Pamoja na ukweli kuwa Wazanzibar wana matatizo ya msingi ambayo yameshindwa kupatiwa ufumbuzi kwa muda mrefu, na kwamba baadhi ya matatizo hayo yanatokana na muungano, kuna uwezekano mkubwa wa Zanzibar kushindwa kushikamana iwapo dai lao la kutaka kujitenga na Muungano litaafikiwa. Wanazo tofauti kubwa ndani ya vyama vyao vya siasa na visiwa vyao vya Unguja na Pemba ambazo hazijapatiwa suluhisho la kweli na la kudumu. Ndoa ya Cuf na CCM inaimarishwa na kuwepo kwa Bara inayoonekana kama adui wa pamoja (common enemy) wa pande hizo mbili (Cuf na CCM kwa upande mmoja na Unguja na Pemba kwa upande mwingine.) Nje ya muungano hiki kinachounganisha umoja wao sasa hakitakuwepo. Wananchi wa kawaida wanaweza kudhani mslahi yao yatapewa kipaumbele wakati huo lakini wasikumbuke kuwa hao wanaowasukuma kuelekea Zanzibar huru wana matarajio ya kujinyakulia fursa za kujineemesha binafsi ama na jamaa zao wa karibu fursa ambazo kwa sasa zinaminywa na kuwepo kwa muungano na hivyo wakajikuta wamehadaiwa kama baadhi yao walivyohadaiwa katika mashirikiano ya vyama vya CUF na CCM. Mimi kama mtanzania mpenda amani, ningemshauri Raisi Kikwete kwa kuwa ameonyesha nia ya kurejesha utulivu Zanzibar kwa hatua zake mbalimbali alizozichukua hadi sasa (ikiwa ni pamoja na kuruhusu mjadala wa katiba) aikamilishe nia hiyo kwa kuwapa watanzania fursa ya kuujadili muungano. Hapa tulipofika sasa hatuna uchaguzi ila kuujadili muungano. Tukiendelea na kujifanya hatuoni haja ya kuujadili muungano tutafika hatua mbaya zaidi. Tutatoka kwenye kubaguana kisiasa (angalao hilo ni historia kwa sasa huko Zanzibar) na kuingia kwenye kubaguana kiudini (hili linaendelea kwa kasi kwa sasa) na kuishia kwenye ubara na Uzanzibara (hili lilitabiriwa kutokea na kuna kila dalili za kuwezekana kutokea). Lakini pia tukiruhusu muungano uvunjike katika mazingira haya ya jazba tutashuhudia miungano mingine ya CUF na CCM na Unguja na Pemba ikisambaratika na kulazimika kuwa na kambi za wakimbizi Unguja, Mombasa ama Dar es Salaam. Kwa hekima yako Raisi Kikwete waweza kulinusuru hili lisitokee. Mungu ibariki Tanzania.