Nyuma yako (Riwaya ya S. Mollel)

SteveMollel

JF-Expert Member
Jul 12, 2015
8,331
23,504
Ni muda sasa, natumai mpo poa wazee. Nimewakumbuka kweli na basi nilipopata muda kidogo wa kuandika, nikaona niwasalimu kwa Riwaya hii nzima na ya kijasusi ya NYUMA YAKO.

Nikiri kwamba muda wangu ulikuwa finyu kufanya jambo kubwa sana na niliandamwa na 'mafurushi' ya majukumu hivyo kupelekea mwendo wa kasi kwenye uandishi na uwasilishaji, lakini juu ya yote hayo, hautafadhaika.

Karibu hapa .... utasoma na kufurahia kwa kila n'takachotuma kwa mujibu wa ratiba yangu. Kama utaona wakawia, hamu imezidi subra, utanifuata pembeni nikuuzie yote kamili. Ni safari ya MISIMU MINNE.

NOTE: Nilishawahi ituma humu lakini haikukoma mpaka mwisho wake. Hii ni mara ya pili na itaenda mpaka kikomo.
 
*NYUMA YAKO --- 01*



Hongkong, China. 2018.
.
.
Jana nilikuwa ufukweni mpaka majira ya saa tisa za usiku. Nilikunywa pombe nyingi na kula pia, vyakula vya kichina nadhani wavijua, vingi vya ajabu, kama isingelikuwa ni kwa ushawishi wa rafiki yangu, Jack Pyong, haki nisingetia mdomoni chochote kile kati ya nilivyokula.
.
.
Jack Pyong, jamaa mfupi wa kichina, ni rafiki yangu kwa muda mrefu sasa, takribani miaka nane. Amekuwa ni kiongozi wangu kila nijapo China, na zaidi mshawishi wangu mkubwa wa kuja huku China kila tupatapo likizo.
.
.
Ni mwanaume mcheshi sana. Ana asili ya China ila kiuraia yeye ni Mmarekani. Na kwasababu anapenda sana kushinda akitazama tarakilishi, macho yake yamekuwa mabovu, haoni vizuri pasipo msaada wa miwani, hivyo muda mwingine huwa namuita macho manne.
.
.
Jana hiyo usiku, kama nakumbuka vema na si akili ya pombe, Jack Pyong alinitambulisha pia kwa mwanamke fulani wa kizungu mkazi wa New Zealand. Mwanamke huyo alikuwa na macho yaliyojawa na haya, nywele nyeusi ndefu na gauni lake lilikuwa jekundu lenye dotidoti zinazong'aa.
.
.
Hivyo tu! ... ni hivyo tu ndivyo ninavyovikumbuka toka usiku wa jana, hamna kingine. Ni Jack, huyo mwanamke na kula na kunywa, basi! Mengine kichwa changu kimegoma kabisa kuyakumbuka.
.
.
Hapa niwapo kitandani, hata macho sijayafumbua, najaribu sana kukumbuka ila wapi! Nadhani sasa napaswa kuamka. Niamke na kumtafuta Jack, nadhani yeye atakuwa ana kumbukumbu nzuri kuliko mimi.
.
.
Lakini hayo ya jana ya nini? Sidhani kama yana umuhimu wowote. Nilisonya na kuminya lips, nikajigeuza upande mwingine wa kitanda na kuendelea kulala. Sikujali mwanga wa jua ulikuwa umeshaingia vya kutosha ndani ya chumba changu. Nilijisemea nipo likizo basi acha nilale mpaka usingizi ukate kabisa.
.
.
Sikujua hata nini kilikatisha usingizi wangu mpaka kuwaza yale ya jana. Nilipuuzia nikarudi kwenye jitihada zangu za kuutafuta usingizi ila punde zikakatishwa kiukatili na hodi mlangoni. Kabla huyo aliyegonga sijamsikia sauti yake, nikawa nimeshajua atakuwa ni Jack Pyong! Hakuna mtu ambaye angegonga mlango wangu kwanguvu zaidi ya mpuuzi huyu!
.
.
"Amka we zoba!" Alifoka Jack Pyong akibamiza mlango. Haki nilimchukia kwa dakika hizi. Nilijibandua kitandani, kiuzembe nikaujongea mlango na kuufungua nikiwa nimekunja ndita.
.
.
"Jack unaweza niacha nikakaa kwa amani, tafadhali?"
.
.
Alikuwa ameshika simu yake mkononi, amevalia pajama ya pinki! Hivi mwanaume unavaaje pajama ya pinki? Nikiwa namshangaa, kabla sijasema kitu, akan'tolea macho yake akinionyeshea kioo cha simu, "hivi we lofa, hujaona calls za general?"
.
.
"General? ... unamanisha inspector general?" Nikababaika. Hapa kidogo mawazo yangu yakatoka kwenye pajama ya Jack Pyong na macho yakakauka usingizi.
.
.
"Ndio, general!" Jack Pyong akanijibu akizama ndani. Akashusha pumzi ndefu akiketi kitandani, "Amenipigia mara nane! Mara nane, Tony," alisema huku mimi nikifunguafungua mashuka kutafuta simu yangu. "Nilivyopokea tu, kitu cha kwanza kuniuliza yu kwapi Marshall?"
.
.
"Ukamjibuje?" Hapa nikauliza huku nikiendelea na msako wangu. Kusema ukweli sikuwa najua wapi niliweka simu yangu. Nilikuwa natafuta hapa kitandani ila sina uhakika. Pombe ya jana ilikuwa imenivuruga akili. Nilikuwa natafuta huku kichwa kikiniwaka, nitakuwa nimeitupia wapi?
.
.
"Nikamjibu haupo karibu na mimi," akanguruma Jack Pyong, "akaniambia nikutafute haraka iwezekanavyo!"
Kumbe ndo' maana ulikuwa umevaa pajama ya kike? Nikajisemea mwenyewe kifuani huku nikiendelea kutafuta. Nikamaliza msako pasipo kuona.
.
.
"Jack, haukuona simu yangu?" Nikamuuliza nikiwa nimeshika kiuno, macho yanatazama huku na kule kusaka.
.
.
Akan'tazama,
.
.
"Simu yako mimi natolea wapi? ... Tony, au ulimhonga yule mwanamke?"
.
.
"Mwanamke yupi?"
.
.
"Si yule ... yulee ..."
.
.
"Unamaanisha yule m-new Zealand?"
.
.
"Hahah nilitaka nikuone tu, kumbe unamkumbuka enh?"
.
.
"Jack, huu si muda wa masikhara. Mbona mimi sikuhangaika na hiyo pajama yako ya kike?" Hapa Jack Pyong akajitazama kisha akaniangalia kwa hasira.
.
.
"Sioni simu yangu, Jack. Nisaidie kutafuta."
.
.
"Mie najua ilipo? ... sikia, Tony, chukua simu yangu uongee naye, acha kun'potezea muda."
.
.
Nikachukua simu hiyo na kuweka namba za simu, nilikuwa nimezihifadhi kichwani namba za General, nikapiga na kuweka simu sikioni.
"Tony, umefunguaje simu yangu?" Jack Pyong akaniuliza akininyooshea kidole. "Umejuaje password yangu? We mjinga, umejuaje password yangu?"
.
.
Sikumjibu, punde General akapokea.
.
.
"Mkuu, unaongea na Anthony Marshall hapa."
.
.
"Marshall," General akaita na kusema, "nataka ufike ofisini haraka iwezekanavyo!"
.
.
"Sawa."
.
.
Akarudia tena, "namaanisha haraka iwezekanavyo!" Kisha akakata simu. Nikamtazama Jack Pyong na kumuuliza, "Umesikia General alichosema?"
.
.
"Nitasikiaje na wewe ndo' ulikuwa unaongea naye?" Jack akateta akinipokonya simu yake.
.
.
**
.
.
Kabla sijaendelea nadhani kuna haja ya kujitambulisha. Kwa jina, nadhani hilo tayari ushalijua, acha niachane nalo. 'Anyway', naitwa Anthony Marshall, ndilo jina langu rasmi. Jack hufupisha kuniita Tony, ila kazini najulikana zaidi kwa jina la Marshall. Mimi ni mkazi wa New York, Marekani. Ni ajenti wa shirika la upelelezi la Marekani, CIA (Central Intelligence Agency).
.
.
Sina mke wala mtoto, wala mchumba. Ndio. Na si kwamba umri haujafikia, hapana. Nina miaka thelathini na tano hivi sasa. Pengine sijapata mwanamke sahihi, au ni kazi zinanibana sana. Ila hiyo sababu ya kwanza ndiyo yenye mantiki zaidi.
.
.
Kwa upande wa kazi, sasa ni takribani miaka nane tangu niwe katika shirika la CIA, nikihusika zaidi na kategoria jenzi ya watu waliopotea na kutekwa.
.
.
Mpaka sasa, kwa mkono wangu, nimeshasaidia uokozi wa wamarekani kumi na moja waliopotea na watano waliotekwa nchi mbalimbali haswa Somalia na uarabuni. Nimekwepa risasi zisizohesabika na kupata jeraha karibia kwenye kila sehemu ya mwili wangu.
.
.
Sina haja ya kukwambia nimepitia magumu kiasi gani. Hatari kiasi gani. Bila shaka mwajua ajenti wa taasisi ya siri ya upelelezi anayoweza kukumbana nayo anapokuwa kazini. Lakini ajabu ni kwamba nimekuwa nikiyafurahia hayo. Napenda kazi yangu. Napenda ninachokifanya.
.
.
Tatizo ni kwamba, nakaa muda mwingi sana mbali na nyumbani. Kuna muda mpaka naweza jisahau kama kwangu ni New York! Kukaa miaka mitano, mitatu, miwili au hata kumi ukiwa nchi ya ugenini ni jambo la kawaida kwa ajenti wa CIA. Kukutana na watu wageni machoni, kuzungumza lugha za kigeni kama mzawa, kubanwa kiuno na bunduki, ni mambo ya kila siku hayo, si ya kushangaza tena.
.
.
Kazi yangu kama ajenti, pasipo kujali ni wapi natumwa, ni kukusanya taarifa nyeti na muhimu kisha kuzituma nyumbani kwa ajili ya hatua zaidi. Na pale panapohitajika, kujiingiza kwenye kombati kwa ajili ya jambo fulani, haswa kujiokoa pumzi yako na wale ambao unawalinda.
.
.
Sababu hiyo basi, natakiwa kuwa mkufunzi wa mapambano pasi na silaha na nikiwa na silaha pia. Lakini zaidi, kuwa mwepesi mno kwenye kuchambua hali na kufanya maamuzi yenye tija. Ninaposema mwepesi mno, namaanisha kweli hivyo. Mimi na Jack Pyong, huwa tunasema kabla risasi haijakufikia, inabidi uwe umeshaamua cha kufanya.
.
.
Hivi hilo litawezekanaje? Kuna muda tunajazana ujinga sana na Jack! Ila tu ni kuonyesha namna gani ambavyo mtu inabidi uwe mwerevu na mwenye akili nyepesi sana. Na hivyo basi ndo' maana CIA huwa inaweka madaraja na kuwa wachaguzi sana kwa watu wanaowaajiri.
.
.
Wakikagua kuanzia GPA ya mtu awapo kozi, lakini pia namna anavyojieleza, kuchambua na kuhitimisha mijadala yenye mikanganyiko ndani ya muda mfupi. Mtu mwenye 'sense' zaidi ya tano za binadamu. Zaidi ya hapo, akiwa tena mwenye ujuzi wa lugha nyingi, haswa Kiarabu, Dari, kikorea, kituruki, kichina, kisomali, kiindonesia na kadhalika.
.
.
Kwa upande wa Jack Pyong, aaaahmmm, sijui kwanini walimchukua kwakweli. Hajui kupambana, hajui lugha yoyote zaidi ya kiingereza na kichina. Utumizi wake wa silaha ni hafifu haswa na ninapomsihi ajifunze zaidi huniambia hana muda huo kwani CIA hawakumchukua kwa ajili ya kupambana.
.
.
Labda anachojivunia ni utaalamu wake nyuma ya 'keyboard' na ujuzi wake kwenye mambo ya sayansi. Ni mwerevu sana kwenye hayo, na basi hataki mengine kabisa.
.
.
Lakini mbali na ubishi huo, ni rafiki mmoja mzuri sana, japo kuna muda huwa ananipotosha. Ni mtu wangu wa karibu sana na mara nyingi nakuwa naye kazini na mbali ya kazini.
.
.
Yeye pia hana mke wala mtoto, bali mchumba tu ambaye huitwa Violette. Mwanamke huyo ni Mmarekani na amekuja naye hapa Hong Kong kwaajili ya likizo hii.
.
.
Nadhani utambulisho huo unatosha. Mengine utayajulia kadiri nikusimuliapo yanayotukia kwenye kisa hiki cha kukuacha mdomo wazi. Kisa ambacho nimekipa jina la NYUMA YAKO kwa maana kwamba, si kwasababu unatazama mbele, ukadhani nyuma ya mgongo wako mambo yamesimama. Lah! Ukiwa unatazama mbele, nyuma pia kuna mambo yanaendelea, na mambo hayo yanaweza yakawa ya hatari kuliko uwazavyo.
.
.
Na kwasababu haujayapa kipaumbele kama yale ya mbele, mambo haya ya nyuma huwa ya ghafla na hatarishi zaidi, yakikuacha ukiwa umelala chini hujiwezi, damu zakububujika.
.
.
Tazama nyuma yako. Huenda kuna mchezo unaendelea ambao hauuoni.
.
.
.
***
 
*NYUMA YAKO --- 02*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Na kwasababu haujayapa kipaumbele kama yale ya mbele, mambo haya ya nyuma huwa ya ghafla na hatarishi zaidi, yakikuacha ukiwa umelala chini hujiwezi, damu zakububujika.

Tazama nyuma yako. Huenda kuna mchezo unaendelea ambao hauuoni.

ENDELEA

SURA YA PILI …

Ni kwa muda mfupi kwa kadiri tulivyoweza tukawa tumefika Marekani, New York. Safari hiyo ni ya umbali wa masaa kumi na tano na dakika thelathini na tatu. Lakini kwasababu ya mambo ya masaa, kijografia Hong Kong ipo mbele kimajira kuliko Marekani hivyo tukafika siku hiyo hiyo tuliyotokea Hongkong, Jumatano, huku Marekani yakiwa ni majira ya mchana.

Ni ajabu enh? Basi ili tusipotazane hapa, maana kuna mikanganyiko zaidi huko mbele, acha tueleweshane kwa ufupi. Dunia huzunguka toka Magharibi kuelekea Mashariki, kwahiyo basi upande wa Mashariki huwai kuliona Jua kuliko ule wa Magharibi. Tupo pamoja?

Kwahivyo basi, ukiwa Hong Kong unatangulia kuliona na kulichoka jua kabla hata Marekani hawajaliona. Na wakuta Hong Kong ikiwa ni Jumatano, bado Marekani ni Jumanne au Jumatatu usiku baadhi ya maeneo machache ya Magharibi ya mbali. Kwahiyo kusafiri kutoka Hongkong kwenda Marekani, ni safari unayopoteza muda, yaani badala ya muda kuongezeka, unakuwa unapungua maana umetoka Mashariki kurudi Magharibi ambapo kupo nyuma kimasaa.

Natumai umenielewa.

Lakini hapa New York si ambapo tulikuwa tunaelekea. Makao makuu ya CIA yapo Virginia, umbali wa maili mia nne na nane toka jiji la New York. Kwa mwendo wa basi ingetugharimu masaa saba kasoro, hatukuwa na muda huo wa kupoteza kwahiyo ikatulazimu kuchukua ndege ili angalau tutumie lisaa limoja na robo hivi kufika Virginia.

Tukafanya hivyo, pasipo kupumzika, tukafika Virginia majira ya saa tisa alasiri. Nikamwacha Jack Pyong na mpenzi wake mie nikienda mpaka makao makuu kukutana na Inspector General, bwana Ethan Benjamin, mwanaume wa makadirio ya miaka hamsini kasoro haba.

“Karibu, Marshall,” akanikaribisha akinionyeshea kiti. Nikaketi na kumtazama. Alikuwa tayari ananitazama kwa umakini kana kwamba mwalimu wa usafi akitafuta kasoro kwenye sare ya mwanafunzi.

Bwana Ethan ni mtu mmoja mpole sana. Ni mara chache sana utamsikia akipaza sauti yake. Hupenda kutumia macho na maneno machache tu haswa akikukumbusha juu ya uwepo wako kwenye taasisi nyeti kama hiyo, CIA.

Mara kadhaa amekuwa akisema kabla ya kuwaruhusu maajenti wakafanye kazi zao, CIA ni moyo wa Marekani, hivyo msifanye taifa kuwa mfu.

Ni ngumu sana kumjua kama yupo kwenye msongo wa mawazo ama furaha. Uso wake ni mfichavi mzuri sana wa hisia. Najaribu sana kuwa kama yeye, lakini naishia kushindwa. Haswa nikiwa na mpumbavu Jack Pyong.

Akasafisha koo lake na kuniambia, “Marshall, nina kazi kubwa sana ya kukupatia. Najua hautaniangusha.” Akili yangu ikaanza kuwaza itakuwa kazi gani hiyo ya kunitoa kwenye likizo yangu na kuitwa moja kwa moja na Inspector General? Ndivyo tulivyofundishwa. Yakupasa kuwaza ya mbele, hata kubashiri kwa mantiki pale unapoona kuna haja ya kufanya hivyo. Halikuwa kosa.

Ila sikuweza kuwaza sana kwa maana nilipaswa pia kuweka akili na masikio yangu kwenye kinywa cha mkuu wangu wa kazi.

“Hapa tuongeapo, Raisi amepotea,” akasema kisha akanyamaza akin’tazama kwa kunisoma. “Alikuwa njiani akielekea Berlin, Ujerumani, kwenye mkutano wa mataifa makubwa kiuchumi, lakini mpaka sasa tuongeapo hajulikani alipo, na inasemekana ndege yake imeanguka huko mbali ya bahari ya Pasifiki.”

Kauli hiyo ikatosha kunitoa macho kwa mshangao. Nikajitengenezea vema kitini na kumtazama Mkuu akinena.

“Taarifa haijatangazwa rasmi, lakini haiwezi kukaa kabatini kwa muda. Hili laweza kuwa shambulizi la kigaidi, nina mashaka nalo. Na mpaka kukuita hapa maana yake ni kwamba nina mashaka nalo.”

Akanyamaza na kunitazama kwa sekunde mbili, alafu akaniita, “Marshall.”

“Ndio, Mkuu.”

Akasema, “Nishatoa maelezo haya kwa mkuu wako wa kitengo. Unachotakiwa kukifanya ni kwenda kumtafuta Raisi popote alipo. Kama amekufa, tuletee mwili wake hapa niamini. Na pia … vichwa vya hao waliohusika!” akiwa anasema hayo maneno ya mwishoni alikuwa anaminyia kidole chake juu ya meza, macho akiyakaza.

Kwa kuongezea zaidi akaniambia nitashirikiana na inspekta wa FBI (Federal Bureau of Investigation) Miss Danielle James kuhusiana na chochote kile cha upelelezi ntakachokihitaji ndani ya nchi. Hii ni kwasababu CIA huwa wanahusika zaidi na mambo ya nje, nchi za kigeni, wakati FBI wao wakihusika na intelijensia ya ndani ya nchi, kukusanya taarifa, ushahidi, na kushurutisha sheria.

Hivyo kuna nyakati huwa tunategemeana kutekeleza majukumu yetu.

“Utamkuta hapo nje,” akasema mkuu na kumalizia tena, “Usiniangushe, Marshall. CIA ni --”

“Moyo wa Marekani,” nikamsaidia kumalizia kisha nikatikisa kichwa na kutoka nje ya ofisi. Nikakutana na Danielle, mwanamke mkakamavu mwenye nywele nyekundu akiwa amevalia suti rangi ya kahawia. Akanisalimu nami pia nikamsalimu kisha nikaenda kukaa naye kwa ofisi yangu kwa muda mchache mno, nikionelea ni kheri kwanza niende kwenye eneo la tukio kumtafuta Raisi, alafu nitakuja kurejea kuongea naye zaidi.

“Kwahiyo unaonaje?” akaniuliza. Kwakweli sikuwa najua nini ametoka kuongelea, kwani mawazo yangu yalikuwa mbali kidogo. Nilikuwa najaribu kuwaza ni wakina nani watakuwa na ‘guts’ za kufanya tukio kubwa kama hilo? Na amewezaje kufanya vivyo ingali ulinzi wa Raisi huwa ni wa hali ya juu?

“Daniella, tutaonana. Sawa?” nikamuaga nikinyanyuka kuuendea mlango, nikaufungua na kumtazama. Mwanamke huyo akatikisa kichwa kabla hajanyanyuka na kujiendea zake. Mimi nikarejea pale kitini na kuwaza kwa muda kidogo juu ya namna ya kuenenda. Punde nikatungua koti langu jeusi lililopo ndani ya ofisi, nikaliweka begani na kutoka.


**

Ni hivi, katika oparesheni kama hii, siwezi kwenda mwenyewe. Nahitaji msaada toka kwa watu wengine ambao tutaunda timu ya kufanya kazi. Ndani ya CIA kuna kitengo cha shughuli maalum, kwa jina ‘The Special Activities Centre’, kifupi SAC. Kitengo hichi kimegawanyika kwenye makundi mawili; PAG na SOG.

Oparesheni za kisiasa na kiuchumi huendeshwa na ‘The Political Action Group’, kifupi PAG. Hawa wanahusika na ushawishi wa kisiasa na wa kichumi wa Marekani dunia nzima. Na oparesheni zenye hatari ya juu kijeshi hufanywa na ‘The Special Operation Group’ kifupi SOG.

Wahusika wa SOG huwa hawabebelei nguo au kitu chochote cha kuwaonyesha kuwa wao wametokea Marekani. Na hii ni kwasababu muda wowote ule ambapo mambo yakienda kombo, basi Marekani wanaweza kukana kuhusika nao.

Ndani yake kunakuwa na watu wenye ujuzi wa hali ya juu, ambao wengi wao hutolewa kwenye kitengo cha special force au tuite komando toka jeshini. Na kwakufanya mambo kuwa mepesi na ‘manageable’ huwa wachache tu kwa kila oparesheni.

Hivyo basi kwakuwa kila kitu kilishakuwa bayana, nilipoonana na mhusika wa kitengo cha SAC (The Special Activities Centre), akanikabidhi vijana wanne kwa ajili ya kazi akiwa amefuata maelekezo ya Inspector General. Kwahiyo kutokana na kazi tuliyokuwa tunaelekea kufanya, sisi tukawa ni SOG (The Special Operation Group).

**

Ulikuwa ni usiku sasa wa saa mbili tukiwa angani ndani ya ndege ya mapambano. Tukiwa tumekaa kwa kutazamana, tukamsika rubani akitangaza kusema tunaingia eneo la tukio hivyo basi tuanze kujiandaa kwa ajili ya kuchumpa.

Tukaweka kila kitu sawa; begi la parachuti na miwani ya kutusaidia kuona usiku. Tulikuwa tumevalia nguo nyeusi za kombati zisizo na bendera, pia tumebebelea vifaa kadhaa vya kutusaidia kimapambano na kuzamia. Punde rubani aliposema tumefika, mkia wa ndege ukafunguka nasi tukarukia nje pasipo kujiuliza.

Tukachukua kama dakika sita tukiwa hewani tukibebwa na maparachuti tunasukumwa na upepo. Tulipotua, ilikuwa ni kisiwani, tukiwa tunafuata ramani, tukatembea upesi mpaka kufika eneo la ufukweni. Palikuwa kimya haswa. Nikatazama tena kwenye ramani yangu kuhakikisha. Ni kweli nilikuwa mahali ninapostahili.

Hapakuwa na alama ya kitu chochote hapo. Maji yalikuwa yanasukumwa na upepo kutengeneza mawimbi, na miti inatikisika kutengeneza muziki.

Hapa ndiyo nikajua ya kuwa sisi ni watu wa kwanza kufika hapo. Ina maana tangu Raisi aangukie maeneo hayo, hakuna mtu aliyewahi kukanyaga hapo.

**
 
*NYUMA YAKO --- 03*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Hapakuwa na alama ya kitu chochote hapo. Maji yalikuwa yanasukumwa na upepo kutengeneza mawimbi, na miti inatikisika kutengeneza muziki.

Hapa ndiyo nikajua ya kuwa sisi ni watu wa kwanza kufika hapo. Ina maana tangu Raisi aangukie maeneo hayo, hakuna mtu aliyewahi kukanyaga hapo.

ENDELEA

Kidogo nikapata maswali juu ya namna gani jambo hili lilivyokuwa la siri. Siri mpaka pale aidha mwili wa Raisi utakapopatikana au mpaka pale wahusika watakapojulikana. Lakini itachukua muda gani? Hapa nikakumbuka kauli ya Inspector General, kuwa jambo hili haliwezi kukaa kabatini kwa muda mrefu.

Na kwa kuwaza tu, tayari mashaka yatakuwa yameshaambaa miongoni mwa watu. Raisi wa Marekani kutoonekana kwenye mkutano mkubwa kama huo na ingali huku nchini ameshaaga, ni wazi kabisa, ni kitu cha kuzalisha mashaka na maswali.

“Tazama kule!” alisema kamanda mmoja niliyeambatana naye. Tulisonga huko alipokuwa ameelekezea, tukakuta mojawapo ya mabaki ya ndege, kidogo tena tukaona zaidi na zaidi, hapa tukapata maswali, ni kwamba ndege ililipuka kabla ya kuzamia ndani ya maji ama?

Ila hapana. Mabaki haya hayakuonyesha dalili ya kuungua. Huenda wakati ndege inapoteza mwelekeo na kwenda kombo, baadhi ya viungio vyake vilishindwa kukinzana na upepo mkali basi vikabanduka na kunyofoka.

Japo tuliweza kung’amua jambo hilo na kujiaminisha kuwa kweli ndege ilikatiza eneo tulilopo, tukajikuta tukiwa na matumaini mfu sasa juu ya uhai wa Raisi. Ni wazi ndege itakuwa imezama majini, na kwa mahesabu ya kawaida mpaka muda huo tangu tukio litokee, ni ngumu kwa mtu kuwa hai ndani ya maji.

“Sasa tunafanyaje?” akaniuliza mmoja wa kamanda niliyekuwa naye kikosini.

“Tunazama ndani ya maji,” nikamjibu nikimtazama. “Ni lazima tupate mwili wa Raisi, hai au mfu!” nikaongezea taarifa kisha nikatazama huku na kule ndani ya msitu wa kisiwa.

Kulikuwa ni giza na kimya.

Giza na kimya.


**


Sauti ya ndege wa kwanza iliniamsha toka usingizini. Nilijua ni asubuhi sasa japo hakukuwa kumekuchwa na jua. Niliamka na kuangaza, wenzangu walikuwa wamelala. Nikanyanyuka na kuifuata bahari kwa ukaribu. Hapo nikiwa nimeweka mikono yangu mfukoni, nikangaza mandhari, pia nikajiuliza maswali kadhaa ya kipuuzi.

Muda kidogo wenzangu nao wakaamka, basi bila kupoteza muda tukaanza kufanya mpango wa kuzamia ndani ya maji. Wawili miongoni mwetu walikuwa ni watu wenye ujuzi huo, walivalia mitungi ya gesi na vinyago vya majini kisha wakazama.

Tukawangoja kwa takribani lisaa limoja, wakaibuka wakiwa na watu wawili ambao tuliwatambua kama marubani kutokana na sare zao. Kwa kusaidizana, tukapeleka miili hiyo ufukweni.

“Ndege ipo kwenye kina kirefu sana,” alisema mmoja wao aliyezamia. “Yachukua muda kufika na kurudi toka huko, takribani zoezi la dakika ishirini.”

“Hamjauona mwili wa Raisi?” nikawauliza.

“Hapana, hatujauona. Ila hatujamaliza kukagua ndege nzima.”

Wakazama tena, na ikatuchukua kama lisaa lingine kwa wao kuibuka tena juu. Mara hii walikuwa wamewabebelea watu wengine wawili ambao walikuwa wafanyakazi wa ndani ya ndege. Nikawauliza tena kuhusu Raisi, wakanijibu hamna. Hawajamwona.

Nikamwambia mmoja wao, “Nikabidhi nami vifaa nizamie.”

Tukazama humo na mie nikatafuta sana ndani ya mabaki yale ya ndege. Sikuona mwili wa Raisi, zaidi ya kukutana na miili ya watu wengine, wafanyakazi na maajenti wa secret service ambao wanahusika na ulinzi wa Raisi. Nilikaa humo sana nikikagua kila eneo pasipo mafanikio. Mwishowe mpaka mtungi wa gesi ukaanza kuishiwa. Sikuwa na budi kupanda juu kabla mtungi huo haujawa mzigo.

“Vipi, umeona kitu?” akaniuliza mmoja wa wenzangu.

“Hapana,” nikamjibu nikitikisa kichwa. “Nimeambulia hiki tu.” nikawaonyesha tai mkononi mwangu. Wakaichukua na kuitazama. Wote tukakubaliana kuwa tai ile ilikuwa ni ya Raisi. Nyuma yake ilikuwa na bendera na nembo ya Marekani.

“Sasa itakuaje?” akauliza mmoja wao. “Ina maana atakuwa ameangukia kwengine?”

“Inawezekanaje?” nikawahi kutia shaka. “Inawezekanaje aangukie kwengine alafu tai ikabakia ndani ya ndege.”

“Sasa atakuwa wapi?”

“Sijajua,” nikajibu nikiangaza msitu. “Ni ajabu kwake kutoonekana na huku tai kubakia ndani ya ndege! Hii inamaanisha alikuwapo ndani. sasaa …” kwa muda kidogo nikawaza. “Pengine yatupasa kuanza msako wa kisiwa hiki kizima na maeneo yake ya karibu.”

Basi tusipoteze muda tukaanza kufanya hivyo. Tukazunguka kisiwa kizima kwa masaa kadhaa tusione lolote. Hakukuwa na alama yoyote ya binadamu humo. Zaidi tukiwa tunakaribia kufanya kazi yetu hiyo, nikaona mojawapo ya nyayo za binadamu ufukweni. Nikaita na kuwataarifu wenzangu.

“Unadhani itakuwa ni ya nani?”

“Pengine wavuvi. Au wewe unadhaniaje?”

“Wavuvi?” nikapata swali. “Wavuvi tokea wapi?”

Tulipotazama kwa mbali upande wetu wa kaskazini, tukagundua kuwapo kwa kisiwa kingine. Kisiwa hicho kilikuwa kikubwa kuliko hiki cha sasa, nacho kikiwa kimezibwa na misitu ya kijani.

“Twende huko tukatazame,” mmoja akashauri, lakini mimi nikasita, “Sidhani kama Raisi atakuwapo huko.”

“Sasa unadhani atakuwapo wapi?”

“Sijui, ila nahisi ni maeneo ya hapahapa karibu.” nikashauri, “turudi kule kwenye ndege.”

“Kufanya nini huko na tumeshatoka?”

Hapa nilipata shaka na nikajilaumu kwanini mawazo niliyokuwa nayawaza muda huo sikuwa nayo hapo kabla. Nilihisi kuna haja ya kuhesabu wale watu waliokuwemo ndani ya ndege. Juhudi kubwa ni kung’amua kuna maajenti wangapi waliobakia humo ili tutambue kama Raisi alitokomea mwenyewe au alitokomea na baadhi ya maajenti wa secret service.

Tukipata jibu la swali hili basi kwa namna moja ama nyingine tutajua nini cha kufanya. Kufanya hilo vema, tukawasiliana kwanza na kitengo cha Secret service watujuze idadi kamili ya maajenti walioongozana na Raisi, pia wafanyakazi waliokuwamo ndani ya ndege.

Baada ya kujua hilo, tukarejea kule kwenye ndege na kuzamia tena, mara hii nikizama peke yangu kutokana na uhaba wa mtungi wa gesi. Ulikuwa umebakia mmoja ambao ndiyo upo kamili. Nikiwa nafanya hili kwa ustadi, nikagundua kulikuwa na upungufu wa maajenti wawili wa secret service.

Hapa sasa nikapata mashaka. Nao watakuwa wapi? Wameenda na Raisi ama walipotelea maeneo tofauti? Lakini kwanini wao na si wengine?

Maswali haya yalinifanya kichwa changu kiwake moto na hata hatimaye kuishia kuona kuna haja ya sisi kuondoka huko kisiwani ili twende tukatafute majibu nchini kisha tujue namna ya kuenenda.

Lakini kabla ya kwenda huko, nikaona pia ni stara tukaenda kupekua na kisiwa kile ambacho ni kikubwa kipakanacho na hichi tulichopo kwa upande wa kaskazini. Lengo ni kuhakikisha hakuna makandokando yoyote tuliyoyabakiza kwenye eneo la tukio. Tukiondoka basi tumeondoka ‘for good’.

Tukaogelea kwa dakika kadhaa. Tulipofika huko, tukashikilia silaha zetu vema na kuanza kuzama ndani ya kisiwa. Kadiri tulivyokuwa tunazama humo na giza likawa linakua. Miti ilikuwa mingi sana na tena yenye matawi na majani mapana.

Tukatembea kwa muda wa kama dakika nane, mmoja wetu akaona damu ardhini.

“Unadhani kutakuwa na watu hapa?” akauliza. Kabla hatujajibu tukastaajabu nyavu imetusoma na kutukusanya, alafu ikatupeleka juu kabisa ya mti! Nyavu hiyo ilikuwa ngumu haswa na ilitubana mno kiasi cha kuhema kwa tabu.

Tulizama mtegoni! Na hatukuwa na ujanja wowote ule wa kufanya kwani viungo vyote vilikuwa vimebaniwa mwilini. Kurusha macho huku na huku, kidogo tukasikia sauti ya filimbi, na kitu cha mwisho kabisa kukikumbuka ikawa ni maumivu ya kitu kama mwiba mgongoni mwangu. Nikapoteza fahamu.

Nilikuja kugundua baadae ya kwamba tulichomwa sindano za sumu.


**


Nilikuwa kizani sifahamu kinachoendelea, ila kadiri muda ulivyokuwa unaenda, nikaanza kujihisi mwili wangu. Nilijihisi nipo chini tena sina nguo. Mwili unapigwa na baridi kali.

Kichwa nacho kilikuwa kinanigonga, na kwa mbaali nasikia sauti za ngoma. Nikajaribu kufungua macho nitazame. Sikuwa naona vema, nadhani ni kwasababu ya madhara ya ile sumu tuliyochomwa nayo. Nilikuwa naona maruweruwe, watu kama mawingu!

Watu hawa walikuwa wanacheza kwa kuzunguka. Walikuwa wengi na katikati yao kulikuwa na kitu. Ni nini hiki? … nilijaribu kutazama lakini sikuwa naona vema. Mwili ulikuwa mdhaifu na uliochoka sana.



***
 
*NYUMA YAKO -- 04*

*Simulizi za series*

Niliwaza, je watu hawa ndiyo watakuwa na mwili wa Raisi na wale maajenti wa secret service? Nikajikakamua nisimame lakini sikuweza abadani! Sikujua walikuwa wametutilia nini. Nilijihisi mzembe kwa kiwango cha lami! Maungio ya mwili yalikuwa hayajiwezi, mdomo umekauka na masikio nayahisi yamoto!
Kuna muda ulimi nao nilikuwa nauhisi mchungu sana. Nikimeza mate ni kana kwamba yananikaba ama kuniunguza koo! Nilijichukia sana. Kama ningeweza kujitoa kwenye mwili huo, ningefanya vivyo niwe huru. Niliuhisi mzigo.
Kidogo nikawakumbuka wenzangu. Nikajikunja mwili na kuangaza ndani ya eneo tulilopo. Sikuwa naona kitu. Kulikuwa ni kiza tu. Hata nilipokaza macho yangu ya kilemavu kutazama, sikuambulia!
Kwa mbali nilisikia sauti ya mtu akikoroma, ila sikuwa namwona. Nikatamani kumwita mtu huyo, koo likagoma kabisa. Sauti haikuwa inatoka. Nilijitahidi hata nipaze sauti ya kuhema kwanguvu kama ishara lakini ikashindikana, ni kama vile koo lilijawa na vidonda, na mapafu nayo yamesinyaa!
Kusema ukweli sijui ni nini ambacho tulitiliwa. Sijui ni sumu ya namna gani yenye kumtenda mtu vibaya kiasi kile mpaka utamani kufa.
Kwa ustadi wangu wote, sikuwahi kukutana na sumu ile. Nilijiuliza wametumia kitu gani hicho, mti gani? Ua gani? Mmea gani huo? Kweli sikuwa na majibu.
Nilijikuta nikirejea sakafuni na kulala maana hakuna cha maana nilichokuwa nafanya. Kama niko sahihi, baada ya dakika kama tano hivi, nikasikia sauti ya mlango ukifunguliwa. Sikujua kilichoendelea, ila kidogo mkono wangu ukadakwa, nikanyanyuliwa vuup! Nikaburuzwa kupelekwa nje ya jengo tulokuwapo huku watu wawili waliokuwa wananibebelea wakiwa wanaongea lugha nisiyoelewa.
Kama baada ya dakika moja, wakanibwagia chini, pale eneo ambao niliwaona watu wakiwa wanacheza ngoma, kisha sauti nzito ikasema maneno ya ajabu kwanguvu, mara ngoma ikakoma.
Kidogo nikawasikia na wenzangu wakiwa wanatupiwa hapo chini. Bado kulikuwa kimya. Na nadhani tulivyomalizika kutupiwa hapo chini ndipo nikasikia kishindo cha mtu.
Kishindo kilikuwa kikubwa kiasi cha kunifanya niwaze atakuwa ni nani huyo? Mtu mwenye mwili mpana na uzito wa mtoto wa tembo?
Nikadakwa kama kikaratasi na kisha kunyanyuliwa niketi kitako. Nikapanuliwa mdomo na kumiminiwa kimiminika kichungu haswa. Nilipomeza, japo kwa tabu mno, nikaanza kupata ahueni. Kimiminika kile kilinikata sumu kabisa na kunifanya nianze kujihisi ahueni ya binadamu. Macho yalipata uwezo, mwili ukawa na nishati.
Nilistaajabu ni dawa gani ile ambayo iliweza kunipa ahueni haraka vile. Japo nimetumia dawa nyingi za hospitali, sikuwahi kuona ahueni ya upesi kiasi kile. Nilitazama, mbele yangu, nikamwona mtu mmoja mpana kana kwamba mbuyu. Nywele zake zilikuwa nyeusi na ndefu.
Mwili wake umejawa na michoro mbalimbali, shingoni amevalia mkufu wa mifupa ya wanyama na amejisitiri sehemu zake za siri kwa majani yaliyofumwa vema.
Hakuwa na sura ya urafiki. Macho yake yalikuwa makubwa na mekundu yakitingwa na ndita pana kama matuta. Alinitisha. Na namna alivyokuwa ananitazama, nilihisi anataka kunimeza.
Mbali na yeye, watu wengine wote ambao walikuwa wamesimama wakitutazama, nao walikuwa wametukodolea macho. Nao nyuso zao zatisha. Sijui walikuwa wamepakaa nini usoni. Mikononi wamebebelea mikuki mirefu yenye kupambwa na manyoya ya tai. Wanawake kwa wanaume, watoto kwa watu wazima.
Sasa yule mwanaume ambaye amenipatia dawa, mwanaume mpana mwenye uso wa kutisha, akaniuliza, "Sheeta ghasi cha?" Akinikazia macho.
Watu wote walikuwa kimya kana kwamba hamna mtu. Nikatambua kuwa mtu huyu atakuwa ni mwenye nafasi ya juu katika jamii hii. Mtu mwenye kuogopwa na kuheshimiwa. Aidha ni kiongozi au tabibu mkuu.
Lakini lugha aliyoizungumza kwangu ilikuwa mpya. Sikumwelewa. Nilitikisa kichwa na kumwambia kwa lugha yangu kuwa sijamwelewa. Sijawahi kusikia lugha yake hata mafunzoni japo tumesoma lugha kadhaa huko.
Basi mtu huyo akawatazama wenzake na pasipo kusema kitu, mmoja wao akasonga mbele. Huyu alikuwa ni kijana fulani mrefu mwembamba. Nywele zake zilikuwa fupi nyeusi, macho yake makubwa na makali.
Akanitazama, kisha akanisogelea karibu na kuniuliza, "mmetokea wapi? Na hapa mmekuja kufanya nini?"
Nikatambua kuwa kijana huyo alikuwa anazungumza lugha yetu. Nilistaajabu kidogo. Huenda ni mtu ambaye alishawahi kutoka na kwenda kuyajua ya nje ya jamii yao. Kumbe hata yule bwana alipoangaza kando, alikuwa amempa ishara ya yeye kuongea nasi.
Kidogo nikapata tumaini. Kama watatuelewa basi wangeweza kutusaidia na hata kutuachia huru maana hatukuja kuwadhuru bali kutimiza kazi yetu ya msako.
"Tupo hapa kutafuta miili iliyo--"
"Anguka toka kwenye nyota juu?" Akanikatisha kwa swali. Nikamtikisia kichwa, "ndio. Miili iliyoanguka toka kwenye nyota. Nyota ya juu!"
Akamtazama yule bwana mkubwa na kumwambia kwa ile lugha yake. Yule bwana mkubwa akanitazama alafu akaukita mshale wake chini kwa mkono wake wa kushoto.
Akataka kusema nami jambo, akakumbuka hatuelewani, akamtazama yule bwana mdogo na kumwambia nini aniulize.
"Je, mmeshapata mlichokuwa mnakitafuta?"
"Hapana!" Nikawahi kujibu na kisha kuwauliza, "mmeona chochote kile?" Hakunijibu, badala yake akafikisha taarifa kwa yule bwana mkubwa.
Sikujua walikuwa wanawaza nini vichwani mwao, ila walionekana kujawa na mashaka fulani baada ya kuwajibu maswali yao machache. Walijadili kidogo, kama wakielekezana kitu, na mara wakalipuka kwa hasira.
Nikiwa namwona yule bwana mkubwa akiwa amefura, akamimina maneno yake kwa yule bwana mdogo ambaye punde akanieleza kilichosibu.
"Hata kama tungeona kitu, tusingewaeleza. Hatutaki kuhangaika nanyi wauaji na waharibifu wa amani. Tutawaua hivi punde mkawe chakula cha samaki!"
Nikashangazwa, "ni nini kosa letu?" Yule bwana mdogo akafoka akieleza kuwa sisi ni maadui kwao. Tulishawahi kuvamia kijiji chao na kuwamaliza wenzao, ikiwemo kiongozi wao na hata wazazi wa huyo bwana mdogo aliyekuwa mkalimani!
Habari hizi zikanishtua. Na hata kama wale wenzangu wangelikuwa wazima kama mimi, yaani wamepewa dawa ile ya unafuu, wangelishtuka pia. Sikujua ni nini watu wale walikuwa wanazungumzia.
"Hii ni mara yetu ya kwanza kuj--"
"Mwongo!" Nikakatishwa na yule bwana mdogo. Uso wake ulikuwa umebadilika, anang'ata meno na kunitazama kiuchungu.
"Ninyi ni wauaji! Mlidhani tutawasahau? Mlinifanya kuwa yatima, na sasa mmerudi kutuangamiza sote?"
"Sijui nini wazungumza," nikajitetea. "Sijui lolote kati ya hayo mnayotuhusisha nayo. Hatujawahi kuja hapa isipokuwa mara hii..." nikiwa naongea kujieleza, mara watu hao wakaanza kugongesha vitako vya mikuki yao chini na kuimba kwa pamoja "hal! Hal! Hal! Hal!" Sauti yao ilikuwa kubwa kiasi nikaamua kunyamaza maana sikuwa nasikika.
Lakini zaidi nikaogopa maana sikuona kama ni ishara njema. Japo sikuelewa kilichokuwa kinazungumzwa, ila matendo yalinipasha maana. Anamaanisha nini mtu aimbaye hivyo na huku akikata shingo yake kwa kiganja cha mkono?
Tukanyanyuliwa na kutiwa nyavuni,nyavu ngumu iliyotuteka mtegoni, alafu tukaanza kuburuzwa kupelekwa eneo ambalo hatukuwa tunalijua, huko kwenda kuadhibiwa pia kwa kosa tusilolijua.
Tulizama zaidi misituni, mbali na kijiji. Safari nzima wakiwa wanaendelea kuimba "hal! Hal! Hal!" Wakigongesha mikuki ardhini!
Kwa takribani kama dakika nane tukitembea, ndipo wakasimama na kukoma kuimba. Nilipolikagua eneo hilo, nikaona miti mikubwa ikiwa imetengeneza umbo la pembe tatu. Miti hiyo mipana kana kwamba mibuyu, ilikuwa imechorwachorwa sura za ajabu na imefungwafungwa kamba.
Sikufahamu kwanini miti hiyo ilikuwa mikubwa kuliko mingine iliyokuwa imezunguka hapo. Na pia kwa muda huo sikuwa najua kwanini wametuleta kwenye miti hiyo na si mingine. Ila niliwaza pengine ilikuwa ni miti ya madhabahu. Sehemu ambapo wanafanyia shughuli zao za kidini kama vile matambiko na ibada.
Sasa hapo walituleta kutufanyia nini?
Yule bwana mkubwa, kiongozi, akawatazama vijana wanne wa kiume, wakasonga mbele na kutunyaka alafu wakatutia kambani na kutufungia mitini. Wakatukaza haswa kisha wakaimba hapo kwa muda kidogo yule bwana mkubwa akitunyunyizia maji yake ya dawa. Walipomaliza wakaanza kujiondokea.
"Tafadhali msituache hapa!" Nikawaita na kuwasihi. "Hatuhusiki na mlichokisema, tunaomba mtuache huru!"
Hakuna aliyejali, ila yule bwana mdogo alibaki nyuma ya wenzake waondokao. Naye alikuwa wa mwisho akitutazama. Na kabla hajatokomea, akanisogelea karibu na kuniambia,
"Unaona hizo sura mitini, ni za wale tuliowafungia hapa na kuwaacha. Unajua kwanini miti hii ni minene? ... Ni kwasababu inakula watu!" Alafu akatabasamu.
Nikamuuliza, "lakini mbona wewe ni wa tofauti na wenzako? Umejuaje lugha yetu?"
Akaniuliza, "hayo ndiyo maneno yako ya mwisho ukielekea kufa?" Kisha akatikisa kichwa. "Nilidhani wewe ni mwerevu."

**
 
*NYUMA YAKO -- 05*

*Simulizi za series*


Nikamuuliza, "lakini mbona wewe ni wa tofauti na wenzako? Umejuaje lugha yetu?"
Akaniuliza, "hayo ndiyo maneno yako ya mwisho ukielekea kufa?" Kisha akatikisa kichwa. "Nilidhani wewe ni mwerevu."
ENDELEA
Na asiendelee kuongea nami, akashika njia aende zake. Nikamwita asijali. Akaendelea kuondoka akipiga mluzi. Lakini nilipomwambia maneno haya, akasimama.
"Nina kitu kwa ajili yako!"
Akanitazama na kisha akakunja sura kama atiaye shaka alafu akanijongea na kuniambia, "sina muda wa kupoteza nawe ewe bwana wa manjano. Ni nini hiko wataka kuniambia?"
"Kama unataka nikuambie niweke huru toka kwenye nyara hizi!" Nikamsihi. Akatabasamu na kisha kucheka kidogo kana kwamba mtu mwenye utumbo mtupu. "Unadhani mimi ni mjinga kama wewe?" Akaniuliza.
"Ujinga wangu uko wap?"
Akatahamaki, "hujioni ulivyo mjinga? Uliwaua watu wa kijiji hiki alafu ukaja tena ukiwa hujiwezi. Unadhani wewe ni mwerevu?"
"Sikuwahi kuj--"
"Ishia hapo! Siko kuskiza ngonjera zako. Kama huna cha kuniambia, acha niende kwa amani nawe ubaki hapa kutafunwa na mti!"
"Ninacho ... ninacho cha kukuambia. Na najua utafurahi ukikisikia."
Akabaki akin'tazama kwa macho ya mchoko. Hakutaka tena kusema kitu bali asikie hicho ambacho nataka kumwambia.
"Umeona ewe bwana mdogo, nina namna ya kukufanya uishi chini ya maji!"
Nikamwaona akikunja ndita za umakini kwa mbali. Hapa nikajua mada yangu imemgusa.
"Kama afanyavyo samaki, nawe utaishi, kuona na kuzamia. Je, hiko si kitu cha maana kukwambia?"
Nilitazamia jambo hilo litakuwa geni kwake. Niliomba iwe hivyo, kwani kama ingelikuwa tofauti, basi ningeambulia kuachwa nijifie. Hapana. Nilikuja hapa kumsaka Raisi na si kifo.
Akanicheka. "Unamaanisha mtungi wa hewa na mawani ya kuziba macho?" Akaniuliza akibinua mdomo. Akacheka tena mpaka akidaka magoti yake na kushikilia tumbo lake.
"Skiza ewe mtu wa manjano. Mimi si mjinga kama unavyofikiri kichwani mwako. Unadhani sijui unavyovizungumza?"
Akanipa maswali juu yake, mbona ni mwerevu kiasi hiki? Kumbe mtu huyu si tu kwamba anajua lugha yetu, bali pia na teknolojia! Hapa ilinibidi nifanye kazi ya ziada.
"Sawa, basi nitakupa cha kukufanya uone nyakati za usiku!" Nikasema kwa kujivuna. "Utatembea kama mchana usijikwae kisiki au kudumbukia shimoni!"
Hapa akanyamaza kwa muda, macho yakiwaza, alafu akaniuliza, "sasa umeona unidanganye?"
Nikajua hili kwake ni geni.
"Nidanganye ya nini na wakati naomba kubakiziwa uhai tena nikiwa nimezingirwa na maji pande zote?"
Akabinua mdomo na asiseme chochote, akaenda zake. Nikamwita asigeuke nyuma abadani mpaka anatokomea. Nikalaani sana. Nikajiuliza ni nini nitafanya na wakati mikono na miguu yangu imefungwa kwa kamba kiasi kile?
Tukio hilo likanikumbusha mbali sana. Mbali ya mwaka juzi ambapo niliagizwa kwenda kuwakomboa baadhi ya mateka wa kimarekani waliokuwa wanashikiliwa na wanamgambo wa Boko Haram huko nchini Nigeria.
Nakumbuka, nikiwa nimeambatana na wanaume wanne , wamarekani weusi, wa kikosi maalum (special forces), tukiwa mgahawani, tulizingirwa na kuwekwa chini ya ulinzi na watu sita ambao walikuwa wameficha nyuso zao na kubebelea bunduki aina ya ak 47.
Watu hawa kwa namna tulivyowatazama walikuwa ni wanamgambo wa Boko Haram, haswa kutokana na mitandio waliyokuwa wamejivika nayo usoni mbali na kombati walizovaa.
Walituamrisha tunyooshe mikono juu na kututaka tuendee gari walizokuja nazo. Tukafanya hivyo pasipo ubishi. Wakatusweka na kutimka tukielekea mahali tusipopajua kwa maana walitia vichwa vyetu ndani ya mifuko meusi.
Wakiwa wanatupeleka huko, wakawa wanateta kwa lugha ya kiarabu ambayo tulikuwa tunaisikia, wakifurahia kukamatwa kwetu na namna ambavyo wao watanufaika kwa kuongeza mateka wa kimarekani kwenye ghala.
Lakini walijuaje kama sisi ni wamarekani? Ilikuwa ni rahisi sana, na 'in fact' ni sisi ndiyo tulifanya wakatujua hivyo. Hapo mgahawani tulikuja na gari, Nissan double cabin nyeupe, yenye chapa ya USAID ubavuni. USAID ni shirika la Marekani.
Tukiwa mgahawani, tukawa tukizungumza kiingereza chetu, kiingereza cha lafudhi ya Marekani. Na zaidi mgahawa huo ulikuwa ukipatikana katika moja ya kanda ambazo ni mhanga wa mashambulizi ya mara kwa mara ya Boko Haram, kaskazini mashariki wa Nigeria, hivyo kutokea kwa wale wajamaa kilikuwa ni kitu cha kutegemewa. Kitu ambacho unaweza kukibashiri!
Wakiwa wanazungumza hayo yao, tena sisi tukiwa tunawaelewa, nasi tukawa tunazungumza kwa ishara, 'sign language' pasipo wao kuhisi wala kuelewa.
'Sign language' ama 'paralinguistic language' ni lugha isiyo na maandishi ama sauti. Ni utaalamu wa kufikisha ujumbe kwa namna ya kupeana ishara 'signals' na mwenzako akakuelewa na kujibu.
Hiki ni miongoni mwa vitu tujifunzavyo tuwapo mafunzoni kwaajili ya kujiandaa na mazingira mbalimbali ukiwa mhitaji wa kuwasiliana.
Kwa kutumia miguu yetu, tukaminyana, na pia kwa kutumia mikono yetu ambayo ilikuwa imefungwa, tukagusana kwa vidole tukifikishiana ujumbe.
Baada ya hapo, tukangoja. Mwendo wa kama nusu saa tukiwa kimya, ila sio tukiwa malofa. Mmoja wetu tulimpatia kazi ya kuhesabu majira na zoezi la kutushtua pale atakapokuwa ameona mahesabu tuliyoyapanga yametimia.
Kwa muda wa kawaida, kama tulivyokuwa tukiwaza kuwa watu hawa watakuwa wanatupeleka msitu wa Sambisa ambao ni moja ya ngome ya Boko Haram, ilikuwa yachukua kama lisaa limoja na dakika kumi na mbili endapo gari ikienda kwa mwendo wa kilomita themanini kwa lisaa.
Na kama halitoenda kwa mwendo huo, basi tena linakuwa jukumu na mpanga mahesabu kupiga mahesabu hayo kutokana na mwendo ulivyo. Kwa nilivyokuwa nahisi, gari lilikuwa linaenda kilomita mia na ishirini kwa lisaa. Sikuwa mbali na ukweli. Kidogo mahesabu yangu yalikaribiana na mkokotoaji yakiachana kwa kama sekunde kumi na sita tu!
Nikabinywa pajani. Hiyo ilikuwa ni ishara kuwa muda uliokuwa umetengwa sasa umekaribia, zimebaki sekunde nne tu. Nikabinywa na vidole vinne, vitatu, viwili, mwishowe kimoja! Kidogo gari likazama kwa korongo barabarani, hapo hapo, ndani ya dakika chache, tukanyanyuka na kutupa miili yetu mahali tulipokuwa tukisikia sauti za watu na kuhisi uwepo wao!
Ilikuwa ni kitu cha upesi na kushtukiza!
Kule kwenye bodi mulikuwa na wanamgambo sita, watatu wakikalia kushoto na watatu kulia, na basi kwasababu sisi tulikuwa watano kwa idadi, ilikuwa rahisi kuleta shambulizi lenye tija kwa kufuata mipango tuliyopanga kuwa wawili wataenda huku na watano wataenda upande mwingineo.
Ilikuwa pia rahisi kwasababu wanamgambo wale hawakuwa kwenye balansi muda mfupi baada ya gari kupitia mtikisiko. Hivyo, baada ya kufanya hivyo, nikawahisha kichwa changu kwenye mikono ya mwenzangu, akanivua mfuko kichwani.
Kutazama, nikawaona wanamgambo wawili wakiwa wanajiweka tenge kushambulia kwa risasi. Wawili walidondoka chini barabarani, wawili wengine wakiwa wameshikilia bomba la gari kutafuta balansi!
Haraka nikajitupa samasoti kwa chini kuwafuata. Nikamtengua mmoja miguu, na yule mwingine alipotaka kunishambulia, nikajikinga na mwili wa mwenzake, alafu nikampokonya bunduki yule niliyemtumia kama ngao na kisha mwili wake nikamtupia mwenziwe, wote wakadondoka chini!
Nikasikia ti-ti-ti-ti! Haraka nikajilaza chini. Kutazama nikaona mwenzetu mmoja akiwa amedondoka kwa kushindiliwa risasi! Tulikuwa tukishambuliwa na dereva.
Nikatulia na kufyatya risasi moja, ikamdungua kichwa na kummaliza papo hapo, gari likaanza kwenda mrama, lakini kabla halijaleta madhara, mmoja wetu akaliwahi na kuliweka kimyani, kisha tukaendeleza na safari kwenda huko msituni.
Basi kwakuwa wale wenzangu walikuwa na ngozi nyeusi wakajivika nguo za wale wanamgambo na kisha kuigiza kuwa wameniteka kwa lengo la kuzama ndani ya ngome.
Kwa kufupisha habari hiyo, ambayo pengine nitakuja kuisimulia vema siku nyingine, kilichonifanya niikumbuke ni namna tulivyokuta mateka wakiwa wamefungwa kamba mitini, wamarekani na wengine toka nchi za Ulaya. Na kwasababu za kioparesheni, nami nikatiwa kambani kama wale mateka wengine, lakini kamba yangu ilikuwa legevu kwa maana kwamba punde mambo yatakapoharibiwa nitoke hapo.
Ilikuwa ni tofauti na oparesheni ya Raisi kule kisiwani kwani kamba ya kisiwani ilikuwa imekazwa haswa na hakukuwa na namna ya mimi kuchoropoka isipokuwa kwa msaada. Na tofauti kabisa na Nigeria, siku hiyo wenzangu wote walikuwa hawajiwezi. Hawakupewa tiba kama ilivyokuwa kwangu, hivyo siku hiyo mimi ndo' nilikuwa na jukumu la kuwaokoa.
Muda ukaenda na giza la usiku likafika. Punde kidogo, baada ya giza hilo kuingia, nikaanza kutambua kwanini tulifungiwa kwenye miti ile mipana. Nilianza kuhisi mgongo wangu unafinywa kuzamia ndani, na kadiri muda ulivyokuwa unaenda, nikawa nahisi maumivu makali ya mgongo.
Nikajitahidi kujichoropoa, wapi! Zaidi nikajiongezea maumivu zaidi. Niliporusha macho kuwatazama wenzangu, nikawaona wakiwa wametulia tuli. Hawakuwa na fahamu!
Nikahisi usiku huu ndiyo mwisho wetu.

**
 
*NYUMA YAKO -- 06*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA
Nikajitahidi kujichoropoa, wapi! Zaidi nikajiongezea maumivu zaidi. Niliporusha macho kuwatazama wenzangu, nikawaona wakiwa wametulia tuli. Hawakuwa na fahamu!
Nikahisi usiku huu ndiyo mwisho wetu.
ENDELEA
Hata nikainamisha kichwa changu kama kristo msalabani, sasa nimekwisha. Mwanaume miliyeshiriki kwenye misheni kadhaa za hatari, nakuja kuuawa na hawa washamba wa msituni. Aibu iliyoje?
Ila, nikajadili na nafsi yangu, haikuwa kama nilivyokuwa nawaza. Hamna mtu aliyedhani hapa kuna watu, na zaidi ya yote, kwenye shambulio la kushtukizwa, hamna mjanja. Atakayemuwahi mwenziwe basi ndo anakuwa mshindi. Hata simba akiwa mbugani, anawezwa wahiwa na nyoka, akamalizwa!
Hapa tulikuwa tumewahiwa, na japo lilikuwa jambo chungu kwangu, ila ndiyo ulikuwa uhalisia. Sikuwa na ujanja wa ziada.
Nikiwa nimejikatia tamaa, nangoja sasa 'nimezwe' na ule mti kama tulivyonenewa, nikahisi kitu huko msituni! Masikio yangu yakasimama na macho yangu yakang'aza. Ilikuwa ni kama kishindo cha mtu au mnyama ila sikuona kitu!
Kishindo hicho hakikukoma, kikaendelea tena na tena na kunijaza hofu huenda akawa mnyama wa mwituni. Endapo akitokea hapo tutajiteteaje? Nikapata mawazo yaliyonipa tena nguvu ya ajabu kupambana na kamba nilizofungiwa.
Nikapambana kujisukuma na kusukuma, waapi! Zaidi nikajitia alama nyekundu mwilini, pia majeraha na maumivu tu! Sikufanikiwa wala kwa dalili!
Kishindo kikaendelea kusikika huko gizani msituni na mara sauti ikasema, "ewe mtu wa manjano, bado upo?"
Nikaitambua sauti hiyo kuwa ya bwana yule mdogo. Bwana azungumzaye lugha yetu. Yeye alitokea upande wangu wa kushoto baada ya punde na kisha kunisogelea kwa karibu.
Akanitazama machoni. "Naona bado upo. Vipi, unaendeleaje?"
"Hali inazidi kuwa mbaya," nikamjibu na kumsihi, "naomba uniweke huru!"
"Si kwa haraka hivyo," akasema akitikisa kichwa chake, kisha akahema akinitazama kama mtu anayefurahia mateso yangu. Akaniuliza, "kwanini mlivamia kijiji chetu? Ni nini tuliwakosea?"
Nikamtazama kwa macho yangu malegevu. Uso wake ulikuwa unang'azwa na mwanga wa mbalamwezi. Nikafungua kinywa changu kikavu na kumwambia, "sijawahi kuja hapa, hii ni mara yangu ya kwanza. Nikuambieje unielewe?"
Mara akatoa kijiwe fulani nyuma ya mgongo wake. Kilikua ni kijiwe kidogo kimachong'aa. Kwa mwanga ule uliokuwepo nilikiona ni kijiwe chenye rangi nyekundu, sikujua mwangani mwa jua kingeonekanaje.
Akaniuliza akinionyeshea kijiwe hicho, "ni hichi ndicho mnatafuta?"
"Hapana!" Nikajikakamua kukanusha. "Sina shida na chochote toka kwenu. Nimefika hapa kumtafuta mtu aliyepotea, na si vijiwe!"
"Mtu gani huyo? Yule aliyedondoka toka kwenye nyota?" Akaniuliza akishika kidevu chake.
Nikamkazia, "Ndio huyohuyo! Je, umemwona?"
"Ndio. Nimemwona."
Hapa nikatoa macho. "Yupo wapi? ... tafadhali nipatie mtu huyo nasi tutaondoka msituone tena!"
Akatulia kidogo. Akanitazama kwa mafikirio alafu akaniuliza, "nikikuonyesha utanipatia nini?"
"Chochote kati ya tulivyokuja navyo!"
"Mi' nataka kile cha kuonea usiku. Mimi ni mwindaji. Nahisi kitanisaidia sa--"

"Nitakupatia, usijali!" Nikamkatiza. "We twende nionyeshe wapi alipo mtu huyo!"
Basi akanifungua kamba na tukaanza safari. Lakini hakuwa mjinga, aliniweka mbele yeye akiwa nyuma yangu. Mkononi alibebelea mkuki na kinywani alikuwa ameshikilia filimbi kwa lips zake. Filimbi hii, kwa alivyoniambia, ingemwamsha kila mtu kijijini aje kunitafuta endapo ningejitia ukaidi.
Sikupanga kuwa mkaidi. Lah! Hamu yangu ya kuuona mwili wa mtu ambaye nilihisi ndiye namtafuta ilikuwa kubwa kuliko kufanya njama za kutoroka.
Tukasonga, akiwa ananielekeza, mpaka eneo fulani ambapo alinitaka nisimame na kutulia. Nikafanya hivyo. Hapo toka kwenye kibanda kimoja kidogo kilichotengenezwa kwa matawi ya miti, akapenyeza mkono wake na kutoa mti mmoja mrefu, sikujua wa nini, akatoa pia na dude fulani kama rungu kisha akaniambia tuendelee na safari.
Tulipotembea kwa muda kidogo akaniamuru nisimame na kisha akaniambia, "mwili huo upo humo shimoni, utazama humo uangaze, nami nitakuvuta kwa mti utoke nje!"
Alipoyasema hayo akaniwashia lile dude nililodhani ni rungu, tena kwa haraka akitumia mawe, alafu akanishikisha ule mti mrefu nami nikazama na ginga la moto ndani ya shimo.
Lilikuwa ni shimo refu, na kadiri nilivyokuwa nazama nikawa nahisi harufu ya mzoga puani mwangu. Zaidi na zaidi. Na nikiwa sasa nimefikia nchani mwa fimbo ile ambayo nimeishikilia, nikawa nimefika chini kabisa! Kumbe ile fimbo ilikuwa na vipimo sawia kulingana na shimo.
Nikaangaza kutazama na ginga langu la moto, humo nikaona miili kadhaa, na mmoja kati yao, ambao ulikuwa mpyampya tuseme, ukawa umekamata macho yangu. Mwili huo ulikuwa mpana na wenye kuvalia suti nyeusi. Ulikuwa umelala kifudifudi.
Nikachuchumaa na kuugeuza niutazame. Haukuwa wa Raisi! Nikawaza utakuwa ni miongoni mwa wale maajenti wasiokuwepo kule ndani ya ndege. Sasa mwili wa Raisi utakuwa wapi? Nikajiuliza nikiendelea kuangazaangaza. Sikuuona!
Nilishika kiuno changu na kushusha pumzi ndefu.
"Vipi? Si huo?" Akaniuliza yule bwana mdogo juu ya shimo.
"Hapana, si wenyewe!"
Nikamwomba mti, anivute juu. Nilipopanda nikakung'uta mwili wangu na kumuuliza, "hakuna mwingine ninaoweza kutazama?"
Nikamwona akibinua mdomo wake. "Hapana, hili ndilo shimo pekee lililopo hapa."
Nikanyamaza nikiwaza. Akan'tazama na kunitahadharisha, "lakini makubaliano yetu si yapo palepale?"
Sikumjibu. Mimi nilikuwa na mawazo yangu kichwani. Akili yangu yote ilikuwa inawaza namna gani ambavyo naweza kuupata ama kuuona mwili wa Raisi. Hali hiyo ikampatia hofu yule bwana mdogo, nadhani akahisi nitamgeuka. Akanionyeshea mkuki wake na kuniambia tena, "makubaliano yetu si yapo palepale?"
"Ndio," nikamjibu kumtoa hofu. "Makubaliano yetu yapo palepale!"
Kidogo akatulia. Kwa muda huu nikawa nimemtengeneza rafiki. Nikapata mwanya wa kumuuliza kwanini aliniamini akanifungulia pale mtini ilhali mwanzoni walin'tilia shaka.
Akanitazama kwanza. Akatabasamu kwa mbali na kuniambia, "wewe sio kama wale! ... wale waliokuja kutuvamia na kuwaua wenzetu!"
"Umejuaje kuwa sisi sio wale?"
"Kwasababu ya kile kijiwe!" Akanijibu aking'aza macho. "Watu wale waliokuja na kuwaua wenzetu hawakuwa wanataka kingine zaidi ya mawe! ... wewe nilikuona upo tofauti. Sikuona tamaa ndani ya macho yako punde nilipokuonyesha kile kijiwe."
"Lakini tuliwaambia mwanzoni kuwa sisi tunamtafuta mwenzetu!"
"Ndio, ila si rahisi kuamini ... poleni."
"Basi naomba ukawasaidie wale wenzangu kama ulivyofanya kwangu."
"Siwezi!"
"Kwanini?"
"Mimi sina ile dawa waliyokupa wewe."
"Nani anayo?"
"Yule aliyekupa wewe. Anaitwa Toliso."
"Hauwezi kwenda mwomba? ... hauwezi ukamwambia kuwa sisi si kama wale waliokuwa wanawadhania?"
Bwana yule akanyamaza. Akausimika mkuki wake ardhini na kisha kidevu chake akakiweka juu ya kitako cha mkuki. "Si rahisi kama unavyodhani," akanijibu akiwa ameng'ata meno yake.
"Bwana yule, Toliso, ni mkatili na mkali. Hawezi kunielewa."
Nikamsogelea karibu na kumshika bega. "Tafadhali, sisi hatuna hatia. Hakukuwa na haja ya kutuadhibu namna ile. Kama kuna namna yoyote ambayo naweza kukusaidia kupata hiyo dawa, nambie nami nitafanya kwa moyo wote!"
Akatikisa kichwa kisha akafungua kiganja chake. "Kabla hatujaendelea na majadiliano yoyote, nipe kwanza kile ulichoniahidi."
"Nitakupatia il--"
"Nipe!" Akasisitiza akinikazia macho , basi nikaona si tabu, nikaongozana naye mpaka kule upande tulioingilia kisiwani. Huko tukute vile vitu tulivyoviacha, mitungi ya hewa na hata hiyo miwani ya kutazamia usiku.
Bahati tukavikuta, nikamkabidhi. Akajaribisha na kuona ni vema, imempendeza. Akafurahi sana. "Hii nitaitumia kuwindia nyakati kama hizi!" Akasema akitabasamu. Hata meno yake yaling'aa kinyume na kiza.
Nikamkumbusha, "fanya basi tukapate ile dawa!"
Akaiweka ile miwani kibindoni alafu akanitazama, "ewe bwana wa manjano, mbona wewe mbishi sana! Huoni kheri nimekusaidia ukaenda zako?"
"Nitaendaje pasipo wenzangu? Moyo wangu utakuwa mzito!"
"Sikia ... si kwamba sitaki kukusaidia. Namwogopa sana Toliso. Mkono wake ni mwepesi sana kutoa adhabu. Si mtu anayejishauri mara mbilimbili kummaliza mtu!"
"Nitakusaidia dhidi yake."
Akatabasamu, "wewe? ... unadhani unaweza kupambana na Toliso?"
"Kwanini nisiweze?"
Akashindwa kujibana na kicheko. Alipomaliza kucheka akaniambia, "mwili wako unaingia mara mbili na nusu ya Toliso. Akikudaka na mikono yake kama mibuyu, atakukamua mpaka hayo macho yatoke nje. Hujionei huruma?"
"Bwana mdogo," nikamwita nikimtazama. "Nitafanya lolote lile, nitapita kwenye hatari yoyote ile kuwasaidia wenzangu. Naomba tusipoteze muda, tuelekee huko haraka!"
Akanitazama katika namna ya kunionea huruma. Kwa namna hiyo nikajua ni kwanini anamzungumzia Toliso katika namna ya hofu. Ila nadhani bado nami hakuwa ananijua vema. Hakuwa anajua mimi ni mtu wa namna gani. Tangu tuingie kwenye mikono yao, hajaona vumbi langu. Sikushangaa kwanini alikuwa ananitilia shaka.
Hakuwa anajua japo mimi si nyani mzee, nimekwepa ncha nyingi za mishale!
Basi kwakuwa nimemlazimisha na kumsihi sana, tukaenda huko.

**
 
*NYUMA YAKO --- 07*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Hakuwa anajua japo mimi si nyani mzee, nimekwepa ncha nyingi za mishale!
Basi kwakuwa nimemlazimisha na kumsihi sana, tukaenda huko.
ENDELEA
Ilikuwa ni safari iliyotuchukua muda wa dakika kama kumi na tano hivi, tukawasili mbele ya kijumba kidogo, mbavu za mbwa. Nyumba iliyotindwa na majani na kusimikwa na miti minene. Haikuwa na madirisha, mlango ulikuwa wazi.
Kutoka humo, mtu alikuwa akikoroma sana kana kwamba simba au mtu aliyekabwa. Bwana mdogo yule, ambaye sasa njiani aliniambia jina lake, aitwa Buyu, akaniambia huyo akoromaye ni Toliso. Kijiji kizima wamfahamu kwa tabia yake hiyo, lakini kisitupumbaze kwani amekuwa akisemwa kuwa hulala macho!
Yaani japo anakoroma hivyo, huwa macho, na kitu kidogo tu chaweza kumwamsha na kumdaka mvamizi wake. Nilijifunza kuwa Toliso ni mtu mwenye kupewa mawazo mengi ya kutisha. Mtu anayeogopwa na kudhaniwa si wa kawaida. Niliendelea kulithibitisha hilo kadiri tulivyozidi kusonga, ila kwangu mimi halikunijengea woga hata kidogo.
Sikuona kama mtu wa kunifanya nihofie. Nimepita sehemu nyingi nikakutana na wengi wa kunihofisha na wote nikawalaza chini. Atanishindaje huyu wa kwenye ulimwengu wa nyuma?
Bwana mdogo akanitazama na kuniambia, "sasa nazama ndani, niombee nitoke salama. Na kama si hivyo, usidiriki kujitokeza ukapambana, we nenda zako!"
Sikutaka kubishana naye hapa, nikamkubalia kazi iende kwa wepesi. Akazama ndani na kwa uangalifu, nikiwa namchungulia mlango akasonga akinyata.
Alipozidi kuzama ndani nikawa simwoni sasa kutokana na giza, na ndani hakukuwa na mwanga hata kidogo kutokana na ukosefu wa madirisha. Sasa nikawa nategemea masikio yangu kusikia kinachoendelea japo nayo muda fulani yalikosa taarifa kutokana na ukimya wa hatua za bwana mdogo yule, Buyu.
Zikapita sekunde kama kumi hivi, nadhani alikuwa akiangaza kutafuta ile dawa. Kwenye sekunde ya kumi na moja, kwa mujibu wa makadirio yangu, nikahisi sauti ya kitu kikidondoka! Moyo wangu ukafanya pah! Nilihofu huenda Toliso akaamka na kumsababishia matatizo Buyu, ila haikuwa hivyo, nikaendea kusikia sauti ya mtu akikoroma. Angalau nikapata afueni.
Nikaendelea kutulia nikiskiza. Zikapita tena sekunde tano, hapo ndiyo nikapata jaka la moyo! Sauti ya mtu akikoroma ilikata ghafla na mara sauti nzito ikavuma kusema, "Taris khanje?"
Na kabla sijasikia chochote, nikaona mwanga umewaka ghafla mule ndani. Hapo nikamwona Toliso akiwa chini ameshikilia taa mkono wake wa kushoto! Taa hiyo haikuwa kama ambayo waijua wewe. Lah! Ilikuwa ni kama buyu lililozungushiwa utepe unaopitisha mwanga, ndani yake kulikuwa na wadudu wadogowadogo wengii ambao mikiani mwao walikuwa wakitoa mwanga.
Nilishangazwa na sayansi hii! Baadae nilikuja kujifunza kuwa, kuwasha taa hiyo, ni kwa kutikisa hao wadudu waliomo ndani, wakiamka hujiwasha kama ni kiza. Ukiweka buyu chini, basi nao hulala na kujizima!
Basi kuamka kwa Toliso hakukuwa jambo la kawaida kwa Buyu, hata kwangu pia. Bwana huyo, mzito mrefu na mpana, alisimama akimtazama Buyu ambaye alikuwa amesimama pembeni ya shelfu yake nyeusi. Buyu akahofu sana, nilimwona akitetemeka. Aliwahi kuomba msamaha na kuomba abakiziwe uhai wake. Japo sikuwa najua lugha anayoizungumza, matendo yake yalionyesha hayo niyasemayo.
Nikamwona Toliso akiweka taa yake chini, kisha akabinjua vidole vyake na kuviliza mifupa. Akanguruma akisema lugha yao ya ajabu kisha akamnyaka Buyu na kumnyanyua juu kwa mkono mmoja!
Hapo nikamwona Buyu akibadili sura. Hakuwa mwenye huruma tena bali aliyefura hasira. Na akiwa amekabiwa juu, akawa anarusharusha mateke na ngumi ambazo hazikusaidia chochote kwa Toliso! Zaidi mwanaume huyo akacheka na kukodoa macho yake ya kutisha! Akamminya zaidi Buyu.
Hapo ndiyo nikaona ni muda wangu muafaka wa kujongea kumwokoa Buyu. Nikazama kwa fujo!
"Mwache!" Nikaropoka. Bwana yule akanitazama na kisha akasema kwa lugha yake nisiyoielewa, akamtupia Buyu chini na kunisogelea. Akanitazama na kutabasamu.
"Usidhani kama mimi nakuogopa," nikamwambia nikimnyooshea kidole na kumtazama machoni. Alikuwa ni mrefu kuliko mimi. Alinitazama kana kwamba mtoto mdogo!
Ghafla akanisukumia nje ya jengo lake, nikipaa nikatua chini na kujibamiza mgongo! Mgongo uleule ambao ulikuwa na maumivu ya pale mtini!
Akanisongea kwa hatua zake nzito, kisha akasimama karibu na mimi. Hapo akajivuna kwa lugha na sauti yake ya kukoroma. Kidogo nikasikia sauti kali ya filimbi! Aliipuliza Buyu. Sikujua ni kwasababu gani. Basi bwana yule, Toliso, akaninyanyua juu na kunisogeza usoni mwake, akanitazama kwa sura ya kebehi.
Hakuwa anajua 'anadeal' na mtu wa aina gani. Bila shaka alidhani mimi na wale watu anaowatawala tuko sawa. Nikaona sasa ni muda wa kumwonyesha utofauti.
Hataka nikamkita kwenye 'angle' dhaifu ya shingo, akaniachia na kudaka shingo yake. Hajakaa sawa, nikazunguka na kumzaba teke kali la uso, akadondoka chini kama mzigo!
Kutazama nikaona watu wakiwa wamejongea hapo. Walikuwa wamebebelea mikuki mikononi mwao, ila hawakunidhuru. Wakawa wamesimama wakinitazama mimi na Toliso. Hapo ndiyo nikajua maana ya ile filimbi ya Buyu!
Kidogo Toliso akajikusanya na kuamka. Akanyoosha shingo yake kah-kah! Alafu akanguruma na kunifuata kwa hatua pana. Hatua moja tu akawa amenifikia, akarusha ngumi yake, nikaikwepa kisha haraka nikakwea kifua chake na kumtifua na goti la kidevu! Akazubaa kwa maumivu. Nikapaa juu na kumzika na teke la kisogo, akadondoka chini asiamke tena!
Hapo Buyu akanisogelea na kunitazama kwa mshangao. "Umemmaliza!" Akatahamaki. Akanikumbatia kwanguvu na kunishukuru sana kisha akawageukia watu wake na kuwaongelesha maneno nisiyoyelewa. Baadae ndipo nikaja kujua kuwa Toliso alimwambia Buyu kuwa yeye ndiye aloyewamaliza wazazi wake kwakuwa walikuwa wakaidi.
Na baada ya kufanya hivyo, akasingizia mateka wa kizungu waliokuja kuvamia kijiji hicho. Basi, katika namna hiyo, nikawa mkombozi! Wanakijiji wakaninyanyua juu kwa shangwe wakiimba nyimbo zao, lakini mimi nikawasihi kwanza wakawasaidie wale wenzangu kule msituni mitini!
Upesi wakachukua dawa na taa ya Toliso, tukaelekea huko msituni na kuwapatia dawa wale wenzangu. Angalau wakapata ahueni, wakapatiwa pumziko maana walikuwa wamechoka mno! Tuliwakuta wakiwa wamebabuka migongoni. Migongo imekuwa mekundu kama bendera.
Hivyo usiku huo ukawa umepita hivyo. Nililala kwa uzito sana maana nilikuwa nimechoka sana kwa purukushani, lakini hata hivyo, kama ilivyo kawaida, nikajitahidi kuamka mapema, japo si mapema yangu iliyozoeleka. Niliamka jua likiwa limeshang'aza.
Kutazama nikaona wanakijiji wakiwa wanaendelea na shughuli zao. Wengine walikuwa wanatwanga, wengine wanakata nyama, wengine wanakata matawi na magome ya miti, wengine wakiwasha moto na kadhalika.
Mimi nilikuwa ndani ya chumba kidogo, sikujua ni cha nani, tangu nilipoingia usiku mpaka muda huo wa asubuhi sikuona mtu humo, nadhani walinipatia kwa heshima. Nilitoka humo na kuangaza angaza pia kujinyoosha mwili wangu alafu nikamtafuta bwana yule mdogo na kumweleza haja yangu, "naombeni mnisaidie kumsaka Raisi wangu. Naamini atakuwapo maeneo haya."
Basi kwa kushirikiana na watu wao, tukaanza kusaka kila eneo. Wale wenzangu walikuwa bado wapo mapumzikoni, bado hawakuwa wanajiweza kuzungumka. Tukazunguka kisiwa kizima na baada ya hapo tukazunguka na baharini kwa kutumia mitumbwi yao. Hatukuona kitu kabisa!
Sasa imani yangu ikaanza kunitoka. Raisi hakudondokea huku. Au Raisi hakuwa kwenye ndege! Sikudhani kama kazi hii ingeanza kwa ugumu mapema hivi ...

**
 
*NYUMA YAKO --- 08*

*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Basi kwa kushirikiana na watu wao, tukaanza kusaka kila eneo. Wale wenzangu walikuwa bado wapo mapumzikoni, bado hawakuwa wanajiweza kuzungumka. Tukazunguka kisiwa kizima na baada ya hapo tukazunguka na baharini kwa kutumia mitumbwi yao. Hatukuona kitu kabisa!
Sasa imani yangu ikaanza kunitoka. Raisi hakudondokea huku. Au Raisi hakuwa kwenye ndege! Sikudhani kama kazi hii ingeanza kwa ugumu mapema hivi ...
ENDELEA
Saa nne asubuhi, jengo la J. Edgar Hoover, makao makuu ya FBI.

Nilikuwa hapa nikiwa na shida ya kumwona Miss Daniele James, mpelelezi wa ndani wa swala hili la kupotea kwa Raisi. Alikuwa mtu aliyetingwa sana, alikuwa akitoka hapa na kuingia kule, kule na hapa, alipokuja kutulia ilikuwa ni kama baada ya dakika kumi tangu niingie hapo.
Akanitazama kwanza alafu akachukua faili toka kwenye shelfu, akalipekua upesi na kisha kama mtu anayenidhihaki kwa mbali, akaniuliza, "umepata nini huko, Anthony?"
Nikashusha kwanza pumzi ndefu, nikatikisa kichwa changu na kubinua lips pasipo kusema kitu. Akatabasamu kwa mbali. Akatazama tena faili lake kwa ukimya kidogo, nikamuuliza,
"Ni nini wewe umepata?"
Akanitazama kwanza, akafunga faili lake na kunitazama kwa macho ya kichovu ila yaliyo imara. Akaniuliza, "nikikuambia Raisi ametekwa, utasemaje?"
"Kwanini unasema hivyo?" Nikamuuliza. Sentensi yake hii ilinivuta na kunifanya niwe makini zaidi. Akakuna kwanza kichwa chake.
"Anthony, kwa namna nilivyofuatilia na kutazama baadhi ya matukio, natokea kuamini kuwa huenda Raisi akawa ametekwa, tena kabla ya ndege kupaa!"
"Lakini imewezekanaje hilo?"
"Sijajua, badi sijalikamilisha jambo hilo. Lakini kwa ushahidi nilioupata, naona niko sahihi kusema ninayoyasema."
"Naomba basi unijuze," nikamsihi.
"Usijali, wewe ni mshirika wangu kwenye hili, ila ..." akanitazama akinikodolea. "Unajua hivi sasa upo kwenye ardhi ya Marekani, I am the boss here, sawa? Utafuata yale nitakayokuwa nakuambia na kukuelekeza."
Kabla sijajibu, akaendelea kumwaga maneno. "Kutokana na utafiti mdogo nilioufanya, nikisaidiwa na Secret services, nimebaini kuwa Raisi alikuwa anaumwa hapa karibuni. Hali yake kiafya haikuwa nzuri sana, tuseme hivyo. Na kama utakuwa ulifuatilia vema utakuwa umegundua hakuwa akihudhuria baadhi ya office matters kwa sometimes."
"Sikuwa nafuatilia," nikawahi kumhabarisha. "Nilikuwa zangu likizo, na kidogo nikajitenga na mambo haya ya kuumizana vichwa."
Lengo langu la kumweka bayana ni kumtengenezea mazingira ya yeye kunihabarisha juu ya kila kitu anachokijua. Nilitaka adhanie kuwa mimi ni pipa tupu na hivyo basi anijaze na kila taka anayoijua yeye.
"Basi kama haukuwa unajua, ndo' nakujuza. Swala hili lilinifanya nifuatilie kidogo hili jambo na kuona ni kwa namna gani linaweza likawa na mahusiano na kupotea kwa Raisi, ila bado sikuona mahusiano ya moja kwa moja."
"Sasa mbona ukasema Raisi huenda akawa ametekwa?" Nikamuuliza. Akafungua droo yake na kutoa chupa fulani aitumiayo kuhifadhia vikorokoro, humo akatoa mashine ya kumsaidia mtu mwenye pumu kuhema.
Mashine hiyo ilikuwa imehifadhiwa ndani ya kifuko kidogo kilaini. Akanionyeshea, "unaona hii? Ni ya Raisi!"
Nikakidaka na kukitazama vema. "Umekipata wapi?"
"Uwanja wa ndege!" akanijibu akifunga droo yake. "Kilikutwa kikiwa chini. Haingii akilini kuwa kitu hicho kitakuwa kimedondoka kwa bahati tu. Raisi huwa nacho muda wote, aidha mkononi au mfukoni. Na hatua nne toka kilipookotwa, kuna alama mbili za tairi ya gari!"
Akanitolea picha na kunionyesha. Kwa namna alama hizo zilivyo, ilionyesha wazi kuwa usafiri ulotumika hapo ulikuwa ni mdogo. Kwa mahesabu ya upesi, ni vile vigari vidogo viwavyowandawanda uwanja wa ndege.
Ina maana kimojawapo kitakuwa kilihusika na kumsafirisha Raisi? Lilikuwa fumbo. Nikiwa natazama picha hiyo, simu yangu ikaita mfukoni. Nikaitoa na kutazama. Ni Jack Pyong! Nikapokea na kumuuliza, "nini shida?'
"Njoo ofisini mara moja. Una mgeni!" Aliniambia hivyo kisha akakata simu. Nikafiriki kidogo juu ya alichoniambia kabla sijarudisha kichwa changu kwenye ile picha na kisha usoni mwa Daniele.
"Kuna kingine ulikipata?"
"Hapana, si rahisi kama unavyowaza, Anthony."
"Najua. Vipi umefanya mawasiliano na watu wake wa karibu?"
"Mkewe hayupo kwenye mood ya kuongea. Tangu mumewe aliporipotiwa kupotea, amekuwa wa kulia na kujitenga. Sijajua kwa sasa kama atakuwa radhi."
"Ni muhimu kuongea naye."
"Najua, Anthony. Nataka sana kufanya hilo ila siwezi kumlazimisha. Yuko depressed hivi sasa, nadhani muda unaweza kumtuliza."
"Vipi kuhusu makamu wa Raisi?"
"Nimeongea naye mara moja. Unajua hivi sasa amekuwa busy sana maana ni yeye ndiye aliyekaimu kiti cha Uraisi. Natazamia kuonana naye hapa karibuni kwa mazungumzo zaidi."
"Basi utakapoenda huko, usisite kunihabarisha twende wote. Sawa?"
Akanitazama kwanza kisha ndiyo akasema, "sawa, usijali." Kidogo nikahisi sauti ya mngurumo mfukoni. Ilikuwa ni simu. Nikaitoa na kuitazana, nikaona ishara ya ujumbe toka kwa Jack Pyong. Sikuusoma, nikanyanyuka na kumuaga Daniele.
"Tutaonana muda wowote!"

**

"Kama utakuwa hujaniitia la maana wewe macho manne, nitakumaliza!" Niliropoka nikiingia ofisi ya Jack Pyong. Ofisi yake na yangu hutenganishwa kwa umbali wa hatua thelathini za mtu mzima. Kwenye upande wa kuingilia ndani ya jengo, ofisi yake i karibu na mlango, ila kwa upande wa kutokea, yangu i karibu. Kama hujalelewa, achana nayo isikuumize kichwa.
Nilimkuta Jack Pyong akiwa amerelaksi kwenye kiti chake, miguu ameweka juu ya meza na mikono yake ameifanya mto kulazia kichwa. Ana 'swing' kutoka kushoto kwenda kulia, kulia kwenda kushoto. Mezani hapo kuna kopo kubwa la kahawa nyeusi.
Akanitazama na kutabasamu.
"Nawe ukaja upesi, sio?" Kisha akacheka na kugonga vivanja vyake. "Mjinga kweli wewe. Mgeni gani huyo wa kuja kukufuata huku?" Hapo nikachomoa simu yangu na kuutazama ule ujumbe alionitumia nikiwa na Daniele,
'Yule dada wa Hong Kong yupo hapa!'
Laiti ningeusoma ujumbe huu nikiwa kule kwa Daniele, nisingesumbuka kuja kwa huyu lofa. Ningejua ananidanganya wazi kwani mwanamke yule hakuwa anatambua kama mimi nafanya kazi CIA. Sikumwambia hilo.
Nikamzaba Jack Pyong kofi la kichwa na kumwambia, "hivi unajua nilikuwa kwenye mambo ya maana?"
"Yapi?" Akaniuliza kwa masikhara. "Hata hili nililokuitia ni la maana!"
"Lipi hilo?"
"Si la huyo mgeni! Huyo mwanamke! ... kuwa mkweli, Anthony. Bado unamkumbuka, sio?"
Nikavuta kiti na kuketi. Nikamtazama Jack Pyong na kumwambia, "kama kuna kitu nitakuwa nakumbuka kuhusu huyo mwanamke, ni simu yangu tu. Si vinginevyo. Nahisi yeye ndo' alichukua simu yangu."
"Hapana, Tony," Jack akatikisa kichwa. "Ni moyo wako ndio aliuchukua, si simu!"
"Jack, hivi kuna muda unaacha masikhara na kuwa serious?"
Akanyamaza. Akanitolea simu yake mfukoni na kisha kuifungua. Akanipatia. "Ebu tazama!"
Nilipoangaza nikaona 'chatting' zake na mtu fulani kwenye mtandao wa whatsapp. Nilipotazama picha ya mtu huyo anayechat naye, nikagundua ni yule mwanamke mzungu wa kule Hong Kong! Nikamtazama Jack nikimtumbulia,
"We macho manne, kumbe ulikuwa na namba yake!"
"Sikuwa nayo. We huoni mwanzo wa text? ... ni yeye kanitafuta. Hata jina bado sijamtunzia."
"Amekupataje?"
Akapandisha mabega juu, "sijui!"
Nikatazama tena zile jumbe. Walikuwa tu wamejuliana hali na kukumbushiana ile siku. Nikamuuliza, "Kwanini hukumuuliza juu ya simu yangu?"
"Simu ipi, Tony? ... unadhani ana simu yako?" Jack akaniuliza akinitazama. Akanipokonya simu yake na kuendelea kutext.
"Anaweza akawa anajua. Jaribu kumuuliza."
Hakunijibu, kidogo akatulia kisha akasema, "Usijali, anakuja Marekani. Utamuuliza hayo yote."
"Are you serious?"
Akanionyeshea simu yake. "Yes, I am."
Niliposoma hizo texts nikaona ahadi ya mwanamke huyo kuja Marekani mwisho mwa juma. Kidogo nikatahamaki.
"Sasa ushindwe mwenyewe!" Jack Pyong akasema na kunikonyeza. Pasipo kumuaga, nikanyanyuka na kutoka ndani ya ofisi yake. Huko nyuma akapayuka, "baadae saa tatu tukutane dinner!"
Sikumjibu, nikaenda zangu. Nilipofika ofisini nikaketi na kuwaza juu ya mambo yale ambayo Daniele alinieleza. Mosi, Raisi kuumwa. Pili, kifaa chake cha kupumulia kuokotwa uwanja wa ndege. Kidogo nikawa nimepotezwa fikirani mpaka pale ambapo mlango wangu uligongwa.
"Nani?"
Sikujibiwa, mlango ukafunguliwa. Alikuwa ni mwanamke mrefu mwembamba mwenye miwani mikubwa ya kumsaidia kuona. Mwanamke huyu aitwa Jolene, ni mfanyakazi mwenzangu, yeye akijihusisha kama secretary.
"Nina ujumbe wako," alisema akinijongea.
"Sasa Jolene si uwe unabisha hodi?"
Hakunijibu. Akanitazama na macho yake kama ya paka kisha akaweka kikaratasi mezani na kwenda zake. "Yani mwanamke huyu ana matatizo kweli!" Nikalalama nikiokota kile kikaratasi.
Niliposoma nikakutana na ujumbe, "NITAFUTE" kisha chini yake kuna namba za simu na anwani ya eneo.

**
 
*NYUMA YAKO -- 09*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Hakunijibu. Akanitazama na macho yake kama ya paka kisha akaweka kikaratasi mezani na kwenda zake. "Yani mwanamke huyu ana matatizo kweli!" Nikalalama nikiokota kile kikaratasi.
Niliposoma nikakutana na ujumbe, "NITAFUTE" kisha chini yake kuna namba za simu na anwani ya eneo.
ENDELEA
Nilitaka kumwita Jolene nimuulize kuhusu huo ujumbe ila nikaona si staha. Kwanza kwa namna nilivyomuona ni kama vile amechoshwa, lakini zaidi ya hapo, anaweza akawa hana majibu ninayotaka. Nikafikiri kidogo kisha nikanyanyua simu yangu na kupiga simu ile iliyoandikwa karatasini.
Ikaita mara mbili na kupokelewa. Kabla sijanena, nikaulizwa, "Marshall?" Sauti ilikuwa 'moderate', si nzito wa nyepesi. Ila ndani yake ilikuwa na mkazo.
"Ndio, ni mimi. Wewe ni--"
"Fanya tuonane," sauti ikanikatisha. "Fuata anwani iliyoandika hapo, fika." Kabla sijanema tena, simu ikakatwa. Hapo nikabakia na maswali. Ni nani huyu mwenye kuniamuru kiasi hiki?
Niliweka simu yangu mezani nikiwaza. Sikutaka kwenda huko. Lakini pia kwanini nisiende? Huwezi jua ... ila nitabainishaje kuwa si mtu mbaya? ... kapata wapi namba yangu ya simu?
Niliona sasa nina haja ya kwenda kuonana na Jolene kwa maswali haya, lakini sikunyanyuka ujumbe ukaingia kwenye simu yangu, "nina jambo la kukuambia kuhusu Raisi!" Nilipotazama namba, ilikuwa ni ileile niliyotoka kuwasiliana nayo hapo awali.
Nikanyanyuka na kuweka koti begani, nikatoka ofisini. Kurusha macho kumtafuta Jolene, sikumwona. Sikujibughudhi, nikaelekea nje na kujipaki kwenye gari langu kisha nikatimka kwenda huko kulikoelekezwa kwenye anwani. Kimahesabu haikuwa mbali sana na mahali pangu pa kazi, kama vile kilomita kumi tu.
Nikiwa barabarani, nikapata wazo la kumshirikisha Daniele kuhusu hili. Kiutaratibu hii ilikuwa ni kazi ya FBI agent, yaani Daniele, ila kwasababu nalipokea wito, sikuona haja ya kuuvuka.
Nikanyanyua simu na kumpigia. Kwa umbali, toka kule Washington DC mpaka hapa Langley, Virginia, ni maili mia moja sabini na tisa. Kwa mujibu wa taarifa za GPS waweza kutumia masaa matatu kasoro kufika hapa endapo ukitumia usafiri wa gari, kama ndege ni dakika arobaini tu, ndiyo maana haiwii ugumu sana kuonana na Daniele, huko Washington DC.
Simu iliita kidogo akapokea. Nikamsihi aje huku mikimwelekeza eneo na sababu. Nikahisi kabisa amejawa na hamu. Habari hiyo ilimpa msukumo uliomfanya upesi aniambie, "nakuja!" Kisha akakata simu.
Nilifanya hivyo si tu kwasababu ya utaratibu, la hasha, bali pia usalama wangu na kesi ile mezani. Endapo basi litakapotokea lolote lile, kuwapo na mtu atakayeweza kutoa taarifa nyuma yangu.
Basi nikaendesha baada ya hapo, kwa kama dakika kadhaa tu, nikawa nimefika kwenye nyumba elekezi. Ilikuwa ni nyumba ya ukubwa wa wastani, mbele yake kukiwa na bustani ndogo ya majani na maua.
Kabla sijashuka na kwenda, nikaikagua kwa macho ya wepesi. Nilipojiridhisha, nikatoka garini na kugonga mlango mara mbili. Kidogo ukafunguliwa na mtoto mdogo wa kike, makadirio ya kama miaka nane, tisa ama kumi hivi. Akanitazama kwa kunikagua.
"Hey, upo na yeyote ndani?" Nikamuuliza. Hakunijibu. Akaendelea kunitazama na kisha akaufungua mlango kwa upana. Nikazama ndani. Hapo nikiwa nimejikamilisha kwa kubebelea bunduki yangu ndogo ndani ya koti kwa dharura ya ulinzi.
Nikaketi sebuleni. Yule mtoto akaenda chumbani, pasipo kuniongelesha, na punde akarejea akiwa na mwanaume mwenye makamo ya umri wa miaka hamsini hivi kama sijakosea.
Mrefu na mwenye mwili mpana. Uso wake kama mstatili na kidevu chake ni pacha. Akanitazama kwanza kisha akajongea na kuketi.
"Anthony Marshall?"
"Ndio, ni mimi."
"Karibu. Naitwa O'neil," akanipatia mkono.
"Nashukuru kukufahamu bwana O'neil. Nimeitikia wito wako."
Kabla hajaendelea akarusha macho yake dirishani na kisha akaniuliza, "una uhakika umekuja peke yako?"
"Nadhani ..."
"Inabidi uwe na uhakika."
"Sijaangaza kama kuna mtu ananifuata. Hukuniambia hilo hapo awali."
"Yah! Nilifanya makosa. Hapa unatakiwa kuja mwenyewe, Marshall." Alisema hayo akiwa ananitazama kwa umakini sana kana kwamba mtu anayecheza mchezo wa 'chess'. "Sitaki mtu yeyote aanze kunifuatafuata. Nina mjukuu wa kumtazama. Na maisha yangu napenda yakiwa yangu binafsi."
Nikatulia na kumuuliza, "Ulitoa wapi mawasiliano yangu?"
"Kutoka kwa mkuu wako," akanijibu kwa kujiamini kisha akasema, "sikia Marshall, unaweza ukawa haunijui, ila mimi ni mtu ambaye nimetumikia taifa kwa miongo mingi. Inaweza ikawa haina haja sana ya kusema hivyo, ila lililo kuu ni kwamba mimi ni rafiki wa mtu huyo aliyepotea. Huyo ambaye unamtafuta kama nipo sahihi."
Nikanyamaza kimya nimsikize.
"Pengine naweza nikawa nahusika na upoteaji wa Raisi. Sasa nalijua na kujilaumu sana kwa hilo. Kama ningelichukua hatua mapema, huenda hivi sasa ningekuwa naye hapa badala yako. Najuta sana..."
Akanyamaza kidogo. Bado sikuongea. Nilimpa nafasi aendelee kujieleza pasipo kuhukumu kwa wepesi ama kuingilia alimradi alikuwa ameniita kunieleza jambo.
"Siku mbili kabla ya Raisi hajasafiri, nilionana naye. Hakuwa na muda wa kukaa na mimi sana kwani alikuwa ametingwa na kuna mahali anaenda. Ilikuwa ni upesi tu, na hata alipokuja hapa, hakuwa akiongozana na watu wengi kama mjuavyo, bali na watu wanne tu ambao walikuwa wamevalia suti nyeusi.
Alifika na ndani ya dakika akawa ameondoka! Mkononi mwangu aliniachia ujumbe huu," akaingiza mkono mfukoni na kutoa kipande kidogo cha karatasi ngumu nyeupe, akanikabidhi.
Nilipokisoma kilikuwa na ujumbe ulioandikwa kwa kalamu nyeusi ukisema, "NIPO SHIDANI." Nikamtazama yule mwanaume mwenyeji wangu, yeye akaendelea kunena.
"Sikupata muda wa kumuuliza ni shida gani hiyo ... kama unavyojua, si rahisi kuwasiliana na Raisi. Huwa ni mpaka yeye anitafute. Mara ya mwisho alipon'tafuta, ikawa ni siku yake ya kusafiri. Alimtuma mtu mmoja ambaye hakunieleza jina, na mtu huyo akaja kunifikishia ujumbe mwingine."
Akaweka kituo alafu akatoa tena karatasi toka kwenye mfuko wa pili. Mara hii huu ujumbe alikuwa ameuandika mwenyewe kwa mwandiko wake akiwa amenakili ujumbe aliopewa na mtu huyo.
"MUNICH, 2345," ujumbe ulisomeka hivyo. Nilipomuuliza maana yake, akaniambia hajui. Na hata huyo mtu aliyemletea, hakumwona tena tangu hapo.
"Unaweza ukamtambua mtu huyo ukimwona?"
Akanitikisia kichwa. "Hata picha zake ninazo."
"Naomba nizione."
Akageuza uso wake na kumtazama yule binti aliyenifungulia mlango. Akamtikisia kichwa kwa ishara na binti huyo akaenda chumbani. Kidogo, akarejea na picha mkononi, akanikabidhi.
Nikazitazama picha hizo. Nikagundua zilikuwa zimetolewa kwenye CCTV camera. Hazikuwa na ubora mkubwa ila angalau ziliweza kutambulika.
"Ni ajenti wa Secret service," akaniambia bwana yule. Nikazihifadhi picha hizo na kumuuliza, "sasa kwanini wahofia na kuishi hivi kama swala?"
"Nishakuambia mwanzoni," akanijibu. "Sitaki kuharibu maisha yangu. Hata wewe nimekutafuta kwasababu nahisi rafiki yangu atakuwa anahitaji msaada huko aliko!"
"Wapi?"
"Sijui! Na ndiyo maana nikafanya utaratibu wa kukutafuta. Huenda taarifa zangu zikakusaidia! ... na kwa usalama wangu, sitaonana na wewe tena baada ya hapa."
"Vipi kama nikihitaji taarifa nyingine toka kwako?"
"Sina taarifa ya zaidi na hiyo, Marshall. Kama nikiipata, basi nitakutafuta kama nilivyofanya leo. Kwani ulijua kama kuna mtu kama mimi?"
Basi nikamuaga na kwenda zangu, kichwani nikiwa nimepanga kumtafuta ajenti yule wa Secret Service na kisha, kama itawezekana, maana ya ujumbe ule wa MUNICH.
Nilipozama ndani ya gari na kuendesha kidogo, Daniele akanipigia. Nikapokea na kumwelekeza wapi tukutane. Ndani ya muda mfupi tukawa ndani ya gari langu. Nikamweleza yale niliyoyapata kwa mwanaume yule.
Maelezo hayo yakamfanya atamani sana kumwona yule bwana O'neil. Akanisihi huenda akawa anamfahamu mtu huyo na hivyo basi nimpeleke akahakikishe. Japo nilimwambia bwana huyo hatapendezwa na hilo, hakunisikia. Sikuwa na namna bali kumpeleka.
Tukachukua kama robo saa kufika. Nikagonga mlango na kuita. Kimya. Nikagonga tena na kuita kwanguvu, bado kimya! Kidogo mbeleni tukagundua kuwa bwana huyo hakuwapo tena hapo.
Tulivunja mlango na kusaka. Hakukuwa na kitu.

**
 
*NYUMA YAKO -- 10*

*Simulizi za series*



ILIPOISHIA

Tukachukua kama robo saa kufika. Nikagonga mlango na kuita. Kimya. Nikagonga tena na kuita kwanguvu, bado kimya! Kidogo mbeleni tukagundua kuwa bwana huyo hakuwapo tena hapo.

Tulivunja mlango na kusaka. Hakukuwa na kitu.

ENDELEA

“Atakuwa ametoroka,” akasema Daniele.

“hapana,” nikakataa. “sidhani kama huku ni kutoroka bali kujiepusha. Kama nilivyokuambia hapo awali, hakutaka haya mambo?”

“Kwani ni nini anachoficha?” Daniele akauliza akinishikia kiuno.

“Anaficha uhai na usalama wake,” nikamjibu na kisha nikatembea kuelekea gari. Naye Daniele akanifuata. Alipoingia tukajadili maswala kadhaa na kunifunza kuwa “Secret Service” hawakuwa wakihusika na upelelezi wa swala hili la upotevu wa Raisi.

“Kwa sababu za kiuwajibikaji, hawakuhusishwa ili kutoa mwanya wa mkono wa ziada kuwapeleleza hata wao endapo kutakuwa na mahusiano yoyote yale,” Daniele alisema akiwa anatazama mbele kana kwamba gari lipo kwenye mwendo.

Kisha akanitazama na kuniambia kiudadisi, “tunaweza kwenda Washington?” Sikujibu akaongezea, “inabidi tukatafute taarifa za huyo ajenti wa Secret Service ambaye akimletea ujumbe huyo mzee!”

Secret Service ni taasisi ya kiintelijensia inayohusika na ulinzi wa Raisi, Makamu wa Raisi na familia zao kwa ujumla. Wao ni chombo shurutishi cha kisheria kama ilivyo kwa FBI japo majukumu hutofautiana. Kwa ufupi taasisi hiyo huitwa USSS.

“Ni sawa,” nikamjibu Daniele. Niliona wazo lake linapendeza. Inawezekana kumpata ajenti huyo wa Secret Service ikawa ni hatua ya muhimu kwenye zoezi letu. Basi tukaenda huko kwa kutumia ndege. Tulipowasili, tukanyookea moja kwa moja kwenye makao makuu ya United States Secret Service (USSS). Huko tukakutana na Director, bwana Owen Allen, mwanaume mwembamba mwenye masikio mapana, macho madogo na lips nyembamba. Tukamweleza shida yetu.

Akiwa ameshikilia picha ya mtu tumtakaye, akasema, “huyu alikuwa ni miongoni mwa waliokuwa zamu ya kumlinda Raisi.” Kisha akaminya lips na kufinya macho. “ila siku ambayo Raisi alipotea, hakuwa zamu. Hakuambatana naye.”

“Sasa yupo wapi?” akauliza Daniele akimtazama Director kwa umakini.

“Amefariki,” Director akajibu kisha akatupatia picha tatu toka kwenye droo yake. Zilikuwa ni picha za jengo linaloungua kuelekea majivuni.

“Tunaamini alifia humo. Mwili wake ulipatikana ukiwa umejeruhiwa sana, ngumu kutambulika. Hatukuwa na namnna zaidi ya kuufanyia taratibu za kuuzika.”

“Na vipi kuhusu familia yake?” nikamuuliza. “hana mke wala watoto?”

“Hakuwa na mtoto. Alikuwa anaishi na mwanamke ambaye aliachana naye muda mrefu kidogo kabla ya ajali hiyo kutokea.”

“Una picha ya mwanamke huyo?”

“Hapana.”

“Kuna habari yoyote ambayo aliwahi kufikisha kuu ya usalama wa Raisi?”

“Hamna habari ya kushtua. Zilikuwa ni habari za kawaida kutokana tu na majukumu yake.”

“Nino chanzo cha ajali yake hiyo? Mmechunguza mkajua?”

“Kwa mujibu wa wataalamu, ni ajali ya gesi. Bwana huyo alikuwa akitumia gesi kupikia.”

“Kabla ya ajali hiyo, hakuna dalili au mabadiliko yoyote ambayo bwana huyo aliyaonyesha?”

Director akabinua mdomo na kutikisa kichwa. Akaongezea, “alikuwa ni mfanyakazi mzuri sana. Sidhani kama anastahili kutiliwa shaka.”

“Vipi kuhusu bwana ---” nikasita. Niliona si stara kuntambulisha bwana O’neil. Kwa namna hiyo niliona ni kheri nikanyamaza kama ambavyo yeye alivyokuwa anahitaji. Faragha ya maisha yake.

Basi tukaaga na kwenda zetu.



***



Saa tatu usiku, Mgahawa wa Lemaire, Virginia.



Mezani nilikuwa na Jack Pyong na mchumba wake, Violette. Tulifika hapo muda si mrefu na hata bado hatukuwa tumeagiza chochote toka kwa mhudumu. Wakati Jack anaangaza macho yake, nikamuuliza, “kwanini mgahawa huu, Jack?”

“mzuri!” akanijibu kifupi na kisha akaniuliza, “kwani kuna tatizo bwana Tony?”

“Hapana, ila ni kama vile hamna mgahawa mwingine ndani ya jiji hili.”

“Tony, hapa kakuita nani?”

“Wewe!”

“Na mimi ndiye ntalipia bills, shida yako nini?”

“Kwani nilikuomba uniite?”

“Sasa mbona ukaja?”

Kabla sijajibu, jibu ambalo natumai lingemkera, mhudumu akawa amefika hapo. Mdada mrembo mwenye tabasamu usoni.

“Naweza kuwasaidia?”

Tukamuagiza chakula, nami angalau kinyongo changu kifuani dhidi ya Jack kikawa kimekauka.

“Nadhani sasa hivi ungekuwa kwenye kitanda chako cha baridi umejikunyata. Si ndiyo Tony?” Jack akan’chokoza. Sikutaka kumjibu. Chakula kilikuwa kitamu kuliko maneno yake ya kijinga. Huenda hii ndo’ ikawa sababu yake kupendelea mgahawa huu, chakula cha moto na kitamu.

“Maisha ya upweke mabaya sana Jack,” akaendelea kuhororoja. “inabidi ufanye namna uwe na pa kupumzikia!” hapa Violette akamwonya juu ya mdomo wake lakini nikijua ni kazi bure maana Jack hatosikia.

Uzuri sikujali, na kulikuwa na sababu nyingine ya kunifanya nimpuuzie. Chakula. Niliujaza mdomo wangu chakula, nikatafuna nikitazama wateja wengine waliofika hapo.

Sikukaa muda mrefu, nikasikia sauti ya mtu akikokota viatu vyake. Kabla sijageuka, sauti hiyo ikakoma na mara kutazama, mtu akaniangukia, nikawahi kumdaka! Naye Jack Pyong akainama kama aliyetaka kumdaka. Kumtazama mtu huyo, nikamkumbuka! Alikuwa ni yule mwanamke niliyekutana naye kule Hong Kong!

Nikiwa katika mshangao huo, mara nikashuhudia Jack Pyong akipiga magoti na kufunua kidude kidogo cha rangi ya zambarau. Akiwa amemtazama Violette, akamwambia, “Utakubali kuwa mke wangu?”

Violette alikuwa amepigwa na duwaa. Hakutegemea kile kitu. Hata mimi sikutaraji kabisa. Na hapa ndipo nilipofahamu ya kuwa mwanamke yule ambaye tulikutana naye Hong Kong, ndiye aliyeleta pete ile. Kwahiyo, Jack alikuwa ametufanyia surprise watu wawili kwa mpigo!

Akakumbatiana na Violette na sisi, mimi na yule mwanamke mgeni, tukaishia kupiga makofi na kuwapongeza.

“Jack, uliwezaje kuliweka siri hili hata kwangu?”

Akatabasamu. “Nilipanga kukwambia, ila niliona nawe uwe ni miongoni mwa watakaoshangazwa. Vipi? Nadhani umependa wazo langu sio?”

Nikamtazama yule mwanamke kando yangu. Alikuwa ndiye yuleyule. Macho makubwa, nywele nyeusi. Hakika alikuwa anavutia. Na kwa namna alivyokuwa ananitazama alinifanya nihisi maungio yangu ya mwili hayafanyi kazi.

“Umekuja kufanya nini Marekani?” nikamuuliza. Akan’tazama na kutabasamu.

“Kutalii.”

“Kweli?”

“Ndio! Kwani haiwezekani? Au Marekani si sehemu ya kutalii kama Hong Kong?”

“Ni majuzi tu umetoka Hong Kong, itawezekanaje uwe huku kutalii?”

Akamtazama mhudumu aliyekuwa amefika hapo, akamwagiza kinywaji na kisha akan’tazama kuendeleza soga.

“Nimekuja kusoma, Tony.”

“Na unajua jina langu!”

Akacheka kidogo akifunika kinywa chake. “kwanini nisijue. Uliniambia mwenyewe? .. aah sasa naamini siku ile ilikuwa ni pombe ipo kichwani sio?”

“Siku gani?”

“Kule Hong Kong kwenye party!”

“Tulitambushana mimi na wewe?”

“Maskini Tony. Ilikuwa ni mara yako ya kwanza kunywa?”

“Yah! Kama si huyu fala, nisingegusa kilevi!” nikasema nikimtazama Jack Pyong.

“Kwahiyo haukumbuki hata kama ulinibusu na kunikumbatia?”

“Nilifanya hivyo?” Nikauliza nikikodoa. Akacheka tena akifumba mdomo wake kwa kiganja. “Kipi sasa wakumbuka Tony?”

“Nadhani ni sura yako tu. Hiko kitu hakikutoka kichwani.”

“Kweli, naona.” Alisema hivyo kisha akanitazama akiwa kimya. Kwa muda nikahangaika kutafuta kauli yangu mdomoni. Na kama vile mtu aliyefahamu ‘struggle’ ninayopitia akatabasamu kwambali kisha akaniuliza, “vipi Tony, kuna kitu unataka sema?”

Kabla sijasema jambo, mhudumu akampatia juisi na mrija. Ilikuwa ni juisi baridi ya tufaha. Hapo akanywa mafundo kadhaa kabla hatujaendelea na maongezi yetu machache. Alijitambulisha kwa jina la Kelly na kama alivyoniambia hapo awali, yeye alikuwapo hapo kwa ajili ya kusoma, chuo kikuu cha Harvard kitivo cha sheria.

Nilipotaka kufahamu juu ya wapi alipotokea, akanisihi nisiwe na haraka. Kila kitu kitajulikana taratibu.

“Maisha yangu yapo ‘simple’ and ‘straight’, Tony. Utajua kila kitu ndani ya muda mfupi. Lakini ukiwa ‘interested’.”

Baada ya hapo, Jack Pyong na Violette hawakukaa sana, wakatuaga wanaenda zao. Jack akanikonyeza akiwa anaenda zake.

“Sasa,” Kelly akachokoza mada. “Wewe hauondoki? Unalala hapa nini?”

Nikatabasamu kisha nikatazama saa yangu. Yalikuwa ni majira ya saa tano sasa usiku. Kweli muda ulikuwa umeenda. Nilimtazama Kelly na kumuuliza juu ya makazi yake, akaniambia kuwa amefikia kwenye apartment moja ndani ya Virginia.

“Kwanini Virginia na si Massachusetts huko karibu na chuo cha Harvard?”

Akatabasamu pasipo kuonyesha meno. Mashavu yake yalituna na macho yake kujifinya.

“Kwasababu ndo’ sehemu ambapo nina mwenyeji!”

“Mwenyeji? Hapa Virginia?”

“Ndio.”

“Wapi huko?”

Kabla hajajibu akaingiza mrija mdomoni mwake na kufyonza juisi.



**
 
*NYUMA YAKO -- 11*
.
.
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
.
.
Akatabasamu pasipo kuonyesha meno. Mashavu yake yalituna na macho yake kujifinya.
“Kwasababu ndo’ sehemu ambapo nina mwenyeji!”
“Mwenyeji? Hapa Virginia?”
“Ndio.”
“Wapi huko?”
Kabla hajajibu akaingiza mrija mdomoni mwake na kufyonza juisi.
.
.
ENDELEA
.
.
Alifyonza akiwa ananitazama, na alipohakikisha hakuna alichobakiza ndani ya glasi, akajisafisha lips zake kwa ulimi kisha akasema, “Nadhani unamjua mtu huyo. Hivyo ni bora kukwambia ni nani kuliko mahali.”
“Ni nani huyo?”
“Jack. Jack Pyong.”
“Serious?”
“Yah! Yeye ndo’ mwenyeji wangu hapa.”
“Kelly, umekuwa ukijuana na Jack kwa muda gani?”
“Kwa muda kidogo …” akatazama saa yake ya mkononi. “Tony, nimekawia. Sipendi kutembea nyakati za usiku. Naomba niende sasa.”
“Usijali, nitakusogeza na gari yangu.”
Hatukukaa tena hapo, tukanyanyuka na kuendea usafiri nilokuja nao, tukajipaki na tukaanza safari ya kumpeleka kwake, huko ambapo amefikia. Tukiwa safarini nikaendeleaa kumdadisi juu yake na Jack Pyong.
“Nilijuana naye kwa muda kidogo. Ni mtu mwenye maneno mengi na mcheshi pia hivyo haikuchukua muda kuunda naye urafiki!”
Kwahiyo basi kwa mujibu wa Kelly, walikutana na Jack Pyong huko kwenye mtandao wa Facebook na kuwa marafiki. Na kwakuwa walikuwa wote ndani ya Hong Kong basi ikawa rahisi kukutana na kutambulishana. Hapa sasa nikafahamu kuwa Jack alikuwa na mengi ya kunifahamisha kuhusu Kelly. Sikutaka kumchosha mwanamke huyu kwa maswali yangu yasiyokuwa na mwisho.
Basi baada ya habari hiyo, sasa ikawa ni kama zamu ya Kelly kuniuliza mimi. Aliniuliza maswali lukuki juu ya kile kinachoendelea ndani ya Marekani, haswa kupotea kwa Raisi. Kabla sijaendelea, acha nikuweke wazi kuwa ingawa Raisi alikuwa kweli amepotea, bado serikali ya Marekani haikuwa imekiri hilo wazi.
Hii ilikuwa ni aibu kubwa kwa taifa kama la Marekani linalosifika kwa intelijensia ya hali ya juu. Ilikuwa ni dhihaka na matusi makubwa kwa taasisi zote za kiintelijensia, ni kivipi Raisi apotee? Hata mtu ukimweleza kuwa Raisi wa Marekani amepotea ni wazi atakuna kichwa chake akijiuliza inawezekanaje?
Hivyo basi, taarifa zisizo rasmi zilikuwa zikisimamia kuwa Raisi anaumwa na yupo chini ya uangalizi. Kitu ambacho kilikuwa kinyume kabisa na ukweli. Ingawa tulifanya hivyo, lakini bado minong’ono ikazagaa na watu wakiwa wananena hata huko mtaani kuwa huenda wanadanganywa. Mbona huyo Raisi anayesemekana kuumwa, haijulikani yupo hospitali gani na nini haswa kinachomsumbua?
Hivyo kwa namna moja ama nyingine sikushtushwa sana na maswali ya Kelly. Nilijitahidi kutoonyesha hisia zozote usoni, nikazidi kumpumbaza kuwa Raisi anaumwa na yupo chini ya uangalizi na uchunguzi, na si zaidi ya hapo. Niliendelea kusimamia kile ambacho tulitaka jamii iamini wakati tukihaha kuutafuta ukweli.
“Ni kweli, Tony?”
“Yah! Ni kweli. Kwanini unnauliza hivyo? Vipi, kuna lolote ulilosikia?”
“Vipi kama Raisi atakuwa amepotea?” akauliza akiwa anatazama kana kwamba mtu anayetoa masimulizi. “Hivi Marekani itafanyaje? Patakalika kweli?”
Nikatabasamu pasipo kumjibu. Punde akanisihi nisimamishe gari. “Nimeshafika!” akanishukuru na kisha akafungua mlango wa gari akiniaga. Nikamtazama aelekeapo. Alipotelea njiani nisijue ameenda wapi. Sikujali sana, nikatimka zangu.

**

‘Kuna kitu umepata?’
‘Hapana. Marshall, nadhani kuna haja ya kwenda Munich!’
Usiku huu wa saa sita nilikuwa nachat na ajenti Daniele. Nikiwa nimejilaza kitandani, yeye pamoja na timu yake walikuwa wakihaha kukusanya kila taarifa wanayoweza kupata juu ya swala hili la upotevu wa Raisi kutokana na data tulizopata toka kwa bwana O’Neil.
Hawakuwa wakilala wala kupumzika, kazi ilikuwa pevui haswa tofauti na kwa upande wangu.
‘Kuna haja ya kwenda Munich. Nadhani tunaweza kupata kitu huko Marshall!’ Daniele aliendelea kupendekeza. Na kwakweli niliona kuna haja hiyo japo bado kile kitendawili cha Munich 2345 hakikuwa kimeteguliwa.
Kidogo nikapata mawazo hapa. Ile namba 2345 ilikuwa inamaanisha nini haswa? Ni mwaka? Masaa? Ama anwani ya nyumba? Njia pekee ya kupata majibu hayo ilikuwa ni kwenda Munich, Ujerumani.
Na basi Daniele akaniambia kuwa, wakati yeye akiwa huku nchini, atahakikisha anaonana na mke wa Raisi na pia Makamu wa Raisi kwa taarifa na mahojiano zaidi. Ilikuwa ni kama vile tumegawiana majukumu. Kuchati kukaishia hapo.
Kabla sijalala nikamtafuta Jack Pyong kwa njia ya ujumbe nikimtaka afanye anachokijua kuhusu MUNICH 2345. Nikakaa kusubiri majibu, kama lisaa hivi, kimya. Nadhani alikuwa amelala au yupo busy na mchumba wake. Mwishowe nami nikalala.
Asubuhi kuamka, majira ya saa kumi na moja, nikakuta ujumbe kwenye simu yangu toka Jack Pyong.
‘Ndo nini hiyo?’ sikumjibu. Nikaona kuna haja ya kuonana naye uso kwa uso nipate kumweleza, pia kumjuza juu ya safari yangu kwenda Munich. Basi nikajiandaa na katika majira ya saa mbili asubuhi nikakutana na Jack faragha. Nikamweleza kile ninachotaka kukijua, akaniahidi atalifanyia kazi. Kwa mara ya kwanza alikuwa ameongea la maana.
Nilipomwambia kuhusu safari ya Munich, nikimshawishi twende wote, hapa akasita. “Nitamwachaje Violette? Unajua ni jana tu nimetoka kumvesha pete!”
“Jack, kumbuka hii kazi ni kubwa. Tunapigania taifa. Tafadhali fikiria mara mbili.” Kisha nikaondoka nikaenda kukutana na Mkuu wa kazi na kumweleza juu ya mipango yangu, kwenda huko Munich. Jioni ya siku hiyo akanihakikishia kwenda huko kila kitu kikiwa tayari.
Ilipofika majira ya saa moja jioni, nikawa nipo ndani ya ndege, United Airlines, nikielekea Munich, Ujerumani. Safari itakayonigharimu takribani masaa kama kumi na dakika thelathini. Nikafika Franz Josef Strauss Airport majira ya asubuhi ya saa mbili, nikajipatia chumba ndani ya MOXY Munich hotel nilipopumzikia kabla ya kuanza harakati zangu.
Nilipitiwa na usingizi nikiwa nangojea ujumbe toka kwa Jack Pyong. Nilikuja kuamka baada ya kusikia hodi mlangoni mwangu ambapo baada ya kusonya, nikajongea mlango na kuufungua. Alikuwa ni mhudumu wa kike akinijia kunieleza juu ya malazi na chakula kisha akaenda zake.
Baada ya hapo nikaoga na kutoka kwenda kutalii mji wa Munich. Kulikuwa na haja ya mimi kulijua jiji hilo kwa namna fulani kwakuwa nilitarajia kulifanyia kazi. Nikatembea mitaa kadhaa, hata kula nikala huko , chakula cha mchana na jioni. Kwenye majira ya saa mbili usiku, nikapanda usafiri wa uma nirudi hotelini.
Sikuona haja ya kupanda taksi kwasababu nilikuwa nataka kujua zaidi kuhusu jiji hilo.
Nikiwa ndani ya usafiri, nikaketi nyuma kabisa nikiwa nimepakana na mwanaume mmoja atafunaye bubblegum. Alivalia koti jeusi la ngozi na uso wake ulikuwa serious akitazama mbele. Kitu ambacho kingenifanya nimkumbuke mwanaume huyo ni namna ambavyo mustachi wake ulikuwa mpana na mrefu, na pengine macho yake ya kusinzia.
Mbali na hivyo sikumjali sana. Nilipowasili nimapotakiwa kushuka, nikanyanyuka, na yeye huku nyuma yangu akasimama, sikujali sana, nikashuka na punde naye akafanya hivyo.
Hapa niliposhukia palikuwa na umbali kidogo na hotelini. Tuseme ni kama mwendo wa dakila kumi. Na nilishukia hapa, kwa makusudi ya kuendeleea kuusoma mji kwani niliona ni vema pia endapo nikafahamu eneo linalozunguka mahali nilipofikia.
Nikatembea nikiwa nimedumbukiza mikono yangu mfukoni. Hatua zangu zikiwa pana ila za taratibu nikirusha macho kushoto na kulia.
Nikiwa katika zoezi langu hilo, kama baada ya dakika mbili, nikagundua kuna watu wawili wananifuata kwa nyuma. Wote walikuwa wanaume na sikuwaona vema kutokana ma uelekeo wa mwanga. Ila kidogo baada ya kusonga, nikamtambua mmoja wao kuwa ndiye yule niliyekaa naye kwenye usafiri wa basi. Mwanaume mwenye mustachi na koti la ngozi.
Sikujua wanataka nini kwangu, ila ni wazi niliamini dhamira yao si safi, basi nikaongeza ukubwa wa hatua zangu na mikono nikaitoa mfukoni iwe huru kwa kufanya lolote lile.
Nilipofanya hivyo nao wakajiongeza. Nikahisi hatua zao zimeongezeka na sasa wanakaribia kukimbia. Hapa nikawaza upesi, je swala langu la kukimbilia hotelini litakuwa na maana? Vipi kama hawajui ninapokaa, si n’takuwa nimewapeleka? Lakini pia nikawaza, je watakuwa ni watu wenye taarifa za ujio wangu wa kigeni katika jiji hili, nchi hii?
Watakuwa ni watu wanaohusika na kupotea kwa Raisi?
Maswali haya yakanifanya nisione stara kuwakimbia. Pengine naweza kupata kitu kitakachonisaidia na upelelezi wangu. Basi nikafanya hiyana na kujifichia ndani ya kichochoro fulani. Hapo punde nikawaona wakija, wakaduwaa kutafuta na kutazama.
Mimi nilikuwa nimejibana nyuma ya ndoo kubwa ya malighafi ya chuma nyepesi, ndoo ya kuhifadhia uchafu. Kwakuwa kichochoro hiki hakikuwa na taa, haikuwa rahisi kwao kuniona. Lakini … walianza kuhisi nitakuwa nimejifichia hapo. Nikawaona wakitazamana na mmoja akamtikisia kichwa mwenzake kisha taratibu wakaanza kusonga wakifuata ndoo niliyokuwa nyuma yake!
Mikono yao ya kulia niliiona ikiwa imezama kotini. Bila shaka kushikilia bunduki.
Hapa ikanilazimu nifanye maamuzi ya upesi kuokoa roho yangu.

**
 
*NYUMA YAKO – 12*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Mikono yao ya kulia niliiona ikiwa imezama kotini. Bila shaka kushikilia bunduki.
Hapa ikanilazimu nifanye maamuzi ya upesi kuokoa roho yangu.
ENDELEA
Ni upesi nikanyanyuka nikiwa nimebebelea ile ndoo ya taka, nikawatupia! Wakiwa wamedaka na kudondoka nayo chini, nikawawahi nisiwape muda wa kujiandaa. Mmoja nikampoka bunduki na kisha nikamdaka na kumwekea tundu la bunduki kichwani nikimwamuru mwingine aweke silaha yake chini.
“Fanya upesi kabla sijammwaga mwenzio ubongo!”
Huyu niliyekuwa nimemdaka alikuwa ni yule mwanaume niliyekuwa naye kwenye basi. Mwenzake, mwanaume mrefu mwenye mwili mpana, akan’tazama kwa mashaka kama mtu ajiulizaye nini cha kufanya.
“Nimesema weka silaha chini!” Nikamwamuru. “sitasema tena sasa hivi, utaokota maiti ya mwenzako!”
Basi akainama na kuweka silaha yake chini akiwa anan’tazama kwa kukodoa.
“Ninyi ni wakina nani?” nikauliza. “Kwanini mnanifuata?”
Kimya. Hamna aliyenijibu. Nikarudia tena kuwauliza mara hii nikikaza sauti zaidi, lakini haikuleta tofauti! Hakuna aliyenijibu.
“Sina muda wa kupoteza na ninyi! Kama hamtanipa majibu ya maswali yangu basi nitawamaliza maana haitakuwa hasara kwangu.”
Nilipomaliza tu hiyo kauli, bwana yule niliyekuwa nimemkaba, akawahi kuudaka mkono wangu wenye silaha, akajigeuza upesi akitaka kufanya shambulio kwa ngumi ila kwa upesi nikamkwepa, na nilipoona yule mwenzake ametwaa bunduki aliyoiweka chini, nikafanya jitihada za haraka za kumdaka mwanaume yule mwenye mustachi na kisha nikajikinga naye.
Hapo mwenzake akapata kigugumizi cha kufyatua bunduki, nikamtupia risasi mbili na kumlaza chini hajiwezi. Kisha mwanaume yule niliyemkaba nikamziraisha na kumweka begani. Ikanipasa niondoke mapema eneo hilo kwani milio ya bunduki ingewafanya vyombo vya usalama kujongea hapo muda si mrefu.

**

Saa moja usiku …

Baada ya kutoka kuoga, nilijifuta maji na kisha kumjongea mateka wangu ambaye nilikuwa nimemfungia kitini. Alikuwa bado hajarudi fahamuni hivyo nikamwagia maji na kumtaka ajibu maswali yangu kama salama ya roho yake.
Lakini mwanaume huyo hakuogopa kabisa. Akiwa anan’tazama usoni, akaniambia hatajibu swali langu hata moja. Na nikitaka nimuue pasipo kujichosha. Hapo ikabidi nitafute namna ya kumfanya aongee.
Nikamnyanyua na kumpeleka bafuni. Nikamvika mfuko wa kitambaa kichwa kizima na kuanza kumwagia maji usoni mwake kumnyima pumzi. Akahangaika sana. Lakini kila nilipouvua mfuko huo na kumuuliza, bado hakuwa tayari!
Nikamtesa sana mpaka mwishowe akawa amepoteza nguvu kabisa. Macho yalilegea na mdomo akaacha wazi akitapika maji, ila bado hakuwa amenipa majibu ya maswali yangu. Bado alikuwa na roho ngumu!
Basi nikaona nimpe mapumziko alafu tutaendelea tena muda utakaporuhusu, kwa muda huo nikawasiliana na Daniele na kumwambia yaliyotukia. Naye akaniambia hatua aliyofikia pamoja na timu yake. Siku hiyo alikuwa ameonana na Makamu wa Raisi na pia mke wa Raisi. Wote alifanikiwa kuwafanyia mahojiano lakini hakuna kikubwa alichoking’amua, zaidi mke wa Raisi alikuwa anaumwa na anatazamia kwenda kwao, Australia, kwa ajili ya mapumziko.
Na zaidi ya yote, alipata taarifa kuwa O’Neil, yule bwana aliyetupatia kiasi kidogo cha taarifa, amekutwa akiwa amekufa huko Massachusetts! Mwili wake umekutwa ukiwa mtupu na ishara ya kupitia mateso.
Habari hiyo ikanishtua kwa namna yake. Nani atakuwa amemuua O’Neil? Na je kifo chake kitakuwa na mahusiano na taarifa zile alizotupatia?
Nikamtaka Daniele afuatilie kwa undani juu ya kifo hicho kwani kitakuwa nacho kina mlango wa kutupeleka tunapopahitaji. Basi hata nilipokata simu, nikaendelea kuwaza juu ya kifo cha O’neil. Si bure mzee yule hakuwa anataka kujihusisha na haya mambo!
Lakini kifo hiko kikanipa maswali sana juu ya wauaji. Je pia watakuwa wanajua kuhusu mimi na taarifa zile za bwana O’neil?
Mara mlango ukagongwa na kuniamsha toka kwenye lindi la mawazo. Nikanyanyuka toka kitandani na kwenda mlangoni kumkuta mhudumu. Mwanamke mrembo mwenye mashavu mekundu. Aliniambia kuhusu chakula, kipo tayari kwenye hall, lakini kabla hajaenda, bwana yule niliyekuwa nimemfungia bafuni, akaanza kupiga kelele akigugumia!
Mhudumu akan’tazama kwa hofu, nami kumpoza nikamwambia huyo ni mwenzangu yu hoi anaumwa. Lakini ni wazi maneno hayo hayakumkosha mhudumu, akaenda zake akiwa na sura ya mashaka, na hata mwendo wake ukiwa wa kasi!
Muda kidogo, kama dakika mbili, mlango ukagongwa kwanguvu. Kabla sijauendea nikauliza, “Nani?” sauti ya kiume ikanijibu, “Staff!”
Taratibu nikasonga na kuchungulia nje kwa kupitia tundu mlangoni. Huko nikaona majibaba mawili wakiwa wamevalia sare za hoteli. Walikuwa ni walinzi. Hapa nikapata kujua kuwa mhudumu yule alienda kutoa taarifa juu ya sauti ile alosikia chumbani mwangu.
Nikaufungua mlango, na pasipo kuonyesha lolote usoni mwangu, nikawauliza, “naweza kuwasaidia?”
“Tumekuja kufanya ukaguzi chumbani mwako!” mmoja akajibu akinitazama machoni.
“Mtakaguaje chumba cha mteja?” nikawauliza nikiwakunjia ndita.
“Ndugu, ni jukumu letu kuhakikisha kuna usalama ndani ya hoteli. Kama unaona ni shida, basi tuwaite polisi watekeleze hilo!” akasema yule bwana aliyejielezea hapo awali. Kidogo nikafikiria na kuona ni kheri nikawaruhusu watu hao waingie ndani na kufanya ukaguzi kuliko ujio wa polisi hapo.
Basi, kama watu wanaofahamu kinachoendelea, wakanyookea bafuni, huko wakamkuta bwana yule niliyemfungia. Wakamfungua kamba toka kwenye kiti na kumweka huru. Kisha mimi wakaniweka chini ya ulinzi wakinituhumu kama mtekaji!
“Upo sawa?” Mmoja akamuuliza yule bwana waliyemwacha huru. Naye kwa uchovu akawajibu, “nipo sawa, nashukuru.”
Wakamuuliza kwanini mimi nilimfungia kule bafuni, naye akatoa maelezo ya wongo kuwa nilitaka kumuua kisa nikitaka pesa toka kwake, basi walinzi wakapiga simu polisi kutoa taarifa juu yangu.
“Huyo anawaongopea,” nikapaza sauti. “ni yeye ndiye anataka kuniua. Yeye pamoja na mwenziwe!”
Lakini nani aniamini? Mazingira yalikuwa yananisaliti na kuninyooshea kidole kuwa mimi ni muuaji. Basi tukiwa hapo, ndani ya muda mfupi tu, yule jamaa, jambazi, kwa upesi akawadhibiti walinzi wa hoteli na kuwaweka chini ya ulinzi. Alitumia bunduki niliyompokonya. Bunduki hiyo nilikuwa nimeiweka kwenye droo ya kitanda.
Alipofanikisha hilo, akaninyooshea tundu la risasi na kuniamuru niseme kile kilichonileta Ujerumani. Tena niseme upesi kabla hajanimaliza aende zake.
Nikamwambia huku nikinyoosha mkono juu, “mimi ni mtalii tu! Sitambui kwanini wanifuatilia namna hii!”
“Usinifanye mimi ni mjinga! Natambua kinachoendelea na kama uki—” hakumalizia, nikawa nimemtupia stuli iliyokuwa imesimama kando yangu. Stuli hiyo kwakuwa niliitupa kwanguvu, ikafyeka miguu yake na kumwangusha chini! Kabla hajaamka, walinzi wakamuwahi kumpokonya silaha, ila ajabu akafurukuta kwanguvu na kumtupa mlinzi mmoja kando kwa kumkandika teke zito. Na huyo mwingine akamchapa kiwiko na kisha ngumi nzito, akalala kando amezirai.
Kabla hajateka tena bunduki, nikajitupa na kuunyoosha mguu wangu kuisogezea mbali kwa teke, alafu nikaunyanyua kutaka kumkandika kifuani. Akakwepa. Akajirushia mgongo kunifuata. Akatupa ngumi yake, nikaiyeya, ya pili nikaidaka na kuiviringita! Akajizungusha na kutupa kiwiko, nacho nikakisogezea pembeni na alafu kumdaka shingo yake na kumkaba kwanguvu zangu zote.
Akatapatapa akituma viwiko vyake. Havikunipata. Ila kimoja kilitifua mbavu yangu na kunipa maumivu makali. Nikavumilia na kuendelea kumkaba. Akatupa tena kingine, hakikunipata, cha tatu kikanitifua tena. Hapo nikashindwa kuvumilia!
Bwana huyu akajichomoa toka kwenye mikono yangu na kisha akaniadhibu kwa ngumi ya shavu la kulia. Mdomo ukalowana damu. Lakini sikumruhusu achukue bunduki. Alipotaka kufanya hivyo, nikamuwahi kumvuta. Akatupa teke, nalo nikamdaka na kumvuta kwanguvu, alafu nikamrukia mgongoni na kumkaba tena. Mara hii mikono yake niliikandamizia na magoti yangu, hakuweza kufurukuta!
Akapoteza kabisa nguvu. Macho yakaanza kuelekea juu. Nikalegeza mikono yangu na kumuuliza ametumwa na nani. Kwa mbali nikamsikia akisema, “Rodolfo!” kisha akazirai!

***
 
*NYUMA YAKO – 13*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Akapoteza kabisa nguvu. Macho yakaanza kuelekea juu. Nikalegeza mikono yangu na kumuuliza ametumwa na nani. Kwa mbali nikamsikia akisema, “Rodolfo!” kisha akazirai!
ENDELEA
Basi nami sikukaa tena hapo kwakuwa polisi walikuwa njiani na mimi sikutaka kusumbuana nao. Nikawaaga wale walinzi, na kwasababu walishaona ya kuwa sina tatizo, wakaniacha nikaenda zangu. Kutoka tu ndani ya hoteli, nao polisi wakafika hapo wakitumia gari dogo. Upesi wakazama ndani.
Nikasimama hapo kutazama, punde nikaona wakitoka wakiwa wamemshikilia yula jamaa. Wakamzamisha ndani ya gari lao na kutimka. Nikashusha pumzi ndefu na kuendelea na safari yangu.
Nikajongea kwa umbali mdogo kabla sijasimamisha taksi inipeleke hoteli nyingine. Huko nikachukua chumba namba 289, na kujipumzikia kitandani nikitafakari yale yaliyotoka kujiri.
Rodolfo ni nani? Nilijiuliza hilo swali. Atakuwa ni mtu wa aina gani huyo na kwanini ametuma watu kunifuata? Hapa nikajikuta nikiamini kuwa Rodolfo atakuwa anahusika na MUNICH 2345. Hata hivyo anaweza akawa anahusika na kupotea kwa Raisi!
Nikajigeuzia upande wa kushoto nikiendelea kutafakari namna ambavyo matukio haya yalivyosukwa. Huku O’neil anauwawa kwa kuteswa huko Marekani, nami navamiwa na kutishiwa uhai! Hakika hapa palikuwa pana fumbo.
Mara simu ikaita, nikainyakua na kuiweka sikioni. Alikuwa ni Jack Pyong!
“Hey Jack, vipi?”
“Hali si nzuri, Tony!” sauti ya Jack ikaongea kwa kutetemea. Tangu nimjue Jack sikuwahi kumsikia akiongea katika namna ile. Nilihisi sauti yake imetepeta woga ndani yake.
“Kuna nini, Jack?” nikauliza nikiwa najitengeneza kitandani. Niliketi kitako na kukunja sura kulazimisha umakini.
“Sijui nini kinaendelea, Tony. Leo nimenusurika kupigwa risasi na mtu nisiyemfahamu!”
“Serious?”
“Ndio. Hapa nahofia hata kwenda nje!”
“Umetoa taarifa kazini?”
“Hapana, sijatoa. Nahofia, Tony. Nahofia kumhusu Violette!”
“Sikia, basi fanya hivi, toa taarifa makao, alafu utanambia nini watafanya!”
Simu ikakata. Hapana, nikaipiga upesi na kuibandika sikioni.
“Tony, umenielewa?”
Akacheka. “We fala umeamini nilichokuambia?” Nikanyamaza kwa hasira. Nikang’ata meno yangu nikinguruma. “Jack, unajua mambo mengine usiyaletee masikhara!”
“Wewe ukiyafanya sio masikhara sio?” akajibu kwa kebehi. Nikasonya na kumuuliza,
“Sema umenipigia nini?”
“Nataka nikupe marejesho ya kazi yako! Ile ya MUNICH 2345.”
“Enhe ni nini umepata?”
“Vitu vingi tu. Nashindwa kujua nishike lipi niache lipi!”
“We niambie vyote, nami nitajua cha kufanya…”
Basi akapendekeza kunambia kimtiririko maana moja laweza pelekea jingine, nami nikatumia akili yangu kukitunza alichoniambia na hata nikapanga kesho yake asubuhi na mapema, kwenda kuitafuta nyumba nambari 2345 ndani ya jiji hili la Munich.
Mengine utayafahamu baadae… huna haja ya kupapatika, mambo bado ni mengi mbeleni.

**

Saa tano asubuhi …

Nilifunga mlango wa taksi baada ya kukamilisha malipo yangu. Nikatengenezea koti langu mwilini na kutazama mtaa ambao nilikuwa nimeshushwa. Hapo kulikuwa na nyumba kadhaa zikiwa zimesimama kwa kufuatisha barabara hii ya lami.
Na kama nilivyokuwa nimemuelekeza dereva taksi, alikuwa amenishusha mbele ya nyumba ninayotakiwa kushukia. Nyumba yenye anwani 2345!
Nikaitazama nyumba hii kabla ya kuijongea. Ilikuwa ni nyumba tulivu isiyo na dalili ya makazi. Madirisha yake yalikuwa yamejaladiwa na vioo yakiwa hayana mapazia.
Nikanyanyua miguu mpaka mlangoni, nikagonga mlango na kutulia nikiskizia. Hamna kitu. Nikagonga tena na tena, hamna kitu! Sasa nikaanzaa kuamini kuwa humo ndani hamna watu. Nikachungulia dirishani kwa ufupi alafu nikaujaribisha kuusukuma mlango. Haukufunguka.
Nikausukuma kwa nguvu kidogo, ukatenguka na kufunguka! Taratibu nikausogeza na kuzama ndani. Nikarusha macho yangu huku na kule kwa tahadhari huku mkono wangu wa kuume ukiwa karibu na nyonga ya mguu, kwa tahadhari ya kuchoropoa silaha.
Ndani ya nyumba hii kulikuwa na samani za zamani, buibui na vumbi. Ni nyumba iliyotelekezwa, tena si karibuni. Niliingia mpaka chumbani na hata jikoni nisikute alama yoyote ya uhai au uwepo wa binadamu. Nikiwa nimerejea hapo sebuleni, kwa chini mbali ukutani, nikaona vipandevipande vya vyupa.
Nikavisogelea na kuokota kipande mojawapo na kukitazama. Kilikuwa ni kipande cha picha. Nikajaribu kuonganisha vipande kadhaa vya vyupa hivyo, nikapata kuona picha ya mwanamke mwenye nywele nyeusi na macho yalopoa.
Lakini sura yake sikuweza kuiona vema kama nilivyotaka. Vipande vingine vya chupa vilikuwa vimesagika vibaya hivyo kupoteza kabisa maana zake. Na nilipotazama vema, nikabaini kuwa katika picha hiyo, huyo mwanamke alikuwa ameketi na mtoto.
Sasa ni kheri ya picha ya huyo mwanamke, ya mtoto ndiyo ilikuwa haionekani kabisa, nyang’anyang’a! Nisingeweza kutambua lolote lile isipokuwa rangi ya nywele zake. Rangi ya dhahabu.
Basi nikapiga picha kadhaa kwa kutumia simu yangu alafu nikazama ndani kule chumbani kwa nia sasa ya kukagua makabati nione ni nini nitapata. Nikaona nguo za mtoto waa kiume, na za mwanamke. Lakini zaidi nikaona kifaa cha kusaidia kupumua kwa watu wanaosumbuliwa na tatizo la pumu!
Hapa sasa nikapata kukumbuka kuhusu kifaa hicho. Kifaa alichonionyeshea Daniele kuwa wamekiokota uwanja wa ndege wakidhania ni cha Raisi. Ina maana ile ilikuwa ni ishara au?
Nikakiweka kifaa hicho kibindoni, lakini kabla sijaendelea na kazi ya upekuzi, nikasikia gari ikisimama kwa ‘kuchuna’ breki kali huko nje. Haraka nikajongea dirisha na kutazama.
Nikaona wanaume watatu wakiwa wamevalia nguo nyeusi wakishuka toka kwenye Volkswagen modeli ya zamani. Gari hiyo kwa ubavuni ilikuwa na chapa ya samaki na maneno ya kijerumani yakimaanisha kampuni ya uvuvi.
Wanaume hao walikuwa na sura ya kazi, na nikadhani huenda wakaja mule nilipokuwapo, ila lah! Wakanyookea nyumba ya pili na kuzama humo. Sikujua walienda kufanya nini, na sikujua kwanini niliwatilia shaka. Nilihisi tu si watu wema.
Basi nikapiga moyo wangu konde na kuendelea kusaka. Sikupata cha maana, baada ya kama dakika kumi, nikaona nitoke humo ndani niende zangu nikiwa nimelenga kutafuta serikali ndogo ya eneo hilo ili nipate walau taarifa juu ya wakazi wa hapa.
Nilipotoka nikatazama ile nyumba jirani ambayo iliwameza wale watu niliokuwa nawatilia mashaka. Sikuona jambo. Muda si mrefu,, kwa mwendo wangu wa haraka, nikawa nimefika kituoni ambapo nilipanda gari nikilenga kuelekea kwenye ofisi ndogo za wilaya. Ikanichukua kama dakika kumi tu kufika hapo. Nikazama ndani na kueleza shida yangu.
Nilijitambulisha kama James Tuck toka Marekani na nimefika hapo kumuulizia ndugu yangu ambaye anakaa Munich kwani nimefika kwake sikumkuta.
Mhudumu akaniuliza kuhusu anwani yake, nikamtajia. Muda si mrefu akanielekeza mahali pa kwenda, yaani kama balozi wa mtaa, huko nitapata majibu kamili na ya uhakika.
Kwahiyo nikajiresha tena kituoni na ndani ya muda mfupi nikawa nimefika nilipoelekezwa. Nikamkuta mzee mmoja mnene mfupi akiwa anakunywa bia aliyoitunza kwenye glasi kubwa. Nikamsalimu na kumweleza shida yangu. Akaniambia ya kuwa mwanamke huyo aliyekuwa anakaa kwenye yale makazi alipotea na hakuna mtu anayejua wapi alipo hata sasa.
“Ni kama miezi mitano sasa. Taarifa pekee tuliyonayo ni kwamba jirani yake aliona gari aina ya van ikimpakia na kwenda naye, yeye pamoja na mtoto. Hakumuaga mtu yeyote, hivyo hamna anayefahamu.”
“Vipi kuhusu namba ya usajili ya van hiyo?” nikauliza.
“Hamna mtu aliyeijali,” akanijibu huyo mzee. “Nani atasumbuka na kunakili namba za magari na ingali haikuonekana kama ni tukio la shuruti?”
“Na vipi kuhusu huyo jirani? Yupo?”
Mzee akatikisa kichwa na kunambia, “naye hayupo!”
“Amehama?”
“Hakutoa taarifa kama anahama. Sijui alipoelekea.”
Nilipompeleleza zaidi nikagundua kuwa huyo jirani anayemwongelea alikuwa anakaa kwenye ile nyumba ambayo niliwaona watu wakiingia humo. Nikamuuliza, “Ina maana hapo pana wakazi wapya?”
“Ndio, kuna wanaume wa kiwanda cha mbao hapo,” akanijibu kishaa akagida fundo la bia. Lakini …
Wale wanaume mbona hawakuonekana kama wafanyakazi wa kiwanda cha mbao? Nilijikuta nikitia shaka. Mbona gari yao ilikuwa na chapa ya samaki kama ni hivyo?

**
 
*NYUMA YAKO – 14*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
“Ndio, kuna wanaume wa kiwanda cha mbao hapo,” akanijibu kishaa akagida fundo la bia. Lakini …
Wale wanaume mbona hawakuonekana kama wafanyakazi wa kiwanda cha mbao? Nilijikuta nikitia shaka. Mbona gari yao ilikuwa na chapa ya samaki kama ni hivyo?
ENDELEA
Maswali hayo yalibaki kichwani hata wakati natoka kwenye jengo hilo. Nilikuwa nawaza na nikaona endapo nikiendeleza mawazo hayo basi naweza jikuta nagongwa na gari barabarani.
Nikatembea zangu mpaka kituoni na kukwea basi. Kama nipendavyo nikaenda kukaa nyuma, kichwa nikakiegeshea kitini na huku macho yangu yakiwa yanatazama mji. Namna vitu viendavyo nyuma wakati sisi tukienda mbele.
Wakati huo pia nikiwa nawaza kumwambia Jack Pyong juu ya yale niliyoyakuta kule kwenye nyumba yenye anwani elekezi ili anambie kama kuna kingine cha kufanya baada ya hapo kama vile alivyoniahidi hapo awali.
Nikiwa katika ombwe hilo, basi likasimama na kunifanya nizingatie. Kwa macho yangu ya kipelelezi nikayarusha kutazama nani anashuka kana kwamba namjua mtu huyo, kabla sijatoa huko macho nikaona wanaume wawili wakiwa wanapanda basi. Wanaume hawa walinifanya niwatazame zaidi kwa namna walivyovaa na hata mwonekano wao maana nilihisi walikuwa wakifanania na wale niliowaona kwenye ile nyumba ya pembeni na 2345!
Wakati nikiwatazama, mmoja wao akanitazama pia tukakutana macho kwa macho! Tukatazamana kwa kama sekunde tatu kabla hajageuza uso wake kutazama kando. Mimi nikaendelea kumtazama zaidi na zaidi, na hata yeye alilitambua hilo.
Niliwakagua kwa macho yangu na kujiridhisha kuwa huenda wakawa na silaha ndani ya makoti yao. Basi nikaanza kufikiria namna ya kuwakabili kama ni mimi wananifuatilia …
Tukaenda kwa mwendo wa kama dakika sita, nikasimama na kutoa ishara kuwa nashuka kituo kinachofuata kwa kubinya kamba ya kumshtua dereva.
Hivyo tukasonga kidogo tu, na basi likaanza kupunguza mwendo kuashiria laenda kusimama. Liliposimama, nikanyanyuka na kushuka.
Hapa sio nilipotakiwa kushuka ila niliona panastahili mimi kushukia kwasababu ya uwingi wa watu. Hiyo ni kwasababu za kiusalama.
Nikazama ndani ya watu na kujichanganya lakini kwa wakati huohuo nikiwa natazama kama nyuma yangu nafuatwa. Sikuona watu. Wanaume wale hawakushuka. Nikaendelea kuzamia na kuzamia huko hata mahali ambapo sipajui alimradi kujihakikishia usalama. Nilipoona ni salama sasa, nikatulia kwenye benchi na kutoa simu yangu mfukoni, nikawasiliana na Jack.
“Jack, nimetoka kwenye ile anwani! … sijakuta mtu huko!”
“Kabisa?”
“Ndio. Ni samani za zamani na mabaki ya nguo na picha … na kifaa cha kuhemea!”
“Unaweza kun’tumia hiyo picha?”
“Sidhani kama utaielewa, ilikuwa condensed kwenye kioo, imevunjikavunjika.”
“Haionekani hata kidogo?”
“Kwa mbali, ila ni ya mwanamke tu. Ya mtoto haionekani kabisa!”
“Gosh!” Jack akalaumu. Nikamuuliza,
“Vipi, hamna namna ya pili kama ulivyonieleza?”
“Ipo, ila hiyo ya pili nilikuambia itakuwa confirmed na hiyo ya kwanza. Sikukuambia hivyo, we fala?”
“Sasa nifanyeje?”
Akanielekeza mwonekano wa mtoto, kisha akanisihi nirudi kule kwenye anwani 2345 ili nikahakikishe kama huyo mtoto alikuwa anaishi hapo kwa kutumia taarifa za majirani.
Nikamuuliza, “Jack, huyo mtoto ana nini? Kwanini yeye?”
“Sijui, Tony. Ila fanya nilichokuambia kwa maana hiyo MUNICH 2345 itakuwa ni yeye.” Aliponieleza hayo akasema, “Nipo busy na shemeji yako, baadae!” kisha akakata simu.
“Pumbavu!” nikalaani nikiiweka simu kibindoni, kisha nikatoa kile kifaa cha kuhemea ambacho nilikiokota kule kwenye anwani 2345 na kukitazama kwa umakini.
Nikagundua kifaa hicho kilikuwa kimechorwa katuni kwa kutumia ‘marker pen’ rangi ya bluu. Marker pen inayoelekea inaelekea kufifia sasa.
Mchoro huo wa katuni ulikuwa ni wa mwanaume aloyechorwa kwa mtindo wa njiti na nywele zake zikisimama kama vijiti. Nikawaza atakuwa nani huyo? Huenda akawa ni huyo mtoto ambaye Jack anamwongelea?
Sikuwaza sana juu ya hicho, nikakiweka kile kifaa kibindoni kisha nikatazama kushoto na kulia alafu nikaanza kuchukua tena hatua kutoka jengoni humo.

**
Saa tisa alfajiri …

Ngo! Ngo! Ngo! Ngo!
Punde mlango ukafunguliwa, akatoka mwanamke mzee ambaye alinikagua upesi kwa macho yake ndani ya miwani yenye lenzi kali kisha akaniuliza haja yangu.
Tulikuwa tunatumia lugha ya kijerumani.
“Tafadhali, naomba kuulizia,” nikasema kwa sauti ya upole. Mwanamke huyo akatambua, nadhani kwa lafudhi yangu, kuwa mimi mgeni. Akafungua mlango na kunikaribisha ndani.
Nilipoketi akaniuliza kama ningependelea maji ama bia. Ni tamaduni ya wajerumani kunywa bia. Nikamwambia nahitaji maji na ndani ya muda mfupi mkononi mwangu nikawa nimeshikilia glasi ya maji safi.
Kwa muda huo mdogo niliokuwa nimekaa hapo, niligundua kuwa mzee huyo anaishi mwenyewe. Nyumba ilikuwa pweke japo safi na ipo kwenye mpangilio mzuri.
Akaketi na kuniuliza wapi nilipotokea, nikamlaghai natokea Uingereza, alafu pasipo kupoteza muda nikamuuliza juu ya jirani yake, yule anaekaa kwenye anwani 2345. Hii nyumba ya huyu mzee ilikuwa ni ya tatu toka pale kwenye nyumba namba 2345.
Basi huyo mzee akajaribu kuvuta kumbukumbu, ungeliona hilo kwa macho yake, kisha akanangalia na kunieleza yale anayoyajua kuhusu jirani huyo, yaani mwanamke na mtoto wake.
Kwa mujibu wa maelezo yake nikagundua kuwa mwanamke aliyekuwa anakaa kwenye ile anwani alikuwa anaishi mwenyewe pamoja na mtoto wake wa kiume. Na pia alikuwa mgeni, kutokea Marekani.
“Mara kwa mara nilikuwa namsikia akiongea na mwanae kwa kiingereza safi, ila alikuwa anajua pia na kijerumani!”
Hapa sasa ndiyo nikaanza kujenga picha. Kama wakazi hao walikuwa ni wamarekani kwanini walikuwa wanaishi Ujerumani? Na watakuwa na mahusiano gani na Raisi aliyepotea mpaka kumpatia rafiki yake anwani ya nyumba?
Nikamdadisi huyo mzee juu ya mwonekano wa mtoto huyo aliyekuwa anakaa na huyo mama, akanieleza kuwa mwenye nywele nyekundu na mashavu makubwa na macho ya dhani ya paka.
Kwa maelezo zaidi, nikapata kujiuliza kwanini mtoto yule alichora picha ya njiti kwenye kifaa chake cha kuhemea. Yule hakuwa yeye. Sikujiuliza sana nikaaga niende zangu nikiwa sijayanywa yale maji niliyopewa.
Nilifanya hivyo kwasababu za usalama, huwezi jua anaweza akawa ametia nini. Kila mtu ni wa kumtilia mashaka kwenye ulimwengu wa kiitelijensia.
Nilipotoka , nikarusha macho kwenda kwenye ile nyumba ya kando ambayo nilikuwa nikiitilia mashaka. Ile nyumba ambayo iliwameza wale watu ambao walikuwa wakivalia nguo nyeusi. Hapo sikuona mtu, lakini kabla sijageuza shingo yangu nikamwona mtu dirishani akichungulia.
Mtu huyo upesi alitoka dirishani na kupotea!
“Hawa watu ni wakina nani?” nikajiuliza nikitembea zangu kuelekea kituoni, ila mara hii, tofauti na ya kwanza, nikahisi nafuatiliwa kwa mapema zaidi! Kwa mahesabu yangu ambayo yalikuwa sahihi, kulikuwa na gari linalokuja nyuma yangu, tena kwa kasi!
Basi nikaongeza kasi ya mwendo wangu na alafu ile kona ya kwanza nikaikata na kuanza kukimbia upesi. Na kabla gari hilo linifuatalo halijachomoza, nikawa nimejibana nyuma ya nyumba!
Nikachomoza kichwa changu kwa udogo na kuangaza. Punde lile gari likapita hapo likiwa katika mwendo wa pole. Ilikuwa ni Volkswagen modeli ya zamani. Madirishani niliwaona wanaume wakiwa wanachungulia na kurusha macho yao kutafuta jambo. Nyuso zao hazikuwa za amani.
Vuuuuuuupp! Wakapita! Lakini ikiwa imepita kama sekunde mbili tu, mara nikasikia sauti ikifoka kwa kijerumani, “Unafanya nini hapo!” kutazama alikuwa ni bwana wa kijerumani ambaye amevalia kaptula tu, kifua wazi.
Sauti yake ilikuwa kali sana, na majibu yake niliyaona punde tu maana nilisikia sauti ya gari ikivuma na mara ikaja kutuama mbele ya ile nyumba! Kutazama, nikaona mwanaume akitokea na mkono wa bunduki, akayaftua risasi mfululizo! Nilikwepa kwa kujibana kwenye nyumba. Yule mwenyeji aliyenifokea nikamwona akiwahi haraka kuzama ndani!
Kidogo nikasikia milango ya gari ikifunguliwa, hapo nikaona tena si pa kukaa. Kutazama nyuma yangu, yaani ya nyuma ya nyumba ile, kulikuwa na ukuta wa mbao, haraka nikaufata na kuukwea kama nyani!
Nilipotua upande wa pili, nikaanza kukimbia kuufuata ukuta mwingine wa nyumba niliyozamia. Kidogo, nikasikia watu wengine wakitua, walikuwa ni wanaume wawili ambao wananifukuzia! Wakaanza kurusha risasi kwa fujo! Kwa pupa!

***
 
*NYUMA YAKO – 15*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Nilipotua upande wa pili, nikaanza kukimbia kuufuata ukuta mwingine wa nyumba niliyozamia. Kidogo, nikasikia watu wengine wakitua, walikuwa ni wanaume wawili ambao wananifukuzia! Wakaanza kurusha risasi kwa fujo! Kwa pupa!
ENDELEA
Basi haraka nikachumpa kuuvuka ukuta mwingine, hapa hata sikuushika ukuta huu bali kuruka kama samaki. Nikatua kwa ustadi na kisha kukimbia upesi kwanguvu zote kuufuata ukuta mwingine, nao nikiwa nimeukaribia, wanaonikimbiza wakawa wametua. Wakaendelea kufyatua risasi kama njugu!
Hapa moja ikanipunyua mkono na kunisababishia jeraha. Ila sikukoma kukimbia kuokoa nafsi yangu. Nikaruka tena kwenye ukuta mwingine na mwingine na mwingine, alafu nikajificha pahala.
Wale watesi wangu wakasonga wakiwa wameduwaa. Wakatazama kushoto na kulia mimi nikiwa nawachora toka kwenye ua kubwa. Hawakuwa wananiona. Ila kama sijakosea, mmoja wao akahisi huenda naweza nikawa nimejibana nyuma ya ua. Nikaona akimshtua mwenzake akitazama eneo nililopo.
Kuona hivyo, basi upesi nikachomoka na kuwafyatulia risasi. Wote wakalala chini na kunipa amani kwa muda. Nikatoka hapo nyuma ya ua na kukimbia upesi. Nikaruka ukuta mwingine na kuzama barabarani, sikuona mtu nyuma, nilikuwaa mwenyewe sasa. Kidogo nikakutana na gari, nikasimamisha na kumwamuru dereva atoke ndani, alipotii nikazama ndani ya gari na kutimka.
Ila sikufika mbali sana na hilo gari, nikaliacha na kudaka lingine. Nalo liliponisogeza umbali kidogo, nikaliacha na kupanda basi la uma. Nikaenda kabisa nyuma ya basi na kusimama huko. Nilijihisi salama sasa.
Nikafika hotelini na nikiwa naelekea chumbani mwangu, dada wa mapokezi akaniita. Mwanamke mwenye sura pole na mashavu mapana ndani ya sare. Nikamjongea taratibu nikiwa najiuliza nini shida? Akanitazama na kisha akaangalia tarakilishi yake na kuniuliza, “Kuna mgeni wako ulimtuma?”
“Mgeni?”
“Ndio! Kuna mwanaume alikuja hapa kukuulizia.”
“Aliniuliziaje?” nikatahamaki. Basi yule mhudumu akanambia kuwa alitumia maelezo ya mwonekano wangu, na hivyo alivyoniona tu akapata kujua kuwa ndiye mimi. Nami nikamuuliza mtu huyo aonekanaje? Akanieleza.
Maelezo yake yakajenga picha kichwani mwangu kuwa mtu huyo atakuwa ni miongoni mwa wale wajamaa ambao nilipanda nao basi kabla sijawapotea.
Ina maana wameshajua makazi yangu mapya? Nikaona hapa si mahali pa kukaa tena. Nikanyookea chumbani mwangu na kuanza kukusanya vitu muhimu kutoka kwenye begi, haswa pesa na kadi. Lakini kabla sijatoka, nikasikia hodi mlangoni! Nikatulia tuli nikipepesapepesa macho yangu. Kidogo sauti ya kiume ikasema, “mhudumu!” kisha kugonga tena mlango.
Sikusema kitu. Nikaweka silaha yangu mkononi na kujongea mlango. Sijaufikia, nikastaajabu mlango umekumbwa na teke! Ukang’oka na kunivamia na kunidondosha chini!
Kutazama, nikamwona mwanaume akiwa amevalia nguo nyeusi. Sura yake haikuwa ngeni. Alikuwa ni miongoni mwa wale wanaume niliopanda nao basi kabla sijawapotea. Mkononi mwake alikuwa amebebelea bunduki!
Basi haraka nikaunyanyua mlango na kujikinga nao. Bwana yule akatupa risasi kama tano vile pasipo kupumzika, zote zikaishia mlangoni. Mimi nilipochomoza na kumtwanga yangu moja, akawa amekwisha! Alidondoka chini kama mzigo akiwa ameachama mdomo.
Upesi nikanyanyuka na kumtazama. Punde nikasikia sauti kali ya mwanamke ikipiga yowe huko mbali. Hapa nikahisi hamna tena usalama, huenda kuna wavamizi wengine! Nikatoka ndani kushika korido, ila uso kwa uso, umbali wa kama hatua kumi na nane, nikaonana na wanaume wawili wakiwa wanakuja wamebebelea bunduki!
Upesi nikarudi ndani. Nikasikia vishindo vya watu vikikimbia kuja. Nikavunja dirisha na kutokea nje. Chumba changu kilikuwa ghorofa ya kwanza, nikarukia huko chini nikitulia pazia lililokuwa limefunikia magari yaliyoegeshwa, kisha nikajitupia chini na kukimbia!

**

“Kama nisipofanya mambo haya upesi, nadhani yatazidi kuniwia vigumu zaidi na zaidi!” niliteta na Jack nikiwa nimeketi kwenye kiti ndani ya nyumba ya kupumzikia. Niliongea naye kwa muda sana na mwishowe alipokata simu nikajilaza kitandani na kuwaza mambo kadha wa kadha.
Kwa maelezo ambayo nilimpatia Jack, aliniambia yanasawiri na namna alivyokuwa anawaza lakini asiniweke bayana kipi ambacho kipo kichwani mwake, akataka ningoje kwa muda kidogo. Hivyo hapo nilipokuwa nimejilaza nilikuwa namngoja.
Zikapita kama dakika sita, usingizi ukaanza kuninyemelea. Nilisinzia nikipambana na macho yangu mazito. Ikiwa kama dakika ya nane kama niko sahihi, simu yangu ndiyo ikaita Jack akirudi tena hewani.
“Sasa sikia …” akaanza kwa kauli hiyo kisha akanambia kuhusu yule mtoto ambaye alikuwa anakaa na mama yake kwenye nyumba yenye anwani 2345. Kumbe alishamtambua mtoto huyo na kunituma kwenda kumuulizia mwonnekano wake ilikuwa ni kwa ajili ya kuthibitisha tu.
Lakini mtoto huyo ni nani haswa? Hakuwa anafahamu japo nishamwambia kuwa ni Mmarekani. Na kuhusu mama yake, Jack hakuwa na taarifa naye hata kidogo!
Ilikuwa ni ajabu kidogo kwani Jack aliniambia alifanikiwa kum – trace mtoto huyo kupitia game la ‘Subway Surfers’ ambalo humo ndani, kwa ridhaa, wachezaji huweza kuunganisha na mtandao wao wa Facebook ili washindane na marafiki zao.
Lakini zaidi, unaweza ukatazama kuona wachezaji gani wana points nyingi ulimwengu mzima. Basi kwa kupitia huko, Jack Pyong akakuta jina la MUNICH 2345. Na aliposaka jina hilo mtandaoni akitumia picha aliyoiona humo mchezoni, akafanikiwa kulipata. Kwa ufupi, jina la mtoto huyo huitwa Brussels, lakini jina lake la mchezoni hutumia MUNICH 2345, yaani jina la anwani ya nyumba alokuwa anakaa.
“Sasa tunaweza tukampata wapi yeye na mama yake?” nikamuuliza Jack.
“Usijali,” Jack akan’toa hofu. “Mpaka kufikia kesho n’takuwa nishapata!” tukamaliza maongezi na mie nikajilaza sasa.
Nikiwa usingizini, nadhani kwasababu ya kupitia purukushani hapa karibuni za mara kwa mara, nikaota ndoto ya kunishtua. Nilijikuta nikinyanyuka upesi na kushikilia bunduki yangu lakini nilipotazama huku na kule sikuona kitu. Nilikuwa mwenyewe!
Kidogo usingizi ukawa umenitoka. Nikashika simu yangu na kuperuzi, nikaukuta ujumbe toka kwa Daniele. Alikuwa akinijulia hali na kuniuliza wapi nilipofikia. Ujumbe huo ulikuwa umetumwa dakika tisa nyuma.
Nikaujibu kisha nikaweka simu pembeni. Sikutarajia kama Daniele angeujibu kwani ilipita muda kidogo tangu autume lakini kinyume na matarajio yangu, akajibu punde tu. Na hapo ndipo nilipoingia naye kwenye uwanja wa kuchat kw muda kidogo akinieleza mambo kadha wa kadha.
Lakini zaidi lililokamata hisia zangu ni mashambulio mawili ambayo Daniele na timu yake waliyapitia ingali wakiwa kazini. Kwa mujibu wa Daniele, walishambuliwa na mwanamke mmoja na wanaume watatu. Ingawa walikuwa wameficha nyuso zao lakini waliwatambua kutokana na maumbo yao ya mwili.
Shambulio la kwanza lilitokea wakiwa wametoka kwenye nyumba ya Makamu wa Raisi na ya pili wakitoka kwenye ofisi ya Wizara ya usalama wa ndani!
“Watu wangu wawili wameuawa kwasababu ya mashambulizi hayo, na hata kupotea kwa baadhi ya nyaraka. Nimepeleka taarifa kwenye uongozi, wakaniongezea ulinzi.”
Nami nikamshauri kushirikiana na Jack Pyong kwenye mambo kadhaa haswa ya kiteknolojia kwani anaweza kumsaidia. Kwa mawasiliano zaidi nikampatia namba za Jack na hata kumtaarifu Jack juu ya swala hilo.
Baada ya hapo, nikalala.

**

Saa kumi na moja asubuhi…

Nina uhakika simu ilinguruma mara moja tu kabla sijaamka. Niliitazama nikiwa nimekunja uso wa usingizi, kwenye kioo nikaona nimetumiwa na Jack ‘location’ ya eneo ambalo naweza kumpata yule mtoto ambaye tulimjadili.
Basi usingizi ukanikata papo hapo, nikanyanyuka nikaoga na kuvaa kisha kushika barabara kwenda huko ambako Jack alikuwa amenielekeza. Mahali mbali kabisa na jiji la Munich. Tena msituni. Ulikuwa ni kama mwendo wa masaa matano kasoro kwa basi mpaka kufika huko. Huko wenye msitu huo wa ‘Black forest’ ambapo ndipo location ilipoongoza.
Mpaka kupata na kupanda basi ikawa tayari ni saa moja asubuhi, safari ikaanza. Kama kawaida nilikuwa nimekaa nyuma ili nipate nafasi ya kutazama abiria wote ndani ya basi, watakaoshuka na wale watakaoingia.
Nikiwa nimekaa huko nikawa nawaza sana kichwani mwangu, mtoto huyo atakuwa anafanya nini huko Black Forest?
Yupo mwenyewe au na mama yake?
Je wapo wenyewe au na watu wengine?
 
*NYUMA YAKO – 16*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Nikiwa nimekaa huko nikawa nawaza sana kichwani mwangu, mtoto huyo atakuwa anafanya nini huko Black Forest?
Yupo mwenyewe au na mama yake?
Je wapo wenyewe au na watu wengine?
ENDELEA
Basi mawazo hayo yakanifanya nisisinzie ndani ya basi nikawa natazama dirishani na muda mwingine mlangoni pale ambapo basi lilikuwa linasimama.
Tulipotembea kwa muda wa kama lisaa limoja, basi likasimama nasi, watu ndani ya basi, tukapata wasaa wa kununua vitu vya kuchangamsha kinywa na kujaza matumbo kisha safari ikaendelea.
Hapo tukatembea kwa lisaa limoja tena tukawa tumefika Black Forest. Nikashuka na nikiwa natazama simu yangu nikaanza kusonga.
Haki ulikuwa ni msitu mkubwa sana. Sikujua kwanini uliitwa Black Forest, yaani msitu mweusi, na kwa muda huo bado sikuwa najua kwanini msitu huo ni maarufu nchini Ujerumani.
Ulikuwa umeota mgongoni mwa safu ya milima. Hapa kukiwa kimya na kwa mtu mwenye woga akikaa mbali aogope hata kukatiza.
Basi kwakuwa maelekezo ya kwenye simu nilishayameza, nikaweka simu mfukoni na kuendelea kuzama msituni. Nikatembea kwa kama kilomita moja na nusu, bado milima tu ilikuwa imenizingira, mbele na nyuma yangu kwa sana.
Nilipomaliza kilometa mbili, kwa mahesabu ya harakaharaka, nikaanza kujiuliza kama kweli nitakuwa nimefuata maelekezo ninayotakiwa kwani sikuwa naona alama wala ishara yoyote ya binadamu.
Nikatoa simu yangu mfukoni nitazame. Nilikuwa sahihi. Nikairejesha na kuendelea kukwea. Kidogo kwa umbali, nikaona kijumba cha rangi nyeupe. Kilikuwa ni kijumba pweke maana kikipakana na miti pekee.
Basi nikazidi kusonga na kusonga, nikiwa naamini sasa kile kijumba ndipo mahali ninapotakiwa kufika. Na niliposonga zaidi na zaidi nikagundua kuwa kile hakikuwa kijumba bali nyumba, ni unbali tu ndio ulikuwa unafanya paonekane padogo.
Lakini … nikapata maswali. Mtoto yule atakuwa anafanya nini huku msituni kwenye nyumba ile? Na kama yupo na mama yake, kwanini wanaishi huku? Mbali kabisa na dunia?
Mawazo haya yakanipa hoja niliyotokea kuiamini. Kuna kitu hakipo sawa. Na hivyo natakiwa kubeba kila aina ya tahadhari ninapoelekea kwenye nyumba hiyo.
Niliposonga, nikiwa nimebakiza umbali wa kama robo kilometa kuikuta ile nyumba, nikatulia na kuitazama vema kuikagua. Nilipokuwa nimekaa palikuwa ni eneo la juu kidogo hivyo palinipa fursa ya kutazama vema.
Kwa usalama zaidi nikalala chini na nikatenga dakika kama kumi za kukagua eneo hilo kabla ya kupasogelea zaidi.
Basi nikiwa hapo, nikatulia tuli sana. Palikuwa ni eneo tulivu mno ukiondoa upepo usukumao matawi ya miti.
Ikiwa kama imepita dakika tano tangu nilale hapo, nikastaajabu kichwa changu kikisukumizwa na kitu kigumu kisha sauti ya kijerumani ikaniamuru, “Tulia hivyo hivyo!”
Nami nikatii nikiamini kuwa mtu huyo amenishikia bunduki.
Akaniuliza mimi ni nani na hapo nafanya nini, tena akiwa ananisisitizia nisigeuke kumtazama. Kwa taratibu nikamjibu mimi ni mtalii na nalishangaa kuona nyumba hiyo msituni.
Akaniamuru nisimame nikiwa nimenyoosha mikono juu. Nikatii. Bado nikiwa simtazami. Akanipekua upesi kwa mikono, akahisi nina silaha. Akaichomoa, ilikuwa ni bunduki yangu. Hapo ndiyo nikaona akitupa mti kando na kutumia silaha yangu kuniwekea kichwani!
Kumbe hata silaha hakuwa nayo.
Sasa akaniamuru nigeuke. Nilipofanya hivyo nikakutana na mwanaume aliyevalia hovyo, ndevu nyingi na kofia ya soksi nzito kichwani. Mkononi mwake alikuwa amebebelea tunda, papai, akila kana kwamba sokwe mtu.
Akaniuliza, “unataka kufa?”
Sikumjibu. Akarudia tena swali lake, “Unataka kufa?”
“Hapana!” nikamjibu, asiniongeleshe kitu akashika njia kwenda zake. Alipopiga hatua tatu akanigeukia na kunambia, “kama hutaki kufa, nifuate!”
Basi mimi nikamfuata. Njiani nikamuuliza yeye ni nani na anafanya nini humo msituni. Hakunijibu. Alikuwa kimya akiwa anakula tunda lake ambalo halijamenywa!
Baada ya kama dakika kumi za kutembea, tukafika mbele ya kijumba dhoofu, kimesanifiwa kwa magogo na majani. Humo akazama ndani na kunitaka mimi nikae pale nje. Kidogo akatoka akiwa amebebelea kikombe cha bati ambacho sikujua mule ndani ameweka nini. Akawa anakunywa.
Akanitazama kana kwamba ndo’ mara ya kwanza ananiona alafu akaniuliza, “wewe ni nani?”
“Nishakwambia hapo awali,” nikamjibu. Akakunja uso na kuuliza, “muda gani? Nimekutana na wewe popote pale?”
Nikastaajabu. Nikadhani ananifanyia utani.
“… hata silaha yangu umechukua wewe!” nikamweleza. Akajitazama na kujikuta na bunduki. Haraka akanirushia akinitazama kwa mashaka. Hapa nikafahamu na kuthibitisha kuwa mtu huyu hakuwa sawa.
Nikamweleza mimi naitwa Jerry na nilikuwa nataka kufahamu juu ya nyumba ile iliyopweke msituni!
“Nyumba ipi hiyo?” akaniuliza akiwa ameweka kituo kutafuna.
“Ile ambayo ulinikuta naitazama,” nikamjibu. Akan’tazama kwa mashaka kisha akaniuliza, “ipi hiyo?”
Nikaona isiwe tabu nikamwelekeza. Ajabu alikuwa anaifahamu. Kumbe bwana huyu ana tatizo la kupoteza kumbukumbu za karibu. Alipojua ninachokiongelea, akaendelea kutafuna kisha muda si mrefu akaniuliza, “Una biashara gani hapo?”
“Nataka tu kujua,” nikamjibu na kuongezea, “Ni wakina nani wanaishi hapo?”
“Sijui nani anaishi hapo!” bwana yule akan’jibu. Kabla sijaongea, akaendelea, “Huwa naona watu kadhaa hapo. Sijui nani anapaishi?”
“Unaweza kunambia watu hao ni wa aina gani? Yaani wapoje?”
“Wapo kama wewe!”
“Kivipi? Namaanisha mwonekano wao? …” nikamwona akifikiria pasipo malengo. Nikamkatisha kwa kumuuliza, “Vipi, ushawahi kumwona mtoto hapo? Mvulana mwenye nywel nyekundu?”
Akanitikisia kichwa kukataa.
“Na je mwanamke? Hujawahi mwona mwanamke hapo?”
Akanitikisia tena kichwa akibetua mdomo. Alafu akang’ata tunda lake na kutafuna.

**

Baada ya dakika nane …

“shhhiiii!” nikamwonya yule jamaa yangu mwehu niliyemkuta ndani ya msitu. Alikuwa nyuma yangu wakati mimi nikiwa nimejibanza mtini natazama nyumba ninayotaka kuelekea.
Nilipomwonya hivyo, akafunga mdomo wake, nami nikarusha macho yangu kutazama ile nyumba ambayo kwa muda huo ilikuwa ipo kama hatua kumi na mbili tu tokea tulipo. Bado palikuwa kimya. Ni kama vile hakukuwa na mtu hapo.
Nami nilikuwa nimevalia mavazi ya hovyo sana kama mtu yule niliyeongozana naye. Nilimwomba mavazi yake ili basi yakanisaidie pale mambo yatakapokuwa yamenielemea.
Nilipoona ni kimya tu, nikatoka hapo mtini nikiwa nimemwelekeza yule jamaa wangu abakie hapohapo mtini nami nitarejea. Nikaelekea mbele kabisa ya ile nyumba na kujifanya nikiimba wimbo ambao hata siujui na huku nikitazamatazama huku na huko na kuokotaokota vitu vya ajabu.
Punde akatoka mwanaume mmoja aliyekuwa amevalia sweta nyeusi inayokaba koo na suruali jeans ya bluu mpauko. Mkononi alikuwa na bunduki ndogo. Akan’tazama na kuniuliza kwa amri, “wewe nani?” Alikuwa anatumia lugha ya kijerumani.
“Mimi Jerry!” nikamjibu, kisha nikampuuzia na kuendelea kuokotaokota vitu. Akapaza sauti, “hey! Sikia!” nikamtazana.
“Hapa si mahali pa kuchezeachezea, sawa? … potea!”
Kabla sijasema kitu, yule jamaa wangu niliyemwacha mtini akatoka na kupaza sauti akiuliza, “Ninyi! Mnafanya nini hapo?”
Nikamwona yule jamaa aliyetoka ndani ya nyumba akishikwa na tahadhari. Akaikamata silaha yake vema akiwa amekunja sura. Mara akaninyooshea na kuniuliza. “mnafanya nini hapa?”
Yule jamaa kule pembezoni mwa mti akapaza sauti, “muue huyo! Kwanza amevalia nguo zangu! Sijui kazitoa wapi?”
Yaani alikuwa ameshasahau kuwa yeye ndo’ kanipa!
Nikamtazama kwa kushangaa lakini huku nikijipapasa kufuata silaha yangu. “Phili, unasemaje?” nikamtunga jina upesi. Kabla jamaa yule hajajibu, nikawa nimeshapata silaha yangu kiunoni, nikaichomoa upesi na kumwonyeshea yule jamaa aliyetoka ndani ya nyumba.
“Weka silaha chini!” nikamwamuru. Akawa mbishi. Naye alikuwa ameninyooshea bunduki akiwa amen’tolea macho.
“Siweki, weka wewe!”
Nikamwambia, “unajua sisi tuko wawili. Unadhani yule ni chizi sio?”
Akageuza shingo yake kumtazaama yule jamaa wangu kule pembeni ya mti. Jamaa akatabasamu kama mdoli.
“pale ana silaha, anasubiri nimpe amri tu. Usiwe mjinga, weka silaha chini nyoosha mikono juu!” nikamsihi. Akafikiri kidogo.
“Wewe ni nani?” akaniuliza. “Muamerika?”
Sikumjibu.
“Hautatoka ndani ya msitu huu salama. Hata kama ukiniua.” Akasema akinitikisia kichwa. Mimi nikaendelea kumsihi, “weka silaha chini! Mara hii sitaongea tena, sina muda wa kupoteza!”
Basi akatii amri yangu baada ya kun’tazama kwa sekunde tatu.

***
 
*NYUMA YAKO – 17*
*Simulizi za series*

ILIPOISHIA
Sikumjibu.
“Hautatoka ndani ya msitu huu salama. Hata kama ukiniua.” Akasema akinitikisia kichwa. Mimi nikaendelea kumsihi, “weka silaha chini! Mara hii sitaongea tena, sina muda wa kupoteza!”
Basi akatii amri yangu baada ya kun’tazama kwa sekunde tatu.
ENDELEA
Nikazama naye ndani nikiwa nimemwekea bunduki kichwani. Sebuleni nikawakuta wanaume wawili ambao nikawaamuru waweke silaha chini la sivyo nitammaliza mwenzao. Ajabu wakatii. Nikasonga kidogo na kumwamuru mmoja wao akafungue milango, nipate kuona yaliyondani.
Wakati anafanya hivyo nikawa nawataza kiumakini wasifanye jambo lolote. Ndani ya chumba cha kwanza nikampata mtoto na mama yake. Mtoto yule ambaye nilishaambiwa na Jack Pyong.
Nikawaamuru wasonge mbele na kwa tahadhari nikawafyatulia risasi wale wanaume watatu miguuni washindwe kunifukuza nitakapotoka hapo kisha nikamwamuru yule mtoto ambaye nimemtoa humo ndani aziokote silaha na kunipatia. Baada ya hapo tukatoka ndani na kuzama msituni, hamaki yule bwana mwehu naye akaungana na sisi. Tukawa tunakimbia.
Sikujua tunaelekea wapi, ila nilitaka tu twende mbali na lile eneo kwa usalama wetu. Lakini tukiwa tunasonga, kidogo yule mama, mama ambaye nimetoka kumwokoa kwenye mikono ya wale wadhalimu, akanishauri tuelekee upande wetu wa mashariki.
Nami pasipo kubisha, maana sikuwa na huo muda, tukaongoza kwenda huko tukiwa tunakimbia. Kidogo, tukasikia sauti za pikipiki nyuma yetu. Tulipogeuka na kuangaza hatukuziona. Zilikuwa mbali ila kiuhakika zikija uelekeo wetu.
Tukakazana kukimbia, na kama baada ya dakika mbili, sasa tukaanza kuona pikipiki zikija kwa kasi nyuma yetu. Zilikuwa tatu kwa idadi. Kila moja ikiwa imebebelea watu wawili wawili, wa nyuma akiwa amebebelea bunduki!
Nikapaza sauti, “kimbiaa! Kimbia!” lakini ni wazi tusingeweza kimbia zaidi ya kasi ya pikipiki. Na nilihofia endapo watu wale wangeanza kufyatua risasi ingetuwia vigumu kupona.
Kweli, risasi zikaanza kurushwa kwa fujo! Zikapasua na kutoboa miti huku zikitupunyua na kupita kando za masikio yetu. Kidogo, yule jamaa mwehu tuliyekuwa tunaongozana naye, akabamizwa risasi ya mgongo! Niliona damu zikowa zinaruka kama vumbi, na mara akadondoka chini!
Ulishawahi mwona farasi akidondoka ingali yu kwenye kasi? Namna anavojikita na kujivunjavunja? Naam ndivyo ilivyokuwa kwa bwana huyu. Alidondoka vibaya mno, nahisi alivunjika vibaya sana haswa uti wake wa mgongo na shingo.
Nilitamani sana kumtazama kwa kujali lakini sikuwa naweza maana kufanya hivyo kungekuwa ni kutaka kifo. Nikaendelea kukimbia pamoja na wale niliowaokoa, lakini sasa mambo yakiwa magumu zaidi. Niligundua risasi zote zilikuwa zimenielekea mimi, kuniangusha chini, kwani zilinipita pembeni ama kupasua miti niliyokuwa nayo karibu, na hatimaye moja ikan’tifua begani!
Bahati haikunipasua mfupa, bali ilizama kwenye nyama na kunifanya nivuje damu kwa wingi. Vitu vingine ni kama bahati tu. Muda mwingine Mungu humsaidia mja wake pale anapokuwa anatenda lile lililojema, huwa naamini hivyo. Kuna muda niligeuka kutazama nyuma na kumbe muda huohuo risasi ilitupwa kunipasua kichwa, hivyo kugeuka kwangu kukawa kumeniokoa!
Risasi ikaparasa shavuni kwa upesi na kwenda kukomea mtini! … pah! Hata nikatahamaki.
Ila nilikuja kujifunza kuwa, watu wale waliokuwa wanatukimbiza walikuwa wamedhamiria kunimaliza mimi na si yule mwanamke na mtoto. Niliona wao wakiwa hawalengwi wala kudhamiriwa. Risasi hazikuwa zikiwapunyua na kuwawinda bali mimi na yule jamaa yangu ambaye tayari ameshalambishwa vumbi!
Basi kujua hilo, nikaanza kujisogeza kwa yule mwanamke na mtoto mpaka kujiweka mbele yao ingali sijui wapi tunapoelekea. Kwa kufanya hivyo, ghafla risasi zikakoma kurushwa. Kumbe nilikuwa sahihi!
“Usifyatue! Usifyatue!” nilisikia sauti ikiamuru kwa kijerumani. Hapa ndiyo nikajua na kuthibitisha kumbe wale mateka bado walikuwa wa thamani kwa wale wadhalimu. Bado walikuwa wanawahitaji na hiyo ni kumaanisha bado kuna kazi hawajaimalizia.
Lakini kukaa huku mbele ya mateka kusingelidumu kwa muda! Pikipiki zilikuwa zinakuja kwa kasi nyuma yetu na sasa ungeweza kusema kwamba, baada ya kama dakika moja tu, tutakuwa tumeshafikiwa na kunyakuliwa!
Kwahiyo basi hapa ilinilazimu kutafuta namna ya kutuweka salama. Nikachomoa bunduki mbili toka kiunoni mwangu na kuanza kuwatupia risasi wale waliokuwa wanatukimbiza. Kwa kufanya hivyo wakapunguza kasi na hata kuzubaa kwa kujikinga dhidi ya risasi!
Na kumbuka wao walikuwa hawawezi tena kunitupia risasi kwakuwa najifichia kwa watu wasiotaka kuwaua.
Nikawadungua watatu, wawili walikuwa madereva, mmoja akiwa abiria. Nikawa nimebakiza pikipiki moja. Nayo baada ya kusonga karibu zaidi, nikamfyatulia dereva risasi, akaikwepa na kumpata abiria wake. Akadondoka chini dereva akiendelea kutufuata.
Basi baada ya kuona amebakia mmoja, tena dereva ambaye alikuwa ameweka nguvu zake kwenye usukani, nikasimama na kumweka vema kwenye rada alafu nikamfyatulia risasi mbili kwa wakati moja, nikapasua mabega yake na kumfanya achie usukani! Kabla hajadondoka chini, nikamtupia tena risasi nyingine, ikatoboa kofia yake ngumu na kumpasua kichwa, akajifia.
Basi mimi nikarudi nyuma, nikawamalizia wale wengine walioko chini kwa mbali, kisha nikachukua pikipiki ya yule aliyekuwa mbele kabisa, niliyetoka kumuua punde, kisha nikambeba yule mwanamke na mwanaye na kutimka kwa kasi!
Nikaendesha pikipiki hiyo kana kwamba nacheza mchezo wa kwenye kompyuta ama simu. Nilikwepa miti kama mchezo huku nikisababisha hofu kubwa kwa wale niliowapakia. Walikuwa wakipiga yowe na kunisihi nipunguze kasi lakini sikuwaskiza kwani nilikuwa najua ninachofanya. Nilitaka kuumaliza msitu huu angalau niikute lami na kunyoosha nayo.
Kidogo tena tukasikia sauti za pikipiki zatujia. Nikaongeza kasi zaidi, punde tu, tukafika mpakani! Hapa tulikuwa tumesimama juu ya korongo, na huko chini, kama mita mia tano, kukiwa na mto mkubwa wenye maji ya kasi!
Nikakunja kona na kuanza kuambaa ambaa na hili korongo kwenda upande ambao mto unaelekea. Kama dakika tatu, kwa nyuma, wakatokea watu waliokuwa juu ya pikipiki sita! Wakawa wanatukimbiza kwa kasi sana, kasi zaidi ya pikipiki yetu.
Na kidogo tu, wakaanza kutupa risasi kwa fujo. Hawakuwa wanalenga watu bali pikipiki, nadhani lengo lao lilikuwa ni kupasua matairi ama kutusababishia ajali watukamate. Nilijitahidi kuiyumbisha pikipiki kuwakwepa ila napo nikaona kuna hatari ya kuwabwaga abiria.
Nikaendelea kukazana na mwendokasi. Lakini napo nisifike mbali, mbele yetu tukaona watu wakiwa wamesimama, watano kwa idadi, wakiwa wameziba njia na pikipiki zao. Mikononi wamebebelea bunduki na wamezielekezea upande wetu!
Hapo nikamsikia yule mwanamke niliyembeba akisema, “tunakufa!” naye mtoto wake akadakia kwa kusema vivyo hivyo, “tunakufa!” Mimi nikawaambia, “nishikeni kwanguvu!”
Kisha nikaminya mafuta na kuelekezea pikipiki korongoni! Tukashika ardhi kwa muda mdogo tu kabla pikipiki haijapaa hewani kwa muda wa kama dakika moja na kisha kutumbukia kwenye maji!
Waaah!!

**
Nilipoyazidi nguvu maji, nikatoa kichwa changu na kutafuta watu niliozama nao. Sikuwaona! Si kwamba maji hayakuwa na nguvu, hapana, bali angalau niliweza kuyamudu tofauti na mwanzoni tulipozama, yalikuwa na nguvu mno!
Nilitazama kushoto na kulia, bado tulikuwa ndani ya msitu, na bado sikuwa nawaona ‘watu wangu’. Nilipiga mbizi nikijitahidi kwa nguvu kuelekea maji yanapotokea, ila kidogo nikasikia sauti ya kike toka nyuma yangu, “msaada!”
Nilipopinda shingo kutazama, nikamwona yule mwanamke akipambana kumsaidia mwanaye. Lakini maji yakimzidi nguvu, akizama na kunyanyuka na kunywa maji!
Basi upesi nikarudi na kumfikia. Nikamnyakua mtoto na kumtaka anishike wakati mimi nikiwa natumia mkono wangu mmoja kupiga mbizi twende pakavu. Mtoto hakuwa ana ufahamu. Kichwa chake kilikuwa kinavuja damu.
Tulipofika pakavu, nikamtazama mtoto na kubaini alikuwa amejigonga kwenye jiwe ingali tu mtoni. Na kwa namna alivyokuwa anatoka damu, inabidi ifanyike namna upesi ya kumsaidia, la sivyo alikuwa anatuacha!
Nikamwambia mama yake, “gandamizia mahali pa jeraha, nakuja!” mimi nikaenda kutafuta majani yatakayoweza kumsaidia jerahani.

***
 

Similar Discussions

10 Reactions
Reply
Back
Top Bottom