Nusu ya mabasi nchini ni hatari

JamiiForums

JF Official Account
Nov 9, 2006
6,202
5,012
Posted by BabuK | May 15, 2012

WAKATI kukiwa na kilio cha ongezeko la ajali zinazosababisha vifo vya mamia ya Watanzania, uchunguzi wa gazeti hili umebaini hatari kubwa ya ongezeko la ajali kutokana na nusu ya mabasi yanayotumika nchini kuwa mabovu na hatari.

Ili kukabili hali hiyo na kunusuru maisha ya Watanzania, zaidi ya Sh bilioni moja zinahitajika kujengea miundombinu ya kuwekea mitambo maalumu itakayobaini tatizo la ubovu wa magari usioonekana kwa macho ya wakaguzi.

Sambamba na fedha hizo, inahitajika sheria ya ukomo wa muda wa matumizi ya magari, kusafirisha abiria ili kuwaepusha na ajali zitokanazo na ukuukuu wa vyombo hivyo, kwani kwa sasa haupo. Aidha inatakiwa Mamlaka maalumu ya kushughulikia usalama huo.

Katika hatua ya awali ya kuokoa maisha ya Watanzania kutokana na ajali za barabarani, imebainika kuwa mitambo minne imeshaingizwa nchini kutoka Italia na Afrika Kusini kukagulia magari ya aina zote.

Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwepo kwa kasoro katika vyombo vya moto vinavyotumia barabara nchini, hususan Dar es Salaam, licha ya kukaguliwa na askari wa usalama barabarani na kupewa vibali vinavyoviruhusu kutumika.

Vile vile, uchunguzi huo umebaini kuwapo magari yenye stika za Mamlaka ya Usafiri wa Majini na Nchikavu (SUMATRA) zilizoghushiwa, ili kujipa uhalali wa kutembea barabarani yakiwa na upungufu mwingi, ukiwamo wa kuchomoka vifaa, kuzima bila dereva kuwa na taarifa na kutoa moshi unaochafua mazingira.

Mengi ya magari hayo yenye rangi zinazopendeza nje, yanaelezwa kupumbaza askari wa usalama barabarani na kuendelea na usafirishaji wa abiria katika mazingira ya hatari bila wasiwasi.

Madereva kadhaa wa daladala waliozungumza na gazeti hili kwa masharti ya kutotajwa majina, walithibitisha kuendesha magari hayo, huku yakiwa na matatizo mengi ya kiufundi kutokana na umasikini.

“Daladala nyingine tunaringa nazo lakini tunazibembeleza ili tupate mlo wa siku. Wengi wetu tuna zaidi ya miaka 12 ya udereva wa daladala, lakini hatuoni cha kujivunia, ni kuvuta moshi na kulazimisha sukani tu, kwa sababu matajiri wanalazimisha yawe barabarani hata kama yamechoka. Angalia hili, halifai, hapa na pale limezima,” alisema dereva wa kwanza na kuongeza:

“Unajua matajiri wetu ndio walewale, ukiacha kazi kwa huyu leo au kesho utakuwa kwa yule na kesho kutwa utarejea kwa wa awali. Magari tunayopewa ni yale yale ya miaka nenda rudi, kwa hiyo tunayajua.

“Mengine yapo barabarani kwa miaka 30 sasa na ukiangalia kwenye makaratasi, utakuta umri umeghushiwa, lakini ndiyo hivyo, hatuwezi kupiga kelele, hatusikiki.”

Dereva mwingine alieleza siri ya kupenya kwao mikononi mwa wakaguzi wa magari wa kikosi cha usalama barabarani na kupata hati inayoonesha ubora wa magari yao kuwa ni pamoja na kuyafanyia matengenezo katika maeneo machache wanayojua kuwa wakaguzi hao watayagusa.

“Kwa kuwa tunajua trafiki wanalenga wapi, pindi tunapohisi dalili za ukaguzi tunayafanyia matengenezo ya muda kwenye breki, taa, vioo vya mbele na kuweka vifuniko vipya kwenye sukani. Wao wakija kukagua, wanakwambia washa taa, zima, kanyaga breki, kata kona … dereva mjanja anapata kila kinachotakiwa na kuingia barabarani,” alisema.

Dereva huyo aliongeza kuwa wanaosababisha uzembe huo ni wamiliki wanaotaka magari yao yafanye kazi saa 24 kwa siku saba na hivyo kuyanyima muda wa uchunguzi wa kiufundi na kutengenezwa.

“Ndiyo maana udeiwaka umekithiri. Hakuna dereva halali anayeweza kuendesha gari kwa saa 24 kila siku na kwa kuwa matajiri wanataka hesabu kila jua linapozama, tunalazimika kuwapa tunaojua watatusaidia kuzitafuta bila kujali ujuzi wao wala leseni, ilimradi tunawaambia wasigonge, siku inapita. Lakini ukweli ni kwamba daladala zetu za ‘kibongo’ hazipumziki kwa muda unaotakiwa, ndiyo maana zinakufa ovyo,” alisema.
Sumatra yadanganywa

Uchunguzi ulibaini pia kuwa kwa namna moja au nyingine, Sumatra inadanganywa na wamiliki wa magari kuhusu taarifa muhimu zinazotakiwa na Mamlaka hiyo, ili itoe leseni.

Miongoni mwa taarifa hizo ni umri wa magari, anuani za wamiliki, nakala za mikataba ya ajira ya madereva na leseni za udereva za wanaopaswa kuyaendesha.

Baadhi yao wamekuwa wakikabidhi Sumatra picha, nakala za leseni za udereva na viambatanisho vingine vinavyozungumzia ndugu zao au watoto wa wajomba zao ambao si madereva halisi walio kwenye daladala.

“Ndiyo maana yake, hata gari hili ninaloamsha kila siku, dereva wake anayetambulika Sumatra si mimi. Nimeliendesha kwa miaka mingi na sijasababisha ajali. Anayetambuliwa na Mamlaka hiyo anaendesha RAV4 yake kwa shughuli zake, sasa tatizo linakuja pale ninapotaka kupumzika na kumpa msaidizi, lazima niwe roho juu maana hata akigonga hawezi kufanywa kitu kwani hakuna anayemjua,” alisema dereva wa tatu.
Sumatra wazungumza

Sumatra wakizungumzia hatari hiyo, walikiri upungufu huo na kusisitiza kuwa unaanzia kwa wakaguzi wa magari wanaowapa waomba leseni hati zinazoonesha kuwa magari yao yako sawa kwa kila kitu.

“Sisi hatutoi tu leseni ya usafirishaji mpaka tuone hati ya askari wanaokagua magari, wanapoingia barabarani na kugundulika kuwa na matatizo, inakuwa ni jinai inayohusu Polisi moja kwa moja,” alisema Meneja wa Leseni wa Sumatra, Leo Ngowi.

Ngowi alisema pia kuwa yapo magari wanayoyagundua mapema, kuwa na matatizo licha ya kupitishwa na wakaguzi hao na hivyo kuwanyima leseni na kuwashitaki kwa kuwa na stika za kughushi za Mamlaka hiyo.

“Ni kweli magari yaliyoghushiwa umri yapo, lakini mengi tunayakamata kabla ya kuyapa leseni kutokana na ukaguzi tunaoamua kuufanya sisi wenyewe baada ya kuona hitilafu za wazi.

“Kuna aliyerudisha umri wa kutengenezwa gari lake kwa miaka 14, yaani lilitengenezwa mwaka 1989 akadanganya kwenye kadi kuwa ni la mwaka 2003, lakini mkanda ulimuumbua, kwa kuwa ulikuwa na maelezo yote bila yeye kujua,” alisema Ngowi na kuongeza kuwa kesi za aina hiyo zinazojumuisha kughushi stika pia zipo 17 tangu Januari hadi Machi.

“Kesi nne zinazohusu waliopenya na kupata leseni ziko mahakamani na 13 ziko Polisi Magomeni katika hatua za upelelezi. Ingawa hawa wameghushi umri na kudanganya kuwa magari yao yaliingia yakiwa na umri wa chini ya miaka 10, tumewashitaki kwa kughushi stika zetu, mengine ni ya askari wenyewe.”

Wakati akisema hivyo, Mkurugenzi wa Barabara wa Mamlaka hiyo, Aron Kisaki alisema hata hivyo Sumatra inajitahidi kutekeleza majukumu hata yasiyoihusu, ili kuhakikisha usalama wa abiria.

“Ni hatari kweli, na matatizo hayo yanatokea kila siku. Trafiki wanatumia macho kukagua wakati matatizo mengine hayaonekani kwa juujuu. Suluhisho hapa ni usafiri wa kampuni na mitambo ya kukagua magari tu, vinginevyo wajanja wa kughushi watachezea akili na uhai wa watu, kwa kujua kuwa hakuna vifaa vya kuwabaini mara moja.

“Hadi sasa daladala zilizosajiliwa ni 6,000 lakini hakuna mwenye uhakika kuwa zote ni salama”.

Akizungumzia sheria inayoelekeza kutoingizwa nchini kwa magari yenye umri wa miaka 10 kwenda juu, Kisaka alisema hata hiyo haikupaswa kuwapo na imekuwapo kutokana na umasikini wa Watanzania.

“Na ikiwapo hiyo, itungwe itakayosema ni kwa muda gani gari lifanye biashara ya kusafirisha abiria, vinginevyo wamiliki wataendelea kuyaacha barabarani magari yao ili yazalishe hata kama yanatoa kutu.

“Ukaguzi wenyewe si wa kutumia vifaa, sasa ilimradi gari linathibitishwa kutembea kwa macho tu, si kila mmiliki atataka lake limletee fedha? Nani atapaki? Mitambo maalumu inahitajika ili kumaliza tatizo kama wafanyavyo Rwanda,” alisema Kisaka.

Baadhi ya askari waliohojiwa, walikiri kutokuwa na vifaa vya kukagua magari wala kipimo cha ulevi wa madereva na kwamba wanatumia uzoefu wa macho kubaini hitilafu za wazi.

Mkuu wa Chuo cha Usafirishaji cha Taifa (NIT), Zacharia Mganilwa aliliambia gazeti hili kuwa tayari mitambo minne imeingizwa nchini kutoka Italia na Afrika Kusini kwa ajili ya ukaguzi wa magari ya aina zote.

“Tatizo lililobaki ni fedha kwa ajili ya ufungaji, kwa sababu kila mmoja unahitaji Sh milioni 200 ili uwekwe katika eneo litakaloruhusu hata malori kuingia na kukaguliwa. Ni mitambo ya kisasa na hakuna gari bovu litakalopenya,” alisema.

“Ilianza kuingia Desemba na sasa tunasubiri sehemu ya mzigo wa mwisho utakaoingia mwezi mmoja kuanzia sasa,” alisema Mganilwa.

Kwa maelezo yake, mitambo hiyo itafungwa Mbeya, Arusha, Dar es Salaam kwenye eneo la chuo hicho na Mwanza.

“Kwa mikoani tunatarajia kuzungumza na TEMESA (Wakala wa Ufundi na Umeme wa Serikali) ili tutumie majengo ya Serikali kuifunga, naamini gharama ya ufungaji itapungua katika maeneo hayo, vinginevyo fedha ni changamoto kubwa kwetu,” alisema Mganilwa.

Alisema wakifanikisha kuifunga, ajali zitakwisha, kwa kuwa magari mabovu yatajiondoa yenyewe barabarani.

“Wakati tukitafuta fedha na kusubiri bajeti ya Serikali kuona kama tutatengewa fedha kwa ajili hiyo, tunafuatilia mchakato ulioanza kuhusu kuanzishwa kwa Mamlaka ya usalama barabarani, itakayoshughulikia ukaguzi huo, ni ama Serikali au watu binafsi watakaohusika na kazi hiyo, lakini si trafiki.”
Alisema, trafiki wanaitwa wakaguzi wa magari kwa mazoea tu, lakini wanachokifanya si ukaguzi na wala hawajasomea ukaguzi wa magari.

“Mitambo ikianza kazi, watabaki kusimamia sheria itakayotungwa kulazimisha watu wapeleke magari yao kukaguliwa na si wao kuyakagua, Mamlaka ndiyo itashughulikia hilo. NIT itatumia mitambo hiyo kufundisha wakaguzi namna ya kuitumia ili kuweka mambo sawa,” alifafanua.
 
Last edited by a moderator:
Lazima ijulikane kuwa pana gharama na tuzikubali hizo gharama ili kunusuru maisha yetu na kuboresha usafiri

1)Kuzuia magari ya zamani mfano yasiozidi miaka 5 maana yake mitaji ya kununulia kupanda x2= nauli kupanda x2
2)Kununua mitambo + watumishi ukaguzi = kuongezeka kwa gharama za uendesheji, nauli maisha kwa ujumla.
3)Ukiongeza kila kigezo cha gharama eidha mtaji,uendeshaji, mlolongo ukaguzi = kupunguwa idadi ya wawekezaji,
kuongezeka tabaka kwa wadau walio nacho na wasionacho, Ukabaila kukomaa, ummaskini kuongezaka kwa wengi.

MWISHO WA SIKU NI KAMPUNI CHACHE SANA NA ZENYE UWEZO HASA KUTOKA NJE YA NCHI
ZITAWEZAKUENDESHA SHUGHULI ZA DALA DALA NA UCHUMI KUMILIKIWA/KUCHUKULIWA NA WAGENI
 
Data ndio tatizo kubwa kwa wabongo, yaani mtu anakuja anasema kafanya utafiti na nusu ya magari, habari yote data ni magari 6,000 tu ndio yamesajiliwa sumatra yaani hii yenyewe sio halisi.

Mtoa hoja numbers please, magari mabovu kuyajua inahitaji billions? sio bora mzitumie kuweka guarantee iliwakope magari mapya.
 
Back
Top Bottom