Njia ya uhakika ya kufuta malaria nchini ni kuharibu mazalia ya mbu

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,318
33,125
Kuna habari njema kwamba vifo vitokanavyo na malaria vimeanza kupungua kwa kiwango kikubwa nchini kutokana na matumizi vyandarua vyenye dawa.
Taarifa za kupungua kwa vifo hivyo ziliwekwa wazi juzi jijini Dar es Salaam wakati wa maadhimisho ya siku ya malaria duniani ambayo kitaifa yalifanyia jijini Dar es Salaam.

Tanzania imekuwa na mikakati mbalimbali ya kupambana na malari, ukiwemo wa kugawa vyandarau vyenye sawa kwa kila familia ili kila mwananchi atumie, hivyo kupunguza vifo vinavyotokana na maambukizi malaria.

Kumekuwa na taarifa kwamba mpango wa kugawa vyandarua kwa kila familia umesaidia kupunguza kwa kiwango kikubwa vifo vya wanawake wajawazito na watoto chini ya miaka mitano.

Wakati kampeni ya kugawa vyandarua ikiendelea, pia serikali iko katika mikakati ya kuzalisha dawa za kuua mazalia ya mbu.

Chini ya mpango wa serikali ya Tanzania na Cuba kiwanda cha kutengeneza dawa hizo kinajengwa Kibaha, Pwani, ili kuhakikisha upatikanaji wa uhakika wa dawa hizo na hivyo kusaidia kuteketeza mazalia ya mbu kote nchini.

Ingawa juhudi kubwa za kitaifa na jamii ya kimataifa katika miaka ya hivi karibuni zimeelekezwa zaidi katika mapambano dhidi ya Ukimwi ugonjwa usiokuwa na chanjo wala tiba, ukweli mmoja unabakia bila kupingwa kwamba malaria bado ni ugongwa unaoongoza duniani kwa kuuwa zaidi hasa katika nchi za ulimwengu wa tatu, Tanzania ikiwamo.

Malaria ni tishio kubwa la uhai wa binadamu, hasa wanawake wajawazito na watoto chini ya miaka mitano; ndiyo maana tunasema kuwa pamoja na taarifa kwamba kuna mafanikio yamefikiwa katika kupambana na malaria kwa watu kutumia vyandarua vyenye dawa hivyo kupunguza vifo vitokanavyo na ugonjwa huo, kazi iliyoko mbelke yetu kama taifa bado ni kubwa.

Tunasema haya kwa sababu pamoja manufaa ya wazi kabisa ya kutumia vyandarua vyenye dawa, sisi tunaamini kuwa njia ya uhakika na ya kudumu ya kukabiliana na janga la malaria ni kupambana na mbu. Upambanaji huu ni lazima uwe wa kuwateketeza.

Tunapozungumza habari ya kuteketeza mbu tunakusudia kuteketeza mazingira ya mazalio ya mbu. Kazi hii ni ngumu, ina gharama kubwa lakini ndiyo ya kweli na uhakika ya kukabiliana na malaria.

Tumesikia kuwa kiwanda kinajengwa Kibaha kwamba serikali kwa kushirikiana na kampuni ya Labiofam ya Cuba, wanajenga kiwanda hicho ili kujenga uwezo wa upatikanaji wa dawa za kuteketeza mazalio ya mbu.

Tunasema bila kuficha hisia zetu kwamba pamoja na faida zinazoweza kupatikana kwa kutumia vyandarua vyenye dawa, na tukithamini sana mafanikio yalioyokwisha kufikiwa kwa kuvitumia hadi sasa, tunaamini kushughulika na mazalia ya mbu ndiyo nji ya kweli na hakika ya kuangamiza malaria nchini.


Bado mazingira ya makazi ya watu wetu ni machafu mno, mazalia ya mbu yametapakaa kila mahali, mijini na vijijini.

Maji machafu yaliyotuama yamezagaa maeneo mbalimbali ya miji yetu, maji machafu ya vyooni yanatiririshwa ovyo kila mahali; usafi wa mazingira ni vitu ambavyo kwa hakika havisumbui sana akili za watu wetu. Ni kama vile watu wamezoea kuishi na uchafu na kuacha mbu wakizaliana katika makazi yao.

Kila tukitafakari hali hii tunapatwa na woga kwamba pamoja na mapambano dhidi ya malaria kugharimu taifa hili mabilioni ya shilingi mwaka baada ya mwaka, tutaendelea kuwa kama watu waliofungwa kwenye mduara wa umasikini kama hatua za kisera, kisheria na kikanuni hazitachukuliwa kukabiliana na hali hii.

Tunasema haya tukikikusudia kwamba wakati serikali ikijitahidi kujenga kiwanda hicho, na wakati umma ukitarajia kuanza kuona dawa hizo zikitumika kunyunyuziwa kwenye mazalia ya mbu, kama jamii haitabadilika na kukubali kuwa wadau wa kweli wa kukabiliana na

mazalia ya mbu hatutaondoa ugonjwa huu miongoni mwetu.

Ni kwa jinsi hii tunashauri kwamba sasa iwe ni lazima kwa mujibu wa sheria kila kaya, kila mkazi wa eneo husika kuhakikisha kuwa hakuna mazingira ya mazalia ya mbu katika eneo lake, serikali za mitaa, kuanzia halmashauri hadi kwenye mitaa kuwe na ufuatiliaji wa hakika, hatua zichukuliwe ili kujenga utamaduni mpya wa ushiriki wa jamii kwa ujumla wake katika vita hii.
Bila kufanya hivi, mwaka baada ya mwaka mabilioni ya shilingi yatatumika, lakini malaria itaendelea kuota mizizi nchini.

CHANZO: NIPASHE
​
300px-Anopheles_stephensi.jpeg







 
  • Thanks
Reactions: BAK
Back
Top Bottom