nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
Saturday, 13 August 2011 20:50 |
AWAOMBA RADHI WABUNGE, WATANZANIA Neville Meena, Dodoma BUNGE jana lilipitisha bajeti ya Wizara ya Nishati na Madini huku baadhi ya wabunge wakiitahadharisha Serikali kuondokana na utamaduni wa kuwa na mipango ya dharura ambayo wamesema ni chanzo cha rushwa, wizi na ufisadi.Bajeti hiyo ilipitishwa jana baada ya Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja na Naibu wake, Adam Malima, kujibu hoja za wabunge na kuwasilisha mpango wa dharura wa kukabiliana na tatizo la umeme nchini. Ngeleja aliza kuijibu hoja kwa kuwaomba radhi wabunge na Watanzania kwa ujumla kuhusu makosa yaliyofanywa na wizara yake, hatua ambayo inatafsiriwa kuwa ni kukubaliana na ushauri tolewa hivi karibuni na Waziri wa Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki, Samuel Sitta, jijini Mbeya akisema Serikali inapaswa kuwaomba radhi Watanzania kutokana na mgawo wa umeme. Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini, January Makamba, alikuwa wa kwanza kutoa tahadhari hiyo pale alipoliambia bunge kuwa "Sasa dharura ifikie mwisho, na mpango huu wa dharura uwe wa mwisho maana haya mambo ya dharura yamekuwa kichocheo cha rushwa, wizi na ufisadi". Makamba pamoja na wabunge wengine walitoa kauli hizo Bunge lilipokaa kama kamati, baada ya Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja kuwasilisha mpango wa dharura wa kuliondoa Taifa gizani ambao utaigharimu Serikali Sh523 bilioni kwa miezi minne ambayo ni Agosti hadi Desemba, mwaka huu. Onyo la Wabunge Hoja ya ukomo wa mipango ya dharura iliungwa mkono na Mbunge wa Kibakwe (CCM), George Simbachawene na Mbunge wa Same Mashariki (CCM), Anne Kilango Malecela ambao walisema mipango ya dharura katika sekta ndogo ya umeme ni chanzo cha ufisadi. Kilango alisema Serikali iwe na dhamira ya kweli ya kufikia mwisho wa mipango ya dharura katika kuzalisha umeme nchini na kwamba, taarifa rasmi za Bunge (hansard) zilizopo zinathibitisha uwepo wa dharura nyingi katika suala la uzalishaji wa nishati hiyo. "Tukubaliane, haya mambo ya dharura ndiyo yamekuwa yakitengeneza mianya yote ya ufisadi, sasa lazima tuwe na dhamira ya kweli ya kukomesha hali hii," alisema Killango na kuongeza: "Tunahitaji kuwa na uwezo kuzalisha umeme wetu wenyewe na kuondokana na dharura hizi, tuwe kama Msumbiji ambao wanauza umeme wao Afrika Kusini, tunaweza tukidhamiria". Naye Simbachawene alisema baadhi ya watu wanapenda dharura na kwamba, huenda wananufaika na uwezo wa dharura hizo. "Kuna wengine wanapenda kweli mipango ya dharura, mimi nadhani iwe mwisho na hali hii isiendelee tena," alisisitiza Simbachawene. Mbunge mwingine aliyezungumzia suala hilo ni Joseph Selasini wa Rombo (Chadema) ambaye alitahadharisha kwamba tatizo la umeme ni sawa mgonjwa ambaye anastahili huduma na kwamba wale wanaolishughulikia "wasinywe uji wa mgonjwa". Kwa mujibu wa Selasini, hoja za wasiwasi wa wabunge kuhusu miradi ya dharura ni za msingi na kwamba, uzoefu unathibitisha kuwepo kwa ufisadi, rushwa na wizi wa mali ya umma kupitia miradi hiyo. Alisema ikiwa ufisadi utaingia katika mchakato wa sasa wa mpango wa dharura ni sawa na kunywa uji wa mgonjwa na kwamba ikiwa hivyo, hali itakuwa mbaya zaidi kiasi cha kutishia uchumi na mustakabali wa nchi (mgonjwa atakufa). Mkamba Makamba ambaye pia ni Mbunge wa Bumbuli (CCM) alikosoa uamuzi wa Serikali wa kuweka sehemu ya mitambo ya Symbion katika mikoa ya Dodoma na Arusha akiseme ni ya gharama kubwa na ni lazima iwepo idadi kubwa ya magari ya kusafirishia mafuta. "Kusafirisha mafuta kutoka Dar es Salaam hadi Dodoma ili kuendesha mtambo wa kuzalisha megawati 100 unahitaji malori 50 ya kufanya kazi hiyo na malori 25 hapa Dodoma huku magari mengine yawe yanapakia. Hizi gharama hizi ni kubwa pengine Serikali ilitazame hili," alisema January. Mikopo ya Benki Baadhi ya wabunge wakiongozwa na Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe, walikosoa mpango wa huo wa dharura wa Serikali kutegemea zaidi fedha zinazotokana na mikopo ya benki ambayo ina riba kubwa za kibiashara. Mbowe ambaye ni Mbunge wa Hai (Chadema) alisema, "Kila mara zimekuwa zikitolewa kauli nzuri na Serikali hiihii na wizara hiihii ambayo ndiyo imetufikisha hapa tulipo. Sasa tungetaka watwambie wata-manage (watasimamia) vipi suala hili?" alihoji Mbowe na kuongeza: "Ni watu hawahawa ambao wameshindwa ku-deliver (kuleta tija) siku zote au Serikali inakubaliana na ushauri wetu wa kuunda task force (kikosikazi) kwa ajili ya kutekeleza mpango huu!" Alisema licha ya Serikali kuahidi kuwa fedha zilizokopwa zitalipwa, mzigo wa deni hilo utakaobebwa na Watanzania na ni matokeo ya uzembe wa Serikali ambayo imekuwa ikipanga mipango isiyotekelezeka. Alisema kwa kuwa Serikali imekopa kwa masharti ya kibiashara lazima tahadhari ichukuliwe ili matatizo ya umeme yasivuke mpaka na kusababisha matatizo makubwa zaidi kwa wananchi kupitia mikopo hiyo. Kwa upande wake, mbunge wa Ubungo, John Mnyika aliukosoa mpango huo huku akihoji sababu za Serikali "kukimbilia kukopa benki" badala ya kuchukua fedha katika matumizi yasiyo ya lazima. Alisema katika bajeti mbadala iliyosomwa na kambi ya upinzani, kulikuwa na mapendekezo ya vyanzo mbadala vya fedha ambavyo vingeiwezesha Serikali kupata zaidi ya Sh500 bilioni kama ushauri wake ungezingatiwa. Kwa mujibu wa Mnyika hata ahadi za Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, aliyoitoa wakati akiondoa bajeti ya nishati bungeni Julai 18, mwaka huu hazikuzingatiwa katika utafutaji wa fedha za dharura. Hata hivyo, Pinda alisema hawakuweza kupata fedha katika mafungu mengine ya Serikali kama ilivyoitarajiwa, ndiyo maana waliamua kutafuta fedha za mkopo kutoka benki. "Tanesco hadi sasa wana deni linalofikia shilingi bilioni 300, halafu leo hii tunaendelea kuwabebesha mzigo wa mkopo mwingine mkubwa. Tungeweza kuepusha kadhia hii kwa kutumia vyanzo vingine vya fedha. Hivi vipo vingi!" alisema Mnyika ambaye pia ni Waziri Kivuli wa Nishati na Madini. Kwa upande wake Ngeleja alisema wizara yake imechukua Sh10.3 bilioni kutoka katika matumizi yasiyokuwa ya lazima ndani ya Wizara na miongoni mwake ni kufuta mpango wa kujenga ofisi ya kanda ya madini jijini Dar es salaam na kufuta baadhi ya posho zisizokuwa na tija. Naye mbunge wa Mkanyageni, Mohamed Habib Mnyaa (CUF), alieleza kutoridhishwa na mpango huo wa Serikali kwa maelezo kwamba tatizo hilo ni la muda mrefu na kwamba ni wa gharama kubwa kwa wananchi. Mnyaa alisema zipo kampuni nyingi ambazo zinaweza kuziuzia Serikali mitambo ya umeme katika muda wa miezi miwili na kwamba, hoja ya Serikali kuwa ununuzi wa mitambo mipya ya kuzalisha umeme unahitaji mchakato mrefu, siyo ya kweli. Kadhalika Mbunge wa Bariadi Mashariki, John Cheyo (UDP), alisema Serikali inapaswa kuacha utamaduni wa kutekeleza wajibu wake kwa kusukumwa huku akisema hana imani iwapo mpango huo utaweza kutekelezwa. Alitaka Tanesco kugawanywa ili kuleta tija ya shirika hilo ambalo licha ya kufanya kazi kwa muda mrefu limeshindwa kujiendesha kwa faida."Tanesco is overlodead (limezidiwa) kwa hiyo ninapendekeza ligawanywe katika sehemu tatu kama ambavyo imewahi kusemwa kuwa kuwepo sehemu ya generation (uzalishaji), transimission (usafirishaji) na distribution (usambazaji)," alisema Cheyo. Watendaji wa Wizara Baadhi ya wabunge pia walitaka Serikali kuchukua hatua dhidi ya watumishi wa Wizara ya Nishati na Madini ambao wamekuwa kikwazo cha utekelelzaji wa mipango ya wizara hiyo.Mbunge wa Ludewa (CCM), Deo Filikunjombe alisema Serikali inapaswa kuwachukulia hatua watumishi ambao wamesababisha Tanesco kuwa Shirika la "usambazaji wa giza", badala ya kusambaza umeme. Alimtaka Waziri Ngeleja kuchukua hatua za kuisafisha wizara yake na kwamba, licha ya Katibu wake Mkuu kusimamishwa kazi kwa ajili ya kupisha uchunguzi dhidi yake, bado kuna watumishi wengine ambao wanatakiwa kuchukuliwa hatua ili kuwezesha kazi za wizara hiyo kufanyika. Mbunge wa Kilindi (CCM), Beatrice Shelukindo kwa upande wake aliweka wazi kuwa wizara hiyo inahitaji kufanya mabadiliko makubwa ya kiutumishi ili kuwezesha mipango ya serikali kutekelezwa. Ngeleja aomba radhi Mapema wakati akijibu hoja za wabunge, Ngeleja aliwaomba radhi wabunge na Watanzania kwa ujumla kwa kile alichosema kuwa ni makosa yaliyofanywa na wizara yake. Hatua ya kuomba radhi inatafsiriwa kuwa ni kukubaliana na ushauri uliotolewa na Waziri Sitta katika mkutano wa hadhara wa CCM mkoani Mbeya hivi karibuni akisema Serikali ilipaswa kuomba radhi kutokana na matatizo ya umeme nchini. Hata hivyo kauli hiyo ya Sitta ilimweka matatani baada ya kushambuliwa waziwazi na baadhi ya makada wa CCM wakiongozwa na Mwenyekiti wa chama hicho mkoa wa Dar es Salaam, John Guninita, akiseme waziri huyo anaidhalilisha CCM mbele ya umma. Lakini jana Ngeleja alionekana kukubaliana na Sitta kwani alitumia takriban dakika kumi kuomba radhi kwa kile alichosema kuwa ni makosa yaliyofanywa ama na yeye mwenyewe akiwa waaziri mwenye dhamana au na watendaji wake katika wizara hiyo ya nishati na madini. "Leo nawasilisha bajeti hii ikiwa ni mara yangu ya nne, napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa yale ambayo yalijitokeza pengine yamenigusa mimi kuliko yalivyowagusa wabunge wengine," alisema Ngeleja na kuongeza: "Yapo mambo ambayo hayajawahi kutokea nikiwa katika wizara hii ya nishati na madini. Lakini ninaamini kutenda kosa si kosa, bali kurudia kosa ni tatizo kubwa sana". |