwa kupata kitu, kila nilipoenda hata kuomba kusafisha vyombo, waliniambia hawahitaji watu. Mpaka giza linaingia, sijapata kitu. Tumbo likawa linadai haswa.
Sikuwa na namna bali kulala vivyo hivyo huko ufukweni. Nilitafuta mahali ambapo pangenikinga kidogo na upepo mkali wa bahari, kakibanda, nikajiegesha hapo nikijikunyata.
Nikawaza sana sana pasipo mafanikio. Mwishowe usingizi ukanibeba, ila ukiwa ni wa kukatakata. Nadhani sababu ya njaa na kuhisi sipo eneo salama.
Ukiwa ni usiku mzito, kama majira ya saa saba hivi, nikiwa nimefumba macho yangu, nikasikia sauti ya mwanamke ikipiga kelele. Nikashtuka na kuketi kitako upesi. Nikatazama kushoto na kulia, sikuona kitu!
Sauti hiyo ikaendelea kulia na kunifanya ninyanyuke kuangaza maana ilikuwa inaomba msaada. Niliposkiza vizuri nikatambua inatokea upande wangu wa mashariki, upesi nikakimbilia huko, kidogo nikawaona wanaume wawili, mmoja alibebelea rungu la baseball na mwingine ana kisu wakiwa wanamkimbiza mwanamke fulani mnene.
Kidogo wakamkamata mwanamke huyo na kumtupia chini! Mmoja akampokonya mkoba wake kwanguvu na kumwamuru anyamaze kimya.
Hapo ndipo nikaona kuna haja ya kwenda kumsaidia mwanamke yule. Nikasonga pasipo kujiuliza mara mbilimbili mpaka karibia na eneo ambalo wapo. Nikapaza sauti, “Hey! Mwachieni mwanamke huyo huru!” nilikuwa natumia lugha ya kijerumani. Hicho sikuwa nimekisahau. Basi wanaume wale wakanitazama na kushtuana kwa mmoja kumgusa mwengine bega kisha wakajiandaa kwa kukamatia silaha zao.
Mmoja, yule mwenye kisu, akanifuata kwa pupa. Akatupa mkono wake wenye kisu, nikaukamata na kuuvunja alafu nikamviringita na kumpatia teke kali la tumbo, akarukia huko!
Mweziwe kuona hivyo basi naye kurupu akanifuata na rungu lake, naye nikamkabili kwa wepesi kabla sijampokonya rungu lake na kumwadhibu nalo kwanguvu mara tatu, akabaki hapo chini akilalamia maumivu. Kwanguvu nikampokonya mkoba wa yule mwanamke na kumfuata mhanga kumjulia hali.
Mwanamke huyo kanambia yupo sawa, ni maumivu kidogo ya mgongo ndiyo alikuwa nayo. Nikampatia mkoba wake na kumtakia usiku mwema lakini kabla sijaenda akanishukuru sana na akaniuliza,
“Mtu mwema kama wewe wafanya nini usiku huu hapa?”
Nikatabasamu kidogo kabla sijamwambia jibu ambalo kwa namna moja lilimshangaza, “Sina makazi.”
Akan’tazama kwa huruma.
“Kweli?”
“Ndio, nalikuwa nimelala kule ufukweni kabla ya kusikia sauti yako ikiomba msaada.”
Akan’kagua upesi kabla hajatabasamu usoni mwangu.

**

“Hapa ni kwangu!” alisema akinifungulia mlango. Ilikuwa ni nyumba ya ukubwa wa wastani ikiwa imefumbwa na uzio mwepesi wa nondo zilizojenga mistari. Tokea eneo lile ambapo tukio la kukabwa lilitokea mpaka hapa ni kama umbali wa nusu maili.
“Karibu sana, jisikie huru!” akanambia akionyesha meno yake madogo.
“Ahsante!”
Nikaketi kochini na kuangaza kidogo sebule yake ndogo iliyopambwa vema. Nikamuuliza, “Waishi mwenyewe hapa?”
“Hapana, nipo na wanangu. Watakuwa wameshalala.”
Akaketi na kuvua viatu vyake. Akanishukuru tena na kisha akanambia, “kama isingalikuwa gari langu kuharibikia huko mbali nisingekuwepo pale kwa miguu. Lakini Mungu wa ajabu, alimtuma malaika wake kuniokoa.”
Nikatabasamu nisiseme kitu. Akan’tazama na kuniuliza, “Imekuaje hauna makazi?”
“Hata nikikueleza sijui kama utaamini,” nikasema kabla sijatazama chini. Akan’toa hofu,
“Usijali, ntakusikiliza.”
“Sijui kwanini sina makazi,” nikamjibu. “Sijui kwanini nipo kwenye hali hii. Sikumbuki kitu chochote!” nikamweleza kisha kukawa kimya kidogo.
“Nashukuru maana unenisaidia,” nikamweleza nikimtazama. “Sikuwa na pa kulala. Naomba unisaidie kwa kipindi kifupi, natumai kumbukumbu zangu zitarejea na kila kitu kitakuwa sawa.”
“Usijali,” akaniambia akinitikisia kichwa. “Utapumzika hapa na tutaangalia cha kufanya.”
Basi hatukukaa hapo sana maana ulikuwa ni usiku mkubwa na alitaka kupumzika. Akaniacha mimi pale sebuleni yeye akienda chumbani. Nikalala hapo mpaka asubuhi ambapo niliamshwa na makelele ya watoto.
Nilipofumbua macho nikamwona mtoto wa kiume na wa kike. Walikuwa wa makamo sawa, kama miaka mitano hivi. Walinitazama kwa mashaka kabla hawajaendelea na mbio zao kuelekea nje.
Kidogo akaja msichana wa miaka kumi na, akanisalimu na kisha akaenda zake. Alikuwa amevalia begi mgongoni. Nadhani alikuwa anaenda shule ama chuo. Naye alinitazama kwa maulizo kabla hajapotelea zake.
Nilipokaa hapo kwa muda kidogo, ikiwa ni majira ya saa tatu asubuhi kwa mujibu wa saa ya ukutani, mwanamke yule mwenye nyumba akanijia. Alikuwa ana tabasamu usoni mwake japo machoni bado usingizi ulikuwa umemjalia.
“Umemkaje?”
“Salama. Vipi wewe?”
“Salama tu. Ule pale ni mlango wa bafuni na choo. Waweza kwenda kuoga kisha upate kifungua kinywa.”
“Ahsante.”
Nikafuata maelekezo yake kwenda huko. Nikiwa bafuni nakoga, kama baada ya dakika tano tu, nikasikia mlango wa bafu ukigongwa kwa nguvu. Sijaitikia, yule mwanamke akafungua na kunisihi kwa sauti ya woga. “Usitoke humu ndani ya bafu. Tafadhali!”
Hakuwa ananitazama, bali akirushia macho yake pembeni asinione uchi. Kabla sijamuuliza chochote, akawa ameshatoka na kuufunga mlango akiniacha na maswali.
Sikuendelea kuoga tena.
 
*NYUMA YAKO -- 26*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Nikafuata maelekezo yake kwenda huko. Nikiwa bafuni nakoga, kama baada ya dakika tano tu, nikasikia mlango wa bafu ukigongwa kwa nguvu. Sijaitikia, yule mwanamke akafungua na kunisihi kwa sauti ya woga. “Usitoke humu ndani ya bafu. Tafadhali!”
Hakuwa ananitazama, bali akirushia macho yake pembeni asinione uchi. Kabla sijamuuliza chochote, akawa ameshatoka na kuufunga mlango akiniacha na maswali.
Sikuendelea kuoga tena.
ENDELEA
Nilitega masikio yangu nipate kusikia kinachojiri. Nilisonga karibu na mlango nikiwa nimejiveka taulo kwa dharura ya lolote litakalotokea basi lisinikute uchi. Niliposkiza kwa ufupi nikajua kuna magombano, watu wawili walikuwa wanazoza kwa kutumia lugha ya kijerumani, mmoja mwanaume ambaye sikumtambua kwa sauti yake na mwingine mwanamke ambaye ni wazi alikuwa ni yule mwanamke mwenyeji wangu.
Kama haitoshi magombezano hayo yaliambatana na kuvunjwa kwa vitu kadhaa.
“Yuko wapi?” Mwanaume alifoka. “Nasema yuko wapi? Sema kabla sijakuua!” Baada ya hapo nikasikia sauti ya kofi na yowe toka kwa mwanamke. Kidogo nikasikia sauti ya kishindo cha mtu na mara mlango wa bafuni nilimo ukafunguliwa kwanguvu! Uso kwa uso nikakutana na mwanaume mpana mrefu aliyekuwa amefura haswa.
Alinikodolea na kusema akininyooshea kidole, “Umekwisha!” Akazama ndani ya bafu na kujaribu kunishambulia. Nilimsihi aniskize lakini hakuwa tayari, alidhamiria kuniumiza ama tuseme kuniua kabisa, hivyo ikanipasa nitetee uhai wangu.
Sikuhangaika naye sana, alikuwa ni mtu mwenye ‘maguvu’ mengi na mzito. Nilifanikiwa kumkabili kwa mapigo matatu akawa yu chini hoi. Nikatoka bafuni na kwenda kukutana na yule mwanamke mwenyeji wangu, yeye alikuwa amelala chini akiwa analia.
Nikamnyanyua na kumtazama, uso wake ulikuwa unavuja damu, alikuwa amjeruhiwa vibaya. Nikamsihi nimpeleke hospitali lakini hakuwa tayari kabisa badala yake akawa ananishauri niondoke upesi kwa usalama wangu.
“Nenda, nitakuwa salama usijali!” Aliniambia akinisukuma, lakini ningemwachaje vile? Nilimwomba aende hospitali basi hata pale nitakapoondoka, bado akaendelea kunisisitiza niende na saa hii akinipa vitisho, “atakumaliza yule! Si mtu mzuri kabisa!”
Akiwa analia akanambia kuwa watoto wake walikutana na baba yao huyo na kumwambia kuwa yupo na mwanaume nyumbani. Alikiri mume wake ni mhalifu na mkatili, ni mtu ambaye hafikirii mara mbilimbili kummaliza mtu.
“Nisingependa nikuweke matatizoni, tafadhali nenda.” kauli yake hiyo ilinisababishia maumivu makali kwani niliona mimi ndiye nilimsababishia matatizo. Nilitamani sana kumsaidia, roho yangu haikuwa radhi kabisa kumwacha hapo. Lakini kwasababu ya shinikizo lake nikaona nitimize agizo lake. Nikanyanyuka na kujongea mlango, nikajiendea.
Nilipiga hatua kumi na mbili, kama nipo sahihi, mbali na eneo lile. Ghafla nikasikia makelele ya mwanamke toka kwenye nyumba ile, hapo nikasita nikisimama na kuwekeza jitihada kwenye masikio yangu. Alikuwa ni yule mwanamke anapigwa, halikuhitaji elimu kulibaini hilo. Sikuweza kuvumilia, basi nikarejea kumsaidia.
Nilifungua mlango kwa pupa na kuangaza. Nilichokiona ni yule mwanaume akiwa amemshika mwanamke yule nywele zake, mkono wake ukiwa unachuruza damu. Nikamwamuru, “Mwachie huyo mwanamke upesi!” nikamwamuru nikiwa namkodolea haswa. Mapigo yangu ya moyo yalikuwa yanaenda mbio kwa hasira. Nilimwona mwanaume huyu ni mnyama kabisa.
Kwa kiburi, akaniambia, “Utanifanya nini nisipomwacha?” kabla sijajibu nilimwona mwanamke yule akipambana kunusuru nywele zake. Alikuwa anahisi maumivu, ungeliona hilo kwa namna alivyokuwa amekunja sura yake akiugulia na kugugumia.
“Usipomwacha nitakuadhibu kwa kipigo ambacho hujawahi pewa tangu uzaliwe!” nikamwambia nikimnyooshea kidole. Basi akamtupia kando yule mwanamke na kunifuata. Laiti angelijua niliyokuwa nimempangia kichwani mwangu basi asingediriki kupiga hata hatua moja karibu yangu. Niling’ata meno na kukunja ngumi, nikamwona akichomoa kisu nyuma ya mgongo wake.
“Nitakuua na kukufukia nyuma ya bustani. Na hamna mtu atakayekuja kuniuliza chochote!” alibwatuka, nami nisiseme kitu bali nikimngoja nimfundishe adabu.
Alipokaribia, naam, nikampa kitu roho inapenda. Nilimsubiri arushe kisu chake, nikaudaka huo mkono na kuutegua uache silaha kisha nikamvuta na kumwadhibu kwa kumtwanga ngumi nzito chini ya kidevu chake. Akiwa anapepesuka, nikamzika na teke zito lililonyanyua mwili wake mzito kwa kiasi chake na kisha kumbwagia chini. Alikuwa hoi asiyejiweza.
“Twende!” nikamwambia mwanamke yule nikimsogelea. Nikamnyanyua na kutoka naye ndani kwenda nje. Moja kwa moja nikamwongoza mpaka hospitali ambapo aliingia ndani kupata huduma mara moja. Uzuri alikuwa na kadi yake ya afya akiambatana nayo. Kumbe wakati mwanaume huyo anamdaka alikuwa yu njiani kujiondokea zake.
“Sasa kwanini haukutaka kwenda na mimi?” nikamuuliza. Alikuwa tayari amehudumiwa, kwa kiasi uso wake umefunikwa na bandeji.
“Nimeshakuambia, sitaki kukuingiza kwenye matatizo,” akaniambia akiwa ananitia huruma haswa. Nilikuwa naona hastahili yale anayopitia. Kila alipokuwa anateta neno moyo wangu ukawa unapiga kwa kunigusa.
“Matatizo yapi?” nikamuuliza. “Mume wako naweza kummudu, hawezi kunipa shida kabisa.”
Akan’tazama. Jicho lake la kushoto lilikuwa limefunikwa kiasi na bandeji.
“Unaweza kupambana naye lakini vipi kuhusu kundi lake? Hayupo mwenyewe!” aliposema hayo akapangusa pua yake kwa mgongo wa kiganja kisha akasema kwa sauti inayotikiswa na kilio.
“Watakusaka na kukuua kisha wakakutupie baharini. Nami sitaishi kwa amani tangu leo.”
Nikampa moyo, hatokumbwa na lolote mimi nikiwa hai. Ila kitu kilichokuwa kinanifikirisha ni namna gani atarudi kule kwake kwa yule mwanaume katili.
“Inabidi utafute mahali pengine pa kukaa, sawa?” nikamshauri. “Kuhusu watoto wako nadhani wataelewa maamuzi yako.” alipofuta makamasi mepesi yalokuwa yanamchuruza, akasema akiwa anatazama chini, “Wale si watoto wangu bali wa mume wangu.”
Hapa nikaona basi ni rahisi kwake yeye kuwa salama, lakini pia nikapata picha kwanini watoto wale waliweza kwenda kumpandikiza maneno baba yao huko walipokutana naye.
“Kwanini usiwe mwenyewe? Kwanini unaishi na mwanaume katili kama yule?”
Hapo ndipo nikajifunza kuwa mwanamke huyo hayupo kimapenzi na yule jamaa, bali kwa hofu. Yapata miaka mitatu iliyopita ndipo mahusiano yao yalianzia baada ya mwanaume huyo kumpoteza mke wake kwenye mazingira ya kutatanisha. Kwa muda wote huo alikuwa akiishi akijua mke wa mwanaume huyo alipata ajali, lakini siku moja alikuja kuubaini ukweli baada ya mwanaume huyo kumwadhibu na kumtamkia kuwa akiendelea kuwa mkaidi basi atammaliza kama alivyofanya kwa mkewe na kisha akamtupia baharini!
“Nisingeweza kumtoroka, mtandao wake ni mkubwa hapa Berlin. Ningejifichia wapi?” alimalizia kwa kauli hiyo akiwa anadondosha machozi.
Tuliondoka hapo hospitali tukaenda mahali pa kupumzikia alipopalipia kwa kutumia pesa yake mwenyewe. Huko tukakaa kwa siku mbili kwa amani kabisa, yeye akiwa kwenye chumba chake na mimi changu. Nilijitahidi kwa kadiri ya uwezo wangu kumjali lakini bado nikajiona napwaya. Nilihisi nahitaji kufanya kazi niingize kipato. Nisingeweza kumtegemea mwanamke huyo siku zote hizo.
Usiku wa siku ya tatu, pasipo kuaga, nikatoka na kwenda kwenye moja ya klabu ya usiku. Huko nikajitahidi kukutana na wafanyakazi wa klabu hiyo na kujinasibu nahitaji kazi ya kulinda eneo hilo.
“Wewe?” aliuliza mmojawao, jamaa mwenye mwili mpana na uso mwekundu. Sikio lake la kulia alikuwa amelitoboatoboa na hereni kadhaa. Mdomo wake mdogo ulikuwa umefichwa na ndevu nyingi mithili ya beberu asiye na matunzo.
“Ndio, mimi!” nikamjibu nikimtazama usoni pasi na kupepesa mboni. Basi akanitazama kwa sekunde kadhaa kisha akanipa ishara ya kichwa kuelekea upande wake wa kulia. Nikaongozana naye na punde nikajikuta ndani ya ofisi ndogo alimokuwa amekaa jamaa mwembamba ndani ya suti. Jamaa huyo hakuwa anaonekana vema kutokana na kuchezacheza kwa mwanga. Alikuwa anavuta sigara kubwa na amezungukwa na wanawake takribani saba ambao vifua vyao vilikuwa wazi.
“Vipi?” akamuuliza yule mwanaume aliyenileta, yule jamaa akajieleza kunihusu na kisha akakaa kando akiwa amefumbata mikono yake.
“Sogea karibu kijana!” yule jamaa akaniamuru. Niliposonga karibu zaidi ndipo nikamgundua bwana huyo, si kwa jina, lah! Bali umri wake. Alikuwa makamo sawa na mimi. Haikunishangaza kwa namna anavyoheshimika, alikuwa ni ‘mkuu’. Nadhani ndivyo ilivyo popote pale.
“Kipi kinachokufanya udhani unaweza kazi hii?” akaniuliza akinitazama. Niliona macho yake mara kadhaa mwanga ulipopita na kujiendea.
“Kwasababu naweza kupambana,” nikamjibu. Hiko ndicho kitu pekee ambacho nalikuwa na uhakika nacho kuwa naweza. Uzuri nilijithibitishia hilo mara mbili ama tatu hapo nyuma baada ya kupoteza kumbukumbu zangu zote.
Lakini bwana yule alionyesha wazi hakuniamini. Alimtazama jamaa yule aliyenileta na kisha akampa ishara ya kichwa, nikashangaa bwana huyo ananifuata.

**
 
*NYUMA YAKO --- 27*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Kipi kinachokufanya udhani unaweza kazi hii?” akaniuliza akinitazama. Niliona macho yake mara kadhaa mwanga ulipopita na kujiendea.
“Kwasababu naweza kupambana,” nikamjibu. Hiko ndicho kitu pekee ambacho nalikuwa na uhakika nacho kuwa naweza. Uzuri nilijithibitishia hilo mara mbili ama tatu hapo nyuma baada ya kupoteza kumbukumbu zangu zote.
Lakini bwana yule alionyesha wazi hakuniamini. Alimtazama jamaa yule aliyenileta na kisha akampa ishara ya kichwa, nikashangaa bwana huyo ananifuata.

ENDELEA

Kabla sijauliza bwana huyo akanikamata na kuninyanyua juu kisha akanikung’uta kichwa cha kifua na kunibwaga chini. Nilibanwa sana na kifua. Nilikohoa mara kadhaa nikijaribu kuvuta hewa kwa wakati huohuo. Sijakaa vema, bwana huyo kama mtu ambaye hakuridhika, akanifuata kwa upesi. Hapa ikanilazimu namna kujikomboa la sivyo nitapewa kadhia nisiyotarajia.

Upesi nikafyatua miguu yangu kufyagia miguu ya mwanaume huyo lakini sikufanikiwa, bwana huyo aliyumba kana kwamba meli dhorubani akitazamia kutafuta balansi. Nami nisimruhusu asifanye hivyo, nikajiamsha upesi na kumkandika teke! Bado hakudondoka. Aliyumbayumba sana. Nami saa hii sikumfanya jambo nikamwacha ajitulize.

Akanguruma kama simba akinitazama. Akakunja ngumi zake na kunifuata akipiga hatua kubwa. Aliponikaribia akatupa ngumi kama tano, zote nikazikwepa na kisha nikamtafutia nafasi ya kumkandika ngumi moja ya pua, akachuruza damu! Kuanzia hapo akawa haoni vema. Sasa nikafanya vile nilivyokuwa nataka mimi.

Nikapata fursa ya kumpa mapigo matatu na bwana huyo akalala usingizi mzito chini akiwa hajiwezi. Nikamtazama kwa uhakika, na mara nikasikia mtu akipiga makofi. Nilipotazama nikamwona yule jamaa aliyekuwa ameketi kochini akinyanyuka. Bado sigara yake ilikuwapo mdomoni.

“Safi sana! Safi sana!” akapayuka baada ya kutoa sigara kinywani. “Umepata kazi moja kwa moja.”

“Nashukuru sana!” nikamtazama na kuinamisha kichwa kidogo.

“Unaitwa nani? Sogea … sogea karibu!”

Nikasonga na kumtazama usoni. “Naitwa Tarrus,” nikajisemea jina la kwanza kuja kichwani mwangu.

“Tarrus!” akastaajabu. “Jina zuri kabisa! Kuanzia sasa utakuwa mlinzi wa chumba cha watu wa hadhi ya juu, sawa?”

“Sawa.”

“Sasa nenda nyumbani kesho uwapo hapa majira ya saa tatu usiku. Umenielewa?” aliuliza akiwa ameweka mkono wake begani mwangu.

“Ndio, nimeelewa,” nikamjibu na kwenda zangu. Nilifika kwenye makazi yangu majira ya saa nane kasoro usiku. Njiani kwenye basi watu walikuwa wakinitazama sana kwa kunihofu. Nalikuwa nimetapakawa na damu. Sikuwa naonekana sawa. Lakini sikujali, na kifuani mwangu kilichokuwa kinanifurahisha ni kwamba nimepata kazi, basi.

Nilimkuta mwenzangu akiwa amelala, na wala nisimsumbue nikajiendea kuoga na kisha nikapumzika. Kesho yake kwenye majira ya saa tatu asubuhi ndipo tukaonana na nikatambua kuwa mwanamke huyo alifahamu kuwa jana niliondoka.

Alinitazama kwa jicho fulani kisha akanywa fundo moja la hai na kuuliza, “Mbona hukuniaga?” nikamtazama kana kwamba sijui anachokiongelea.

“Ulitoka jana. Ulidhani sitajua?”

Nikatabasamu kisha nikanywa mafundo mawili ya chai iliyokuwa inaelekea kuwa vuguvugu, “Yah! Nilitoka mara moja. Nilitumai kurudi mapema.”

“Ulienda wapi?” akaniuliza akinitazama. Nilijihisi nafanyiwa usahili. Sikujua nini alikuwa ananiwazia kichwani ila ni bayana hakikuwa chema.

“Nilienda kutembea tu, kwani kuna shida?” nikatania, lakini bado sikuweza kuuvunja uso wake uliokuwa ‘serious’. Akiwa ananitazama, akasema, “Tafadhali usijiingize kwenye uhalifu.” hapa sasa nikajua nini alikuwa anawaza.

“Mji huu si rafiki wakati wa usiku! Tafadhali usije ukaingia kwenye hayo mambo!” aliendelea kusisitiza. Niliona namna macho yake yalivyokuwa yamebeba dhamira kubwa. Hakuwa anatania. Kwa muda kidogo nikapata kuwaza namna ambavyo mwanamke huyo anavyowaza kichwani mwake. Kwanini alikuwa anaongelea vile? Kwa namna moja ama nyingine nikakubaliana na nafsi yangu kuwa mwanamke huyo alikuwa ana kovu la uhalifu.

“Najua ninachofanya. Siwezi nikajihusisha na mambo kama unayoyawazia,” nikamtoa hofu.

“Unajua,” akadokeza na kusema, “Sikufahamu hata jina lako ni nani? Sijui hata wapi unatokea, ukipata matatizo utaniweka shidani … na ..” akaweka kituo kwanza. Niliona macho yake yakidondokea mezani akisema “… nitakuwa mpweke nisiye na amani.”

Nikamtazama na kutabasamu kwa mbali. Nikamshika bega lake na kumwahidi nitakuwa naye na nitamlinda kwa kadiri niwezavyo. Lakini kumtoa hofu zaidi nikamwambia kuwa nilienda kutafuta kazi na nimepata. Kuanzia siku hiyo majira ya saa tatu usiku nitakuwa natoka kwenda kazini.

“Nimelazimika kufanya hivyo, hali yetu haiwezi kuwa hivi milele,” nilimwambia nikiwa natazama macho yake. Alinishangaa kwa muda kidogo alafu akatabasamu kiuwongo.

“Unadhani hiyo ni kazi sahihi kwako?” akaniuliza.

“Sipo kwenye nafasi ya kuchagua kazi saa hii!” nikamwambia nikimshika mkono wake wa kushoto. “Tunachohitaji hivi sasa ni pesa. Tutaishije katika jiji hili pasipo fedha?”

“Najua …” akasema akiwa anatazama chini. Mara akanitazama na kuniuliza, “Utakuwa salama kweli?”

“Ndio, kwanini nisiwe?” nikamwambia kwa kujiamini. “Nitakuwa salama na wewe pia utakuwa salama, nimekwishakuahidi hilo. Umesahau?”

Hapa nikamwona akitabasamu kweli. Hakutia tena neo bali akaendelea kunywa zake chai. Yalipofika majira ya mimi kwenda kzi nikajiandaa na kumuaga. Akanisisitiza tena niwe salama. Nikamkubatia na kwenda zangu.

Nilipofika maeneo ya kazi nikaonana na yule jamaa aliyenipokea jana, yaani yule mwanaume mpana mwenye mwili niliyepambana naye. Uso wake ulikuwa mwekundu, pua yake ameifunika na bandeji. Akanitazama kwa macho ya paka na mbwa alafu akanionyeshea ishara ya kichwa. Nikaongozana naye mpaka kule kwenye ofisi ya yule mwanaume meneja. Tulimkuta akiwa ameketi kwenye kochi lake kama ada ila akiwa mwenyewe. Nadhani muda wa wale wasichana kuja haukuwa umefika au siku hiyo hakuwa na ratiba nao.

Mezani alikuwa na vileo kadhaa kana kwamba kuna tafrija ilhali yupo mwenyewe.

Huko nikapewa nguo ya kazi, tisheti nyeusi yenye maandishi meupe mgongoni, ‘SECURITY’, na pia vifaa kadhaa vya vya kufanyia kazi mathalani vifaa vya ukaguzi na pingu.

“Kuwa makini,” akaniambia yule bwana meneja. “Walinde wateja na sio uwaangamize,” akanipa angalizo kabla hajatoa ishara ya sisi kutoka humo chumbani. Tulipotoka tukaenda ndani ambapo watu walikuwa wakifurahia kwa kucheza muziki na kunywa. Huko tukasimama kana kwamba masanamu tukitazama watu wakiwa wanaburudika.

Hakika hii kazi inachosha, yaani wenzako wakiwa wanakula raha wewe umekaa kuwakodolea. Sikuwa na budi bali hivyo. Niliwakodolea kila pande mpaka mpaka pale yalipofika majira yangu ya kuondoka, saa kumi na moja asubuhi.

Nikiwa nimechoka kwa kusimama na kutembeatembea, nilipoketi kwenye basi nikajiona kama nipo peponi. Nilijihisi amani mpaka moyoni mwangu. Mwili ulipoa kabisa mifupa ya jointi ikihema.

Nilipofika nikamkuta mwanamke Katie, yule mwanamke ninayekaa naye, akiwa amekwisha amka. Alikuwa ameketi sebuleni akiwa anakunywa chai. Jina hili la Katie si jina lake halisia, nilimpachika tu kama vile ambavyo mimi nilijipachika jina la Tarrus. Niliona akitumia jina bandia litamsaidia kiusalama.

“Karibu!”

“Ahsante, mbona mapema sana?” nilimuuliza nikiketi kochini.

“Nilikuwa macho tangu saa kumi, nilidhani utakuja muda huo,” alinijibu akinitazama kana kwamba mama amtazamavyo mwanaye mpendwa.

“Uwe unalala tu!” nikamshauri. “Mimi nitarejea tu, hakuna tabu!”

Hakunijibu kitu, akatabasamu kisha akaendelea kunywa chai. Nilipotoka kuoga na kuketi naye ndipo akaniuliza ya kazini. Hali ilikuwa shwari kabisa, na kwa namna moja ama nyingine kila mmoja wetu alikuwa na matumaini juu ya siku za usoni.

Lakini siku moja …
 
*NYUMA YAKO --- 28*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Nilikuwa macho tangu saa kumi, nilidhani utakuja muda huo,” alinijibu akinitazama kana kwamba mama amtazamavyo mwanaye mpendwa.

“Uwe unalala tu!” nikamshauri. “Mimi nitarejea tu, hakuna tabu!”

Hakunijibu kitu, akatabasamu kisha akaendelea kunywa chai. Nilipotoka kuoga na kuketi naye ndipo akaniuliza ya kazini. Hali ilikuwa shwari kabisa, na kwa namna moja ama nyingine kila mmoja wetu alikuwa na matumaini juu ya siku za usoni.

Lakini siku moja …

ENDELEA

… Nilijawa na hofu sana. Ikiwa ni siku ya tano tangu nimeanza kazi, nilikawia sana kurudi nyumbani. Ikiwa ni majira ya saa kumi na moja kabla sijatoka, meneja akaniita akitaka kuonana na mimi. Siku hiyo kulitokea na vurugu kubwa toka kwa wanaume wanne walevi lakini nikajitahidi kwa uwezo wangu kuwamudu na kuwafanya wateja wawe salama. Meneja alinipongeza kwa kazi niliyofanya na kwa kiasi fulani akajawa na mashaka juu ya uwezo wangu huo.

Kwa muda kidogo akanifanyia ‘interview’ ambayo hapo awali hakunifanyia. Nilistaajabu kidogo. Alitaka kujua wapi nimetokea na nilikuwa najishughulisha na nini. Sikutaka kumwongopea, ila ni hakika ningemwambia kuwa sina kumbukumbu yoyote, asingeniamini. Hivyo basi kwa kubuni tu taarifa nikamwambia kuwa nilikuwa mwalimu wa mojawapo ya ‘gym’ hapo jijini. Na kwakuwa tulishindwana mahesabu ndipo nikaacha na kutafuta kazi nyingine.

Basi baada ya interview hiyo nikawa nimekawia kwa kama lisaa ama masaa mawili. Nilipofika nyumbani, tofauti na vile nilivyokuwa nimezoea, sikumkuta Katie. Mahali anaponywea chai palikuwa patupu na hata mazingira ya makazi yalikuwa pweke.

Nikaita pasipo na majibu. Nikagonga mlango wa chumbani mwake pasipo mafanikio. Nilipoufungua na kuangaza, sikumwona mtu. Nikajiuliza ni wapi atakapokuwa amekwenda. Kwa usalama wake nafahamu asingeliweza kutoka na kwenda kuzurura!

Nikapekua shuka lake na kubaini kulikuwa na damu. Nilipoenda bafuni na kutazama vema, nikabaini pia kuna matone ya damu karibia na mlango huo kwa ndani! Hapa nikajawa na mashaka sana. Nikatoka na kwenda kumuuliza mhudumu kumhusu Katie lakini naye akasema hakumwona.

“Uliona mtu yeyote akiingia ndani mbali na yeye?” nikauliza.

“Hapana, sijamwona yoyote,” akanijibu na kuongezea, “Labda kama yule mwenzangu atakuwa ameona vivyo. Yeye ameondoka hapa asubuhi ya mapema.”

Mbaya mimi na Katie hatukuwa na mawasiliano, nilishindwa hata kusema nimpigie simu na kumuuliza. Nikiwa hapo ‘counter’ kidogo nikakumbuka namna ambayo inawez kutusaidia. Nikimtazama mhudumu nikamuuliza, “Tunaweza tukaangalia kwenye cctv?” nikiwa nanyooshea kidole cctv kamera ambayo imetundikwa juu ya kuta konani. Yule mhudumu akatanua lips zake na kutikisa kichwa, “Hazifanyi kazi hizo!”

Nilipotaka kulaumu nikajikuta nikikumbuka gharama ya eneo hilo. Si bure ni bei nafuu! Nikadaka kiuno changu nikiwa nawaza kweli. Je nirudi kule nyumbani kwa Katie nikamtazame? … ama niripoti polisi?

Mmmh polisi? Hapa nikajiuliza mara mbilimbili. Vipi kama rekodi yangu ya nyuma si nzuri, si nitakuwa nimejipeleka mdomoni mwa mamba?

Nikangoja kama nusu saa, nilipoona bado kimya, nikajikusanya toka kwenye kiti cha maulizo na kuusongea mlango wa hoteli niende zangu nyumbani kwa Katie. Nikiwa nimeacha mlango wa hoteli kwa kama hatua tano, nikastaajabu kumwona Katie! Kwa upande wa mashariki ya hoteli alikuwa anasonga karibu akitembea upesi.

Nilimjongea na kuzama naye mpaka ndani. Nilimweleza shaka langu naye akanijibu alikuwa ametokea hospitali baada ya kuumwa ghafla.

“... hazikuwa siku zangu lakini nilimiminikwa na damu nyingi. Nilikuja kubaini hilo wakati naamka majira ya saa kumi. Nilidhani nitarejea kwenye hali yangu ya kawaida lakini haikuwa vivyo. Niliendelea kutokwa na damu tu. Nilikungoja lakini ulikawia, hivyo nikaona niende hospitali mwenyewe.” alipomaliza kusema hayo akanitazama na kisha akasema kwa sauti ya chini, “Samahani kama nilikusababishia hofu.” sauti yake hiyo ilinifanya niwe ‘mlaini’ katika namna ya ajabu. Niliishia kutabasamu na kusema, “Usijali.” alafu baada ya kumtazama kidogo nikamuuliza,

“Sasa upo sawa?”

Akanitikisia kichwa. “Nipo sawa, nashukuru.”

Siku ikawa imeenda vivyo. Lakini, katika namna ya ajabu, kuna muda fulani nikawa nawazia safari ya mwanamke huyo kwenda hospitali. Si kwamba nilikuwa siamini kama ameenda huko, lah! Bali nilikuwa natilia shaka usalama wake.

Vipi kama huko njiani akawa ameonekana? Au kuna mtu alikuwa anamfuatilia kubaini wapi anaishi? Basi nilijikuta nawaza na kupuuzia mawazo hayo …

Nawaza na kuyapuuzia.


**


Majira ya saa tatu usiku, klabuni …


Nikiwa kwenye majukumu yangu ya kila siku, si muda mrefu tangu nimewasili, mara mwanamke fulani mrefu akanijongea na kusimama karibu kabisa na mimi. Mwanamke huyu nikamtambua kama Jolene, mwanamke anayehudumu ndani ya klabu kwa kucheza mbele za wageni na hata siku zingine kuhudumu vinywaji kwa wale wageni wenye hadhi ya juu.

Mwanamke huyu alikuwa ni mrembo haswa, mwongeaji na pia mcheshi. Sikuwa nimezoeana naye, kiuhalisia sikuwa nimezoeana na mtu yeyote hapo, aidha walinzi wenzangu ama wanawake wa ndani. Mimi nilikuwa ni mtu wa kufanya kazi na kurudi nyumbani tu, hivyo kwa kiasi fulani nilishangaa kumwona mwanamke huyo akinijongea.

Akanitazama kwa kunirembulia alafu akasema, “Hellow handsome guy!” kisha akalamba lips.

“Una shida gani, Jolene?” nikamuuliza nikimkazia macho lakini hakuonyesha woga. Akanitazama kana kwamba pipi ya kijiti alafu akauliza kwa kuninong’oneza, “nikikwambia nina shida gani utanisaidia?” nikashusha pumzi ndefu kwa pua na kusema, “Jolene, nipo kazini. Waweza kuniacha tafadhali?” akanikonyeza. Akaweka kidole chake kwenye lips zangu na kisha akakipeleka kwenye lips zake alafu akajiondokea akinong’ona, “Tuonane baadae!”

Nikabaki namtazama mpaka anaishia. Sikuwa naelewa nini mwanamke huyo alikuwa ananiwazia kichwani. Nikiwa kwenye lindi hilo, mara nikasikia sauti ya kiume ikisema kando yangu, “Kuwa makini.” nilipotazama upande wangu wa kushoto nikakutana na mlinzi mwenzangu.

“Ni demu wake Mike. Nadhani unafahamu mahusiano yako na Mike yapoje,” aliposema vivyo hakungoja hata nimuulize, akaendelea zake na doria. Mike ni yule jamaa ambaye alinipokea na kunipeleka kwa meneja, kisha niapewa usahili wa kupambana naye. Sikutaka kuwazia sana hayo mambo nikaendelea na kazi yangu.

Kwenye majira ya saa kumi na moja alfajiri, nikarejesha vifaa vyangu vya kazi na kwenda kupata maji alafu nikabadili nguo niondoke. Lakini nikiwa naondoka, nikasikia sauti ya kike ikiniita. Nilipotazama nikamwona Jolene.

“Ningoje twende wote!” alipaza sauti. Sikumngoja nikaendelea na safari yangu. Huko nyuma yangu nikamsikia akikimbia. Aliponikaribia akaniuliza, “Una shida gani, Tarrus?” alikuwa amevalia suruali ya mpira inayombana, rangi ya kijivu, na topu rangi ya pinki aliyomechisha na raba zake mguuni.

“Mbona upo hivyo?” akaniuliza akinikunjia sura.

“Kwani unataka nini Jolene?” nikamuuliza. Akashika kiuno chake na kusema, “Nataka tu nikupongeze kwa kile ulichofanya jana. Kama isingekuwa wewe wale watu wangenijeruhi!”

“Usijali, ni kazi yangu,” nikamjibu vivyo na kwenda zangu, nyuma akanifuata. Nilipofika karibia na lango ndipo nikagundua Mike, akiwa amesimama na wenzake wawili kwenye sakafu ya juu, alikuwa ananitazama kwa umakini.


***
 
*NYUMA YAKO --- 29*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Mbona upo hivyo?” akaniuliza akinikunjia sura.

“Kwani unataka nini Jolene?” nikamuuliza. Akashika kiuno chake na kusema, “Nataka tu nikupongeze kwa kile ulichofanya jana. Kama isingekuwa wewe wale watu wangenijeruhi!”

“Usijali, ni kazi yangu,” nikamjibu vivyo na kwenda zangu, nyuma akanifuata. Nilipofika karibia na lango ndipo nikagundua Mike, akiwa amesimama na wenzake wawili kwenye sakafu ya juu, alikuwa ananitazama kwa umakini.

ENDELEA

“Jolene!” mara Mike akaita. Jolene alipogeuka na kutazama, akamwonyeshea Mike kidole cha kati kisha akaendelea zake na safari ya kunifuata. Tulikuja kuachana kwenye vituo vya basi mimi nikielekea upande tofauti na yeye. Njiani alikuwa akiniuliza maswali mbalimbali juu ya maisha yangu binafsi, wapi nakaa, nini napenda kunywa na kadhalika. Nilimjibu maswali yake hayo kwa neno moja moja tu.

Nilipofika nyumbani nikamkuta Katie akiwa ameketi kunisubiri. Siku hiyo nikajadiliana naye kuondoka mahali pale tulipokuwa tunaishi. Tunatumia pesa nyingi sana kukaa hapo tofauti na kama tungetafuta sehemu, hata kama ni ndogo, tukakaa vema.

“Ni wazo zuri, Tarrus!” akasema kwa tabasamu kisha akaniuliza ni wapi ningependelea kuishi.

“Katie, unajua fika mimi sina kumbukumbu hizo. Hata kama ningekuwa nazo bado nisingefaa kuchagua hilo. Unaonaje ukapendekeza wewe?” baada ya kufikiri kidogo akasema, “Vipi kama leo tukatembea mji huu na kuamua hilo kwa pamoja?” nikaona wazo lake ni jema. Basi nikapumzika na kwenye majira ya saa kumi kasoro jioni tukatoka kwenda kuutembelea mji tuone wapi patatufaa.

Tulifanya zoezi letu kwa kama masaa matatu, tukapata eneo moja zuri, nafuu na karibu zaidi kwa kazi yangu. Tukakubaliana na mwenye makazi kuwa malipo nitayafanya mwishi wa juma hilo, naye pasipo ajizi akanikubalia.

“Karibu sana,” akasema na kuongezea, “kama kutakuwa na mabadiliko yoyote basi mtanijuza.” tukamshukuru na kwenda zetu. Tukapitia mgahawani kupata chakula na kusogeza muda. Nilikuwa nimeazimia kupitia kazini moja kwa moja nikiachana na Katie.

Hapo tukala na kuongea kwa kama masaa mawili tena. Tulicheka na kupiga soga. Tuliteta na kunanga. Ilipowadia saa tatu ya usiku, nikaona nimuage Katie niende kazini naye aende nyumbani.

Lakini kabla sijafanya vivyo, nilihisi kuna mtu anatutazama. Mwanaume huyo mnene aliyekuwa amelaza nywele zake kwa ustadi alikuwa akitutazama kwa jicho la kando tokea upande wetu wa mashariki kusini. Sahani yake ndogo ilikuwa tupu kwa muda akijisomea gazeti.

“Unamjua mwanaume yule?” nikamnong’oneza Katie nikionyeshea ishara kwa mboni zangu za macho. Katie alimpotazama mwanaume huyo akanirejeshea uso na kutikisa kichwa. Niliona chembe za hofu usoni mwake. Sikutaka ahofie hivyo nikafanya namna ya yeye kupuuzia hayo, “Nimependa suti yake. Unadhani nitapendeza nikivaa vivyo?”

Akatabasamu na kuzungusha macho yake kutazama dari. “Kwanini umefikiria hivyo?”

Nikatabasamu.

“Kuna ubaya?”

“Hamna. Nadhani utapendeza, Tarrus. Inabidi uvae hivyo siku tukitoka tena.”

Nikatabasamu pasipo kumwonyesha meno alafu nikamtaka anyanyuke sasa twende. “Nitakusindikiza kwenda nyumbani.”

“Hautaenda kazini tena?” akawahi kuniuliza akinitolea macho yake kwa mbali.

“Nitaenda,” nikamjibu na kuongeza, “lakini nitajihisi mwenye amani nikikufikisha nyumbani.”

Basi tukajiendea zetu nikiwa makini kutazama kama jamaa yule atakuwa anatufuata. Sikumwona kabisa mpaka nafika nyumbani kumwacha Katie.

Nilipohakiki kuwa mazingira ni salama, nikajiondokea kwa kujiweka kwenye basi kwenda kazini moja kwa moja. Baada ya kuvuka vituo viwili ndipo nikamwona mwanaume yule niliyemtilia mashaka mgahawani akipanda basi hilo, mkononi akiwa ameshika gazeti lake.

Nilimtazama lakini yeye hakufanya vivyo. Aliketi kabisa mbele yangu na muda wote akawa anatazama mbele, kwa kadiri nilivyomtazama hakukuwa na muda ambapo alikunja shingo yake kun’tazama.

Basi kwasababu za kiusalama, nikaona itakuwa vema kama nikashuka kituo tofauti na kile cha kazini, endapo mwanaume huyo atakuwa ananifuata basi itakuwa rahisi kumpoteza.

Lakini je atakuwa ametufuatilia mpaka kule kwenye makazi yetu? Nilijiuliza.

Nikajongea mlangoni nikimtazama mwanaume yule. Bado hakunitazama. Nikashuka na kuanza kurusha miguu nikistaajabu kuona basi haliendi. Sikutazama nyuma. Kidogo nikahisi mtu anatembea.

Nikaongeza mwendo wangu maradufu, na baada ya kutembea kwa kama hatua thelathini nikatazama nyuma. Hapo ndipo nikakutana na yule mwanaume macho kwa macho! Alikuwa kama umbali wa hatua kumi na mbili tokea nilipo. Macho yake makubwa na mustachi mwembamba juu ya mdomo. Mkono wake wa kuume umebebelea gazeti.

Pasipo kuongea tukatazama kwa kama sekunde nne na mara mwanaume yule akapiga hatua moja kurudi nyuma na kisha akaanza kukimbia!

“Wewe ngoja!” nikabweka nikimkimbiza. Mwanaume huyo alikuwa ni mnene kwa umbo ila mwepesi haswa. Koti lake la suti pamoja na tai vilipepea akiyoyoma. Nilijitahidi kumkimbiza lakini bado akiwa ameniacha kwa umbali kiasi. Nilitumai atachoka karibuni hivyo sikukata tamaa.

Nilimkimbiza mpaka mahali ambapo niliona akizamisha mkono ndani ya koti lake la suti na punde akachomoa bunduki ndogo. Hapo upesi nikajibana kwenye ukuta, akageuka na kutupa risasi mbili kisha akaendelea kukimbia. Mulikuwa ni vichochoroni. Nilipokuja kutoka na kumfuatilia, nikawa nimempoteza! Sikumwona tena.


**


“Unakuja kazini saa hii?” ilikuwa ndiyo salamu niliyopewa na Mike. Alikuwa amesimama langoni yeye pamoja na wenzake wawili. Yalikuwa ni majira ya saa tano ya usiku.

“Kulikuwa na dharura,” nikamjibu nikitaka kuingia ndani. Akaniwekea mkono wake mpana kifuani mwangu akisema, “Si haraka hivyo!” nikamtazama kumsikiza.

“Sikia we boya, sawa? … kaa mbali na Jolene kabla sijatenganisha kiungo kimoja kimoja cha mwili wako na kumpa mbwa wangu. Tumeelewana?”

Nikamtazama kwa kama sekunde tano kisha nikasema, “Sina muda na wewe, wala huyo mwanamke wako, sawa? … alafu siku nyingine ukinifanyia huu ujinga, nitapoteza meno yako yote ya mbele. Tishia hao mbwa wako nyuma!”

Akataka kuanzisha mapambano lakini upesi wenzake wakawahi kumtuliza. “Hey Mike, huu si muda wa kufanya haya mambo! Chill!” akanitazama na uso wake mwekundu, mimi nikazama zangu ndani ya klabu pasipo kumjali. Nikabadili nguo zangu na kuchukua vifaa vya kazi, nikaanza kutazama usalama.

Nilipofanya kazi yangu kwa muda kidogo nikagundua kuna kitu hakipo sawa. Sikumwona Jolene mahali anapokuwa kila muda wa kazi. Sikujali sana lakini kadiri muda ulivyoenda nikiwa simwoni nikapata haja ya kutaka kujua.

Nikamfuata mmoja wa washirika wa Jolene na kumuuliza kumhusu mwenzake. Mwanamke huyo alikuwa ametingwa sana na kazi. Alinitazama kwa ufupi na kuniambia, “Kamtazame chumba chekundu.” kisha akaendelea na kazi zake.

Chumba chekundu ama ‘red room’ ni chumba ambacho wanawake hao wahudumu huwa wanakitumia kwa ajili ya maandalizi kabla ya kuanza kazi. Humo kuna nguo zao za kazi lakini pia na vifaa vya kujifanyia urembo.

Basi nikasonga huko, nilipofika karibu na mlango wa chumba hicho nikasikia sauti ya mwanamke ikiwa inagugumia kwa kilio. Nikagonga mara tatu kisha nikafungua mlango huo na kutazama ndani. Kwenye kona, godoroni, nikamwona mwanamke akiwa amejikunyata analia. Kwikwi zimemkaba akipambana kuvuta makamasi.

Mwanamke huyo nilimtambua kama Jolene.

Nikamjongea nikimuulizia hali yake. Hakuwa anajibu. Nilipomvuta kichwa na kumtazama, alah! Nikamwona akiwa ana majeruhi makubwa usoni na anatiririsha damu pomoni.

Nikahamaki sana na kumwonea huruma. Lakini zaidi nikapatwa na hasira. Sikumuuliza nini kilitokea kwani nilishafahamu. Nikanyanyuka na kuuendea mlango upesi! Damu yangu ilikuwa inachemka.


**
 
*NYUMA YAKO --- 30*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Mwanamke huyo nilimtambua kama Jolene.

Nikamjongea nikimuulizia hali yake. Hakuwa anajibu. Nilipomvuta kichwa na kumtazama, alah! Nikamwona akiwa ana majeruhi makubwa usoni na anatiririsha damu pomoni.

Nikahamaki sana na kumwonea huruma. Lakini zaidi nikapatwa na hasira. Sikumuuliza nini kilitokea kwani nilishafahamu. Nikanyanyuka na kuuendea mlango upesi! Damu yangu ilikuwa inachemka.

ENDELEA

Kama mbogo aliyejeruhiwa nikamwendea Mike aliyekuwa amesimama nje, nikakomea mbele ya uso wake nikimtazama kwa hasira. “Nisikie wewe mpumbavu!” nikapaza sauti yangu na kufanya watu kadhaa waliokuwepo hapo nje kunitazama. “Hili ni onyo langu la mwisho kwako. Onyo langu la mwisho, sawa? … ukimgusa yule mwanamke tena, kwa namna yoyote ile, nitakuvunjavunja usiamini macho yako. Nitakufanya hata mama yako mzazi asitambue maiti yako!”

Mike akaangua kicheko mpaka kuinama akiwa ameshika tumbo lake. Anacheka sana na hata wale wenzake waliokuwa nyuma wakamuunga mkono kwa kukenua. Walipomaliza, Mike akiwa bado ana makandokando ya kicheko, akanitazama na kusema, “we fala umesemaje?” kabla sijajibu akasema haya, “Nitamfanya chochote nitakacho na hakuna yeyote atakayeingilia. Si wewe wala mdudu yeyote!”

Alipomalizia kusema hayo alikuwa amesogea zaidi karibu yangu. Kwakuwa alikuwa amenizidi urefu basi akawa anan’tazama kwa chini akiwa amefuma ndita zake. Sikuwa namwogopa abadani, zaidi alikuwa ananipandisha hasira zaidi.

Nilijitahidi kwanguvu zangu zote nisifanye jambo la kipumbavu lakini niliona stara yangu ikiniponyoka. Nashukuru kabla ya kufanya jambo, kuna mtu akaja na kutuambia tunaitwa na meneja.

Kumbe meneja alikuwa anatutazama kwa kupitia kamera wakati tukiyafanya yote hayo.

Tukatoka na kuongozana mpaka ofisini kwa meneja, huko tukamkuta mwanaume huyo akiwa anatazama video zake kadhaa ambazo zinaletewa taarifa na kamera ambazo zimesambaa maeneo mbalimbali klabuni. Pamoja naye walikuwapo wanawake watano waliokuwa wamevalia chupi pekee, vifua wazi.

Hapo tukasimama kwa kama dakika moja pasipo meneja kutuongelesha. Alikuwa anavuta sigara yake kubwa akiwa anaendelea kutazama video zake.

Mike akanitazama kwa jicho baya na kunisemea jambo kwa kunong’ona. Nami nikamtazama pasipo kusema jambo. Kwa ufupi nikatoa macho yangu kwake maana niliona ningeweza kufanya jambo ambalo ningelijutia.

Ikiwa inaelekea dakika ya pili, meneja akageuza kiti chake na kutuuliza kama tumechoshwa na kazi. Alimpa kila mtu wasaa wa kujieleza. Mike akatumia muda wake kunikanda na kugusia namna ninavyomfuatilia na kumsababishia matatizo.

Ulipofika wasaa wangu, nikaeleza kwanini nalikuwa kwenye mgogoro na Mike. Mimi kama muajiriwa wa eneo hilo nalikuwa na jukumu la kuhakikisha usalama wa watu wote, ikiwamo na wafanyakazi wenzangu, hivyo nimezama kwenye mgogoro na Mike kwasababu tu ya kutimiza jukumu langu hilo.

“... Amemsababishia Jolene majeraha makubwa. Badala ya kufanya kazi yake, sasa amejifungia akilia na kugugumia chumbani!”

Niliposema hayo nikaona uso wa meneja ukibadilika. Alimtazama Mike na kumuuliza kama niyaongeayo ni kweli, Mike akakanusha. Basi upesi meneja akaagiza Jolene afike ofisini. Alipofika akamtazama na kuthibitisha kuwa mwanamke huyo alikuwa ameadhibika. Tena si kidogo.

“Nini kimekutokea Jolly?” Meneja akauliza akimtazama Jolene kwa macho ya kuguswa. Jolene alikuwa anatazama chini, bado akiwa amebanwa na kwikwi.

“Ni Mike,” Jolene akajibu kwa ufupi. Meneja akaagiza Jolene apatiwe huduma ya kwanza upesi, na akiwa amefura akamzaba Mike kofi kali na kumwonya, “Ukirudia tena kufanya huo upuuzi wako, nitakupoteza! Nadhani unanifahamu vizuri, Mike!”

Mike hakusema jambo. Alikuwa anatazama chini mikono akiwa ameifumbata nyuma.

“Na kuanzia leo, utakuwa chini ya Tarrus, sawa?” meneja akafoka. Akamfukuza Mike atoke ofisini, nikabaki mimi na yeye pekee.

“Sikia Tarrus,” Meneja akasema akiwa anaketi. Akaweka sigara yake mdomoni na kunyonya mapafu mawili kabla hajaendelea kuongea, “Nimekukabidhi majukumu makubwa, nadhani na wewe unalitambua hilo, si ndio? …” akavuta tena sigara. Hakuwa ameniuliza ili nijibu bali ahakikishe kwamba nipo naye pamoja.

“Kama kutakuwa na tatizo basi utaniambia, sawa? Mambo mengine tutayajadili kadiri siku zinavyoenda. Ila kuanzia sasa ukae ukijua kwamba siku yoyote, muda wowote naweza kukuita kwa ajili ya ulinzi, sawa?”

Nikatikisa kichwa kumkubalia.

“Usijali,” akasema uso wake ukiwa umefunikwa na moshi wa sigara. “Hata malipo yako nitayaongeza kuwa mara mbili na sasa.” aliposema hayo akaniruhusu nikaenda zangu. Sikuona kama kazi hiyo aliyonikabidhi ni kubwa sana, lah! Niliona ni yaleyale tu ya kila uchwao mpaka pale kesho yake nilipobaini majukumu zaidi.

Mwanamke mmoja afanyaye kazi ndani ya eneo hilo, alinijia nikiwa katika majukumu yangu akaniambia naitwa na meneja ofisini. Nilipofika huko nikamkuta meneja akiwa ameketi mwenyewe, ‘amekunja nne’.

Akaniambia kuna watu watafika hapo muda si mrefu na alikuwa anataka niwe naye karibu.

“Kuwa macho, Tarrus,” aliniambia sentensi fupi yenye uzito. Nilibaini alikuwa anamaanisha anachokisema kwa namna alivyon’tazama. Nami kumwonyesha tupo pamoja, nikamtikisia kichwa na kukaa bayana.

Muda si mrefu, kama baada ya dakika sita tu tangu tuongee, meneja akasema, “wameshafika,” akiwa anatazama moja ya runinga zake. Niliporusha macho yangu kuangaza, nikawaona watu wanne wakiwa langoni. Watatu walikuwa wamevalia suti nyeusi na mmoja akiwa amevalia shati la ‘beach boy’ pamoja na bukta. Haikuwia ugumu kufahamu wale watatu walikuwa ni walinzi wakimlinda yule bwana aliyevalia bukta.

Punde meneja akaniagiza nishuke chini na kuwaongoza wale mabwana mpaka ofisini. Nikafanya vivyo, muda si mrefu tukawa wote ofisini. Bwana yule aliyevalia bukta alikaa akitazamana na meneja, walinzi wake wakiwa nyuma yake. Mimi nilikuwa nyuma ya meneja. Mtu mmoja pekee.

Wakaongea kwa muda kidogo na mara meneja akafungua mojawapo ya droo yake na kutoa mifuko miwili yenye unga mweupe ndaniye. Akaweka mifuko hiyo mezani na kumtazama yule bwana. Hakumesemesha jambo lakini walielewana. Bwana yule akavuta mfuko mmoja na kuutoboa kwa kidole chake cha mwisho kisha akatia kidole mdomoni kuonja.

Baada ya muda kidogo akamwambia meneja kuwa pesa yake itatumwa punde atakapouza kitu hicho. Akiwa anasema vivyo akawa ananyoosha mkono wake achukue mfuko wa pili wa unga, mara meneja akamdaka mkono wake na kusema, “Hapana! Sitakubali iwe vivyo saa hii!” kisha akavuta mifuko yake karibu.

“Una shida gani, G?” akauliza yule bwana akiwa ameduwaa. Akawatazama watu wake kwa mshangao na kisha akarudisha macho yake kwa meneja. “Tangu lini hauniamini?”

“Tangu ulipokaa pasipo kunilipa kwa miezi sita sasa!” akafoka meneja na kuongezea, “sasa hivi sitafanya biashara kichaa na wewe tena.”

Yule jamaa akashusha pumzi ndefu kisha akafikiri kwa muda kabla hajasema, “Sawa, nitakupa pesa ya mzigo wako uliopita, alafu huu tutaongea zaidi mbele.”

Meneja akatikisa kichwa. “Utanipa pesa yangu, na huu hautaondoka nao mpaka uulipie!”

Kidogo kukawa kimya. Walitazamana kwa kama sekunde tano alafu yule jamaa akamgusa mlinzi wake mmoja kwa kiwiko, hapa nikawa ‘attention’ zaidi, mlinzi huyo akatoa mkebe na kuuweka mezani, ulikuwa umejawa na pesa.

Yule bwana akamwambia meneja atazame hizo pesa na yeye yupo radhi kumwachia kama watakubaliana. Bado meneja akashikilia msimamo wake. Mara hii akabamiza meza kwanguvu akiwa anafoka.

“Sirudii nilichosema, Lorenzo!”

Hapa nikaona mlinzi mmoja aliyekuwa ameambatana na yule jamaa akichomoa kitu nyuma ya kiuno chake.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom