Ni yepi madhara ya kukosekana kwa uzalendo?

Bishop Hiluka

JF-Expert Member
Aug 12, 2011
7,140
14,678
*Ifuatayo ni makala yangu iliyotoka kwenye gazeti la KULIKONI la leo tar 19 Agosti, 2011.

Makala zangu mbili zilizotangulia nilielezea kuhusu miaka 50 ya uhuru wetu na kugusia
kwamba matatizo yetu yamesababishwa na kukosekana uzalendo, jambo ambalo limenifanya
kuonekana mpinzani. Msomaji mmoja amehoji kama naelewa maana ya neno hilo, kwa kuwa
nimeonekana kulitumia sana katika mambo ambayo yeye anadhani hayakupaswa.


Pia ameonesha wasiwasi wake kuwa makala zangu zilibeba ujumbe mmoja tu; kuikosoa Serikali
ya Chama Cha Mapinduzi kwa mawazo ya kiupinzani. Japo hakunieleza waziwazi lakini alikusudia
kuniambia kuwa mimi ni mpinzani wa serikali, kwa kupinga hata mazuri yaliyofanyika.


Ningependa kuweka wazi msimamo wangu kwake na kwa wengine kuwa mimi sina chama na
wala sijawahi kuwa mwanachama wa chama chochote cha siasa katika maisha yangu. Kwa kifupi
sitaki kuwa na chama, hivyo sifungwi na itikadi za chama chochote na siandiki kwa utashi wa
chama au mtu mwingine, ndiyo maana nipo huru kutoa mawazo yangu.


Pia siipendi siasa kwa kuwa kwangu siasa ni "si hasa", ila navutwa kuandika kuhusu siasa kwa
kuwa napenda kutoa mchango wangu kuhusu mustakabali wa nchi yetu.


Nirudi kwenye mada husika - Uzalendo – nijuavyo neno hili maana yake ni mtu kuipenda nchi yake,
uzalendo ni miongoni mwa tabia njema ambazo inatakiwa ziwe ni pambo la mtu. Tabia hii ina athari
kubwa sana katika kuchochea maendeleo ya mtu binafsi na nchi yake kwa ujumla. Uzalendo
humsukuma mtu kuithamini na kuionea fahari nchi yake, vitu ambavyo ni chachu na hamira ya
maendeleo. Uzalendo humfanya mtu kuitakia mema nchi yake.


Kiongozi yeyote mzalendo husukumwa na mapenzi kwa nchi yake, hawezi kulazimisha kununua
ndege ya rais ya mabilioni hata kama wananchi wake watakula nyasi. Kiongozi mzalendo hawezi
kujilimbikizia mali haramu ambazo upatikanaji wake una utata.

Je, viongozi matajiri wamefanya biashara gani madarakani hadi wakaupata utajiri walio nao kama si kukosa uzalendo kwa nchi yao? Hivi utajiri wa viongozi hawa umelipiwa kodi ya mapato? Ni kweli wana mapenzi ya dhati kwa Watanzania wenzao katika kuondokana na madhila ya umaskini yanayowasibu?


Kiongozi yeyote mzalendo hawezi kuchukua 'ten parcent' ili kupitisha mikataba ya kinyonyaji ambayo
italeta maafa kwa wananchi na kumfaidisha mgeni ambaye akishapata akitakacho ataondoka zake.
Leo hii pesa za kodi ya wananchi zinaishia kujenga mahekalu na kununua magari ya kifahari ya
viongozi ili-hali wananchi wanaendelea kuwa masikini, wanaoishi chini ya mstari wa ufukara ambapo
asilimia 80 yao wanaishi vijijini wakitegemea kilimo cha jembe la mkono.


Uzalendo ni kitu adimu sana katika serikali nyingi za Kiafrika japo watawala wawapo majukwaani
huhubiri uzalendo utadhani ni nguo un
ayoweza kuinunua dukani au kwa machinga. Wanasahau
kuwa uzalendo uko moyoni, uzalendo ni sumu ya unyonyaji, uzalendo ni sumu ya rushwa,
uzalendo ni sumu ya ukandamizaji, uzalendo ni sumu ya uonevu, uzalendo ni dawa kwa wananchi.


Kukosekana kwa uzalendo huwafanya viongozi kujivua majukumu yao ya kuhakikisha wananchi
wanapata fursa sawa katika kushiriki masuala ya maendeleo ya kiuchumi na kijamii. Viongozi ambao
hushirikiana na wafanyabiashara wasio waaminifu kufanya udanganyifu katika biashara kwa kuwauzia
wananchi bidhaa zilizo chini ya kiwango cha ubora, kuwapunja katika mizani au kuwauzia kwa bei
ya juu kupita kiasi.


Kiongozi au mwananchi mzalendo ni yule afikaye kazini mapema kwa muda utakiwao na kufanya
kazi kikamilifu kwa mujibu wa taratibu za kazi, atokaye kazini kwenda nyumbani kwa muda
uliopangwa. Ukosefu wa uzalendo ndiyo umefanya viwanda vingi kufa, mashirika ya umma yamekufa
na kuongeza idadi ya wazururaji na wakaa vijiweni ambao walikuwa wameajiriwa kwenye mashirika
hayo.


Ukosefu wa uzalendo unasababisha umasikini katika nchi nyingi za Kiafrika kuwa ni wa Kujitakia.
Umasikini wa aina zote mbili: umasikini wa nchi na umasikini wa watu walio wengi katika ujumla wao.
Yaani tunashindwa hata kujinasua kwenye hili moja la kuwa na umasikini wa watu tu huku nchi
ikiondoka kwenye utegemezi wa wahisani, kama sasa ambapo bajeti yetu haikamiliki bila kutegemea
wahisani.

Inapotokea serikali imekuwa masikini hadi kuendeshwa kwa misaada toka nje ya nchi huku
ikiendeshwa na viongozi matajiri kuliko serikali yao, ndipo kunapokuwa na maswali, halafu mbaya
zaidi na wananchi nao wakawa masikini hadi kufikia kiwango cha kushindwa kufanya lolote.


Umasikini umekuwa kikwazo dhidi ya demokrasia na kikwazo dhidi ya utawala bora kwa kuwa wezi
wa mali za umma, walaji rushwa na mafisadi ndio wenye tabia za kuwanunua wapiga kura walalahoi
kwa njaa na umasikini wa kupindukia.


Ni muhali bali uongo mweupe mtu kudai kuwa anaipenda nchi yake huku anawasahau wananchi
wake ambao wamemfanya yeye awepo hapo alipo na kuneemesha kundi dogo la marafiki wake na
familia yake. Kielelezo na nembo kuu ya kuonesha taswira ya uzalendo wake kwa nchi yake kiwe ni
kuwahudumia wananchi wake; katika hali na mali.


Ni wajibu na jukumu la kila mmoja wetu kuipenda nchi yake. Mwanafunzi mwenye uzalendo na nchi
yake ni yule anayesoma kwa hima juhudi na bidii huku akizingatia miiko na taratibu za elimu ambazo
ni pamoja na kuwaheshimu walimu wake na kanuni zote za shule sambamba na kushirikiana na
wenzake.


Naomba kuwasilisha...
 
Back
Top Bottom