Ni ishara mbaya kwa serikali ? Mhadhiri

Mtoto wa Mkulima

JF-Expert Member
Apr 12, 2007
681
126
Ni ishara mbaya kwa serikali ? Mhadhiri

2007-10-24 08:59:31
Na Ellen Manyangu


Kukithiri kwa vitendo vya raia kuvamia vituo vya polisi bila kujali silaha zao pamoja na kuwazomea viongozi ni ishara ya kuchoshwa na mwenendo wa serikali yao.

Mkuu wa Kitivo cha Elimu ya Jamii na Mambo ya Kale wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk. Abu Mvungi, alisema kuwa watu wengi wamechoshwa na jinsi serikali inavyoendeshwa na hivyo wamekata tamaa na kuamua kujichukulia sheria mikononi bila kujali athari zake.

Dk. Mvungi alikuwa akitoa maoni yake kuhusu wimbi la wananchi kuvamia vituo vya polisi kwa lengo la kuwaua watuhumiwa bila kuogopa ama kujali bunduki za askari hao.
Aliishauri serikali itafakari vitendo hivyo na kurudisha imani kwa wananchi.

Dk. Mvungi alisema watu wanapoamua kuwazomea ama kuwavamia askari wakiwa na silaha za moto, wanakuwa wamekata tamaa na wengi wao wamechanganyikiwa na maisha.

`Vitendo vya rushwa na nchi kuongozwa katika utaratibu ambao hautoi haki ni moja ya matatizo yanayowafanya wanachi kukosa imani na serikali yao na kuishi kama wamechanganyikiwa,` alisema.

Aliongeza kuwa sheria zimekuwa zikiheshimika pale zinapotumika vyema na si vinginevyo.

`Mfano kama mwananchi wa kawaida anaamua kuziheshimu sheria kwa kumpeleka kituoni mtu aliye mkwaza lakini mhalifu huyo akifikishwa huko sheria zinapindishwa na kesho yake anaonekana yupo mitaani akitamba. Lazima sheria iwe msumeno ikate pande zote na sio pande moja ya wanyonge,` alisema Dk. Mvungi.

Alisema kama mtuhumiwa angekuwa anafikishwa kituoni na haki ikatendeka, tena kwa wakati mfupi ni wazi kuwa kusingekuwepo na matukio ya kujichukulia sheria mikononi.

Aliongeza kwamba hili lisichukuliwe kama tatizo wananchi kutokuwa na elimu ya sheria bali ni kutotumika kwa sheria hizo vizuri.

Dk. Mvungi alisema kuwa kwa sasa serikali inakabiliwa na tuhuma nyingi lakini hakuna kauli ya maana iliyotolewa na Rais wa nchi.

`Unadhani kama Rais anasikia tuhuma nzito zinazoendelea kutolewa na watu halafu anajibu kuwa ni demokrasia ya watu kutoa maoni yao hivi unadhani wananchi watakuwa na imani na serikali yao tena?`, alihoji msomi huyo.

Alisema anaamini kusingekuwepo na matukio ya kuzomewa kwa viongozi huko mikoani na sehemu zingine kama wangeonekana wapo huko kwa masilahi ya wananchi.

`Mwananchi wa kawaida anayeishi kwa mlo mmoja... Halafu anaambiwa kuna kiongozi anakuja kuwahutubia kuhusu kuondoa umasikini akiwa na msururu wa magari ya kifahari ambayo yanamfuata nyuma na yeye anapita juu kwa juu na ndege mkoa kwa mkoa unadhani huyo kiongozi atasikilizwa?` alihoji Dk. Mvungi.

Alisema sasa wakati wa kusema kuwa tunaondoa umaskini kwa maneno na kudanganyana kwa kutembeleana na magari ya kifahari umepitwa na wakati na kikubwa kilichobaki ni kufanya vitu kwa vitendo.

Shabu Kibaja wa Temeke anasema anaamini tabia ya watu kuvamia vituo ili kuwaua watuhumiwa inasababishwa na rushwa.

`Rushwa imekithiri kwenye vyombo vya sheria. Wakosaji wanaachiwa huru na sasa wananchi wamechoka. Wanaamua kutumia nguvu kupata haki,` anasema.

Shabu anasema wananchi wakichoshwa na jambo hakuna risasi inayoweza kuwazuia wasichukue haki yao pale wanapoitaka.

Jackson Moyo wa Mwenge alipotakiwa kutoa maoni yake alidai kwamba yeye anaona kuna sababu mbili zinazopelekea watu kuamua kuvamia vituo vya polisi kuwasulubu watuhumiwa.

Alizitaja sababu hizo kuwa ni pamoja na kesi kuchukua muda mrefu na watuhumiwa kuachiwa huru, hususan na polisi, baada ya `kuongea nao vizuri`.

`Mimi ninakubaliana na Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Bw. Saidi Mwema, kwamba ni kosa kwa wananchi kujichukulia sheria mkononi kuwaadhibu watuhumiwa, lakini wakati anapokemea hilo, alikemee pia jeshi lake litende haki kwani linachangia tatizo,` alisema Bw. Moyo.

Juzi, Bw. Mwema aliwaonya wananchi kuacha tabia ya kuvamia vituo vya polisi kwa lengo la kuwaadhibu watuhumiwa.

Alisema kufanya hivyo ni kosa kisheria na kwamba tabia hiyo inahatarisha maisha ya wananchi kwani askari polisi wanaruhusiwa kisheria kuzuia mfungwa kutoroshwa, ikibidi hata kuua.

Aliwataka wananchi kufuata sheria kwani `uhalifu hauondolewi kwa kufanya uhalifu`.

Mwezi huu matukio ya kujichukulia sheria mkononi yalijiri huko Singida ambapo wavamizi walivunja kituo cha polisi na kumuua mtuhumiwa wa mauaji.

Wilayani Chato, Kagera wanavijiji walichoma makao makuu ya polisi ili kumuua mtuhumiwa aliyedaiwa kukutwa akiwa na ngozi ya binadamu. Lakini tukio hilo ulikuwa uvumi tu. Hakukuwa na mtuhumiwa wa aina hiyo.

Huko Tanga raia walivunja ofisi ya kijiji na kumuua mtuhumiwa wa mauaji aliyekuwa amefungiwa humo akisubiri kupelekwa polisi.

SOURCE: Nipashe
 
Back
Top Bottom