Nimesikitishwa sana! Kumbe mama mkwe kaweka CCTV camera kwenye nyumba aliyotupa

Robert Heriel Mtibeli

JF-Expert Member
Mar 24, 2018
21,339
51,881
NIMESIKITISHWA SANA; KUMBE MAMA MKWE ALIWEKA CCTV CAMERA KWENYE NYUMBA ALIYOTUPA.

Anaandika, Robert Heriel.

Niweke wapi USO wangu!
Mambo yote hadharani!
Tupu zangu zipo ukweni,
Wanazitazama tadhani Filamu ya ngono,
Wanayatazama maungo yangu, afadhali yangekuwa maungo ya nje lakini mpaka Uchi wangu wanautazama, uchi wangu! Jamani uchi wangu! Siri zangu zote Nani asiyezijua? Nauliza, huko ukweni Nani asiyejua tupu yangu?

Masikini Taikon wa Fasihi, hii ndio dunia, walisema ni hadaa! Wengine wakasema Tambara bovu! Naye kezilahabi alisema Dunia uwanja wa Fujo! Mmmmh! Haya nawe Taikon utasema dunia ni nini?
Kwa kweli Mimi Taikon siwezi sema lolote Kwa wahenga walishamaliza yote.

Siku jua lilipotoka Magharibi likachwea Mashariki, ukweni waliniona sina jipya chini ya jua. Walitaka nimuoe Binti Yao, hata Kama nilikuwa fukara wa Mali lakini waliridhika na Utajiri wangu wa tabia na maadili yaliyotukuka ya Kiafrika, wakaona ni Bora wanipe Mimi binti Yao, wakanipa.

Mahari nikatoa, haikuwa mahari kubwa lakini ilikuwa ya thamani na ambayo ni zaidi ya Fedha na dhahabu. Wakaniambia watanipa sharti moja, nalo nikiwaahidi kulitimiza hiyo ndio ingekuwa mahari YANGU. Nikawasikiliza; wakasema watanipa binti Yao kwa sharti moja tuu,nalo ni kutochepuka na kutomuacha siku zangu zote za maisha yangu ningali naishi Duniani.

Kwa kweli lilikuwa sharti kubwa mno Kama Wanaume mjuavyo. Lakini nikajiapiza kulitekeleza kwani ni kweli nilimpenda binti Yao Kwa dhati yote. Lakini Hilo la kutochepuka Kwa kweli sikuwa na uhakika nalo.

Basi tukaanza kuishi, Raha zilitujia kabla ya karaha kutulaki Kwa mbele. Kumbe wakati Raha ikitokea nyuma karaha hukujia Kwa mbele.

Moyo wa mwanamke ni Kama Bua la mhindi, ukiuangua huwaka Sana lakini huwahi kuzima upesi. Tena hauna uvumilivu hata kidogo, moyo wa mwanamke ni Kama riadha ya mbio fupi na katu hauziwezi mbio ndefu.
Atakupenda Leo lakini sio miaka yote.
Atakuvumilia siku tatu lakini sio siku Saba.
Atakupa dakika moja lakini Katu hayatafika masaa. Lazima akuchoke, akudharau na kukudhihaki.

Tena nikajua yakuwa mwanamke ni mbinafsi, hupenda kujaliwa kuliko kujali. Hupenda kupewa kuliko kutoa. Hupokea, huchukua huku akikataa kurudisha.

Akitoa hutoa Kwa masimango moyoni ikiwa atakuheshimu Kwa siku tatu, lakini siku ya Saba atakusimanga.

Tukapanga nyumba, ilikuwa nyumba ndogo isiyo ya hadhi. Mke wangu hakuipenda, alitabasamu Kwa kujilazimisha kunifariji Kwa siku moja lakin siku ya Saba yakamshinda akaanza maneno ya ubaya, hakutaka tuzungumze Kwa ukaribu isipokuwa Kwa sauti tadhani alikuwa akizungumza na mtu aliyeumbali wa kilometa.

Basi Mama yake,ndiye Mama Mkwe wangu akatuita siku ya siku ya kuzaliwa ya binti yake, akatuzawadia nyumba. Hakika tulifurahi Sana na kumshukuru kwani tulijua ule ugomvi unaotokana na kuishi kwenye makazi mabovu ungeisha baina yangu na Mke wangu.

Ilikuwa nyumba nzuri ya kisasa, Kama ungependa ungeifananisha na KASRI kubwa la kifalme, ndio ni Kama kasri ambalo lilisheheni kila Aina ya fahari ndani yake. Sitaki kuelezea Bustani zake nzuri zenye maua mazuri yaliyovutia sio macho tuu ya mwanadamu Bali mpaka vipepeo wazuri wapole wakuvutia, sitaki kuelezea Bwawa la kuogelea lililokuwa ndani yake, labda ungeniuliza samani zilizondani yake, hakika Mama Mkwe alituweza, samani zake zilitosha kuelezea mamilioni ya pesa yaliyoteketea. Mdomo wako ungebaki wazi hakika.

Basi tukaishi penzi letu likiwa limechipua upya tadhani majani kipindi cha masika baada ya ukame.

Tulifanikiwa kupata watoto wawili kabla Jinamizi Baya kuivamia nyumba yangu. Sitaki kusimulia mambo haya. Yananitoa machozi, yananiumiza moyo wangu. Lakini Acha niseme tuu huenda moyo wangu utaachia!

Maneno maneno yakazuka Kama mzuka. Yakavuma vuuvuuu! Kama vuvuzela nisiweze hata kulala. Ikawa hekaheka kivumbi na jasho; kelele na mipasho.

Nilikaa chini Kama jini licha ya kuwa yalikuwepo masofa, nikalala sakafuni Kama mzimu wa mwituni.

Mke wangu akaanza kunigeuka, kunidhihaki, kuniteta sio Faraghani tuu Bali mpaka hadharani. Hiyo ndio demokrasia aliyoiita usasa na haki sawa.

Sikuwa na maamuzi kwani ni mpaka Bunge likae, Spika ningekuwa Mimi lakini Rais angekuwa Nani Kama sio Mama Mkwe aliyenipa nyumba niishi na binti yake.

Uanaume wangu uligeuka urembo tuu ndani ya Ile nyumba.
Awali ilikuwa nyumba nzuri ya kifahari lakini kitambo kidogo iligeuka kaburi lililopambwa vizuri na kupakwa chokaa Kwa ustadi lakini ndani yake ililala mifupa yangu na mwili wangu uliooza huku mke wangu akigeuka mlinzi wa Hilo kaburi.

Hiyo ingevumilika, lakini siku moja Mama Mkwe alikuja kunikemea baada ya kujaribu kumtia adabu binti yake baada ya kuwachapa watoto yeye akaingilia na kujitolea maneno ya hovyo.

Nikamwambia mam Mkwe; Je ni dhambi kuwafunza watoto wangu mwenyewe adabu. Na Kama mama Yao atakengeuka naye nikimfunza adabu Mimi kama mume wake ni kosa?

Mama Mkwe akanijibu;
Tangu lini ulikuwa Mume WA Binti yangu?
Ungekuwa Mume ungeishi kwenye nyumba yangu hii?
Ungekuwa Mume ungeshindwa kumlisha binti yangu mpaka nikaamua kumpa Kampuni yangu ili ajipatie kipato akulishe wewe na kukuza kitambo chako hiko?

Unakula tuu alafu hata kazi yenyewe hujui,
Hujui kukata mauno,
Hujui kutwanga kwenye kinu mpaka mahindi yakataka.
Hujui kulifua Dafu likatoa nazi.
Hujui kukanda Unga WA ngano mpaka ukashikamana ukatepeta tepetepe!
Hujui kunyoosha na kukunja vizuri mpaka binti yangu nikamwambia atafute kijana wa kunyoosha na kukunja vizuri.
Unalala Kama upo msalabani badala ya kukunjuka na kujifyatua!
Upoupo tuu!
Unashindwa hata na jogoo! Bora jogoo hukimbiza Kwanza ndipo apande Kwa Mtetea,lakini wewe hatakukimbiza huwezi, bado unataka binti yangu akuheshimu?
Binti yangu anataka akimbizwe haswa,

Nakupa nafasi ya mwisho, usipojirekebisha nitakufukuza kwenye nyumba yangu"

Mama Mkwe alimaliza, nikamuuliza wewe yote hayo umeyajulia wapi?

Akanijibu, nyumba ya Mkwe haikosi Kamera. Kila kinachofanyika mle ndani anakiona na kukisikia kwani ameseti Kamera na mitambo ya kurekodi kinachoendelea.

Basi nawasihi Vijana wadogo ambao hamjaoa. Nyumba ya mkweo ukipewa ukae ukijua inakamera na vinasa sauti.
Aibu zako zote zitaonwa na kurekodiwa.

Tena usiikimbilie Mali ya ukweni au ya Mkeo Kwa maana hiyo hiyo ndio itakayokuhangaisha hapo baadaye.

Basi ndivyo ilivyokuwa,
Mimi Taikon Kwa sasa aibu zangu zote wakwe zangu wameziona,
Utupu wangu,
Kama ni ugoigoi wote hadharani. Loooh!

Acha nipumzike sasa!

Robert Heriel
Taikon wa Fasihi
Kwa sasa Dar es salaam
 
Ila sasa kamera zingine za Mama Mkwe ni chawa tu, zinatanguliza maslahi binafsi. Halafu hawa wagogo kwa tabia zao za kuombaomba hawakosi kukubali nyumba za wakwe kupewa.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom