Ni lazimia Jeshi la Polisi litambue mauaji dhidi ya raia hayakubaliki

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,318
33,125
KATUNI(639).jpg


Jana mamia ya wakazi wa mji wa Songea walifanya maandamano ambayo yaliishia kuuawa kwa watu wawili baada ya polisi kufyatua risasi za moto wakiwatawanya kwa nguvu watu hao.

Polisi wanadaiwa kuchukua uamuzi huo wa kuua baada ya juhudi za kuwataka watu hao watawanyike kushindikana, aidha mabomu ya machozi nayo yanadaiwa hayakufua dafu.

Tukio hilo baya kuliko yote kuwahi kutokea katika mji wa Songea lilitokana na kilio cha muda sasa cha wakazi wwake kwa vyombo vya usalama kwamba kumekuwa na mfululizo wa vitendo vya mauaji ya kinyama vinavyofanywa na watu wasiojulikana kwa kitambo sasa, na takribani watu sita wamekwisha kuuawa katika mazingira ya kutatanisha.

Baada ya kulalamikia vitendo hivyo, wananchi hao jana waliamua kungia barabarani kwenda kwa Mkuu wa Wilaya kudai haki yao ya kuhakikishiwa usalama, lakini badala ya kupata walichokuwa wanatafuta waliishia kutawanywa na idadi ya vifo ikaongezeka kwa kuuawa kwa watu wawili, hivyo

kufanya maisha ya wananchi yaliyokatizwa kikatili kufikia wanane, polisi wakichangia vifo hivyo kwa kuua watu wawili.
Ingawa hadi sasa hakuna taarifa zozote za kina juu ya chanzo cha mauaji ambayo yameutikisa mji wa Songea kwa kitambo sasa, kuna uvumi mitaani kwamba mauaji hayo yanashikamanishwa na imani za kishirikina na mambo ya mapenzi kwa kuwa eti kila anayeuawa ananyofolewa sehemu zake za siri.

Ni vigumu kujua kwa hakika nguvu iliyo nyuma ya mauaji haya, lakini itoshe tu kusema kuwa wananchi wameingiwa na hofu kwa kuwa kila uchao mmoja wao anauawa katika mazingira ya kutatanisha na kibaya zaidi wauaji hawajulikani, na hakuna dalili kwamba watajulikana katika kipindi kifupi kijacho.

Tunafikiri hali hii kwa vyovyote imeamsha taharuki kwa wakazi wa manispaa hiyo kiasi cha kuamua kwenda kwa watawala ili wajue nini kinafanyika katika kukomesha hali hiyo.

Inawezekana kabisa maandamano hayo hayakuwa na kibali cha polisi, na inawezekana kabisa hata haja ya kuomba kibali haikuwapo kwa sababu ya aina ya jambo lenyewe ambalo si tu ni la dharura kubwa bali pia linahusu uhai wa wakazi wa mji huo. Kwa maana hiyo, suala hili lilipaswa kuchukuliwa kwa aina ya kipekee na kwa tahadhari kubwa.

Taarifa zinasema kuwa polisi waliamua kutumia risasi za moto baada ya wananchi hao kuanza kurusha mawe na kuharibu mali, yakiwamo magari ya polisi; lakini pia baada ya kuona hata mabomu ya machozi hayafui dafu kwa waandamanaji hao.

Tunasema hali hii kwa ujumla wake ni ya kusikitisha na kwa kweli ni jambo la bahati mbaya sana limeachwa hadi likafika hatua hiyo.
Tunajua kila raia ni mlinzi katika nchi yake, kiwango cha wajibu wa kiulinzi wa raia wa kawaida na cha askari polisi ambaye amefunzwa na

kukabidhiwa jukumu hilo kisheria kwa maana ya kuwa na nyenzo, ni tofauti sana, ndiyo maana wananchi hawa wanaamini ulinzi wao unaweza kuhakikishwa na vyombo vya dola, kama polisi.

Ndiyo maana wakawa wanakwenda kwa watawala kuuliza kulikoni ulinzi wao unayumba kiasi cha kufanya kila mkazi wa mji huo kuishi kwa hofu na kihoro kikubwa bila kujua nani atafuata katika msururu wa mauaji ya kutatanisha?

Wakati tunaandika tahariri hii yapo matukio mengine ya mwezi huu tu ya polisi kutumia bunduki na risasi walizopewa kulinda raia lakini wakazigeuza dhidi yao, mojawapo ni hili tukio la mkoani Mbeya ambako mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Theofilo ameuawa kinyama kabisa.
Haya ni mambo yanayohoji vitendo vya baadhi ya askari polisi kama kweli wapo kwa ajili ya ulinzi wa raia na mali zao au wako kwenye shughuli nyingine.

Wakazi wa Songea wametatizwa na kivuta miguu kwa vyombo vya dola katika kudhibiti mauaji dhidi yao, lakini hata pale walipojawa na hisia kali na kutaka kuhakikishiwa usalama wao na watawala na vyombo vya dola, wameishia kushuhudia si damu nyingine kumwagika tu, bali vifo vingine vikiongezeka na kuongeza simanzi kwao.

Sisi tunaamini kwamba kwa vyovyote vile, polisi ambao wamefuzu sawasawa mafunzo yao na wakati wote wanaongozwa na weledi katika kazi, suala la kuua raia ni jambo la mwisho kabisa katika kukabiliana na maandamano yoyote.

Tunafikiri Jeshi la Polisi linapashwa kukaa chini na kujiuliza kama kweli askari wake wote wako juu ya mstari wa weledi katika kutimiza wajibu wao, vinginevyo tunajenga na kupalilia utamaduni wa kuua raia ovyo kwa kuwa tu tumekabidhiwa bunduki.

CHANZO: NIPASHE
 
Polisi wameonyesha jinsi walivyo katili, mbumbumbu na mananga wa fani hiyo. Kuna namna nyingi za kukabiliana na maandamano. Hiyo ya kutumia risasi ni ya mwisho kabisa na hutumika kama waandamanaji pia wana bunduki. Inasikitisha sana !!!
 
Back
Top Bottom