Ninakubali mkuu lakini nikisoma Historia na ya kutafuta mwenyewe ni kwamba wakuja hao waliweza tu kuchungulia fursa maana toka Sykes alipoletwa Dar toka Pangani na Effendi Plantan walijiunga kwenye kundi la Wakuja ambalo lilikuwa linajikomba kwa Wahindi.Mtchoro,
Ndiyo faida ya kuandika.
Umepata na wewe nafasi ya kuchangia histori ya nchi yetu.
Hebu soma hii hapo chini:
GEREZANI FAMILY DAY
Ahsanteni sana Wanagerezani kwa siku nzuri ya hii Jumapili khasa kwa ile biriani ya kumwaga.
Allah atuzidishie mapenzi na mshikamano.
Leo kwa mara yangu ya kwanza nimehudhuria Gerezani Day.
Kwa hakika ni siku ya kupendeza sana ingawa kwa namna fulani kuna majonzi kidogo yanakuja pale unapowafikiria wale ambao ulikuwanao udogoni mkicheza mpira Kidongo Chekundu na wao wametangulia mbele ya haki.
Kidongo Chekundu leo haipo lakini pamejengwa viwanja vya michezo.
Kwangu mimi ni mara yangu ya kwanza kuhudhuria siku hii na In Shaa Allah naomba iwe narejea na kurejea kila mwaka hadi mwish wa umri wangu.
Laiti kama si kwa kuwa nipo katika Group hakuna ambae angenijua kwa sura ila watu wachache sana pengine wasiozidi hata watano.
Kutoka mwaka wa 1952 nilipozaliwa mimi Mtaa wa Kipata hadi leo miaka mingi imepita.
Kuna baadhi ya watu umri wangu na wengine chini kidogo nimeweza kuwatambua kwa sura zao kuwa zinakuja akilini lakini majina hayaji.
Ngoja nikuchukueni safari yangu ya Gerezani ilivyokuwa na nataka In Shaa Allah niifungamanishe na Dar es Salaam ile ya 1950/60 ambayo naamini wanagerezani wachache sana wanaijua kwani leo pale wengi niliowaona ni vijana sana.
Huenda wengine mimi nimecheza na baba zao.
Nimetokea nyumbani kwangu Magomeni Mapipa nyumba ya kwanza ambayo ina kumbukumbu kubwa kwangu ni pale nilipopinda kona kulia kuingia Mtaa wa Kipata (Sasa Mtaa wa Sykes).
Nimeacha kuitaja ofisi ya CCM ambayo pale ilikuwa ofisi ya African Association iliyojengwa kwa kujitolea kila siku ya Jumapili kuanzia mwaka wa 1929 – 1933.
Nyumba ya kwanza yenye kumbukumbu kubwa kwangu iko mkono wa pili yaweza kuwa ni nyumba ya tatu hivi kutoka Lumumba Avenue na Mtaa wa Sykes.
Leo hapo kuna kituo cha kuuza petroli.
Hii ilikuwa nyumba ya Liwali Abdallah Simba wa Songea ambae nyumba yake nyingine ilikuwa Mtaa wa Somali (Sasa Omari Londo).
Babu yangu aliishi nyumba hii miaka wa ya 1920 ingawa yeye alikuwa na nyumba yake Mtaa wa Mbaruku na Congo jirani na nyumba ya Aziz Ali.
Nyumba hiyo ndipo alipokulia baba yangu.
Umuhimu wa nyumba hii ni kuwa baba yangu kayaona yote ya harakati za uhuru akiwa pale na kanieleza mengi.
Mkabala na nyumba hii ni nyumba ya Kleist Sykes ambae katika video aliyotengeneza Mohamed Ghassani kampa jina, ‘’Mbuyu wa Mzizima.’’
Video hiyo nimekuwekeeni hapa kwenye Group toka jana usiku.
Mtakumbuka kuwa mliponikaribisha kuzungumza nilikuelezeni kuwa harakati za kuiokomboa Tanganyika kutoka ukoloni wa Waingereza zilianza nyumba hii.
Kleist alikuwa katibu muasisi wa African Association na aliishi nyumba hii na wanae wote walizaliwa hapo.
Ndani ya nyumba hiyo wakati wa TAA Ally Sykes mwaka wa 1953 alificha mashine ya kudurufu ambayo ndiyo aliyokuwa akichapa makaratasi ambayo Waingereza waliita ya ‘’uchochezi,’’ akawa anayatawanya kwa wananchi wajiunge na TAA ili TANU itakapokuja kuundwa mwaka wa 1954 iwe na wanachama wa kutosha.
Historia ya Ally Sykes sote tunaijua.
Katika nyumba hii ndipo siku chache baada ya kuundwa kwa TANU Ally Sykes na kaka yake Abdul walikaa mchana mmoja kumsubiri Mwalimu Nyerere aje kuwapa habari za usajili wa chama cha TANU.
Alipofika pale Nyerere aliwapa habari mbaya kuwa TANU imekataliwa usajili.
Nyumba ile haipo na badala yake kuna gorofa ndefu.
Jengo hili hili linahitaji kuwekewa kumbukumbu.
Nimeswali Msikiti wa Kipata na ukanikumbusha ule msikiti mdogo wa zamani.
Mkabala wa nyumba hii NO. 18 alikuwa akiishi mama yangu Mkubwa Bi. Mwanaisha Bint Mohamed ambako Nakioze alikuwa na genge lake akiuza mboga na matunda.
Hili jina "Naikioze," alipewa kwa kuwa wateja wake walikuwa wakilalamika kwa ughali wa bei za vitu vyake yeye akiwaambia, ‘’Acha usinunue nakioze.’’
Nyumba hii ilikuwa ya Bi. Mkubwa mmoja akiitwa Bint Salum.
Nakumbuka mwaka wa 1956 wakati Princess Margaret alipokuja Tanganyika.
Siku ile nilikuwa hapa kwa mama yangu mkubwa na kwa kuwa mtaa wa nyuma ni Mtaa wa Kitchwelle alikokuwa anapitishwa akitokea uwanja wa ndege nakumbuka sana kuwa mimi nilisimama mbele ya duka la Toti pamoja na umma mkubwa wa watu na wanafunzi wa shule kumpungia Princes Margaret tukiwa tumeshika, ‘’Union Jack,’’ bendera ya Uingereza.
Naingia Mtaa wa Sikukuu nakata kushoto kutokea Mtaa wa Sykes kulia kwenye kona ndipo ilipokuwapo nyumba ya Mzee Clement Mohamed Mtamila mmoja wa viongozi wa African Association aliyekuwa katika ya TAA na baadae Mwenyekiti wa TANU 1955.
Siku zile TANU ilikuwa na Rais na Mwenyekiti ambae alifanya kazi zaidi kama mwenyekiti wa Halmashauri ya TANU.
Mwalimu Nyerere alipoandikiwa barua ya achague mawili siasa au ualimu, barua ile ilijadiliwa kwenye kikao kwenye nyumba hii na mmoja wa wajumbe alikuwa Bi. Tatu bint Mzee ambae alikuwa anaishi Gerezani Mtaa wa Kirk Street sasa Mtaa wa Lindi.
Jengo hili linastahili kuwekea kumbukumbu.
Nimepita Mtaa wa Lindi kwenye kona kulikuwa na kinyozi Muingereza na pale palikuwa barza kubwa ya wana TANU wakikaa kuzungumza.
Hii ni sehemu muhimu ya kuwekewa kumbukumbu na hivi sasa kuna ujenzi pale wa kujenga ofisi ya CCM.
Ukiwa hapo nyumba ya Bi. Mruguru bint Mussa mama yake Abdul Syks unaiona ile pale na watu wengi wa Gerezani wanakumbuka kumuona Nyerere akipita pale kwa Muingereza kaongozana na Abdul Sykes wanakwenda kumsalimia Bi. Mruguru.
Wazalendo hawa wawili mara nyingine walikuwa wanasiamama hapo kutupiana maneno na wana TANU wenzao na ilipoanza Congress watatupiana makombora na wafuasi wa Zuberi Mtemvu aliyekuwa President wa Congress, kisha hao watapita.
Mtemvu alikuwa akiishi Mtaa wa Somali ambao sasa ni Mtaa wa Omari Londo.
Gereza ni ina kumbukumbu nyingi na ni muhimu sana kumbukumbu hizi zihifadhiwe kwa kizazi kijacho vinginevyo historia ya Gerezani yote itapotea.
Tofauti na wenzao kama Kilwa Association au lile kundi la Wasukuma na Wanyamwezi ambao walikuwa wanataka haki ya weusi.