"Niwie radhi Mhe..." - Meghji

Mzee Mwanakijiji

Platinum Member
Mar 10, 2006
33,474
39,987
Ni sehemu ya maneno ambayo Balozi Mmoja wa nchi za Magharibi alianza kuyatumia alipotaka kuonesha ni jinsi gani nchi wafadhili zimeanza kuwa na shaka na uwajibikaji wa serikali ya awamu ya nne. Katika ripoti ambayo KLH News imeipata kutoka ndani ya kikao hicho kilichofanyika leo.. Balozi huyo aliamua kumtolea uvivu Waziri Meghji (aliyekuwa hapo pia)... Taarifa zaidi ... bado inasubiriwa..
 
Membe hakuwepo? maana aliwaambia wasiingilie mambo ya ndani ya nchi ili hali akijua wao ndio watoa fwedha
 
ukizingatia amekuwa muoga wa safari,afta salome kututoka..mama meghji anaweza ugua,hicho kikao kilikuwa wapi?
 
Jamani JF hapa mnaonjeshwa tu... mambo yote kuanzia kesho.. na Jumatano hadi Mkutano Mkuu wa CCM unapoanza ndipo kule kumkoma nyani giledi.. kutatimilika.... na siku mkutano wa CCM utakapoishi wiki ile itakuwa ni funga kazi kwani wapinzani watapewa Ultimatum...
 
Balozi wa Uingereza nchini, Philip Parham, mbele ya Meghji, Katibu Mkuu wake Gray Mgonja, katika kikao maalumu kwa ajili ya kutoa taarifa ya wafadhili katika mjadala wa utekelezaji wa bajeti ya serikali ya mwaka 2006/07, katika mkutano ulioshirikisha wadau mbalimbali wa maendeleo na watendaji wa serikali. alisema maneno yafuatayo:

Success is far from assured. I hope you will forgive me, Honourable Minister (Meghji), if am candid about our perception. We want to provide the extra support which is vital for Tanzania at this critical juncture. But it is a simple political fact that higher levels of financing from development partners require higher levels of perfomance from the government.

Today's environment is significantly more challenging than last year's. Development partners feel less confident about Tanzania today than in 2006"

Katika mkutano huo, tunaambiwa Joseph Butiku, alikuwamo!!!!!
 
Kazi ipo.
shukrani Halisi kwa kumega angalau hako ka quote. wapo watu wangesema huo ni udaku.
 
Wahisani waja juu

*Wasema wameanza kupunguza imani kwa Tanzania
*Hata hivyo waridhishwa na vipaumbele vya Kikwete
*Katibu Mkuu Kilimo, Chakula ashtushwa na masharti


Na Mwandishi Wetu

BALOZI wa Uingereza nchini, Bw. Philip Parham, ambaye ni Mwenyekiti wa Washiriki 14 wa Mpango wa Uchangiaji wa Bajeti (GBS) amesema washiriki hao wamepunguza imani kwa Tanzania mwaka huu, kuliko ilivyokuwa mwaka jana.

Akizungumza Dar es Salaam jana, katika siku ya kwanza ya mkutano wa mwaka wa wadau wa maendeleo wa siku tano wenye lengo la kutathimini mapato na matumizi ya Serikali kwa mwaka huu, Balozi huyo alisema kupungua kwa imani kumesababishwa na wasiwasi walionao wahisani, kwenye mambo makuu mawili.

Jambo la kwanza ni kuwapo kwa hali inayojitokeza ndani ya jamii kuitaka Serikali kuonesha ongezeko la mapato yake linavyoboresha mahitaji ya msingi kwenye maisha ya maskini na kuonesha wazi wazi kuwa inafanya hivyo.

La pili ni Serikali kutakiwa kuimarisha uwajibikaji wake kwa wadau, ikiwa ni pamoja na kuonesha kwa vitendo kuwa inapiga vita rushwa.

Balozi Parham alisema wasiwasi huo umekuwa ukizungumzwa na maofisa wa Serikali, asasi za jamii, wanataaluma na wananchi kwa ujumla.

Alisema mambo hayo yanayowapa wasiwasi yanatoa changamoto na fursa kwa wahisani, Serikali na wadau wengine wa maendeleo, na kuongeza kwamba ameridhishwa kuona kuwa mambo hayo yenye wasiwasi yapo kwenye maeneo makuu matano ya maendeleo yaliyo kwenye makubaliano kati ya Serikali na washirika wa maendeleo.

Aidha, Balozi huyo alisema kama mambo hayo hayatatolewa maelezo ya kina, yanaweza kuathiri utendaji wa misaada inayotolewa moja kwa moja kwenye bajeti ya Serikali na utoaji mzima wa misaada katika kipindi cha muda wa kati.

Hata hivyo, Balozi Parham alisema ushirikiano mzuri kati ya Serikali na Washirika wa Maendeleo katika kipindi cha miaka kumi iliyopita, unampa imani kuwa katika kipindi cha siku nne zilizobaki watafikia hatua nzuri itakayoonekana.

Kuhusu kuwapo kwa matokeo ya utekelezaji wa sera za Serikali, Balozi huyo alisema hatua za maendeleo zilizopigwa na Tanzania, zimesababisha kuongezeka matarajio kutoka kwa jamii kwenda kwa Serikali yao na hivyo kuongezeka kwa changamoto kutoka kwa vyama vya siasa vya Upinzani, vyombo vya habari na asasi za jamii.

Alisema hata hivyo, Tanzania ina upungufu kwenye mfumo wa utoaji taarifa zilizofanyiwa utafiti wa kina kuhusu matokeo ya maendeleo yaliyofikiwa. Kwa mujibu wa Balozi Parham, taarifa hizo zinapaswa kuonesha jinsi fedha zilizoingia kwenye mfumo wa Bajeti zinavyotoka katika mfumo wa miundombinu, huduma bora na fursa mpya kwa watu maskini.

Alisema Tanzania inatakiwa kutoa taarifa za kutosha kuhusu matumizi ya fedha za bajeti na matokeo yake, kwenye maendeleo ili iendeleze sera nzuri na kutumia fursa adimu kwa ufanisi.

Balozi huyo alisema takwimu sahihi za matokeo ya matumizi ya fedha za bajeti, pia zinahitajika kulinda imani ya washiriki wa maendeleo na kutawala matarajio ya jamii ya ndani ya nchi na ya kimataifa.

Kuhusu vita dhidi ya rushwa, Balozi alisema wamevutiwa kuona vita hiyo ni moja ya vipaumbele muhimu vya Rais Jakaya Kikwete na kuongeza kuwa uongozi wake kwenye vita hiyo ni muhimu kwa maslahi ya Taifa na kwa maskini ambao mara zote wanakuwa wahanga wa vitendo vya rushwa.

Alibainisha, kwamba nchi washirika katika maendeleo wanasubiri kwa hamu ripoti ya ukaguzi wa mahesabu ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT), hasa katika akaunti ya deni la nje ya nchi na jinsi Serikali itakavyochukua hatua.

Alieleza kuwa jinsi wanavyoisubiri Ripoti ya BoT ndivyo wanavyosubiri matokeo ya uchunguzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na kuongeza kuwa wanaelewa uzito wa kazi waliyonayo TAKUKURU na kwamba wakiombwa msaada, watakuwa tayari kusaidia.

Kutokana na hali ilivyo sasa, Balozi huyo alisema wamefurahi kutengeneza na kuwasilisha masharti ya wahisani kwa Wizara ya Fedha mwezi uliopita, na kuongeza kuwa masharti hayo yana lengo la kuepuka taarifa za mshituko na kuhakikisha uamuzi unafanyika kwa kufuata majadiliano ya ndani kati ya Serikali na wahisani.

Alisema washiriki wa maendeleo watatumia matokeo ya mkutano huo wa siku tano wakati wanafanya uamuzi juu ya msaada wao kwenye bajeti ya mwaka 2008/9.

Naye kiongozi mwingine wa wahisani wanaotoa misaada nchini, Bw. David Stanton, alisema shinikizo kwa Serikali kutakiwa kuonesha matokeo ya maisha bora kwa wananchi ni kubwa sana wakati huu, kuliko wakati mwingine wowote.

Bw. Stanton alisema wakati vyombo vya habari, Bunge na asasi nyingine zinazotumia fursa ya kidemokrasia zinatoa changamoto kwa Serikali kuonesha matokeo, wahisani nao wanapata ujumbe wa aina hiyo hiyo, kutoka kwa walipa kodi na mawaziri katika nchi walizotoka.

Matamko hayo yalisababisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Bw. Gray Mgonja, ambaye ni Mwenyekiti wa mkutano huo unaoendeshwa kwa mfumo wa kujadili mada, kuomba taarifa ya maandishi ya Balozi Parham.

Akichangia hoja hiyo, Bw. Mgonja alisema kutoonekana kwa maendeleo kunatokana na vipaumbele vinavyotumiwa na mzungumzaji na kutolea mfano wa hatua za maendeleo zinazoonekana kwenye uwezo wa nchi kujitegemea kwa chakula, upatikanaji wa maji na mawasiliano kati ya vijijini na mijini.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa Kilimo na Chakula, Bw. Peniel Lyimo, alisema ameshtushwa na kitendo cha wahisani kutoa masharti, kwa kuwa kinarudisha nyuma hatua iliyopigwa katika uhusiano kati ya Tanzania na nchi wahisani kwenye utoaji misaada.

Alisema kuwapo masharti kunaondoa dhana ya ushirikiano na kuongeza kuwa kunarudisha nyuma juhudi zilizofanyika na kuwataka kujadili ufanisi na uhakika badala ya kurudisha masharti yaliyokataliwa karibu miaka kumi iliyopita.

Washiriki hao wa maendeleo ni Benki ya Maendeleo Afrika (ADB), Kanada, Denmaki, Umoja wa Ulaya (EU), Ufini, Ujerumani, Ayalandi, Japani, Norwei, Uholanzi, Uswidi, Uswisi, Uingereza na Benki ya Dunia.

GBS ni mojawapo ya njia zinazotumiwa na washiriki wa maendeleo kuisaidia Tanzania ambapo chini ya mpango huo, fedha zinazotolewa na washiriki wa maendeleo zinaingia moja kwa moja katika bajeti ya Serikali.

Serikali nayo hutumia fedha hizo katika utekelezaji wa Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini Tanzania (MKUKUTA).

Mwaka huu, habari zinasema washiriki hao wanatarajia kutoa sh. bilioni 881.3 zikiwa ni mchango wao chini ya GBS ambayo ni asilimia 38 ya jumla ya misaada inayotolewa kwa Tanzania.

Hivi karibuni, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bw. Bernard Membe, aliwajia juu mabalozi wa kigeni nchini, ambao wamekuwa wakizungumza na vyombo vya habari kuisema Serikali na kukiuka Azimio la Vienna.

Aliwataka mabalozi kuwasiliana na ofisi yake kwani ndiko kutimiza azimio hilo na si vinginevyo.

Source: Majira
 
Kazi ipo.
shukrani Halisi kwa kumega angalau hako ka quote. wapo watu wangesema huo ni udaku.

Saharavoice, hapa hakuna cha udaku, wao wacha walete maroroso yao kupoteza mwelekeo lakini moto umeshawaka na umeshika kasi... Hivyo ni vipande tu... Mambo ya ndani ni mazito zaidi na ndio maana hata wao kwa wao mambo si shwari kabisaaaa, wanashikama mashati
 
Success is far from assured. I hope you will forgive me, Honourable Minister (Meghji), if am candid about our perception. We want to provide the extra support which is vital for Tanzania at this critical juncture. But it is a simple political fact that higher levels of financing from development partners require higher levels of perfomance from the government.

Today's environment is significantly more challenging than last year's. Development partners feel less confident about Tanzania


Mambo ni kuwekwa hadaharani tu!
 
Sasa hapo Mh waziri nani alimfuta aibu hiyo, maana nijuavyo kwa muingereza kufikia kukwambia live namna hiyo ujue mambo yamefika pabaya!
 
Wahisani watoa onyo

na Irene Mark
Tanzania Daima

KWA mara ya kwanza katika miaka ya hivi karibuni, nchi wafadhili zimetangaza rasmi kwamba imani waliyokuwa nayo kwa Serikali ya Rais Jakaya Kikwete kwa mwaka huu wa fedha imepungua kuliko ilivyokuwa mwaka jana.
Kutokana na hali hiyo basi, wahisani wanaotokana na kundi la nchi 14 zinazotoa misaada katika bajeti, wameitaka serikali kuchukua hatua za haraka kurejesha imani hiyo ambayo kuporomoka kwake kunachangiwa pamoja na mambo mengine, wasiwasi walionao katika matumizi ya fedha za misaada na mikopo wanayotoa kwa Tanzania.

Tamko hilo la kwanza na la aina yake, lilitolewa jana Dar es Salaam na Balozi wa Uingereza nchini, Philip Parham, wakati akitoa taarifa ya wafadhili walipokuwa wakijadili utekelezaji wa bajeti ya serikali ya mwaka 2006/07, katika mkutano ulioshirikisha wadau mbalimbali wa maendeleo.

Akizungumza mbele ya Waziri wa Fedha, Zakia Meghji, balozi huyo ambaye nchi yake imepewa heshima ya kuwa mwenyekiti wa mataifa hayo 14 wahisani, alibainisha kuwa serikali inapaswa kuhakikisha kuwa misaada inayotolewa na wao inasaidia kuimarisha maisha duni ya watu maskini.

Kwa kuonyesha uzito wa kauli hiyo nzito dhidi ya serikali ambayo kwa miaka mingi sasa imekuwa kipenzi cha nchi wahisani, balozi huyo kabla ya kusema maneno hayo alianza kwanza kumwomba radhi Waziri Meghji kwa atakayoyasema, akisema ameamua kuwa muwazi kwa kueleza kile wafadhili wanachokiona.

"Mafanikio bado yapo mbali. Ninaamini Mheshimiwa Waziri (Meghji) atanisamehe iwapo ninataka kuwa mkweli kuhusu mtazamo wa wahisani…Mazingira ya leo yanatoa changamoto zaidi kuliko ilivyokuwa mwaka uliopita. Leo imani waliyokuwa nayo wahisani wa maendeleo imepungua kuliko ilivyokuwa mwaka 2006," alisema balozi huyo.

Kutokana na hali hiyo, Balozi Parham akionekana kuwasemea wahisani wenzake wengine ambao katika bajeti ya mwaka huu walichangia kiasi cha dola za Marekani milioni 673, sawa na asilimia 15 ya bajeti nzima, aliitaka serikali kuimarisha uwajibikaji kwa wadau wake, kikubwa akikitaja kuwa ni kukabiliana na ufisadi.

Alisema washirika wa maendeleo wanataka kuongeza misaada kwa Tanzania hasa katika kipindi hiki kigumu ambacho misaada zaidi inahitajika.

Hata hivyo, alibainisha kuwa viwango vya juu vya ufadhili kwa upande mmoja, kwa upande mwingine vinahitaji utendaji makini kutoka serikalini.

Kuhusu washirika wa maendeleo, balozi huyo alibainisha kuwa wanapokea mwangwi wa hali halisi ya Tanzania kutoka kwa maofisa wa serikali, asasi za kiraia, wasomi na wananchi kwa ujumla katika mambo mawili makubwa.

Balozi Parham aliyataja mambo hayo kuwa ni uhitaji wa serikali kutafsiri bajeti na kuifanya ionyeshe maendeleo halisi na kuinua hali ya wananchi maskini.

"Lakini ni jambo la wazi kwamba kisiasa, viwango vya juu vya ufadhili kutoka washirika wa maendeleo vinahitaji viwango vya juu vya uwajibikaji serikalini.

"Hofu kubwa ya washirika wa maendeleo, kama ambavyo inaonyeshwa pia na maofisa wa serikali, vikundi vya kijamii, wasomi na wananchi kwa ujumla inahusu masuala hayo mawili," alisema.

Alisema hali inajionyesha kuwa ili kushinda vita dhidi ya rushwa, serikali ya Rais Kikwete imelifanya hilo kuwa kipaumbele, jambo lililogeuka kuwa mjadala wa kitaifa ambao waathirika wakuu ni wananchi maskini.

Aidha, Balozi Parham alimtaka Waziri Meghji kusema ukweli kuhusu tuhuma nyingi za rushwa kwa washirika wa maendeleo, wawekezaji muhimu na Watanzania wote kwa ajili ya kurudisha imani ya serikali.

Akizungumzia haja ya matokeo kuonekana, balozi huyo alisema serikali inapofanikiwa kutimiza matarajio yake, imani ndivyo inavyoongezeka na akasema hali hiyo ndiyo huifanya serikali kukabili changamoto kutoka kwa wapinzani wake wa kisiasa, vyombo vya habari na asasi nyingine za kijamii.

Katika hilo alisema kama kuna eneo ambalo Tanzania imeshindwa basi ni lile la kuwa na mifumo inayoweza kuonyesha bayana kwamba fedha zinazotolewa na wahisani katika bajeti zinazaa matunda ya wazi kwenye maeneo kama yale ya kuimarika kwa miundombinu, huduma za kijamii na kuongezeka kwa fursa za kimaisha kwa watu maskini.

Akitoa mfano, alisema ingawa katika miaka ya hivi karibuni, kumekuwa na ongezeko kubwa la maendeleo ya elimu ya sekondari kwa shule, nyingi zaidi kujengwa, madarasa kuongezeka na kuimarika kwa hosteli, bado kumekuwa na ufinyu wa taarifa zinazoeleza uwiano uliopo kati ya idadi ya wanafunzi na ya walimu wanaowafundisha.

Hali hii alisema imesababisha kutokuwapo kwa taarifa za kutosha kuhusu idadi ya walimu waliohitimu sawasawa, mahitaji halisi ya walimu hao na vifaa vingine vya kufundishia.

Kama hiyo haitoshi, alisema kwa upande wa elimu ya msingi, hali ni hiyo hiyo kwamba, wakati takwimu zikionyesha kuwa idadi ya watu wanaojiunga na elimu hiyo imefikia asilimia 97, kiwango ambacho ni cha juu kabisa, takwimu za idadi ya watu na zile za kiafya zinaonyesha kupungua kwa idadi ya wanafunzi wanaoandikishwa kuanza elimu ya msingi.

Kutokana na ukinzani huo wa takwimu, balozi huyo aliitaka serikali kuchukua hatua ya kuchunguza kasoro hizo, ikiwa ni pamoja na kuainisha mikakati ya kulinda mafanikio yaliyofikiwa na kubainisha kwa uhakika kabisa kiwango cha mafanikio katika elimu ya msingi.

Akizungumzia rushwa, Balozi Parham alisema ni muhimu kwa serikali kuonyesha kuwa ipo hai kwa kuchunguza tuhuma zinazoelekezwa kwake na kupeleleza vilipo vielelezo vya tuhuma hizo.

"Tunasubiri kwa shauku taarifa ya mkaguzi wa Benki Kuu (BoT), madeni ya nje na majibu ya serikali kuhusu suala hili. Pia tunangoja matokeo ya uchunguzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU)," alisema balozi huyo.

Akihitimisha kusoma risala yake, balozi huyo alisema wamepata taarifa ya Wizara ya Fedha kwa mwezi uliopita inayoeleza masharti ya wafadhili.

Hata hivyo, katika kile kilichoonekana kama kujibu mapigo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Peniel Lyimo, alisema kuwa masharti ya wafadhili yanakwamisha maendeleo ya serikali, hali inayosababisha wafadhili kuiendesha nchi.

"Hawa mabwana wana masharti magumu sana, ndiyo maana tunashindwa kuyafikia maendeleo… hii inasababisha nchi yetu kuendeshwa na wafadhili badala ya kujiendesha wenyewe," alisema Lyimo ambaye ana uzoefu na shughuli za wafadhili, kwani amewahi kuwa Katibu Mkuu katika Wizara ya Fedha kwa muda mrefu.

Baadhi ya wadau waliohudhuria mkutano huo ni mabalozi, maofisa na watendaji wa serikali, watu mashuhuri, wanasiasa na wasomi mbalimbali.
 
I like it... I like it.....

Hoja hujibiwa kwa hoja. Ninategemea this time Muungwana ata-come up na majibu halisi, na sio generalized answer kwamba hizi ni kelele za wapinzani. Je, mabalozi nao ni wapinzani? Anadhani wadanganyika wa leo ni sawasawa na wale wa mwaka 47....

C'mon politicians... Kuweni wakweli na mumwogope Mungu... Jibuni hoja kwa kutoa hoja, na si vinginevyo...
 
Wahisani watoa onyo
Hata hivyo, katika kile kilichoonekana kama kujibu mapigo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika, Peniel Lyimo, alisema kuwa masharti ya wafadhili yanakwamisha maendeleo ya serikali, hali inayosababisha wafadhili kuiendesha nchi.

"Hawa mabwana wana masharti magumu sana, ndiyo maana tunashindwa kuyafikia maendeleo… hii inasababisha nchi yetu kuendeshwa na wafadhili badala ya kujiendesha wenyewe," alisema Lyimo ambaye ana uzoefu na shughuli za wafadhili, kwani amewahi kuwa Katibu Mkuu katika Wizara ya Fedha kwa muda mrefu.

aahahha sijawahi kucheka kama leo. in fact kama wahisani wanatoa 40 per cent ya bajeti, then ilibidi hata baraza la mawaziri wachague 40 per cent.

in short wanahisa kwenye nchi yetu 40 percent. u don't like that, jitegemee kwenye bajeti. simple
 
Back
Top Bottom